31 Oct 2017



Pasipo kutarajiwa, jana, Jumatatu ya Oktoba 30, 2017, anga za habari huko nyumbani Tanzania zilitawaliwa na habari moja nzito: mmoja wa wana-CCM maarufu, Mbunge kwa tiketi ya chama hicho tawala anayewakilisha jimbo la Singida Kaskazini, na Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bwana Lazaro Nyalandu, alitangaza kujivua uanachama wa CCM na kuomba kujiunga na chama kikuu cha upinzani cha Chadema.


Tukio hilo lilileta mshangao mkubwa kwa sababu kadhaa. Kwanza, licha ya matamshi ya hivi karibuni ya Nyalandu kuhusu haja ya kurejeshwa mchakato wa Katiba mpya, sambamba na kuwasihi wabunge wenzie wa CCM kupinga kwa nguvu zote jaribio la kurefusha muda wa Rais madarakani, hakukuwa na dalili kubwa na za waziwazi iwapo kuna ‘kutofautiana’ kati ya Nyalandu na chama chake.


Na hata kama kungekuwa na dalili hizo – kwa kificho au wazi – bado wananchi wengi wangepokea habari hizo kwa mshtuko mkubwa.

Sababu ya pili ya mshangao kuhusu tukio hilo ni ukweli kwamba mwanasiasa wa chama tawala kuamua kujiunga na upinzani, tena miaka mitatu hivi kabla ya uchaguzi mkuu, ni suala ambalo licha ya kuhitaji ujasiri mkubwa pia linaacha maswali kadhaa ambayo pengine sio rahisi kuyapatia majibu.

Hadi wakati ninaandika uchambuzi huu, kilicho bayana kuhusu sababu za Nyalandu kuchukua uamuzi huo ni sababu alizotanabaisha mwenyewe katika tamko lake kwa umma.

Akizungumza jana, mwanasiasa huyo alidai sababu ya kuchukua uamuzi huo ni kutokuridhishwa na mwenendo wa hali ya kisiasa nchini ikiwa ni pamoja na ukiukwaji wa haki za kibinadamu, ongezeko la vitendo vya dhuluma wanavyofanyiwa Watanzania na kutokuwepo kwa mipaka ya wazi ya mihimili ya dola yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

Lakini hata kabla ya kuchukua uamuzi huo jana, Nyalandu alishaonyesha dalili ya kutofautiana na wana-CCM wenzie, hasa kwa uamuzi wake wa kumtembelea Mbunge Tundu Lissu wa Chadema aliyelazwa huko Nairobi, Kenya kufuatia jaribio la kumuua. Hadi sasa, Nyalandu anabaki kuwa kiongozi wa ngazi za juu wa CCM kumtembelea Lissu huko Kenya.


Huku kukiwa na tetesi kwamba uongozi wa juu wa CCM umewapiga marufuku viongozi wake kujihusisha na suala la Lissu, uamuzi wa Nyalandu kwenye Kenya ‘kinyume na maagizo ya chama chake’ ulihisiwa kuwa ungemwingiza matatizoni.

Dalili nyingine kuwa mwanasiasa huyo hakuwa akipendezwa na baadhi ya mienendo ndani ya CCM ni pale alipoibuka kuhamasisha haja ya kuanzisha upya mchakato wa kupatikana Katiba mpya, sambamba na kuhamasisha wana-CCM wenzake dhidi ya jitihada za chini chini kuongeza muda wa Rais madarakani.

Masuala yote hayo mawili yalitarajiwa ‘kumsababishia matatizo’ mwanasiasa huyo.

Hata hivyo, kuna ‘sababu mbadala’ kuhusu uamuzi wa Nyalandu kujiuzulu. Kuna taarifa kwamba kuna uchunguzi unaofanyika dhidi ya mwanasiasa huyo kuhusiana na utumishi wake kama Waziri wa zamani wa Maliasi na Utalii. Taarifa hizo ambazo bado ni tetesi hadi muda huu, zinaweza kupewa uzito zaidi na ‘screenshot’ inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, ikidaiwa kuwa ni ya mazungumzo ya kundi la Whatsapp la viongozi wanawake wa CCM.

Katika ‘chat’ husika, mmoja wa makada wa kike wa CCM anadai kuwa kuna uchunguzi unaofanyika dhidi ya Nyalandu alipokuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, na kwamba uamuzi wa kujiondoa CCM na kuomba kujiunga na Chadema una lengo la kugeuza suala hilo kuwa la kisiasa pindi akichukuliwa hatua.

Pengine swali muhimu linaloendelea kutawala vichwa ni “kwanini HASWA Nyalandu amejiuzulu?” Kuna sababu alizotoa yeye mwenyewe, ambazo kwa kiasi kikubwa zinaleta mantiki, lakini pia kuna hiyo tetesi kuwa amechukua uamuzi huo kama tahadhari pindi akianzishiwa tuhuma za ufisadi.

Tuchambue sababu zote mbili, yaani alizotoa mwenyewe na hizo tetesi. Kwa vile hatuna maelezo yenye uhakika yaliyo kinyume na sababu alizotoa Nyalandu, nadhani kwa kuzingatia busara tu, itakuwa sio sahihi kudhani anaongopa. Unapopinga kauli ya mtu basi shurti uwe na kauli mbadala yenye uthibitisho. Kwahiyo, angalau kwa muda huu, hakuna sababu za msingi za kupinga sababu alizotoa mwanasiasa huyo.

Kuhusu tetesi za kuwepo kwa mchakato wa ‘kumshughulikia kutokana na tuhuma za ufisadi,’ kuna mantiki kwa mbali, na utata kwa mbali pia. Sio siri kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ilikuwa kama ‘makao makuu’ ya ufisadi. Wizara hiyo ilikuwa kama ile ya Nishati na Madini, ambapo mawaziri lukuki walihamishwa au kuondolewa madarakani kutokana na tuhuma za ufisadi.

Kwamba Nyalandu alipokuwa Waziri wa Maliasili na Utalii kulikuwa na tuhuma za ufisadi, hilo halina mjadala. Lakini kwa kuzingatia kanuni ya asili ya haki, tuhuma hizo zinabaki tuhuma tu mpaka zitakapothibitishwa.

Kwahiyo, hadi hapa, mantiki ya mbali kuhusu uwezekano wa uchunguzi wa tuhuma za ufisadi dhidi ya Nyalandu ipo. Hata hivyo, utata wa mbali ni kwamba katika mazingira ya kawaida tu, na tukijifanya kuamini (angalau kwa minajili ya uchambuzi huu) kwa Nyalandu anafahamu kuhusu uchunguzi huo, je isingekuwa mwafaka kwa yeye kupambana na suala hilo akiwa CCM kuliko nje ya chama hicho tawala?

Sawa, kuna hiyo hoja ya “amehama CCM na anataka kuhamia Chadema ili pindi akichukuliwa hatua, suala hilo lionekane la kisiasa,” lakini ikumbukwe kuwa suala la muhimu sio “suala lionekane la kisiasa” bali “lisitokee kabisa.” Na katika mazingira ya kawaida, huo uamuzi wa tu Nyalandu kuhama CCM na kuikosoa hadharani unatosha kuipa serikali ya chama hicho tawala na taasisi zake “hasira” dhidi ya mwanasiasa huyo. Na hapo hatujagusia uwezekano wa mwanasiasa huyo kujiunga na “adui nambari moja wa CCM” yaani Chadema.

Kwa mtazamo wangu, kama ni kweli kuna uchunguzi unaoendelea au unaotarajiwa kufanyika kuhusu Nyalandu basi yayumkinika kuhisi kwamba ingekuwa rahisi zaidi kwa yeye kupambana na suala hilo akiwa ndani ya CCM kuliko nje ya chama hicho chenye historia ya siasa za kinyongo, visasi na majitaka.

Lakini kuna ‘angle’ kubwa zaidi katika uamuzi huo wa Nyalandu. Yawezekana amesoma vema upepo wa kisiasa huko nyumbani chini ya utawala wa Rais Magufuli, na kubaini vitu kadhaa. Moja laweza kuwa kinachoonekana kama wananchi wengi kutoridhishwa na utawala wa Magufuli, ndani na nje ya CCM. Keyword hapa ni ‘kinachoonekana,’ nikimaanisha pengine ni hisia tu kuwa kuna wananchi wengi wasioridhishwa ilhali ukweli ni kinyume na hisia hiyo.

Kwa minajili ya uchambuzi huu, tufanye kuwa hisia hizo zipo kweli. Kwahiyo, kwa vile Nyalandu alikuwa miongoni mwa makada wa CCM walioomba ridhaa ya chama hicho kuwa wagombea wa urais mwaka 2015 lakini haukufanikiwa, basi pengine anataka kutupa kete yake kupitia upande wa upinzani.

Lakini sio tu kusukumwa na nia ya kuwania urais, lakini yayumkinika kuhisi kuwa mazingira yaliyopo muda huu yanampatia mwana-CCM yeyote nafasi nzuri ya kukikimbia chama hicho. Sio siri kuwa hisia kwamba Magufuli ana dalili za udikteta zinazidi kushika hatamu. Kwa maana hiyo, hata mtu mwenye sababu zake binafsi akikurupuka na kutamka “ninahama CCM kwa sababu utawala wa Magufuli ni wa kidikteta” ataeleweka kirahisi, na anaweza kuungwa mkono kirahisi pia.

Kwamba Nyalandu anaweza “kuruka kutoka kwenye ngalawa na kuingia majini kwenye bahari yenye papa na nyangumi” sio suala dogo. Kama kuikosoa CCM ukiwa ndani ya chama hicho ni hatari, sote twafahamu nini kinachoweza kumkumba anayediriki sio kukosoa tu bali pia kuhama chama hicho tawala. Kwa mantiki hiyo, kwa sababu yoyote ile – iwe hizo alizotaja mwenyewe au tetesi za uchunguzi wa ufisadi – mwanasiasa huyo amefanya maamuzi magumu, na yayumkinika kuamini kuwa amejiridhisha vya kutosha kabla ya kuchukua uamuzi huo.

Kuna mambo matatu yanayoweza kutoa mwangaza kidogo. Kwanza, hivi karibuni, Waziri mpya wa Maliasili na Utalii, Dokta Hamis Kigwangallah alinukuliwa akisema kwamba anayo orodha ya watu mashuhuri, viongozi wastaafu na wabunge wanaojihusisha na ujangili, na atahakikisha anawashughulikia.

Pili, jana katika hotuba yake akiwa huko Mwanza, Rais Magufuli alikumbushia kuhusu Mahakama Maalum ya Ufisadi, ambayo pasi kuuma maneno, imekuwa kama kichekesho kutokana na kukosa kesi. Rais kuitaja mahakama hiyo ‘isiyo na ufanisi angalau hadi sasa’ inaweza kumaanisha kilekile alichokigusia Waziri Kigwangallah kuhusu ujangili.

Na tatu, ‘vijana wa Lumumba’ (makada wa CCM kwenye mitandao ya kijamii) walishaanza kuzungumzia ‘ufisadi wa Nyalandu’ mara tu alipoenda Nairobi kumjulia hali Lissu. Na kasi yao ya mashambulizi dhidi ya Nyalandu imepamba moto zaidi jana baada ya mwanasiasa huyo kutangaza kujiondoa katika chama hicho tawala.

Lakini pia kuna tamko la Humprey Polepole, ‘katibu Mwenezi’ wa CCM kuhusu uamuzi huo wa Nyalandu. Binafsi nilitarajia tamko kali na pengine lililosheheni kebehi kama sio kashfa (na Polepole ni hodari sana kwenye maeneo hayo), lakini reaction ya msemaji huyo wa CCM imekuwa ‘muted.’ Sana sana ameishia kudai kuwa Nyalandu amejiondoa kwa sababu ameshindwa kuendana na kasi ya awamu ya tano. Pia amejaribu kuonyesha kuwa mwanasiasa huyo sio ‘mtu mkubwa’ ndani ya chama hicho tawala. Huyu si Polepole tunayemfahamu kwa umahiri wake wa ‘kusema ovyo.’ Huenda ‘upole’ wake una sababu flani.

Japo kauli ya Kigwangallah na ya Rais Magufuli, sambamba na ‘vijana wa Lumumba’ kumwandama Nyalandu, na ‘upole’ wa Polepole yanaweza kuwa mambo ya kawaida tu, lakini pia yanaweza kutoa mwangaza kuhusu uamuzi huo wa Nyalandu. Hata hivyo, kama nilivyotanabaisha awali, sidhani kama mazingira hayo yangetosha kumfanya Nyalandu kuchukua uamuzi huo mzito.

Kwamba Nyalandu ataandamwa baada ya kuchukua uamuzi huo, hilo halina mjadala. Kama asipoandamwa na ngazi za juu za CCM au kupitia taasisi za dola/umma basi ‘vijana wa Lumumba’ watakesha mitandaoni kumchafua. Pamoja na ukongwe wake katika siasa si Tanzania tu bali barani Afrika kwa ujumla, kwa kiasi kikubwa CCM inaendekeza mno siasa za kisasi, kinyongo na adui mkubwa wa ukweli. Kuikosoa CCM au serikali yake ni kama kusaini ruhusa ya kusumbuliwa kwa kila namna.



Na ni muhimu kutambua kuwa Nyalandu alikuwa akifahamu kuhusu ‘mabalaa’ yanayomsubiri baada ya kuchukua uamuzi huo mzito. Angalia yanayomsibu Yusuph Manji, mtu aliyemwaga mamilioni ya fedha kuifadhili CCM lakini amebaki kuwa ‘kielelezo cha hasira za CCM.’

Je CCM wakiamua kulipa kisasi kwa Nyalandu watafanikiwa? Inategemea sana busara za Magufuli. Yote yanayoelezwa kuwa ‘ufisadi wa Nyalandu’ yailikuwa na baraka za mtangulizi wa Magufuli, yaani Rais Kikwete. Kwahiyo, kama ambavyo jitihada zozote za kumbana Lowassa zilivyoshindikana kwa vile zingeishia kumchafua pia Kikwete, ndivyo jaribio la ‘kulipiza kisasi kwa Nyalandu’ linavyoweza kumtia matatani JK.


Licha ya kuelezwa kuwa Nyalandu alikuwa mmoja wa watu wa karibu wa JK, pia ni muhimu kutambua kuwa mmoja wa watu wake wa karibu ni mke wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa, Mama Anna. Mara baada ya kurejea Tanzania kutoka Marekani, Nyalandu alikuwa miongoni mwa washauri Mama Anna Mkapa, katika uendeshaji wa taasisi ya Mfuko wa Fursa Sawa kwa Wote (EOTF).

Kwa maana hiyo, jaribio lolote la ‘kumwandama Nyalandu’ linaweza kuzua kile Waingereza wanaita ‘unintended consequences,’ au ‘matokeo yasiyokusudiwa kwa Kiswahili.

Pia ni muhimu kutambua u-kimataifa wa Nyalandu. Mwanasiasa huyo ana mahusiano mazuri na wanasiasa wenye nguvu kubwa hususan nchini Marekani. Japo ‘nguvu’ zao zinaweza kutofua dafu kwa Magufuli, lakini sote twafahamu kuwa ni vigumu kwa Tanzania yetu kuwa na ‘jeuri’ katika umasikini wetu.


Hatma ya Nyalandu akifanikiwa kuhamia Chadema ikoje? Binafsi, ninahisi mambo makuu mawili. Kwanza, ujio wake katika chama hicho kikuu cha upinzani unaweza kuamsha msisimko mpya wa siasa za ndani na nje ya chama hicho, na Tanzania kwa ujumla.

Kwa upande mmoja, anaweza kuendeleza hoja zake kama hiyo ya kudai kurejeshwa kwa mchakato wa Katiba mpya, suala ambalo Chadema na washirika wake wa UKAWA ni kama wamelitelekeza.

Lakini pengine kubwa zaidi ni uwezekano mkubwa wa Nyalandu kuwa mmoja wa wagombea wa Urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi mkuu ujao mwaka 2020. Kwamba amejiondoa CCM kwa hiari yake (angalau kwa mujibu tunachofahamu hadi muda huu) na kujiunga na Chadema kwa hiari yake, anaweza kuwa na faida ya ziada kuliko majina mengine mawili yanayotajwa kuhusu urais mwaka 2020 kupitia Chadema, Mawaziri Wakuu wa zamani, Lowassa na Sumaye.


Kwamba Nyalandu ni ‘mwana-CCM pekee aliyemjali Lissu kwa kumtembelea huko Nairobi,’ na ukweli kuwa yeye na Lissu wanatoka mkoa mmoja, wanaweza kujenga ‘dream team’ inayoweza kuirejesha Chadema enzi za kina Dkt Slaa, Zitto na Mbowe.

Lakini pia katika mazingira yaliyopo sasa, Chadema imekuwa kama haina mpango wa kushiriki uchaguzi mkuu ujao. Maandalizi yanayopaswa kufanyika sasa – miezi 36 tu kabla ya uchaguzi huo – ni kama hayapo. Ndiyo, Magufuli kapiga marufuku shughuli za kisiasa, lakini ni lini Rais kutoka CCM aliwahi kuridhika shughuli za wapinzani?

Kwa maana hiyo, ujio wa Nyalandu unaweza kuamsha matumaini kwa chama hicho kikuu cha upinzani kuhusu nafasi yake katika uchaguzi mkuu ujao.

Hata hivyo, kuna vikwazo vikuu viwili. Cha kwanza, ni lile lililojiri baada ya Lowassa kujiunga na CCM, Kwa minajili ya kumbukumbu tu, Chadema ilimwandama Lowassa kuwa ni ‘baba wa ufisadi’ kwa takriban miaka 9 mfululizo, kisha ghafla wakampokea na kumfanya mgombea wao wa Urais katika uchaguzi mkuu uliopita. Kwa busara za kawaida tu, huwezi kumchafua mtu kwa muda wote huo kisha ukategemea kumsafisha ndani ya miezi mitatu. Japo makada wa chama hicho hawataafiki, athari za kumpokea Lowassa na kumfanya mgombea wao zinaendelea kukisumbua chama hicho.

Kama ilivyokuwa kwa Lowassa, baadhi ya viongozi wa Chadema walishawahi ‘kumpaka’ Nyalandu wakimwita fisadi, hali inayoweza kutumiwa na CCM kudai kuwa ‘Chadema ni kimbilio la mafisadi.’ Hata hivyo ni rahisi kwa chama hicho cha upinzani kuwauliza CCM, “mpaka mwanasiasa awakimbie na kujiunga nasi ndio mnaanza kumwita fisadi?” Ni hoja inayoingilia akilini.


Je Nyalandu atapata mapokezi mazuri huko Chadema? Kama kauli ya Lowassa jana kuwa Chadema itakuwa ‘imelamba dume’ pindi Nyalandu akijiunga na chama hicho inaashiria chochote basi kuna uwezekano mkubwa wa mafanikio makubwa kwa mwanasiasa huyo.

Hata hivyo, ukweli kwamba Nyalandu ni miongoni mwa watu wenye sifa na uwezo wa kuwa wagombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020 unaweza kupelekea mgongano dhidi yake na majina mengine yanayotarajiwa kuwemo kwenye kinyang’anyiro hicho, yaani Lowassa, Sumaye na Lissu.

Hili sio tatizo kubwa sana iwapo maslahi ya Chadema – badala ya maslahi ya mtu au kikundi binafsi – yakiwekwa mbele. Kwamba kufanyike tathmini ya kutosha kufahamu nani anayeweza kukiwezesha chama hicho kuing’oa CCM madarakani hapo mwaka 2020.

Kwamba Nyalandu anaweza kuleta hamasa kwa wana-CCM wengine (Membe?) kujiunga na Chadema, na kama ujio wake huko Chadema utaleta matokeo chanya, ni suala la muda. Lililo bayana hadi muda huu, uamuzi wake huo wa ghafla umetushtua wengi ikiwa ni pamoja na CCM na makada wake. Na yayumkinika kuamini kuwa uamuzi huo utaleta msisimko mpya katika siasa za Tanzania.

Mwisho, uchambuzi huu umetokana na uelewa wangu wa siasa za Tanzania, na unaweza kuwa sio sahihi kulingana na mitazamo tofauti. Jiskie huru kuchangia maoni, kunikosoa au hata pongezi zinaruhusiwa. Siku zote ninajitahidi kwenda mbali zaidi ya kuripoti tu matukio badala ya kuyachambua kwa undani zaidi. Asanteni na siku njema



30 Sept 2017

Mara baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka juzi nilipata ujumbe kutoka kwa watu kadhaa wakinieleza kuwa kwa namna moja au nyingine niliwasaidia kufanya maamuzi ya kumpigia kura aliyekuwa mgombea wa CCM, John Magufuli.

Unajua, moja ya makosa makubwa waliofanya wana-UKAWA kwenye kampeni za uchaguzi huo ni kutojihangaisha kulifikia kundi muhimu la wapigakura nchini Tanzania: wananchi wasiofungamana na chama chochote.

Ili kulielewa vema kundi hili, inabidi kuangalia idadi ya wanachama wa CCM na UKAWA (kwa kuzingatia uchaguzi wa mwaka 2015). Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa CCM ina wanachama milioni 8. Makadirio ya idadi ya wanachama wa UKAWA ni angalau milioni 5. Kwahiyo makadirio ya jumla ya wapigakura wenye kufungamana na vyama vya siasa ni takriban milioni 13. Tanzania ina watu zaidi ya milioni 50, tukitoa hao milioni 13 tunabakiwa na watu milioni 37. Tukienda kwenye idadi ya waliojiandikisha kupiga kura walikuwa milioni 23 hivi. Kwahiyo, kimahesabu, takriban watu milioni 10 (milioni 23 waliojiandikisha kutoa milioni 13 wenye ufuasi wa vyama vya siasa) walikuwa wapigakura wasiojihusisha na chama chochote.

Tofauti na UKAWA ambayo viongozi na wanachama wake walielemea zaidi kuhamasishana wao kwa wao, wenzao wa CCM waliwalenga hao takriban milioni 10 wasiofungamana na chama chochote.

Na kimsingi, mie japo sikuwa mpigakura, nilikuwa katika kundi la watu wasio na vyama. Mara ya mwisho kuwa mwanachama wa chama cha siasa ilikuwa mwaka 2005, na takriban miaka 15 baadae, sheria ilinizuwia kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Mwaka 2006 nilianza kufuatilia skandali ya Richmond iliyokuwa ikimhusisha aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa. Naweza kwa uhakika kuwa nilikuwa bloga pekee niliyevalia njua suala hilo, sambamba na kuliandikia makala mbalimbali katika magazeti ya ‘Kulikoni’ na baadaye ‘Mtanzania’ na hatimaye Raia Mwema. Ufuatiliaji huo ulinigharimu mno lakini hilo si la muhimu kwa sasa.

Kutokana na bughudha niliyopata kuanzia mwaka 2006 na kuendelea, haikuwa ajabu kwa mie kuunga mkono harakati za Chadema kupambana na ufisadi. Na mwaka 2010 nilishiriki kikamilifu kumnadi mgombea urais wa Chadema, Dkt Wilbrord Slaa. Hata baada ya uchaguzi huo, niliendelea kuunga mkono sera hiyo ya ufisadi ya Chadema. Hata hivyo, sikuwahi kuwa mwanachama wa chama hicho.

Mwanzoni mwa mwaka 2015 nilikuwa miongoni mwa watu waliopiga kelele kwenye mitandao ya kijamii kuwataka UKAWA watangaze mgombea wao wa kiti cha urais mapema hasa ikizingatiwa kuwa CCM walikuwa na safari ndefu ya ‘kung’oana macho’ kugombea kuteuliwa na chama chao kuwania urais. Hata hivyo, kelele hizo hazikuzaa matunda, na utetezi mkubwa ulikuwa “UKAWA inajibidiisha kushughulikia daftari la wapigakura sambamba na kuhamasisha wapigakura watarajiwa kujiandikisha.” Hatimaye tulikuja kufahamu kuwa mbinu hiyo ya “kununua muda” ililenga kumwandalia nafasi Bwana Lowassa endapo asingepitishwa huko CCM. Muungano wa vyama makini vinne vya upinzani unasubiri ‘kapi’ kutoka chama tawala!

Kufupisha stori, mara baada ya UKAWA kumtangaza Lowassa kuwa mgombea wao, kwa sie wengine ilikuwa haiwezekani tena kuunga mkono umoja huo uliojumuisha vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.

Kwa vile wagombea wakuu katika uchaguzi huo walikuwa Lowassa na Magufuli, ilikuwa vigumu kumpinga Lowassa bila kumsapoti Magufuli. Kwahiyo japo awali nilijaribu kuepuka kumnadi mgombea wa CCM, Magufuli, mazingira yaliyokuwepo – pamoja na mkataba wa kutoa huduma ya usadi (consultancy) – ilipelekea nami nianze kumnadi Magufuli. Haukuwa uamuzi rahisi hasa kwa kuzingatia serikali ya CCM ilivyonitenda kuanzia mwaka 2006 nilipoanza kufuatilia skandali ya Richmond.

Ushiriki wangu kwenye kampeni haukuwa rahisi. Katika maisha yangu yote sikuwahi kutukanwa kiasi nilichotukanwa katika kampeni za uchaguzi huo. Jitihada zangu za kuwaelewesha watu kwanini nimelazimika kumuunga mkono Magufuli hazikusaidia kitu. Pengine kibaya zaidi ni kwamba wakati wa kuelekea uchaguzi huo nilifiwa na baba yangu, marehemu Mzee Philemon Chahali. Baadhi ya watu bila utu walitumia msiba huo kuingiza uhasama wa kisiasa.

Pamoja na mvua ya matusi ya kila aina, niliendelea na jukumu la kumnadi Bwana Magufuli. Nadhani mchango wangu mkubwa zaidi ulikuwa kwa wapigakura waliokuwa hawajafungama na chama chochote. Na nilifahamu kuhusu hilo baada ya uchaguzi ambapo baadhi yao walinieleza bayana kuwa ushawishi wangu kwao ulipelekea kufanya uamuzi wa kumpigia kura mgombea huyo wa CCM.

Lakini tukiweka kando ‘sababu zangu binafsi,’ Magufuli alionekana kama mgombea bora zaidi ya mpinzani wake Lowassa. Pamoja na sababu nyingine, wakati Magufuli alikuwa ‘mgombea wa CCM kutoka CCM,’ Lowassa alikuwa mgombea wa UKAWA kutoka CCM.

Hatimaye uchaguzi ukafanyika na Magufuli akaibuka mshindi. Kama kuna kitu kilichonipa matumaini sana kuhusu urais wa Magufuli ni hotuba yake aliyoitoa wakati wa uzinduzi wa bunge la Jamhuri ya Muungano. Katika hotuba hiyo, Magufuli alionyesha kuwa mtu anayezielewa vema shida za Watanzania hususan janga la rushwa na ufisadi, na akaapa kushughulikia kwa nguvu zake zote. Na alipoomba Watanzania wamwombee katika vita hiyo ngumu, naamini hata miongoni mwa wale ambao hawakumpigia kura waliitikia wito huo wa kumfanyia maombi.

Kisha zikaja ziara ya kushtukiza na taratibu tukaanza kuingiwa na matumaini mapya ya “mrithi halisi wa Nyerere/Sokoine.” Na dunia pia ikaungana nasi kusherehekea kiongozi huyo adimu, na ikaibuka alama ya reli #WhatWouldMagufuli Do iliyotamba kila kona ya dunia. Na haikupita wiki bila kushuhudia “tumbua majipu.”

Kwa kufurahishwa na kuridhishwa na utendaji wake, mie ‘nikajipinda’ na kuandika kitabu cha tathmini ya urais wa Magufuli, siku 55 tu baada ya yeye kuapishwa kuwa Rais wa tano wa Tanzania. Watu kadhaa walinikosoa kwamba haikuwa sahihi kwangu kufanya tathmini hiyo mapema kiasi hicho. 


Kwa wakati huo niliona walionikosoa kuhusu suala hilo kama watu wenye chuki binafsi dhidi ya ‘mkombozi’ Magufuli.

Dalili ya kwanza kwamba huenda kuna walakini katika utawala wa Magufuli ni pale alipotangaza baraza lake la mawaziri ambalo ilituchukua wiki kadhaa kulisubiri. Lilipotangazwa, sio tu lilikuwa kubwa kuliko ahadi yake kuwa angeunda serikali ndogo tu ili kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali, bali pia lilijumuisha baadhi ya sura ‘zenye utata.’ Miongoni mwa sura hizo ni Profesa Muhongo, ambaye alilazimika kujiuzulu katika serikali ya Awamu ya Nne kutokana na kuhusishwa na skandali ya Tegeta Escrow.

Kuna tuliouona uteuzi wa mtu kama Nape Nnauye kuwa ni wa kisiasa zaidi, huku sura kama Simbachawene, Lukuvi na Profesa Maghembe zikijenga ishara kuwa huenda mambo hayajabadilika kama tulivyotarajia.

Kisha kukafanyika uteuzi wa mabalozi ambao ulionekana bayana kama kutumia nafasi hizo nyeti kuwaondoa watu flani kwenye nyadhifa zao huko CCM. Baadhi yetu tukaanza kujiuliza, “hivi hatujayashuhudia haya huko nyuma?” Lakini tukaendelea kuwa na matumaini.

Dalili ya kwanza kabisa kuwa pamoja na mazuri yake yaliyowavutia Watanzania wengi na kona mbalimbali duniani, Bwana Magufuli ana mapungufu yake ni pale serikali yake kupitia ‘shujaa wa sasa’ Nape Nnauye ilipozuwia haki ya mamilioni ya Watanzania kusikiliza matangazo ya moja kwa moja ya Bunge. Niwe mkweli, wanaomwona Nape shujaa huwa siwaelewi kabisa. Ningemwona shujaa laiti angetumia ukongwe wake ndani ya CCM kumweleza bosi wake Magufuli kuwa wazo la kuzuwia matangazo ya bunge live ni fyongo, na laiti Magufuli angemomea basi angejiuzulu kishujaa badala ya kusubiri kufukuzwauwaziri kwa kupambana na ‘kimeo kingine cha Magufuli’ yaani Daudi Albert Bashite.

Baadaye likaja zuwio dhidi ya mikutano na maandamano ya vyama ya siasa. Awali baadhi yetu tulijipa matumaini kwamba “ah huu ni muda wa kuchapa kazi. Hayo maandamano na mikutano ni ya nini muda huu?” Kwahiyo kwa wakati huo ili-make sense.

Mara tukakumbwa na janga la tetemeko la ardhi huko Kagera. Ikategemewa Rais angekwenda kuwafariji wahanga hasa ikizingatiwa kuwa anatoka Kanda ya Ziwa. Hakwenda hadi baadaye. Na alipokwenda akatoa hotuba isiyopendeza kuisikiliza. Maneno kama “serikali haikuleta tetemeko la ardhi” sio ya busara hata kidogo. Pia akaongopa kwa kudai hakuna serikali duniani inayotoa misaada kwa wahanga wa majanga ya asili. Sijui muda huu anajisikiaje akiona kwenye runinga jinsi serikali ya Marekani inavyowahudumia wahanga wa vimbunga.

Baadaye kukusikika taarifa mbalimbali za tishio la uhaba wa chakula, lakini badala ya kuwafariji wananchi, Magufuli akawaropokea kwamba serikali yake haitotoa chakula kwa vile serikali haina shamba.
Na wakati mmoja alipita sijui Nzega au Urambo, mwananchi mmoja akamwambia “njaa Mheshimiwa.” Hilo jibu alilotoa utadhani ugomvi. Pamoja na majibu mengine ya ngebe akasema “njaa, kwani mnataka niingie jikoni kuwapikia?” Ovyo kabisa.

Likatokea tukio la maaskari polisi wanane kuuawa huko Kibiti lakini Amiri Jeshi Mkuu akaenda kufungua mabweni chuo kikuu cha Dar es Salaama badala ya kwenda kuaga miili ya askari hao.

Pia kulijitokeza tukio la ‘kupotea’ kwa kada wa Chadema Ben Saanane ambaye hadi ‘kupotea’ kwake alikuwa akihoji kwa nguvu kubwa kuhusu PhD ya Magufuli. Baadhi tulimsihi awe makini (kwa sababu dalili zilishaanza kujionyesha kuwa Magufuli ni mtu wa aina gani) lakini bahati mbaya hakusikia ushauri wetu. Hadi leo haijulikani nini kimemsibu kijana huyo japo Chadema nao hawawezi kukwepa lawama katika poor handling ya suala hilo. Kumekuwa na kauli zinazokinzana kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho kama ile ya mwenyekiti Mbowe kuwa Ben alitekwa huku Mbunge wa chama hicho Saeid Kubenea akidai kuwa kada huyo anaonekana vijiweni. Kwanini chama hicho hakijawabana viongozi hao kufafanua kauli zao, only God knows!

Lakini kama kuna tukio lililompotezea heshima kubwa Bwana Magufuli ni lile la Mkuu wa Mkoa Paul Makonda kuvamia stesheni ya redio na runinga cha Clouds  akiwa na askari wenye silaha. Siku chache baadaye huku baadhi ya watu wakitarajia angemtimua Makonda, Magufuli akatufanya sote mabwege kwa kumtetea Makonda huku akidai yeye hapangiwi kazi, yeye ndo Rais, na kumwita Makonda mchapakazi. Yaani Mkuu wa Mkoa amevamia kituo cha habari, kitendo ambacho ni kosa la jinai, halafu Rais anamsifu kuwa ni mchapakazi?
Uswahiba wa Magufuli na Makonda umechangia mno ugumu wa kuchunguza tuhuma kuwa mkuu huyo wa mkoa amefoji jina analotumia pamoja na cheti cha kuhitimu kidato cha nne. Laiti Magufuli angekuwa mwajibikaji kama tunavyoamini basi angeamuru uchunguzi kuhusu suala hilo.

Na kwa wanaofahamu yanayoendelea ‘nyuma ya pazia,’ inadaiwa kuwa vetting aliyofanyiwa Bashite ilionyesha bayana mapungufu yanatajwa kumhusu yeye, na ‘Bwana mkubwa’ akashauriwa kuchukua hatua stahili lakini hakufuata ushauri huo.

Hili la Bashite limeendelea kuwakera watu wengi sana, hasa ikizingatiwa kuwa mtu huyo anatumia ipasavyo upendeleo anaopewa na Magufuli, na kufanya dharau za wazi kama ile ya kupigiwa saluti na vingozi wa ngazi za juu wa jeshi la polisi huku amevaa kapelo. Hiyo ni dharau ya hali ya juu kwa vyombo vyetu vya dola.



Na Magufuli ataingia kwenye vitabu vya historia kwa serikali yake kulifungia gazeti la kila wiki la Mwanahalisi kwa miaka mitatu, na siku 10 baadaye akalifungia gazeti jingine la kila wiki la Raia Mwema kwa siku 90. 

Na kama kuna gazeti lilijitahidi mno 'kumnadi' Magufuli ni Raia Mwema. Nakumbuka makala nyingi katika gazeti hilo wakati wa kuelekea kwenye uchaguzi zilisheheni habari 'nzuri' kuhusu Magufuli.

Pengine si vibaya nikitumia fursa hii kueleza kuwa sababu hasa iliyonifanya niache uandishi wa makala katika gazeti hilo ni kwamba lilihojiwa na 'vijana wa Magufuli' kuhusu mie lakini wahusika hawakuona umuhimu wa kunieleza wala kuandika kuhusu habari hiyo.


Na kilichopelekea bwege huyo kudadisi kuhusu mie ni TWEET...Yes, just a tweet, a #FutureTweet to be precise. 

Kanuni muhimu katika chombo cha habari ni kwamba unyanyasaji wa taasisi yoyote ile dhidi ya mwenzenu ni unyanyasaji dhidi yenu nyote. Gazeti hilo lilipaswa kunijulisha kuhusu kilichotokea au kukiandika kama habari gazetini. Lakini bahati nzuri mie mzoefu wa 'dark arts' nikafahamu mapema kilichokuwa kinaendelea.

Hata hivyo, kitendo cha gazeti hilo nilikiona kama usaliti, nikaamua kuachana nao. Hata hivyo, mie sina kinyong'o nao na ndio maana jana nililaani na kupiga kelele kuhusu hatua hiyo ya serikali.

Haya yanatokea wakati Tanzania bado ipo kwenye mshtuko kufuatia jaribio la kumuua mwanasiasa ambaye amekuwa mpinzani mkubwa wa Magufuli, mbunge wa Chadema Tundu Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria cha TLS. Chuki inayopandikizwa dhidi ya wapinzani imepelekea takriban asilimia 99 ya viongozi wa CCM kuogopa kwenda kumjulia hali Lissu huko Nairobi alikolazwa.

Lakini pengine kipimo halisi cha mambo kwenda kinyume na matarajio ya baadhi yetu kuhusu Magufuli ni kwamba tangu aingie madarakani, zaidi ya viongozi na wanachama 400 wa Chadema wamekamatwa na polisi. Imefika mahala, wakuu wa wilaya wanakamata viongozi wa Chadema kila wanapojisikia. Na pengine kibaya zaidi ni ukweli kwamba taratibu jamii inaanza kuzowea kuona viongozi na wanachama wa upinzani – hususan Chadema – wakidhalilishwa na kukamatwa kiholela.

Jambo jingine la kusikitisha kuhusu utawala wa Magufuli ni utitiri wa sheria kandamizi kuhusu uhuru wa habari. Licha ya sheria ya makosa ya mtandao ya mwaka 2015 ambayo ni kazi ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete, tayari kuna sheria ya Huduma za Habari, ambayo ‘shujaa Nape’ alihusika kwa kiasi kikubwa, na sasa kuna kinachoitwa ‘Kanuni za Maudhui ya Mitandao ya Kijamii,’ ambayo laiti zikipitishwa zitakuwa balaa kubwa.

Na huku Chadema ikishuhudia viongozi na wanachama wake wakinyanyaswa ovyo ovyo, kuna kila dalili kuwa mgogoro unaoendelea ndani ya chama cha CUF una mkono wa serikali hasa kwa kuzingatia mwenendo wa ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa (taasisi ya serikali) kuibeba waziwazi kambi ya mwanachama aliyejiuzulu kwa utashi wake Prof Lipumba, ambaye from nowhere alirudi chamani na kudai yeye bado mwenyekiti.

Majuzi, Magufuli katumwagia siri kwamba kuna siku aliombwa ushauri na Spika Ndugai kuhusu uteuzi wa wajumbe wa kamati ya bunge. Hiyo ina maana kuwa bunge limewekwa mfukoni na mhimili wa serikali. Kadhalika, kauli za Jaji Mkuu ‘mpya’  baada ya jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu zinajenga taswira ya mhimili wa mahakama nao kuwekwa mfukoni na mhimili wa serikali.

Katika kuhitimisha makala hii ndefu ninarudia swali lililobeba kichwa cha habari: nini kilichomsibu Magufuli hadi kubadilika kiasi hiki? Kauli yake kuwa alisukumwa kuchukua fomu ya urais inazidi kuleta mkanganyiko kwamba labda alikuwa anafahamu fika hana uwezo wa kuongoza taifa letu lakini akakubali tu kutokana na shinikizo hilo, ambalo hata hivyo hatujui limetoka kwa watu gani.

Dalili kwamba ‘Magufuli atabadilika’ (kurejea kuwa yule tuliyemwona ni mkombozi wetu) ni finyu. Kwa vile maamuzi yake mengi yanamtengenezea maadui zaidi ya waliopo, kuna kila dalili kwamba atazidi kuwa mkali ili ‘kujilinda.’ Tutegemee uhuru wa kujieleza/habari uendelee kubinywa zaidi kadri bwana mkubwa anavyozidi kutukumbusha yeye ndio Rais, asiyeambiwa nini cha kufanya, anayejua siri zote na nchi yetu, na vitu kama hivyo.

Nimalizie kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuhusu rai ya mara kwa mara ya Rais Magufuli kuwataka Watanzania tumwombee. Na tufanye hivyo kwa bidii kubwa ili Mwenyezi Mungu amwonyeshe njia sahihi ya kuliongoza taifa letu kwa kuzingatia haki na usawa. Tumwombee aondokane na 'fear of the unknown,' apate muda wa kupumzika badala ya kukesha macho akihofia 'the unknown.' Aachane na chuki dhidi ya kila anayemkosoa hata kama kukosoa huko ni kwa nia njema. Tumwombee awe na busara ya kutokitumia 'kitengo' kama kampuni yake binafsi. Ajiulize, kwanini licha ya ulinzi wake wa 'kufa mtu' bado siri zinavuja? Jibu jepesi: ukiwafanya watu wazima tena wenye utaalamu nyeti kuwa kama watoto, inakuwa 'mwaga ugali nimwage mboga.' Na asije kukasirishwa na makala hii...

Ni wazi kuwa ndoto za kuikomboa Tanzania yetu kiuchumi haziwezi kufanikiwa katika hali ya sasa ya siasa za vitisho, kunyanyasa wapinzani, “watu wasiojulikana,” na vitu kama hivyo. 

Mungu ibariki Tanzania


8 Sept 2017



Jana, Septemba 07, 2017, majira ya mchana, zilipatikana taarifa kwamba Tundu Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Mbunge wa Singida Mashariki, Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani, na Rais wa Chama cha Wanasheria (TLS), amepigwa risasi kadhaa na kujeruhiwa vibaya.

Tukio hilo la kutisha lilitokea jijini Dodoma, wakati Mbunge huyo aliposhuka nyumbani kwake eneo la Area D, inakoelezwa alienda kwa ajili ya kujipatia mlo wa mchana.

Kabla ya kuingia kiundani kwenye makala hii, nitumie fursa hii kutoa salamu za pole kwa Lissu, na kumwombea apone haraka. Salamu za pole pia kwa viongozi, wanachama na wafuasi wa Chadema, chama ambacho Lissu amekuwa akikiwakilisha kwa ufanisi mkubwa.

Pia ni vema nitahadharishe mapema kwamba intelijensia sio sayansi timilifu kwa asilimia 100, kwa kimombo wanasema “intelligence is not an exact science.”

Okey, sasa tuingie mtamboni. Hadi muda huu kuna dhana za msingi tatu ambazo zinatokana na‘mchujo’ wa dhana mbalimbali.

Dhana ya kwanza na ambayo pengine ni maarufu zaidi ya zote ni kwamba jaribio hilo la mauaji ya Lissu lina mkono wa dola. Kwamba sio siri kuwa Lissu amekuwa ‘akiisumbua mno’ serikali, ambapo wafuasi wake wanamwona kama jasiri asiye na uoga wa kusema ukweli, ilhali wapinzani wake wakimwona kama mchochezi.

Yayumkinika kuhitimisha kwamba kama kuna mwanasiasa wa upinzani ambaye amekuwa ‘mwiba mchungu’ kwa serikali ya Rais John Magufuli basi si mwingine bali Lissu.

Na pengine kinachoongeza uzito kwenye dhana hii ni ukweli kwamba Agosti 18 mwaka huu, Lissu aliwaeleza wananchi kwamba anafuatiliwa.

Namnukuu "Naomba kabla sijaanza Mazungumzo yangu nimuombe Mkuu wa idara ya Usalama wa Taifa anaitwa Kipilimba au Inspekta Generali wa Polisi Simon Sirro, wale vijana ambao wamewatuma na kwa wiki tatu mfululizo wananifuata kila nilipo wanaotembea na gari ya Toyota premio namba T460CQV, jana niliwakaba Kanisani St. Peter's.



Kwa upande mwingine serikali ya Magufuli ni kama ilikuwa inatafuta ‘kulaumiwa bure.’ Kwa sababu, Hadi muda huu hakuna sababu moja ya msingi kwa serikali hiyo kuyafanya maisha ya wanasiasa wa upinzani yawe magumu kiasi hiki. Magumu kwa maana ya kuwanyima kila aina ya fursa ya kufanya siasa (political space).

Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, zaidi ya viongozi na wafuasi 400 wa Chadema wameshakamatwa tangu Magufuli aingie madarakani. Mtu atayedai kuwa kiongozi huyo ‘anawachukia wapinzani’ hatoonekana mtu wa ajabu japo huenda akatupwa jela.

Katika hotuba zake mbalimbali, Rais Magufuli ameshindwa kuficha hisia zake dhidi ya upinzani na wapinzani. Juni 12 mwaka huu, Rais Magufuli alimweleza Spika Job Ndugai maneno yafuatayo

“Tumia mbinu hiyohiyo ya kuwafanya wasiropokee Bungeni, waropokee nje na kule tutadili nao vizuri kwasababu wanapokua kule ndani wana kinga wanaweza wakatukana chochote, sasa kinga wanayoitumia vibaya bungeni kainyooshe wewe. Wawe wanatoka kule bungeni, ukishamfukuza hata mwezi mzima… atakuja aropokee huku, na mimi nakueleza waache waropokee huku nitadili nao, wala siwatishi lakini hatuwezi kuwa kwenye vita wewe unaanza kugeuka kupiga wale wanaokwenda mbele…. ni nafuu unyamaze ukalale.”

Kwa kuangalia jinsi watendaji wa serikali ngazi za mkoa na wilaya wanavyochuana na polisi kuwanyanyasa wapinzani, hususan wa Chadema, dhana kuwa serikali ina mkono katika jaribio la mauaji ya Lissu ni kama ‘ready-made.’

Hata hivyo, pamoja na ‘dalili zote’ kuashiria uwezekano wa mkono wa serikali katika jaribio la kumuua Lissu, dhana hii inakosa mantiki kiuhalisia. Ni kwamba hakuna tija kwa serikali kumuua Lissu. Sawa, sio siri kuwa uhusiano kati ya serikali na Lissu/ wapinzani sio mzuri, lakini haitokuwa na tija yoyote kwa serikali ya Magufuli kumuua Lissu.

Na hata kama ingekuwa lazima ‘aondoke,’ basi kuna ‘njia mwafaka zaidi’ za mauaji ya watu maarufu (assassination), huku 'kifo cha ajali' ikiwa maarufu na rahisi zaidi.

Halafu kinachotatiza katika tukio la jana, na kinachopunguza zaidi nguvu ya dhana kwamba ‘kuna mkono wa serikali,’ ni jinsi waliofanya shambulio hilo walivyoonekana kama wanahitaji publicity ya kutosha. Kwanini? Jibu lipo kwenye uchambuzi wa dhana ya tatu.

Dhana ya pili ni dhaifu kuliko nyingine mbili. Hii inahusisha mbio za urais mwaka 2020. Kwamba kila siku Lissu amekuwa akijitengenezea mazingira ya mgombea mwafaka wa Chadema/Upinzani katika uchaguzi mkuu ujao, wala halina mjadala. Sio kwamba Lissu amekuwa hodari katika masuala mbalimbali kwa vile anataka urais (hajawahi kutamka nia ya kugombea nafasi hiyo) lakini umahiri wake bungeni na katika masuala ya kisheria na kitaifa kwa ujumla, unamfanya kuwa kipenzi cha takriban kila mfuasi wa Chadema.

Dhana hii dhaifu inasema kuwa jaribio hilo la mauaji ni kazi ya wapinzani wa kisiasa wa Lissu, hususan ndani ya chama chake.

Udhaifu wa dhana hii ni kwamba, kama ambavyo kwenye dhana ya kwanza, hakuna tija katika kumdhuru Lissu hadharani. Kwamba hata kama kungekuwa na lundo la wapinzani wa kisiasa wa Lissu huko kwenye chama chake, kwanini wafanye ‘operesheni’ hiyo waziwazi badala ya kuandaa mkakati wa siri?

Na kama ilivyokuwa kwenye dhana ya kwanza, hata kama wapinzani wa kisiasa wa Lissu ndani ya chama chake wangekuwa wahusika, kwanini basi tukio hilo lifanyike katika mazingira ya ‘kusaka publicity kwa nguvu’?

Hiyo inatuacha na dhana moja, ya tatu, na ya mwisho. Ya mwisho lakini sio haba katika mantiki. Dhana hii inaeleza kwamba jaribio hilo la mauaji limefanywa makusudi na kile wajuzi wa mambo wanaita ‘rogue elements.’  Hizi zilitusumbua sana katika utawala wa Awamu ya Nne wa Rais Jakaya Kikwete. Rogue elements hizi zinajumuisha watumishi halali wa vyombo vya dola wanaofanya shughuli zisizo halali. Nani anawatuma? Hiyo ni habari nyingine.

Kuna kitu kinachofahamika kama ‘Deep state.’ Kila nchi ina tafsiri yake kuhusu ‘deep state’ lakini tafsiri nyepesi kwa mazingira yetu ni ushirika wa watu wenye nguvu katika serikali na jamii – mfano vigogo (hususan wa zamani) wa vyombo vya dola, wafanyabiashara wenye uwezo mkubwa na wanasiasa kutoka upande wowote ule, lakini zaidi chama kilichopo madarakani.

Dhana hii inaliona tukio la kujaribu kumuua Lissu kama njia rahisi ya kuichafua serikali ya Rais Magufuli, ambayo kwa bahati mbaya/makusudi ilishajitengenezea mazingira ya kulaumiwa pindi la kutokea likimtokea mwanasiasa wa upinzani kama Lissu. Rais anaposhindwa kudhibiti ‘chuki zake’ dhidi ya wapinzani, anawapa nafasi nzuri ‘wabaya wake’ kutenda kitu kisha ikawa rahisi tu lawama kuelekezwa kwake.

Ndio maana dhana ya kwanza – kwamba kuna mkono wa serikali ya Magufuli kwenye jaribio la kumuua Lissu – inaonekana kama yenye uzito kwa vile "kuna sababu ready-made.”

Dhana hii inapata uzito kutokana na ukweli kwamba Magufuli amejitengenezea maadui wengi, wenye nguvu, na baadhi yao wakiwa viumbe hatari. Kuna watu waliozowea kuishi maisha ya kifalme ambao sasa wanalazimishwa kuishi maisha ya kawaida. Hawa watu wakipata upenyo wa kumdhuru Magufuli, hawatosita kufanya hivyo.

Lakini kwa vile ni ‘vigumu mno’ (angalau kwa wakati huu) kufanikisha jaribio la kumdhuru kiongozi huyo, njia nyepesi inaweza kuwa katika ‘kuua character yake,’ ambayo bahati nzuri kwa ‘wabaya wake,’ sio nzuri sana.

Kumekuwa na malalamiko kadhaa hasa kutoka upande wa upinzani kumtuhumu Magufuli kuwa ni dikteta. Na ukifuatilia mwenendo wa siasa zetu kwa muda huu, sio siri kwamba kuna chembe chembe za udikteta. Kwahiyo, ni rahisi kwa ‘wabaya wa Magufuli’ kutumia mwanya huo kujenga picha ya “serikali ya dikteta yamuua mpinzani wake mkubwa.”

Na hilo linatuleta kwenye suala la publicity. Kwamba jaribio la mauaji hayo liwe na mwangwi wa kutosha ndani na nje ya Tanzania. Mwangwi huo ni wa makusudi ili uakisi taswira inayojengeka kuwa ‘Magufuli ni dikteta. Na madikteta hunyanyasa wapinzani wao, na ikibidi hata kuwaua.’

Kwahiyo, kama kuna funzo kubwa kwa Magufuli katika tukio hili ni kuepuka mazingira yaliyopo ya uhasama mkubwa dhidi ya upinzani hususan Chadema. Kiongozi huyo anatambua fika kwamba kuna watu wapo radhi kufanya lolote lile kumng’oa, na kwa vile ‘njia za kawaida’ sio rahisi, basi inakuwa ‘anything goes,’ liwalo na liwe.

Na dhana hii ya tatu inaleta uhusiano kati ya tukio la jana la jaribio la kumuua Lissu na lile la hivi karibuni la kuchomwa moto kwa ofisi za kampuni ya uwakili wa IMMA. Kama hili la Lissu, tukio la moto nalo lilifanyika katika mazingira ya kuvutia publicity, yaani kama kulikuwa na jitihada za makusudi za kuushawishi umma kwamba “mnaona huyu dikteta Magufuli anakoelekea? Sasa anachoma hadi ofisi wa ‘wabaya’ wake.”

Nihitimishe uchambuzi huu kwa kueleza bayana masuala mawili matatu. Kwanza, lengo la uchambuzi huu mfupi sio kuingilia kazi za vyombo vya dola vinavyoendelea na uchunguzi kuhusu jaribio la kumuua Lissu. Nimefanya uchambuzi huu kama mtu mwenye uelewa wa masuala ya intelijensia na siasa za Tanzania yetu, ikiwa ni pamoja na “yanayojiri nyuma ya pazia.”

Pili, lengo la uchambuzi huu sio kumshawishi mtu yeyote abadili mtazamo wake kuhusu “nani ana/wanahusika.”

Mwisho, kama nilivyotanabaisha awali, tasnia ya intelijensia sio sayansi kamilifu kwa asilimia 100 (intelligence is not an exact science). Kwa maana hiyo, japo uchambuzi huu ni karibu kabisa na hali halisi, sio rahisi sana kufikia hali halisi yenye uhakika wa asilimia 100.

Nimalizie kwa kumtakia afya njema Bwana Lissu huku nikiamini kuwa malaka husika zitafanya kila jitihada kuwanasa wahusika, sio tu kwa minajili ya serikali kujinasua bali ili Bwana Lissu atendewe haki.

17 Jul 2017

Kabla ya kuingia kwa kina kwenye uchambuzi huu, ni muhimu kueleza bayana kwamba japo maana, mbinu na ufanisi wa uchambuzi wa kiintelijensia ('intelligence analysis' kwa kimombo) kati ya mie niliyepo hapa Glasgow na afisa mchambuzi wa intelijensia aliyepo Dar zaweza kuwa karibu na sawa, mazingira kati yangu na ya afisa huyo ni tofauti. Tofauti sio kwa vile mie nipo Uingereza na afisa husika yupo Tanzania bali vitu kama shinikizo la kupata majibu upesi na nyenzo mbalimbali kama vile watoa habari, mafaili, nk.


Pili, nitajitahidi kadri nitakavyoweza kuepuka 'mtazamo wangu' na badala yake niongozwe na kanuni za uchambuzi wa kiintelijensia. Hata hivyo, ni muhimu kufahamu kuwa moja ya nyenzo muhimu kwenye intelijensia ni mwanadamu, iwe kwenye kukusanya taarifa za kiintelijensia, kuchambua au kushauri. Kwahiyo, japo nitajitahidi kuepuka 'mtazamo wangu,' siwezi kuepuka ubinadamu wangu kama mchambuzi wa kiintelijensia wa somo husika.


Kwa kifupi, tuanze na tunachofahamu hadi muda huu. Kwa mujibu wa taarifa zilizopo mauaji yanayojumuisha eneo la Mkuranga, Kibiti na Rufiji (MKIRU) yalianza Januari 2015 na hadi sasa yamegharimu uhai wa watu 40 wakiwemo askari polisi 13.


Tukisema tuorodheshe mlolongo wa kauli za viongozi mbalimbali, wa serikali na wa jeshi la polisi, basi huenda itabidi kukesha hapa, au kuandika kitabu kizima. Hata hivyo, kwa kifupi, miongoni mwa kauli hizo ni kama ifuatavyo

Rais John Magufuli

Kwa ujumla, Rais Magufuli ametoa matamko makubwa matatu kuhusu mauaji yanayoendelea katika eneo la MKIRU. Tamko la kwanza ni salamu za rambirambi alizotoa kufuatia mauaji ya askari polisi wanane, ambapo alilaani mauaji hayo. Hiyo ilikuwa April 14 mwaka huu. 


Tamko la pili la Rais lilikuwa  majuzi alipofanya ziara mkoani Pwani ambapo Juni 20 aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa serikali na vyombo vya dola ili kukomesha mauaji hayo. Rais alieleza kuwa watu wanaofanya vitendo hivyo vya mauaji "tunakaa nao, tunawaficha, ni watoto wetu." Kadhalika, Rais Magufuli alieleza kuwa "serikali ya Awamu ya Tano sio ya kuchezewa" na kudai kuwa "(wauaji hao) wameshaanza kunyooka."


Hata hivyo, siku moja baada ya Rais kutoa kauli hiyo ya kutia matumaini, askari polisi wawili waliuawa na gari lao kuchomwa moto, pengine ikiwa ni jibu la wauaji hao kwa Rais aliyedai kuwa "wameshaanza kunyooka."


Tamko la tatu la Rais, na pengine kali kuliko hayo mawili, lilitolewa jana  jijini Dar wakati wa uzinduzi wa upanuzi wa Bandari ya Dar, ambapo katika kilichoonekana bayana kuwa majibu kwa rai ya Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa kwa Rais Magufuli kumtaka atafakari kuhusu 'mashehe wa Uamsho' wanaosota gerezani kwa miaka minne sasa bila kesi yao kuamuliwa.


Katika tamko hilo Rais aliwaomba wanasiasa wanaosema kuwa hawa (mashehe wa Uamsho) wameshikiliwa kwa muda mrefu "wajizuwie midomo yao," na kudai kuwa "hata kuna watu kule Marekani walikaa Guantanamo muda mrefu," na kudai kuwa (wanaoongea kama Lowassa kuwa kesi yao ishughulikiwe) inaweza kuwafanya watu kuhisi (anayesema hivyo) ni "mmoja wao."


Rais Magufuli alihoji "kwanini hata siku moja mtu asijitokeze kualaani wanaouawa bila hatia kule (MKIRU), lakini kwa kutafuta sifa za kisiasa, mtu anatoka anasema watu wako ndani muda mrefu." Rais aliwataka polisi kufanya kazi yao, na kuwaagiza kuwakamata "hao wanaoropoka waisaidie polisi," na "msiogopee sura, awe na mwendo wa haraka, polepole au kukimbia, mkamateni kusudi akaisaidie polisi kule ndani."


Rais alidai pia mtu aliyekamatwa na sare 500 za jeshi zilizokamatwa hivi karibuni "inaonekana anahusiana na walioko ndani (mashehe wa Uamsho)." 


Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri wake  Yusuph Masauni


Kwa nyakati mbalimbali, viongozi hawa wawili wametoa kauli kadhaa kuhusiana na mauaji yanayoendelea huko MKURU. Kuorodhesha kauli zote kwahitaji makala nyingine pekee, lakini kwa kifupi, Waziri Mwigulu ameshanukuliwa akidai kuwa "mauaji hayo yana harufu ya kisiasa," na kuhoji "Ujambazi gani huo wa Wana CCM tu? Hako kamchezo tumeshakagundua. Dhahiri, huo ni ushamba wa vyama vingi.” 


Waziri Mwigulu alikwenda mbali zaidi na kudai kuwa chanzo cha mauaji hayo ni chuki za vyama vya upinzani dhidi ya CCM.


Awali Waziri Mwigulu alieleza Bungeni kuwa serikali imeshabaini kuwa  wanaohusika na mauaji hayo wanatoka maeneo ya Mkuranga, Kibiti na Rufiji, na kwamba changamoto ya mauaji hayo ipo mbioni kutatuliwa.


Kwa upande wake, Naibu Waziri Masauni amenukuliwa akieleza kuwa serikali inalipa kipaumbele suala hilo na lazima mauaji hayo yadhibitiwe. "Tuweze kuharakisha zoezi hili ambalo kwa hakika kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu kwa sisi tunaosimamia haki na uhai wa raia wasio kuwa na hatia hii vita lazima tushinde inshaallah,” alinukuliwa Masauni hivi karibuni.


IGP Sirro na mtangulizi wake IGP Mangu:


Wakati IGP Simon Sirro ameanza jukumu hilo la ukuu wa jeshi la polisi wakati jeshi hilo likikabiliwa na changamoto za mauaji ya MKURU, mtangulizi wake IGP Mangu huenda akakumbukwa zaidi kwa onyo lake la kuwasaka "watu waliofurahia mauaji ya askari wanane," kauli ambayo ilionekana kama 'kusaka adui wa kufikirika.' Hata hivyo, suala hilo aliloongelea IGP Mangu lilipaswa kuibua tafakuri pana na endelevu kuhusu uhusiano mbovu kati ya jeshi la polisi na wananchi. 


Kadhalika IGP Mangu alieleza kuwa jeshi lake lingeanza kutumia nguvu ilizonazo kulazimisha upatikanaji wa taarifa kuhusu mauaji hayo.


Kwa upande wa IGP Sirro, masaa machache tu baada ya kukutana na wazee wa Kibiti na Rufiji kujadiliana nao kuhusu mauaji hayo, mkazi mwingine aliuawa na watu wasiojulikana. Awali, IGP Sirro aliwaeleza waandishi wa habari kuwa "wauaji hao hawatachukuwa muda mrefu kukamatwa" na kwamba "siku zao zinahesabika." Kadhalika, mkuu huyo mpya wa jeshi la polisi alidai kuwa maongezi yake na wazee wa Kibiti na Rufiji yatafanikisha kukamatwa kwa wauaji hao.


Baada ya kuteuliwa wadhifa huo, IGP Sirro alitangaza dau la shilingi milioni 10 kwa yeyote atakayetoa taarifa zitakazowezesha kukamatwa kwa wahusika wa mauaji hayo.


Juni 25 mwaka huu, IGP Sirro alinukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa jeshi lake halifahamu wahusika wa mauaji hayo, kauli iliyokinzana na ya bosi wake, Waziri Mwigulu kwamba chanzo cha mauaji hayo ni chuki ya vyama vya upinzani kwa CCM.

Julai 5 mwaka huu, IGP Sirro alieleza kuwa mauaji hayo ya MKIRO 'yana mkono kutoka nje ya nchi' bila kufafanua nchi gani inayohusika. Kadhalika, taarifa hiyo iliyaeleza mauaji hayo kama yaliyokuwa yakiendelea kwa takriban miaka mwili sasa.


Edward Lowassa: 


Rai ya Lowassa kwa Rais Magufuli kuhusu hatma ya 'mashehe wa Uamsho' nimeitaja hapo juu, lakini kwa urefu, habari hiyo ipo HAPA.


Zitto Kabwe


Kufuatia kilichotafsiriwa kama majibu ya Rais Magufuli kwa Lowassa, kiongozi mkuu wa chama cha upinzani cha ACT- Wazalendo Zitto Kabwe alitoa maoni yake katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook. 


 Uchambuzi wa kiintelijensia

Hadi muda huu, hakuna kikundi kilichojitokeza hadharani kudai kuhusika na mauji hayo. Hata hivyo, bila hata kuhitaji uzoefu wa kishushushu, sio vigumu kuhisi kuwa 


1. Mauaji hayo yanafanywa na kikundi maalum
2. Wahusika ni watu wenye uelewa/uzoefu wa mbinu za mauaji 

Hata hivyo, licha ya kutojitokeza kikundi chochote kudai kuhusika na mauaji hayo, taarifa zilizopatikana siku chache zilizopita zilieleza kwamba kuna ujumbe uliotumwa na 'wahusika wa mauaji hayo,' unaosomeka kama ifuatavyo
Tunawatangazia wananchi tumewaua hawa kwa sababu wanadhulumu watu kwa kutumia kazi zao na yeyote atakayefanya kazi hapa au nje ya hapa tutamtafuta hadi nyumbani kwake. 

Sisi tumejitolea kufa kuliko kuishi, kwa hiyo dereva au raia popote uwaonapo toa taarifa iwe nyumbani au kazini.

Hakuna njia ya kumaliza dhuluma isipokuwa chuma tu, hapa chuma tuuu!
Kwa mujibu wa taarifa, ujumbe huo uliandikwa kwa kalamu na kisha kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Turudi nyuma kidogo hadi mwaka 2013 ambapo kulitokea uhasama mkubwa kati ya Polisi na baadhi ya wakazi wa Kibiti kufuatia kifo cha mkazi mmoja wa eneo hilo, Athuman Hamis aliyefariki kutokana na majeraha aliyoyapata kutokana na kipigo cha polisi (kwa mujibu wa maelezo ya wakazi hao).

Habari kamili ipo HAPA


Katika kufanya uchambuzi wa kiintelijensia wa suala kama hilo la mauaji hayo ya MKIRU, yahitajika vitu viwili. Kwanza, kuwa na maelezo sahihi kuhusu tatizo husika, na pili, matokeo tarajiwa zaidi ni yapi.

Katika uchambuzi wa mauaji hayo ya MKIRU, ninatumia moja ya njia za uchambuzi wa kiintelijensia, inayojulikana kama ACH - Analysis of Competing Hypotheses - yaani Uchambuzi wa Dhana Zinazoshindana.

Hatua ya kwanza ni kutambua dhana husika. Ili kupata dhana hizo, niliendesha kura ya maoni isiyo ya kisayansi kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Vipengele vinne vilivuounda swali husika vilitokana na maelezo mbalimbali yaliyokwishatolewa kuhusu zinazoweza kuwa sababu za mauaji huko MKIRU

Kama inavyoonekana katika 'tweet' hiyo yenye matokeo ya kura ya maoni, dhana kuu nne ni 
  1. Ugaidi
  2. Chuki za kisiasa
  3. Chuki za wananchi dhidi ya Jeshi la Polisi
  4. Uhalifu kama mwingine
Kuorodhesha dhana hizo (kama ilivyo hapo juu) na kuzipitia kwa kina zaidi na kujumuisha 'ushahidi uliopo' kwa kila moja (kama inavyofuata hapa chini) ni hatua ya pili ya ACH.

Tuanze na dhana kuwa mauaji hayo yanatokana na chuki za wananchi. 'Ushahidi' kuhusu dhana hii ni wa aina mbili. Kwanza, Januari 23, 2013, kulijitokeza vurugu kubwa huko Kibiti zilizolazimu jeshi la polisi kutumia helikopta kuzidhibiti. Vurugu hizo zilitokana na kifo cha mkazi mmoja wa Kibiti aliyefariki Hospitali ya Taifa Muhimbili alikopelekwa kutibiwa majeraha ambayo ilidaiwa aliyapata kutokana na kupigwa na polisi.

Vurugu hizo zilipelekea Barabara ya Kilwa kufungwa kwa zaidi ya amsaa matatu, na hivyo kuathiri usafiri kwenda mikoa ya Mtwara na Lindi; sambamba na wananchi kuvamia kituo kimoja cha polisi na kuchoma moto nyumba moja ya polisi.


'Ushahidi' wa pili wa dhana kuwa chanzo cha mauaji ya MKIRU ni chuki za wananchi dhidi ya jeshi la Polisi ni ripoti maalum ya kiuchunguzi ya Gazeti la Mwananchi iliyochapishwa Mei 26 mwaka huu. 

Kwa kifupi, ripoti hiyo inaeleza kwamba wengi wa wakazi wa MKIRU ni masikini wenye elimu duni, na tegemeo lao kubwa la kipato ni kuvuna raslimali nyingi zilizopo eneo hilo na kuzuza. Biashara kubwa ambayo vijana wanajihusisha nayo ni uchomaji na uuzaji wa mkaa, uvunaji magogo kwa ajili ya mbao, uuzaji wa kuni na mazao mengine ya mashambani kama vile mpunga na mihogo, imeajiri vijana wengi katika maeneo hayo.

Hata hivyo, kwa mujibu wa ripoti hiyo, kumekuwa na unyanyasaji mkubwa unaofnywa na mamlaka za mitaa, maofisa wa Idara ya Maliasili, jeshi la mgambo na polisi. 

Licha ya mamlaka husika kuweka lundo la vizuizi, pia wananchi hao walilalamikia 'kodi za kukomoana.' Kwa miaka mingi sasa, wananchi wamekuwa wakilalamikia vizuizi hiyo kuwa kitovu cha dhuluma na uonevu mkubwa wanaofanyiwa wananchi na wasimamizi wa vizuizi ambao wamekuwa wakikadiria kodi za kukomoa, kutaifisha magunia ya mkaa na mbao na mali nyingine za wananchi.

Wananchi hao wanadai kuwa  uonevu na dhuluma  vimechokoza hasira za vijana wengi, ambao "kazi zao ndio mkaa, kuni na mbao au mihogo." Kuhusu matumizi ya silaha, ilielezwa kuwa  vijana wengi katika maeoeneo hayo  wana mafunzo ya mgambo na JKT huku wakiwa hawana ajira nyingine zaidi ya kutegemea biashara hizo.

“Si suala la kidini. Ni manyanyaso tu. Leo unadhulumu watano, kesho kumi, hawa wakiji-organise unatarajia nini?” aliuliza mkazi mmoja wa eneo hilo, na kuongeza kuwa ingawa dhehebu moja la kidini lina vijana wengi lakini halina uhusiano na mauaji.
Kuhusu dhana nyingine kwamba mauaji ya MKIRU yantokana na ugaidi, kuna 'ushahidi' wa matukio mbalimbali kwa takriban miaka mitano sasa ambayo japo serikali imekuwa ikiyaita kuwa ni ujambazi, yana viashiria vya ugaidi.
Moja ya vitu vinavyoleta ugumu katika kutanabaisha ugaidi au lani kasumba iliyoshamiri kitambo ambapo baadhi ya wanasiasa wamekuwa wepesi kuwatuhumu wapinzani wao wa kisiasa kuwa wanapanga au wanajihusisha na vitendo vya kigaidi kwa minajili tu ya uhasama wa kisiasa.
Baadhi ya wanasiasa wa chama tawala CCM, kwa nyakati tofauti wamewahi kuvituhumu vyama vya upinzani vya CUF na Chadema, na baadhi ya viongozi na wanachama wake, kuwa wahusika wa ugaidi, tuhuma ambazo mara zote hazikuweza kuthibitishwa.
Japo magaidi hupendelea wafahamike kuwa ndio wahusika wa tukio la kigaidi, kunapojitokeza watu wasio na hatia kutuhumiwa kuwa ndio magaidi, hiyo inaweza kurahisisha kazi ya magaidi halisi.
Katika mlolongo wa matukio mbalimbali yenye viashiria vya ugaidi, Julai 2 mwaka huu, Rais Magufuli aligusia kuhusu 'mashehe wa UAMSHO' ambao wapo gerezani kwa zaidi ya miaka minne sasa wakisubiri hatma ya mashtaka ya ugaidi yanayowakabili. Katika hotuba yake jijini Dar, Rais Magufuli aliashiria kuwa kuna uhusiano katika ya mauaji ya MKIRU na mashehe hao wa UAMSHO, huku akiibua taarifa mpya kuwa hata sare 500 za jeshi zilizokamatwa jijini Dar zilikuwa na uhusiano na mashehe hao/ 'ugaidi' huko MKIRU.

Kadhalika, Julai 5 mwaka huu, IGP Sirro alinukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa mauaji ya MKIRU yana 'mkono wa nchi za nje.' Kingine cha muhimu katika maelezo ya IGP Sirro ni kubainisha kuwa mauaji ya MKIRU yamekuwa yakiendelea kwa zaidi ya miaka miwili.

Tukio jingine ni pamoja na lile la Mei mwaka jana huko Mwanza ambapo kulitokea mapambano makali kati ya askari wa jeshi la polisi wakisaidiwa na wenzao wa Jeshi la Wananchi dhidi ya kilichoelezwa na serikali kuwa ni genge la majambazi. Mapambano hayo yalielezwa kuwa na uhusiano na uvamizi kwenye msikiti wa Rahman jijini humo, ambapo kulitokea mauaji ya kutisha baada ya watu wasiofahamika kuvamia msikiti huo na kuwauwa kwa kuwachinja  Imamu aliyekuwa akiswalisha swala ya Isha, Ferouz Elias (27) na waumini wawili, Mbwana Rajab na Khamis Mponda.
[​IMG]
Tukio jingine lilitokea Novemba 22 mwaka jana ambapo Jeshi la Polisi lilikamatwa wanawake wanne na watoto wannewaliodaiwa kuwa katika mafunzo ya kigaidi, huko Vikindu, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam


Tukio jingine ni lile la Machi 2 mwaka juzi ambalo lililozua taharuki miongoni mwa Watanzania wengi kufuatia kuibuka kwa video yenye ujumbe ulioashiria uwepo wa kundi linalopambana na jeshi la polisi kwa sababu za kidini


Kadhalika, Juni mwaka 2015, taasisi ya ACLED ilitoa taarifa iliyoonyesha kulikuwa na ongezeko la matukio yenye viashiria vya ugaidi. Ripoti hiyo iliyoambatana na majedwali yanayoonyeshwa mwenendo wa matukio hayo ilitokana na taarifa mbalimbali katika vyombo vya habari vya Tanzania.
Figure 1 Number of Conflict Events & Fatalities in Tanzania, from June 1, 2014 - May 25, 2015

Taarifa hiyo ambayo unaweza kuisoma HAPA ilibainisha kwamba Tanzania ina vikundi vidogo vya kigaidi vyenye uhusiano na kundi la Al-Shabaab la Somalia au Al-Hijra la Kenya. Vikundi hivyo ni pamoja na Ansar Muslim Youth Centre cha mjini Tanga.

Pia, Novemba mwaka 2013, Jeshi la Polisi lilifanikiwa kuwakamata watu 69 waliokuwa kwenye kilichoelezwa kuwa ni mafunzo ya kigaidi kuhusu kundi la Al-Shabaab. 

Vilevile, takriban mwezi mmoja kabla ya tukio hilo, watu  wengine 11 walikamatwa na Polisi mjini Mtwara wakituhumiwa kujihusisha na kundi la Al-Shabaab.

Kadhalika, mwezi huohuo,  mfanyabishara Juma Abdallah Heri alikamatwa na polisi kwa tuhuma za kufadhili vikundi vya kigaidi nchini Tanzania.

Mwendelezo wa matukio hayo ni pamoja na lile la April mwaka jana ambapo zilipatikana taarifa kuwa Mtanzania Issa James Mwesiga aliuawa na kundi la Al-Shabaab nchini Somalia kwa tuhuma za ujasusi. Inaelezwa kuwa Mtanzania huyo alijiunga na kundi hilo la kigaidi mwaka 2013.


Agosti 2015, Watanzania sita walikamatwa huko Garissa, nchini Kenya wakiwa njiani kuelekea Somalia kujiunga na kundi la Al-Shabaab. Walikutwa na mabomu saba na bastola saba.


Awali, Machi mwaka huohuo, mwanamke mmoja, Ummur Kayr Sadir, alikamatwa na wenzie wawili wakiwa safarini kwenda Somalia kujiunga na kundi hilo la kigaidi.

Septemba mwaka jana, taasisi ya Intergovernmental Authority on Development (IGAD) ilitoa ripoti iliyoeleza kuwa kundi la Al-Shabaab lilikuwa ikifanya jitihada kubwa kupata wafuasi wa kiume na kike wa kujiunga na kundi hilo, hata nje ya Somalia (lilipo kundi hilo) na Tanzania, Uganda, Ethiopia na Djibouti zilikuwa zilikilengwa katika jithada hizo.

Februari 28 mwaka jana, watu watatu waliuawa na polisi jijini Arusha, huku taarifa zikieleza kuwa watu hao walikuwa wanakikundi wa Al-Shabaab.

Juni mwaka jana, watu wanane waliuawa kinyama huko Tanga, ikiwa ni wiki mbili tu baada ya tukio jingine la kinyama jijini Mwanza ambapo Imamu wa msikiti wa Rahman na waumini wawili walichinjwa.

Oktoba mwaka jana, polisi walimkamata mwalimu mmoja wa madrasa huko Bagamoyo kufuatia taarifa za wananchi kwa polisi. Mwalimu huyo alikamatwa akiwa na watoto 22 ambapo polisi pia walikuta maandiko mbalimbali ya kuhusu ugaidi na walikuta bomu la gesi nyumbani kwa mwalimu huyo.

Mei mwaka jana, kikundi kilichojitambulisha kama Ahl Kalf Mujahidina kilitoa wito kwa Waislam kuwa wajiunge nacho, ambapo kilieleza kuwa kimeweka makazi yake kwenye mapango ya Amboni huko Tanga. 


April mwaka jana zilipatikana taarifa za kuundwa kwa kundi jipya la kigaidi linalofahamika kama Jahba East Africa ambalo lilijitangaza kuwa wafuasi wa kundi hatari la kigaidi la ISIS. Kadhalika kundi hilo lilidai kuwa miongoni mwa wafuasi wa filisofia yake wapo nchini Tanzania.

 

Kwahiyo hadi hapa, tumeshaona dhana mbili na 'ushahidi' wake, na sasa tumalizie na dhana mbili zilizosalia. Dhana nyingine ni kwamba mauaji hayo ya MKIRU yanayokana na chuki za kisiasa. 'Ushahidi' pakee katika dhana hii ni kauli ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba, kwamba mauaji hayo 'yananuka siasa.'

Na dhana ya nne na ya mwisho ni kwamba mauaji hayo ni matukio ya uhalifu kama matukio mengine. 'Ushahidi' kuhusu dhana hiyo ni ukweli kwamba takwimu za uhalifu nchini Tanzania kwa mwaka 2013 na 2014  na 2015 zinaonyesha mauaji kama kosa kubwa la pili kwa ukubwa (wingi) nyuma ya ubakaji katika kundi la makosa dhidi ya binadamu.

Hatua ya tatu ya ACH inahusisha kuandaa 'matrix' yenye dhana husika, kwa minajili ya kupima 'consistency' au inconsistency.' Pia kuna fursa ya kupima kuaminika na kulandana kwa kila dhana. 



Hatua ya nne ya ACH inahusisha kuangalia 'diagnosticity' - uwezekano wa dhana kuwa sahihi. Kadhalika katika hatua hii, dhana yenye/zenye mapungufu - kwa maana ya kwamba hazijitshelezi kueleza somo linalochunguzwa - yaweza/zaweza kuondolewa. Na katika somo hili la mauaji ya MKIRU, nimefikia hitimisho la kuondoa dhana mbili za 'mwisho' (nitaeleza maana ya 'mwisho' mbeleni) yaani "chuki za kisiasa" na "mauaji hayo ni uhalifu kama mwingine." Kwahiyo ninabakiwa na dhana mbili, yaani "ugaidi" na "hasira za wananchi."

Hatua ya tano ya ACH inatokana na hatua ya nne na imenipelekea kuwa na matrix yenye dhana mbili, ya ugaidi na hasira za wananchi.



Hatu ya saba ya ACH ni kuripoti matokeo ya uchambuzi. Najua hayo majedwali ya matrix yanaweza kumchanganya msomaji lakini nyenzo muhimu kufikia hitimisho la karibu zaidi na ukweli. Ikumbukwe kuwa intelijensia sio sayansi timilifu kwa asilimia 100 - kwa kimombo wanasema "intelligence is not exact science." Kwahiyo, dhana, ushahidi wake, na msaada mkubwa wa ACH unanipeleka kufikia hitimisho lifuatalo.

1. Kumekuwa na harakati za muda mrefu za kusambaza na hatimaye kuimarisha ugaidi nchini Tanzania. Katika uchambuzi huu, ushahidi uliotumika umeanzia mwaka 2013, miaka minne iliyopita. Hata hivyo, jitihada hizo za kusambaza/kuimarisha ugaidi zimekuwa kama za kulipuka na kufifia (sporadic), japo kama tukiamini kuwa mauaji ya MKURU ni sehemu ya harakati hizo, basi hitimisho linakuwa kwamba harakati hizo zimefanikiwa kujikita.

2. Chuki ya wakazi wa maeneo husika zinasaidia kufanikisha harakati hizo za magaidi hao. Katika matrix ya pili iliyobakiwa na dhana mbili badala ya nne za awali, kuna 'consistency' katika 'uhusiano' wa dhana ya ugaidi na chuki ya wananchi. Pengine hili limechangiwa na mamlaka husika kutofanyia kazi vilio vya wakazi wa eneo hilo (rejea taarifa ya kiuchunguzi ya Gazeti la Mwananchi kuhusu maujai ya MKIRU).

3. Kauli ya IGP kuwa mauaji hayo yana mkono wa kutoka nje inapewa uzito na matukio mbalimbali yaliyotumika katika uchambuzi huu. Na  katika hitimisho langu, natafsiri kuwa mauaji yanayoendelea katika maeneo ya Mkuranga, Kibiti na Rufiji ni ugaidi unaofanywa na kundi lenye asili ya nje ya Tanzania lakini lenye ufuasi wa kutosha nchini humo, na linapatiwa msaada na wakazi wa eneo hilo.

4. Kuhusu 'mashehe wa UAMHO,' hakuna ushahidi wa moja kwa moja kuthibitisha kauli ya Rais Magufuli hivi karibuni iliyoashiria kuwa kuna uhusiano kati sare za jeshi zilizokamatwa hivi karibuni, mashehe wa UAMSHO na mauaji ya MKIRU. Kinachowezekana ni wahusika (magaidi) wanaweza kutumia suala la mashehe hao kama sababu ya kufanya ugaidi wao. 

5. Tukiafikiana kuwa mauaji ya MKIRU yanafanywa na magaidi, na tukiafikiana pia kuwa magaidi hao wanaweza kutumia suala la 'mashehe wa UAMSHO' kama moja ya sababu zao, bado ni muhimu kuepuka kulifanya suala hilo kuwa linatokana na masuala ya kidini. Kama ambavyo kuna wanasiasa wanaotumia mauaji hayo kuendeleza chuki za kisiasa na hatusemi siasa ndio chanzo cha mauaji hayo, ndivyo ilivyo kwa wanaoweza kutumia dini kama kisingizio cha kufanya ugaidi. Hili ni muhimu sana kuzingatiwa kwa sababu asilimia kubwa ya wakazi wa MKIRU ni Waislamu, na kuhusisha ugaidi huo na Uislamu/Waislamu sio tu itaathiri uwezekano wowote wa ushirikiano baina ya wakazi wa eneo hilo na vyombo vya dola/serikali bali pia inaweza kuzua balaa la machafuko ya kidini.

6. Tukiafikiana kuwa kinachoendelea huko MKIRU ni ugaidi basi itabidi pia tuafikiane kuwa mapambano dhidi ya ugaidi yanahitaji uwekezaji mkubwa kweli intelijensia kuliko matumizi ya nguvu. Taarifa kwamba baadhi ya wakazi wa maeneo ya MKIRU wamelazimika kuhama makazi yao kwa "kuhofia vipigo kutoka kwa Polisi" zinafanya uwezekano wa kupata ufumbuzi kuwa mgumu. 

7. Kwa wanaofahamu vema pwani ya mkoa wa Pwani sambamba na jiografia yake na mikoa ya jirani watatambua kuwa wingi wa "vipenyo" (ambavyo hadi hivi karibuni vilikuwa vikitumika kama 'njia za panya' kuingiza na kutoa bidhaa mbalimbali) na mtawanyiko wa makazi yaliyochanganyika na mashamba, mapori na misitu, vinaweza kuwa mazingira mwafaka kwa watu hao wenye nia mbaya. 

Nihitimishe uchambuzi huu kwa kusisitiza kuwa intelijensia sio exact science. Nimejitahidi kadri nilivyoweza kuongozwa na ACH kufikia hitimisho husika. Lengo la kufanya uchambuzi huu sio kuonyesha mapungufu ya mtu au taasisi fulani. Nimekuwa nikitumia ACH kwa majukumu yangu binafsi, na nimeona sio vibaya kuitumia kwenye suala hili la MKIRU. Hakuna anayelazimishwa kuafikiana na uchambuzi huu.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.