10 Feb 2017


Kwamba Idara yetu ya Usalama wa Taifa imekuwa ikibebeshwa lawama mbalimbali kwa takriban 'kila baya' linaloihusu Tanzania yetu, sio siri. Ni kitu cha wazi ambacho ninaamini hata wana-Usalama wetu pia wanakifahamu.

Hata hivyo, kwa kiasi kikubwa lawama hizo huchangiwa na uelewa mdogo au usiopo kabisa kuhusu dhamana muhimu ya taasisi za usalama wa taifa kwa nchi husika, na jinsi taasisi hizo zinavyofanya kazi muda wote kuhakikisha usalama wa nchi husika.

Lakini pengine kabla ya kuingia kiundani kuhusu mada yangu, nigusie maongezi yangu na jamaa yangu mmoja, shushushu mstaafu kutoka nchi moja ya Afrika Magharibi. Jana aliamua 'kunifungukia,' kwanini mtu mwenye umri wa kati kama yeye ni 'shushushu mstaafu' (tumezowea kuona wastaafu wakiwa watu wenye miaka 50 na kuendelea, lakini huyo bwana ni wa umri wa miaka thelathini na kitu tu).

Alinidokeza kwa kifupi kuwa alilazimika 'kutoroka' nchini kwake baada ya kufeli kwa jaribio la mapinduzi katika taifa analotoka ambalo huko nyuma lilikuwa kama linapendelea zaidi mapinduzi kuliko chaguzi.  Alidai kuwa "mapinduzi hayo yalikuwa ni kwa minajili ya kuikwamua nchi hiyo kutoka katika nira ya utawala wa kidikteta wa kijeshi."

Hadi kufikia hatua hiyo ya maongezi hayo, ilitokana na huyo jamaa kuwa alitembelea kwenye ukurasa wangu wa Facebook, na kuona matangazo ya kitabu changu kuhusu taaluma ya Uafisa Usalama wa Taifa (USHUSHUSHU). Awali hakuelewa kitabu kinahusu nini kwa sababu maelezo yote kuhusu kitabu hicho yapo kwa Kiswahili, na yeye haielewi lugha hiyo. Alichofanya ni "kuomba msaada wa Google Translate," na akaweza kufahamu kitabu hicho kinahusu nini.

Akanambia kuwa amevutiwa sana na kitabu hicho kwa sababu kwa Bara la Afrika lina uhaba mkubwa mno wa katika fasihi simulizi kuhusu taaluma ya Uafisa Usalama wa Taifa. Na akanishauri nianze haraka iwezekanavyo kukitafsiri kitabu hicho kwa lugha ya Kiingereza ili kiweze kuwafikia wana-Usalama wengi zaidi katika nchi mbalimbali zenye uhaba mkubwa wa maandiko ya wazi kuhusu taaluma yao.

Japo sijawahi kuliongelea hili hadharani, moja ya mafanikio mkaubwa mno ya kitabu hiki yamekuwa katika wananchi wa kawaida kuielewa Idara ya Usalama wa Taifa kwa mtazamo chanya zaidi, hasa kutokana na maelezo ya kina ya kazi za taasisi hiyo muhimu kabisa kwa ustawi na uhai wa taifa lolote lile.

Angalia pongezi za msomaji mmoja wa kitabu hicho


Na kwa hakika, licha ya kuandika kitabu hicho kwa ajili ya jamii kwa ujumla, walengwa wakuu pia ni maafisa usalama wa taifa popote pale walipo. Kwa umahiri mkubwa, kitabu kimeepuka 'kuandika yasiyopaswa kuandikwa,' na kuwekea mkazo katika maoeneo ambayo licha ya kujenga ufahamu, yanasaidia kuwaelimisha raia kuwa Idara za Usalama wa Taifa ni kama roho na pumzi za taifa lolote lile. 


Naomba kutumia fursa hii kuwakaribisha ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa kukinunua kitabu hiki kwa minajili ya kujielimisha, sambamba na kupata mtazamo wa 'akina sie' ambao ni wadau wa sekta ya Usalama wa Taifa. 

Kadhalika, kitabu hiki ni dedicated kwa Maafisa wa Usalama wa Taifa popote pale walipo, hasa kwa kutambua safari ndefu na ngumu waliyopitia hadi kufika walipo sasa, na "kuwa kwao macho masaa 24 ya siku 365 za mwaka" kwa minajili ya usalama wa mataifa yao. 


Kwa walio nje ya Tanzania, kitabu kinapatikana www.chahalibooks.com na AMAZON 

Kwa Tanzania, kitabu kinapatikana katika maduka ya vitabu yafuatayo


DAR ES SALAAM:

TPH BOOKSHOP, 24 Samora Street jirani na Sapna (Simu 0687-238-126/ 0759-390-082);
GENERAL BOOKSELLERS, Mtaa wa Mkwepu (Simu MAMA MEENA 0784-887-871)
DAR ES SALAAM BOOSHOP, Mtaa wa Makunganya (Simu MR MPONDA 0657-827-172)
MLIMANI BOOKSHOP, Kariakoo (Simu 0754-269-042)
ZAI BOOKSHOP, Kariakoo (Simu0754-292-532)
ELITE BOOKSTORE, Mbezi Beach Tangi Bovu karibu na Goba Road (Simu 0754-767-336)

MOSHI: APE BOOK, Rindi Lane, Opoosite I&M Bank (Simu 0754767336)

ARUSHA: KASE BOOKSTORE, ELCT Building, Joel Maeda Street

TANGA: HAFAT BOOKSHOP, Barabara ya Saba (Simu HASSAN SHEDAFA 0767-216-403)

MWANZA:
GUNDA BOOKSHOP Karibu na NHC Regional Office Bantu Street/Kemondo (Simu 0753-969-421)
VICTORIA BOOKSHOP, along Bantu Street, Kemondo (Simu 0755-375-034)

MUSOMA: NYAMBUSI BOOKSHOP, Opposite NMB Bank Main Branch (0767-578-565)

IRINGA: LUTENGANO INVESTMENT (Bakwata House), Miomboni St mkabala na Akiba House (Simu 0763-751-978)

KIGOMA: NDAMEZYE ENTERPRISES, Mkabala na NBC Bank (0713534116)

MBEYA VOLILE BOOKSHOP, Mount Loleza, mkabala na TRA (Simu SANGA 0754412075)

MOROGORO: Wasiliana na Marcelino kwa simu 0767612566 ; 0621081500; 0655612566. 






9 Feb 2017

MWEZI Machi mwaka jana, watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Nottingham cha hapa Uingereza walichapisha matokeo ya utafiti wao kuhusu kushamiri kwa tabia ya uvunjaji wa sheria. Katika matokeo hayo ya utafiti uliochunguza nchi 159, Watanzania tuliibuka vinara kwa kuwa watu wanafiki kupita kiasi, tukifuatiwa na watu wa Morocco.
Na mifano ya unafiki wetu ipo mingi tu, sisi ni miongoni mwa wapinzani wakubwa wa suala la ushoga. Lakini ukitaka kufahamu unafiki wetu katika suala hilo, nenda kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram, shuhudia lundo la mashoga wa Kitanzania waliojitundika huko, wakifanya vitu vichafu kabisa, huku wakiwa na “followers” hadi laki kadhaa, hao si tu ni Watanzania wenzetu bali ni miongoni mwa sisi ‘wapinga ushoga.’ Unafiki wa daraja la kwanza.
Na sababu kuu tunayoitumia kupinga ushoga ni imani zetu za kidini. Na kwa hakika tumeshika dini kweli, hasa kwa kuangalia jinsi nyumba za ibada zinavyojaa. Lakini kuthibitisha unafiki wetu, ucha-Mungu huo sio tu umeshindwa kudhibiti kushamiri kwa ushoga (na usagaji) bali pia kutuzuia tusishiriki kwenye maovu katika jamii.
Kwa taarifa tu, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa miaka michache iliyopita na taasisi ya Pew ya Marekani, Watanzania tunaongoza duniani kwa kuamini ushirikina. Na kwa mujibu wa taarifa ninazozipokea kutoka huko nyumbani, ushirikina umeshamiri mno kiasi kwamba sasa ni kama sehemu ya kawaida ya maisha ya Watanzania.
Wacha-Mungu lakini tumebobea kwenye ufisadi, rushwa, ujangili na biashara ya dawa za kulevya. Na asilimia kubwa ya kipato haramu kinachotokana na uhalifu huo kinachangia kushamiri kwa “michepuko” na “nyumba ndogo.”
Mfano wa karibuni kabisa kuhusu unafiki wetu ni katika mshikemshike unaoendelea hivi sasa huko nyumbani (Tanzania) ambao watu kadhaa maarufu aidha wametakiwa kuripoti polisi au ‘kuhifadhiwa’ na polisi wakichunguzwa kuhusiana na biashara ya dawa za kulevya. Hali hiyo inatokana na tangazo rasmi la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ‘kujitoa mhanga’ kukabiliana na biashara hiyo haramu.
Lakini licha ya kuwepo kwa lundo la lawama mfululizo kwa serikali kuwa imekuwa ‘ikiwalea’ watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya, tangazo la Makonda limesababisha kuibuka kwa lawama lukuki dhidi yake, huku wengine wakidai anatafuta ‘kiki (sifa) za kisiasa’ na wengine kudai amekurupuka kwa kutaja majina ya watu maarufu, na wengine wakimlaumu kwa kukamata ‘vidagaa’ na kuacha ‘mapapa.’
Kwa watu hao, na wapo wengi kweli, Makonda atashindwa kama alivyoshindwa kwenye amri zake nyingine. Sawa, rekodi ya Mkuu wa Mkoa huyo katika ufanisi wa maagizo yake sio ya kupendeza. Hata hivyo, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kiongozi sio tu ametangaza vita dhidi ya biashara ya dawa za kulevya bali pia ametaja baadhi ya majina ya wahusika, na kuwafikisha polisi. Hili ni tukio la kihistoria.
Lakini ‘wapinzani’ wa RC Makonda sio wananchi wa kawaida tu. Kuna ‘wapinzani wa asili,’ mbunge wa Chadema, Tundu Lissu, ambaye aliandika ujumbe mtandaoni, “kuwataja vidagaa na kuwaacha nyangumi/papa si ajabu ni moja kati ya mambo ya ovyo ya awamu ya tano.” Huyu ni mnafiki wa mchana kweupe. Sasa kama anawajua hao nyangumi/papa si awataje?
Kilichonisikitisha zaidi ya vyote ni kauli za Waziri Nape Nnauye alipozungumza na waandishi wa habari huko Dodoma. Pamoja na mambo mengine, Waziri Nape alidai kuwa, “ …watumiaji ni wengi lakini wanaoonekana zaidi ni wale wenye majina makubwa,” (sijui kwa mujibu wa utafiti gani); “Kama wizara tunaunga mkono juhudi za kupambana na dawa za kulevya, tatizo ni namna ya kushughulika na wahusika ikiwemo busara” (sijui alitaka tatizo lishughulikiwe kwa namna gani – na kwa nini hakuongoza kwa mfano kwa kutumia namna hiyo – na sijui busara ipi iliyokosekana katika utekelezaji wa agizo la Makonda); “Tunaunga jitihada za mapambano lakini ni vizuri lifanywe katika namna ya kulinda haki ya mtuhumiwa ili heshima yake isipotee” (haelezi hiyo ‘namna ya kulinda haki ya mtuhumiwa ili heshima yake isipotee’ ni kitu cha aina gani)
Nilimshutumu vikali Waziri Nape kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter (nilim-tweet yeye mwenyewe), na kumweleza bayana kuwa alihitaji kutumia busara badala ya kukurupuka kutetea wasanii wanaotuhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya. Kadhalika, kama mtendaji wa serikali, alikuwa na nafasi nzuri kuzungumza na watendaji wenzake wa serikali faragha badala ya kuongea suala hilo hadharani. Kadhalika, kuonekana anahofu zaidi kuhusu “brand” (thamani/hadhi ya msanii, kwa tafsiri isiyo rasmi) badala ya athari kubwa zinazosababishwa na biashara ya dawa za kulevya sio busara hata kidogo.
Nihitimishe makala hii kwa kutoa wito kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba naye ajitokeze hadharani kuongelea suala hili maana amekuwa kimya mno. Awali, naibu wake alipohojiwa na wanahabari alikuwa mkali na alitoa kauli zisizopendeza. Ili vita hii ifanikiwe ni lazima serikali iwe kitu kimoja na viongozi na wananchi kwa ujumla waache unafiki, na wampe ushirikiano RC Makonda na Jeshi la Polisi.
Tanzania bila dawa za kulevya inawezekana

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali

7 Feb 2017

Related image

Mara "Makonda hili, Wema lile," mara "Mapapa, mara vidagaa." Habari kama hizo zinaumiza vichwa. Hata hivyo, kuna habari tamu, na zisizoumiza kichwa,  kwa wapenzi wa mifululizo (series) ya tamthiliya za kishushushu. Hapa twaongelea HOMELAND na 24. Zimerejea hewani kwa kasi mpya, ari mpya na nguvu mpya. Haha!

Season 6 ya Homeland imeshafika episode ya tatu sasa, na kila episode ni nzuri mno. Yaani hizo dakika 55 za kila episode ni kama zinayeyuka tu. 
Sekou
Katika episode ya kwanza, Sekou Bah, kijana Mmarekani Mweusi Muislam, ana-post video mtandaoni baada ya kurekodi katika maeneo ambayo siku za nyuma kulitokea matukio ya kigaidi. Baadaye anakamatwa na shushushu wa FBI Ray Collins na kufunguliwa mashtaka ya ugaidi.

Carrie, sasa ni mfanyakazi katika shirika lisilo la kutengeneza faida (not-for-profit organisation) linaloshughulikia kuwatetea Wamarekani Weusi walio Waislam. Anakutana na Sekou ili kuwa wakili wake.

Pia Carrie anamtembelea Quinn ambaye ni kama amewehuka kutokana na kuwekwa chumba chenye gesi ya sumu, katika hitimisho la season 5. 
Saul na Dar Adal ni mabosi wa ushushushu, na wanampa taarifa Rais mteule, mwanamama Elizabeth Kaine. Baada ya briefing hiyo, Dar anaelezwa hofu yake kuhuthu uimara wa Rais Mteule, na baadaye anakutana na jasusi wa Mossad, Tovah Rivlin.

Katika Episode ya Pili, Carrie na Reda, profesa wa sheria anayefanya kazi na Carrie, wanamuuliza Sekou kuhusu dola 5,000 zilizokutwa na FBI chini ya kitanda chake. FBI wanadai fedha hizo ni kwa ajili ya Sekou kuzipeleka Nigeria kuwasaidia Boko Haram.
Reda na Carrie
Carrie anakuja kubaini kuwa fedha hizo zilitolewa na FBI kwa rafiki wa Sekou aitwaye Saad, ambaye ni mtoa habari wa FBI, ili kumpeleleza zaidi Sekou. Carrie anamvaa Saad, ambaye baadaye anaripoti kwa FBI kuwa ametishiwa na Carrie, na hiyo inatishia uwezekano wa Sekou kupew adhabu nafuu.

Dar Adal akutana na Rais Mteule Keane kumhabarisha kuhusu programu ya nyukilia ya Iran kwa kushirikiana na Korea ya Kaskazini. Saul amtembelea Carrie na kumtuhumu kuwa ni mshauri wa siri wa Rais Mteule Keane. Dar apata picha za siri zinazomwonyesha Carrie akiingia Ikulu kwa siri.

Katika episode ya tatu, Carrie anamjulisha Sekou kuwa (yeye Carrie) 'amelikoroga' kwa kuongea na Saad, na sasa FBI wanataka kudai kifungo cha miaka 15 kwa Sekou badala ya miaka 7. Sekou anaghadhibika, anamtimua Carrie, ambaye anajisikia vibaya. Hata hivyo, anafanikiwa kupata rekodi ya siri ya maongezi kati ya Conlin wa FBI na Saad, na anaitumia kama turufu yake.
Saul
Saul anafika Abu Dhabi ili kumhoji Farhad Nafisi, 'mtu wa mafedha' wa Iran. Nafisi anajiingiza mkenge hadi kukamatwa baada ya kumtembelea kahaba ambaye kumbe ni afisa wa Mossad. Mahojiano hayazai matunda, japo Nafisi anapewa kibano kikali. Baadaye Saul anaripoti kwa Dar kuwa hakupata lolote, lakini Dar anatoa taarifa tofauti kwa Rais Mteule, kitu ambacho baadaye Carrie anamfahamisha Rais Mteule

Hiyo ndo HOMELAND SEASON 6 ilipofikia hadi sasa. Episode 4 itarushwa wiki hii. Nitakueleza hapo chini jinsi unavyoweza kuona tamthiliya hii na nyinginezo bure. 

Sintoongelea 24 kwa leo kwa sababu ndo kwanza natarajia kuangalia episode ya kwanza kati ya mbili zilizokwishaoonyeshwa. Hata hivyo, nimesoma 'reviews' zake, zote zinaisifia kwa kiwango cha juu. Ila tu ni kwamba Jack Bauer hayupo, na badala yake ni staa mweusi Corey Hawkins, aliye-act kama Dr Dre kwenye filamu ya Straight Outta Compton.



Sasa, ukitaka kuangalia Homeland, 24 na series yoyote ile, au filamu, au mechi za soka kimataifa, unahitaji kitu kinaitwa KODI. Hiki kinageuza runinga ya kawaida kuwa 'smart TV.' Kama hujawahi kufahamu kuhusu 'smart tv,' basi kwa kifupi ni zenye uwezo wa kufanya kazi kama kompyuta, ikiwa ni pamoja na kutumia internet kwenye TV hizo.

Maelezo ya jinsi ya kutumia KODI yapo HAPA. Nitaelezea kwa kirefu kuhusu kifaa hicho, kwenye mada zangu kila wikiendi kupitia #ElimikaWikiendi

24 Jan 2017

Mazingira yote yalikuwa 'yameiva' kwa vyama vya upinzani kufanya vizuri kwenye chaguzi za madiwani. Angalau kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Zanzibar, vyama vya upinzani 'vya Bara' (Chadema, ACT- Wazalendo, nk, isipokuwa CUF) vinaweza kuwa na 'kisingizio' kuwa upinzani huko, kwa maana ya CUF pekee, umepaganyika mno na isingekuwa rahisi kuchukua jimbo la Dimani. 

Lakini vyama vyetu vya upinzani haviwezi kuwa na excuse ya maana kutokana na matokeo mabaya kabisa waliyopata katika chaguzi hizo. 

Mwaka juzi, wakati Tanzania yetu inakwenda kwenye uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, uchaguzi ambao mie binafsi nililazimika kumpigia debe mgombea wa CCM, Dkt John Magufuli, baada ya 'Chadema kutusaliti' kwa kumpokea aliyekuwa kada maarufu wa CCM, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, niliwakumbusha mara kwa mara ndugu zangu wa UKAWA kwamba, kwanza, ni ukosefu wa busara kutegemea vyama vya upinzani kufanya vema katika mazingira yaleyale yaliyowafanya wafanye vibaya katika chaguzi zilizotangulia.

Vyama vya upizani vilivyoshiriki katika chaguzi hizo za madiwani viliingia vikiwa katika mazingira yaleyale yaliyovifanywa vibwagwe na CCM katika uchaguzi mkuu wa 2015.

Kibaya zaidi, hadi leo, si Chadema, NCCR Mageuzi, CUF au ACT-Wazalendo waliofanya 'post-mortem' (taarifa ya uchunguzi inayoeleza chanzo cha kifo) ya kwanini vyama husika vilifeli. Badala ya kufanya tathmini ya kina kuhusu sababu zilizovikwamisha vyama hivyo mwaka 2015, kumekuwa na mwendelezo wa porojo kuwa "njia ya Ikulu 2020 ni nyeupe."

save image


Kama kuna chama ambacho kinapaswa 'kusikia maumivu zaidi' kutokana na matokeo ya chaguzi hizo basi ni Chadema, kwa sababu wafuasi wa chama hicho - na kidogo ACT-Wazalendo - ndio pekee miongoni mwa vyma vyote vya upinzani nchini Tanzania, kuendeleza harakati za siasa, licha ya zuwio la serikali ya Rais Magufuli.

Kwamba, zuio hilo halijaathiri wafuasi wa Chadema kutumia teknolojia ya  mitandao ya kijamii, kuanzia Twitter, Whatsapp, Facebook, Jamii Forums, nk kuiban a mfululizoCCM na serikali yake. 

Lakini hapohapo kuna walakini. Ndio, ni wajibu wa vyama vya upinzani kuikosoa CCM na serikali yake. Hata hivyo, kukosoa tu hakutoshi hasa pale ambapo panapohitajika ufumbuzi.

Mifano ni mingi, lakini tuchukulie tishio la baa la njaa. Wakati serikali ya Rais Magufuli na CCM wakisisitiza kuwa hakuna tishio hilo, vyama vya upinzani vikiongozwa na Chadema vimekuwa mstari wa mbele kuonyesha kuwa tatizo hilo lipo.

Lakini kuonyesha tatizo tu bila kujaribu kutafuta ufumbuzi sio busara sana. Na baadhi yetu tulipomsikia Lowassa akisema, namnukuu "Serikali imesema haitoi chakula, mimi nimejadiliana na chama changu tumeona tufanye mpango wa kuwatafutia chakula Watanzania.”

Hicho chakula kiko wapi? Kuwapa wananchi matumaini kisha kutotekeleza ahadi husika ni hadaa. Lakini kuna wanaoshangaa eti "mbona licha ya 'kiburi cha serikali ya CCM kuhusu tishio la njaa' badi chama hicho kimeibuka kidedea kwenye chaguzi za madiwani?"

Jibu jepesi ni kwamba CCM "is the devil they know," kwamba pamoja na mapungufu yake, inaweza kutoa mifano hai ya ilivyowahi kuwasaidia wananchi siku za nyuma. Na hata kama inafanya 'kiburi' kuhusu tishio la njaa, angalau "haijatoa ahadi hewa" kama hiyo ya Bwana Lowassa.

Hebu pata picha: siku chache kabla ya chaguzi hizo, CCM 'yajipiga bao yenyewe' kwa kushikilia msimamo kuwa hakuna njaa na hata ikiwepo hakutokuwa na chakula cha msaada. Chadema kwa kushushiwa bahati hiyo, wanachangamka, wanakusanya misaada ya chakula, na kufanya harambee ya kuwasaidia watu wenye uhaba wa chakula. Naam, pengine serikali ingetaka kuingilia, lakini ninaamini nguvu ya umma ingekuwa upande mmoja na Chadema katika dhamira yao hiyo nzuri. Kwa bahati mbaya imebaki kuwa nzuri tu, na haijatekelezwa.

Kutekelezwa kwa ahadi hiyo kungeweza kutafsiriwa na CCM kama rushwa kwa wapigakura lakini mwenye njaa anachojali ni mkono kwenda kinywani na wala sio amepewa chakula kama msaada au rushwa. Ninaamini kabisa kuwa laiti ahadi ya Lowassa na Chadema yake kuhusu kuwasaidia wananchi wanaokabiliwa na baa la njaa ingetimizwa, basi pengine muda huu chama hicho kingekuwa kinachelekea ushindi.

Tukiweka kando suala hilo, ndugu zangu wa Upinzani, hususan Chadema wameendelea kuwa na imani fyongo kuwa "CCM inachukiwa mno," na "chuki hiyo dhidi ya CCM itapelekea kura kwa Wapinzani." Wanachopuuza ndugu zangu hawa ni ukweli kwamba udhaifu wa CCM sio uimara wa Upinzani. 

Ikumbukwe kuwa wakati CCM inaweza kusubiri hadi mwaka 2020 ili ianze kampeni za kubaki madarakani, Wapinzani wanapaswa kutumia muda huu kuwaonyesha Watanzania kuwa wao wanaweza kuwa mbadala wa kweli wa CCM. Lakini tunachoshuhudia ni Upinzani kuwa 'bize zaidi' kuiongelea CCM badala ya kutenda vitu vitakavyowapa matumaini Watanzania kuwa vyama hivyo ni mbadala sawia.

Ndugu zangu wa Chadema wana mtihani mkubwa zaidi. Pengo lililoachwa na Dokta Slaa limeshindwa kuzibika. Katibu Mkuu aliyepo madarakani anaweza kukisaidia sana chama hicho akiamua kuachia ngazi kwa hiari yake mwenyewe. Ninaamini mtu kama Godlisten Malisa, kada mwenye uwezo mkubwa, anaweza kushika wadhifa huo na akaibadili Chadema. 

Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa chama hicho Bwana Freeman Mbowe, yupo kwenye wakati mgumu mno pengine kuliko muda wowote ule wa maisha yake ya kisiasa. Mbowe anaandamwa na madeni yanayoweza kuathiri mno biashara zake. Japo deni sio jinai, kiongozi wa upinzani kuandamwa na madeni au kutolipa kodi kwa miaka kadhaa ni kitu kinachotoa taswira mbaya kwa wananchi.

Kuna lawama kadhaa zinazorushwa kwa Rais Magufuli kuwa anazitumia taasisi za serikali kama  vile TRA na NHC "kumwandama" Mbowe, lakini ukweli ni kwamba dawa ya deni ni kulipa. Na Chadema inaweza kuingia matatani ikitetea "ukwepaji kodi wa Mbowe" kwa sababu sote twajua kuwa hilo ni kosa (japo si la jinai).

Halafu kuna hizi 'drama' zinazoweza kuwavunja moyo watu wasio na chama lakini wanatafuta chama cha kukiunga mkono. Suala la 'kupotea' kwa kada wa Chadema, Ben Saanane, limeacha doa kubwa kwa chama hicho. Kwa upande mmoja, ilichukua wiki tatu tangu kada huyo adaiwe kupotea kabla ya uongozi wa chama hicho kutoa tamko rasmi. Lawama zaidi zaweza kwenda kwa Mbowe kwa vile Ben alikuwa msaidizi wake binafsi. 

Na Chadema walipotoa tamko rasmi kukfuatiwa na mkanganyiko mkubwa zaidi: huku Mbowe anadai Ben katekwa, kule Tundu Lissu anadai vyombo vya dola vinajua kada huyo yuko wapi, na pale, gazeti la Mwanahalisi la mbunge wa chama hicho Saed Kubenea likaeleza kuwa "Ben yupo, amekuwa akionekana kwenye vijiwe vya chama hicho." Na baada ya jithada fupi mtandaoni zilizoambatana na alama ya reli #BringBenBackAlive na kuchapishwa fulana, suala hilo limekufa kifo cha asili. Huu ni uhuni wa kisiasa maana hatutegemea chama makini kinachojitanabaisha kuwa mbadala wa CCM kuendesha mambo yake kienyeji hivyo.

Kuna tatizo jingine ambalo Chadema wamekataa katakata kulishughulikia. Kabla ya kumpokea Lowassa, ajenda kuu ya Chadema ilikuwa vita dhidi ya ufisadi. Ujio wa Waziri Mkuu huyo wa zamani ulikilazimisha chama hicho kuachana na ajenda hiyo ambayo kwa kiasi kikubwa sana ndio iliyokiwezesha chama hicho kuwa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania.

Na kwa vile Rais Magufuli amejaribu kuifanya vita dhidi ya ufisadi kuwa moja ya ajenda zake kuu, Chadema kwa muda huu haina ajenda kuu yenye mvuto kwa wananchi. Chama hicho kimegeuka kuwa cha kusubiri matukio kisha kuyadandia. Sawa, ni kazi ya vyama vya upinzani kukikosoa chama tawala/kuikosoa serikali, lakini hiyo sio kazi pekee. Na kwa kusubiri matukio, Chadema inakuwa kama "inaendeshwa na CCM."

Niliandika kwa kirefu katika vitabu vyangu viwili kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, kimoja kabla ya uchaguzi huo na kingine baada, kwamba asilimia kubwa ya wapigakura nchini Tanzania sio wanachama wa CCM au vyama vya upinzani. Kwamba mtaji  mkubwa kwa chama chochote kinachotaka kushinda uchaguzi ni ku-win hearts and minds za hao wasio na chama chochote. Kundi hili ndilo lililompa ushindi Magufuli mwaka 2015.

Katika hilo, tatizo kubwa la vyama vyetu vya upinzani ni 'kudanganganyana wao kwa wao kuhusu mshikamano, umoja na wingi wao.' Badala ya kufanya jtihada za ku-reach out kudni la watu wasio na vyama, wao wapo bize kuhamasishana wenyewe kwa wenyewe. Basi angalau kuhamasishana huko kungeendana na kuwavuta watu wasio na vyama, ambao ni turufu muhimu kwenye chaguzi zetu.

Nilwahi kuandika huko Facebook, kuwa 'hasira sio mkakati (wa kisiasa)' kwa kimombo "anger is not a strategy.' Sio siri kuwa wafuasi wa upinzani wana hasira, ni hii sio dhambi wala kosa, lakini wanakosea kudhani kuwa hasira hiyo itawaletea mafaniko ya kisiasa. Hawataki kujifunza kwenye mifano hai ya hasira ambazo zimebaki kuwa hasira tu: hasira dhidi ya Tanesko zimeshindwa kuifanya taasisi hiyo iache uhuni wa mgao wa umeme wa milele; hasira dhidi ya huduma mbovu zinazotolewa na baadhi ya makampuni ya simu hazijaziathiri kwa namna yoyote ile; hasira dhidi ya TFF haijaweza kuifanya Taifa Stars iache kuwa kichwa cha mwendawazimu.

Hasira ili iwe na manufaa shurti iambatane na programu makini ya kuleta mabadiliko kusudiwa. Na hili liliusiwa na Dkt Slaa, kwamba mabadiliko ya kweli yatapatikana tu kwa kuwa na programu makini zitakazohusisha watu makini.

Pengine wapinzani watajitetea kuwa zuio la Dkt Magufuli linalokataza mikutano na maandamano ya vyama vya siasa (isipokuwa CCM) limewaathiri kwa kiasi kikubwa katika kujitengenezes mazingira bora ya ushindi kwenye chaguzi hizo. Mie siafikia kabisa zuio hilo la Rasi Magufuli, lakini wapinzani wangeweza kulitumia 'kumpiga bao yeye na CCM' kwa kulitekeleza kwa kuelekeza nguvu zao 'mtaani,' kuwatumikia wananchi zaidi ya 'wanavyoangushwa na CCM/Serikali.'

Nihitimishe makala hii kwa kutoa wito kwa vyama vya upinzani kukaa chini na kufanya post-mortem ya chaguzi za madiwani, na kutengeneza programu makini (sio hizo operesheni zisizo na kichwa wala miguu) zitakazosimamiwa na kutekelezwa na watu makini. Na wafuasi wa vyama hivyo waache kupoteza muda mwingi kwenye kukosoa tu CCM na serikali huku wakikwepa kuelekea focus yao kwenye vyama vyao. Ni hivi, kama vyama vya upinzani vimeweza kumng'oa moja wa madikteta hatari duniani huko Gambia, Yahya Jammeh, basi hakuna sehemu ambapo upinzani hauwezi kukiong'oa chama tawala madarakani. Lakini hilo halitotokea kwa kujidanganya kuwa "CCM inachukiwa sana." Kuchukiwa kwa CCM sio kupendwa kwa Chadema, au Cuf, au chama kingine cha upinzani. 

ANGALIZO: Mada husika ilikuwa kwa ajili ya makala kwenye gazeti la Raia Mwema lakini nimechukua mapumziko ya uandishi wa makala kwenye gazeti hilo wakati nikisubiri marekebisho flani kutoka kwao.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.