Showing posts with label EDWARD LOWASSA. Show all posts
Showing posts with label EDWARD LOWASSA. Show all posts

8 Jul 2015

Ufuatao ni waraka kutoka kwa Chama cha DP kinachoongozwa na Mchungaji Christopher Mtikila kumpiga mwania nia ya Urais Edward Lowassa

KATIKA UCHAGUZI MKUU HUU
TUSIRUHUSU MAFISADI WALICHEZEE TAIFA
Edward Lowasa ni balaa kwa Taifa!

Democratic Party (DP) inatarajia kufikisha Mahakamani chama cha
CCM pamoja na wanachama wake sita, Edward Lowasa na wengine,
kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Tanzania, kwa kosa kubwa sana la kuvunja Katiba na Sheria za Nchi kwa kuanza kampeni ya Uchaguzi kabla ya wakati unaopasa kwa mujibu wa Sheria.

1. Tunao ushahidi mzito unaothibitisha kwamba Edward Lowasa na
wenzake walianza kampeni ya urais ndani ya chama chao kabla ya
wakati, na kwamba chama chao kiliwapa adhabu ya kutofanya siasa
kwa miezi 12. Lakini safari hii Lowasa ameanza kampeni ya urais
Arusha kwa mkutano mkubwa sana wa hadhara wa kampeni haramu
na kumwaga rushwa ya kutisha!

2. Kama ni wadhamini alipaswa kuwapata katika ofisi za chama chake, katika mikoa nane (8) tu Tanganyika na mikoa miwili tu Unguja na Pemba, wadhamini 45 tu katika kila mkoa. Lakini Edward Lowasa amefanya mikutano nchi nzima, ya kuwaahidi maelfu ya wananchi katika kila mkutano wa hadhara, mambo atakayofanya kama wakimpa kura zao awe Rais! Hii ndiyo kampeni halisi, ambayo ni ukiukaji wa Katiba na Sheria za Nchi! Uchaguzi Mkuu unaendeshwa na Sheria, hivyo ni lazima Sheria ichukue mkondo wake dhidi yake kwa kuivunja.

3. Edward Lowasa amevunja Katiba ya Nchi na Sheria ya kiwango cha
fedha kinachoruhusiwa kutumika katika shughuli halali za Uchaguzi,
kiasi kwamba CCM na Taasisi zote za uchunguzi wa kifedha nchini,
upelelezi wa Jinai na Usalama wa Taifa ni mlazima wanayo kazi muhimu sana ya kupata ukweli kuhusu haya mabilioni ya fedha yanayomwagwa nchini na fisadi Edward Lowasa, ameyapata wapi na kwa namna gani, kumehusika ‘’Money laundering’ au la, kama mapato ya mapesa hayo yote ni halali, na kama mapato hayo yote yalilipiwa kodi inayopasa kwa ajili ya Taifa.

Ni marufuku kabisa tena ni makufuru Edward Lowasa kuruhusiwa
kugombea urais, kwa sababu amevunja Katiba ya Nchi na Sheria na
Kanuni za Uchaguzi. Sifa mojawapo ya kustahili kugombea uongozi wa nchi yoyote ni maadili mema na uzingatiaji wa Sheria, Kanuni na
taratibu za Utawala wa Sheria
4. Edward Lowasa, kwa kujimilikisha maeneo nchi nzima kwa kutumia kifisadi Uwaziri wake wa Ardhi, ameliweka Taifa katika hatari kubwa ya mmwagiko wa damu baina ya wakulima na wafugaji, baada ya kueneza nchi nzima makundi ya ng’ombe wake, na kusababisha mapigano makali ya mara kwa mara kila mahali nchini kati ya wafugaji wake na wakulima. Kwa sababu ya uovu huu hata katika kampeni yake haramu Lowasa ameshindwa kusema lolote juu ya kilimo, ingawa ndio uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu na ndiyo shughuli inayotunza uhai wa asilimia 95 ya wananchi!

Kwa kuwaingilia wakulima katika ardhi yao, kuwaua ovyo, kuwaonea
kiasi cha kufisha matumaini yao katika kilimo, kumeifanya kauli mbiu ya “Kilimo kwanza” kuwa porojo tu ya kisanii!

5. Edward Lowasa ni mwiko kabisa kupewa kugombea urais, kwa
sababu siyo tu aliutumia kifisadi Uwaziri wa Ardhi akajitajirisha na
kujipatia maeneo makubwa ya ardhi nchini kote, bali alitumia kifisadi
zaidi uwaziri wa nchi katika ofisi ya Waziri Mkuu, katika uagizaji wa
mashangingi ya Wabunge, mawaziri, wakuu wa Mikoa na Wilaya.

6. Edward Lowasa alikemewa mnamo mwaka 1995 na Mwalimu Nyerere anayeenziwa na CCM lama “Baba” yao, alipotaka kugombea urais, kwa sababu alikuwa fisadi papa, wala hakuweza kujitetea kwavile utapeli wote aliojitajirishia ulikuwa mezani. Leo baada ya mabiashara haramu mengi na kulipora sana Taifa kukiwa ni pamoja na utapeli wa “kununua mvua Thailand” na kuliibia Taifa mabilioni ya fedha kwa kutumia kampuni hewa ya RICHMOND, huyu ni fisadi-nyangumi. Ni mlemavu wa rushwa tu wa kununuliwa na mapesa machafu anayomwaga Lowasa, anayeweza kumruhusu fisadi Edward Lowasa agombee urais.

Sifa za mtu wa kukugombea Urais zimeelezwa bayana na Mwenyezi
Mungu katika Kumbukumbu la Torati 17:15-20, ambazo Edward
Lowasa hana hata mojawapo! Lowasa awali alikemewa na Mwalimu
Nyerere ambaye CCM wanamuenzi kama “Baba” yao, kuwa hafai kabisa kuwania urais, kwa sababu alikuwa fisadi papa, kama alivyomtangaza hata Reginald Mengi pale alipolazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu kwa ajili ya wizi kwa kampuni hewa ya Richmond, lakini leo akiwa fisadi la kutisha zaidi kuliko papa eti anataka urais!
Si ajabu kwamba magabacholi yalioipora vibaya sana Nchi hii kama Sigh Setti na hata Nazir Karamagi wote wamo katika genge la Edward
Lowasa! Si ajabu hata fisadi Reginald Mengi leo kuungana na fisadi
Lowasa yakizingatiwa machafu yake yeye mwenyewe, na kuhusika kwa Mengi na mauaji ya Chacha Wangwe, pamoja na mpango wa Chadema
wa kumwua Mchungaji Mtikila, waraka feki wa kujaribu kuupotosha
ukweli ukatangazwa kwa ITV yake.

Katika uwaziri wake katika ofisi ya Waziri Mkuu, na katika Uwaziri wakewa Ardhi na Uwaziri Mkuu, Lowasa alifanya ufisadi ambao katika nchi kama China zenye uchungu na maslahi ya mataifa yao angekuwa wa kupigwa risasi hadharani, lakini katika nchi yetu anatafuta urais!

7. Edward Lowasa AFYA yake imempiga marufuku kugombea Urais!
Kwa ajili ya kila ajira duniasni kote, moja ya mashart makuu ni lazima mwombaji awe na afya iliyo bora, ndiyo sababu ni lazima ajira ya kila mwombaji itegemee taarifa ya kitaalamu ya madaktari, inayothibitisha kwamba hana dosari kiafya. Sharti hili ni la lazima kwa sababu:
a. Majukumu yote atakayopewa mwajiriwa atayatekeleza kikamilifu
kwa kutumia viungo vya mwili wake, kwahiyo viungo vyake vyote
ni lazima viwe katika hali iliyo imara kwa ajili ya kazi.

b. Hata kama kwa uthibitisho wa kitaalamu wa madaktari mwajiriwa
anazo akili nzuri kichwani mwake, akiwa na hitilafu katika viungo
vingine vya mwili wake huathiri afya ya akili zake na uwezo wa
utendaji wa akili zake.

c. Kazi ya Rais ni ngumu sana, kwa sababu ni pamoja na kusimamia
shughuli zote za maendeleo ya nchi nzima, na matatizo yote
yanayowatokea wananchi wote kila walipo, na kusimamia
utekelezaji wa majukumu yote ya watendaji wote katika Taifa,
hivyo kwamba maamuzi sahihi yanatokana na afya bora yenye
kuhakikisha uwezo unaopasa wa kiakili wakati wote

d. Hitilafu katika afya hudhoofisha uwezo wa kifikira na kusababisha
maamuzi mabovu, ambayo huleta athari mbaya sana kwa Taifa. Na
udhaifu huo huathiri mpaka maadili na hata uzalendo wa huyo
kiongozi mdhaifu. Kwa mfano akipatikana Rais anayeishi kwa
matumaini, kwa hofu ya kupoteza uhai kabla hajaweka sawa
mambo yake na ya familia na jamii yake atatumikia maslahi yake
zaidi kuliko Taifa, tatizo hilo la afya likawa limelikosesha Taifa
kipaumbele, na kuliangamiza kimaendeleo!
e. Wanaowania kugombea urais ni lazima wachunguzwe kwa makini
sana afya zao, kwa sababu kukifanyika makosa akatawazwa
mwenye hitilafu za kiafya, atakwenda kuwa mzigo mzito sana kwa
Taifa, hususan ugharamiaji wa utunzaji wa uhai wake ndani na nje
ya nchi, kukosekana na umakini anaopasa kuwa nao kwa ajili ya
dhamana kubwa aliyopewa n.k.

Kutokana na AFYA yake kuwa dhaifu sana hata kwa kumwona kwa
macho tu, kabla ya uchunguzi wa kitaalamu ni kwamba Edward Lowasa hawezi kabisa kugombea Urais. Kwani amekosa sifa muhimu sana ya afya bora, ambayo ni ya lazima kwa mtu yeyote anayestahili kupewa dhamana kubwa sana ya kuliongoza Taifa. Pengine hata kugombea urais kwenyewe anatafuta kutokana na hitilafu ya kiafya, iliyosababisha udhaifu katika kufanya maamuzi, hivyo amejikuta kwa bahati mbaya anagombea asichokiweza kabisa.

Ni lazima wagombea wote wa Urais, wa Ubunge na hata wa Udiwani
wachunguzwe kwa makini afya zao kabla ya kupewa kugombea, na hata kuchunguzwa tena katikati ya muhula wa utumishi wao, kama kweli tunalithamini na kuliheshimu Taifa.

Sifa za urais ni wito au uhanga kwa ajili ya Nchi ambao ni zaidi ya
maadili ya kizalendo, maono, vipawa na AFYA BORA. Ni dhana potofu
sana kwamba sifa ya urais ni kushabikiwa na umati wa watu! Kwa
sababu wengi hufuata mapesa na husombwa hata na magari ili umati
wa kishabiki tu upatikane. Lakini kumpenda mtu huwa lazima kuwe na sababu, wakati ushabiki ni pepo mchafu au ‘psychological deficiency’.





5 Jun 2015


Tafsiri: CEORT ina furaha kuwa mwenyeji wa mdahalo wa kwanza katika historia ya Tanzania kwa wanaowania urais. Tutaweka uchumi kuwa mada kuu ya mdahalo huo mwaka huu, na sio watu (wagombea) au rangi za vyama. Sumaye, Balozi Amina Salum Ali, January Makamba, Bernard Membe na Samule Sitta watakuwa wa kwanza kutangaza vipaumbele vyao kisera kwa taifa katika shughuli hiyo. Cha kusikitisha, EDWARD LOWASSA amekataa kushiriki. Ungana nasi hoteli ya Hyatt (jijini Dar es Salaam) Jumatatu ijayo saa 2 asubuhi.Midahalo mingine miwili na watangaza nia wengine ikiwajumuisha wanasiasa wa upinzani itafuata.

Huyu LOWASSA ndiye anayehamasisha mchakmchaka wa maendeleo? Ni rahisi sana kuwahadaa watu kwa kuwahubiria porojo lakini yahitaji ujasiri na uwezo wa kiongozi kushirikia mdahalo wa kuwashawishi Watanzania kwanini unafaa kuwaongoza


Tunahitaji Rais mpinga ufisadi si wa kujitetea eti yeye si fisadi

HATIMAYE baada ya taarifa za muda mrefu zisizo rasmi, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, alitangaza mwishoni mwa wiki iliyopita dhamira yake kukiomba Cchama Cha Mapinduzi (CCM) kimpitishe kuwa mgombea wa kiti cha urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.

Taarifa za Lowassa kutaka urais zimekuwa zikivuma kwa muda mrefu mno, na kwa hakika haikuwa jambo la kushangaza alipoamua majuzi kuzibadili taarifa au tetesi hizo kuwa jambo kamili.

Binafsi, baada ya kuisikia hotuba yake aliyoitoa jijini Arusha mbele ya halaiki ya wananchi nimebaki na swali moja la msingi: Lowassa ana kipi hasa cha kuwafanya Watanzania waamini kaulimbiu yake ya ‘safari ya matumaini.’
Sijui kwenu wasomaji wapendwa, lakini kwangu kubwa linalonifanya nimkumbuke Lowassa ni kashfa ya Richmond ambayo hatimaye ilisababisha ajiuzulu wadhifa wake wa Uwaziri Mkuu.

Na kwa sababu anazojua yeye mwenyewe, hotuba yake ya Arusha haikugusia suala hilo ambalo awali alipozungumza na waandishi wa habari alidai angeliongelea kwa kirefu. Tayari kuna baadhi yetu tunaoanza kuhoji uwezo wa mwanasiasa huyo kushika nafasi nyeti ya urais, na swali ni hili: kama ndani ya wiki moja anaweza kuahidi kuzungumzia kashfa ya Richmond na kisha asizungumzie, je mustakabali wa taifa letu utakuwaje mikononi mwa mtu anayeweza kuvunja ahadi anazojiwekea mwenyewe?

Pengine katika hatua hii ni muhimu nitanabaishe kuwa sina tatizo na Lowassa kutumia haki yake ya kikatiba na kidemokrasia kuwania urais. Hiyo ni haki ya kila Mtanzania mwenye sifa stahili. Lakini kwa hakika natatizwa sana na uadilifu wake.

Licha ya suala la Richmond, ambalo amedai yeye hahusiki, kuna hoja ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ‘kumwekea vikwazo’ huko nyuma katika nia yake ya urais, ambapo inaelezwa kuwa Nyerere alitatizwa na utajiri mkubwa wa mwanasiasa huyo usio na maelezo ya kuridhisha.

Na majuzi Lowassa katamka bayana kuwa anauchukia umasikini. Na amekiri kuwa yeye ni ‘tajiri kiasi.’ Lakini pengine Watanzania wengi wangependa sana kufahamu chanzo cha utajiri wake kwa sababu sote tunajua mtu haamki tu na kujikuta tajiri. Sawa, amekuwa mtumishi wa umma kwa muda mrefu, lakini kwa jinsi anavyomudu ‘kumwaga pesa’ katika shughuli mbalimbali, ni vigumu kuamini kuwa chanzo cha fedha hizo ni utumishi wake wa muda mrefu serikalini pekee.

Nyakati kadhaa amekuwa akitueleza kuwa kuna marafiki zake wanaomchangia fedha ‘anazomwaga’ katika hafla mbalimbali. Je, ni marafiki gani hao? Lakini kubwa zaidi, vyanzo vya utajiri wao ni vipi hasa?

Kadhalika, mwanasiasa huyo ameonekana kuzungukwa na wanasiasa wenzake kadhaa ambapo miongoni mwao ni majeruhi wa skandali mbalimbali za ufisadi. Waingereza wana msemo, nionyeshe marafiki zako, nami nitakueleza wewe ni nani’ (show me your friends and I will tell who you are). Hivi Lowassa anaweza kutueleza lolote kuhusu ukaribu alionao na watu hao?

Kwa upande mwingine, mie nilipoisikiliza kwa makini hotuba yake ya majuzi huko Arusha niliona kama ninamsikiliza mtu ambaye tayari ameshapitishwa na chama chake kugombea urais na kilichobaki ni taratibu tu za kumkabidhi wadhifa huo. Sina tatizo na kujiamini kwake lakini kuna wanaojiuliza, hivi huyu mtu asipopitishwa na chama chake itakuwaje?

Kuhusu kaulimbiu yake ya ‘safari ya matumaini,’ bahati nzuri siku moja tu baada ya kuitangaza, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willbroad Slaa, akawafumbua macho Watanzania kwa kuwaeleza kuwa kinachohitajika sio safari ya matumaini bali ya uhakika. Watanzania wamekuwa wakiishi kwa matumaini kwa muda mrefu sana; matumaini kwamba siku moja nchi yao itaondokana na umasikini ilionao na kuishi kulingana na utajiri lukuki iliyojaliwa nao; matumaini ya kuondokana na janga la ufisadi linalozidi kuota mizizi; matumaini ya kuona sarafu yao ikiacha kuporomoka kwa kasi; matumaini ya mgawo wa umeme wa kudumu kufikia kikomo; matumaini ya maisha bora kwa kila Mtanzania waliyoahidiwa miaka 10 iliyopita na timu ya uchaguzi ya Rais Jakaya Kikwete ambayo ilikuwa ikiongozwa na Lowassa, na matumaini mengine kadha wa kadha

Hapana, Watanzania wanaotaka safari ya uhakika, kama alivyosema Dk. Slaa, na sio ya matumaini hewa kama yaliyoahidiwa miaka kumi iliyopita na yamebaki kuwa historia tu.

Awali, Lowassa alidai kuwa moja ya vipaumbele vyake vikuu ni elimu, na kuleta kaulimbiu nyingine ya elimu kwanza. Labda kabla ya yeye kuiponda kaulimbiu ya kilimo kwanza angewaambia Watanzania kwa nini imebaki kuwa porojo tu lakini hiyo yake itatekelezwa kwa vitendo.

Pengine atazungumzia uanzishwaji wa shule za kata. Tukiweka kando matatizo kadhaa yanayozikabili shule hizo, maarufu kama ‘Santa Kayumba,’ ni muhimu Watanzania wenzangu kutambua kuwa hazikujengwa kutoka hela za mfukoni mwa Lowassa. Ninaelewa kwa nini mwanasiasa huyo anaweza kutaka kujichukulia pointi kwenye suala hilo; kasumba iliyojengeka miongoni mwetu kwamba mtu akiajiriwa kutimiza wajibu fulani na analipwa kutimiza wajibu huo anaonekana mchapakazi. Yaani tumefika mahala kuwa inatarajiwa mtu akipewa majukumu atafanya ubabaishaji, Kwa hiyo yule atakayefanya kinyume cha kuwajibika, basi inakuwa kama miujiza.

Sidhani kama Lowassa ana moja la kuwaeleza wananchi kuwa hili nililifanya kwa jitihada zangu kama Edward na sio Waziri Mkuu niliyekuwa ninalipwa mshahara kutimiza wajibu huo.

Tukirejea kwenye hotuba yake, binafsi sikusikia jambo lolote geni ambalo hatulifahamu. Sote tunajua kuhusu umasikini wetu, sote tunafahamu kuhusu matatizo yote aliyoyataja katika hotuba yake. Na kwenye tatizo la foleni za magari jijini Dar es Salaam amnbazo amedai atazimaliza ndani ya miezi 12, niseme tu kuwa hiyo ni porojo.

Kwanza, kwani alipokuwa Waziri Mkuu huko nyuma tatizo hilo halikuwepo hadi hakuona haja ya kulitatua? Pili, foleni sio tatizo jijini Dar es Salaam tu bali hata kwenye majiji makubwa ya Ulaya na katika mabara mengine. Kwetu linakuwa tatizo sugu zaidi kutokana na miundombinu mibovu na idadi kubwa ya uhamiaji mijini isiyoendana na wahamiaji, sambamba na wingi wa magari yakiwemo yasiyostahili kuwepo barabarani.

Amejitahidi kutueleza matatizo ambayo kila mmoja wetu anayafahamu. Hata hivyo kama ilivyo kwa maradhi, suala sio tu tabibu kuelezea mgonjwa anakabiliwa na tatizo gani la kiafya bali kumwelekeza tiba na hatimaye kumpatia tiba husika. Wanasiasa wetu hawaishiwi umahiri wa kuyajua matatizo ya wananchi, hata kama wanasiasa hao hawajawahi kukumbana na matatizo hayo ‘ana kwa ana.’ Sawa, ili kuweza kulitatua tatizo ni lazima kujua chanzo chake, lakini haina manufaa kutaja tu matatizo tuliyonayo pasi kuyaeleza yametokana na nini au jinsi gani tunaweza kuyakabili.

Nikiri kwamba nilipata hasira kumsikia Lowassa akiwaimbia wananchi kuhusu ‘mchakamchaka wa maendeleo’ bila kuwaambia maendeleo hayo yataletwa vipi, na kwa nini miaka zaidi ya 50 tangu tupate Uhuru (na Lowassa akiwa mtendaji wa serikali katika miaka kadhaa katika hiyo) bado tunasuasua kimaendeleo.

Nimalizie makala hii kwa kurejea nilichoandika hapo awali kuwa Lowassa ana haki kikatiba kuwania urais. Hata hivyo, name kama Mtanzania pia nina haki ya kuelezea bayana kuwa mwanasiasa huyu hafai kuwa rais wetu ajaye, sababu kubwa zaidi ikiwa ni suala la ufisadi wa Richmond.

Hatuhitaji mgombea wa urais ambaye badala ya kutueleza jinsi ya kukabiliana na moja ya matatizo makubwa kabisa yanayoikabili Tanzania, yaani ufisadi, anatumia muda mwingine kujitetea kuwa yeye sio fisadi.


Wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni huu: tunastahili kilicho bora. Haiingii akilini kabisa kuamini kuwa mtu aliyelazimika kujiuzulu kwa kashfa ya ufisadi akiwa Waziri Mkuu, atakuwa kiongozi bora akishika urais. Ni muhimu kufumbua macho na masikio na kuacha kuamini hizo porojo ambazo tumekuwa tukizisikia miaka nenda rudi lakini Tanzania yetu inazidi kudidimia.

21 May 2015

WAZIRI mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, ameanza kuwaandaa wafuasi wake kwa uwezekano wa kujiunga na mojawapo ya vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Raia Mwema limeelezwa.

Taarifa ambazo gazeti hili limezipata kutoka katika kambi ya mgombea huyo zinaeleza kuwa amepiga marufuku mazungumzo yoyote ya kutafuta mbadala wake ndani ya CCM na kutaka nguvu yote ielekezwe kwake.

Gazeti hili limeelezwa kuwa wapo watu walio ndani ya kambi yake wanaoamini kwamba anahitajika mwanasiasa mwingine ndani ya kundi hilo ambaye anaweza kuvaa viatu vya Lowassa endapo CCM itaamua kumkata au kuendeleza adhabu yake ya kutofanya shughuli za siasa aliyopewa na chama chake.

Hata hivyo, kundi hilo linadaiwa kuwa na wakati mgumu kwa madai kwamba Lowassa hataki kusikia chochote kuhusu suala hilo.

“Anasema yeye ndiyo Plan A, Plan B na Plan C. Kama, kwa sababu yoyote ile, CCM itaamua kumpitisha mgombea mwingine na si yeye, yuko tayari kujiunga na Ukawa lakini si kubaki ndani ya chama.

“Hili ndilo jambo linalotusumbua sana kwa sasa. Hakuna vita ambayo ina mpango mmoja tu. Lazima muwe na mpango zaidi ya mmoja. Huku Pwani wanasema ukienda kuteka maji wakati wa ukame, ni muhimu uwe na ndoo na kidumu cha kushika mkononi.

“Kwenye kutembea na ndoo mtu unaweza kujikwaa na maji yote yakamwagika na kile kidumu cha mkononi ndiyo kikakuokoa. Sasa huyu bwana hataki kusikia habari ya kidumu.
“Anataka twende kutafuta maji na ndoo moja tu ambayo ni yeye. Hili linatupa shida kidogo kwa sasa,” alisema mbunge mmoja wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye ni mtu wa karibu na mtarajiwa huyo.

Katika kambi ya Lowassa, kuna majina ya wanasiasa vijana ambao wanatajwa kuwa tayari kuvaa viatu vyake endapo CCM itaamua tofauti na matarajio yao.

Miongoni mwa wanasiasa wanaotajwa kuwa katika kambi ya Lowassa na ambao kambi inayotaka Plan B inawapendekeza ni Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi, Mbunge wa Sengerema William Ngeleja, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba.

Miongoni mwa wanaotajwa, Dk. Nchimbi anaelezwa kuwa na nguvu zaidi kutokana na ukweli kwamba ndiyo mwenye ushawishi zaidi ndani ya chama kutokana na ukweli kuwa amekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kwa zaidi ya miaka 10.

Kimsingi, kwa upande wa Tanzania Bara, hakuna mwana CCM aliyedumu katika Kamati Kuu ya chama hicho kwa muda mrefu kuliko Nchimbi miongoni mwa waliomo sasa, ukimwondoa Rais Jakaya Kikwete.


Anasema Mbunge huyo: “ Tunajaribu kumshawishi Lowassa akubali kuwa akikosa yeye, basi apatikane mtu ambaye ataweza kuyafanya yale aliyopanga kuyafanya kupitia CCM. Kwa sasa, hili hajakubaliana nalo,” kilisema chanzo hicho cha gazeti hili ambacho hakikutaka kuwekwa jina lake wazi.

Hata hivyo, kwa vile Ukawa si chama cha siasa, kama Lowassa ataamua kuhama CCM, ni lazima ajiunge na mojawapo ya vyama vinavyounda Ukawa ambavyo ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), NCCR-Mageuzi, Chama cha Wananchi (CUF) na National League (NLD).

Akizungumzia taarifa hizo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alisema kwa sasa hawataki kujihusisha na mambo ya ndani ya CCM na badala yake wanaangalia namna ya kukishinda kwenye Uchaguzi Mkuu ujao.

“Sisi sasa hivi lengo letu kubwa ni kuijenga Ukawa kitaasisi na kuifanya iwe tishio katika Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika baadaye mwaka huu.

“Kamanda, sitaki kuzungumza kama tutampokea au hatutampokea Lowassa kama akiamua kuhamia Ukawa. Mambo ya CCM waachie CCM wenyewe. Mimi nakuhakikishia kuwa wakati wa uchaguzi ukifika; CCM wamweke Lowassa, au Membe, sijui Makongoro Nyerere ama yeyote mwingine, Ukawa itashinda tu kwenye uchaguzi huo,” alisema Mbowe kwa kujiamini.

Juhudi za kuwapata wenyeviti wenza wengine wa Ukawa, Profesa Ibrahim Lipumba, James Mbatia na Emmanuel Makaidi hazikufanikiwa hadi tunakwenda mitamboni juzi Jumatatu.

Kwa sasa, Lowassa na wanasiasa wengine watano ndani ya CCM wako katika kifungo cha muda usiojulikana walichowekewa na chama chao kutokana na madai ya kukiuka taratibu za chama hicho.

Wanasiasa wengine walio katika kifungo hicho ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira; Waziri wa Mambo ya Nje, Benard Membe; Ngeleja na waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye.

Ilivyokuwa chaguzi mbili zilizopita
Taarifa hizi za uwezekano wa Lowassa kuhamia Ukawa hazitofautiani na zile zilizoibuka mwaka 2005 wakati ilipodaiwa kuwa Kikwete angehamia Chadema endapo CCM isingempitisha.

Wakati huo, zilikuwapo taarifa kuwa CCM ilikuwa na mpango wa kumwondoa Kikwete kwenye kinyang’anyiro hicho kutokana na kutokidhi vigezo vya kimaadili vya chama hicho.
Hata hivyo, Kikwete hatimaye alipitishwa na chama chake kuwania urais na kushinda kwa kishindo.

Katika Uchaguzi Mkuu uliopita wa mwaka 2010, baadhi ya wanachama wa CCM walitajwa kutaka kujiunga na Chama cha Jamii (CCJ) na mmoja wao, Fred Mpendazoe, aliachia ubunge wake kabla ya wakati ili kuanza kazi ya kukijenga chama hicho.

Wakati huo, CCJ ilidaiwa kuwa na mkono wa wana CCM waliokuwa wakipinga kukithiri kwa ufisadi ndani ya chama hicho.

Miongoni mwa majina mazito yaliyokuwa yakihusishwa na kujiunga na CCM yalikuwa ni Samuel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe.

CHANZO: Raia Mwema

WAKATI HUOHUO,

BALOZI wa kudumu wa Umoja wa Afrika (AU), huko Marekani, Mtanzania Amina Salum Ali, ametangaza  kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, 2015.

[aminaali.jpg]
Balozi Amina ametangaza uamuzi wake huo mapema leo  jijini Dar es Salaam.

Itakumbukwa ya kuwa Balozi Amina ambaye alidumu kwa muda mrefu kama waziri kwenye serikali ya Rais mstaafu wa Zanzibar, Dkt. Salmin Amour Juma, almaarufu kama (Komandoo), aliwahi kutupa karata yake kuwania urais wa Zanzibar, kabla ya kujitoa.

Huyu anakuwa mwana mama wa kwanza kwenye historia ya chama cha Mapinduzi CCM, kutangaza kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Hali kadhalika, Balozi Amina rekodi yake ya kwanza ni kuwa mwanamke wa kwanza kuwa balozi wa kudumu wa AU huko Marekani.

Mbali na kuwahi kuwa waziri, Balozi aAmina ndiyo muasisi wa taasisi ya Zanzibar Women Welfare Trust, inayojishughulisha na kupambana na afya ya akina mama na watoto hususan kwenye eneo la maambukizi ya VVU.



28 Nov 2013


MAKALA hii ni mwendelezo wa ile iliyochapishwa katika toleo lililopita la gazeti hili, iliyobeba kichwa cha habari ‘Nani kinara wa CCM urais 2015?’
Lakini kabla sijaingia kiundani, nadhani ni vema nikarejea nilichoandika katika makala iliyopita kuhusu kukua kwa uwezekano wa CCM kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu ujao. Wiki iliyopita ilishuhudia chama kikuu cha upinzani cha CHADEMA, kikiingia katika mtafaruku mkubwa ambao licha ya kutishia uhai wake unazidi ‘kupapalia’ mazingira mwafaka ya ushindi kwa CCM.
Awali, CHADEMA ilitangaza kuwavua madaraka viongozi wake waandamizi watatu, Zitto Kabwe, Dk. Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba na kuwapa siku 14 kujieleza kwa nini wasivuliwe uanachama baada ya kupatikana kwa nyaraka inayodaiwa kulenga kukihujumu chama hicho.
Jumapili iliyopita, Zitto na Kitila waliitisha mkutano na waandishi wa habari ambao kimsingi haikusaidia japo kupunguza moto unaozidi ‘kuunguza nyumba ya CHADEMA.’ Kwa kifupi, wanasiasa hao wawili walipinga vikali shutuma zilizoelekezwa kwao na kuhalalisha kile kilichotafsiriwa na uongozi wa chama hicho kama hujuma, huku wao wakibainisha kama matumizi ya demokrasia kwa minajili ya kuiboresha CHADEMA.
Pasi haja ya kuingia kwa undani katika sokomoko hilo, ni wazi kwamba uamuzi wa kuwavua madaraka viongozi hao na msimamo uliotolewa na ‘wahanga’ hao unaendeleza mapambano ya madaraka ndani ya CHADEMA. Kubaki au kuondoka kwa akina Zitto hakuwezi kukirejesha chama hicho katika mahala kilipokuwa. Kibaya zaidi, japo hakuna tathmini yoyote iliyokwishafanywa kuhusu athari za mgogoro huo, ni wazi Watanzania wengi wameanza kupoteza matumaini kwa chama hicho kilichotarajiwa sio tu kutoa upinzani mkubwa kwa CCM bali pia hata kuweza kuingia Ikulu mwaka 2015.
Nihitimishe suala hili la CHADEMA kwa kutanabaisha kuwa japo inafahamika kuwa lolote linawezekana katika siasa, ukweli kwamba tumebakiwa na takriban mwaka na ushee tu kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao, sambamba na ukweli kuwa hakuna dalili ya mgogoro huo wa CHADEMA kumalizika hivi karibuni, itakuwa vigumu mno kwa chama hicho kujipanga upya na vyema, kuweza kutoa ushindani wa maana katika Uchaguzi Mkuu ujao. Nitaijadili kwa kirefu hatma ya CHADEMA katika makala zijazo.
Tukiendelea na mada ya urais kwa tiketi ya CCM, niliahidi kuwa wiki hii nitajadili ‘odds’ (uwezekano wa kufanikiwa au la) zinazowakabili wanasiasa wawili ambao tathmini yangu inawaona kama ndio vinara katika mbio za kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete kupitia CCM, yaani Edward Lowassa na Bernard Membe.
Pengine hadi siku chache zilizopita, kikwazo kikubwa kwa wote wawili kingeweza kuwa uwezekano wa CCM kubwagwa na CHADEMA katika Uchaguzi Mkuu ujao. Lakini kwa kuzingatia mwenendo ulivyo katika chama hicho kikuu cha upinzani, yayumkinika kuhitimisha kuwa kikwazo hicho ni kama kimekufa kifo cha asili.
Kwa upande wa Lowassa, doa kubwa linaloonekana kuendelea ‘kuchafua’ jina na wasifu wake ni tuhuma za ufisadi wa Richmond. Bila kujali kuwa uamuzi wake wa kujiuzulu uwaziri mkuu kufuatia kashfa hiyo ni ‘kutolewa kafara’ au ‘alivuna alichopanda,’ tafsiri ya haraka kwa wananchi wengi wa kawaida inabaki kuwa ‘ni vigumu kumtenganisha mwanasiasa huyo na moja ya matatizo makubwa kabisa yanayoikabili nchi yetu, yaani ufisadi.’
Ukweli kwamba Tanzania yetu sio tu ni moja ya nchi masikini sana bali pia inazidi kuwa masikini huku ufisadi ukizidi kushamiri, umesababisha kujengeka kwa hisia (pengine zisizopendeza) kuwa kila mwenye uwezo wa kifedha ni fisadi. Hisia hizo hazimsaidii Lowassa ambaye kwa siku za hivi karibuni amekuwa mstari wa mbele katika harambee za kuchangisha mamilioni ya fedha hususan kwenye taasisi za dini. Badala ya ukarimu wake kumjenga kama kiongozi anayejali, kuna wanaotafsiri jitihada zake hizo kama ‘rushwa’ ya kutaka urais mwaka 2015.
Kadhalika, kuna hisia hasi kuwa hata hizo fedha anazotoa kusaidia miradi mbalimbali ‘ni chafu’ kwa maana ya hisia kuwa huenda ni zile zilizotokana na tuhuma za ufisadi. Kibaya zaidi, kutofahamika chanzo cha kinachotajwa kama utajiri mkubwa wa mwanasiasa huyo kunaimarisha hisia hizo za ufisadi.
Vile vile, na hili linawagusa wote-Lowassa na Membe- ukweli kwamba wanasiasa hao wanatajwa kama sehemu muhimu ya ‘mtandao’ uliomwingiza madarakani Rais Kikwete mwaka 2005, unaleta hisia za ‘mvinyo mpya kwenye chupa ya zamani’ (kwa wasiofahamu, thamani ya mvinyo inaelemea sana kwenye ‘ukale’ wake na si upya wake)
Sasa, kama tukiafikiana kuwa mtizamo wa Watanzania wengi ni kuwa utawala wa Kikwete (ambao uliingizwa madarakani na ‘mtandao’ uliowashirikisha Lowassa na Membe) umetawaliwa zaidi na tuhuma za ufisadi huku hali ya maisha ya Mtanzania ikizidi kuwa ngumu, kwa nini basi watu hao wapewe fursa ya kuboronga mambo zaidi?
Faraja kubwa kwa Lowassa (na hata Membe kwa ‘uhusika wake katika mtandao) kuhusu tuhuma za ufisadi ni ukweli mchungu kuwa Watanzania ni wepesi kusahau ‘mabaya.’ Wanasiasa wetu wengi wanafahamu kuhusu udhaifu huo ambao kwa kiasi kikubwa umewasaidia wengi kuendelea kuwapo madarakani licha ya ‘madudu’ yao.
Iwapo ‘kete ya fedha’ niliyobainisha katika makala iliyopita kuwa inamsaidia sana Lowassa itaendelea kutumika, basi kuna uwezekano mkubwa wa mwendelezo wa ‘who cares?’ (nani anajali?) ambapo mahitaji ya muda mfupi kama vile sukari, khanga, mchele na mengine kama hayo yatafunika mahitaji ya muda mrefu kama vile kuondokana na umasikini sambamba, kupambana na ufisadi, na hatma ya taifa letu kwa ujumla.
Kwa upande wa Membe, kikwazo kikubwa kwake ni kutokuwa maarufu ndani na nje ya CCM. Na ukubwa wa kikwazo hicho unatokana na ukweli kwamba ‘mpinzani’ wake, yaani Lowassa, ni mwanasiasa maarufu kuliko wote ndani ya CCM hivi sasa (bila kujali umaarufu huo ni stahili au la). ‘Wajuzi wa mambo’ wanaeleza kuwa inahisiwa Lowassa anaungwa mkono na zaidi ya asilimia 75 ya viongozi wa chama wenye uwezo wa kufanya uamuzi, huku wengi wao wakiwa watu waliofanyiwa fadhila zilizosababisha wawepo madarakani hivi sasa.
Tegemeo pekee kwa Membe dhidi ya Lowassa ni lile nililogusia katika makala iliyopita; nafasi ya Idara ya Usalama wa Taifa katika kumpata mgombea urais ajaye (ndani ya CCM). Kama kuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Lowassa kuingia Ikulu, na pengine kumsaidia Membe kupata fursa hiyo, ni pale Idara hiyo itakapoamua ‘kumbeba mwenzao’ (Membe ni shushushu mstaafu). Na hilo si gumu kama inavyoweza kudhaniwa. Moja ya maeneo ambayo mashushushu wetu wanayomudu sana ni hujuma (sabotage) na uzandiki (subversion).
Ni hivi, kwa vile tayari kuna hisia za ‘uchafu’ kuhusu Lowassa (yaani tuhuma za ufisadi) basi haitokuwa vigumu kwa mashushushu kuzikuza na kuziendeleza katika namna ya kile kinachofahamika kama character assassination. Lakini kwa vile Lowassa bado yupo katika ‘himaya’ ya Idara ya Usalama wa Taifa (kama waziri mkuu wa zamani, anapatiwa huduma za ulinzi na Idara hiyo) ni rahisi kwa mashushushu kuibua mengi (ya kweli au hata ya kutunga) dhidi yake, iwapo wataona haja ya kufanya hivyo.
Kwa hiyo, kwa kifupi, kufanikiwa kwa Membe kutategemea kukwama kwa Lowassa. Na pengine katika hatua hii, ni vema nikitanabaisha waziwazi kuwa mwana-CCM anayeongoza katika kinyang’anyiro hicho ni Lowassa akifuatiwa kwa karibu kiasi na Membe.
Nihitimishe makala hii kwa kueleza kuwa mada hii ni endelevu, kwa maana ya kuwa nitaendelea na uchambuzi na mjadala huu kadri tunavyoelekea Uchaguzi Mkuu ujao. Hata hivyo, ninapenda kurejea tena mtizamo wangu kuwa CCM kurejea tena madarakani mwaka 2015 ni janga kwa Watanzania. Chama hicho tawala sio tu kimeishiwa na kila mbinu ya kuongoza nchi lakini pia hakipo kwa ajili ya maslahi ya Watanzania. Na kama uchambuzi huu ulivyoonyesha kuwa uwezekano mkubwa wa aidha Lowassa au Membe kuwa mgombea kwa tiketi ya chama hicho ni kwa aidha fedha au ‘sanaa za giza’, yeyote kati yao atakapopata urais hatokuwa tofauti na utawala uliopo madarakani hivi sasa ambao nao ulitumia mbinu ya ‘mtandao.’
Kwa bahati mbaya au makusudi, watu tuliodhani wangeweza kutusaidia kuiondoa CCM madarakani, yaani CHADEMA, wanaonekana kuwa ‘bize’ kupigana ngwala kugombea madaraka ndani ya chama chao. Sasa kama zoezi dogo tu la kupata uongozi wa chama linasababisha ‘watiane vidole machoni’ kwenye uongozi wa nchi itakuwaje? Ni ukweli mchungu lakini usioepukika na hivyo ni vema kujiandaa kisaikolojia kuendelea kuwa chini ya utawala wa CCM (ninatamani kuwa na suluhisho mbadala lakini sijalipata hadi muda huu)

Soma zaidi kuhusu:

- See more at: http://raiamwema.co.tz/nani-kinara-wa-ccm-urais-wa-2015-ii#sthash.RAQui2j5.dpuf

24 Nov 2013


KAMA nilivyoahidi katika makala yangu ndani ya toleo lililopita la gazeti hili maridhawa, wiki hii nitafanya uchambuzi kuhusu kinyang’anyiro cha kumpata mgombea urais kwa tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu ujao, mwaka 2015.
Kwa wanaofuatilia safu hii, niliwahi kugusia mada hii katika toleo la Oktoba 26, 2011 ikibeba kichwa cha habari “Mizengwe na mitego ya mgombea urais kutoka CCM.” Mengi yametokea kati ya wakati huo na sasa, na kwa vile Uchaguzi Mkuu unazidi kujongea, nimeona ni muhimu kurejea tena mada hii.
Pengine msomaji unaweza kubaini mabadiliko kidogo katika mtizamo wangu kuhusu uwezekano wa CCM kung’oka madarakani 2015. Ninaomba kukiri kwamba chokochoko zisizo na msingi zinazoendelea ndani ya chama kikuu cha upinzani (na tegemeo la wengi kuiondoa CCM madarakani, CHADEMA, zinanifanya nikubaliane na ukweli mchungu kuwa fursa za chama tawala kushinda tena katika uchaguzi mkuu ujao zinazidi kuongezeka.
Na moja ya mambo ya kusikitisha zaidi kuhusu CHADEMA ni kuibuka kwa kundi la ‘wahuni wa kisiasa’ waliojipachika joho la uanaharakati. Kwa wababaishaji hao, kuanza kukubalika kwa chama hicho kumetoa fursa kwao kufahamika kwa namna moja au nyingine. Ni tatizo lilelile sugu katika jamii yetu la kusaka umaarufu hata kwa mambo ya kipuuzi, Waingereza wanasema ‘famous for nothing.
Sasa ‘wahuni’ hawa wamebinafsisha ajenda ya CHADEMA kupambana na ufisadi na kujipa hakimiliki kuwa wao pekee ndio wenye uelewa na mbinu za kukiwezesha chama hicho kufanikisha ajenda hiyo. Pasi kujali madhara ya uhuni wao kwa hatma ya chama hicho, wamejikuta wakitumiwa na maadui wa CHADEMA kwa njia isiyo ya moja kwa moja - kwa ‘remote control.’
Lakini kuashiria kuwa chama hicho kina wakati mgumu japo uongozi wake wa juu unaendeleza porojo za “njama za CCM na Usalama wa Taifa,” imefika mahala Mwenyekiti wa chama hicho ngazi ya mkoa anabandika tuhuma nzito dhidi ya Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, kwenye blogu yake. Hivi pamoja na madudu ya CCM unatarajia ‘utoto’ wa aina hiyo?
Tuelekee huko CCM sasa. Kwanza ninaomba kuweka bayana kuwa uchambuzi huu umeelemea katika uelewa wangu wa siasa za huko nyumbani, maongezi yangu na watu walio karibu na siasa hizo, na taarifa mbalimbali katika vyombo vya habari (vya ‘asili’ na vya ‘kisasa’)
Kwa mtizamo wangu, hadi muda huu wanasiasa wawili wanaoongoza katika kinyang’anyiro cha kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete hapo 2015 ni aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa na Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Kwa ‘pembeni’ kidogo kuna Waziri Mkuu wa zamani Frederick Sumaye na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samuel Sitta. Kimsingi, majina mengine yanayosikika kama William Ngeleja, John Magufuli na wengineo ni ya ‘kuchangamsha gumzo’ zaidi kuliko kuwa na uzito wowote wa maana.
Pengine baadhi ya wasomaji wangetamani nisiandike hivi lakini kimsingi hauepukiki, kama mazingira yatabaki kama yalivyo muda huu (constant) ni vigumu kwa mwanasiasa yeyote yule ndani na nje ya CCM kumzuia Lowassa kuwa rais mwaka 2015. Ninaomba nikiri kuwa ninatamani isiwe hivyo (kwa sababu binafsi ninaamini kuwa hafai kuwa Rais) lakini ukweli una tabia moja: kuuchukia hakuufanyi uwe uongo.
Turufu kubwa ya Lowassa ni uwezo wake mkubwa wa kifedha japo mwenyewe amekuwa akikanusha na kudai kuwa mamilioni anayoyamwaga katika harambee mbalimbali ni michango ya rafiki zake (hajawahi kuwataja wala kutueleza vyanzo vya utajiri wao).
Inaelezwa pia kuwa mwanasiasa huyo amejijenga mno ndani ya CCM kiasi cha kuwa sahihi kuhitimisha kuwa ana nguvu zaidi ya Mwenyekiti wa Taifa, Kikwete.
Sasa, huhitaji japo kozi ya muda mfupi ya siasa za nchi yetu kufahamu kuwa katika zama hizi fedha ndio nyenzo muhimu zaidi ya kumwezesha mwanasiasa kushinda uchaguzi kuliko kitu chochote kile. Mpigakura mwenye njaa hana habari na sera ya chama bali anachofikiria ni pishi ya mchele, doti ya khanga au kilo ya sukari.
Kwa upande wa Membe, turufu zake muhimu zaidi ni tatu. Kwanza, nafasi yake kama Waziri wa Nje inamweka karibu sana na Rais Kikwete kwani wanasafiri pamoja takriban katika kila ziara ya Rais nje ya nchi. Huhitaji kuwa mdadisi kufahamu kuwa watu wanaosafiri pamoja kwa miaka 10 mfululizo wana ukaribu kiasi gani.
Pili, kuna taarifa zisizo rasmi kuwa Membe anaungwa mkono na familia ya Kikwete. Katika moja ya mahojiano, mmoja wa watoto wa Kikwete, Ridhiwani, alikiri bayana kuwa anadhani Membe anaweza na anafaa kuwa Rais. Siasa za kifamilia zinaweza kubadilika lakini kwa angalau kwa sasa hali ipo hivyo.
Tatu, na kwangu hii ndio turufu muhimu zaidi, Membe ni ‘shushushu mstaafu.’ Pengine ni vigumu kuelezea kwa undani umuhimu wa kigezo hiki, lakini kwa kifupi, ni vigumu sana kwa mwanasiasa kuingia Ikulu pasi kuungwa mkono na Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi husika (angalau katika ‘demokrasia changa’). Mashushushu, kama watumishi wengine wa vyombo vya dola, wana tabia moja ya kumuunga mkono ‘mwenzao.’
Lakini sambamba na hilo ni kile kinachofahamika kama ‘sanaa za giza’ (dark arts), yaani kwa lugha ya kawaida, zile mbinu zinazosababisha kura kuyeyuka katika mazingira ya ajabu. Tukiamini kuwa mashushushu watamuunga mkono Membe, kwa nini basi wasiende mbali zaidi kuhakikisha kuwa anashinda kwa ‘gharama yoyote’ (na ‘gharama’ hapa si lazima iwe fedha)?
Kwa hiyo licha ya uwezo mkubwa wa kifedha wa Lowassa (tukiweka kando kukanusha kwake kuwa yeye si tajiri), Membe anaweza kumshinda kwa mbinu (ambazo kwa mtizamo wangu zinaweza kuhusisha watumishi wa sasa na wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa)
Kuhusu Sitta, nafsi yangu inanituma kuamini kuwa haitokuwa jambo la kushangaza endapo miezi michache kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 tukakutana na kichwa cha habari kama hiki “Sitta: Lowassa ni chaguo la Mungu.” Kwa nini nina hisi hivyo? Binafsi ninamwona kama mwanasiasa asiyeaminika, anayeendeshwa na siasa za kusaka umaarufu na hata ‘rahisi kutulizwa.’ Kwa kifupi, Sitta anaendeshwa zaidi na imani (kuwa anaweza kuwa rais) kuliko uhalisia.
Kwa Sumaye, japo pengine ni mapema mno ‘kumpuuza,’ nafasi pekee ya yeye kuwa rais ni nje ya CCM. Tatizo kubwa kwa mwanasiasa huyu ni kwamba lugha anayoongea haieleweki ndani ya chama hicho. Naam, amejitokeza kuwa msemaji wa wanyonge na mkemeaji mkubwa wa ufisadi lakini sote tunafahamu kuwa hiyo sio sera ya CCM (angalau kwa vitendo na si kauli za majukwaani).
Nafasi hairuhusu kuangalia ‘odds’ dhidi ya Lowassa na Membe (ninataraji kufanya hivyo katika matoleo yajayo), lakini muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii nilishiriki katika mjadala mzito kuhusu hatma ya Tanzania yetu hususan jinsi ya kuzuia uwezekano wa kumpata Rais atakayetokana na rushwa. Pia tulijadili tatizo la rushwa na namna ya kulimaliza.
Kwa bahati nzuri, mjadala huo uliofanyika katika mtandao wa kijamii wa Twitter ulimvutia mwanasiasa kijana na Mbunge wa Tanzania kwenye Bunge la Afrika Mashariki, Abdullah Mwinyi. Kwa kifupi, alitueleza kiini cha tatizo la rushwa, na nini kinaweza kufanyika kupambana na tatizo hilo sugu. Bila kuingia undani kuhusu mjadala huo, ulipofikia tamati takriban kila mshiriki alikiri kuwa “kumbe CCM bado ina hazina zaidi ya hayo majina tunayoyasikia kila siku.”
Je, wanasiasa kama Abdullah, mtoto wa Rais wa Awamu ya Pili Mzee Ali Hassan Mwinyi wanaweza kuwa chaguo mbadala (alternative choice) hasa ikizingatiwa kuwa hawana ‘mawaa’ kama ya Lowassa au Membe (nitayajadili mbeleni)?
Nihitimishe makala yangu kwa kusisitiza jambo moja: japo kwa jinsi hali ilivyo ni muhimu kujiandaa kisaikolojia kuiona CCM ikiendelea kuwa madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu ujao, bado kuna umuhimu mkubwa kwa chama hicho kikongwe kupumzishwa kwani kimeshindwa kazi.
Si Lowassa, Membe, Sitta au Sumaye anayeweza kuibadili CCM irejee misingi aliyoasisi Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Tegemeo dogo katika chama hicho ni damu mpya kama za akina Abdulla Mwinyi, japo pengine ni mapema mno kuhitimisha hilo.
ITAENDELEA...


- See more at: http://raiamwema.co.tz/nani-kinara-wa-ccm-urais-wa-2015#sthash.fO09a0nd.dpuf

2 Jun 2012

 
AKIRI TATIZO LA AJIRA KWA VIJANA KUWA BOMU, ASEMA LISIPOTATULIWA LITALETA MACHAFUKO BARANI AFRIKA

Peter Saramba na Mussa Juma, Arusha
RAIS Jakaya Kikwete amekiri kuwa ukosefu wa ajira kwa vijana ni tatizo kubwa na kwamba lisipotafutiwa ufumbuzi wa kudumu linaweza kusababisha vurugu, machafuko na uasi wa umma, hata kwa nchi zinaoongozwa kwa misingi ya kidemokrasia, kama inavyotokea sasa katika nchi za Kiarabu.

Onyo hilo la Rais Kikwete linafanana na lile ambalo limekuwa likitolewa mara kwa mara na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, lakini, linapingana na kauli ya Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka ambaye Machi 21 mwaka huu, alimjibu Lowassa akisema, "Kitendo cha wanasiasa kuendelea kusema tatizo la ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka, siyo kweli."

Jana akifungua mkutano wa mwaka wa Magavana wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) Jijini Arusha, Rais Kikwete alisema moja ya sababu kuu ya machafuko yanayoshuhudiwa sasa kwenye ukanda wa nchi za Kiarabu, ni matokeo ya ukosefu wa ajira kwa vijana na watu kukata tamaa.

“Siyo kweli kwamba machafuko yanayoshuhudiwa kwenye nchi za Kiarabu ni matokeo ya Serikali za nchi hizo kukaa madarakani kwa kipindi kirefu kama wengi wanavyodhani. Ukweli ni kwamba hayo ni matokeo ya ukosefu wa ajira na watu kukata tamaa ya maisha,” alisema Rais Kikwete.

Alisema bila kutafutia ufumbuzi wa haraka, tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana ambao wengi hukimbilia mijini kusaka hali bora ya maisha, hata nchi zenye kuongozwa kidemokrasia, zinaweza kukumbwa na machafuko na uasi wa umma.

Rais alitumia fursa hiyo kuishukuru Denmark kwa kutoa fedha za kusaidia Mfuko wa Ajira kwa Vijana barani Afika, akisema ni moja ya mapendekezo kadhaa yaliyotolewa na kamati maalum ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya kiuchumi barani Afrika ambayo yeye na Rais wa AfDB, Dk Donald Kaberuka, walikuwa wajumbe.

Mapema Rais wa Ivory Coast, Allasane Ouattara aliyehudhuria mkutano huo aliunga mkono kauli hiyo ya Rais Kikwete kwa kusisitiza kuwa vijana lazima wawekewe mazingira mazuri na kuwezeshwa kukabiliana na kumudu changamoto za kiuchumi, kitamaduni na kiteknolojia wanazokabiliana nazo.

“Lazima wasaidiwe na wawekewe mazingira bora ya kupata fursa za ajira na kujiajiri, bila kufanya hivyo ni kukaribisha matatizo na machafuko yanayotokana na ongezeko la mahitaji na kukata tamaa katika miji yetu inayokua kila kukicha kutokana na ongezeko la vijana wanaosaka ajira na maisha bora,” alisema Rais Ouattara.

Rais Ouattara aliyetumia muda mwingi kumshukuru Rais Kikwete na viongozi wenzake wa Kiafrika kwa kusaidia upatikanaji wa amani nchini mwake alitaja changamoto kadhaa zinazokabili Bara la Afrika, kuwa ni mabadiliko ya tabia nchi, ukame, uhaba wa chakula na ukosefu wa amani kwa baadhi ya sehemu.

Mambo mtambuka 
Ili kukabiliana na tatizo hilo, Rais Kikwete alitaja mambo kadhaa yanayopaswa kufanyika ikiwa ni pamoja na kukuza na kuboresha sekta ya kilimo kwa kuongeza uwekezaji na kuacha kutegemea kilimo cha mvua badala yake itumie fursa ya vyanzo vingi vya maji.

“Bara la Afrika linaweza kuzalisha mazao ya kilimo na kujitosheleza kwa chakula na kubakisha ziada ya kuuza nje hadi kuwa ghala la chakula duniani iwapo uwekezaji katika sekta ya kilimo utapewa kipaumbele,” alisema Rais Kikwete.

Kuhusu miundombinu, Rais Kikwete aliipa changamoto AfDB kuongeza juhudi katika ufadhili na udhamini wa miradi ya maendeleo barani Afrika, ikiwemo miradi ya miundombinu aliyosema ni moja ya changamoto zinazokwaza maendeleo ya Afrika.

Alisema pamoja na kukwaza mawasiliano kwa njia ya barabara, reli na anga, uduni wa miuondombinu pia huchangia bei kubwa ya bidhaa na huduma katika nchi za Kiafrika kutokana na gharama kubwa ya usafirishaji.

Rais Kikwete alisema uwepo wa miundombinu ya uhakika siyo tu itawahakikishia wakulima vijijini soko na bei ya uhakika kwa mazao na bidhaa zao, lakini pia itapunguza kasi ya watu kuhamia mijini inayozikabili miji mingi barani Afrika.

Akizungumzia uwekezaji katika nyanja ya uchumi mdogo, Rais alisema  uwekezaji huo ndiyo njia pekee ya kuboresha na kuinua uchumi wa watu wa kawaida huku ikitumia vema soko lake la ndani kwa kutumia bidhaa zinazopatika barani humo badala ya kuendelea kutumia fedha nyingi kuagiza bidhaa kutoka nje, hata zile zinazopatikana nchi jirani.

Rais Kikwete alisema ili kupiga hatua kimaendeleo, Afrika kupitia AfDB na wahisani wengine wa ndani na nje lazima iwekeze katika ujenzi na uboreshaji wa miuondombinu ambayo ni nyenzo muhimu kimaendeleo.

Kuhusu sekta ya utali, alisema licha ya  Afrika kujaliwa vivutio vingi vya utalii, sekta hiyo bado haichangii kikamilifu uchumi wa bara hilo kutokana na kukabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo miundombinu mibovu, ukosefu wa safari za ndege za kimataifa na bei kubwa ya safari ndege chache za kimataifa zinazofanya safari zake barani Afrika.


Lowassa na ajira
Novemba 15, mwaka jana akiwa katika harambee ya ujenzi wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Makasa, Parokia ya Nyakato, Mwanza, Lowassa alionya kuhusu tatizo hilo na kulitaka Kanisa lisaidie kujenga vyuo vya ufundi.

Alitoa takwimu akisema utafiti wa mwaka 2006, ambao hata hivyo, hakusema ulifanywa na taasisi gani, ulionyesha kuwa tatizo hilo kwa sasa limekuwa na kufikia asilimia 15 huku likigusa zaidi vijana wenye umri wa miaka kati ya 15 hadi 24 ambao ndiyo nguvukazi ya taifa.

Novemba 29, mwaka huo wa jana akiwa harambee ya ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Usharika wa Amani Sabasaba, Singida, Lowassa alionya tena kuhusu tatizo hilo la ajira. 

Mwezi Machi mwaka huu akiwa katika sherehe za uzinduzi wa Jimbo jipya la Kanisa Katoliki Ifakara alirejea kisema: “Nawaomba maaskofu katika miradi yenu mlipe kipaumbele suala la tatizo la ajira kwa vijana.... hili kama tulivyosema ni bomu linalosubiri kulipuka...”

Hata hivyo, kauli hiyo mpya ya Lowassa, ilijibiwa na Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana Gaudensia Kabaka Machi 21 akisema, "Siyo kweli  kudai Serikali hayaijafanya kitu, wanakuwa hawaitendei haki na kuongeza kwamba, utafiti uliofanywa na wizara yake kwa kushirikiana na Taasisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), unaonyesha kuwa tatizo hilo limepungua kwa asilimia 1.2.

CHANZO: Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.