7 Jun 2016

Heri ya siku yako ya kuzaliwa, dear Sintah. Mwenyezi Mungu akujaalie kila la heri na baraka katika maisha yako. Asante sana kwa kuwa ndugu mwema. Siku zote umekuwa kama ndugu uliyezaliwa tumbo moja nami. Siku yako ya kuzaliwa imeangukia wakati mwafaka, mwanzo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, na kwahiyo naomba pia kukutakia Ramadhan Kareem.

2 Jun 2016

NINAANDIKA makala hii nikiwa na uchungu mkubwa. Uchungu huo unatokana na habari niliyoiona mtandaoni lakini sikuitilia maanani mwanzoni hadi nilipoisoma muda mfupi kabla ya kuandika makala hii.

Habari hiyo ni kuhusu uamuzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kuwarudisha nyumbani wanafunzi 7,000. Hilo la kuwarudisha nyumbani tu sio jambo dogo lakini kibaya zaidi ni namna ya utekelezaji wa uamuzi huo.


Katika mazingira ya kawaida, na nikiamini kuwa wanafunzi hao wanatoka sehemu mbalimbali za nchi yetu, kuwaamuru waondoke chuoni hapo mara moja pasipo maandalizi ya kutosha sio tu ni kukosa ubinadamu bali pia kunahatarisha usalama wao.

Kwa mujibu wa maelezo kidogo yaliyopatikana hadi sasa, uamuzi huo wa kuwatimua wanafunzi hao umetokana na kinachoelezwa kuwa ni matatizo ya ufundishaji wa stashahada ya kozi maalumu ya ualimu wa sayansi.


Sitaki kabisa kuamini kuwa matatizo hayo yalijitokeza ghafla kiasi cha kusababisha uongozi wa chuo hicho kuchukua uamuzi huo wa ghafla. Haiwezekani kwamba uongozi wa chuo ulilala na kuamka na kukutana na matatizo hayo. Lazima uongozi huo ulikuwa ukifahamu kuhusu suala hilo muda mrefu na ulipaswa kutafuta njia mwafaka za utatuzi.

Waingereza wana usemi kwamba, “mipango mibovu huleta matokeo mabovu.” Kozi husika haikujitengeneza yenyewe, iliandaliwa na kuangaliwa ufanisi wake ungepatikanaje. Mambo kama hayo huchukua miezi kama sio miaka. Sasa iweje ghafla uongozi wa chuo ukurupuke na kueleza kuwa kuna matatizo?


Kwa mujibu wa gazeti moja la kila siku la huko nyumbani, Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idris Kikula alipotakiwa kufafanua kuhusu suala hilo alikiri uwepo wa tatizo hilo na kuelekeza kuwa atafutwe afisa uhusiano wa chuo hicho kwa maelezo zaidi.

Kwa upande wake, afisa huyo, Beatrice Baltazar, alieleza kwamba kusimamishwa kwa wanafunzi hao kulitokana na agizo la serikali na chuo hicho kimetakiwa kulitekeleza.


Ninapata shida kuamini kuwa serikali hii inayotumia kauli mbiu ya “Hapa Kazi Tu” inaweza kufanya uamuzi wa kukurupuka kiasi hiki bila kujali mustakabali wa wanafunzi hao.


Taarifa za magazeti mbalimbali zinaonyesha kuwa wanachuo waliofukuzwa wamejikuta katika wakati mgumu, huku ikidaiwa kuwa baadhi ya wanachuo wa kike wameamua kujihusisha na ukahaba ili kujikimu. Ni rahisi kulaumu pindi msichana au mwanamke anapoamua kuutumia mwili wake kukidhi mahitaji yake ya fedha lakini moja ya sababu zinazoweza kumshawishi mtu kujiingiza kwenye vitendo visivyofaa kama ukahaba ni pamoja na kusaka ufumbuzi wa matatizo yanayomkabili.

Katika mazingira ya kawaida tu, mwanafunzi wa kike anapojikuta hana pa kulala wala kula, na ikizingatiwa kuwa mafisadi wa ngono wametapaa kila kona, kilichotokea huko Dodoma kinawaweka wanachuo wa kike katika mtihani mgumu ambao unaweza kuwa na athari za muda mrefu kisaikolojia.


Cha kusikitisha zaidi ni kwamba tukio hilo lisilopendeza limetokea wakati Bunge likiendelea na vikao vyake huko Dodoma. Kila mwanachuo aliyetimuliwa ana mwakilishi hapo bungeni, kwa maana ya mbunge wa jimbo lake. Na katika mazingira ya kawaida, wabunge walipaswa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa njia mwafaka zinatumika kutatua suala hilo sambamba na kuwapatia misaada wanachuo hao.


Lakini kama ilivyo kwenye kero nyingine majimboni, wabunge wengi wamekuwa na ufanisi mdogo katika kuelezea shida zinazowakabili wana-jimbo wao. Yayumkinika kuhisi kuwa laiti kila mbunge ambaye mwana-jimbo wake ni mwathirika wa uamuzi huo usio na busara na usio wa kibinadamu angeamua kupigana ‘kufa na kupona’ basi huenda serikali kupitia uongozi wa chuo hicho ungebadili uamuzi huo.


Tukio hili ni mwendelezo tu wa mazingira magumu yanayowaandama wasomi wa kesho. Kwa kiasi kikubwa, upatikanaji wa elimu nchini umekuwa kama adhabu, kuanzia shule ya msingi hadi chuo kikuu.


Japo tunatambua kuwa uwezo wa serikali yetu ni mdogo kumudu gharama za elimu, na pia ikizingatiwa kuwa kuna vipaumbele vingine lukuki vinavyoikabili serikali yetu, lakini wakati mwingine kinachohitajika sio fedha bali busara tu.


Katika suala hili ninalozungumzia, ni dhahiri kuwa laiti uwepo wa matatizo husika ungebainika mapema na kutafutiwa ufumbuzi kwa njia stahili, basi tusingejikuta tuna kundi la maelfu ya wanafunzi wanaohangaika kurudi majumbani huku hawajui hatma yao kielimu na kimaisha ikoje.


Kuna wanaodhani kuwa jeuri za maofisini au katika sehemu za huduma huchangiwa na mazingira magumu ya elimu huko nchini. Kwamba, mtu baada ya kuhitimu masomo au kozi yake, na kuteseka vya kutosha, anakuwa na ‘hasira’ kiasi kwamba fursa ya kuitumia elimu yake kazini yaweza kuambatana na ‘kisasi’ kwa yeyote aliye mbele ya uso wake. Haipaswi kuwa hivyo lakini tutarajie nini kwa watu waliopata elimu kana kwamba wapo jela?


Sitarajii makala hii kubadili chochote kwa sababu tayari uamuzi umekwishafanyika na hatua zisizo za kiungwana zimekwishachukuliwa, yaani kuwafukuza wanachuo husika. Hakuna uwezekano wa fulani kusoma makala hii na kubadili uamuzi huo. Hata hivyo, bado kuna fursa ya busara kutumika kulitatua suala hilo.


Ni muhimu kwa serikali na uongozi wa chuo hicho kuandaa utaratibu wa kuwasiliana na wanafunzi hao kuwafahamisha kuhusu hatma yao. Na kama ambavyo mwajiri anavyolazimika kumfidia mwajiriwa anayesimamishwa kazi ilhali hajafanya kosa lolote, utaratibu mahsusi uandaliwe kufidia gharama walizoingia wanachuo hao kutokana na uamuzi huo wa ghafla.


Nimalizie makala hii kwa kuiomba Serikali ya Rais Dk. John Magufuli kuanza jitihada za makusudi za kuyatengeneza mazingira ya elimu kuwa rafiki, yenye kumvutia mwanafunzi au mwanachuo kujiona ananufaika kwa ajili yake na taifa na sio kama amefanya kosa kujiunga au kuwepo kwenye taasisi ya elimu. Elimu sio ukombozi kwa mtu binafsi tu bali taifa kwa ujumla. Kama tunaandaa wasomi wa kulitumikia taifa letu kwa ufanisi na uzalendo basi maandalizi hayo yaambatane na kuwajengea mazingira mwafaka.



Hivi kama umeshawahi kutishiwa kifo huko nyuma, kwa maana ya vyombo vya dola kukutaarifu kuwa maisha yako yapo hatarini, utajisikiaje ukipata barua-pepe kama hiyo niliyoiambatanisha hapo chini?

Naam, huko nyuma, nilishawahi kufahamishwa na vyombo vya usalama hapa Uingereza kuwa kuna mpango wa kunidhuru. Nilielezea kwa kirefu kuhusu tukio hilo la kutisha HAPA. Sasa mambo kama haya yakishakutokea maishani, unajifunza kutochukulia vitu kirahisi, kwa lugha nyingine, 'unakuwa unaishi kwa machale.' Sio kama inazuwia kwa asilimia 100 uwezekano wa mtu kudhuru, lakini angalau inapunguza nafasi za mwenye nia ovu.

Sasa leo naingia kwenye barua-pepe zangu nakutana na 'tishio' hili. Mwanzoni nilishtuka kidogo, maana hiyo barua pepe ina dalili nyingi za kuonyesha ni ya kweli. Nikajiambia kuwa kabla ya kukimbili kuripoti polisi, hebu niangalie anwani ya aliyeituma kwangu. Nikagundua kuwa hiyo https://goo.gl/zj173Y ni email address ya mzee mmoja mstaafu huko Marekani. 

Kisha nika-Google "I have been paid to kill you" nikabaini kuwa ni utapeli maarufu mtandaoni japo ukikumbana nao mara ya kwanza waweza kudhani ni wa kweli. Inaelezwa kuwa ukishatumiwa email ya vitisho kama hiyo, mtumaji anakuonya usiwasiliane na vyombo vya dola, na kukutaka uwasiliane nae ndani ya masaa 24. Ukijibu tu basi vitafuata vitisho zaidi, lakini pia utaambiwa uanze kufanya malipo ili kumwezesha huyo 'muuaji amuuwe mtu mwingine badala ya wewe aliyetumwa kukuuwa.' Yaani matapeli hapo wanakujengea picha uwaone kama wasamaria wema wanaookoa maisha yako.

Kwahiyo, ukipokea email kama hii, IPUUZE. USIIJIBU, maana ukiijibu tu utawapa moyo matapeli hao kukutisha zaidi. Puuza na block address ya aliyeituma (not that itasaidia ku-block, kwa sababu hao matapeli wana maelfu ya email feki). La muhimu hapa sio email bali maudhui ambayo ni UTAPELI. Kuwa makini 

Nimeona niwashirikishe wasomaji wapenda ili kesho na keshokutwa, ukikumbana na utapeli huu, usije uka-panic. Ila kwa hakika, ni vigumu kupuuza vitisho vya matapeli hawa laiti wanachotishia kishawahi kukutokea maishani.

Endelea kutembelea blogu hii kwa habari mbalimbali za teknolojia na makala nyinginezo. 

30 May 2016

Mitandao ya jamii imeturahisishia maisha kwa kiasi kikubwa. Sasa tunaishi katika dunia kama kijiji ambapo tukio likotokea sehemu moja ya dunia linafahamika sehemu nyingine muda huohuo bila kutegemea radio, runinga au gazeti pekee. Kadhalika, mitandao ya kijamii imetuwezesha kufahamiana na watu wengi popote walipo duniani bila kukutana ana kwa ana.

Pamoja na mazuri mengi ya mitandao ya kijamii, kuna upande wa pili usiopendeza kuhusu mitandao hiyo ya kijamii. Licha ya kutupatia fursa ya kufahamiana na watu mbalimbali muhimu, mitandao hiyo pia imetoa fursa kwa watu waovu wanaoitumia kwa minajili ya kufanya maovu yao.

Katika makala hii ninaongelea kuhusu tishio kubwa na lililotapakaa kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook, ambapo watu waovu huweka hufungua akaunti feki na kuweka profile feki zinazoambatana na picha za warembo wa kuvutia. Watu hawa wanaweza kuwa aidha wanawake au wanaume lakini hiyo haijalishi kwa sababu lengo lao sio zuri.

Wanachofanya ni rahisi. Wanafungua akaunti feki kwa maana ya jina na taarifa husika, kisha wanaweka picha kadhaa za msichana mrembo. Picha zinazotumika zaidi ni za warembo wa Afrika Kusini. Kama wengi wetu tunavyofahamu, mabinti wengi wa nchi za Kusini mwa Afrika wamejaliwa shepu zenye mvuto. Kwahiyo, tapeli husika anaweka picha kama tano hivi kwa kuanzia, nyingi au zote zikiwa katika pozi za kuvutia kama sio kutamanisha.

Baada ya hapo wanaanza kuomba urafiki (friend requests) kwa kasi ya kimbunga. Kwa makadirio ya chini, mara baada ya kukamilisha profiles zao feki, matapeli hao hutuma friend requests kati ya 100 hadi 300 kwa mkupuo.

Jinsi ya kuwatambua sio ngumu sana. Cha muhimu nikuzingatia kanuni muhimu ya matumizi ya mtandao (Internet) yaani "ukiona ni kizuri kupita maelezo, basi kitlie shaka," wanasema "if it is too good to be true, them may be it is not true." Kanuni hiyo pia ina umuhimu mkubwa katika matumizi ya barua-pepe. Ukipata email kutoka kwa mtu usiyemjua anayedai ana mamilioni ya dola na anataka kuweka kwenye akaunti yako, huyo ni tapeli tu. Hakuna mtu mwenye akili timamu, hata awe tajiri kiasi gani, ambaye yupo tayari kumpatia mtu japo dola 10 tu (achilia mbali hayo mamilioni) mtu asiyemjua.

Kwahiyo, ukipata friend request kutoka kwa binti mrembo kupindukia ilhali hamjuani, basi washa king'ora cha tahadhari. Kitu cha kwanza kabisa ni kuangalia profile husika. Angalia mtu huyo amejiunga lini na Facebook. Pili angalia idadi ya marafiki wapya. Ukikutana na profile inasema "X amekuwa friends na Y na watu 100 au zaidi (kwa mkupuo)" basi uwezekano mkubwa ni kwamba huyo ni tapeli 'anakulia taimingi..'

Kingine ni kuangalia aina ya marafiki zake, Mara nyingi matapeli wa aina hiyo hujifanya wa jinsia ya kike lakini friends wao wengi kabisa kama sio wote ni wanaume. Sio dhambi wala kosa la jinai kwa mwanamke kuwa na marafiki wengi wa kiume kuliko wa kike lakini 'unapaswa kuchezwa na machale.'

Lakini ili kupata uthibitisho zaidi, unaweza ku-save moja ya picha za mtu huyo kwenye computer yako kisha nenda kwenye ukurasa wa kutafuta utambulisho wa picha kwenye Google. 

Ngoja nikuelekeze jinis ya kutumia tovuti hiyo inayoitwa Google Image.

1. Kwanza, ni rahisi zaidi kuitumia Google Image kutafuta utambulisho wa picha kwenye computer kuliko kwenye simu au tablet. Kwahiyo maelezo ninayotoa hapa ni ya kutumia Google Image kwa computer na sio simu au tablet. Andika anwani hii https://images.google.com 


2. Ukishaingia hapo, bonyeza hapo kwenye alama ya kamera kwa ajili ya ku-search kama ilivyo pichani



3. Ukishabonyeza hapo, bonyeza palipoandikwa 'upload an image' kama inavyoonekana pichani,



4. Kisha bonyeza palipoandikwa 'choose file.'



5. Baada ya kubonyeza hapo, nenda sehemu uliyo-save ile picha unayohisi ni feki.



6. Upload picha hiyo



7. Angalia matokeo 

Njia hiyo hapo juu ni muhimu sana sio kwa ajili ya kuangalia kama picha ni feki kwenye Facebook tu bali kwa kuhakiki picha mbalimbali unazokutana nazo mtandaoni.

Hata hivyo, wakati mwingine matokeo ya Google Images search yanaweza yasikupe jibu unalotarajia. Ushauri wangu ni kuzingatia tahadhari nilizotoa awali. Na kumbuka, "if it is too good to be true, may it is not true."

Waweza ku-accept friend request na kusubiri kama huyo 'binti' ataanzisha maongezi nawe. Mara nyingi, akianzisha maongezi, anaweza kukuomba namba ya simu au ya  Whatsapp. Ukimwomba yake atakwambia simu imeharibika aua imeibiwa. Sasa katika mazingira ya kawaida tu, waweza kushawishika kusema "basi nitakununulia simu mpya" au "nitakutumia simu mpya." Hapo utakuwa umeshajigeuza ATM.

Hata hivyo, haina maana kuwa kila binti mrembo atakaye-request friendship kwenye Facebook ni tapeli. Na sio kila friend atakayekuomba msaada kwa Facebook ni tapeli. Kuna watu wanaomba misaada ya dhati. Cha muhimu ni "kuwa na machale."

Ni muhimu kutambua kuwa ushauri niliotoa hapo juu haumaaniishi kwamba 'matapeli wa Facebook' ni mabinti au wanawake pekee. Tunaishi zama za ajabu kabisa ambapo kuna ' vijana wengi tu wa kiume au wanaume wazima wanaowinda akinadada au kinamama wa kuwalea au kuwatapeli.' Kwahiyo ushauri huo ni kwa jinsia zote. 

Kwa akinadada au kinamama , ukikutana na 'handsome boy' mwenye dalili kama hizo hapo juu, basi ni muhimu kuskilizia 'machale' yako. Ndio kuna akina Brad Pitt kibao ambao bado wapo single na wanatafuta marafiki wa kike au wenza, lakini wengine ni matapeli tu.

Endelea kutembelea blogu hii kwa makala mbalimbali kama hii na nyinginezo. Na ususahau ku-share na mwenzio kwa sababu SHARING IS CARING.

29 May 2016

Mama mpendwa,ilikuwa siku kama yale leo,miaka minane iliyopita,uliondoka hapa duniani wakati tunakuhitaji sana.Japo miaka minne inaweza kuonekana ni muda mrefu kusahau machungu,kwangu mwanao imeshindikana.Kila siku ya Mungu ninaposali kukuombea pumziko na raha ya milele huko ulipo,hujikuta napatwa na uchungu usioelezeka.Kwa kifupi,mama mpendwa,kila siku baada ya kifo chako-siku kama ya leo miaka minane iliyopita,imeendelea kuwa ni hudhuni na majonzi yasiyoelezeka.

Mama mpendwa,ulikuwa ni zaidi ya mama kwangu,kwa mumeo marehemu Baba Mzee Chahali (aliyeungana nawe huko peponi mwaka jana),na kwa wanao wote na ndugu na jamaa.Nakumbuka mwaka 2005 nilipokuja likizo nyumbani,ulirukaruka kwa furaha,ukanikumbatia na kunipakata mwanao,ukaniandalia maji ya kuoga,ukanifanya nijsikie kama mtoto mchanga. Sikujua kuwa furaha ile ya mzazi kumwona mwanae waliopoteana kitambo kidogo sintoipata tena maishani.Inaniuma sana.
Marehemu mama akicheza siku ya harusi ya mwanae wa nne. Yeye na marehemu baba walijaliwa kupata watoto tisa, mmojaalifariki  na tukabaki wanane, wanaume sita na wanawake wawili.
Nakumbuka wakati huo ambapo wewe na marehemu Baba mlikuwa mnasherehekea miaka 50 ya ndoa yenu,ulinipa mafundisho mengi kuhusu maisha,ndoa, upendo na zaidi ni kumweka mbele Mungu katika kila ninalofanya. Kabla ya kifo chako, nilikuwa nauangalia mkanda niliowarekodi wewe na  marehemu Baba,na kila nilipofanya hivyo niligundua kuwa nina bahati ya pekee kuwa na wazazi wanaonipenda kiasi hicho. Sikujua kuwa mahojiano yale ndio ulikuwa wosia wako na marehemu baba kwangu mwanenu. Kwa sasa sina nguvu ya kuangalia video hiyo, kwani kila nikijaribu naishia kububujikwa na machozi.

Nakumbua nilipokwenda chumba cha maiti na kukuona umelazwa kwenye zile friji wanzohifadhia maiti. Nilikugusa mama,nilitaraji muujiza kwamba ungeamka na ndoto ile mbaya ingeisha. Hukuamka hadi leo hii.

Hospitali Teule ya Mtakatifu Fransisko ambapo marehemu mama alilazwa akiwa amepoteza fahamu kwa zaidi ya miezi mitatu hadi alipofariki siku kama ya leo miaka minane iliyopita

Mama,inaniuma sana kwani nilipokuja kukuuguza Februari 2008 ulikuwa umeshapoteza fahamu. Ulipokuwa Muhimbili na baadaye St Francis, Ifakara,nilikuwa najaribu kukusemesha.Kama vile ulifahamu mwanao nimekuja kukuuguza,kuna nyakati ulikuwa unatoa tabasamu lako lenye mwanya ulionirithisha. Nikategemea ungemka na kunieleza japo neno moja.Kwa bahati mbaya hadi unafariki hukuweza kuniambia chochote. Iliniuma sana, inaniuma sana na itaendelea kuniuma sana, mama.

Kabla marehemu baba hajaungana nawe huko uliko, nilikuwa na wakati mgumu sana kila nilipopiga simu nyumbani kwa wakati wa uhai wako, nilizowea kuwa nikimaliza kuongea na Baba anakupa simu wewe tupige stori. Na kila nilipoongea nawe nilijisikia kudeka kutokana na upendo wako usiomithilika. Baada ya kifo chako, na kabla marehemu baba hajafariki, kila nilipompigia simu mzee huwa nilijikuta najisahau na nataka kumwambia Mzee akupe simu niongee nawe,kisha nakumbuka kuwa hauko nasi. Sasa ndio imekuwa uchungu maradufu kwani kila nikipiga simu nyumbani, ninatamani kuongea nawe na marehemu baba kisha nakumbuka kuwa hampo nasi.

Nyakati nyingine baadhi ya watu wangu wa karibu (ninao wengi kutokana na malezi bora uliyonipatia) huwa wananiona kama dhaifu ninapowaeleza uchungu nnilio nao takriban kila siku tangu ufariki wewe na baadaye marehemu baba.Siwalaumu,kwani wanachojitahidi kufanya ni kunishawishi nikubali ukweli kuwa hampo nasi na haiwezekani kuwarejesha. Kuna wakati wananichukiza kwani najihisi kama hawaelewi jinsi kifo chako kinavyoniathiri.Lakini baadaye akili hunirejea na kutambua wanachofanya ni kujaribu kunisaidia tu.


Mama mpendwa, sijui nisemeje. Rafiki zako wakubwa, wanao vitinda-mimba,Kulwa na Doto, ndio wananitia uchungu zaidi, Wanawa-miss mno wewe na marehemu baba kwa sababu ndio uhusiano wenu ulikuwa zaidi ya kati ya wazazi na vitinda-mimba wao. Nakumbuka siku zile nawapigia simu na kuwasikia mnacheka,mnataniana na kunipa kila aina ya faraja. Kwa sasa imebaki kumbukumbu tu.

Mama mpendwa,siku ya mazishi yako Padre alituambia maneno haya: "Mama Adelina alikuwa mtu wa watu, na kila anayemjua anafahamu hilo. Japo mnaomboleza kifo chake, lakini mnapaswa kupata faraja kuwa kutokana na matendo yake mema, Baba Yake wa Mbinguni Ameamua kumchukua.Sote tulimpenda lakini Mungu alimpenda zaidi,na ndio maana amemchukua." Maneno hayo ndio nguvu pekee inayonisaidia kumudu kufanya mambo mengine maishani. Nguvu nyingine niliyonanyo ni imani kuwa wewe na marehemu baba mnaendelea kutuombea huko mlipo.

Nyumba ya milele ya marehemu Adelina 

Basi naomba nikuage tena mama kwa kumwomba BWANA AKUPATIE NA MAREHEMU BABA PUMZIKO LA MILELE NA MWANGA WA MILELE AWAANGAZIE, MPUMZIKE KWA AMANI AMEEN.


27 May 2016


Makala hii imechapishwa katika toleo la wiki hii la gazeti la RAIA MWEMA lakini tovuti ya gazeti hilo haijaweka habari mpya, kwahiyo nimeonelea ni vema nikiitundika hapa (na sina hakika lini Raia Mwema wata-update tovuti yao). Kichwa cha habari cha makala hii gazetini kinaweza kuwa tofauti na hiki nilichotumia kwenye blogu. 

Ijumaa iliyopita itabaki kuwa siku ya kumbukumbu kwa muda mrefu katika siasa za nchi yetu na medani nzima ya uongozi wa taifa letu. Siku hiyo, kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi mno, Rais wa nchi yetu alimtimua waziri wake mwandamizi ‘bila kuuma maneno’

Tukiweka kando zama za utawala wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, tangu tupate uhuru hadi alipong’atuka mwaka 1985, kipindi ambacho kutokana na urefu wake kilishuhudia majeruhi kadhaa wa kisiasa, kwa zaidi ya miaka 30 Tanzania yetu haijashuhudia kulichofanywa na Rais Dkt John Magufuli mwishoni mwa wiki iliyopita ‘alipomtumbua’ aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga kwa kosa la kuingia bungeni akiwa amelewa.

Uzito wa hatua hiyo unatokana zaidi na mambo makuu matatu. Kwanza, Kitwanga ni rafiki wa muda mrefu wa Rais Magufuli, na wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka jana, alimtambulisha kama mtu anayemfahamu vizuri, waliyesoma pamoja Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Bila kujali uzito wa kosa la Kitwanga, ilihitaji ujasiri mkubwa kwa Magufuli kumtimua ‘hadharani’ rafiki yake huyo.

Pili, uzito wa hatua hiyo unatokana na hicho nilichokiandika katika paragrafu iliyotangulia; katika miaka 10 ya utawala wa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi wa Awamu ya Pili, miaka 10 ya utawala wa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa wa Awamu ya Tatu, na miaka 10 iliyomalizika mwaka jana ya utawala wa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete wa Awamu ya Nne, hakujawahi kutokea hatua kama hiyo aliyochukua Rais Magufuli.

Kila ilipojitokeza kasoro ya kiutendaji, marais waliotangulia waliishia aidha kufanya mabadiliko ya baraza la mawaziri pasipo maelezo ya kutosha kuwa “uwaziri wa flani umetenguliwa kwa sababu flani” au pengine waziri kutolewa wizara moja na kupelekwa wizara nyingine. Na hali hiyo ya ‘boronga hapa uhamishiwe kule’ ilikuwepo pia katika zama za Awamu ya Kwanza ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.

Kwa kifupi, Dokta Magufuli amevunja mwiko wa kisiasa uliodumu kwa muda mrefu mno, na kwa hilo tu anastahili kila aina ya pongezi, sio tu kwa sababu ya kuandika upya historia ya taifa letu bali ukweli kwamba hatua hiyo inamtambulisha Rais wetu kama mtu anayeweka mbele zaidi maslahi ya taifa letu kuliko maslahi binafsi.

Tatu, miaka nenda miaka rudi, baada ya kuingia kwenye mfumo wa siasa za vyama vingi, marais wetu kama wenyeviti wa chama tawala CCM, wamekuwa wakijitahidi kadri wawezavyo kujifanya ‘viziwi’ kila zinapojitokeza ‘kelele’ kutoka vyama vya upinzani. Kabla ya ‘kutumbuliwa,’ baadhi ya vyama vya upinzani vilikuwa vikimlalamikia Rais Magufuli kuwa ‘anamlinda Kitwanga’ kuhusiana na kashfa ya ufisadi ya Lugumi, na vilikuwa vikipiga kelele kumtaka ‘amtumbue’ Kitwanga.

Sasa, katika mazingira ya kawaida tu, ingeweza kuwa vigumu kwa Dkt Magufuli kumtimua Kitwanga kwa kuhofia “kuwapa wapinzani ushindi wa bure” katika suala hilo. Kwamba, wapinzani wangeweza kujigamba kuwa shinikizo lao ndio limepelekea Rais ‘kumtumbua’ rafiki yake.

Na katika hilo, ni muhimu kutambua kuwa Dkt Magufuli “ana wabaya wake ndani ya CCM,” na angeweza kuchelewa kumtimua Kitwanga kwa vile “wabaya wake hao” wangeweza kutafsiri kitendo hicho kama udhaifu, kwa maana ya “kuendeshwa na kelele za Wapinzani.”

Kwa kiwango kikubwa, hatua hiyo ya Dkt Maguguli imepokelewa vizuri na Watanzania wengi, hasa ikizingatiwa kuwa licha ya ‘kumtumbua Kitwanga,’ suala zima la kuchukua hatua stahili pale inapohitajika ni kama kitu kigeni kwa wananchi wengi, ikizingatiwa kuwa kwa muda mrefu nchi yetu imekuwa ikiongozwa kwa siasa za kulindana. Kwahiyo, ahadi za Dkt Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu na baada ya kuapishwa kuwa rais, kwamba hatomwonea aibu mtu yeyote zimethibitika zaidi katika suala hilo la ‘kumtumbua’ Kitwanga.

Hata hivyo, Tanzania yetu imegawanyika kuliko wengi tunavyoiona. Na mgawanyiko mkubwa wa nchi yetu ni athari ya moja kwa moja ya uchaguzi mkuu uliopita. Kuna kundi kubwa tu la wenzetu ambao hadi dakika hii hawataki kuamini kuwa “mgombea wao alishindwa.” Hapa namzungumzia mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Sasa kwa wenzetu hao, Dkt Magufuli sio tu “hakushinda kihalali” bali pia ni “dikteta anayetumbua watu bila kuzingatia sheria, mwenye jazba, nguvu ya soda” na kila baya unaloweza kumuongelea kiongozi.

Waungwana hawa walikuwa wakipiga kelele mno kumtaka Rais amwajibishe ‘swahiba wake’ Kitwanga ili kuwezesha uchunguzi wa kashfa ya Lugumi ufanyike kwa ufanisi zaidi hasa kwa vile nafasi ya Kitwanga kama Waziri mwenye mamlaka juu ya Jeshi la Polisi ingeweza kuathiri uchunguzi huo.

Akina sie pia tulimshauri Rais afikiri kutengua uwaziri wa Kitwanga, lakini tunapopishana na wenzetu hao ni kwamba hata baada ya Rais “kusikiliza kilio cha kumtaka amtumbue Kitwanga” bado wanamlaumu. Baadhi wanadai kuwa “kumtumbua Kitwanga ili kuuwa suala la Lugumi.” Wengine wanakwenda mbali zaidi na kudai “suala hilo ni mchezo wa kuigiza usioingia akilini.” Wanasema eti “Kitwanga ametolewa kafara ili kuwanusuru vigogo flani.”

Lawama kwa Dkt Magufuli hata baada ya kuweka kando urafiki na kuchukua hatua stahili dhidi ya swahiba yake, zinaweza kumvunja moyo. Tukumbuke, yeye ni binadamu kama sie. Na ni wazi, unapokubali lawama kutoka kwa mtu wako wa karibu ili tu kukidhi matakwa ya jamii, kisha ukaishia kulaumiwa na baadhi ya wanajamii, inavunja moyo. Hata hivyo, ninatumaini kuwa Dkt Magufuli hatoyumbishwa na lawama hizo. Kimsingi, zilikuwepo, zipo na zitaendelea kuwepo kwa sababu tatizo sio anachofanya bali imani fyongo ya “wenzetu” kuwa aliyepaswa kuwa rais ni yule “mtu wao.”

Kama kuna lawama au kasoro inayoweza kujadiliwa basi ni kuhusu utaratibu wa kiusalama uanaofahamika kama “vetting.” Kabla ya kuteuliwa, jina la Kitwanga lilipelekwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa ajili ya kufanyiwa vetting. Swali, je Idara hiyo ilishindwa kubaini kuwa “Kitwanga ana kasoro ya ulevi ambayo sio tu ingeweza kuathiri utendaji kazi wake bali pia ingeweza kuhatarisha usalama wa taifa”? Je inawezekana kuwa Idara hiyo ilitekeleza jukumu lake ipasavyo lakini ‘mfanya uteuzi’ akapuuzi ushauri wa mashushushu hao?

Huu sio muda wa kunyoosheana vidole. Kama Idara yetu ya Usalama wa Taifa ilizembea kwenye vetting basi na ijirekebishe haraka. Kama ‘mfanya uteuzi’ alipuuzia ushauri wa mashushushu hao basi ameshapata funzo muhimu.

Ikumbukwe kuwa hadi muda huu hatufahamu kuwa ‘tatizo la ulevi wa Kitwanga’ limeathiri vipi utendaji wake wa kazi kama Waziri wa wizara nyeti ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kiusalama, hakuna kitu majasusi kutoka nchi za nje wanaombea kama kukutana na mtendaji wa serikali katika eneo nyeti ambaye ana udhaifu kama huo wa ulevi. Na ninaamini kuwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa wanafahamu fika jinsi majirani zetu walivyojaza majasusi ndani ya Tanzania yetu, hususan baada ya ujio wa Dkt Magufuli unaoanza kuifanya nchi yetu kuwa tishio kiuchumi kwa majirani zetu.

Ni matumaini yangu makubwa kuwa kutafanyika uchunguzi wa kina kuhakikisha kuwa mapungufu ya Kitwanga hayakuathiri usalama wa taifa letu kwa maana ya kwamba hakuna aliyetumia ‘ulevi wake’ kum- “blackmail” ili atoe siri za serikali.

Kiu kubwa kwa Watanzania kwa muda huu ni kuona Bunge litachukua hatua gani dhidi ya ‘mwenzao.’ Hata hivyo, ishara mbaya zimeanza kuonekana baada ya Naibu Katibu wa Bunge, John Joel, kunukuliwa akidai kuwa “hakuna kifungu chochote cha kanuni za Bunge kinachomzuwia mtu kuingia Bungeni akiwa amelewa.” Yaani hawa waheshimiwa wana kinga dhidi ya Kanuni za Utumishi wa Umma zinazokataza “tabia inayovunja heshima ya utumishi kwa umma hata nje ya mahali pa kazi” kwa mfano ulevi.

Lakini kubwa zaidi ni kuona kuwa ‘kutumbuliwa’ kwa Kitwanga haukuathiri uchunguzi wa suala tete la Lugumi. Kimsingi, kwa kutolewa uwaziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kamati Teule ya Bunge inayochunguza suala hilo sasa haina kisingizio chochote cha kutowapatia Watanzania kile wanachostahili: ukweli kamili kuhusu suala hilo.
Nimalizie makala hii kwa kumpongeza Rais Dkt Magufuli kwa kuwakumbusha watendaji wote wa serikali kuwa “zama za nchi kujiendesha yenyewe (autopilot) zimekwisha, na sasa ‘Hapa Ni Kazi Tu’.” Kwamba kiongozi atakayezembea atatumbuliwa bila kuonewa haya. Kadhalika, hongera nyingi kwa Rais wetu kwa kuweka mbele zaidi maslahi ya taifa kuliko maslahi binafsi, umekubali lawama kuliko fedheha. Mwenyezi Mungu akulinde katika utendaji kazi wako, wenye hila mbaya washindwe na uendelee kuwatumikia Watanzania kwa uwezo wako wote.

Mungu Mbariki Rais wetu Dkt John Magufuli.
Mungu Wabariki Watanzania wote wenye kuitakia mema nchi yetu.

Mungu Ibariki Tanzania.

24 May 2016

Sakata la kutumbuliwa kwa aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, linazidi kutawala vichwa vya habari, huku maendeleo mapya yakiashiria kuwa kuna mengi yanayoweza kuwa yanaendelea 'nyuma ya pazia.'

Jana, watu waliojitambulisha kama 'wana-jimbo wa Misungwi' walitoa tamko kwa waandishi wa habari. Hebu ndugu msomaji mpendwa, fanya kulisoma tamko hilo kwanza, kisha bingirika nami kwa uchambuzi zaidi, and trust me, sintokuangusha haha!

First thing first, hawa 'wana-jimbo wa Misungwi' WAMETUMWA NA NANI? Ninauliza hivyo kwa sababu hisia yangu ya sita inanituma kuamini kuwa hawajajitolea wenyewe tu kutoa tamko hilo. Hawa wametumwa, no doubt about that. Lakini hatujui nani kawatuma.

Kwa kuitegemea tena hisia yangu ya sita, yayumkinika kuhisi kuwa hao 'wana-jimbo' ni wapambe tu wa Kitwanga. Twende mbali zaidi, ninahisi watu hao ni sawa na spika tu ya kumwezesha Kitwanga asikike.. 

Tetesi zinaeleza kuwa Kitwanga alikuwa 'mtu wa kinywaji' kitambo sasa. Na kwa wenzetu ambao hawajawahi kugusa kinywaji, ukweli upo hivi: hakuna mtu anayeitwa 'mnywaji wa muda mrefu.' Mtu wa aina hiyo ni MLEVI. Period. Na ulevi, japo si dhambi au kinyume cha sheria, una athari zake. Kuna mlolongo mrefu wa jinsi ulevi ulivyobomoa maisha ya watu mbalimbali. Kwahiyo, tukiafikiana kuwa Kitwanga ni mlevi, basi ilikuwa suala la muda tu kabla haijamlipukia. Kwa lugha nyingine, Bwana Kitwanga alikuwa kama time-bomb, muda wowote ule lingetokea la kutokea.

Mengi yameshaongewa tangu Kitwanga atumbuliwe na Rais Magufuli hapo juzi, makubwa zaidi yakiwa ni pamoja na madai kuwa ishu hiyo ni mcheoz wa kuigiza. Kwamba kutumbuliwa kwa Kitwanga ni mkakati wa makusudi wa kuiua ishu ya Lugumi. 

Siafikiani na mtazamo huo kwa sababu kama kweli Magufuli alikuwa anataka kumuokoa rafiki yake alikuwa na njia nyingi tu, moja ya wazi ikiwa ni 'kuziba masikio,' kwa maana ya kupuuza kelele za waliotaka Kitwanga atumbuliwe.

Wengine wanadai kuwa kweli Kitwanga alikuwa amelewa, lakini hakulewa kwa hiari yake bali 'kinywaji chake kilifanyiwa utaalam,' wakijaribu kutushawishi kuwa Kitwanga alihujumiwa. 

Hizi ni hisia tu zisizo na uthibithso wowote. Jamaa alikuwa 'chapombe,' na wanaomfahamu hawashangazwi na hilo tukio la majuzi au kutumbuliwa kwake. Pombe sio chai, siku ya siku lazima itamwadhiri mtu.

Madai mengine ambayo yanahusiana na hayo ya 'kinywaji cha Kitwanga kufanyiziwa' yanauhusisha utawala wa Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, ambako ndiko suala la Lugumi lilianzia. In fact, hizo tuhuma za 'kinywaji cha Kitwanga kufanyiziwa' zinawahusu baadhi ya watu waliokuwa karibu na utawala huo. 

Na kama msomaji ulivyoona katika 'tamko la wana-jimbo wa Misungwi' hapo juu, mmiliki wa Kampuni ya Lugumi, Said Lugumi na mtoto wa Rais Kikwete, Ridhiwani, wametajwa kuwa miongoni mwa wanaomhujumu Kitwanga.

Sawa, ishu ya ufisadi wa Lugumi ipo complex lakini kudai kuwa akina Lugumi na Ridhiwani ndo waliomfanyizia Kitwanga hadi akaishia kutimuliwa na Rais Magufuli ni hisia tu zisizo na mantiki. Haina mantiki kwa vile haiingii akilini jinsi gani hao jamaa wangemudu kumhujumu Kitwanga na wakati huohuo kumshinikiza Magufuli amchukulie hatua.

Kwa upande mwingine, Spika Job Ndugai, amejiingiza matatizoni 'kitoto' kwa kauli yake isiyo na busara ianyoashiria kuwa 'ulevi wa Kitwanga ni cha mtoto, kuna waheshimiwa wanavuta bangi na kubwia unga.' Really? Yaani Spika anawafahamu waheshimiwa wanaotenda makosa ya jinai lakini anawahifadhi!? 

Sasa, inasemekana baadhi ya wabunge wameamua kumkalia kooni awataje hao 'wabunge wavuta bangi na wala unga' na ajieleze kwanini hakuwaripoti kwa mamlaka husika.

Kadhalika, baadhi ya 'wazushi' wanamtaka Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kuonyesha uthibitosho kuwa kweli Kitwanga alikuwa 'njwii' siku ile pale Bungeni hadi Rais Magufuli kuchukua hatua ya kumtumbua. Nadhani hii inalenga kumpima ubavu tu Waziri Mkuu Majaliwa kwani kila aliyeona Kitwanga akijibu swlai pale Bungeni hatoshindwa kujua kuwa alikuwa amelewa

Anyway, blogu hii inaendelea kufuatilia ishu hiyo, pamoja na ishu nyingine mbalimbali katika jamii yetu. Pia, kesho, makala yangu katika toleo la wiki hii la jarida la Raia Mwema inajadili kwa kirefu kuhusu suala hilo la Kitwanga kutumbuliwa. Usikose kupata nakala yako.

22 May 2016



Taarifa mbalimbali zinaonyesha kuwa kuna ongezeko kubwa la Watanzania wanaojihusisha na ushoga na usagaji japokuwa vitendo hivyo ni kinyume na sheria za nchi na haviendani na mila na desturi zetu.

Hata hivyo, yawezekana kushamiri kwa vitendo hivyo kunaendana na taarifa za kitafiti kuwa sie Watanzania twaongoza kwa unafiki. Wiki chache zilizopita niliweka bandiko hapa bloguni lililohusu ripoti ya utafiti wa kundi la wasomi katika chuo kikuu cha Nottingham, hapa Uingereza, ulivyobainisha kuwa Tanzania yaongoza duniani kwa unafiki.

Binafsi sikushangazwa na ripoti hiyo hasa kwa vile kuna maeneo mawili yanayothibitisha bayana unafiki wetu. La kwanza ni uhusiano kati ya ucha-Mungu wetu na maovu.

Asilimia kubwa ya Watanzania ni wacha-Mungu. Takwimu zaashiria kuwa takriban asilimia 70 ya Watanzania ni aidha Wakristo au Waislam. Wengi kati ya hao ni watu wasiokosekana kanisani au misikitini. Swali: kama wengi wetu ni waumini kiasi hicho, ni akina nani basi wanaojihusisha na ufisadi, rushwa, biashara ya madawa ya kulevya, ushirikina, na maovu mengine katika jamii?

Tofauti na huko nyumbani, ucha-Mungu hapa Uingereza ni wa kusuasua mno. Watu wengi hapa hawamtambui Mungu na wanajitambulisha kuwa hawana dini. Makanisa mengi yanageuzwa kuwa baa au kumbi za starehe kutokana na uhaba wa waumini.



Lakini licha ya udhaifu katika mahusiano kati yao na Mungu, wenzetu hawa kwa kiasi kikubwa sio wanafiki. Asilimia kubwa kabisa ya watu hawa wanaishi kwa kipato halali, wanaamini katika ukweli, kwa maana ya kusema ukweli na sio wadanganyifu, wanafuata sheria na taratibu mbalimbali, kwa mfano moja ya dhambi kuu hapa ni ukwepaji kodi, kitu ambacho ni kama hobby ya wengi wa wafanyabiashara huko nyumbani.

Eneo la pili ni suala la ushoga na usagaji. Kwa huko nyumbani, suala hili ni mwiko mkubwa, ni laana, ni kinyume na maadili yetu. Lakini kuthibitisha unafiki wetu, sio tu ushoga na usagaji upo bali pia unakua kwa kasi kubwa.

Nenda katika kitchen parties za watu maarufu na 'wakata viuno' ni mashoga huku wengi wa 'makungwi' wakituhumiwa kuwa wasagaji. Inaelezwa kuwa njia moja maarufu ya kusambaa kwa usagaji huko nyumbani ni 'makungwi' wanaofundisha mabinti (kwa malipo) jinsi ya kufanya tendo la ndoa. Hawa wametapakaa jijini Dar na baadhi wanahamia mikoani. Kimsingi, 'darasa la tendo la ndoa' wanalofundisha ni kwa kusagana na 'wanafunzi' wao.

Shughuli za 'madada wa mujini' hazijakamilika kama hakuna akina 'anti naniliu au anti nanihino.' Lakini watu haohao ndio wanaohubiri kwa sauti kubwa kuwa "habari za ushoga na usagaji huko huko kwao (wazungu)."

Kuna kitu kingine 'kichafu' ambacho Watanzania twasifika mno, nacho ni umahiri katika tendo la ndoa kinyume cha maumbile. Kwa kifupi, hii ndio sababu ya kushamiri kwa biashara ya "dawa za makalio feki ya Mchina." Tendo la ndoa kinyume cha maumbile limekuwa kama 'fasheni' kwa wengi wetu huko nyumbani na huku ugenini tunakoishi. 

Sasa, japo tendo la ndoa kinyume cha maumbile sio ushoga per se, kuna hisia kuwa wazoefu wa tabia hiyo "wakikosa nyama wanaweza kula majani." Yaani wanaume wanaopenda tabia hiyo wakikosa mwanamke wanaweza kufanya hivyo na mwanaume shoga.

UTHIBITISHO wa unafiki wetu: Well, sehemu mwafaka zaidi ya kutambua unafiki wetu kuhusu ushoga na usagaji ni INSTAGRAM. Huko, kuna mashoga wanaojinadi waziwazi. Lakini tatizo sio wao kujinadi tu bali ni idadi ya 'followers' wao. Ni wazi kuwa laiti ingekuwa watu wanachukia ushoga 'kihivyo' basi mashoga huko Insta wasingekuwa maarufu kiasi cha kupata followers hadi laki na zaidi.

Profiles hizi pichani chini ni za baadhi tu ya mashoga wa Kitanzania huko Instagram.  Je kama sie sio wanafiki na laiti tungekuwa tunauchukia ushoga 'kihivyo' hao maelfu kwa malaki ya followers kwa hao mashoga wangetaka wapi?


Ukitaka kuchimba zaidi kuhusu 'unafiki' wetu, geukia suala jingine maarufu huko nyumbani: USHIRIKINA. Kwa mujibu wa utafiti wa hivi karibuni wa taasisi moja ya kimataifa inayoheshimika kwa utafiti ya PEW ya Marekani, Tanzania ipo 'matawi ya juu' katika masuala ya juju, ndumba na ngai, tunguri, kamati ya ufundi, wanga...USHIRIKINA... kama inavyoonyeshwa kwenye chati na ramani hapo chini.




Kwa vile lawama pekee hazijengi, ni muhimu kujaribu kuangalia njia zinazoweza kutuondoa katika lindi hilo la unafiki. Binafsi, ninashauri tuwekeze zaidi katika dua na sala za dhati na sio za kinafiki. Au wewe msomaji mpendwa una maoni gani?



21 May 2016


Nianze makala hii kwa kumpongeza Rais John Magufuli kwa hatua aliyochukua jana ‘kumtumbua’ aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, kwa kosa la kuingia Bungeni akiwa amelewa.

Kadhalika, ningependa kutumia fursa hii kumshukuru kwa kuwa kiongozi msikivu. Binafsi, ‘nilikomalia’ sana kuhusu uwaziri wa Kitangwa hasa kutokana na tuhuma kuwa ni mhusika katika skandali ya Lugumi (na tetesi kuwa alikuwa mlevi - japo sikuwahi kuongelea ishu hiyo ya ulevi kwa vile niliona kama suala binafsi, alimradi haliathiri utendaji wake wa kazi). 

Kwa ‘mtaani’ hatua hiyo ya Rais Magufuli inaweza kuonekana ni ya kawaida tu, yaani kiongozi aliyefanya uteuzi wa mtu flani, hatimaye kuamua kuteungua uteuzi huo. Lakini kwa hakika, hatua hiyo ya Rais Magufuli haikuwa rahisi. 

Kwa mujibu wa taarifa, Rais Magufuli na Kitwanga wamekuwa marafiki wa muda mrefu. Wajuzi wa mambo wanaeleza kuwa hata uamuzi wa kumteua Kitwanga kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ulitokana na imani ya Rais Magufuli kwa rafiki yake huyo. Ikumbukwe kuwa wizara hiyo ni moja ya wizara nyeti ambazo kwa kiasi kikubwa hukabidhiwa kwa watu wanaoaminika mno kwa rais husika. 

Kuna kipande cha video kilichosambaa mtandaoni siku za nyuma ambacho kilikuwa kinamwonyesha Rais Magufuli kabla hajawa rais wala mgombea wa CCM, akiwa na Kitwanga, na katika maongezi yao, Kitwanga anasikika akimwambia Magufuli agombee urais (japo ni katika hali ya utani). 

Lakini pia inaelezwa kuwa hata kabla Rais Magufuli hajatangaza baraza lake la mawaziri, Kitwanga alikuwa akijigamba kuwa angepewa wizara nyeti, mara baada ya Magufuli kutangaza kabineti yake, na wizara nyeti ya mambo ya ndani ya nchi akapewa baada ya kutangazwa kabineti hiyo. 

Hata hivyo, suala hili la Kitwanga linapaswa kuamsha maswali kuhuru Idara yetu ya Usalama wa Taifa na utaratibu wa ‘kuwatafiti wateule watarajiwa wa Rais,’ kitu kinachofahamika kitaalam kama ‘vetting.’ Nina uhakika wa asilimia 100 kuwa ‘dossier’ (kabrasha maalum kuhusu mtu maalum) la Kitwanga lilipaswa kueleza bayana kuhusu tabia yake ya ulevi. Je ilikuwaje sio tu akateuliwa kuwa waziri bali pia kuteuliwa kuwa waziri katika wizara nyeti kabisa kwa usalama wa raia na nchi. Je kulikuwa na mapungufu huko Idara ya Usalama wa Taifa au walieleza hilo kabla Kitwanga hajateuliwa lakini likapuuzwa? Ni vigumu kuwa na uhakika wa kipi kilitokea. 

Kwa kuwa lengo ni kwenda mbele na si kunyoosheana vidole tu bila kutoa uushauri au kuleta ufumbuzi, binafsi ninashauri wahusika waangalie wapi walijikwaa, ili wasirudie tena kosa hilo. Vetting ya wateuliwa watarajiwa ni muhimu mno kwa sababu licha ya kuiingiza gharama serikali pale inapolazimu uteuzi husika kutenguliwa, pia inahatarisha usalama wa taifa (watu wanaotimuliwa madarakani ni rahisi kuwa recruited na maadui wa taifa ili 'kulipa kisasi').

Tukiweka kando mapungufu hayo, kitendo cha Dkt Magufuli kumtumbua Kitwanga kinapeleka ujumbe mzito kwa kila mtumishi wa serikali. Kwanza, kinaashiria kuwa Rais anafanyia kazi taarifa anazoletewa (maana hakuwepo Bungeni Dodoma wakati Kitwanga akiwa 'bwii' mjengoni. 

Lakini pia kitendo hicho kinaashiria kuwa mfumo wa mawasiliano ndani ya serikali umerejea kama wa zama za Nyerere, pasipo 'taarifa kuvuja' kabla ya kufika mahali stahili. Hali hii itapelekea watendaji wa serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri kuwa makini zaidi kwani hawajui nani anawachunguza au nini kinaripotiwa kwa Rais kuhusu wao.

Tukiweka hilo kando, binafsi nimefarijika sana baada ya kusikia taarifa za Kitwanga ‘kutumbuliwa’ kwa sababu nilipiga kelele za kutosha kuhusu uongozi usioridhisha wa mheshimiwa huyo. Nilianza kitambo kuhoji kuhusu utendaji kazi wa waziri huyo.

Suala la kwanza ‘kumshikia bango’ lilikuwa kauli zake za utata kuhusu kupambana na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Hili nililiandikia MAKALA HII. 







Baadaye, ikaibuka skandali ya Lugumi, na kwa hakika sikuchoka kupiga kelele, hususan kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kama inavyoonekana hapa chini 



Sambamba na kelele hizo hatimaye niliamua kuandika MAKALA HII 


Ni matarajio yangu makubwa kuwa makala hii itamhamasisha kila msomaji kuwa na msimamo, na kisha kusimama imara katika msimamo huo, sambamba na kuhakikisha kuwa anachosimamia ni sahihi, na kuendelea kuupigania hadi mafanikio yapatikane. Sio kazi rahisi lakini mara nyingi vitu vizuri, au vinavyodumu, huwa havipatikani kirahisi. 

Mwaka 2006, niliandika MAKALA HII kuhusu suala la mkataba wa kufua umeme, uliopelekea skendo ya Richmond, na nikaendelea kupiga kelele hadi mwaka Februari 2008 baada ya mhusika mkuu katika skendo hiyo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujiuzulu. Hata hivyo, ishu hiyo ilinigharimu mno kimaisha. 

Na hivi majuzi, nilijaribu ‘kuwashikia bango’ wahusika wa Mamlaka ya Mawasiliano TCRA, na nikawatwanga MAKALA hii. 


Siku chache baadaye, bosi wa taasisi hiyo akatumbuliwa. 


Na majuzi tu, Ubalozi wetu hapa Uingereza ulitaka kutufanyia 'uhuni' katika ziara ya Waziri Mkuu, ambapo awali kulikuwa na mpango wa kumkutanisha Waziri Mkuu na kundi dogo tu la Watanzania wanaoishi hapa. Kelele nilizoshiriki kuibua zilisaidia, na hatimaye mkutano huo wa Waziri Mkuu ulifanywa kuwa wa wazi kwa kila Mtanzania mkazi wa hapa kuhudhuria. Nimeelezea kwa kirefu kuhusu sakata hili katika MAKALA HII.

Sitaki kujisifu kuwa kelele zangu pekee ndio zinapelekea hatua kusudiwa kuchukuliwa. Hapana. Ninachojaribu kuonyesha ni ushiriki wangu katika harakati za kudai mabadiliko kwa kupitia maandishi, “kelele zetu” iwe hapa bloguni, kwenye mitandao ya kijamii au kwa njia ya makala. Pia, kwa kuwaeleza wasomaji kuhusu mafanikio ya 'kelele zetu' inasaidia kuhamaisha watu wengi zaidi kutambua umuhimu wa harakati kama hizi katika kuleta mabadiliko kusudiwa


Mara nyingi tunapopiga kelele hizo tunaishiwa kukebehiwa, kuonekana vimbelembele, tusio na vitu muhimu vya kufanya katika maisha yetu binafsi, na shutuma kama hizo. Lakini pindi kelele zetu zinapozaa matunda, walewale waliokuwa wakitukebehi huwa mstari wa mbele “kusaka sifa.” 

Kimsingi, harakati hizi sio za kusaka ujiko au madaraka. Ni kile nilichoeleza awali: kuwa na msimamo na kusimama thabiti katika msimamo huo hadi ufumbuzi wa tatizo husika upatikane.

Nimalizie makala hii kwa kumpongeza sana Rais Magufuli kwa ‘kumtumbua’ Kitwanga. Wanaohisi kuwa kutambuliwa huko ni ‘kuficha kombe’ la ishu ya Lugumi, ombi langu kwao ni wavute subira. 

Sakata la Lugumi sasa litachukua sura mpya, na tusishangae kusikia watu wakiburuzwa mahakamani hivi karibuni. Pia suala hili la kutambuliwa Kitwanga linaweza kumpa fursa Rais Magufuli fursa ya kuwatumbua angalau mawaziri mawili hivi ambao mwenendo wao umekuwa wa kusuasua. Fursa ya kuwatumbua inatokana na kutambuliwa kwa Kitwanga ambako kutamlazimu Rais kufanya ‘reshuffle’ ndogo.

20 May 2016


WIKI iliyopita yaweza kubaki kwa muda mrefu kwenye kumbukumbu za Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Kwa upande mmoja, wiki hiyo ilimalizika kwa mkutano kati ya baadhi yao na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, na kwa upande mwingine wiki hiyo ilitawaliwa na mizengwe ya ‘kuzuia’ fursa kwa wengi kukutana na Waziri Mkuu.

Awali, zilipatikana tetesi kwamba Rais John Magufuli angefanya ziara ya kikazi hapa Uingereza, lakini baadaye ikafahamika kuwa Waziri Mkuu Majaliwa ndiye angemwakilisha.

Hatimaye Waziri Mkuu aliwasili hapa kwa mara ya kwanza tangu ashike wadhifa huo, na pia kuwa kiongozi wa kwanza wa kitaifa kuzuru nchini hapa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani.

Wengi wa Watanzania wanaoishi nchini hapa walionyesha kiu kubwa ya kukutana na kiongozi huyo mpya, hususan kusikiliza visheni ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa Tanzania na Watanzania, ikiwa ni pamoja na tunaoishi nje ya nchi yetu.

Hata hivyo, kiu hiyo ilikumbana na kikwazo kutoka Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza, haukujali kutoa taarifa yoyote kwa Watanzania wanaoishi hapa kuhusu ujio wa kiongozi huyo wa kitaifa wala kueleza iwapo angekutana nao kwa maongezi.
Baadaye zikasikika tetesi kuwa Ubalozi huo (aidha kama ofisi au baadhi ya maofisa wake) ulitoa mwaliko kwa takriban watu arobaini hivi kuhudhuria ‘kikao’ na Waziri Mkuu. Tetesi hizo hazikueleza jinsi gani ‘wawakilishi’ hao walivyopatikana, lakini kilichoonekana bayana ni suala hilo kuzingirwa na usiri mkubwa.

Binafsi, nilianzisha jitihada za kuutaka Ubalozi uangalie umuhimu wa kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anayeishi hapa anapatiwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo. Awali niliweka ujumbe kwenye kundi la ‘Whatsapp’ la Watanzania wanaoishi hapa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha.

Baadaye nilichukua jukumu la kuandika makala katika blogu yangu baada ya kuzungumza na Watanzania kadhaa wanaoishi hapa, na ambao walionyesha bayana kutoridhishwa na jinsi Ubalozi wetu ulivyoonekana ‘kuhujumu’ uwezekano wa Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa kukutana na kiongozi wao.

Kwa bahati nzuri, ‘kelele’ za makala hiyo na ‘kilio’ kilichofikishwa kwenye kituo kimoja cha radio huko nyumbani na baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa, zilizaa matunda. Hatimaye, Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa tamko kuwa Waziri Mkuu angekutana na Watanzania wanaoishi hapa.

Ofisi ya Waziri Mkuu pia ilijaribu kujitetea kuwa haikuhusika na maandalizi ya mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa, japo haikuwahi kulaumiwa na mtu yeyote kwa sababu utaratibu uliozoeleka ni kwa Ubalozi (sio Wizara au ofisi za huko nyumbani) kufanya maandalizi ya mikutano ya viongozi wa kitaifa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa upande mwingine taarifa hiyo ilikuwa kama inakanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalumu waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa. Hata hivyo, kulikuwa na uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kwa kundi la watu kadhaa tu kukutana ‘kwa faragha’ na Waziri Mkuu.

Uthibitisho huo ulisikika baada ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu hapa kujirekodi na kuweka ujumbe wa sauti (voice note) kwenye kundi la Whatsapp (la Watanzania wanaoishi hapa) ambapo pamoja na mambo mengine alikebehi jitihada za kutaka Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa wapate fursa ya kukutana na Waziri Mkuu. Alidai kuwa “hata Rais anapoongea na wazee jijini Dar haimaanishi basi wazee wote wa Dar wataalikwa kwenye mkutano huo.” Alidai kuwa hakuna ubaya kuteua watu wachache tu kuzungumza na Waziri Mkuu, na kuongeza kuwa ‘Watanzania wamezoea kuja wengi japo walioalikwa wachache tu.’

Kwa upande mmoja ninaipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ‘kusoma alama za nyakati’ na kuruhusu mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa kuwa wa wazi. Kwa upande mwingine ninaikosoa kwa sababu tamko lake kuwa mkutano huo utakuwa wa wazi sio tu lilitolewa Ijumaa - siku moja kabla ya mkutano – lakini pia haikubainisha muda wala sehemu kutapofanyika mkutano huo. Pengine ni mazoea tu ya huko nyumbani, lakini maisha ya hapa kwa kiasi kikubwa yanaambatana na ‘ratiba kali,’ na taarifa ya muda mfupi na isiyojitosheleza kimaelezo (kama hiyo ya Ofisi ya Waziri Mkuu) inaweza kuwa iliwanyima fursa watu wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

Kwa upande wa Ubalozi wetu hapa, hadi wakati ninaandika makala hii haujafanya jitihada za kuwaomba radhi Watanzania wanaoishi hapa kwa ‘mpango wake fyongo’ ambao laiti ungefanikiwa, basi mkutano huo wa Waziri Mkuu ungekuwa ni kati yake na ‘wateule wachache’ tu. Kadhalika, ofisa ubalozi aliyejirekodi na kukebehi harakati zetu kudai fursa kwa wote kuhudhuria mkutano huo angeomba radhi kwa kauli zake zisizoendana na wadhifa wake wala ustaarabu wetu Kitanzania.

Pengine utata huo ungeweza kuepukika laiti pande mbili zinazohusika na ziara za viongozi wa kitaifa zingewajibika ipasavyo. Kwanza, ubalozi wetu hapa ungeweza kutengeneza mazingira mazuri ya mawasiliano na Watanzania wanaoishi hapa kwa kutumia mitandao ya kijamii au njia nyingine mwafaka. Hisia ni kwamba ‘ukimya’ uliojitokeza kuhusu ziara hiyo ulikuwa wa makusudi (yaani mkutano huo ulipaswa kuwa ‘shughuli ya wateule wachache’).

Pili, idara yetu ya masuala ya usalama imekuwa na utaratibu wa kutanguliza maafisa wake eneo ambalo kiongozi wa kitaifa atatembelea, kitu kinachofahamika kiintelijensia kama ‘advance party.’ Na moja ya majukumu ya waliomo kwenye ‘msafara’ huo ni kubaini yanayoweza kujitokeza wakati wa ziara husika. Kwa hiyo, laiti wangetupia macho ‘sehemu’ za maongezi ya Watanzania wanaoishi hapa (kwa mfano kundi lao la ‘Whatsapp’) basi wangeweza kubaini mapema kuwa kuna kiu ya mkutano na Waziri Mkuu sambamba na shutuma kuwa ubalozi unakandamiza kiu hiyo.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa ofisi zetu za ubalozi popote zilipo ziwe kiunganishi kati ya Watanzania wanaoishi nchi hizo na nchi yetu, sio kwa masuala yanayohusu hati za kusafiria tu na masuala ya kidiplomasia bali kudumisha Utanzania wetu kwa upendo, umoja na mshikamano. Balozi zetu kadhaa zimekuwa zikilaumiwa kwa ‘kutokuwa na msaada,’ sambamba na kauli za jeuri/kiburi kwa baadhi ya maofisa wetu wa ubalozi, hali inayodhaniwa inatokana na baadhi yao kukaa huku nje muda mrefu mno kiasi cha ‘kuwadharau Watanzania wenzao.’

Mwisho, iwe ni kwa busara zake binafsi au ofisi yake, shukrani za pekee kwa Waziri Mkuu Majaliwa kuweza kuongea na Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Takriban kila aliyehudhuria mkutano huo ameridhishwa na hotuba ya Waziri Mkuu ambayo imetoa matumaini makubwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuiboresha Tanzania yetu katika kila eneo.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.