20 Apr 2017


NIANZE makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi kwa familia za askari wanane wa Jeshi la Polisi waliouawa kinyama wiki iliyopita, wilayani Kibiti, mkoani Pwani.
Huu ni msiba wa kitaifa, japo hakuna maombolezo ya kitaifa – sijui kwa vile hatuthamini uhai wa Watanzania wenzetu au tumekwishazoea sana vifo kama vile vya ajali.
Katika moja ya vitu nilivyojifunza katika miaka yangu kadhaa ya kuishi hapa Uingereza ni jinsi wenzetu wanavyothamini uhai. Laiti tukio hili la kuuawa polisi wanane huko Kibiti ndio lingekuwa limetokea hapa, basi huenda kila kitu kingesimama.
Na si hapa Uingereza pekee. Kwa hali ilivyo sasa katika baadhi ya mataifa ya Ulaya Magharibi sasa ni kama "tumekwishaanza kuzoea” matukio ya kigaidi, maana yanatuandama mno, hasa Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani, na majuzi hapa Uingereza.
Katika kila tukio, bila kujali idadi ya waathirika, takriban ndani ya saa moja tangu kutokea tukio husika, Rais au Waziri Mkuu wa nchi husika huongea na wananchi katika runinga mubashara, kutoa pole kwa waathirika, kuwahakikishia usalama wananchi, na kuwaonya wahusika kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Huu ndio uongozi.
Je, sisi hali ikoje? Sana sana ni taarifa ya salamu za rambirambi kutoka kwa Rais, matamko ya hapa na pale ya Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba, na kauli za vitisho za IGP Ernest Mangu – sio kwa “majambazi” bali “wananchi wanaochekelea vifo vya polisi hao waliouawa.”
Japo sio busara kwa mtu yeyote kufurahia kifo cha mtu mwingine – hata kama sio polisi – lakini hilo sio kosa la jinai. Kadhalika, ni vema nguvu ikaelekezwa kwenye tatizo halisi, ambalo Jeshi la Polisi chini ya uongozi wa IGP Mangu haliwezi kukwepa lawama, kwa sababu tishio la usalama mkoani Pwani limedumu kitambo sasa bila kupatiwa ufumbuzi, kuliko ‘tatizo la kufikirika’ (kuwa kuna watu wanafurahia vifo vya polisi hao)
Saa kadhaa baada ya kupatikana taarifa za mauaji hayo, Kamishna wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, alizungumza na waandishi wa habari, ambapo pamoja na mambo mengine alinukuliwa akisema kuwa jeshi hilo "halitokuwa na mzaha wala msamaha" katika operesheni maalumu kuhusiana na tukio hilo. Je, kulikuwa na mzaha na msamaha kabla ya tukio hilo, ambao sasa hautakuwepo wakati wa operesheni husika?
Tukiweka kando kasoro hizo, jambo moja lililonigusa mno ni kukosekana kwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwenye tukio la kuaga miili ya polisi hao. Badala ya kujumuika na wafiwa, Rais alihudhuria hafla mbili (ambazo zingeweza kabisa kusogezwa mbele) za uzinduzi wa hosteli za wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na makazi katika kitongoji cha Magomeni.
Sambamba na hilo, tukilinganisha na matukio makubwa mawili ya hivi karibuni – uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha Clouds na "kutekwa" kwa msanii wa bongofleva, Roma Mkatoliki – mauaji hayo ya polisi hao wanane yalipewa uzito mdogo na Watanzania wengi, angalau huko mtandaoni.
Hali hiyo inasikitisha lakini haishangazi. Sababu moja kuu ya "wananchi wengi kutoonekana kuguswa na mauaji hayo ya polisi wanane" ni ukweli kwamba uhusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi wengi sio mzuri. Polisi wetu kwa kiasi Fulani wamekuwa wakisifika kwa unyanyasaji dhidi ya raia wasio na hatia.
Na kama kuna kitengo cha polisi wetu "kinachochukiwa mno" ni hicho cha FFU (Kikosi cha Kuzuia Ghasia) ambacho askari hao wanane walikuwamo. Japo siungi mkono "chuki" hiyo, lakini naelewa jinsi gani Watanzania wengi wasivyopendezwa na utendaji kazi wa Jeshi la Polisi.
Kwa upande mwingine, jeshi hilo limekuwa likionekana kama "adui wa kudumu" dhidi ya vyama vya upinzani, huku likifanya upendeleo wa wazi kwa chama tawala CCM.
Kwa hiyo, wakati tunaomboleza vifo hivyo vya polisi hao wanane, ni muhimu mno kwa wahusika kuchukua hatua za makusudi kuondoa "uhusiano wa chuki na shaka" uliopo kati ya Jeshi la Polisi na asilimia kubwa ya Watanzania.
Kana kwamba uhusiano bora kati ya Jeshi la Polisi na wananchi sio muhimu ‘sana,’ moja ya nyenzo muhimu ya kujenga na kuimarisha ushirikiano huo, mpango wa Polisi Jamii, ulifutwa kwa sababu wanazozijua wahusika. Polisi jamii ilikuwa kiungo muhimu kati ya polisi wetu na jamii.
Kioperesheni, japo tukio hilo la mauaji ya polisi wanane linaelezwa kuwa ni la kijambazi, binafsi ninahisi kuwa kuna tatizo zaidi ya ujambazi. Na kwa tafsiri ninayoelewa kuhusu ugaidi, basi tukio hilo linastahili kabisa kuitwa la kigaidi. Ni majambazi gani wenye ujasiri wa kuwavizia polisi na kuwaua kwa namna hiyo ya uvamizi wa kushitukiza?
Halafu, hilo sio tukio la kwanza. Na hao polisi wanane sio polisi wa kwanza kuuawa katika eneo hilo, sambamba na wakazi wengine. Yayumkinika kuhitimisha kuwa Jeshi la Polisi na Wizara ya Mambo ya Ndani hawawezi kukwepa lawama, kwa kushindwa kukabili kushamiri kwa mauaji katika eneo hilo.
Sijui Rais Magufuli ameishiwa na zile sindano zake za kutumbulia majipu, au kaishiwa pumzi ya “TumbuaMajipu” lakini ni wazi kuna matatizo ya msingi katika uongozi wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi kwa ujumla. Ukimya wa polisi katika uvamizi huko Clouds, na "kutekwa" kwa Roma, na sasa hili la Kibiti, vilipaswa kumfanya Rais Magufuli achukue hatua.
Moja ya sababu maarufu ya polisi wetu wanapozuia mikutano au maandamano ya vyama vya upinzani huwa "intelijensia." Sasa kama intelijensia ipo kwenye kudhibiti shughuli halali za vyama vya siasa, kwa nini intelijensia hiyo isitumike kwenye kukabiliana na "magaidi" hao wanaotikisa Mkoa wa Pwani?
Nihitimishe makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa familia za askari hao waliouawa kinyama. Pamoja na upungufu wote nilioutanabaisha katika makala hii, hakuna kitu chochote kinachoweza kuhalalisha unyama waliofanyiwa askari hao.
Lakini pia wakati tunaomboleza vifo vyao, ni vema tukatafakari kama taifa kuhusu uhusiano kati ya Jeshi la Polisi (na vyombo vyote vya dola kwa ujumla) na raia, ambao ukiwa bora, unaweza kusaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na taifa kwa ujumla

15 Apr 2017



Nianze makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi kwa familia za askari wanane wa Jeshi letu la Polisi waliouawa kinyama wilayani Kibiti, Mkoani Pwani. 

Huu ni msiba wa kitaifa, japo hakuna maombolezo ya kitaifa - sijui kwa vile hatuthamini uhai wa Watanzania wenzetu au tushazowea sana vifo kama vile vya ajali, nk.

Jambo moja lililonikera mno jana ni ukimya wa wahusika, na mpaka wakati ninaandika makala hii sijasikia kauli yoyote kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi. Labda kuna watakaosema "aanasubiri taarifa kamili." Hapana. Uongozi hauko hivyo. Sie huku Ulaya sasa ni kama "tumeshaanza kuzowea"  matukio ya kigaidi, maana yanatuandama mno, hasa Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani, na majuzi hapa Uingereza.

Katika kila tukio, bila kujali idadi ya waathirika, takriban ndani ya saa moja tangu kutokea tukio husika, Rais au Waziri Mkuu wa nchi husika huongea na wananchi katika runinga mubashara, kutoa pole kwa waathirika, kuwahakikishia usalama wananchi, na kuwaonya wahusika kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Huu ndio uongozi.

Je sie hali ikoje? Sana sana ni taarifa ya salamu za rambirambi kutoka kwa Rais, kama inavyoonekana hapa chini



Hadi wakati salamu hizo za rambirambi zinatolewa, hakukuwa na tamko lolote kutoka kwa uongozi wa jeshi la polisi. Awali, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba alithibitisha kutokea kwa tukio hilolakina akadai "hana taarifa" kuhusu tukio hilo hadi atakapowasiliana na IGP. 


Baadaye, Kamishna wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, aliongea na waandishi wa habari, ambapo pamoja na mambo mengine alinukuliwa akisema kuwa jeshi hilo "halitokuwa na mzaha wala msamaha" katika operesheni maalum kuhusiana na tukio hilo


Je, kulikuwa na mzaha na msamaha kabla ya tukio hilo, ambao sasa hautokuwepo wakati wa operesheni husika?

Tukiweka kando kasoro hizo, jambo moja lililonigusa mno ni ukweli kwamba matukio makubwa mawili ya hivi karibuni - uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha Clouds na "kutekwa" kwa msanii wa bongofleva, Roma Mkatoliki - yalipewa uzito mkubwa na Watanzania kuliko mauaji hayo ya polisi hao wanane.

Inasikitisha lakini haishangazi. Sababu moja kuu ya "wananchi wengi kutoonekana kuguswa na mauaji hayo ya polisi wanane" ni ukweli kwamba mahusiano katika ya Jeshi la Polisi na wananchi wengi sio mazuri. Polisi wetu wamekuwa wakisifika kwa unyanyasaji dhidi ya raia wasio na hatia. 

Na kama kuna kitengo cha Polisi wetu "kinachochukiwa mno" ni hicho cha FFU (Kikosi cha Kuzuwia Ghasia) ambacho askari hao wanane walikuwamo.

Japo siungo "chuki" hiyo, lakini naelewa jinsi gani Watanzania wengi wasivyopendezwa na utendaji kazi wa jeshi la polisi. 

Kwa upande mwingine, Jeshi hilo limekuwa likionekana kama "adui wa kudumu" dhidi ya vyama vya upinzani, huku likifanya upendeleo wa wazi kwa chama tawala CCM.

Kwahiyo, wakati tunaomboleza vifo hivyo vya polisi hao wanane, ni muhimu mno kwa wahusika kuchukua hatua za makusudi kuondoa "uhusiano wa chuki na mashaka" uliopo kati ya jeshi la polisi na asilimia kubwa ya Watanzania.

Kana kwamba uhusiano bora kati ya jeshi la polisi na wananchi sio muhimu "kihivyo," moja ya nyenzo muhimu ya kujenga na kuimarisha ushirikiano huo, mpango wa 'Polisi Jamii,' ulifutwa kwa sababu wanazozijua wahusika. Polisi jamii ilikuwa kiungo muhimu kati ya polisi wetu na jamii.

Kioperesheni, japo tukio hilo la mauaji ya polisi wanane linaelezwa kuwa ni la kijambazi, binafsi ninahisi kuwa kuna tatizo zaidi ya ujambazi. Na kwa tafsiri ninayoelewa kuhusu ugaidi, basi tukio hilo linastahili kabisa kuitwa la kigaidi. Ni majambazi gani wenye ujasiri wa kuwavizia polisi na kuwaua kufuatia 'ambush' kama hiyo iliyotokea eneo la tukio?

Halafu, hilo sio tukio la kwanza. Na hao polisi wanane sio polisi wa kwanza kuuawa katika eneo hilo, sambamba na wakazi wengine. Yayumkinika kuhitimisha kuwa jeshi la polisi na Wizara ya Mambo ya Ndani hawawezi kukwepa lawama, kwa kushindwa kukabili kushamiri kwa mauaji katika eneo hilo. Sijui Rais Magufuli ameishiwa na zile sindano zake za kutumbulia majipu, au kaishiwa pumzi ya #TumbuaMajipu lakini ni wazi kuna matatizo ya msingi katika uongozi wa Wizara ya Mambo ya Ndani na jeshi la polisi kwa ujumla. Ukimya wa polisi katika uvamizi huko Clouds, na "kutekwa" kwa Roma, na sasa hili la Kibiti, vilipaswa kumfanya Rais Magufuli achukue hatua.

Moja ya sababu maarufu ya polisi wetu wanapozuwia mikutano au maandamani ya vyama vya upinzani huwa "intelijensia." Sasa kama intelijensia ipo kwenye kudhibiti shughuli halali za vyama vya siasa, kwanini intelijensia hiyo isitumike kwenye kukabiliana na "magaidi" hao wanaotikisa Mkoa wa Pwani?

Nihitimishe makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa familia za askari hao waliouawa kinyama. Pamoja na mapungufu yote niliyotanabaisha katika makala hii, hakuna kitu chochote kinachoweza kuhalalisha unyama waliofanyiwa askari hao.

Lakini pia wakati tunaomboleza vifo vyao, ni vema tukatafakari kama Taifa kuhusu mahusiano kati ya jeshi la polisi (na vyombo vyote vya dola kwa ujumla) na raia, ambayo yakiwa bora, yanaweza kusaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na taifa kwa ujumla

13 Apr 2017


WANASEMA “wiki nzima katika siasa ni sawa na uhai mzima wa mwanadamu.” Maana ya msemo huo ni kwamba katika siasa, tunaweza kushuhudia matukio mengi katika muda mfupi tu. Kwa lugha nyingine, katika siasa, hata wiki tu ni ndefu kama uhai mzima.
Sasa kama “wiki tu ni uhai mzima” je hali ikoje kwa mwaka mzima? Pengine jawabu lipo kwenye kuiangalia Tanzania yetu, katika kipindi cha takriban mwaka na nusu sasa, kutoka zama za “tumbua majipu” na “hapa kazi tu” hadi muda huu ambapo kila kukicha ni “Bashite hili, Bashite lile,” “Bashite hiki, Bashite kile,” na mengineyo mengi.
Ni vigumu kuandika makala hii ili ifikishe ujumbe unaokusudiwa, kwa sababu takriban kila anayejihusisha na uandishi amekwishapewa angalizo kuhusu nini anatarajiwa kuandika kuihusu Tanzania yetu: habari nzuri tu.
Kwa hiyo inabidi ujuzi wa ziada utumike kuandika habari mbaya lakini ionekane kama nzuri, kwa mujibu wa matakwa ya watawala wetu.
Muda huu ninaandika kitabu kinachofanya tathmini ya “Tanzania: tulikotoka, tulipo, na tuendako” (ndio jina la kitabu husika). Na humo ninajaribu – kwa uhuru mkubwa – kujiuliza kwa mifano hai, nini hasa kimeikumba nchi yetu hadi kufikia hali hii tuliyonayo sasa?
Majuzi nilikuwa nazungumza na mtu mmoja, mzalendo anayefanya kazi kwenye taasisi moja nyeti. Ni maongezi na watu kama hawa yanayonifanya kufahamu yanayojiri nyuma ya pazia. Akanieleza kitu ambacho tangu nilipokisia kimekuwa kikinisumbua sana.
Kwa mujibu wa mzalendo huyo, kuna kikundi hatari ambacho kazi yake kuu ni aidha kunyamazisha watu kwa nguvu au kuepesha mijadala muhimu kitaifa. Kwamba kikundi hicho ambacho ni vigumu kukielezea kwa undani bila kuliingiza gazeti hili matatizoni kinahusika na “utata” wote unaoendelea huko nyumbani muda huu.
Niwatoe pembeni kidogo na kugusia kitu ambacho Rais Donald Trump amekuwa akikiongelea mara kwa mara katika siku za hivi karibuni. Kinaitwa ‘Deep state.’ Jina jingine ni ‘a state within a state’ (dola ndani ya dola).
Deep state anayoilalamikia Trump inaweza kuwa tofauti na inayowezekana kuwepo huko nyumbani. Trump anadai kuwa kuna ushirikiano kati ya taasisi za kiintelijensia za nchi hiyo na baadhi ya watendaji wa serikali, vyombo vya habari, wafanyabiashara na makundi mengine katika jamii, kwa pamoja wakiazimia kumkwamisha Rais huyo mpya wa Marekani.
Tatizo la Trump ni kwamba amekwishaongea upuuzi mwingi mno kiasi kwamba ni vigumu kuchukulia matamshi yake kwa umakini. Na pengine anachokiita ‘deep state’ hakina lengo la kumdhuru kwa kumwonea bali kushughulikia ukweli kwamba tajiri huyo alifanikiwa kushinda urais katika mazingira ya kutatanisha.
Katika Tanzania yetu tumekwishawahi kuwa na mazingira karibu na hiyo ‘deep state.’ Katika siku hizo (mazingira hayaruhusu kubainisha kwa undani kuhusu waliohusika), tulishuhudia watu wakitekwa na kuteswa katika mazingira ya kutatanisha. Nadhani sote tunakumbuka yaliyowasibu Dk. Emmanuel Ulimboka na waandishi wa habari Absalom Kibanda na Saed Kubenea.
Sasa ‘deep state’ imerejea tena, angalau kwa mujibu wa huyo mzalendo ambaye sina sababu ya kutomwamini. Na taarifa zinadai kuwa kuna angalau watu 10 wanaotakiwa “kushughulikiwa.” Baadhi ni wanasiasa wa upinzani na wa chama tawala, na wengine ni watu wenye ushawishi au nafasi muhimu au umaarufu kwenye jamii.
Kwa bahati mbaya, hadi wakati ninaandika makala hii, msanii “Roma Mkatoliki” ambaye pamoja na wenzake walikuwa “wametekwa” kabla ya kupatikana katika mazingira ya kushangaza, alikuwa hajaeleza kuhusu nini hasa kiliwasibu. Hata hivyo, maelezo ya awali yaliyokwishapatikana yanazua utata kuhusu suala hilo.
Msanii anapotekwa, kisha kundi la wasanii wenzake linakwenda kwa kiongozi fulani kuomba awasaidie kumpata mwenzao, na kiongozi huyo anasema kabla ya muda fulani msanii aliyepotea atapatikana, na kweli anapatikana kabla ya ‘deadline’ iliyotajwa na kiongozi huyo, ni wazi “kuna namna” hapo.
Nihitimishe makala hii kwa kutoa ushauri mrefu kwa ndugu zangu wa moja ya idara nyeti nchini Tanzania. Ninyi ndio tegemeo pekee kwenye mazingira kama haya. Kama mimi niliye mbali na huko nyumbani “ninasikia ninachosikia” ni wazi nanyi mtakuwa mnasikia pia. Kuna “uhuni unaofanyika huko mtaani,” na unachafua taswira ya taasisi yenu muhimu na nyeti.
Nafahamu kuwa jukumu lenu ni kushauri tu, lakini ninafahamu pia kuwa mnafahamu cha kufanya pindi ushauri wenu unapopuuzwa na pale zinapofanyika jitihada za waziwazi ku- “undermine” umuhimu wenu. Hivi kweli hizo “rogue elements” zinazohusishwa na “deep state” hazifahamiki? Msipochukua hatua mtahisiwa kuwa mmebariki hayo “yanayoendelea huko mtaani.”
Naomba isitafsiriwe kuwa ninawafundisha kazi. Laiti nisingekuwa na imani nanyi nisingepoteza muda wangu kutoa ushauri huu. Kama ilivyo kwa Watanzania wengi, nina imani kubwa nanyi. Hata hivyo, kuna haja ya haraka ya kuzuia kukua na kushamiri kwa hiyo “deep state.” Ikiachwa, itasababisha madhara makubwa.
Mungu Ibariki Tanzania

5 Apr 2017


Habari iliyotawala mno jana ni taarifa kutoka Ikulu kuwa Rais John Magufuli amemteua kiongozi wa chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo, Profesa Kitila Mkumbo, kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na Umwagiliaji.
[​IMG]
Kwa tathmini ya haraka haraka, taarifa hiyo imepokelewa kwa mitazamo miwili: wanaounga mkono hatua hiyo na wanaoipinga. Wanaoiunga mkono wanaona hatua hiyo ya Magufuli kama mwafaka katika kujenga umoja wa kitaifa na ushirikiano bila kujali tofauti za kiitikadi.


Wanaopinga wanaona uteuzi huo umelenga kuidhoofisha ACT-Wazalendo, mtego ambao haijulikani una malengo gani, na unafiki wa baadhi ya wanasiasa wa upinzani - katika suala hili ni Profesa Kitila na bosi wake Zitto Kabwe ambaye tayari amepongeza uteuzi huo.



Kwa sie tunaoliangalia suala hili 'kwa jicho la tatu,' tunabakiwa na  maswali mengi yasiyo na majibu. Swali mojawapo ni hili: katika hotuba yake moja huko Zanzibar, Rais Magufuli aliapa kutowashirikisha wapinzani kwenye serikali yake (msikilize mwenyewe kwenye video hii hapa chini)



Je Prof Kitila alikuwa 'mpinzani feki kwenye chama feki cha upinzani?'

Na ukiangalia 'upendeleo' aliopewa Profesa Kitila katika wadhifa wake kama mhadhiri wa chuo kikuu cha Dar es Salaam, kisha ukalinganisha na sababu zilizoplekea Profesa Mwesiga Baregu asiongezewe mkataba chuoni hapo, utahisi ipo namna. Hadi wakati Profesa Kitila anapewa 'ulaji' na Magufuli, ushiriki wake kwenye siasa haukuwa tatizo kwa serikali, hiyohiyo 'iliyomkalia kooni' Profesa mzoefu Barefu. 

Lakini pengine unafiki mkubwa wa Profesa Kitila ni ukweli kwamba alishaweka msimamo wake huko nyuma, alipokemea teuzi zinazofanywa na Rais Magufuli kuwachukua wahadhiri pasipo kuandaa wa kurithi nafasi zao. 


Kwahiyo, sidhani kama kuna neno stahili kuhusu Profesa Kitila zaidi ya unafiki. Ndio, alikuwa mtumishi wa serikali, lakini pia alikuwa kiongozi wa chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo. Na hili la unafiki linahusu kotekote, kwenye kazi yake kama mhadhiri - aliyekwishakemea tabia ya serikali kupora wasomi kwenye taasisi za elimu - na kama mwanasiasa ambaye baadhi yetu tulikuwa tukimwona kama tegemeo japo kiduchu kwenye siasa za upinzani. Leo hii, Profesa Kitila ameibuliwa kutoka UDSM na ACT-Wazalendo katika namla ileile BASHITE alivyoibuliwa kwenye u-DC na kupewa u-RC.

Kuhusu Zitto, mie kitambo nimekuwa nikimwona kama mwanasiasa mnafiki. Nani asiyekumbuka ahadi yake ya kutaja majina ya mafisadi walioficha pesa za umma huko Uswisi? Na ni Zitto huyu huyu aliyewahi kurushiwa tuhuma za kuisaliti Chadema baada ya gazeti moja kudaka kile ilichodai kuwa mawasiliano kati ya mwanasiasa huyo na kiongozi mmoja wa Idara ya Usalama wa Taifa. Unaweza kuisoma stori husika HAPA.

Hivi majuzi tu, kulikuwa na tetesi kuwa "Zitto amepotea"

Baadaye "akapatikana" na "akamwashia moto" Rais Magufuli akidai kuwa atakuwa rais wa muhula mmoja tu. Mwanasiasa huyo machachari alilaani kile alichoita "tabia za kidikteta za Magufuli," na kwamba "Watanzania hawatamvumilia (Magufuli) kuwatawala kwa kuwaburuza kidikteta."

Muda si muda, kukajiri 'drama nyingine' kuhusu Zitto, ambaye inaelezwa kuwa alilazimika kujificha ndani ya jengo la Bunge ili asikamatwe na polisi.

Leo Magufuli kamteua Profesa Kitila kuwa katibu mkuu, katika moja ya miujiza ya kisiasa nchini Tanzania, na tayari Zitto 'amebadilika.' Hebu msikie hapa chini


Uzuri mmoja wa unafiki huu ni kwamba Magufuli kawarushia kitanzi Profesa Kitila na Zitto, wajifunge wenyewe au wakikwepe. Kwa sababu wanazozijua wenyewe wamejifunga wenyewe. Nasema hivyo kwa sababu kwa sasa haitowezekana kwa Profesa Kitila kuikosoa serikali kutokana na wadhifa wake huo mpya.

Kadhalika, Zitto na ACT- Wazalendo yake watakuwa na wakati mgumu kuikosoa serikali ambayo "nao wamo" kupitia uwepo wa Prof Kitila. 

Lakini pengine ni vema kukumbuka historia ya wawili hawa katika siasa za upinzani Tanzania. Mie ni mmoja wa watu wanaoamini kwa dhati kuwa laiti wawili hao - Zitto na Kitila - wasingefanya chokochoko ambazo baadaye zilipelekea kufukuzwa kao huko Chadema, basi huenda leo hii Chadema ingekuwa chama tawala. 

Nimaliie makala hii kwa kutahadharisha kuwa si ajabu katika siku chache zijazo mtamskia tena Zitto huyuhuyu anayemwagia sifa Magufuli akielezea kuhusu ishu moja nzito. Baadhi yetu twafahamu kuhusu mkakati fulani dhalimu unaomhusisha Bashite dhidi ya watu flani. Ninatarajia Zitto ataufahamu hivi karibuni. Tuliache hilo, muda utaongea.

Nawatakia siku njema

25 Mar 2017


Kuna wanaotusimanga tuliompigia kampeni Rais John Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 2015. Kwamba sie ndo tumemleta Magufuli. Kwamba bila sie kumnadi, Tanzania isingeshuhudia kipindi hiki cha 'maajabu' ambapo kwa mara ya kwanza tumeshuhudia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam'anayebebwa na Magufuli' akiwa na uhuru wa kuvunja sheria, na yeyote atakayemkemea atakuwa amenunua ugomvi na Magufuli.

Wanaotusimanga wanasahau kitu kimoja. Laiti Upinzani ungekuwa na mgombea imara katika uchaguzi mkuu uliopita, kazi ya kuiangusha CCM ilikuwa rahisi kuliko wakati mwingine wowote ule.

Nakumbuka kada mmoja mwandamizi wa CCM alinieleza wakati wa kampeni kuwa "laiti Wapinzani walivyoungana na kumsimamisha mtu asiye na rekodi yenye mawaa, kwa mfano Dokta Slaa hivi, basi uchaguzi huu ungekuwa mgumu sana kwetu." Alieleza kuwa UKAWA uliirahisishia CCM kampeni ya kumnadi mgombea wake kwa vile, pamoja na sababu nyingine, mgombea wa UKAWA -Lowassa- alikuwa akijulikana vizuri mno huko CCM, kitu kilichowarahisishia kumshinda 'kirahisi.'

Kwahiyo, kabla ya kuachana na suala la lawama hizo, niseme hivi: sie tuliomnadi Magufuli hatukujua kuwa angekuja kubadilika kiasi hiki, lakini laiti Upinzani ungesimamisha mgombea bora, sie wengine wala tusingekimbia, tungefanya kampeni kama mwaka 2010, na kwa vile kwa kiasi kikubwa Upinzani auliamia kuweka kando tofauti zao, basi uwezekano wa kuiangusha CCM ulikuwa mkubwa. Ila hayo yameshapita sasa, tugange yaliyopo na yajayo.

Na yaliyopo tunayaganga vipi? Ni kwamba wakati tunaendelea kukuna vichwa kufahamu kitu gani kilichomsibu Rais Magufuli, aliyeingia kwa kishindo kikubwa sio Tanzania tu bali kimataifa pia, na hadi kutawala dunia na alama ya reli #WhatWouldMagufuliDo hadi kufikia hatua aliyofikia sasa ya kutawala kwa vitisho, jazba, ubabe na kutetea waziwazi uvunjifu wa sheria uliofanywa na RC Makonda, ni vema basi tujipange imara kuzuwia jitihada zozote za kiongozi huyu kuwa wa kutumia mabavu tu.

Kuna mwanafalsafa mmoja aliusia huko nyuma kuwa "ili maovu yashamiri, yahitaji tu watu wema kutofanya lolote." Wenye uwezo wa kupiga sauti dhidi ya maovu tukikaa kimya, labda kwa vile tu tuliwahi kumpigia kampeni Magufuli, au kwa vile "yatapita tu," kuna kila dalili kuwa tunakoelekea sio kuzuri.

Moja ya mambo yanayotatiza sana kuhusu Rais Magufuli ni kile kinachoonekana kama kupenda ugomvi usio wa muhimu. Hilo nimelieleza kwa kirefu katika makala ninayoiambatanisha hapo chini ambayo ilipaswa kuchapishwa na gazeti la Raia Mwema toleo la wiki hii lakini ninahisi haikuchapishwa (njia pekee ya mie kufahamu imechapishwa au la ni kuona makala husika kwenye tovuti ya gazeti hilo, na wiki hii haipo).

Kati ya nilipoandika makala hiyo na leo, kuna matukio makubwa manne yaliyojitokeza. Kwanza ni Waziri wa Habari (na masuala mengine)  Bwana Nape Nnauye kusimamia vema wajibu wake kama waziri husika, kufuatilia uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha redio na televisheni cha Clouds. Nape alipokea ripoti ya Tume aliyounda, na licha ya msimamo wa Magufulikujulikana mapema kuwa "anambeba Makonda," Nape alionyesha ujasiri na kuiweka hadharani ripoti hiyo ambayo awali baadhi yetu tulidhani ingekuwa 'changa la macho.'

Tukio la pili ni uamuzi wa Rais Magufuli kumfukuza kazi Nape kwa kufanya mabadiliko kwenye kabineti yake, na nafasi ya Nape kukabidhiwa Dkt Harrison Mwakyembe, ambaye majuzi tu 'alilikoroga' kwa kupiga marufuku kufunga ndoa bila cheti cha kuzaliwa. Amri hiyo ya kizembe ilitenguliwa na Magufuli siku chache baadaye.

Tukio la tatu ni mkutano wa Nape na waandishi wa habari, ambao tukiweka kando aliyoyasema mwanasiasa huyo, kubwa zaidi lilikuwa kitendo cha afisa mmoja wa usalama (haijulikani kwa hakika kama alikuwa polisi au taasisi nyingine ya dola) kumtolea bastola Nape hadharani. Tukio hilo la kutisha, na lile na Makonda kuvamia Clouds, yatabaki kuwa historia isiyopendeza kwa taifa letu kwani hayajawahi kutokea...labda zama za ukoloni.

Tukio la nne ni 'mafuriko' ya maneno yasiyopendeza kutoka kwa Rais Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa jana wakati anawaapisha Mwakyemba na Profesa Kabudi, aliyerithi nafasi ya Mwakyembe. 

Sitaki kurudia vitisho alivyotoa Rais Magufuli lakini nachoweza kutahadharisha ni kuwa tunakoelekea sio kuzuri. Unapoona Rais anakerwa kwa vile habari zinazomhusu hazijapewa kipaumbele kwenye vyombo vya habari vingi, basi ujue tuna tatizo kubwa. Unapoona Rais anaamini kuwa habari za maandamano ya wafugaji na wakulima kuhusu migogoro ya ardhi ni "habari mbaya mbaya" basi ni wazi huyu si yule tuliyedhani ni tetezi wa wanyonge.

Tulipasw akuona dalili hizo mapema, kupitia baadhi ya kauli zake kama "I wish I could be Jaji Mkuu" na "I wish I could be IGP." Ukiona Rais anatamani madaraka zaidi ya aliyonayo, hiyo ni hali ya hatari.

Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli asikilize ushauri anaopewa na "wataalamu kuhusu hali ilivyo huko mtaani." Kadhalika, ninamsihi Rais wangu apunguze jazba. Hazitamfikisha popote. Aache kasumba ya kutafuta 'mabifu' yasiyo na msingi. Lakini jingine ni ukweli kwamba hatoweza 'kumbeba Makonda' milele, na kuendelea kumkumbatia kijana huyo kunaweza kumgharimu yeye Magufuli binafsi. 

SOMA MAKALA ILIYOPASWA KUTOKA KATIKA RAIA MWEMA TOLEO LA WIKI HII (JUMATANO 23/03/2017) LAKINI HAIKUTOKA (KWA SABABU WANAZOJUA WAMILIKI WA GAZETI HILO)


MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA MACHI 22, 2017

Disemba 31 mwaka juzi, siku ya mkesha wa ‘mwaka mpya 2016, nilichapisha kitabu cha kielektroniki kilichobeba jina “Dokta John Magufuli: Safari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake.”

Pamoja na watu wengi waliokisoma kitabu hicho kukipongeza, wapo pia walionikosoa, hoja yao kuu ikiwa “ni mapema mno kutathmini Urais wa Magufuli katika muda huu mfupi aliokaa madarakani.”
Kwa wakati huo, sikuafikiana na ukosoaji huo, hasa kwa vile tathmini ya uongozi ni kama maadhimisho ya siku ya kuzaliwa: yanaweza kufanywa siku 40 baada ya kuzaliwa, kila mwezi, na kila mwaka kama wote tunavyofanya.

Kwahiyo, sikuona tatizo katika kufanya tathmini ya urais wa Dokta Magufuli, hasa ikizingatiwa kuwa aliingia na “kasi ya kutisha.” Kati ya siku aliyopishwa, Novemba 5, 2015 hadi nilipochapisha kitabu hicho – takriban miezi miwili hivi – Rais Magufuli alimudu kukonga nyoyo, sio za Watanzania tu, bali dunia nzima kwa ujumla kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya uzembe, rushwa, ufisadi, sambamba na ari yake kubwa ya kubana matumizi.

Naamini sote tunakumbuka alama ya reli (hashtag) ‘iliyotikisa’ dunia nzima ya #WhatWouldMagufuliDo ambayo watumiaji mbalimbali wa mtandao wa kijamii wa Twitter katika kila kona ya dunia walijaribu kuonyesha jinsi gani Dokta Magufuli alivyo bora zaidi ya viongozi wengine duniani.

Lakini sababu nyingine ya kuandika kitabu hicho ilikuwa ushiriki wangu binafsi kwenye kampeni za kumnadi Dokta Magufuli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Pamoja na sababu nyingine, niliamua kumnadi kutokana na sababu zangu binafsi dhidi ya mpinzani wake mkuu.

Na haikuwa kazi rahisi kumnadi mwanasiasa huyu, kwa sababu baadhi ya watu walishindwa kabisa kunielewa, huku wengine wakihoji “kwanini unaweza kutusaliti wapinzani na kumpigia debe mgombea wa chama tawala, ambacho wewe binafsi ni mhanga wa unyanyasaji unaofanywa na serikali yake dhidi ya wanaoikosoa?” Na kilichoambatana na kauli hizo ni matusi mazito, udhalilishaji usiomithilika, na mengineyo yasiyostahili kukumbukwa.

Takriban miaka miwili baadaye, nimeshikwa na bumbuwazi baada ya kumsikia Rais Magufuli “akimkingia kifua” Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ambaye majuzi ameandika historia ya matukio ya kisiasa nchini Tanzania kwa kuvamia ofisi za kituo cha habari cha Clouds, akiambatana na askari wenye silaha nzito.

Niweke rekodi sahihi. Awali nilimtetea RC Makonda katika nilichoamini kuwa ni jitihada zake dhidi ya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Niliamini kuwa suala la ‘utata wa elimu yake’ ni sehemu tu ya mikakati za kumwondoa kwenye ajenda hiyo muhimu.

Hata hivyo, baada ya mawasiliano na “wenye uelewa wa yanayojiri nyuma ya pazia la siasa za Tanzania,” nilithibitishiwa kuwa tuhuma dhidi ya kiongozi huyo zina ukweli, na nikaelezwa kuwa “hata Dokta Magufuli anafahamu hilo.” Na kimsingi, awali nilipanga makala hii iwe ya ushauri kwa Rais kuchukua hatua stahili dhidi ya mteuliwa wake huyo “ili kuwatendea haki wanaomshauri.”

Lakini kabla sijawasilisha makala hiyo, ambayo ililenga zaidi kwenye kusisitiza haja kwa viongozi wetu kuzingatia ushauri wa kitaalamu badala ya kuendekeza ajenda binafsi, kukajitokeza tukio la RC Makonda kuvamia huko Clouds.

Nitumie fursa hii kuupongeza uongozi wa kampuni ya Clouds, hususan Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga, kuwa kufanya kile kilichotamaniwa na Watanzania wengi waliokuwa wakisubiri tamko la kampuni hiyo kuhusu tukio hilo la uvamizi wa Makonda, kwamba wasimamie ukweli.

Na kwa hakika, Ruge na Kusaga hawakuwaangusha watumishi wenzao wa Clouds na Watanzania kwa ujumla, wakaeleza “A hadi Z” ya kilichotokea wakati wa uvamizi huo ambao, kwa kumbukum bu zangu, ni wa kwanza kabisa kutokea nchini mwetu.

Ingeweza kuwa rahisi tu kwa viongozi hao wa Clouds “kuweka mbele maslahi yao binafsi” na kubadili maelezo, hasa ikizingatiwa kuwa lolote ambalo wangesema lingeweza kuaminika, lakini wakaamua kuhatarisha uhusiano wao na Makonda pamoja na shabiki mkubwa wa kituo hicho, yaani Rais Magufuli mwenyewe.

Akiongea kwenye uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara za juu, pamoja na mambo mengine Rais Magufuli aliwaomba Watanzania kujielekeza kwenye vitu vya maendeleo badala ya kujielekeza zaidi kwenye udaku. Ikumbukwe kuwa siku chache tu zilizopita, Rais alipiga simu kwenye kituo cha televisheni cha Clouds na kueleza kuwa yeye pia ni shabiki wa kipindi cha Shilawadu, ambacho ni cha “udaku” huo huo anaokemea Rais.

Suala hapa sio tu “kama ni sahihi kwa Rais kuwa shabiki wa kipindi cha udaku, basi isiwe dhambi kwa wananchi kupenda udaku” bali “kitendo cha Makonda kuvamia Clouds sio kujielekeza kwenye maendeleo.”

Dokta Magufuli alikumbusha pia kuwa “kampeni zimekwisha, ulie lakini Rais ni Magufuli, mimi kwangu hapa ni kazi tu, maendeleo.” Hivi kweli Rais anaamini kelele za kutaka Makonda achukuliwe hatua kutokana na uvamizi huko Clouds ni mwendelezo wa kampeni? Au ni “kelele za wasiojua kuwa Rais ni Magufuli”? Na sitaki kabisa kuamini kuwa Rais anaamini kitendo cha uvamizi wa Makonda huko Clouds ni sehemu ya “hapa ni kazi tu.”

Kilichonisikitisha zaidi ni kauli ya Dokta Magufuli kwamba “mnahangaika na viposti vyenu mara hili mara lile, mpaka wengine wanaingilia uhuru wangu kwamba nifanye hivi, ukiniingilia ndio unapoteza kabisa.”

Kwangu binafsi, nimeoiona kauli hiyo ya Rais kuwa kama dhihaka dhidi ya baadhi yetu tulioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni mwaka 2015 kwa kutumia “viposti” hivyo hivyo anavyovidharau. Na sio sahihi kwa Rais kudai tunamwingililia uhuru wake. Yeye ni mtumishi wetu, na tuna haki ya kumweleza matakwa yetu. Huko sio kumwingilia uhuru wake bali kudai stahili yetu kutoka kwake.

Rais alitukumbusha pia kuwa yeye hapangiwi mambo, anajiamini, na ndio maana siku ya kuchukua fomu alikwenda peke yake. Kumtaka amwajibishe mteule wake aliyevamia kituo cha habari sio kumpangia mambo bali kumkumbusha wajibu wake kama kiongozi. Na kupangiwa mambo kama “mwajiriwa wa Watanzania” sio kosa, isipokuwa tu pale “kumpangia mambo” huko kunalenga kuidhuru nchi yetu.

Sawa, Dokta Magufuli alikwenda peke yake kuchukua fomu za kuwania urais, lakini hakufanya kampeni peke yake. Na kwenda kwake pepe yake kuchukua fomu hakumpi ruhusa ya kutuongoza peke yake, bali kwa ushirikiano kati yetu waongozwa na yeye kiongozi. Hivi, sio Dokta Magufuli huyuhuyu ambaye kila mara anatusihi tumwombee, lakini leo anatuona tunamwingilia?

Kadhalika, Rais alimuunga mkono RC Makonda kwa kumwambia kuwa yeye (Rais) ndio anayepanga nani akae wapi na afanye nini…kwahiyo RC Paul Makonda achape kazi. Hivi Rais amesahau kuwa sio yeye kama Magufuli bali taasisi ya Urais ndiyo inayompa nguvu kufanya maamuzi kwa maslahi ya Watanzania wote?

Na je Dokta Magufuli anataka kutuaminisha kuwa ameridhia kitendo cha Makonda kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha, kiasi cha kumtaka Mkuu huyo wa mkoa “aendelee tu kuchapa kazi”? Je hiyo haitompa jeuri Makonda, na hata wengineo, kufanya “abuse of power” kwa vile “Rais kuruhusu”?

Nimalizie makala hii kwa ushauri huu kwa Dokta Magufuli: kwanza, hakuna tija katika kusaka ugomvi usio na umuhimu (picking up cheap fights). Uamuzi wa kuzuwia kurushwa matangazo ya bunge mubashara, kuzuwia mikutano ya vyama vya siasa vya upinzani, kuwaambia wahanga wa tetemeko Kagera kuwa “serikali haikuleta tetemeko hilo” na “kila mtu abebe msalaba wake mwenyewe”, kuwaambia wananchi wanaolalamikia njaa kuwa “wewe Rais huwezi kuwapikia,” nk sio tu ni “kusaka ugomvi usio wa lazima” lakini haziendani na matarajio ya Watanzania kwako Rais wetu.

Vilevile ninaomba sana kumshauri Rais kuzingatia ushauri wa kitaalamu anaopatiwa na wasaidizi wake. Ni vigumu kufafanua katika hili, lakini ninaamini “nimeeleweka.” Taifa litakuwa katika hali mbaya itapofika mahala “washauri watakapotumia njia mbadala kukufikishia ujumbe.” Na ndicho kinachotokea kuhusu “viposti.”

Mwisho, siku zote Rais wetu umekuwa ukimtanguliza Mungu katika hotuba zako mbalimbali na kuwasihi Watanzania wakuombee. Wewe ni Mkristo, na hii ni Kwaresma. Ni kipindi cha maungamo, kusamehe waliotukosea, kuangalia tulikotoka, tulipo na tuendako. Penye Mungu pana upendo, na penye upendo pana haki. Japo hupangiwi cha kufanya, naomba kukushauri uwapatie haki Watanzania kwa kumwajibisha RC Makonda kwa kuvunja haki za Clouds kutokana na uvamizi aliofanya.
Mungu Ibariki Tanzania


Baruapepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @cha



21 Mar 2017



Baada ya tukio la Mkuu wa Mkoa Paul Makonda kuvamia ofisi za Kampuni ya Clouds jijini Dar, Ijumaa usiku, na kuahidiwa na uongozi wa Kampuni hiyo kuwa ungetoa taarifa rasmi jana, watu wengi - ikiwa ni pamoja nami- walihisi kuwa "sio rahisi kwa Clouds kumtosa Makonda, kwa vile ni mshkaji wao."

Sie hapa Uingereza tupo masaa matatu nyuma ya masaa ya Tanzania (japo Jumapili ijayo masaa yatabadilika), na jana nilipoamka, tayari uongozi wa Clouds chini ya Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga ulikuwa umeshatoa taarifa kuhusu kilichojiri Ijumaa iliyopita kuhusu Makonda.

Awali, nilitaka kupuuzia kufuatilia habari hiyo nikihofia "kuharibu siku yangu kwa kuianza na habari mbaya" nikidhani kuwa Ruge na Kusaga "wamemsafisha Makonda."

Hata hivyo, baada ya kutupia macho tweets za Millard Ayo aliyerusha press conference ya uongozi wa Clouds mubashara, nilibaini kuwa Ruge, Kusaga na Clouds kwa ujumla wamefanya kile ambacho kimekuwa kigumu mno kufanywa na Watanzania wengi: kuwa wakweli. Kuwa tayari kupoteza rafiki kuliko kupoteza ukweli.

Kwa wengi hilo linaweza kuwa suala dogo lakini kwa hakika lina umuhimu wa kipekee. Sote twafahamu ukaribu wa Makonda na Clouds, na hata Ruge amekiri kuwa yeye binafsi ni rafiki na Mkuu huyo wa Mkoa.

Kwahiyo, kama ilivyotarajiwa na wengi, ingekuwa rahisi zaidi kwa Clouds "kumbemba Makonda" (kama alivyobebwa na Rais Magufuli) na pengine "stori ingeishia hapo" kuliko kuamua kusimamia kwenye haki na ukweli.

Jana niliwapa angalizo ndugu zangu wa Clouds kuhusu "kukubali kutumika." Nili-tweet hivi


Lakini japo ni rahisi kulaumu kuliko kujihangaisha kujua kwanini flani kafanya kitu tunachomlaumu kukifanya, mazingira ya media zetu yanalazilazimisha kutumika. Kwahiyo, wakati ni rahisi kuwalaumu Clouds "wanapotumika" kuinadi CCM na serikali yake, ni muhimu twenda mbali na kufahamu kwanini wanafanya hivyo.

Ni kwamba, kwa kiasi kikubwa, uhuru wa habari Tanzania bado ni fadhila kutoka kwa watawala. Kwa kiasi kikubwa, chanzo kikuu cha mapato ya vyombo vya habari ni matangazo kutoka serikalini. Kwahiyo, chombo cha habari "kitakachoiudhi serikali" kinaweza kujikuta kinanyimwa matangazo. Hiyo inalazimisha "urafiki" kati ya vyombo hivyo na serikali.

Lakini licha ya matangazo, vyombo vyetu vya habari vinafanya kazi katika mazingira kandamizi, na kwa ridhaa ya watawala badala ya kanuni stahili. Ndio maana, kama tulivyoshuhudia jana, Waziri Nape anapigania "sheria" huku Bosi wake Magufuli anakumbatia ridhaa yake kama mtawala.

Kingine kinachohusiana na tukio hilo ni ukweli kwamba Rais wetu Dokta John Magufuli anaelewa kasoro za wasifu wa elimu ya Makonda...kwa sababu alishajulishwa ukweli huo na "wahusika." Laiti angefanyia kazi ushauri aliopewa, tusingefika hapa. 

Kuna tatizo pia katika jinsi Rais wetu alivyojitahidi kutuonyesha kuwa ni rafiki wa Clouds, na ameshapiga simu mara kadhaa na kurushwa hewani, 

na kusifiwa na watu kibao kuwa "ni mtu wa watu" lakini swahiba wake, Paul Makonda, alipovunja sheria kwa kuvamia ofisi za Clouds, akapuuza "urafiki wake na Clouds" na "kumbeba swahiba wake Makonda." 
Kasoro nyingine ni kudai kuwa yeye Rais anapenda kipindi cha "udaku" cha Shilawadu cha Clouds lakini jana anatuchamba kuwa "Watanzania tunaendekeza udaku." Je ni Rais pekee anayestahili kupenda udaku, lakini ni jinai kwa raia wa kawaida?


Nimalizie makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli aache kupenda ugomvi usio na maana, Waingereza wanaita "cheap fights." Alizuwia "matangazo ya bunge mubashara," na majuzi kajisifu kwa hatua hiyo; lilipotokea tetemeko Kagera, akakaa muda mrefu bila kwenda kuwapa pole wahanga, na alipokwenda akawasemea ovyo, eti "yeye hakuleta tetemeko hilo" na "hakuna serikali duniani inayosaidia wahanga wa tetemeko" (kitu ambacho sio kweli).


Kana kwamba hayo hayakutosha kutibua watu, alipokuwa ziarani mikoani, wananchi walisikika wakimwambia "njaa baba!" akawasemea ovyo "njaa mnataka mie niingie jikoni kuwapikia?" Na jana, amejigamba kuwa anajiamini, ndio maana alikwenda kuchukua fomu ya kuwania urais peke yake. Anajifanya kusahau kuwa hakujipigia kampeni peke yake, na kuna tuliotukanwa mtandaoni tukihangaika kumpigia kampeni.

Nilishaandika kwenye jarida la Raia Mwema kumsihi Rais Magufuli azingatie umuhimu wa kutumia lugha ya kidiplomasia badala ya kuendekeza ukali usio na maana, hasa katika mazingira kama ya jana ambapo hakupaswa kumlinda Makonda kwa uhuni aliofanya huko Clouds. Kusema "hapa ni kazi tu" kwa minajili ya kumlinda Makonda kinatufanya tuliosapoti kauli mbiu hiyo ya "hapa ni kazi tu" kujiskia kichefuchefu. Yaani "hapa ni kazi tu" kwa Mkuu wa Mkoa kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha?


Lakini kosa kubwa alilofanya Magufuli jana sio kumtetea Makonda bali kutupa jawabu la wazi kuwa jeuri ya Makonda inatoka kwa bsoi wake, yaani Magufuli. Kwanini Magufuli anamlinda Makonda kiasi hicho? Baadhi yetu twaelewa lakini huu sio muda mwafaka kuyaongelea hayo. Ila tu Rais wetu afahamu kuwa sapoti ya baadhi ya watu kwake ina ukomo, itafika mahala "akimwaga mboga, watamwaga ugali." I hope hatutofika huko. I hope Rais wetu atatumia busara, kufanyia kazi mapungufu yake eg kuwabwatukia watu ovyo huku anawalea watu kama Makonda, na kuepuka kusaka ugomvi usio na maana.

Historia ina mafundisho mengi kuhusu viongozi walioendekeza jeuri, kiburi, ubabe, dharau na kujiona majabali, na hatma yao haikuwa nzuri.

Waingereza wanasema WRONG IS JUST THAT, WRONG (Kitu kisicho sahihi kiko hivyo tu, hakiko sahihi). Alichofanya Makonda was wrong. Utetezi wa Rais Magufuli kwa Makonda was wrong too. Huo ni ukweli hata kama utamchukiza Mheshimiwa Rais.





16 Mar 2017


MAJUZI, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilifanya Mkutano wake Mkuu Maalum huko Dodoma, ambao pamoja na mambo mengine ulikuwa na ajenda kuu ya "kujadili na kupitisha marekebisho ya Katiba ya CCM ya mwaka 1977 Toleo la 2012, pamoja na kanuni za chama hicho na jumuiya zake."
Nimeyawekea msisitizo maneno "kujadili na kupitisha" kwa sababu inaonekana kuwa wazi kuwa majadiliano yaliyofanyika hayakupaswa kutoyapitisha marekebisho hayo.
Ni rahisi kutafsiri hatua hiyo kama ya kuminya demokrasia (kwa maana kwamba kujadili pekee hakutoshi bali pia kuwepo uhuru wa kuyakubali au kuyakataa mapendekezo husika) lakini pengine ni rahisi pia kutambua kwanini CCM "ilijihami" mapema.
Mabadiliko hayo ya katiba ya chama hicho yamepelekea kupungua idadi ya wajumbe wa vikao vya ngazi za juu vya chama hicho na kupunguza 'kofia mbili' kwa viongozi wenye vyeo ndani ya chama, serikalini au bungeni.
Kutokana na mabadiliko hayo, mwanachama anatakiwa kushika nafasi moja tu ya uongozi, katika ngazi za Mwenyekiti wa Tawi, Kijiji, Mtaa, Kata, Wadi, Jimbo, Wilaya na Mkoa. Wengine ni Makatibu wa Halmashauri Kuu wa ngazi zote, Diwani na Mbunge/Mwakilishi.
Kwa hiyo ni wazi kuwa mabadiliko hayo yanawaathiri 'vigogo' kadhaa wa chama hicho, na pengine ndio maana ikaamuliwa kuwe na "mjadala na kupitisha mabadiliko hayo" badala ya "mjadala na kupitisha au kutopitisha mabadiliko husika."
Kadhalika, mabadiliko hayo yatapelekea kupungua kwa idadi ya wajumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, kutoka 34 hadi 24.
Vilevile, idadi ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho imepungua zaidi ya nusu, kutoka 388 hadi 168.
Miongoni mwa 'vigogo' waliotarajiwa kuathiriwa na mabadiliko hayo kutokana na kushika nyadhifa zaidi ya moja ni pamoja na William Lukuvi, Makame Mbarawa, Dk. Hussein Mwinyi, na Shamsi Vuai Nahodha.
'Kigogo' mwingine ni Mama Salma Kikwete, ambaye licha ya kuwa mjumbe wa NEC wa Mkoa wa Lindi, hivi karibuni aliteuliwa na Rais  Magufuli kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri.
Wengine ni wenyeviti wa CCM mikoa ambao pia ni wabunge, kama vile Joseph Musukuma, Martha Mlata na Deo Simba, ilhali Godfrey Zambi ni mbunge na mkuu wa mkoa, Adam Kimbisa ni Mjumbe wa Kamati Kuu na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma.
Kuna usemi mmoja, kwamba sio kila kitu sahihi ni kizuri, na sio kila kitu kizuri ni sahihi. Uamuzi wa CCM kuwapunguzia wanachama wake kofia zaidi ya moja kwenye uongozi ni sahihi lakini sio mzuri kwa watakaoathiriwa nao.
Jicho la uchambuzi litaelekezwa kwa 'wahanga' hao kadri chama hicho kinavyoingia kwenye mchakato wake wa uchaguzi mkuu baadaye mwaka huu, na kwenye kinyang'anyiro cha urais kupitia CCM katika uchaguzi mkuu ujao, mwaka 2020.
Siku moja kabla ya Mkutano huo Mkuu Maalum, chama hicho tawala kilitangaza adhabu kwa viongozi wake kadhaa, kubwa zaidi ikiwa kuwavua uanachama viongozi 12 akiwemo Sophia Simba, kada mkongwe wa chama hicho na ambaye hadi anapewa adhabu hiyo alikuwa Mwenyekiti wa Taifa wa jumuiya ya wanawake wa CCM (UWT), mjumbe wa Kamati Kuu na Mbunge.
Hatua hizo kali zilizochukuliwa na CCM chini ya uenyekiti wa Rais Magufuli, sambamba na mabadiliko niliyoyaongelea awali, yana tafsiri kuu mbili.
Kwanza, hatua kali za kinidhamu zinapeleka ujumbe kwa wana-CCM wa kada mbalimbali kuwa Rais Magufuli amepania kwa dhati kukisafisha chama hicho tawala.
Pili, mabadiliko kusudiwa, sambamba na hatua kali zilizochukuliwa dhidi ya viongozi kadhaa wa chama hicho, ni mtihani mkubwa, kwa Mwenyekiti Magufuli na CCM kwa ujumla.
Kwa Mwenyekiti Magufuli, hatua hizo zimemwongezea idadi ya maadui zaidi ya wale ambao tayari ni waathirika wa msimamo wake dhidi ya ufisadi na rushwa, ambapo watendaji kadhaa wa serikali wametumbuliwa huku wakwepa kodi wakidhibitiwa, na majangili na 'wauza unga' wakibanwa.
Japo ni mapema mno kufanya tathmini timilifu kwa hatua hizo, ile kuzichukua tu sio tu kwaonyesha dhamira lakini pia ni wazi zimetengeneza maadui wa kutosha dhidi ya Dk. Magufuli.
Katika hili, ni muhimu kutambua kuwa ni bora kuwa na kiongozi atakayechukiwa na kwa kutenda vitu sahihi kuliko atakayependwa kwa kufanya madudu.
Siku moja kabla ya Mkutano huo Mkuu Maalum zilipatikana taarifa za kukamatwa kwa makada watatu wa chama hicho, Msukuma, Hussein Bashe na Adam Malima.
Kilichonisikitisha ni maelezo kuwa "walikamatwa na kuhojiwa na polisi kwa tuhuma za kupanga njama za kuvuruga Mkutano Mkuu Maalum wa CCM."
Katika mazingira ya kawaida, sio rahisi kwa makada hao watatu kupanga kuvuruga mkutano mkubwa kama huo ila yayumkinika kuhisi kuwa kilichofanyika ni kuzuwia kile nilichogusia awali, yaani "sio kujadili na kupitisha tu mabadiliko husika" bali pia "kujadili na kupitisha au kutopitisha mabadiliko hayo."
Hili la kuminya fursa ya upinzani kwa mabadiliko hayo linaweza kuwa na athari kwa chama hicho huko mbeleni. Sauti za manung'uniko ni kitu cha kawaida lakini sauti hizo zikiakisi mtazamo wa watu wengi, zinaweza kuathiri mshikamano wa chama hicho.
Hata hivyo, kwa wanaotarajia kuwa "CCM itakufa kutokana na mabadiliko haya" wanapaswa wazielewe vema siasa za Tanzania yetu.
Si kwamba CCM itatawala milele, lakini kwa mazingira tuliyonayo hivi sasa, hakuna chama mbadala. Huo ndio ukweli mchungu.
CCM wanaweza kukandamiza upinzani dhidi ya mabadiliko ya Katiba yao lakini angalau wameitisha mkutano mkuu, wamejadiliana na kupitisha mabadiliko ya katiba yao, sambamba na wameadhibu waliokiuka taratibu za chama hicho.
Sio kamili, lakini hiyo yaakisi demokrasia kwa kiasi fulani. Kwa takriban vyama vyetu vyote vya upinzani, jaribio la kufanya kilichofanywa na CCM wiki iliyopita linaweza kutishia “kukiuwa” chama husika.
Ukiangalia wapinzani wakuu wa CCM, yaani Chadema, sio tu "wamegoma kabisa" kufanya tathmini ya kilichowaangusha katika uchaguzi mkuu uliopita bali pia wametelekeza turufu yao kubwa na iliyowajengea imani kubwa kwa Watanzania, yaani mapambano ya dhati dhidi ya ufisadi, yaliyoibua 'List of Shame,' skandali nzito kama Richmond, EPA, Kiwira, nk.
Cha kusikitisha ni kwamba vyama vyetu vya upinzani sasa vimekuwa kama vinachezeshwa ngoma na CCM. Wafuasi wa vyama hivyo "wapo bize" kujadili matukio yanayoihusu CCM badala ya kuwekeza nguvu kwenye mustakabali wa vyama hivyo.
Jiulize, hivi ajenda kuu ya Chadema, au CUF au ACT- Wazalendo ni ipi muda huu?
Ni katika mazingira hayo, baadhi ya viongozi wa CCM watavumilia mabadiliko yanayoendelea ndani ya chama chao kwa sababu hakuna mbadala wa chama hicho tawala kwa sasa. Tumebaki na miaka mitatu na miezi saba kabla ya uchaguzi mkuu ujao lakini wapinzani wetu wapo bize kuijadili CCM na serikali yake badala ya kujipanga vyema kwa uchaguzi ujao.
Moja kati ya vitu vilivyoiangusha UKAWA katika uchaguzi mkuu uliopita ni "kusubiri makapi ya CCM" badala ya kutangaza mgombea wao mapema na kisha kumnadi kwa nguvu zote, kipindi ambacho CCM ilikuwa na shika-nikushike ya makada wake 40+ waliojitokeza kuwania kuteuliwa kuwa wagombea wa nafasi ya urais kupitia chama hicho tawala.
Nihitimishe makala hii kwa kupigia mstari uwezekano wa aina mbili
Kwanza, CCM kuibuka imara zaidi baada ya Mkutano huo Mkuu Maalum pamoja na hatua za kinidhamu zilizochukuliwa dhidi ya makada kadhaa, kwa sababu nidhamu katika taasisi yoyote ile ni nguzo ya mafanikio, na pia, ili maendeleo yafikiwe shurti kuwepo na mabadiliko, na mabadiliko hukumbana na vikwazo ambavyo vyaweza kurukwa iwapo kuna nidhamu bora.
Japo yaweza kuwa mapema mno kuhitimisha hili, yayumkinika kusema kuwa “mahesabu ya Magufuli yamelipa” kwa maana ya uamuzi wake wa kumteua Mama Salma kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri hivi karibuni unaweza kuwa umesaidia “kumweka karibu” Rais Mstaafu Jakaya Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti mstaafu wa CCM Taifa, na mwenye ushawishi mkubwa katika chama hicho kuliko Dk. Magufuli mwenyewe.
Pili, mambo mawili – hatua dhidi ya makada walioadhibiwa na mabadiliko yaliyopelekea baadhi ya viongozi kupunguziwa nyadhifa – yanaweza kuzua manung’uniko ndani ya chama hicho. Ni wazi kuwa waliochukuliwa hatua za kinidhamu na walioathirika wa kuvuliwa kofia zaidi ya moja za uongozi hawatofurahishwa na hatua hizo. Hata hivyo, je wana pa kukimbilia? Na hapo ndipo utapobaini kuwa siasa za nchi yetu "zingechangamka sana" laiti tungekuwa na upinzani imara.
Na upinzani imara sio lazima upewe ruhusa na serikali kufanya mikutano/maandamano bali kama ule ulioibua 'List of Shame,' Richmond, EPA, nk…hawakuwa na ruhusa ya kufanya hivyo, na pia wanasiasa kama Dk. Willibrord Slaa na Zitto Kabwe walinusurika kwenda jela kwa ajili ya kuwapigania Watanzania.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.