Showing posts with label ZANZIBAR. Show all posts
Showing posts with label ZANZIBAR. Show all posts

1 Apr 2016

Moja ya masuala yanayotawala anga za habari na mijadala mbalimbali mtandaoni ni uamuzi wa bodi ya taasisi ya Changamoto ya Milenia (Millennium Challenge Corporation) ya Marekani kusitisha misaada kwa Tanzania. Sababu kuu mbili zilizotolewa na bodi hiyo kuhusu uamuzi huo ni marudio ya uchaguzi huko Zanzibar Machi 20, mwaka huu, ambao licha ya kususiwa na chama kikuu cha upinzani cha CUF, ulilalamikiwa kwa kiasi kikubwa na nchi wahisani, ikiwa ni pamoja na Marekani.

Sababu ya pili, kwa mujibu wa bodi hiyo, ni uamuzi wa serikali ya Tanzania kupitisha Sheria Uhalifu wa Mtandaoni (Cybercrime Act) ya mwaka 2015 licha ya upinzani mkali dhidi ya muswada wa sheria hiyo, iliyotafsiriwa kuwa imemlenga kukandamiza uhuru wa habari na haki za binadamu.

Kabla ya kuingia katika uchambuzi huu kiundani, nieleze mtazamo wangu kuhusu sababu hizo mbili zilizotolewa na bodi ya MCC. Kwanza, kwa mtazamo wangu, suala la marudio ya uchaguzi wa Zanzibar ni mzaha wa kidemokrasia, na ni jeraha la kisiasa ambalo historia inaweza kutuhukumu huko mbeleni. Haihitaji uelewa mkubwa wa siasa za Zanzibar kufahamu kuwa kuna ‘sheria isiyo rasmi’ kuwa ‘kamwe CUF hawapaswi kutawala Zanzibar.’ Bila kuuma maneno, hiyo ndo sababu pekee ya kufutwa kwa uchaguzi wa awali (ambao inadaiwa mgombea wa CUF, Seif Shariff Hamad, alishinda), na kuamiriwa uchaguzi huo urudiwe huku CCM ikiwekeza nguvu zake zote kuhakikisha inashinda. Hata kama CUF wasingesusia uchaguzi huo, bado CCM wangeshinda kwa sababu ‘ni lazima iwe hivyo,’ kwa ‘kanuni’ zao.

Je MCC ipo sahihi kutumia kigezo cha Zanzibar kusitisha misaada yao? Kwa upande mmoja, wapo sahihi. Kwanini? Kwa sababu, hata katika mahusiano yetu ya kawaida tu kibinadamu, anayekupa msaada anapata ruhusa pia ya ‘kukutawala’ kwa kukupa masharti ambayo ukiyakiuka, yanaweza kuathiri mahusiano katika ya mtoa msaada na mpokea msaada. Miongoni mwa masharti ya MCC ni pamoja na masuala ya demokrasia, na haihitaji kukuna kichwa sana kubaini kuwa marejeo ya uchaguzi wa Zanzibar, ambayo binafsi ninayaona kuwa ni mzaha wa kidemokrasia, yamewapa MCC ‘kisingizio chepesi’ hata kama hawangekuwa na sababu nyingine.

Mgogoro wa muda mrefu wa kisiasa huko Zanzibar ni zaidi ya jipu. Ni kansa ambayo imeshachafua sura ya Tanzania huko nyuma ambapo kwa mara ya kwanza tulizalisha wakimbizi baada ya vurugu za uchaguzi mkuu mwaka wa 2000. Ni kansa ambayo sasa imewapa MCC kisingizio cha kutunyima misaada yao. Kwa bahati mbaya, au makusudi, hakuna utashi wa kisiasa wa kusaka ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro huo. Kila kiongozi wa CCM, kwa upande wa Bara, anaogopa suala hilo kwa kuhofia ‘kuvunjikiwa na Muungano mikononi mwake.’

Wanasiasa wa Zanzibar sio tu wanaufahamu udhaifu huo bali pia wanautumia vema. Wanaendesha siasa zao cha chuki na uhasama watakavyo wakifahamu fika kuwa hakuna mwana-CCM wa Bara mwenye jeuri ya kuwaingilia.

Sina hakika Zanzibar itaathirika vipi kwa maamuzi ya MCC kukata misaada, lakini kinachowapa kiburi viongozi wa huko ni kwamba ‘Tanganyika’ haina jeuri ya kuisusa Zanzibar, au kuinyooshea kidole katika mwendelezo wa siasa za chuki na ubaguzi.

Lakini kwa upande wa pili, hao MCC ni wanafiki tu. Huhitaji kuwa na uelewa mkubwa wa siasa za kimataifa kutambua unafiki wa Marekani linapokuja suala la demokrasia. Nchi hiyo ni mshirika mkubwa wa tawala za kidikteta kama vile huko Misri, Saudi Arabia na kwingineko. Sawa, labda Zanzibar wamefanya mzaha wa kidemokrasia lakini vipi kuhusu demokrasia isiyopo kabisa huko Saudi? Well, jibu rahisi ni kwamba Zanzibar na Tanzania sio muhimu ‘kihivyo’ kwa Marekani ilhali taifa hilo linazitegemea mno tawala za kibabe za nchi kama Misri au Saudi, hususan katika masuala ya ushushushu/mapambano dhidi ya ugaidi wa kimataifa.

Kuhusu suala la Sheria ya Uhalifu wa Mtandao, hapa kumesheheni unafiki, na upo wa aina mbili: wa Wamarekani na wa sie Watanzania wenyewe. Mie ni mfuatiliaji wa karibu wa masuala ya usalama mtandaoni, ambao kwa namna moja au nyingine unahusiana na hiyo ishu ya Cybercrime Act. Kwa kifupi tu, Marekani ina sheria kandamizi mno dhidi ya uhuru wa raia mtandaoni. Naamini ushaskia kuhusu jamaa anayeitwa Edward Snowden (kama hujamsikia, Wasiliana na Google…haha). Huyu bwana alikuwa mtumishi katika shirika la ushushushu la Marekani linalohusika na kunasa mawasiliano mbalimbali (NSA – National Security Agency), na baadaye nafsi yake ilimsuta, akaamua ‘kuingia mitini’ na kumwaga siri lukuki kuhusu jinsi NSA inavyohujumu haki za raia kimawasiliano. Hawa jamaa wamekuwa wakinasa mawasiliano ya takriban kila mtu, wakishirikiana kwa karibu na mashushushu wenzao wa hapa Uingereza, GCHQ, taasisi ya kishushushu inayohusika na kunasa mawasiliano.

Lakini hata tukiweka kando suala la NSA kunasa mawasiliano mbalimbali (waliwahi kuzua kasheshe kubwa baada ya mashushushu wa Ujerumani kubaini kuwa NSA walikuwa wakinasa kwa siri mawasiliano ya Kansela Angela Markel hadi waliposhtukiwa), mashambulizi ya kigaidi nchini humo mwaka 2001 yalipelekea kuundwa kwa sheria kali kabisa dhidi ya uhuru wa habari na haki za kibinadamu kwa kisingizio cha usalama wa taifa. Kwahiyo, kwa kifupi, ni uhuni tu wa Marekani kudai Sheria ya Makosa ya Mtandaoni inakiuka uhuru wa Watanzania. Sheria zao za wazi na za kificho ni mbaya mara milioni zaidi yetu.

Hata hivyo, katika suala hili la Cybercrime Act, tuna wanafiki kadhaa huko nyumbani. Kwa kumbukumbu tu, mie nilikuwa mtetezi mkubwa wa muswada uliozaa sheria hiyo, yaani Cybercrime Bill, na niliunga mkono kwa nguvu zote jitihada za aliyekuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, kuhusu muswada huo.

Hata hivyo, baadhi ya watu wanaoinyooshea kidole Marekani na wafadhili wengine kuhusu suala la Tanzania kukatiwa misaada walikuwa mstari wa mbele kuziomba nchi wahisani ziingilie kati kuibana serikali ili muswada huo usipitishwe kuwa sheria. Sasa kama uamuzi huo wa Marekani umechangiwa na ‘kelele’ zao hizo, kwanini leo wanalalamika?

Mie niliunga mkono muswada na sheria hiyo kwa sababu ikitumiwa vema ni nzuri. Hebu nenda Instagram kaangalie uanaharamu unaoendelea huko, kuanzia picha za uchi, ushoga na kila aina ya laana. Huo sio uhuru wa habari, ni uwendawazimu ambao kwa hakika ulihitaji sheria kali kuudhibiti.

Na watu waliopita huku na kule kudai sheria hiyo ni kandamizi na ililenga kuwabana wananchi wasiwasiliane, hawatuambii kama baada ya sheria hiyo kupitishwa wameshindwa kuwasiliana na watu wengine. Kwa kifupi, kulikuwa na udanganyifu mkubwa katika kambi ya waliopinga muswada na sheria hiyo. Walitumia uelewa mdogo wa wananchi wengi kuhusu masuala ya mtandao, na kuwajenga hofu feki.

Ninakerwa kuona kundi la wanafiki hawa likiilaumu MCC au Marekani au nchi nyingine wahisani kuhusu suala la kutukatia misaada, kwa sababu wao walikuwa mstari wa mbele kuhamasisha nchi wahisani zichukue hatua, na ‘hatua maarufu’ ya wahisani huwa ni kukata misaada. Badala ya kulalamika, wanafiki hawa wanapaswa kufanya sherehe maana wishes zao zimetimia.

Sasa niangalie upande wa athari za uamuzi huo wa MCC kukata misaada. Taarifa nyingine zinaeleza kuwa kuna wahisani wengine nao wamekata misaada japo kuna mkanganyiko kama hatua hiyo ni mwendelezo wa hatua za huko nyuma au ni mpya.

Tuwe wakweli, kwa watu masikini kama sisi, hatua yoyote ile ya kutupunguzia msaada wa aina yoyote ile itatuathiri. Hilo halihitaji uelewa wa jinsi gani misaada inavyofanya kazi au jinsi gani nchi yetu ilivyo mtegemezi mzoefu wa misaada. Tatizo kubwa hapa kuhusu “kukatiwa misaada kutatuathiri au hakutatuathiri” ni tofauti zetu za kiitikadi. Kwa kiasi kikubwa, suala hilo linaangaliwa katika lensi ya u-CCM na u-UKAWA/Upinzani. Kwa wana-CCM, ni mwendo wa ‘kiburi’ kwenda mbele, kwamba “waende tu na misaada yao,” au “hela yenyewe ilikuwa ya mradi wa kifisadi wa Symbion,” mara “ah misaada gani hiyo yenye masharti kibao.” Wanamhadaa nani? Kama misaada hiyo haikuwa na muhimu, kwanini basi tuliiomba in the first place? Hizi hadithi za sungura kusema “sizitaki ndizi hizi” baada ya kushindwa kuzikia mgombani.

Kwa upande wa wana-UKAWA/Wapinzani, bila kujali kuwa wao kama Watanzania ni wahanga watarajiwa wa uamuzi huo wa nchi yetu kukatiwa misaada, wanakenua meno yote 32 kwa furaha, huku wakiwazodoa wenzao wa CCM kwa vijembe kama “ndio matunda ya ubabe wenu huko Zanzibar, tuone sasa…” au “mtaisoma namba” au “mtakula jeuri yenu…”

Ulemavu huu wa kifikra unaosababishwa na kuliangalia suala la kiuchumi kwa mtizamo fyongo wa itikadi za kisiasa. Naam, suala la Zanzibar ni la kisiasa, lakini athari za uamuzi wa Marekani/MCC/wahisani ni la kiuchumi.

Mie sio mchumi ila ninachoelewa fika kuwa uchumi wetu umekuwa tegemezi tangu tupate uhuru. Kabla ya kuipa kisogo siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, tulikuwa tukapata misaada kutoka kwa marafiki zetu wa mrengo wa Ukomunisti. Baada ya kuuzika Ujamaa, tumekuwa kama puto linaloyumbishwa na upepo, tupo radhi kumpigia magoti yeyote anayeweza kutusaidia. Kimsingi, tuna ombwe la kiitikadi: majukwaani, CCM wanasema sie ni Wajamaa, vitendo vyetu havipo kwenye Ujamaa wala Ubepari, tupu tupo tu. Huo ndo ukweli mchungu kuhusu ubabaishaji wetu.

Kwahiyo, tuache kudanganyana kuwa kukatiwa misaada hakutotuathiri. Huko ni kujipa jeuri tu. Tunachoweza kukubaliana ni kwamba suala hilo limeshatokea, tumeshakatiwa misaada, na si ajabu wahisani wengine wakaamua kufata mkumbo na kufanya hivyo pia.

Jukumu letu kubwa kwa sasa sio kuendelea kunyoosheana vidole bali tuwe kitu kimoja kama taifa bila kujali nani hasa aliyetusababishia tatizo hili. Ni tatizo la Watanzania wote bila kujali itikadi zao. Uamuzi wa wahisani kukata misaada utawaathiri wana-CCM wanaodai hautowaathiri kama ambavyo utawaathiri wna-CUF au Chadema wanaokenua meno yote 32 kufurahia hatua hiyo. Na utatuathiri (angalau kisaikolojia) hata akina sie ambao itikadi yetu pekee ni Tanzania yetu. Huo ni ukweli usiopingika: we are all in this together.

Kuna mambo mawili ya kupigiwa mstari. Kwanza, kwa miaka mingi tumekuwa tukiishi kifahari mno kuliko uwezo wetu. Na kimsingi, uwezo wetu duni haukupaswa kuwepo kwani sie sio masikini hata kidogo. Tuna kila aina ya utajiri lakini kuna majambazi walioigeuza Tanzania yetu kuwa kitu cha kubakwa kila kukicha. Kila mwenye uelewa anafahamu kilichojiri katika takriban miaka 30 iliyopita. Tanzania yetu ilikuwa shamba la bibi, watu wanafisadi wapendavyo kiasi kwamba kuwa na uchungu na nchi ilionekana kama wendawazimu.

Kwa bahati nzuri, Mwenyezi Mungu amesikia kilio cha baadhi yetu na sasa tumempata Rais, Dkt John Magufuli, ambaye anaonekana amedhamiria kurekebisha mwenendo wa mambo. Kikwazo chetu kikubwa kilikuwa ufisadi, lakini sasa Magufuli ameamua kuvalia njuga kupambana na ufisadi kwa nguvu zote. Mwanzo ni mgumu lakini angalau dalili za mafanikio zimeanza kujionyesha. Tumuunge mkono, tuchukie ufisadi, tuongeze uzalendo, tuikwamue Tanzania yetu, tujikwamue nasi wenyewe, tuache kutafuta njia za mkato za mafanikio, tufanye kazi, tache majungu na kusaka sifa za kijinga mitandaoni, tuwajibike.

Twahitaji kujifunga mikanda. Haiwezekani wafadhili wetu waishi kimasikini ilhali sie wafadhiliwa twaishi kama matajiri. Viongozi wetu waache kuchuana na wauza unga kushindana jinsi ya kuishi kitajiri, wawabane wauza unga hao, majangili na maharamia wengine ili tuiokoe Tanzania yetu.

Je twaweza kujitegemea? Absolutely, lakini tusidanganyane kuwa twaweza kufanya hivyo ghafla ghafla. Tukumbuke, mtoto hazaliwi akatembea. Tumekuwa wategemezi mno wa misaada kiasi kwamba tumesahau kuwa twapaswa kujitegemea. Twahitaji kuchukua na kukubali maamuzi magumu ya kutuwezesha kujitegemea. Ni kama kumlazimisha mtoto anayetambua aanze kutembea kwa nguvu. Sio rahisi, lakini tukimkazania anaweza kusimama mwenyewe na baadaye akaweza hata kukimbia. Hilo linahitaji kujitoka mhanga kwa ajili ya nchi yetu, sambamba na kuweka mbele uzalendo badala ya maslahi binafsi.

Jambo jingine, kwa hisia zangu, japo suala la Zanzibar na Cybercrime Act zinatajwa kama sababu za uamuzi wa kutunyima misaada, ninashawishika kuamini kuwa baadhi ya nchi wahisani hawapendezi na kasi ya Rais Magufuli kuziba mianya ambayo kimsingi licha ya kuwanufaisha mafisadi wa ndani, ilikuwa pia inanufaisha taasisi za kifisadi za kimataifa. Wengi wa majambazi waliokuwa wakitupora fedha zetu mchana kweupe walikuwa hawahifadhi fedha zao katika benki zetu bali zilizopo kwa hao wahisani wetu. Waweza kudhani huu ni utani mbaya, lakini jiulize, je kama unamfadhili mtu pesa za kumsaidia yeye na familia yake, lakini anatumia fedha hizo kununulia bling bling, kuongeza nyumba ndogo, kufanya matumizi ya anasa, nk kwanini usichukue hatua?

Mfano huo unamaanisha hivi: kwanini wahisani wetu walionekana kutokerwa na jinsi pesa walizokuwa wanatupatia zikifisadiwa kila kukicha lakini wakaendelea kutumwagia misaada? Na kwanini sasa, tumempata Magufuli ambaye amepania kwa dhati kupambana na ufisadi, wahisani wanaanza kuleta ‘longolongo’?

Kuna tunaodhani kuwa hao wahisani wanataka tuendelee kuwa wategemezi wao milele. Kwa upande mmoja utegemezi wetu unawapa uhuru wa kukwapua kila raslimali tuliyonayo, na kwa upande mwingine, wananeemesha taasisi zao za fedha kwa vile mafisadi wetu wa ndani wanahifadhi fedha zao kwenye taasisi hizo.

Mwisho, tuache porojo, tuache unafiki, tuwe kitu kimoja, athari za kukatiwa misaada zipo, tukishikamana tutaweza kukabiliana nazo japo mwanzoni itakuwa ngumu. Yawezekana uamuzi huo wa Wamarekani ukawa ‘blessing in disguise’ kwa maana ya kutupa ‘wake-up call’ tuanze kujitegemea kwa lazima badala ya kutembeza bakuli letu huko na kule, kisha kile kidogo kinachopatikana kikaishia kwenye ujenzi wa mahekalu ya mafisadi, ongezeko la magari yao ya kifahari, na kutanua ukubwa wa nyumba ndogo zao.

MUNGU IBARIKI TANZANIA 

11 Aug 2013

Victims Kirstie Trup and Katie Gee

Gazeti la kila siku la Telegraph la hapa Uingereza linaripoti kuwa baadhi ya viongozi wa dini ya Kiislam visiwani Zanzibar wanaamini kuwa shambulio la tindikali dhidi ya mabinti wawili wa Kiingereza, Kirstie Trup na Katie Gee lilifanywa na wafuasi wa kikundi cha UAMSHO, ambacho kinataka Zanzibar ijitenge na Tanzania Bara na kisha kuanzisha sheria kali za Kiislam.

Huko nyuma kumeshatokea mashambulizi dhidi ya viongozi wa dini ya Kiislam na Kikristo, ikiwa ni pamoja na mashambulio ya tindikali na mauaji.

"Ofkoz, itakuwa kazi ya Uamsho," alinukuliwa Sheikh Fadhil Soraga, aliyeshambuliwa kwa tindikali Novemba mwaka jana, na anaamini wahusika katika tukio hilo dhidi yake walikuwa UAMSHO.

Wiki mbili zilizopita, vipeperushi vya vyenye wito mkali wa uchochezi dhidi ya Wakristo vilisambazwa sehemu mbalimbali huo Zanzibar, tukio linalohusishwa na harakati za UAMSHO.

"Siku 10 tu zilizopita, walikuwa wanasema wanaandaa kitu kikubwa. Tukio hili, ambalo Waislamu wote twapaswa kulilaani, ni kazi ya kundi hilo (UAMSHO)," alisisitiza Sheikh Soraga.

Paroko wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph, Zainzibar, Padri Cosmas Shayo naye alikuwa na mtizamo kama huo wa Sheikh Soraga. Mtangulizi wa Padri huyo, Padre Evaristus Mushi, aliuawa kwa kupigwa risasi mwezi Februari, na hisia zimekuwa kwamba UAMSHO walihusika na tukio hilo.

"Hawa watu wamedhamiria kuzusha vurugu  ili kufikia malengo yao," alisema.

"Wanataka kuifanya Zanzibar iwe ya Waislam pekee, na walianza kwa kuwatisha Wakristo na sasa wanataka kuwatisha watalii ambao wanawaona kama Wakristo pia."

Kabla ya shambulio hilo la tindikali, mmoja wa mabinti hao, Katie, alizabwa kibao na mwanamke mmoja mtaani wakati wa mfungo wa  Mwezi wa Ramadhan.

Katie na Kirstie, walikuwa Zanzibar wakifanya kazi kwa kujitolea, baada ya kumaliza masomo yao ya sekondari. Wote wanatoka katika familia zinazojiweza kimaisha. Baba ya Katie ni chartered surveyor,moja ya ajira inayolipa vizuri hapa Uingereza, huku Kirstie alisoma sekondari ambayo ada yake ni pauni 3,375 (zaidi ya Sh milioni 13)  kwa muhula.

Mabinti hao walikuwa Zanzibar kwa mwezi mmoja wakijitolea katika shule ya chekechea ya Mtakatifu Monica, iliyopo Stone Town, kupitia shirika la kujitolea la Art in Tanzania.

Siku moja kabla ya shambulio hilo la tindikali, ali-tweet kwa furaha baada ya kukutana na Rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton, alipozuru Zanzibar hivi karibuni kuhamasisha vita dhidi ya malaria kupitia Clinton Health Access Initiative.

Kwa mujibu wa gazeti la Telegraph, mmoja wa masapota wakubwa wa UAMSHO ni Sheikh Ponda Issa Ponda, anayedaiwa kutumia wiki tatu zilizopita kuhamasisha Waislam Zanzibar 'kuamka kama huko Misri.'

Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali Elieza Feleshi alinukuliwa akisema kuwa Serikali itafanya kila jitihadakumkamata Sheikh Ponda.

Wakati huo huo, gazeti la kila Jumapili la Sunday Mirror lina habari ndefu kuhusu Sheikh Ponda, iliyobeba kichwa cha habari: "Shambulio la tindikali Zanzibar: Mhubiri wa chuki Sheikh Ponda Issa Ponda apigwa risasi na polisi, akamatwa"

Gazeti hilo limeeleza kuwa polisi walimpiga Ponda risasi ya machozi begani kabla ya kumkamata, na sasa yupo mahututi hospitalini.

Habari hiyo inaeleza kuwa Ponda alikwenda Zanzibar kuhamasisha maandamano dhidi ya serikali, na kukiunga mkono kikundi cha UAMSHO, kwa malengo ya kutimua wageni Zanzibar na kuanzisha sheria za Kiislam.



10 Aug 2013

Horrific: The girls suffered "horrendous" burns

Moja ya magazeti makubwa nchini Israel, Jerusalem Post, limeandika kuwa mabinti wawili wa Kiingereza walioshambuliwa kwa tindikali huko ZANZIBAR walikuwa wanaharakati na wanachama wa Shirikisho la Vijana wa Kiyunani (Federation of Zionist Youth).

Kwa namna flani, ukaribu wao na harakati hizo za Kizayuni unaweza kuwa miongoni mwa sababu zilizopelekea mabinti hao, Kirstie Trup na Katie Gee, kushambuliwa. Hisia iliyopo ni waliofanya shambulio hilo walisukumwa zaidi na 'kuwaadhibu Wayunani na marafiki zao,' kama ambavyo imekuwa ikitokea sehemu mbalimbali duniani. Inafahamika kuwa vikundi vyenye msimamo mkali wa Kiislam kama vile Al-Qaeda vimekuwa na uhasama mkubwa na Wayahudi.
The plane

Wakati huohuo, Shirika la Utangazaji wa Uingereza (BBC) linaripoti kuwa serikali ya Zanzibar imetangaza zawadi ya shilingi milioni 10 kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa zitakazopelekea kukamatwa kwa wahusika wa shambulio hilo.

Tukio hilo la kikatili bado linatawala vichwa vya habari kwenye magazeti, TV na radio, hapa Uingereza.

Gazeti la kila siku la Daily Mirror linaelezea jinsi mtalii mmoja kutoka Uingereza,Sam Jones, alivyojitoa mhanga kumwokoa Katie baada ya kumsikia akilia kwa uchungu kutokana na maumivu ya kumwagiwa tindikali.
The two acid attack victims
Sam aliyekuwa visiwani Zanzibar na girlfriend wake, Nadine, alieleza kuwa Katie alikuwa akilia kwa kelele na kuomba amwagiwe maji huku tindikali ikiunguza ngozi yake. Mtalii huyo alifanikiwa kupata maji na kummwagia Katie.

Mhanga mwingine wa tukio hilo, Kirstie, alikutwa na wasamaria wema mtaani akilia kwa uchungu baada ya kumwagiwa tindikali, na walimbeba hadi baharini na kumtumbukiza majini kwa ajili ya kudhibiti madhara zaidi ya tindikali.
Hadi sasa polisi wa Zanzibar wameshawahoji watu saba. Pia wametoa amri ya kukamatwa Sheikh Ponda Issa Ponda, ambaye wanadai alihamasisha shambulio hilo.

1 Jun 2012


Ya Zanzibar si mageni, hata Uskochi yapo
Evarist Chahali
Toleo la 241
30 May 2012


WIKI iliyopita, Waziri wa Kwanza (First Minister, cheo ambacho ni kama Waziri Mkuu) wa Uskochi, Alex Salmond, alizindua kampeni za chama chake cha Scottish Nationalist Party (SNP) kuhamasisha kura ya ‘Hapana’ katika referendum (kura ya maoni ) ya uhuru wa nchi hii inayotarajiwa kufanyika huko mbeleni.
Hoja ya Uskochi kujitenga na Uingereza (kwa maana ya kile kinachoitwa The United Kingdom of Great Britain-England, Uskochi na Wales- and Northern Ireland) imekuwa ikivuma kwa muda mrefu na imepata nguvu zaidi baada ya Salmond na SNP yake kuingia madarakani mwaka 2007.
Kimsingi, sera kuu ya mwanasiasa huyo na chama chake ilikuwa kuhakikisha kuwa hatimaye Uskochi inajitenga kutoka Uingereza.
Walipoingia madarakani tu, SNP walieleza bayana kuwa wana mpango wa kufanyareferendum kusikia maoni ya Waskochi kuhusu wazo hilo la kujitenga.
Hata hivyo, kikwazo ambacho wamekuwa wakikumbana nacho tangu mwanzo ni ukweli kwamba pamoja na tofauti za hapa na pale, ni vigumu kuchora mstari unaoweza kuwatenganisha Waskochi na Waingereza wengine.
Mwingiliano katika takriban kila nyanja ya maisha unawafanya watu hawa kuwa wamoja zaidi kuliko tofauti.
Na wakati naandaa makala hii, Salmond amepata ‘habari mbaya’ kutoka kwa mwendesha kura za maoni (pollster) maarufu hapa Uingereza, Peter Kellner, Rais wa taasisi ya kura za maoni ya YouGov.
Kwa mujibu wa Kellner, kura ya maoni iliyoendeshwa na YouGov Ijumaa iliyopita inaonyesha kuwa wakati ni asilimia 33 tu ya Waskochi wanataka ‘uhuru’ (kujitenga), asilimia 57 wanataka Uskochi iendelee kubaki sehemu ya Uingereza.
Mwendesha kura za maoni huyo amemtahadharisha Salmond kuwa ‘ana mlima mrefu wa kupanda’ kubadili upeo wa wengi wa Waskochi kuhusu nchi yao kujitenga na Uingereza.
Kadhalika, alieleza kuwa kuna ‘vitisho’ kadhaa vinavyoweza kuchangia Waskochi wengi kupinga wazo la kujitenga, na akatoa mfano wa hoja kama wawekezaji kujiondoa Uskochi (kwa kutokuwa na uhakika kama Uskochi itamudu ‘kusimama yenyewe’),  kupoteza ruzuku inayotolewa na Serikali Kuu ya Uingereza (ambayo ni kubwa zaidi ya kodi inayolipwa na Uskochi), matumizi ya sarafu ya pauni ya Kiingereza (British Pound) ambapo kama Uskochi itaamua kutumia sarafu hiyo baada ya kujitenga, Uingereza inaweza kuanzisha hatua za ukalifu (austerity measures) zitakazoathiri uchumi wa Uskochi.
Kadhalika, Salmond ametahadharishwa kwamba hofu nyingine zinazoweza kuwatisha Waskochi kuunga mkono wazo la kujitenga ni pamoja na gharama kubwa za kuendesha nchi kamili (hasa katika kipindi hiki ambapo uchumi wa dunia unayumba) kama vile kumudu kuwa na jeshi kamili, ofisi za ubalozi nchi za nje na gharama za uendeshaji wa taasisi za utumishi wa umma (civil service).
Kimsingi,  katika zoezi lolote lile la kupiga kura, hali ya kutokuwa na uhakika au hofu ya “huko mbele hali itakuwaje” inatosha kuwafanya wapiga kura wengi kuamua kubaki na chama kilichopo au muundo uliopo (iwapo ni referendum ya jambo fulani).
Mbinu hii inatumiwa sana na vyama tawala (ikiwa ni pamoja na CCM) kwenye chaguzi ambapo ujumbe huwa mithili ya ‘zimwi likujualo halikuli likakwisha’ (kwa maana ya chama unachokifahamu ni bora zaidi ya kile kinachoahidi tu pasipo kuwa na mifano hai ya uongozi wa nchi).
Hata hivyo, Salmond na SNP yake wanaendelea na jitihada zao huku wakijipa imani kuwa utajiri mkubwa uliopo Uskochi (kuna mafuta huko Bahari ya Kaskazini) utawezesha kumudu gharama za kuendesha nchi endapo Waskochi wataafiki wazo la kujitenga na Uingereza.
Wakati hayo yakijiri hapa Uskochi, mwishoni mwa wiki huko nyumbani kumekumbwa na habari za kusikitisha ambapo maandamano ya kupinga Muungano huko Zanzibar yaligeuka kuwa machafuko makubwa.
Kama nilivyoeleza katika ujumbe wangu wa Makala za Sauti (Audio Messages, unaoweza kusikia hapa http://goo.gl/r6ngT ), machafuko hayo huko Zanzibar na suala zima la Muungano vinapaswa kuangaliwa kwa mtizamo mpana zaidi.
Binafsi, ninaona kuwa asili ya tatizo la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni waasisi wake, yaani Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Karume. Hapa naomba nieleweke vizuri.
Wazo la Muungano lilikuwa zuri kwa kuzingatia sababu mbalimbali, kubwa zaidi ikiwa ni ukaribu wa asili za watu wa Bara na wa Visiwani.
Lakini tatizo ambalo pengine lilichangiwa zaidi na mazingira ya kisiasa wakati huo, Nyerere na Karume walidhani kuwa ridhaa yao ilikuwa inawakilisha ridhaa ya Watanganyika na Wazanzibari wote.
Kuna ‘busara’ moja ya Kiingereza inayosema kuwa “jambo zuri si lazima liwe na manufaa. Kwa mfano, wakati kumpa chakula kingi mtu mwenye njaa ni jambo zuri lakini matokeo yake yanaweza kupelekea hata kifo kwenye mtu huyo mwenye njaa kali aliyeishia kupewa chakula kingi.”
Ndiyo, kula chakula kingi ukiwa na njaa kali ni hatari, na ndiyo maana watu wanapofunga au wakiwa hawajala muda mrefu huanza mlo kwa kinywaji cha moto (uji au chai).
Sasa, wazo la Muungano lilikuwa zuri lakini kutosaka ridhaa ya wengi ndiko kumetufikisha hapa tulipo sasa. Kwa muda mrefu kumekuwa na manung’uniko kuhusu Muungano, hususan miongoni mwa Wazanzibari.
Hoja kuu imekuwa ni kwamba wanapunjwa, wanaonewa na wengine wanakwenda mbali zaidi na kudai lengo la Muungano lilikuwa ‘kuimeza Zanzibar.’
Kwa bahati mbaya, siasa za Zanzibar zina tofauti kwa kiasi fulani na za Bara. Kwa Visiwani, dini ina nafasi ya kipekee katika siasa. Kwa hiyo, mara nyingi masuala ya kisiasa yanaweza pia kubeba hisia za kidini, jambo ambalo pasipo uangalifu linaweza kuzua balaa kubwa.
Ninapenda kusisitiza kuwa pamoja na hatari zinazoweza kujitokeza kwa kuchanganya dini na siasa, uzoefu na historia vimeonyesha kuwa laiti busara na maslahi ya jamii yakiwekwa mbele ya hisia binafsi, dini inaweza isiwe na madhara katika siasa.
Huko Marekani, kwa mfano, dini bado ina nafasi ya kipekee. Pengine mfano mzuri zaidi ya namna dini inavyoweza kutoharibu siasa ni Ujerumani ambapo chama cha Kansela Angela Merkel (Christian Democratic Union-CDU) ni cha Kikristo. CDU ndio chama kikubwa zaidi cha siasa katika taifa hilo tajiri.
Kadhalika, chama kinachotawala nchini Uturuki, Justice and Development Party-AKP, ni chama cha Kiislamu. Hata hivyo, chama hicho kimefanikiwa kuifanya Uturuki iendelee kuwa taifa lisiloelemea kwenye siasa zinazoongozwa na dini.
Hata hapa Uingereza, Malkia ambaye ndiye mkuu wa nchi (kiheshima zaidi kuliko kiutendaji) pia ni Mkuu (kiheshima) wa Kanisa la Anglikana, na japo Ukristo ni kama ‘dini ya taifa’ lakini nchi hii inaendeshwa kwa sheria za ‘kidunia’ na si za kidini.
Hata hivyo, tatizo la dini ni ukweli kwamba licha ya kugusa hisia binafsi za muumini, mambo ya kidini hayahitaji uthibitisho wa kisayansi (au kidunia).
Tofauti na dini, siasa ni suala la itikadi zaidi kuliko imani (japo imani kwenye itikadi inaweza kuwafanya wafuasi wa chama kukiona kina umuhimu kama dini). Kadhalika, masuala ya dini yanahusisha ‘maisha ya baadaye baada ya haya ya duniani’ ilhali siasa imejikita zaidi kwenye masuala ya sasa au ya hapahapa duniani.
Balaa linakuja pale muumini wa dini anapoanza kuamini kuwa anapopinga Muungano,  kwa mfano, anafanya kazi ya kiroho na inampendeza Muumba. Ni vigumu sana kumdhibiti mtu wa aina hii kwani hata harakati zake zikihatarisha maisha yake, au akaishia kufa, anaamini kuwa atalipwa na Muumba wake.
Kimsingi machafuko yaliyotokea Zanzibar yamechangiwa zaidi na wanasiasa wetu ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wanachelea kile kinachofahamika kama ‘kuogopa laana ya waasisi wa Muungano pindi Muungano huo ukiwavunjikia mikononi mwao.’
Badala ya kuzishughulikia kero za Muungano na kuzipatia ufumbuzi wa kudumu, watawala wetu wamekuwa wakijikita zaidi kwenye kujaribu kutuaminisha kuwa wanalishughulikia suala hilo kwa dhati ilhali wanaligusa juu juu tu.
Tumekuwa na Tume ya Kero za Muungano miaka nenda miaka rudi lakini ufanisi wake umekuwa wa kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Tuache unafiki, ‘kelele’ za kudai mabadiliko ya muundo wa Muungano (na hata hizo za kutaka uvunjiliwe mbali) haziwezi kwisha kwa kuzipuuza au kuwa na ‘tume ya milele’ ya kushughulikia kero hizo pasipo kuja na ufumbuzi.
Lakini kingine ni kuwanyamazia mafashisti wanaohubiri chuki dhidi ya wenzao kwa kisingizio cha kero za Muungano. Huko Zanzibar, baadhi ya wanasiasa wamediriki kudai ni Wabara wanaosababisha Wazanzibari kukosa ajira. Lakini huo ni mlolongo tu wa shutuma za aina hiyo, kwani huko nyuma Wabara walishawahi kutuhumiwa kuwa ndio waliopelekea ukimwi Visiwani humo.
Kwa vile hadi wakati huu ninaandaa makala hii bado hali huko Visiwani haijatulia, naomba nihitimishe kwa kutoa pendekezo la umuhimu wa kuwa na kura ya maoni itakayofidia kosa lililofanywa huko nyuma la kusaka ridhaa ya wananchi kuhusu Muungano.
Kama kura hiyo ya maoni itaamua tuwe na serikali tatu, basi hilo liheshimiwe. Kama itaamuliwa Muungano uvunjwe, basi na iwe hivyo (by the way, kuvunjika kwa Muungano hakutomaanisha kufa kwa Tanzania Bara au Zanzibar, kama ambavyo kuvunjika kwa ndoa hakumaanishi kifo kwa mume au mke aliyetalikiana na mwenzie).
Mwisho kabisa, wakati nikiwasihi viongozi wetu kuharakisha kura ya maoni ninayoamini itasaidia kuleta ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya Muungano wetu, ni muhimu kabisa kwa Serikali zote mbili (ya Muungano na ya Zanzibar) kuchukua hatua kali dhidi ya magaidi waliogeuza ‘madai halali kuhusu Muungano’ kuwa sababu ya kuwashambulia Wabara na kuchoma moto makanisa na mali zake.
Wanachofanya wahalifu hawa hakilengi kusaka suluhu ya Muungano bali wanapenda mbegu za uhasama wa kidini kati ya Wakristo na Waislamu.
Mungu Ibariki Tanzania





FRIDAY, JUNE 1, 2012


#ZANZIBAR REVEALED

 kuna dhana ya kuwa karume aliuawa kulinda muungano, mazingira yote ya kuuawa kwa karume haiihusishi tanganyika kwa namna moja ama nyengine katika mauaji hayo na kwamba ni wananchi walichoshwa na serikali yao. kinachotokea leo zanzibar, ni msingi mbovu wa utawala wa tokea awali na kamwe tanganyika isihusishwe. 

jarida moja la kila mwezi 'Africa Events' la Agosti 1992 (uk. 27) ,linadai sababu za kuuawa kwa Karume zilikuwa za kibinafsi kwa njia ya kulipa kisasi. Inaelezwa kwamba Muhammed Hamud, mtoto wa Hamud Muhammed Hamud, aliyetiwa kizuizini miezi michache baa­da ya mapinduzi ya 1964 akituhumiwa kutaka kuipindua Serikali ya Karume.
Miaka, rnichache baadaye, Luteni Hamud Muhammed Hamud akiwa katika mafunzo ya kijeshi huko Tashkent (Urusi ya zamani), aliambiwa na mwanafun­zi mwenzake kwamba mzee Hamud alinyongwa na Karume akiwa kizuizini hila kufunguliwa mashtaka. Kwa taarifa hiyo, Luteni Hamud alisikika akiapa ange­muua Karume akirejea Zanzibar.
Taarifa ya kusudio la Hamud la kuua ilifikishwa kwa vyombo vya usalama Visiwani na wenzake, lakini hakukamatwa wala kuwekwa wa chini ya uchunguzi mkali ali­porejea Zanzibar; badala yake ali­pandishwa cheo kuwa luteni na Karume mwenyewe.
Jarida hili halisemi lolote juu ya raja Ali Khatibu Chwaya na ko­plo mwingine juu ya kushiriki kwao katika mauaji haya. Hata hivyo,. Kushiriki kwao kunaelekea kutetea dhana ya pili kwamba kwa sababu Serikali Karume ilishindwa kukidhi matarajio ya Wazanzibari wengi, hapakuwa na njia mbadala ila kumwondoa Karume ili kuleta mabadiliko.


Hapa panazuka swali; kama lengo la Hamud la kumuua Karume lilikuwa kulipa kisasi, kwa nini tukio hili lilihusisha watu zaidi ya mmoja? Si hivyo tu; kwa nini watu zaidi ya 1,000 walikamatwa kutokana na mauaji hayo kama haukuwa mpango mpana?
Dhana ya kulipiza kisasi inapungua nguvu kwa kushindwa kusimama kwa miguu miwili. inatuacha njia panda wakati huo ikijaribu kumezwa na dhana mpango wa mapinduzi, kama ilivyodai Serikali.
Inadaiwa kuwa mpango kuipindua, Serikali ya Karume ulibuniwa mwaka 1968 na wanharakati wa mapinduzi ya 1964 wakiwemo raia  na Wanajeshi wachache.
Inasemekana kikao cha mwisho cha mpango huo kilifanyika Aprili 2, 1972 nyumbani kwa Luteni Hamud, ambapo ilikubaliwa kwamba mauaji hayo yafanyike Aprili 7, 1972.
Mpango wa utekelezaji ulikuwa kwamba Hamud na Ahmada wachukue jukumu zito sana la kuiba silaha kutoka Kambi ya Jeshi yaBavuai.


Katika kutekeleza mapinduzi hayo, ambayo mipango na operesheni yake ilifanana kabisa na ya mapinduzi ya 1964, mtu mmoja, Suleiman Sisi, alipewa jukumu la kuongoza mashambulizi kwenye Kambi ya Jeshi la Mtoni na Ahmada alipewa jukumu la Kambi ya Bavuai, Makao Makuu ya Jeshi la Chuo cha Jeshi la Ma­funzo ya Redio ambazo zote ziko eneo la Migombani.


Kambi ya Ubago haikupangi­wa mtekaji kwa kuamini kwamba kama kikosi cha Ahmada kingeweza kuziteka sehemu kili­chopangiwa, Ubago ingesalimu amri sawia.


Kituo cha Polisi Malindi kingetekwa na kikosi ambacho kingeongozwa na Hamud, am­bapo magari yenye redio za mawasiliano yangepatikana kwa watekaji. Ilipangwa kuwa wakati mashambulizi haya yakiendelea, kituo cha Polisi Ziwani kingevamiwa na askari polisi walitarajiwa kuajiriwa na kuongozwa na askari Yusuf Ramadhan.


Mtu mwingine, Amour Dughesh, alipangwa kuteka Ikulu na alipewa jukumu lakumkamata­Karume na kumpeleka Kituo cha Redio kutangaza kupinduliwa kwa Serikali rake.


Inaelezwa pia kwamba baada ya redio kutekwa, ingewekwa chi­ni ya udhibiti wa Badawi Qual­letein, Miraji Mpatani na Ali Mtendeni. Uwanja wa Ndege ungedhibitiwa na Ali Sultan Issa, ambapo Makao Makuu ya Umoja wa Vi­jana wa AS P (ASPYL) yangetekwa na Baramia.


Makao Makuu ya ASPYL ya­likuwa Kituo Kikuu cha Mkuu wa Usalama wa Ndani ya Serikali ya Karume, Kanali Seif Bakari. Kanali Bakari aliongoza kikun­di cha ukatili kilichojiita kamati ya watu 14, kilichotesa na kuua waliodhaniwa wapinzani na Karume. Abdulrahman Mo­hammed Babu, akiandikia jarida la kila mwezi 'CHANGE' (Vol 4 No. 7,) la 1996, ukurasa 11, anakiri:- "Kutaja pekee jina la Kamati ya Watu 14 kulitosha kumtia mtu woga na kutishika”.


 Kamati hii ili­husika na mauaji ya mamia ya Wazanzibari wasio na hatia, waki­wemo, viongozi, wana’mapinduzi wa kimaendeleo kama Abdallah Kassim Hanga, Abdulaziz Twala, Saleh Saadala, Othman shariff na wengine wale waliuawa kwa jina la Karume."


Abdallah Ameir alipewa jukumu la kuzuia mashambulizi kutoka nje siku hiyo yamapinduzi.
Inadaiwa kuwa katika kikao hicho, Aprili 2, 1972 mtu mmoja, Amar Salim Kuku, alidokeza kuwa Ali Salim Hafidh ambaye nafasi yake haikutajwa katika mpango wa mapinduzi wa Aprili 7, angefi­ka Zanzibar na Abdulrahman Babu na wafuasi wake wa Dar es salaam, usiku wa Aprili 6 kwa mtumbwi kuungana na wanamapinduzi wengine.


Ukiwaondoa Luteni Hamud na Kepteni Ahmada katika mpango huu, na kama ni kweli kwam­ba mpango wote ilikuwa jaribio la mapinduzi (coup d'etat) kama ilivyodai Serikali ya Zanzibar, 'basi staili ya mpango huo haiwezi kut­ofuatishwa na ile ya mapinduzi ya umwagaji damu ya Aprili 12, 1964 ,ambao haukuhusisha jeshi.
Mapinduzi ya 1964 ya kushtukizwa dhidi ya utawala wa Sultan Jamshid na majeshi yake, yali­fanikiwa kwa sababu ya utawala huu kujitenga mbali na wananchi, hivyo haikuweza kupata taarifa za mipango ya mapinduzi hayo mapema.


Na kama ni kweli ilivyosema Serikali ya Zanzibar, kwamba mpango wa mapinduzi ya 1972 uli­buniwa tangu mwaka 1968, ilikuwaje JWTZ na Usalama wa Taifa, achilia mbali kikosi cha Us­alama wa Ndani cha Karume (Gestapo), kilichoongozwa na Kanali Seif Bakari kisibaini mapema hadi siku ya kupoteza uhai wa Kiongozi wa.taifa hilo?  Je, si kweli kwamba historia ya 1964 ilikuwa ikijirudia?


Haya yanaweza kuwa maoni ya wengi, wakiwamo wachunguzi wa mambo ya siasa. Mwanazuoni mahiri barani Afrika, Ali Mazrui anabainisha katika kitabu chake 'Africa's International Relations' (uk. 11); "ukizingatia jinsi Sheikh Abeid Karume alivyoitawala Zanz­ibar kwa ukatili na ubaguzi mkubwa, lolote lilitarajiwa kutokea kwake; hakuna aliyetarajia kwam­ba angedumu kwa miaka minane madarakani. Ndiyo maana hati­maye wengi hawakushangaa alipouawa mwaka 1972."

27 May 2012

Naomba kuwaletea toleo la tatu la mfululizo wa Makala za Sauti.Kamanilivyobainisha katika matoleo mawili yaliyopita,hadi sasa bado nipo katika hatua ya majaribio.Ninafanya kila linalowezekana kupata vitendea kazi bora kabisa(ikiwa ni pamoja na softwares mwafaka) ili kukupatia wewe msikilizaji ubora unaostahili.

Katika toleo hili ninazungumzia Vurugu zinazoendelea huko Visiwani Zanzibar na sualazimala Muungano kwa ujumla.Kwa hakika,kiwango cha ubora wa makala hiyo bado sio cha kuridhisha,na pia sijapata kujiamini vya kutosha katika uwasilishaji wa mada husika (kwa mfano kutumia muda kidogo kuamua nitumie neno gani) lakini huu ni mwanzo,na ninadhamiria kwa zaidi ya asilimia 100 kuwa muda si mrefu nitawaletea kitu bora kabisa na mnachostahili kwa dhati.

Labda la mwisho ni kwamba ninafanya kila linalowezekana ili toleo zima la makala husika liwe kwa lugha ya taifa,yaani Kiswahili.Hiyo ni moja ya sababu ya wakati flani kuwa ninahangaika nitumie nheno gani mwafaka la kiswahili.Si kwamba nimesahau lugha yangu ila moja ya madhara ya kuwa huko nje kwa muda mrefu ni hilo.

Karibuni sana,na msisite kunitumia maoni (chagua player yoyote kati ya hizi mbili hapa chini)
 


28 Nov 2010


Waislam wakiwa kwenye swala.Picha hii haihusiani moja kwa moja na habari ifuatayo
Waislam wenye msimamo mkali wanashukiwa kuyachoma moto majengo mawili ya kanisa huko Zanzibar,tukio lililotokea Jumapili iliyopita huku waumini wa makanisa hayo wakipokea vitisho vya kuuawa.

Majengo hayo ya Kanisa la Assemblies of God (TAG) na Evangelical Assemblies of God Zanzibar (EAGZ) katika kijiji cha Masingini kilichopo kilomita 5 kutoka mjini-kati Zanzibar yalichomwa moto takriban saa 2 usiku,kwa mujibu wa Askofu Fabien Obeid wa EAGZ.Polisi wa Mwera walipata taarifa ya tukio hilo kesho yake asubuhi.

Matukio hayo ni mwendelezo wa vitendo vya kuwatisha Wakristo katika eneo hilo lenye Waislam wengi,na kuibua hofu kwamba Waislam wenye msimamo mkali wanaweza kudiriki kufanya lolote lile kuzuwia ustawi wa Ukristo.

“Muislam mmoja alisikika akisema, ‘Tumesafisha eneo letu kwa kuharibu makanisa mawili,na sasa tuna mpango wa kuwaua waumini wa makanisa haya mawili-hatutaruhusu kanisa kujengwa tena,’” alisema muumini mmoja wa kanisa ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe.

Jengo hilo la matofali la TAG lilikuwa katika hatua za mwisho za ujenzi,na kwa mara ya kwanza Jumapili hiyo waumini walifanya ibada katika jingo hilo jipya.Jengo la EAGZ ambalo waumini takrban 30 walihudhuria ibada lilikuwa la udongo.

Pasta Michael Maganga wa EAGZ na Pasta Dickson Kaganga wa TAG walieleza hofu yao kuhusu hatma ya kanisa hapo Masingini.Mapasta wa Zanzibar walitarajiwa kukutana jana (Jumamosi) kujadili namna ya kukabiliana na uharibifu huo,alieleza Mwenyekiti wa Usharika wa Mapasta Zanzibar,Askofu Lonard Masasa wa Kanisa la EAGT.

Kwa muda mrefu Waislam wenye msimamo mkali visiwani Zanzibar,wanaoungwa mkono na baadhi ya viongozi wa serikali katika maeneo husika,wamekwaza uwezekano wa Wakristo kupata ardhi kwa minajili ya ujenzi wa majengo ya ibada.Kuna nyakati ambapo wamebomoa majengo yaliyopo na badala yake kuanzisha ujenzi wa misikiti.

Huku wakikanganywa na kutopata ushirikiano wa serikali katika kuwashughulikia wahusika wa matukio hayo,viongozi wa makanisa wameeleza kuwa uwezekano wa waliochoma moto majengo hayo kukamatwa ni mdogo.Mara nyingi,serikali huegemea upande wa wanaofanya matukio hayo,kuchelewesdha uchunguzi kwa hofu ya kuwaudhi Waislam walio wengi ambao wanapinga kuenea kwa Ukristo.

Mwaka jana,maafisa wa serikali katika eneo la Mwanyanya-Mtoni waliungana na Waislam wa eneo hilo kujenga msikiti katika eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa kanisa la EAGZ,alieleza Pasta Paulo Kamole Masegi.

Pata Masegi alinunua ardhi mwezi Aprili mwaka 2007 kwa ajili ya ujenzi wa kanisa katika eneo hilo la Mwanyanya-Mtoni,na kufikia mwezi Novemba mwaka huohuo tayari kulikuwa na jengo lililotumika kama sehemu ya ibada kwa muda.Muda si mrefu Waislam wa eneo hilo walipinga hatua hiyo.

Mwezi Agosti mwaka jana,Waislam hao walianza ujenzi wa msikiti futi tatu tu kutoka kitalu cha kanisa.Mwezi Novemba mwaka huohuo,Pasta Masegi alianza ujenzi wa kanisa la kudumu.Waislam wenye hasira walivamnia eneo hilo na kubomoa msingi wa jengo hilo,alieleza Pasta huyo.

Viongozi wa kanisa waliripoti tukio hilo kwa polisi,ambao hawakuchukua hatua yoyote- na walikataa kutoa ripoti ya tukio,hivyo kukwamisha suala hilo kufikishwa mahakamani,alisema Pasta Masegi.

Wakati huohuo,ujenzi wa msikiti ulikamilika mwezi Desemba (mwaka jana).Hatma ya mpango wa ujenzi wa kanisa ilielekea kufikia ukomo mapema mwaka huu baada ya Mkuu wa Wilaya Ali Mohammed Ali kumfahamisha Pasta Masegi kuwa hana haki ya kufanya ibada katika jengo husika.

Kihistoria, wafanyabiashara wa Kiislam kutoka Ghuba ya Uajemi walifika visiwani Zanzibar mapema karne ya 10 baada ya kusukumwa na pepo za monsoon katika Ghuba ya Aden.Muungano wa visiwa hivyo na Tanganyika mwaka 1964 (na kuunda Tanzania) uliwaacha Waislam visiwani humo wakiwa na hofu kuhusu Ukristo,wakiuona kama njia inayoweza kutumiwa na Tanzania Bara kuwatawala,na tangu wakati huo kumekuwa na hali ya mashaka.


14 Feb 2009

HEBU KWANZA MSIKILIZE KIONGOZI HUYU WA UMMA HUKO ZENJI ANAVYOJITETEA DHIDI YA WITO WA KUMTAKA AJIUZULU KISHA TUJADILI KIDOGO:



WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Haroun Ali
Suleiman, amesema haoni sababu ya kujiuzulu wadhifa huo kwa madai ya wanafunzi
wengi Zanzibar kufanya vibaya katika mitihani yao ya kidato cha nne.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, alisema utamaduni kama huo haupo Zanzibar na
wangejiuzulu mawaziri wengi wa elimu waliopita akiwamo Katibu Mkuu wa CUF,
Maalim Seif Sharif Hamad.

Waziri Suleiman ametoa kauli hiyo huku kukiwa
na malalamiko kutokana na matokeo mabaya ya mitihani, huku baadhi ya wanasaisa
wakimtaka awaombe radhi Wazanzibari na kutangaza kuwajibika kutokana na
kusimamia vibaya sekta hiyo.

Alisema
kimsingi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inapaswa kupongezwa kutokana na
mafanikio inayopata katika sekta ya elimu, ikiwamo kuongezeka kwa shule za
serikali kutoka sita kabla ya Mapinduzi hadi 134 hivi sasa
.

Inashangaza kuona watu wamekuwa wepesi wa
kulaumu pale matokeo yanapokuwa mabaya, lakini yanapokuwa mazuri hushindwa kumpa
sifa anazostahili.
Tangu kushika wadhifa huo mwaka 2001, kuna
mafanikio makubwa yaliyopatikana kwa vile kiwango cha kufaulu kimeongezeka
kutoka asimilia 77.3 mwaka 2000 hadi asilimia 84.6 mwaka 2007.

Matokeo mabaya yaliyojitokeza mwaka huu si jambo
geni
kwa vile wanafunzi wamekuwa wakifanya vizuri katika baadhi
ya wakati na mara nyingine kufanya vibaya. Akiwa ameshikilia takwimu za kufaulu
wanafunzi tangu mwaka 1971, alisema hata yeye hakufurahishwa na kiwango cha
kufaulu kuanguka mwaka huu kutoka asilimia 84. 6 hadi 77.3.

Mwaka 1982
wakati Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, akiwa Waziri wa Elimu
Zanzibar, kiwango cha kufaulu kilishuka zaidi hadi asilimia 64.4.

Haroun
alisema hivi sasa kuna sababu mbalimbali zinazochangia wanafunzi kutofanya
vizuri ikiwamo upungufu wa vitendea kazi, uhaba wa vifaa vya sayansi pamoja na
walimu wa masomo hayo.

Hata hivyo, alisema Serikali ya Zanzibar kwa
kushirikiana na Serikali ya Marekani imeanza kuchukua hatua za kuondoa uhaba wa
vifaa, ikiwamo vitabu vya sayansi na kujenga shule za sekondari 19 ambazo kila
wilaya itanufaika hapa Zanzibar.

Hadi ifikapo mwaka 2010 tatizo kwa
baadhi ya wanafunzi kukaa chini litakuwa limekwisha pamoja na kuwapo uwiano kati
ya idadi ya wanafunzi na walimu katika darasa. Hivi sasa serikali inaendelea na
programu ya kusomesha walimu katika ngazi mbalimbali ambao watatumika kufundisha
katika shule za sekondari.

Hata hivyo, ni kweli Zanzibar inakabiliwa na
wimbi la walimu wanaomaliza katika viwango vya shahada kukimbilia ajira binafsi
zenye maslahi zaidi. Ili kukabiliana na tatizo hilo, serikali imeamua kupitia
utaratibu wa malipo kwa walimu kuyaboresha zaidi.

Juzi Chama cha
Wananchi (CUF) kilisambaza taarifa kwa vyombo vya habari kikimtaka waziri huyo
kuwaomba radhi wazee na vijana wa Zanzibar kwa kushindwa kwake kuinua na kukuza
elimu Zanzibar.



JAPO SIAFIKIANI NA HOJA ZILIZOTOLEWA NA MHESHIMIWA HUYU KUTETEA UNGA WAKE,NASHAWISHIKA KUKUBALIANA NAE KWENYE KAULI YAKE KUWA UTAMADUNI WA KUJIUZULU HAUPO (SI ZANZIBAR TU BALI TANZANIA KWA UJUMLA).HEBU TUANGALIE MFANO WA CHAPCHAP HUKO ATCL,UNADHANI KWANINI HADI MUDA HUU HAKUNA ALIYEJIUZULU?MAJUZI MMOJA WA MANAIBU GAVANA BOT AMETAJWA MAHAKAMANI KUWA ANAHUSIKA KWA NAMNA FLANI KWENYE SKANDALI LA EPA,KWANINI HAJAJIUZULU KUPISHA UCHUNGUZI?BAADHI YA WATENDAJI WALIOTAJWA KWENYE TUME YA MWAKYEMBE HAWAJAJIUZULU HADI LEO,KWANINI?JIBU LISILOHITAJI TAFAKURI NI HILO ALOTOA MUUNGWANA HUYO WA ZENJE:HAKUNA UTAMADUNI WA KUJIUZULU.JE CHANZO NI NINI?KWA MTIZAMO WANGU TATIZO LIKO KWA WALIOWATEUA WA HAO WANAOPASWA KUJIUZULU.UTAMADUNI HUU UMELELEWA NA UKWELI MCHUNGU KWAMBA MTU ANAWEZA KUAMUA KUJIUZULU PINDI ANAPOBORONGA JUKUMU FLANI LAKINI ALIYEMTUA HAONI UMUHIMU WA KUFANYA HIVYO.FRANKLY SPEAKING,UKOSEFU WA UWAJIBIKAJI KATIKA MAONEO MBALIMBALI UNACHNGIWA ZAIDI NA TABIA YA KULEANA NA KUBEMBELEZANA KATI YA MABOSI NA WALIO CHINI YAO.LAITI KUNGEKUWA NA KANUNI KWAMBA "UKIBORONGA ,UNAWAJIBIKA.USIPOWAJIBIKA UNATIMULIWA" BASI SI AJABU TUNGESHUHUDIA WABABISHAJI WENGI WAKIACHIA NGAZI KUEPUKA FEDHEHA YA KUTIMULIWA AMBAYO MARA NYINGI HUAMBATANA NA KUNYIMWA MARUPURUPU YA KUMALIZA AJIRA.



INACHEKESHA (JAPO INAUDHI BAADA YA KICHEKESHO HICHO) KUMSIKIA MUUNGWANA HUYU WA KIZANZIBARI AKIDAI PONGEZI ZA "kuongezeka kwa shule za serikali kutoka sita kabla ya Mapinduzi hadi 134 hivi sasa".HUU NI UGONJWA MWINGINE UNAOSHAMIRI KILA KUKICHA;KUTUMIA TAKWIMU NZURI ZA IDADI NA KUFUMBIA MACHO TAKWIMU MBAYA ZA VIWANGO (QUANTINTY vs QUALITY).HIVI KUONGEZEKA KWA IDADI YA SHULE NI MUHIMU ZAIDI YA UBORA WA ELIMU INAYOTOLEWA KWENYE SHULE HUSIKA HATA KAMA NI CHACHE?




ANASEMA "watu wamekuwa wepesi wa kulaumu pale matokeo yanapokuwa mabaya, lakini yanapokuwa mazuri hushindwa kumpa sifa anazostahili" KANA KWAMBA PAMOJA NA MATOKEO YA MWAKA HUU KUWA MABAYA BADO WIZARA ILISTAHILI PONGEZI KWA VILE ILIFANYA VIZURI MWAKA JANA.UGONJWA ULEULE WA TAKWIMU ZA MAZURI ZINAZOTUMIKA KUFICHA TAKWIMU ZA MABAYA.




SAFARI YA MAENDELEO YA KWELI BADO NI NDEFU SANA HASA KUTOKANA NA MENTALITY YA BAADHI YA WALIOPEWA JUKUMU LA KUTONGOZA KWENYE SAFARI HIYO,KAMA HUYU MUUNGWANA WA ZENJI.

19 Sept 2008

Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi

Wawakilishi Zanzibar wachachamaa kuambiwa hakuna mafuta

Salma Said, Zanzibar
KAULI ya Mtaalamu kutoka Scotland, David Reading, kwamba kuna uwezekano mdogo wa kupata mafuta na gesi asilia katika visiwa vya Unguja na Pemba imewakera mawaziri na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na kumta aifute.

Lakini mtaalamu huyo alisisitiza kwamba yeye akiwa mshauri ni lazima awaeleze ukweli wa mambo, kwani hata makampuni yaliofanya utafiti siku za nyuma kuhusu mafuta walitoa ripoti ambayo haikueleza uhakika wa kuwepo kwa nishati hiyo.

Reading pia alisema kuwa gharama za utafutaji wa mafuta hayo ambayo hayana uhakika ni kubwa mno.

Mtaalamu huyo alikuwa akizungumza katika semina ya siku moja kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi iliyofanyika jana mjini Ugunja.

Reading alisema katika sehemu nyingi zilizogunduliwa mafuta au kuwepo kwa fununu za kuwapo kwa nishati hiyo, gharama yake ilikuwa ni kubwa ambapo ililazimu makampuni kusitisha kazi kwa sababu hiyo.

Matamshi hayo yalionekana kuwachukiza zaidi wajumbe wa Baraza la Wawakilishi ambapo walimtaka mtaalamu huyo kufuta matamshi yake kwa maelezo kuwa tafiti nyingi zilizofanywa katika miaka ya mwanzoni mwa 1950 zilionesha kuwa yapo mafuta ya kutosha ya kibiashara Zanzibar.

Hoja hiyo iliibua hisia za wajumbe hao za siku nyingi na waalipopata nafasi ya kuchangia, walisema kuwa mafuta ya Zanzibar ni kwa Wazanzibari na kamwe yasifanywe kuwa ya Muungano na kusisitiza msimamo wa kutaka kuondolewa kwa sheria inayoelezea kuwa mafuta na gesi asilia kuwamo katika orodha ya mambo ya Muungano.

Wajumbe hao walisema kuwa huenda suala hilo la mafuta linaweza kusababisha machafuko visiwani, kwani uozefu unaonyesha kwamba nchi nyingi zenye mafuta kuzuka mapigano, hivyo wakashauri suala hilo lisiwe chanzo cha machafuko kwa Wazanzibari.

Waziri wa Utalii, Biashara na Uwekezaji, Samia Suluhu Hassan, alionekana kushangazwa na taarifa za Mshauri Mwelekezi na kuhoji: “Kama uwezekano wa kupatikana mafuta Zanzibar ni mdogo kwa nini serikali ya Muungano ilikataa wazo la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kwenye kamati ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi katika kugawana mapato ya mafuta?”

Hata hivyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma, aliwataka wananchi kuipuuza kauli hiyo ya Mshauri Mwelekezi na kuongeza kuwa ikiwa mafuta hayataondolewa katika orodha ya mambo ya Muungano hatajutia kuona Muungano unayumba.

“Kuna msemo wa kihindi…ipasuke ngoma au ichanike lakini tujue moja kuwa mafuta ya Zanzibar ni kwa Wazanzibari na sio ya Muungano,” alisisitiza waziri huyo.

Kiongozi wa Upinzani katika Baraza la Wawakilishi, Abubakar Khamis Bakari kama walivyo wajumbe wengine waliochangia alisema mafuta yasiwe mambo ya Muungano kwani hata kuingizwa kwake haukufuatwa utaratibu unaofaa.

Mwakilishi wa Jimbo la Gando, Said Ali Mbarouk alisema kwamba Wazanzibari wamezoea kukosa, hivyo haitokuwa jambo la kushangaza ikiwa hakutakuwa na mafuta wakati jambo hilo litakapoondolewa katika orodha ya Muungano, kwani hivi sasa hainufaiki na lolote katika suala la gesi asilia.

Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha akifungua semina hiyo aliwasihi wajumbe hao kutumia busara katika kumpa ushauri mtaalamu huyo ili aweze kupata maoni mwafaka na aweze kuzishauri serikali mbili namna bora ya kugawana mapato yatokanayo na utafutaji na ushimbaji wa mafuta.

Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi, Ali Mzee Ali alisema Wazanzibari wanapochangia kwa ajili ya kutetea nchi yao wasionekane kama ni wasaliti au wana nia ya kugombea urais bali wanatelekeza ahadi yao kwa wananchi ya kuwatetea katika baraza hilo.

Akifunga semina hiyo Waziri wa Maji, Ujenzi Nishati na Ardhi, Mansoor Yussuf Himid aliungana na wajumbe wengine wote kwa kutaka kuwa mafuta yaondolewe katika orodha ya Muungano kwani tokea asili hayakuwa hivyo.

Na leo tena,gazeti hilo linaripoti vituko zaidi vya Wazenji

Mafuta Zanzibar: Hata kidogo katika kinibu tutagawana na mengine kujipaka
Na Salma Said, Zanzibar


Wawakilishi wa Zanzibar wamesema "hata kama ujazo wa mafuta yanayoweza kupatikana Zanzibar ni sawa na glasi ndogo ya kupimia pombe (kinibu), mafuta hayo ni mali ya Wazanzibari watagawana ili watakaoweza wajipake mwilini".


Kauli hiyo ilitolewa jana baada ya mshauri, David Reading, kueleza kuwa mafuta yanayowezekana kupatikana kisiwani humo ni kidogo na kupatikana kwake ni kwa gharama kubwa.


Mtaalamu huyo kutoka Uingereza aliitwa kwa ajili ya kuishauri Serikali ya Mapinduzi (SMZ) na serikali ya Muungano namna bora ya kugawana rasilimali itokanayo na gesi na mafuta.


Kauli hiyo ya Reading pia imesababisha wawakilishi kuingiwa na chuki dhidi ya Wazanzibari walio kwenye serikali ya Muungano, wakiwaita kuwa ni vigeugeu mithili ya vinyonga na wasiojali maslahi ya Wazanzibari.


Akitoa maoni yake kuhusu suala la mafuta na gesi asilia kwa mshauri huyo mwelekezi, mwakilishi kutoka Chama cha Wananchi (CUF), Najma Khalfan Juma alisema kuwa hata kama mafuta ya Zanzibar yatakuwa madogo kiasi cha ujazo wa glasi ndogo ya kupimia pombe ya haramu ya gongo (kinibu), Wazanzibari watagawana hata ikiwa kwa ajili ya kujipaka mwilini.


"Hata kama watajipaka mwilini au wengine watatumia kama dawa ya kuchulia misuli, itakuwa bora zaidi kuliko suala la mafuta kuwa la Muungano," alisema.


Naye mwakilishi wa kuteuliwa na rais, Ali Mzee Ali, ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi, alisukumia shutuma zake kwa mawaziri walio kwenye serikali ya Muungano ambao ni Wazanzibari, akiwaita kuwa ni wanafiki na wanaobadilika kama kinyonga.


“Mheshimiwa mwenyekiti kuna wenzetu ambao wamo katika serikali ya Muungano. Wakija hapa (Zanzibar) wanajifanya ni watetezi sana wa Zanzibar, lakini kumbe ni wanafiki,” alilalamika mwakilishi huyo.


"Tabia ya viongozi hao haiwanufaishi Wazanzibari. Viongozi wa Zanzibar wasiwatilie maanani watu wa aina hiyo kwa kuwa wanatanguliza maslahi binafsi.


Baadaye mwakilishi huyo mteule aligeukia vyombo vya habari vya Zanzibar na kusema:


"Kitu cha kushangaza ni gazeti la Asumini ambalo limesajiliwa hapa Zanzibar. Gazeti hili liliwahi kuandika makala ndefu kuelezea umuhimu wa nishati ya mafuta kuwa ya Muungano. 


Jambo hili si sahihi kwani Zanzibar hainufaiki na lolote na mapato ya gesi inayozalishwa Tanzania Bara," alisema.


“Ninalo hapa, waheshimiwa wajumbe, gazeti la Zanzibar Leo ambalo limechapisha makala kama ile iliyotolewa katika gazeti la Asumini. Sijui makala hii imepenya vipi mpaka ikatolewa humu; hilo anajua mheshimiwa (Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma) Shamhuna.”


Gazeti la Asumini na Radio ya Zenj Fm zinamilikiwa na Kampuni ya Zanzibar Media Corporation, ambayo Mkurugenzi wake ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano, Muhammad Seif Khatib.


Mwakilishi huyo alisema mara nyingi wanaojitokeza kutetea maslahi ya Zanzibar wanaonekana wanafanya kampeni ya urais kwa mwaka 2010, huku wengine wakishambuliwa kwa maneno kuwa hawautaki Muungano ama kuwa na ajenda ya siri jambo ambalo anaamini si sahihi.


Ali Mzee aliwataka wananchi na hasa wajumbe wa baraza la wawakilishi kuungana kuwa kitu kimoja katika kutetea maslahi ya Zanzibar na kuachana na watu aliowaita kuwa 'Wazanzibari Maslahi' kwenye serikali ya Muungano.


Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma aliwataka viongozi wa Zanzibar kutoogopa kufukuzwa serikalini kwa kuitetea Zanzibar kwani mara nyingi mtu anapojitokeza kutetea maslahi ya visiwa hivyo, huambiwa kuwa amechafua hali ya hewa kama ilivyokuwa kwa rais wa zamani wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais, Aboud Jumbe Mwinyi.


“Waheshimiwa tusiogope kunyang'anywa magari," alisema. "Wakitunyang'anya sawa, tutatembea hata kwa miguu lakini lazima tuitetea nchi yetu kwa sababu sisi tumeapa kwa katiba hii (katiba ya Zanzibar) na sio ya Jamhuri ya Muungano.”


Akichangia hoja hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- Fedha na Uchumi, Dk. Mwinyihaji Makame alishabihiana na wenzake, akieleza kuwa katika suala la mafuta hakuna dhamira njema kwa Wazanzibari.


Mwakilishi wa Viti Maalumu (CUF), Zakia Omar Juma alisema umefika wakati sasa kwa Wazanzibari kujikomboa kiuchumi kwa kuungana kutetea mafuta yao kwani mara nyingi Zanzibar inapotaka kujikwamua kiuchumi huwekewa vikwazo na serikali ya Muungano.


Mwakilishi wa Jimbo la Ziwani (CUF), Rashid Seif alisema kwamba inaonekana Zanzibar kuna mafuta ya kutosha na ndio maana watu wa Tanzania Bara (Tanganyika) wanang'ang'ania suala la mafuta kuwa la Muungano licha ya kuwa Wazanzibari wenyewe hawataki.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.