28 Aug 2015


KABLA sijaingia kwa undani katika makala hii, ambayo niliahidi katika toleo la wiki iliopita, nitajadili kwa kina kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli, ningependa kumpa pole mwanasafu mwenzangu Johnson Mbwambo, kutokana na wingi wa ujumbe mfupi wa maneno (sms) na vitisho kila anapoikosoa Chadema.
Mimi pia nimekuwa mhanga mkubwa wa tabia hiyo ya kukera ambayo imejitokeza mara baada ya mgombea wa urais kwa tiketi ya Chadema/UKAWA kujiunga na chama hicho. Hali kwangu ni mbaya zaidi kutokana na uwepo wangu mkubwa kwenye mitandao ya kijamii.
Nimeitwa kila aina ya jina na kutukanwa kila aina ya tusi, huku tuhuma kubwa kila ninapoikosoa Chadema au UKAWA ikiwa eti ‘nimenunuliwa na CCM’ au ‘kuahidiwa kitu fulani’.

Kuna ‘wastaarabu’ ambao wananilaumu bila kutumia lugha chafu. Wanadai kuwa mtizamo wa machapisho yangu katika gazeti hili na katika blogu yangu ulikuwa ni kuiunga mkono Chadema na kuikosoa CCM. Sasa wananilaumu kwa vile eti ‘nimewasaliti’ na kwa kuikosoa Chadema au UKAWA, ninaiunga mkono CCM.
Awali suala hili lilinisumbua sana kwa sababu wengi wa watu hawa walikuwa wakiilaumu serikali ya CCM kwa kuja na muswada wa kupambana na uhalifu wa mtandaoni (Cybercrime Bill) na kudai ulilenga kuwanyima uhuru wao wa kujieleza.
Iweje leo watu haohao wafanye kilekile walichokuwa wakiilaumu serikali: kutunyamazisha wenzao wenye mitizamo tofauti nao? Hivi hapa kuna neno sahihi zaidi ya unafiki?
Hatimaye nimefanikiwa kuelewa chanzo cha tatizo hilo ni kipi: kukata tamaa, kuchanganyikiwa, na kukosa mwelekeo.

Chuki kubwa waliyonayo dhidi ya CCM, sambamba na matamanio ya kukiona chama hicho tawala kinaondoka kwa gharama yoyote ile, kumepelekea watu hao kuweka imani isiyo na ukomo kwa mgombea urais kwa tiketi ya chama chao, yaani Lowassa.
Sasa yeyote atakayeongea chochote kile kinachoonekana kupunguza nafasi ya Lowassa kuingia Ikulu anaonekana kama adui wa mabadiliko.
Wakati nimeanza kuzoea matusi na lugha chafu inayoelekezwa kwangu, wasiwasi wangu mkubwa ni hatma (aftermath) ya uchaguzi mkuu katika nafasi ya Rais.
Ninabaki kujiuliza, hivi hawa watu wenye matumaini makubwa kupindukia kuwa mgombea wao ataingia Ikulu, watakuwa katika hali gani iwapo matokeo yatakuwa kinyume?
Je watakubali tu matokeo na kufanya post-mortem kistaarabu au ndio tutajikuta tunarudi katika hali iliyojitokeza huko Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000 (Mola aepushe)?
Sasa niingie kwenye mada ya wiki hii. Kama nilivyoeleza katika makala tangulizi, nchi yetu itaingia katika uchaguzi huku kwa kiasi mazingira ya uchaguzi yakiwa yanaipendelea CCM.
Na pengine hili ndilo kosa kubwa wanalofanya wafuasi wa UKAWA; kutarajiwa matokeo tofauti katika uchaguzi unaofanyika katika mazingira yaleyale ‘yaliyowaliza’ katika chaguzi zilizotangulia.

Kwamba watu wengi wamechoshwa na CCM wala si suala la mjadala. Maelfu kwa maelfu ya watu wanaojitokeza kwenye shughuli za kisiasa za Lowassa sio kuashiria cha umaarufu wa mwanasiasa huyo bali hiyo kiu ya kuoina CCM inatoka madarakani. Lakini busara kidogo tu zatosha kutufahamisha kuwa kutaka kitu na kupata kitu ni vitu viwili tofauti.
Watanzania wengi waliochoshwa na CCM, wanataka kuiona inaondoka madarakani hata kesho. Lakini kuwezesha matakwa hayo yatimie si suala rahisi. Naomba nieleweke hapa, Ninasema SI RAHISI lakini sijasema HAIWEZEKANI.
Kudhani kuwa CCM itaondoka kwa kutumia wanasiasa walewale ambao wamechangia kuwafanya Watanzania wengi watake chama hicho kiondoke madarakani ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu.
Naam, Lowassa anaweza kuwezesha Chadema/UKAWA kuitoa CCM madarakani lakini sababu zilizofanya CCM ichukiwe haziwezi kuondoka.
Kwahiyo faida kubwa iliyonayo CCM ni mfumo wa uchaguzi na kiutawala ambao unakitengenezea mazuri chama chake na yeye binafsi kufanya vizuri katika uchaguzi huo.
Lakini licha ya faida hizo za kimfumo, Magufuli anaingia katika uchaguzi huo akiwa katika CCM ileile iliyoshinda chaguzi zote zilizotangulia, kihalali au la, lakini safari hii inakutana na upinzani ambao Kimsingi umetengenezwa katika mazingira ya ‘zimamoto’.

Jinsi UKAWA ilivyoundwa na maendeleo yake hadi kufikia hatua ya kusimamisha mgombea mmoja, yaweza kuwa ni moja ya vikwazo kwa umoja huo kufanikiwa kwenye uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika takriban miezi mawili na kitu kutoka sasa.
Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Lakini umoja tunaozungumzia hapa ni ule wenye kujengwa katika misingi ya kuaminiana. Tayari Tumeshuhudia Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, akijiweka kando na aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Prof Ibrahim Lipumba akijiuzulu.
Ni rahisi kutoa majibu rahisi, kwa mfano kuwatuhumu wanasiasa hao ni wenye uchu wa madaraka, lakini ukweli ni kwamba ‘kujitenga’ kwao sio tu kuna athari bali pia kunaashiria mpasuko wa aina fulani katika umoja huo.
Kwahiyo Magufuli na CCM kwa ujumla wataingia katika uchaguzi huo wakiwa kitu kimoja, kwa kiasi kikubwa, ilhali UKAWA wakikabiliwa na ‘sintofahamu’ flani, sio tu ya kuhusu Dkt Slaa na Prof Lipumba, bali pia hizi taarifa zinazosikika kutoka katika baadhi ya majimbo ambapo ‘ndoa’ ya vyama hivyo imeshindikana, yaani licha ya kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja, vyama vinavyounda umoja huo vimejikuta vikisimamisha wagombea tofauti.
Jingine limejitokeza katika uzinduzi wa kampeni za CCM Jumapili iliyopita ambapo chama hicho tawala, kama baadhi yetu tulivyotarajia, kimejaribu kujenga picha kuwa Chadema/UKAWA sasa ni kama kikosi cha pili cha CCM (CCM-B).

Magufuli na timu yake wakiweza kujenga hoja za kueleweka kwanini Lowassa na Chadema/UKAWA yake ni sawa tu na CCM ya waasi, kuna uwezekano wa wapigakura kutafuta hifadhi katika ‘jini linalokujua halikuli likakwisha.’CCM ‘halisi’ ni ‘jini’ wanalolijua, na pengine wasingetaka kufanya majaribio kwa ‘jini’ wasilolijua.
Kana kwamba hiyo haitoshi, Magufuli na CCM kwa ujumla wanaweza kurahisishiwa kazi na ‘historia ya mahusiano kati ya Chadema na Lowassa. Kama kuna mwanasiasa wa CCM aliyeandamwa mno na Chadema kuhusu tuhuma za ufisadi basi si mwingine bali Lowassa.
Kwa kuzingatia muda uliopo, kati ya mwanasiasa huyo kuhama CCM na kujiunga na Chadema na tarehe ya uchaguzi mkuu, yayumkinika kuhitimisha kuwa ni vigumu mno kumsafisha.

Kimsingi, Chadema/UKAWA wamejiambukiza tatizo walilokuwa wakilipiga vita kwa nguvu zao zote. Hakuna ubishi kuwa mafanikio ya chama hicho kikuu cha upinzani yalichangiwa zaidi na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi.
Sasa leo hii wakisimama jukwaani sio tu na mwanasiasa anayetuhumiwa kujihusisha na ufisadi lakini pia Chadema wenyewe walimwandama kwa tuhuma hizo, kisha wajaribu kumsafisha au kukemea ufisadi, ni mkakati wenye dalili ya kutokuwa na mafanikio.
Awali kulikuwa na hisia za ‘mafuriko ya Lowassa’ kuikumba CCM, kwa maana ya wanasiasa wenye nguvu ndani ya chama hicho tawala kumfuata huko Chadema/UKAWA.
Kuna wawili watatu waliohama lakini si wenye ushawishi au nguvu kubwa ya kuiathiri CCM. Na tayari CCM, imewashusha hadhi na kuwaita ‘makapi’ sambamba na kujenga picha kuwa ni wenye uchu wa madaraka.
Kuhama kwa Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, kutoka CCM na kujiunga na UKAWA kunazidi ‘kuchanganya madawa.’ Kubwa zaidi ni kile kilichoonekana kuwa uhasama wa muda mrefu kati ya wanasiasa hao.
Wakati hii ingeweza kuwa turufu kubwa kwa UKAWA, kuwa na mawaziri wakuu wa zamani wawili ndani ya upinzani, lakini tayari zimeanza kusikika tetesi kuwa “Sumaye ameingia UKAWA kama ‘Plan B’ endapo lolote litamtokea Lowassa kiafya.”
Lakini makala hii si ya kuzungumzia mapungufu ya Chadema/UKAWA bali ni kumjadili Magufuli, japo ni vigumu kuzungumzia fursa alizonazo za kuibuka mshindi kwenye uchaguzi mkuu pasipo kujadili ‘urahisi’ unaotokana na kinachoendelea huko UKAWA.
Tukiweka pembeni niliyobainisha hapo juu, matumaini kuwa urais wa Magufuli utakuwa tofauti na huu wa Rais Jakaya Kikwete ni mdogo.
Hilo nilishaliongelea huko nyuma, ambapo yayumkinika kudhani kuwa mgombea huyo wa chama tawala anaweza kuwa na deni la fadhila kwa mtangulizi wake, hasa kwa kuzingatia ‘mahesabu’ yaliyofanyika katika machakato wa CCM kumpata mgombea wake.
Laiti Chadema/UKAWA wasingekuwa na kibarua cha kumsafisha mgombea wao, Lowassa, wangeweza kuwa katika nafasi nzuri kujenga picha kwa wapigakura kuwa miaka mitano ya utawala wa Magufuli haitokuwa tofauti na kumi ya Kikwete, na pengine kupigilia mstari kuwa mengi ya yaliyojiri katika utawala uliopo madarakani yanamhusu mgombea huyo wa CCM pia.
Hata hivyo, iwapo jitihada za kumsafisha Lowassa na kumtenganisha na CCM zitafanikiwa, basi UKAWA na mgombea wao wanaweza kufanya vizuri.
Mwisho, kama kuna kitu kinachoweza kuigharimu CCM na Magufuli ni kupuuzia ukweli kuwa kuna wapigakura wengi wamepoteza imani kwa chama hicho.
Na laiti mwenendo wa kampeni za Magufuli utafuata ‘busara’ za Rais mstaafu Benjamin Mkapa kutumia lugha isiyo ya kistaarabu ya ‘mpumbavu na lofa’ basi sintoshangaa kuona Lowassa akinufaika na ‘kura za huruma’.

Ni muhimu kwa CCM kuongoza kwa mfano ikiwa ni pamoja na kuachana na kampeni za chuki au za ‘utoto wa kisiasa’ (political immaturity), iwaeleze Watanzania wapi ilipokosea hadi baadhi yao kutamani iondoke madarakani, na nini itawafanyia kurekebisha makosa yake.

20 Aug 2015

KAMA nilivyoahidi katika makala iliyopita, wiki hii ninaendelea na uchambuzi wangu kuhusu Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Na kama ilivyokuwa katika makala kadhaa zilizotangulia, uchambuzi wangu utaelemea kwenye kinyang’anyiro cha nafasi ya urais.
Wakati katika makala iliyopita nilijadili fursa na vikwazo kwa wagombea ‘wakuu’ wawili, yaani Dk. John Magufuli wa CCM na Edward Lowassa wa Chadema/UKAWA, wiki hii nitaingia kwa undani zaidi, huku lengo likiwa kuitumia makala hii kufanya uchambuzi kwa mgombea mmoja, na makala ya wiki ijayo itamwangalia mgombea mwingine.
Nianze na Lowassa wa Chadema/UKAWA. Kati ya makala iliyopita na hii, si siri kuwa habari inayotawala zaidi ni kile kinachoitwa ‘mafuriko ya Lowassa’. Shughuli zote zilizomhusisha mwanasiasa huyo katika kipindi hicho kimeandamana na umati mkubwa mno wa watu, kuanzia alipochukua fomu za kuwania urais jijini Dar es Salaam hadi katika mikutano ya kutambulishwa huko Mbeya, Arusha na Mwanza.
Wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli zinazomhusu Lowassa, iwe ni kwa kuandamana au kuhudhuria mikutano, kumewapa matumaini makubwa wafuasi wake kwamba njia ya Waziri Mkuu huyo wa zamani kuelekea Ikulu ni nyeupe.
Sambamba na mahudhurio hayo makubwa, wanachama kadhaa wa CCM wamehama chama hicho tawala na kujiunga na Chadema. Lakini kubwa zaidi ni kuhama kwa baadhi ya viongozi ‘ waliokuwa na majina’ ndani ya CCM.
Kwamba maandamano na mikutano ya Lowaasa inajaza watu wengi mno, hilo halina mjadala. Kwamba matukio yajayo ya mwanasiasa huyo yataendelea kujaza watu pia si suala la mjadala. Kadhalika, kwamba kuna wanachama na viongozi zaidi wa CCM watamfuata Lowassa huko Chadema pia ni jambo la kutarajiwa.
Tusichoweza kuhitimisha kwa uhakika muda huu ni iwapo hamahama hiyo ya baadhi ya wana-CCM na viongozi wao kumfuata Lowaasa huko Chadema itaweza kutafsiriwa katika ushindi katika uchaguzi mkuu ujao hapo Oktoba 25, takribani miezi mawili kutoka sasa.
Licha ya uwepo wa hamasa kubwa kuhusu kujiandikisha katika daftari za wapigakura lililoboreshwa na teknolojia ya kuhifadhi rekodi kwenye kompyuta (Biometric Voter Register kwa kifupi BVR), hadi muda huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi haijatoa idadi kamili ya watu waliojiandikisha.

Lakini licha ya hilo, tayari kuna dalili za kasoro katika suala la BVR ambapo zimepatikana taarifa kadhaa za waliojiandikisha kutoyaona majina yao wakati wanaofanya uhakika. Ukubwa au udogo wa kasoro hiyo bado haujafahamika kwa vile Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haijalitolea ufafanuzi suala hilo.
Hapa nitaunganisha masuala hayo mawili ya hapo juu, yaani idadi kubwa ya watu wanaojitokeza katika shughuli za Lowassa na zoezi la kujiandikisha BVR.
Yayumkinika kuhitimisha kuwa ili wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli za mwanasiasa huyo ziwe na manufaa kwake na chama chake kwa ujumla, basi, kwanza wengi wa watu hao, kama si wote, lazima wawe wamejiandikisha kupiga kura. Bila hivyo wingi wao utabaki kuwa historia tu.
Lakini kwa uzoefu tulionao wengi, kujiandikisha kupiga kura ni suala moja, kufanikiwa kupiga kura ni suala jingine, na kumpigia kura mgombea fulani na kura hiyo kumsaidia ashinde ni suala jingine kabisa.
Nimeshazungumzia katika makala zangu zilizotangulia kuwa moja ya faida kubwa kwa CCM ni mahusiano ya upendeleo kati yake na taasisi mbalimbali za umma. Na ninatarajia wengi wenu ndugu wasomaji mmekuwa mkisikia vilio vya wanasiasa wa upinzani takribani tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi kwamba wanaohisi kura zao zinahujumiwa na chama tawala kwa kusaidiwa na taasisi za umma ‘zinazokipendelea’ chama hicho.
Japo mara zote tuhuma hizo zimeendelea kubaki kuwa tuhuma tu, ushahidi wa kimazingira unaelekea kuzisapoti tuhuma hizo.
Binafsi, nimekuwa nikifuatilia pilika za uchaguzi mkuu kupitia mtandaoni, hususani kwenye mitandao ya kijamii (social media). Majuzi, niliwatahadharisha mashabiki wa Lowassa kuhusu furaha yao inayotokana na wingi wa wahudhuriaji katika shughuli za hadhara zinazomhusu mwanasiasa huyo.
Niliwakumbusha kuhusu chaguzi zilizopita, hususan ‘kasi ya (Agustino Lyatonga) Mrema,’ aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 kupitia chama cha NCCR-Mageuzi, jinsi alivyokuwa maarufu na kujaza halaiki ya watu kwenye mikutano yake, lakini akaishia kubwagwa na mgombea wa CCM, Benjamin Mkapa.
Niliwakumbusha pia kuhusu wingi wa watu waliojitokeza katika mikutano ya kampeni za Dk. Willibrord Slaa, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi mkuu uliopita, mwaka 2010, lakini akishindwa na mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete.
Katika chaguzi zote hizo, pamoja na ule wa mwaka 2000 na 2005, kulikuwa na malalamiko kdhaa kuwa ‘CCM iliiba kura,’ lakini tuhuma hizo zilijifia zenyewe kutokana na kutokuwepo ushahidi halisi, sambamba na vikwazo vya kikatiba kupinga matokeo ya Urais.

Lakini kukumbushia yaliyojiri katika chaguzi hizo kulipelekea mimi kushambuliwa vikali, nikituhumiwa kuwa na ‘chuki binafsi’ dhidi ya Lowassa, huku wengine wakinituhumu kuwa nimenunuliwa na CCM. Na nikakumbushwa kuwa “nenda na wakati, hii ni 2015, achana na habari za 1995”.
Siwezi kuwalaumu watu ambao hawataki kusikikia lolote ‘baya’ kuhusu Lowassa, au jambo linaloweza kuwa kikwazo kwake kupata urais.
Kwa bahati mbaya, ujio wa mwanasiasa huyo huko Chadema unaoonekana kuwabadili wana-Chadema wengi, angalau huko mtandaoni, ambapo watu waliokuwa wakijadili hoja kiungwana, sasa wamekuwa mahiri wa matusi kwa kila anayeelekea kumpinga Lowassa.
Nitawalaumu kwa matumizi ya matusi badala ya kujenga hoja za kistaarabu, lakini sintowalaumu kwa kuwa ‘desperate.’ Wanasema mtu akielemewa na mafuriko basi atang’ang’ania hata unyasi ili ajiokoe.

CCM imewafikisha Watanzania wengi katikia hali hii tunavyoshuhudia. Sapoti kubwa kwa Lowassa sio kwa vile ni mchapakazi au anatarajiwa kuleta ‘miujiza’ bali ni kukata tamaa miongoni mwa Watanzania wengi, Tunasikia watu wakisema “ukiiweka CCM na jini, nitapiga kura yangu kwa jini”.
Lakini wakati kuwa na matumaini yanayotokana na kukata tamaa si tatizo sana, ni muhimu kuzingatia hali halisi. Kuna wanaodai ‘safari hii CCM haiwezi kutuibia kura’ Je kuna tofauti gani ya kimazingira ya uchaguzi katika ya mwaka huu na uchaguzi mkuu wa mwaka 1995,2000,2005 na 2010? Tume ya uchaguzi ni ileile, taasisi mbalimbali za umma zinazoshughulikia uchaguzi huo bado zipo vilevile, na vyombo vyetu vya dola bado vina ‘mentality’ ileile ya kuwaona Wapinzani kama wahaini, na hata Lowassa amekiri kuwa alipokuwa CCM alidhani vyombo vya dola vyalaumiwa bure tu na Wapinzani…hadi alipoonjeshwa ‘jeuri ya polisi’ hivi majuzi.
Lakini tukiweka kando kuhusu tatizo hilo ambalo niliona kama la kimfumo, yaani mfumo unaoipendelea CCM, kuna tatizo jingine ambalo pengine halijawa kubwa sana. Hili ni uwezo mdogo wa Lowassa katika kujieleza.
Unapofanikiwa kukusanya umati wa maelfu ya watu, kisha ukahutubia kwa dakika tano, na katika muda huo mfupi usiseme lolote la maana la kuwafanya waliohudhuria wakumbuke si ukubwa wa umati bali uzito wa hotuba ya aliyewajaza kwa wingi mahala husika, basi hapo kuna tatizo.
Na tatizo hili laweza kuwa turufu kwa mgombea wa CCM, Dk. Magufuli, ambaye anasifika kwa umahiri si tu wa kuongea bali kutoa takwimu nyingi kichwani kana kwamba ni mashine yenye kumbukumbu (memory) kubwa.
Ukizungumzia hilo kwa wana-Chadema/UKAWA, wanasema “nani anataka hotuba? Sisi tunachotaka ni kuondoa CCM tu”. Ninabaki ninajiuliza, “hivi wakifanikiwa ukiondoa CCM, nini kitafuata?” Sipati jibu.
Kwa kifupi, kinachowapa matumaini wana-Chadema/UKAWA na mashabiki wa Lowassa ni hayo ‘mafuriko.’ Iwapo yataweza kujitafsiri katika kura, muda utatupatia jibu (time will tell).
Na iwapo ‘mafuriko’ hayo yatamwezesha Lowassa kuingiza Ikulu, ninadhani hata wana-Chadema/UKAWA wengi hawajui jinsi gani atakavyowezesha kubadili kile kinachowafanya Watanzania wengi wachukizwe kuhusu CCM.

Kwa upande mmoja, kuahidi mabadiliko ni kitu kimoja, kutekeleza ahadi hiyo ni kitu kingine. Kwa upande mwingine, kuwa na nia ya kuleta mabadiliko ni kitu kimoja, uwezo wa kufanikisha nia hiyo ni kitu kingine, na hata pale nafasi ya kuleta mabadiliko inapopatikana, nyenzo na mazingira vyaweza kuwa kikwazo cha kutimiza azma hiyo.
Nihitimishe makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo ambapo nitamzungumzia mgombea wa CCM, Dk. Magufuli kama nilivyomjadili Lowassa katika makala hii.

13 Aug 2015

MAKALA hii ni mwendelezo wa ile iliyochapishwa katika gazeti hili katika toleo la wiki iliyopita. Katika makala hiyo nilijadili kwa kirefu kuhusu kile nilichokiyumkinisha kuwa usaliti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), si tu kumpokea Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa (aliyelazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu kufuatia skandali ya ufisadi wa Richmond), bali pia kumteua kuwa mgombea wake urais kupitia UKAWA.
Kadhalika, pamoja na mambo mengine, nilieleza kusikitishwa kwangu na kile nilichokitafsiri kama mwelekeo wa siasa za Tanzania yetu kutoka mfumo wa awali wa chama kimoja hatimaye vyama vingi na hiki tunachoshuhudia baada ya Lowassa kujiunga na Chadema, ninachokiita ‘chama cha mtu mmoja.’
Katika makala hii nitajadili nafasi za kufanya vizuri katika uchaguzi mkuu ujao kwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt John Magufuli, na huyo wa Chadema/UKAWA, yaani Lowassa, sambamba na vikwazo vinavyowakabili kila mmoja wao.
Nianze na Magufuli. Kwa kada huyo, binafsi ninaona kuwa ana nafasi nzuri ya kushinda hasa kwa sababu, kama alivyotamka Rais Jakaya Kikwete hivi majuzi, CCM ina uwezo na nyenzo kumwezesha mgombea wao kufanya vizuri. Vyote viwili – uwezo na nyenzo – vimeshathibitika kuwa na ufanisi mkubwa katika chaguzi zilizopita.
Na vyote viwili vipo katika pande mbili; halali na isivyo halali. Uwezo halali wa CCM unatokana zaidi na mitandao wake mpana hasa vijijini. Kwa bahati mbaya au makusudi, licha ya maeneo mengi ya vijijini katika nchi yetu kukabiliwa na umasikini mkubwa, pia yana uhaba wa ‘wasomi,’ huku wachache waliopo wakiwa aidha wamekumbatiwa na ‘mfumo unaoilinda CCM’ au wameukumbatia kwa minajili ya kulinda nafasi zao.
Ninaposema ‘wasomi’ simaanishi maprofesa au watu wenye elimu ya juu bali hata wale wenye elimu ya wastani tu ambao ni muhimu sana katika kuhamasisha na kuleta mabadiliko katika nyanja mbalimbali.
Katika mazingira ya kawaida, mtumishi wa umma kijijini anaweza kuwa na chaguo rahisi ‘kuitumikia CCM’ badala ya chama cha upinzani kwa vile hasa kwa vile katika maeneo mengi ya vijijini, ni vigumu kuitofautisha CCM na serikali.
Kuna tatizo la ziada kuhusu ‘wasomi’ wetu. Wakati katika stadi za matabaka, wasomi wanatarajiwa kuwa sio tu kiungo katika ya tabaka la walalahoi na tabaka tawala, wasomi wetu wengi sio tu hawamtaki kujihusisha na tabaka la walahoi bali pia wanajibidiisha – hata kwa kuiga tu – kuwa sehemu ya tabaka tawala. Na Wasomi wachache tulionao vijijini wanaotaka waonekane kama ‘vigogo’ au ‘vingunge’ badala ya wananchi wa kawaida au walalahoi. CCM inatambua udhaifu huu na kutumia ipasavyo.
Ikumbukwe pia kuwa wengi wa ‘wasomi’ hao ndio watumishi muhimu katika shughuli nzima ya uchaguzi, na yayumkinika kuamini kuwa wamekuwa na ‘msaada’ mkubwa kwa CCM katika chaguzi zilizopita, na wanaweza kuendelea kuwa nyenzo muhimu kwa chama hicho tawala.
Lakini pengine kubwa zaidi ni turufu ya CCM hasa katika maeneo ya vijijini kuwa ‘inaweza kuonyesha jinsi ilivyowatumikia wananchi’ tofauti na ‘vyama vya upinzani vinavyokuja kufanya majaribio ya kuongoza nchi.’ Ni hoja isiyo na msingi kwa wenye uelewa wa kuchanganua mambo, lakini kwa huko vijijini, kuipinga kwahitaji kazi kubwa na sio takriban miezi mawili iliyosalia kabla ya uchaguzi mkuu.

CCM inabaki kuwa ‘zimwi likujualo’ ilhali kwa vyama vya upinzani, tegemeo lao kubwa ni kuonyesha mapungufu ya chama hicho tawala, na kutegemea wananchi watawaelewa na kuwaamini, na ‘kucheza bahati nasibu’ ya kuwakabidhi madaraka.
Ukichanganya na ukweli usio rasmi kuwa CCM ni mnufaika mkubwa wa uhusiano wake na taasisi za serikali – Tume ya Uchaguzi, vyombo vya dola, nk – chama hicho tawala kitaingia katika uchaguzi kikiwa na nyenzo na uwezo wa kushindwa hata kama ni kwa tabu.
Kwa kifupi, mazingira yaliyoiwezesha CCM kushindwa chaguzi kuu zilizopita bado yapo na mfumo wa uchaguzi bado unakitengenezea chama hicho tawala nafasi ya kufanya vizuri.
Hata hivyo, ili Magufuli ashinde, inategemea zaidi mshikamano ndani ya CCM. Na nikiongelea mshikamano simaanishi matukio yanayoanza kujitokeza ya makundi ya wana-CCM kadhaa kuhama chama hicho na kujiunga na vyama vya upinzani. Ninamaanisha wanasiasa wenye nguvu na ushawishi katika chama hicho kumuunga mkono mgombea wa chama chao au kumsaliti.

Lakini tangu Lowassa ajiunga na Chadema/UKAWA, sijaona kile kilichotarajiwa kuwa ‘mafuriko’ ya viongozi muhimu wa CCM na maelfu ya wanachama kukiasi chama hicho tawala na kujiunga na wapinzani. Kwahiyo, yayumkinika kuhisi kuwa hadi muda huu Magufuli bado ana sapoti ya kutosha ndani ya chama chake.
Kanuni isiyo rasmi ya siasa za uchaguzi Barani Afrika ni kwamba ‘chama tawala hakishindwi uchaguzi, na kikishindwa basi si kwa sababu wapinzani wana nguvu kubwa bali migongano ndani ya chama tawala inayotoa fursa kwa wapinzani.’ Sawa, labda CCM kumkata jina la Lowassa wakati wa mchujo wa wagombea wake kumesababisha mpasuko wa aina flani, lakini kama nilivyobainisha hapo juu, mpasuko huo sio mkubwa kama ilivyotarajiwa, na sidhani kama unaweza kuwa na athari kubwa kwa CCM.
Kwahiyo, kwa upande wa Magufuli, takriban mazingira yote yaliyowawezewezesha wagombea wenzake wa nafasi ya urais huko nyuma kufanya vizuri bado yapo ilhali vikwazo dhidi ya yeye kufanya vizuri ni hafifu, na pengine vya kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Twende kwa Lowassa. Mtaji mkubwa wa mwanasiasa huyo ni umaarufu wake. Iwapo umaarufu huo unachangiwa na kinachoelezwa kuwa ni uwezo wake mkubwa wa kifedha au ‘uchapakazi’ wake, hilo ni suala linalohitaji mjadala katika makala tofauti. Lakini kilicho bayana ni ukweli kwamba umaarufu ni turufu muhimu kwa mgombea yeyote yule katika uchaguzi.

Turufu nyingine kwa Lowassa ni hali halisi ilivyo katika mahusiano kati ya CCM na Watanzania wengi. Kwa muda mrefu chama hicho tawala kimekuwa kikichukulia chaguzi mbalimbali, kuu na ndogo, kama utaratibu tu wa kukipatia nafasi za uongozi. Hakijawahi kupigania ‘kufa na kupona’ kubaki madarakani. Kwa sababu nilizozitoa hapo juu, ukichanganya na udhaifu wa wapinzani wake, bila kusahau hujuma mbalimbali dhidi yao, tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi, chama hicho tawala kimekuwa kikiingia kwenye chaguzi kikiwa na uhakika mkubwa wa kushindwa.
Hata hivyo, safari hii kinaweza kukumbana na ushindani mkubwa (japo hadi muda huu ni suala la kufikirika zaidi) baada ya kada wake maarufu kabisa, Lowassa, kujiunga na wapinzani. Sasa kwa vile CCM haijawahi na haijazowea kuwa katika mazingira yaliyopo sasa, yayumkinika kuhisi kuwa inaweza ‘kupaniki’ na hivyo kutoa mwanya kwa Lowassa na Chadema/UKAWA yake kufanya vizuri.
Lowassa na Chadema/UKAWA wanatambua bayana kuwa kuna mamilioni ya Watanzania waliokwishaichoka CCM na pengine wangependa kuoina iking’oka madarakani. Ni rahisi kwa wapinzani hao kubainisha ‘maovu’ ya chama hicho tawala kwa sababu mengi yanaonekana waziwazi. Hata hivyo, ni muhimu kukumbuka kuwa kuna ‘mazuri’ kadhaa ya utawala wa CCM, na uzoefuwaonyesha kuwa chama hicho tawala ni mahiri katika kuyanadi ‘mazuri’ hayo, ambayo pia si vigumu kuyaona.
Kikwazo kwa Chadema/UKAWA ni jinsi ya kubadili maelezo waliyoyasimamia kwa muda mrefu kuwa ‘Lowassa ni fisadi.’ Kwa mitizamo wangu, muda uliosalia haitoshi kwa vyama hivyo vinavyounda UKAWA kuwashawishi Watanzania kuwa ‘Lowassa sasa si fisadi kwa vile amejiunga nasi tuliokuwa tunapambana na ufisadi.’ Na kwa bahati mbaya, hasa kwa Chadema ambayo ilikuwa mahiri kukemea ufisadi, Watanzania wengi tu wanaonekana kutafsiri Lowassa kukubaliwa kujiunga na chama hicho ni usaliti kwa wengi waliokiamini.
Hoja kwamba ili ukiondoa CCM kuna haja ya kushirikiana na watu kama Lowassa inakabiliwa na hoja mbadala kuwa ‘kwanini tuwaamini watu msio na uwezo wa kuleta mabadiliko wenyewe hadi mtegemee makapi ya CCM?’ Hoja hiyo mbadala inapewa nguvu na ukweli kuwa UKAWA ‘walisuasua’ kwa muda mrefu kutangaza mgombea wao, na sasa twajua kuwa walikuwa wanamsubiri mwana-CCM kama Lowassa awasaidie.
Lakini mtihani mwingine kwa UKAWA na Lowassa ni huu: Magufuli anagombea urais kwa tiketi ya CCM, ambayo sio tu ni chama tawala na ambacho kipo madarakani hata kabla ya ujio wa mfumo wa vyama vingi, lakini pia kinafahamika kwa wengi. Kwa UKAWA, na hili ni kosa lao kwa kuchelewa kupata mgombea wao wa kiti cha urais, inaonekana kama ni chama ‘kipya’ cha siasa. Laiti muungano huo wa vyama vinne vya siasa (Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD) ungepata mgombea wake mapema, na kumnadi kwa nguvu wakati CCM inahangaika kupata mgombea wake, basi muda huu wangekuwa na kazi moja tu ya kupambana na Magufuli na CCM kwani wao tayari wangeshakuwa wanajulikana kwa wengi.
Vilevile, kuna suala nililozungumzia katika makala iliyopita ambapo, dalili zilizopo zinaashiria uchaguzi wa rais ni katika ya CCM na Magufuli wake dhidi ya Lowassa. Hapa ninamaanisha kwamba ni rahisi kumwona mgombea huyo wa CCM kama anayewakilisha chama chake ilhali kwa Lowassa ni kama ‘mgombea binafsi.’ Utafiti kidogo tu katika vyombo vya habari waweza kukuonyesha msomaji kuwa wakati ‘kampeni’ za CCM zimeelemea zaidi katika kumnadi Magufuli na CCM, kwa Chadema/UKAWA ni suala la kumnadi Lowassa pekee kana kwamba ni mgombea binafsi.
Na hilo linachangiwa na ukweli kuwa UKAWA si chama bali ushirikiano wa vyma ambavyo awali lengo lao lilikuwa suala la mabadiliko ya Katiba. Vyama hivyo vina sera tofauti, na japo vyawezxa kutengeneza ilani moja ya uchaguzi, muda hauko upande wao. Kwa CCM, ni mwendelezo tu wa walichokifanya mwaka 1995, 2000, 2005 na 2010.
Kadhalika, wakati nimetaja kuwa umaarufu wa Lowassa ni mtaji wake mkubwa huko Chadema/UKAWA, pengine ni mapema mno kuhitimisha kuwa umaarufu huo alioupata akiwa CCM, utaendelea kuwa juu wakati huu amejiunga na Chadema/UKAWA. Ikumbukwe kuwa wapinzani wakubwa wa Lowassa alipokuwa CCM hawakuwa ndani ya CCM bali katika vyama hivyohivyo ambavyo leo vimemfanya mgombea wao wa urais. Hilo laweza kuirahisishia CCM jukumu la kumbomoa kwani ‘wanamjua vilivyo.’
Kikwazo kikubwa lakini kisicho wazi ni nafasi ya Idara ya Usalama wa Taifa katika uchaguzi huo, kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizopita. Hata tukiweka kando kile kwenye Baiolojia wanakiita ‘symbiotic relationship’ (uhusiano wa kutegemeana kati ya kiumbe kimoja na kingine) ambapo ustawi wa taasisi hiyo na wa CCM na serikali zake ni wa kutegemeana, Idara hiyo yaweza kutumia ‘kisingizio’ kama ‘Lowassa ni tishio kwa usalama wa taifa letu,’ ambapo kwa taratibu zisizo rasmi za Usalama wa taifa sehemu nyingi duniani, anaweza ‘kudhibitiwa.’ Hili ni gumu kulieleza kwa undani kutokana na sababu za kimaadili.
Nihitimishe makala hii ndefu kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi zaidi kuhusu uchaguzi mkuu kwa ujumla, hususan katika nafasi ya urais, hasa ikitarajiwa kuwa tunaweza kushuhudia mengi zaidi ya tukio lililogusa hisia za wengi la aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba kujiuzulu ghafla, sambamba na ‘sintofahamu’ kuhusu hatma ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dkt Willibrord Slaa.

6 Aug 2015

NINAANDIKA makala hii nikiwa na masikitiko makubwa mno. Siku zote maishani, twajikuta katika kipindi kigumu sana pale mtu tuliyemwamini kwa dhati anapotugeuka. Wanasema, inachukua muda mwingi na jitihada kubwa kujenga uaminifu japo kosa au tukio moja tu laweza kuondoa kabisa uaminifu huo.
Na hicho ndicho walichofanya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) baada ya kukubali kumpokea Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowaasa, sio tu kuwa mwanachama wao bali pia mgombea wao katika nafasi ya urais.
Kama ambavyo tetesi kuwa Lowassa angechukua fomu kuwania urais kwa tiketi ya CCM zilivyozagaa kwa muda mrefu, ndivyo suala la Lowassa kujiunga na Chadema/ UKAWA lilivyokuwa.
Mara baada ya mwanasiasa huyo kukatwa katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake wa Urais, zilisikika tetesi nyingi kuwa kuna uwezekano angejiunga na moja ya vyama vinavyounda UKAWA, na hatimaye kuwa mgombea urais.
Lakini kwa vile Tanzania yetu haina uhaba wa tetesi, baadhi yetu tulidhani kuna ugumu kwa Lowassa kujiunga na UKAWA ni Chadema, kwa vile chama hicho kimejijengea umaarufu mkubwa kwa msimamo wake tuliodhani ni thabiti kupambana na ufisadi na mafisadi.
Na sio msimamo tu dhidi ya ufisadi na mafisadi, Chadema wamelipa gharama kubwa katika harakati zake ambapo baadhi ya wanachama wake walipoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya, huku wengine wakiishia rumande au magerezani kufuatia maandamano mbalimbali ya kutetea maslahi ya taifa na wanyonge.
Hata nilipoona picha zilizodaiwa kuwa ni za Lowassa akihudhuria moja ya vikao vya UKAWA nilijipa moyo kuwa huenda picha hizo zimefanyiwa ‘ufundi,’ wenyewe wanaita ‘photoshop,’ ambapo picha ya mtu inapandikizwa kwenye picha nyingine.
Faraja iliongezeka baada ya akaunti ya habari za Chadema katika mtandao wa Twitter, Chadema Media, kukanusha uwepo wa Lowassa katika kikao hicho. Hata hivyo muda mfupi baadaye, watu wa karibu na Lowassa walibandika picha zaidi katika mtandao huo kuthibitisha kuwa kweli Lowassa alihudhuria kikao hicho.
Na siku moja baadaye,’bomu lililipuka.’ Kupitia matangazo ya moja kwa moja ya televisheni ambayo sie tulio mbali tuliweza kuyaona mtandaoni, viongozi wakuu wa UKAWA walionekana na Lowassa, na baadaye mwanasiasa huyo kutangaza bayana kuwa amejiunga na umoja huo kupitia Chadema.
Ninachoweza kusema kwa kifupi ni kwamba walichofanya Chadema ni usaliti wa hali ya juu, na hakuna maelezo ya aina yoyote yanayoweza kuhalalisha kitendo hicho. Ndio, ni muhimu kwao kuingia Ikulu, lakini ni muhimu zaidi kwa Chadema kutambua imefikaje ilipo leo.
Jibu la wazi ni kama nilivyotanabaisha hapo juu; msimamo wao imara wa kuuchukia ufisadi na kupambana nao kwa nguvu zote, hatimaye ulifanikiwa kuwafumbua macho Watanzania wengi, sio tu kuhusu kansa ya ufisadi bali pia kujenga hisia kwamba chama hicho ni kwa ajili ya maslahi ya mamilioni ya Watanzania wanyonge na wahanga wakuu wa ufisadi.

Kwahiyo, kwa kumpokea Lowassa, mwanasiasa aliyelazimika kujiuzulu kwa tuhuma za ufisadi wa Richmond, Chadema wametelekeza nguzo muhimu iliyokuwa ikikitambulisha chama hicho. Na kama tunavyoina CCM, chama chochote cha siasa kinachotelekeza nguzo zake, sio tu kinapoteza uaminifu wake kwa jamii bali pia chajichimbia kaburi.
Sawa, labda Lowassa anaweza kushinda urais (hili lahitaji mjadala wa pepe yake) lakini haihitaji kuwa na ujuzi wa uchambuzi wa siasa zetu kubaini kwamba mwanasiasa huyo hakujiunga na Chadema kwa vile anakipenda chama hicho au anaafiki sera zao bali amekitumia kama ngazi ya kuwania urais baada ya kukwamishwa na CCM.
Hilo tu lilipaswa kuifumbua macho Chadema. Lowassa huyohuyo aliyejigamba kwamba jina lake halitakatwa akijivunia ‘uchapakazi’ wake, na utumishi wake wa muda mrefu katika CCM, leo hii kaitelekeza CCM licha ya kudai asiyemtaka ndani ya chama hicho aondoke lakini yeye si wa kuondoka.
Ni wazi kuwa Lowassa ni mwanasiasa mwenye tamaa ya madaraka. Sawa, Katiba yetu yamruhusu kugombea uaongozi kupitia chama chochote kile, lakini moja ya sifa nzuri kwa mwanasiasa ni msimamo na kutokuwa na tamaa ya madaraka.
Leo kaitosa CCM kwa kutaka urais, je ataitendaje Chadema katika kutaka mengineyo?
Lakini pia ni ukweli usiofichika kuwa umaarufu wa Lowassa unatokana na ‘sifa’ kuu mbili: uwezo mkubwa wa kifedha ‘zisizo na maelezo ya kutosha’ na skandali ya Richmond. Katika mazingira ya kawaida, na hasa katika zama hizi za ufisadi, ni vigumu mno kumnadi mwanasiasa wa aina hiyo.

Tayari kuna hisia kuwa ‘fedha zilibadilishana mikono’ hadi akina Freeman Mbowe kukubali kumpokea mwanasiasa huyo ambaye walikuwa wakimwandama kila kukicha kwa kumuita fisadi.
Kama ni fedha kweli au ‘umaarufu,’ tayari Lowassa ndio mnufaika maana kwa muda mfupi tu ndani ya chama hicho, mambo kadhaa yameshabadilika.
Mie nazifuatilia kwa karibu zaidi harakati za Chadema kupitia mitandao ya kijamii au tovuti za vyombo vya habari mbalimbali vya huko nyumbani. Nilichobaini katika siku chache hizi baada ya Lowasaa kujiunga na Chadema, ghafla wanachama na mashabiki wa chama hicho wamegeuka ‘mabubu’ kuhusu masuala ya ufisadi.
Na hilo si la kushangaza kwa sababu watamudu vipi kukemea ufisadi ilhali mgombea wao wa urais ni mtuhumiwa wa ufisadi?
Kwa mujibu wa maelezo ya mmoja wa viongozi wa Chadema, Tundu Lissu, chama hicho na UKAWA kwa ujumla walikuwa wakifuatilia kwa karibu mchakato wa CCM kupata mgombea wake, na wao walitaka kuitumia ‘sintofahamu’ hiyo ndani ya CCM kufanikisha malengo yao ya kuingia Ikulu.
Huu ni udhaifu wa hali ya juu. Lakini angalau hii imesaidia kutufahamisha kwanini chama hicho kilikuwa kinasuasua kumtangaza mgombea wake: kilikuwa kinasubiri ‘makombo’ ya CCM.
Watu hawa wanajifanya kusahau kabisa mafanikio makubwa tu waliyoyapata katika uchaguzi mkuu uliopita ambapo walisimama wenyewe, wakapata wabunge wa kutosha na madiwani wa kutosha tu, licha ya mgombea wao, Dkt Willbrord Slaa, kushindwa katika mazingira ambayo baadhi yetu tunaamini yalichangiwa na hujuma.
Na ni katika mazingira hayo, baadhi yetu tunaunga mkono Dk. Slaa kujitenga na Chadema. Ni matarajio yangu kuwa hatokubali kuwa sehemu ya usaliti huu hasa kwa kuzingatia gharama kubwa waliyoingia Chadema, kwa maana ya muda na jitihada, sio tu kukitambulisha chama hicho kuwa ni mtetezi wa wanyonge na kiongozi wa mapambano dhidi ya ufisadi bali pia kukiwezesha kuwa chama kikuu cha upinzani Tanzania.
Awali, nilipopata uthibitisho kuwa Lowassa amejiunga na Chadema nilitamka bayana kuwa ‘impact’ ya tukio hilo yapaswa kuonekana angalau ndani ya siku 7. Na siku hizo saba zimeisha juzi. Tuliambiwa tusubiri ‘mafuriko’ ya wana-CCM kumfuata Lowasaa huko Chadema/UKAWA.
Hadi sasa, hakuna dalili yoyote ya mafuriko hayo. Jina kubwa pekee lililojitokeza kumfuata Lowassa ni Naibu wa Kazi na Ajira, Dkt Makongoro Mahanga, ambaye hata hivyo amechukua uamuzi huo baada ya kubwagwa kwenye kura za maoni. Labda kuna wengine watakaomfuata Lowassa lakini sidhani kama watu hao watakuwa na mafuriko yanayotarajiwa.
Kikwazo kikubwa kwa makada wa CCM waliokuwa wakimsapoti mwanasiasa huyo kumfuata kwenye ‘chama chake kipya’ ni ukweli kwamba tayari vyama vinavyounda UKAWA vilishagawana majimbo.
Sasa sidhani kama kuna mwana-CCM mwenye akili zake atakikimbia chama hicho tawala na kujiunga na vyama vinavyounda UKAWA ilhali anatambua kuwa hata akishindwa ubunge au udiwani katika CCM bado ana fursa ya kuteuliwa kwenye nyadhifa nyingine serikalini.
Na ujio wa wafuasi wa Lowassa ndani ya Chadema na UKAWA unaweza kuvibadili vyama hivyo na kuunda makundi ya, kwa mfano, Chadema- asilia na Chadema-Lowassa. Busara za kisiasa zatuonya kuwa chama chenye mgawanyiko hakiwezi kushinda uchaguzi, na hata kikifanikiwa kushinda, hakitoweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Wakati kwa kumpokea Lowassa Chadema italazimika kutowekeza nguvu za kutosha katika mtaji wake mkuu katika uchaguzi mkuu uliopita – vita dhidi ya ufisadi (hawawezi kupigia kelele ufisadi huko mgombea wao akiwa mtuhumiwa wa ufisadi) – ni vigumu kubashiri watamnadi Lowassa kwa lipi hasa.
Wao ndio walikuwa vinara wa kumwita Lowassa fisadi, sasa muda haupo upande wao kubadilisha maelezo na kumnadi kama mtu safi.
Na hata maelezo ya Lowassa kuwa ‘alipata maagizo ya juu’ katika suala la Richmond hayana uzito kwa sababu kwanini aongee sasa na si wakati alipobanwa hadi kujiuzulu? Sawa, wengi twafahamu kuwa skandali hiyo iliwahusisha watu wengine pia, lakini ukweli unakuwa na nguvu pale tu unapowekwa hadharani wakati mwafaka.
Ni rahisi kwa CCM kuipangua hoja ya Lowaasa kuwa ‘alitumwa’ kwa kumuuliza ‘ulikuwa wapi siku zote hizi usiyaseme hayo hadi sasa ulipoamua kuingia upinzani kwa tamaa yako ya madaraka?’
Nimalizie makala hii endelevu kwa kurejea kuwakumbusha Chadema kuwa dhambi yao ya usaliti itawaandama milele. Hoja kuwa Lowassa ‘anauzika’ na atawasaidia kuingia Ikulu sio tu haina msingi bali pia yaweza kuwagharimu huko mbeleni hasa kwa vile, kama nilivyoandika hapo juu, mwanasiasa huyo hajajiunga na chama hicho kwa vile anakipenda bali kwa ajili ya maslahi yake binafsi.
Nachungulia kidogo tu ‘marafiki zake’ kisha utaelewa nini kinaisuburi Chadema huko mbeleni. Mie si nabii wa majanga (prophet of doom) lakini ninabashiri kuwa ujio wa Lowassa huko Chadema ni mwanzo wa mwisho wa chama hicho.
Inasikitisha kuona ‘People’s Power’ (nguvu ya watu) iliyowavutia wapenda mabadiliko wengi ikiishia kuwa ‘Money’s Power’ (kwa maana ya nguvu ya Lowassa kifedha).Pia inaumiza kuona demokrasia yetu ikipitia mlolongo huu usiopendeza wa ‘chama kimoja→ vyama vingi → chama cha mtu mmoja’ (one party→multiparty→one man’s party)
ITAENDELEA

30 Jul 2015


Kama unavyoona hapo pichani juu, mara baada ya kusikia taarifa kwamba Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa anatarajia kujiunga na vyama vinavyounda Muunganowa Katiba ya Wananchi (UKAWA), niliandika tweet hiyo pichani. Kimsingi, binafsi nilishindwa kabisa kuamini kuwa Dkt Willibrord Slaa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema hadi alipotangaza kujiuzulu, angeweza kukaa chama kimoja na Lowassa. Nilishindwa kabisa kupata picha kichwani kumwona Dkt Slaa akiwa jukwaani anamnadi Lowassa. Nilijaribu ku-imagine kwamba labda kwa vile kuingia kwa Lowassa Chadema kunaweza kukiingiza chama hicho na Ukawa Ikulu, na hivy pengine Dkt Slaa angeweza kumsapoti japo kwa shingo upande, lakini nafsini niliona huo sio tu ungekuwa muujiza - na mie si muumini wa miujiza - bali pia ungekuwa usaliti wa hali ya juu.


Siwezi kujisifu kuwa tweet hiyo ya 'kumsuta' Dkt Slaa imesaidia kumfanya achukue uamuzi huo wa kujiuzulu lakini ninachoweza kusema ni kuwa ninamshukuru kwa kufanya maamuzi magumu ya kujiuzulu hasa ikizingatiwa kuwa neno 'KUJIUZULU' halipo katika kamusi ya wengi wa wanasiasa wetu hata pale wakiwa wanaandamwa na kashfa. Lakini pia ninampongeza Dokta Slaa kwa kusimamia anachooamini.

Kwa hakika Dokta Slaa alisimama kidete kupigana kwa nguvu zake zote dhidi ya ufisadi. Na sifa kubwa ya mwanasiasa huyo ilikuwa umakini wake katika kuwasilisha hoja. Hakuwa mtu wa jazba wala mjivuni. Na kwa hakika alikuwa mwenye kuapanga hoja zake na kuziwasilisha kwa umakini mkubwa. Kwa kifupi, Dokta Slaa aliweza kuwasiliana na umma, iwe katika hotuba au maongezi kama DOKTA hasa, maana moja ya sifa ya usomi ni jinsi ya kuwasiliana na jamii kwa ufasaha.

Kuna watakaokuwa wamefurahi kuona Dokta Slaa amechukua hatua ya kujiuzulu, sio furaha ya kuungana naye kwa kuchukua uamuzi huo mgumu bali kwa vile aidha walikerwa na msimamo wake mkali dhidi ya mafisadi na ufisadi, au walimwona kama mmoja ya sababu zilizopokea Zitto Kabwe kung'olewa Chadema. Furaha hiyo ni ya 'kimburula' kwa sababu Dokta Slaa alikuwa mmoja wa wanasiasa wachache kabisa waliosimama kwa dhati na wanyonge kupigania haki zao. Ukimwondoa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, sioni mwanasiasa mwingine yeyeote yule aliyewajali mno Watanzania kama Dokta Slaa. Na japo nina furaha kutokana na kukataa kushirikiana na Lowassa, na ninampongeza kwa kuwa na msimamo thabiti, kwa upande mwingine nina masikitiko makubwa kuona lulu hiyo ya taifa ikiachana na siasa wakati bado twaihitaji mno.
Dokta Slaa alifanya kazi yake kwa uadilifu mkubwa na kwa hakika kuna idadi kubwa tu ya Watanzania iliyoamini kuwa siku moja angeweza sio tu kuwa Rais wetu bali pia angeweza kuibadili Tanzania yetu. Na kwa kujiuzulu, amethibitisha ni mwasiasa wa aina gani. Badala ya kutanguliza maslahi binafsi na kujiunga na chama kingine cha siasa au kuanzisha chama chake, Dokta Slaa amechukua uamuzi wa kiungwana. Ametambua kuwa tatizo sio CCM pekee bali mfumo mzima wa siasa za Tanzania yetu, kuanzia chama tawala hadi huko Upinzani. Uamuzi wa kujiuzulu utamlindia hadhi yake milele. 

Mimi ni muumini mkubwa wa 48 Laws of Power, na ninaomba nitanabaishe jinsi uamuzi huo wa Dokta Slaa unavyoendana na baadhi ya Laws hizo. Law 34 of Power inasema (ninainukuu)

The way you carry yourself will often determine how you are treated: In the long run, appearing vulgar or common will make people disrespect you. For a king respects himself and inspires the same sentiment in others. By acting regally and confident of your powers, you make yourself seem destined to wear a crown.
Kwa tafsiri ya Kiswahili ni kwamba "Matendo yako ndio yatakavyofanya watu wakuchukuliaje. Katika muda mrefu, kuonekana mtu wa ovyo ovyo kutafanya watu wasikuheshimu. Kwa sababu mfalme hujiheshimu mwenyewe na kuhamasisha watu wengine kujiheshimu na kumheshimu. Kwa matendo makubwa na ya uhakika wa nguvu zako, utaonekana mtu stahili kushika hatamu." 
Na kwa hakika uamuzi wa Dokta Slaa kujiuzulu unamfanya aendelee kuwa sio tu mtu mwenye msimamo bali pia ataendelea kushikilia hadhi na heshima yake kama mtu aliyeuchukia ufisadi kwa dhati hadi kuamua kujiuzulu baada ya fisadi Lowassa kujiunga na UKAWA.
Kuna wanaoweza kumbeza kwa kusema amekimbia vita. Well, Law 36 of Power inatuasa, nanukuu,

...It is sometimes best to leave things alone. If there is something you want but cannot have, show contempt for it...
Kwa tafsiri ya Kiswahili, "Wakati mwingine ni vema kuacha vitu kama vilivyo Kama kuna kitu unakitaka lakini huwezi kukipata, kichukie tu." Na hicho ndicho alichokifanya Dokta Slaa. Alichukia ufisadi na kuwachukia mafisadi kwa dhati. Lakini ghafla akajikuta analetewa fisadi ashirikiane nae kupinga ufisadi. Waingereza wana msemo "You can't put a drug addict in charge of a pharmacy," yaani huwezi kulikabidhi teja liwe msimamizi wa duka la madawa (ambayo kwa kawaida yana madawa baadhi ya madawa kama Heroin ambayo ndio 'chakula' cha mateja). Kwa vyovyote vile, ingekuwa vigumu mno kwa Dokta Slaa kutimiza azma yake ya kupambana na ufisadi akiwa pamoja na Lowassa. Na ndio maana akaamua bora akae kando. Kama ninavyotamka mara kadhaa, huhitaji kuwa kiongozi ili ulete mabadiliko, kuwa raia mwema tu (You don't have to be a leader to bring change. Just be a good citizen).

Law 47 of Power inasema, ninanukuu,

The moment of victory is often the moment of greatest peril. In the heat of victory, arrogance and overconfidence can push you past the goal you had aimed for, and by going too far, you make more enemies than you defeat. Do not allow success to go to your head. There is no substitute for strategy and careful planning. Set a goal, and when you reach it, stop.

Kwa Kiswahili inamaanisha, "Ushindi unapowadia ndio wakati ambao unaweza kuangamia. Katikati ya ushindi, dharau na kujiamini kupita kiasi vyaweza kukusukuma zaidi ya lengo kusudiwa, na kwa kupitiliza lengo hilo, watengeneza maadui zaidi ya uliowashinda. Kamwe usiruhusu mafanikio kupanda kichwani mwako. Hakuna mbadala wa mkakati na mipango makini. Weka lengo, na ukilitimiza, simama."
Hakuna asiyefahamu alichotimiza Dokta Slaa katika mapambano yake dhidi ya ufisadi. Kubwa lilikuwa kuwaamsha Watanzania, na kwa hakika wengi wamefunguka macho dhidi ya ufisadi na wanauchukia kwa dhati. Angeweza kujikaza kisabuni na kusimama pamoja na Lowassa ili aendeleze mapambano dhidi ya ufisadi, lakini sote twafahamu ingekuwa vigumu mno. Na uamuzi wake wa kujiondoa madarakani ni sawa na inavyosema sheria hiyo hapo juu, 'ukitimiza leno, simama.'
Vilevile, Dokta Slaa amefuata vizuri Law 5 of Power inayoonya kuwa "So much dependes on reputation, guard it with your life," yaani "Hadhi ni kitu muhimu sana, ilinde kwa nguvu zote." Sasa, sote tulikuwa tukiitambua Chadema kama kiongozi wa vita dhidi ya ufisadi, lakini ghafla wametusaliti na kumkaribisha papa wa ufisadi katika chama chao. Kwa vile ni mtu makini na msafi, Dokta Slaa ameona kuwa kwa kufanya hivyo, Chadema imejishushia hadhi yake katika uongozi wa mapambano dhidi ya ufisadi, na akaamua kuilinda hadhi yake kwa kujitenga nao. 
Nimalizie makala hii kwa kurudia kumshukuru Dokta Slaa kwa yote aliyoitendea Tanzania yetu. Tunaouchukia ufisadi tutaendelea kumwenzi na kumkumbuka milele. Nitajitahidi huko mbeleni kufanya mawasiliano na Dokta Slaa ili ikiwezekana niweke kumbukumbu ya huduma yake bora kabisa kwa Watanzania kwa kuandika kitabu kinachomhusu. Nitawa-update kuhusu hilo.
MUNGU AKUBARIKI SANA DOKTA SLAA. TANZANIA ISIYO NA UFISADI INAWEZEKANA PASIPO HAJA YA KUWATEGEMEA MAFISADI. 



29 Jul 2015

KWANZA ninaomba radhi kwa safu hii kuadimika kwa takriban wiki mbili mfululizo. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizo nje ya uwezo wangu.

Pili, ninaomba kutoa angalizo kuwa makala hii, niliiandaa mara baada ya vikao vikuu vya Chama Cha Mapinduzi (CCM) huko Dodoma ambapo hatimaye chama hicho kilipata mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu. Nimeihariri ili kufidia yaliyojiri kati ya wakati huo na hivi sasa.

Baada ya kugusia hayo, ninaomba kufanya uchambuzi endelevu kuhusu mchakato wa CCM kumpata mgombea wake wa kiti cha urais, wiki mbili zilizopita.

Nitaonekana mwenye chuki binafsi kwa CCM kama sitakipongeza chama hicho tawala kwa kumudu kufikia hatua ya kupata mgombea wake ‘kwa amani.’ Pamoja na kiu kubwa ya Watanzania kufahamu kada gani wa CCM angeibuka kidedea, kwa kiasi kikubwa mchakato wa kupata mgombea wa chama hicho ulikuwa kama ‘referendum’ kwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa taifa wa chama hicho tawala, kuhusu kada maarufu, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa. Swali kubwa lilikuwa, “Je Rais Kikwete ataweza ‘kumtosa’ rafiki yake?” Wengine walilielekeza swali hilo kwa Lowassa na kuwa, “Atakatwa au hakatwi?” hasa kwa kuzingatia kile kilichoonekana kama kada huyo kuungwa mkono na wanaCCM wengi.

Lakini hatimaye, maswali hayo yalipata majibu baada ya Lowassa kutokuwamo katika ‘tano bora.’ Licha ya makada Emmanuel Nchimbi, Sophia Simba na Adam Kimbisa kutangaza kutoafikiana na mchakato wa kuchuja ‘wagombea,’ zilipatikana taarifa kuwa kungekuwa na jaribio la kumng’oa Rais Kikwete katika uenyekiti wake na kuivunja Kamati Kuu ya chama hicho, masuala yaliyoishia kuwa porojo tu.

Hatimaye, chama hicho kilimtangaza Dk. John Magufuli kuwa mgombea wake, ambaye naye alimteua Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea mwenza wake, akiandika historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwa mgombea mwenza, na iwapo Magufuli akishinda, atakuwa Makamu wa Rais wa kwanza mwanamke nchini Tanzania.

Huko nyuma nilifanya ‘ubashiri’ kuhusu makada gani niliodhani walikuwa na nafasi kubwa ya kupita ‘mchujo wa kwanza.’ Wakati si vigumu kuelewa kwa nini Lowassa alikatwa, bado sijaelewa kwa nini kada aliyetarajiwa na wengi kuwa angepitishwa, Jaji Agustino Ramadhani, hakumudu kuingia japo kwenye ‘tano bora.’ Binafsi ninamsikitikia kada huyo kwani kwa namna fulani, ‘kufeli’ kwake kunatia doa wasifu wake ‘wa kupigiwa mstari.’

Pia ‘kufeli’ kwa kada aliyekuwa akitajwa sana, Makongoro Nyerere, kuliwashtua baadhi ya watu lakini yayumkinika kuhisi kuwa msimamo wake mkali wa kutaka kuirekebisha CCM, na kauli yake ya ‘turudishieni CCM yetu’ ilimtengenezea maadui hususan wanaonufaika na ‘sera za ulaji na kulindana’ ndani ya chama hicho.

Nilibashiri kuwa January Makamba angefanya vizuri, na kwa hakika alifanikiwa kuingia kwenye ‘tano bora,’ hatua ambayo yaweza kumtengenezea mazingira mazuri ya kisiasa iwapo ataendelea kuwa na dhamira ya kuiongoza Tanzania huko mbeleni.

Pia nilibashiri mmoja au wawili wa makada wa kike kufanya vizuri katika ‘mchujo wa kwanza,’ na ilikuwa hivyo. Sambamba na hilo, nilibashiri uwezekano wa kuwa na aidha mgombea urais mwanamke au mgombea mwenza/makamu wa rais mwanamke, na hilo limetokea japo nilitarajia angekuwa mmoja wa makada wa kike waliojitokeza kuwania nafasi ya urais.
Kwa upande mwingine, mwathirika mkubwa kabisa wa mchakato huo ni mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale Mwiru, ambaye pasipo busara aliamua kujidhihirisha kuwa anamuunga mkono Lowassa. Sidhani kama mzee huyo mwenye uzoefu mkubwa wa kisiasa ana washauri wazuri kwani alipaswa kutambua kuwa laiti ‘mgombea wake’ Lowassa akishindwa basi ‘legacy’ yake nayo itayeyuka. Kwa bahati mbaya kwake, Kingunge atakumbukwa zaidi si kama ‘swahiba wa Baba wa Taifa’ bali ‘mkongwe wa kisiasa aliyeangukia pua kwa kumuunga mkono kada aliyetoswa kwenye kinyang’anyiro cha kusaka urais.’ Waelewa wa mambo wanatahadharisha kuwa kujenga hadhi (reputation) ni kitu kinachochukua muda mrefu na kazi kubwa, lakini kosa dogo tu, linaiondoa hadhi hiyo mara moja. Ni rahisi kubomoa kuliko kujenga.

Kwa upande mmoja kuna hisia kwamba Lowassa anaweza asikubali kupoteza mtaji wake wa kisiasa (political capital) katika kilichoonekana kama kuwa na uungwaji mkono mkubwa ndani na nje ya chama chake, kwa kujiunga Ukawa. Akiwa Ukawa na akagombea urais kuhusu swali kwamba atashinda au la, si rahisi kubashiri kwa sasa.

Lakini kwa upande mwingine, jaribio la kuhama CCM linaweza kumgharimu mno mwanasiasa huyo mzoefu. Moja ya athari za wazi ni uwezekano wa kupoteza stahili kadhaa anazopata kama Waziri Mkuu wa zamani. Kadhalika, akihama CCM, chama hicho tawala kinaweza kutumia kila mbinu ‘kummaliza’ kabisa kisiasa. Kama ana washauri wazuri basi pengine ni vema angekubali tu matokeo na ‘kula pensheni yake’ kama Waziri Mkuu wa zamani, bila kuondoka CCM.

Jingine lililojitokeza katika mchakato huo ni ‘kutoswa’ kwa wasaidizi wakuu wawili wa Rais Kikwete, yaani Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilali na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Tafsiri ya haraka ni kuwa katika miaka 10 ya utawala wa Rais Kikwete, tulikuwa na viongozi wakuu wawili wa kitaifa ambao pengine hawakustahili kuwa katika nyadhifa hizo na ndio maana wameshindwa kufaulu katika japo mchujo wa awali. Badala ya kukumbukwa kama Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa zamani, Dk Gharib na Pinda watakumbukwa zaidi kama wasaidizi wakuu wa Rais ambao walifeli ‘mtihani wa kurithi nafasi ya bosi wao.’

Sasa twende kwa Dk. Magufuli. Kwanza, ni kweli kuwa amekuwa akisifika kama mchapakazi. Lakini pengine hili ni matokeo ya kasumba iliyojengeka miongoni mwa Watanzania kwamba kiongozi akitekeleza wajibu wake ambao analipwa mshahara kutekeleza wajibu huo, anaonekana kama ‘malaika.’

Taifa letu limekuwa na uhaba mkubwa wa wazalendo kiasi kwamba kiongozi akitekeleza wajibu au kukemea rushwa anaonekana kama ametoka sayari nyingine. Binafsi, ninamwona Magufuli kama kiongozi wa ‘kawaida’ tu ambaye mara nyingi alizingatia matakwa na matarajio ya mwajiri wake. Kama tunawaona madaktari wakijitahidi kuokoa maisha ya wagonjwa kila kukicha huko hospitalini, au walimu wanaofika mashuleni kufundisha (wengi wao katika amzingira magumu), iweje tumwone Magufuli tofauti kwa vile tu anatekeleza mengi ya majukumu anayotakiwa kuyatekeleza?

Moja ya ‘madoa’ kuhusu uongozi wa Magufuli ni suala la uuzwaji wa nyumba za serikali, suala ambalo halijapatiwa majibu ya kuridhisha. Jingine ni ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali aliyopendekeza hatua stahiki zichukuliwe dhidi yake kama Waziri wa Ujenzi na Dk. Harrison Mwakyembe (aliyekuwa Naibu Waziri) kutokana na ufisadi unaofikia shilingi bilioni 256. Kama ilivyo kwenye uuzwaji wa nyumba za serikali, suala hili nalo pia halijatolewa maelezo ya kuridhisha.

Lakini pengine ni usahaulifu wa Watanzania wengi, au ni kile Waingereza wanaita ‘settling for less’ (kuridhika na kilicho pungufu), ile picha inayomwonyesha Magufuli akipata ‘tiba ya Babu wa Loliondo’ haionyeshi kuwasumbua wananchi wengi wanaoonekana kuwa na matumaini makubwa kwa kada huyo. Binafsi, pamoja na kuheshimu uamuzi wa Magufuli kutegemea ‘tiba hiyo ya porojo,’ nilitarajia msomi kama yeye, tena mwenye taaluma ya Kemia angejihangaisha kutafiti kidogo tu kuhusu ufanisi wa ‘tiba’ hiyo ya kitapeli. Je hili ninalolitafsiri kama ufyongo wa kimaamuzi halitojitokeza katika urais wake iwapo atashinda hapo Oktoba?

Kubwa zaidi ni uwezekano wa Magufuli kuwa ‘Kikwete mpya.’ Sio siri kuwa Rais Kikwete amekuwa ‘shabiki’ mkubwa wa utendaji kazi wa Magufuli. Hilo si kosa. Lakini pengine ‘ushabiki’ huo umechangia pia katika mafanikio ya kisiasa ya kada huyo, na haihitaji uelewa mkubwa wa siasa kubashiri kuwa huenda Magufuli akawa na ‘deni’ kwa Kikwete. Licha ya hofu yangu kuu kuwa tatizo kubwa la ‘urais wa Magufuli’ ni ukweli kuwa ni kada wa CCM ile ile iliyotufikisha hapa tulipo, wasiwasi wangu mwingine ni huo uwezekano wa kuwa na ‘Rais mstaafu by proxy,’ yaani Kikwete kuwa na ‘influence’ kwa ‘rafiki yake’ aliyepo Ikulu.

Kadhalika, ninadhani wengi hatujasahau ukweli kwamba ukosoaji mkubwa dhidi ya kada January Makamba ilikuwa uamuzi wake wa kubainisha visheni ya ‘urais wake’ aliyoiita ‘Tanzania Mpya.’ Ukosoaji huo uliegemea kwenye hoja kwamba mgombea urais kwa tiketi ya CCM atajinadi kwa kutumia ilani ya uchaguzi ya chama hicho. Na japo mgombea ana fursa ya kushiriki kuingiza malengo yake, kwa kiasi kikubwa ilani hiyo huandaliwa na chama chenyewe.

Lakini pengine sasa ndio tunatambua umuhimu wa kuwa na visheni kama ‘Tanzania mpya’ ya kada January kwani hatujui lolote kuhusu visheni ya Magufuli zaidi ya kuambiwa ni kuwa ni mchapakazi. Swali la msingi, je, uchapakazi wake utaendana na matakwa ya CCM katika ilani yake ya uchaguzi? Lakini hata kama chama hicho tawala kitamruhusu Magufuli kuandika ilani yake mwenyewe kwa niaba ya chama hicho, je ukada wake (kama ilivyothibitika katika hotuba yake ya kuombea kura huko Dodoma) hautokuwa kikwazo katika kuirejesha CCM kwenye misingi yake ya awali ya kuwatumikia wanyonge badala ya matajiri ilivyo sasa?

Mara kadhaa nimekuwa nikieleza kuwa moja ya vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya nchi yetu ni kutanguliza itikadi ya kisiasa badala ya maslahi ya chama. Kada au mwanae anayefahamika kujihusisha na biashara haramu au ufisadi hachukuliwi hatua kwa vile ‘ni mwenzetu.’ Vyombo vya dola vinashindwa kuchukua hatua kwa kuhofia ‘kuwaudhi vigogo wa kisiasa’ Na CCM imekuwa kimbilio kwa watu wa kada mbalimbali ikiwa ni pamoja na mafisadi kwa vile sio siri kuwa uongozi katika chama hicho ni mithili ya kinga ya uhakika dhidi ya hatua za kisheria

Tanzania yetu sio tu inahitaji Rais ambaye hana deni la fadhila kwa mtu yeyote yule, atakayetumia ipasavyo nguvu anayopewa na Katiba kuiongoza nchi yetu kwa maslahi ya taifa badala ya kuweka mbele maslahi ya chama, na kwa CCM, mwanasiasa anayetambua kuwa chama hicho kimeporwa na wenye fedha –safi na chafu- na kuwatelekeza wanyonge.
Nimalizie makala hii kwa ahadi ya kuendeleza uchambuzi huu katika makala ijayo nikitarajia kuwa muda huo tutakuwa tumeshamfahamu mgombea wa tiketi ya urais kupitia Ukawa. Pia ningependa kuwahimiza Watanzania wenzangu wajitokeze kwa wingi kujiandikisha katika daftari la wapigakura .

JIUNGE NAMI TWITTER https://twitter.com/Chahali AMBAPO NINAJADILI MASUALA MBALIMBALI

28 Jul 2015

Ninaipenda siasa...kama stadi  (study, yaani kuisoma), lakini kwa hakika ninapata shida sana na jinsi mengi ya ninayosoma katika stadi za siasa (political studies) yanavyogeuka inapokuja kwenye matendo au shughuli za kisiasa an zinazohusiana na siasa. 

Stori kidogo. Fani niliyotamani sana kuisoma na pengine kubobea ni utabibu. Nilitamani mno kuwa daktari. Lakini ndoto yangu ya udaktari ilipata kikwazo baada ya kupata matokeo ya mtihani wa kumaliza kidato cha nne. Japo nilipata A kwenye Kemia na C kwenye Baiolojia, niliambulia D kwenye Hisabati na kufeli kabisa Fizikia ambapo nilipata F. Na japo nilipata Division One, uwezekano wa kuchukua 'combination ya udaktari' yaani PCB (Fizikia, Kemia na Baiolojia) kidato cha tano uliathiriwa na hiyo F ya Fizikia. Uwezekano pekee ulibaki kwenye kujaribu combination ya CBG (Fizikia, Kemia na Jiografia) ambayo ingeniwezesha kuikwepa Fizikia.

Nilipojiunga na kidato cha tano katika sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nikakumbana na vikwazo vingine. Kwanza, Kemia ya kidato cha kwanza mpaka cha nne ni tofauti kwa kiasi kikubwa na ile ya kidato cha tano na cha sita. Kuna kitu inaitwa Physical Chemistry ambayo kimsingi ni kama mchanganyiko wa Kemia, Hisabati na Fizikia. Sasa kama nilivyotanabaisha hapo awali, udhaifu wangu katika Fizikia na Hisabati ulimaanisha kuwa nisingeweza kuimudu Kemia ya High School.

Pili, shule yetu ilikuwa haina mwalimu ya Jiografia, na ilibidi tuwe tunakwenda shule ya jirani ya Tabora Girls' kuhudhuria vipindi vya somo hilo. Angalau Baiolojia haikuwa tatizo japo kiukweli ilihitaji uwezo mkubwa wa kukariri na kuelewa majina ya sampuli za viumbe ambayo mengi yana asili ya Kilatini au Kigiriki. Kwahiyo kwa kifupi, dhamira yangu ya kusoma combination ya CBG ilikufa kifo cha asili.

Hivyo nikaamua kusoma combination yenye masomo ya Historia, Jiografia na Kiingereza. Hii ilikuwa mteremko kwa kiasi kikubwa, lakini ndoto yangu ya kuwa daktari ndio ikayeyuka. Lakini wanasema kile unachotaka sio lazima ndio unachopata (what you wish for is not always what you get).

Sukuma miaka kadhaa baadaye, nikajiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam na hapo nikajikuta nina uchaguzi wa ama kuzamia kwenye sayansi za siasa na utawala wa umma (pilitical science and public administration au sosholijia, elimu inayohusu masuala yya jamii. Mwaka wa pili, nikafanya uamuzi wa kuchukua hiyo choice ya pili, yaani Sosholojia. Kwa hakika niliipenda sana sosholojia. Yaani ilinisaidia mno kuielewa jamii. Miongoni mwa masomo ya kupendeza sana yalikuwa lile lilifundisha kuhusu uhusiano wa jamii, utamaduni na afya; somo la jinsia na uhusiano wa kijinsia, na zaidi ya yote ni sosholojia ya dini ambapo pamoja na mambo mengine tulifundishwa kuhusu Ukristo, Uislamu na Imani za Asili. 

Sukuma miaka kadhaa zaidi mbele, nikapata skolashipu ya kuja hapa Uingereza kusoma Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (Politics and International Relations), mkazo ukiwa kwenye masuala ya usalama. Kwa vile skolashipu ni kama zawadi, mwanafunzi anakuwa hana uchaguzi. Nilitamani sana kuendelea na Sosholojia lakini sikupewa fursa ya kuchagua. Na hivyo ndivyo nilivyojikuta nikiingia kwenye stadi za siasa. Tuishie hapo/

Kwanini nimeelezea stori hiyo? Ni kwa sababu kama nilivyosema awali, ninaipenda siasa kama stadi. Yaani baada ya kutokuwa na choice ya kusoma sosholojia, na 'kulazimishwa' kusoma Siasa, ikabidi niipende tu. Niliipenda pia kwa sababu siasa za kimataifa zina 'raha' yake kuzielewa, ukichanganya na maeneo kama diplomasia, amani na 'ugomvi' (peace and conflicts) na masuala ya usalama wa kimataifa (international security).

Lakini tatizo la siasa kama stadi ni ukweli mchungu kwamba kile unachosoma darasani mara nyingi hakiakisi hali halisi mtaani. Siasa kama fani au stadi sio mbaya, ina mafunzo mengi, inafundisha miongozo mingi na kanuni nyingit muhimu kwa maisha ya mwandamu, lakini mtaani hali ni tofauti.  Sihitaji kuelezea kwa undani kwanini watu wengi wanaichukia siasa. Lakini mfano mwepesi ni kwenye kampeni za uchaguzi ambapo utasikia chama kikitanabaisha sera nzuri kabisa lakini baada ya kuingia madarakani kikaishia kufanya kinyume kabisa na kilichoyaahidi. Na kwa Tanzania yetu tuna mfano hai wa jinsi sera tamu za CCM zinavyoishia kuwanufaisha matajiri na mafisadi huku zikiwadidimiza walalahoi.

Na mfano mchungu zaidi, uliopelekea niandike makala hii, ni jinsi Chadema katika mwavuli wa UKAWA inavyoelekea kuwasaliti mamilioni ya Watanzania kwa uwezekano wa kumpokea fisadi Edward Lowassa kuwa mgombea wa urais.

Jana niliumia mno nilipoona picha kadhaa zinazomwonyesha Lowassa akiwa na viongozi wa UKAWA. Baadaye, mwenyekiti wa NCCR, moja ya vyama vinavyounda UKAWA pamoja na Chadema, CUF na NLD, alitamka bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa kujiunga nao.

Lakini baadaye kidogo nikapata ahueni baada ya kupatikana taarifa zilizothibitishwa na akaunti ya Twitter ya Chadema Media kuwa picha zilizokuwa zinamwonyesha Lowassa na viongozi wa UKAWA ni feki, yaani zilikuwa photoshopped. Hata hivyo furaha hiyo haikudumu muda mrefu baada ya Mbatia na wenzake kutangaza bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa . Na kuna uwezekano leo Jumanne, aidha UKAWA wakamtangaza Lowassa kuwa mgombea wao wa Urais au Lowassa mwenyewe akatangaza kujiunga nao.
Huu ni usaliti mkubwa mno hasa upande wa Chadema, chama kilichojidhihirisha kuwa kinauchukia ufisadi kwa dhati. Sote twakumbuka jinsi Chadema ilivyojipatia umaarufu kwa kupambana na ufisadi, hasa baada ya kutangaza hadharani 'orodha ya aibu' (list of shame) pale Mwembeyanga jijini Dar ambapo walitaja orodha ya mafisadi akiwemo Lowassa. Kadhalika Chadema ilifanya jitihada kubwa kuibua ufisadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na skandali ya Richmond iliyopelekea Lowassa kujiuzulu Uwaziri Mkuu. Vilevile chama hicho kilitufumbua macho kuhusu ufisadi wa EPA, Meremeta, Dowans, Buzwagi, TanGold, Kiwira, nk. Kwa kifupi, ilikuwa haiwezekani kuzungumzia mapambano ya  ufisadi Tanzania bila kuitaja Chadema.

Na katika harakati zake za kupambana na ufisadi, kuna Watanzania wenzetu waliopoteza maisha yao na wengine kujeruhiwa vibaya na kuachiwa ulemavu kwa kukiunga mkono chama hicho. 


Na kwa kuonyesha kuwa Chadema ilikuwa mwarobaini kwa CCM na mafisadi kwa ujumla, chama hicho kilifanyiwa kila aina ya hujuma. Mara kiliitwa chama cha kidini, baadaye kikaitwa cha kikabila, na hadi hivi majuzi kiliitwa chama cha kigaidi. Lakini taratibu Watanzania walifumbuka macho na kubaini kuwa sababu kubwa ya CCM na serikali yake kuiandama Chadema ni kwa vile chama hicho cha upinzani kilichofanya vizuri tu katika uchaguzi mkuu uliopita kinasimamia maslahi ya wanyonge ilhali CCM inatetea mafisadi na ufisadi.
Japo mie binafsi sikuwa mwanachama wa Chadema, nilikiunga mkono kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi kulingana na msimamo wangu kwenye suala hilo. Nilikuwa nina imani kuwa laiti Chadema ikifanikiwa kuingia Ikulu basi kwa hakika safari ya kuipeleka Tanzania yetu mahali inapostahili kuwa inawezekana. 
Sasa hili la kumpokea Lowassa ni pigo kubwa mno na ni usaliti wa hali ya juu kabisa. Ndio, Lowassa anaweza kuwasaidia Chadema na UKAWA kuingia Ikulu. Lakini kwa kuangalia tu maswahiba wa Lowassa utaweza kujua tutakuwa na serikali ya aina gani. Sipati shida kubashiri kuwa tutaishia kuikumbuka CCM. 

Embedded image permalink

Na huo ndio ubaya wa siasa katika vitendo, tofauti na ilivyo nzuri na mwafaka katika stadi. Kwamba kistadi za siasa, Chadema ilijijenga na kupata umaarufu kwa kuzingatia kanuni ilizojiwekea na ikajitambulisha kama chama kilichopo kwa maslahi ya wanyonge, tofauti na CCM iliyokimbia kanuni zake na kuwakumbatia matajiri na mafisadi. Lakini ghafla bin vup, Chadema inaelekea kwenda kulekule ilipo CCM. 

Nimalizie makala hii kwa kuahidi kufanya uchambuzi wa kina kuhusu suala hili katika makala yangu ya wiki ijayo katika gazeti la Raia Mwema. Spoiler alert, wiki hii katika toleo litakalokuwa mtaani kesho ninamjadili Magufuli. 

Asanteni kwa kuchukua muda wenu kunisoma.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.