Showing posts with label MIGOMO. Show all posts
Showing posts with label MIGOMO. Show all posts

18 Oct 2008

Wanafunzi 5,300 na wahadhiri wao zaidi ya 100 wa Chuo Kikuu cha Dodoma, wameanza mgomo usio na ukomo wakishinikiza uongozi wa chuo hicho kuwalipa stahili zao mbalimbali.Wanafunzi hao walikuwa wamebeba mabango mbalimbali yenye ujumbe wa kumtaka Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Shabani Mlacha, kujiuzulu kwa madai kuwa ndiye kikwazo. 

Pia walikuwa wakiimba nyimbo za kuhamasisha mshikamano huku wakimtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwenda chuoni hapo kuwasikiliza. 

Askari Polisi wakiwa kwenye magari walikuwa pembeni ya wanafunzi hao wakiwa tayari kupambana na wanafunzi hao kama wangefanya fujo hivyo kusababisha uvunjifu wa amani chuoni hapo. 

Hata hivyo, polisi hao walijikuta hawana kazi ya kufanya kwani hakukuwa na hali yoyote ya uvunjifu wa amani na wanafunzi hao walionekana kuwa watulivu wakati wote wa kuimba nyimbo zao. 

Katika mgomo huo ulioanza jana, wanafunzi hao wanalalamikia uhaba wa malazi kwa madai kuwa wanachangia Sh. 500 kila siku, lakini baadhi yao wanalala kwenye nyumba za kulala wageni na wengine wakilazimika kulala kwenye chumba kimoja watu wanne. 

Akizungumzia mgomo huo, Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo hicho, Malimi Joramu, alisema sababu nyingine ni uongozi wa chuo hicho kuwatoza wanafunzi Sh. 100,000 kama gharama za matibabu kwa miaka mitatu. 

Alisema malalamiko yao yapo upande wa wanafunzi ambao ni watumishi wa umma ambao hulazimika kuchangia gharama hizo kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, lakini uongozi wa chuo umewataka wote kulipia gharama hizo bila kujali ni mtumishi wa umma au la. 

``Tulishakubaliana na Uongozi wa Chuo mwaka jana kuwa wanafunzi hao wasichangie gharama hizo na wale waliokwisha changia warudishiwe gharama zao, lakini tumeshangaa kwa wanafunzi wa mwaka huu, gharama hizo zimerudishwa tena na wale waliorudishiwa fedha zao, wametakiwa kurudisha gharama hizo,`` alisema Rais huyo. 

Madai mengine alisema ni pamoja na Uongozi wa Chuo kuweka muda mfupi wa usajili wa wanafunzi, ambapo chuo hicho kimetangaza kwamba jana ndiyo mwisho na wale ambao watakuwa hawajajisajiliwa, Chuo hicho hakitawatambua. 

Rais huyo anadai kuwa, muda huo ni mfupi mno ukilinganisha kuwa wanafunzi wengi wanaosoma chuoni hapo wanatoka katika familia maskini na hata walipouomba uongozi wa chuo kuwaongezea muda, ulikataa kufanya hivyo na kushikilia msimamo wake wa kuwafukuza. 

``Tunajiuliza hivi iweje mafisadi wa EPA ambao ni wezi wameongezewa muda wa kulipa fedha walizoiba, sisi ambao ni wanafunzi na tunatoka kwenye familia maskini tunakataliwa kuongezewa muda hata wa mwezi mmoja tu, hii sio haki kabisa,`` alilalamika Joramu. 

Kwa upande wa wahadhiri wa chuo hicho, wao wanadai kutolipwa posho ya kujikimu ya wiki moja ya kuripoti chuoni hapo pamoja na fedha za uhamisho kwa baadhi ya wahadhiri. 

Wengine wamedai hawajalipwa mishahara yao ya mwezi uliopita hali inayowafanya waishi maisha ya kuombaomba, hasa kutokana makali ya maisha kupanda. 

Wahadhiri hao wanaokadiriwa kupita 100, wamegoma kuingia madarasani wakishinikiza kulipwa posho hizo, pamoja na mishahara yao na ikiwa ni vinginevyo, mgomo huo hautakuwa na ukomo. 

Akijibu tuhuma za wanafunzi, Profesa Mlacha alisema gharama za malazi wanazolipia wanafunzi hao, zimepunguzwa kutoka shilingi 700 kwa siku mwaka jana, hadi kufikia Sh. 500 mwaka huu. 

Alisema sababu za kupunguza gharama hizo ni malalamiko ya wanafunzi hao wakidai kuwa ni kubwa na wazazi wao wanashindwa kumudu kulipa. 

``Kutoka na hali halisi ya maisha, tuliwaelewa na tukaamua kushusha hadi kufikia Sh. 500, lakini pamoja na kushusha huko, bado baadhi yao wanaendelea kulalamika kuwa gharama hizo ni kubwa,`` alisema. 

Hata hivyo, Profesa Mlacha alisema chuo hicho kina malazi ya kutosha na kila chumba wanalala wanafunzi wanne kutokana na ukubwa wa vyumba hivyo, kwa kuwa kila mwanafunzi ana kitanda chake. 

Alisema hivi sasa kuna vitanda na magodoro zaidi ya 1,000 ambayo hayajalaliwa na wanafunzi kutokana na wengi wao kuwa hawajaripoti chuoni hapo hadi sasa na kushangazwa na malalamiko ya wanafunzi ambayo aliyaita kuwa ni ya uzushi. 

Kwa upande wa malipo ya matibabu alisema, chuo hicho kilikutana na watendaji wa Mfuko wa Bima ya Afya na kuzungumza nao kuangalia utaratibu wa matibabu ambapo walibaini kuwa, kuna baadhi ya magonjwa ambayo mfuko huo hauyalipii. 

Kuhusu madai ya usajili alisema, hizo ni sheria za chuo kwamba mwanafunzi ambaye hajasajiliwa na chuo, hatambuliki kama ni mwanafunzi. 

``Tangu siku ya kwanza ya mwanafunzi kupata barua ya kuitwa chuoni, anaorodhoshwewa mahitaji yote anayotakiwa kuja nayo, sasa iweje mwanafunzi aje shuleni akiwa hana fedha hata nusu ya gharama hizo, chuo hakitakubali hata kidogo kumsajili mwanafunzi ambaye hajalipa hata nusu ya gharama zinazohitajika,`` alisisitiza. 

Akijibu malalamiko ya wahadhiri, Profesa Mlacha alisema sheria iliyokuwa ikitaka wahadhari hao kulipwa posho hiyo imefutwa, lakini hata hivyo, chuo hicho kimetumia busara ya kuwaombea fedha hizo serikalini na taratibu hizo zilikuwa zinaendelea. 

Hata hivyo, alisema pamoja na kwamba asilimia 80 ya walimu hao hawana sifa za kulipiwa gharama za malazi na chuo, chuo hicho kimejitahidi kuwapatia nyumba ambazo zina kila kitu na kwamba hakuna mhadhiri anayekaa kwenye nyumba za kulala wageni. 

``Wahadhiri hao nao wametufikisha mahali ambapo tunashangaa, mwaka jana tuliwalipa, lakini kutokana na sheria hiyo kufutwa bado tukatumia ubinadamu wa kuwaombea fedha hizo serikalini, lakini wakati suala hilo likishughulikiwa tunashangaa nao wanagoma, chuo hakielewi nia yao ni nini,`` alihoji Prof. Mlacha. 

Aidha, Profesa Mlacha alisema, uchunguzi wa chuo hicho umebaini kuwa, wapo wahadhiri wachache wanaojifanya wanazijua siasa au wanataka kutumia chuo hicho kujifunza siasa. 

``Tumebaini wahadhiri hao ndiyo walioshinikiza mgomo huu, inawezekana wanajifunza siasa ndani ya chuo hiki, lakini tunawaeleza kuwa, hiki sio chuo cha siasa na kama wanataka siasa waende kwenye vyama vya siasa kuonyesha uwezo wao wa kujua siasa,`` alisema Profesa Mlacha. 

Hadi mwandishi wa habari hizi anaondoka eneo la chuo hicho bado wanafunzi hao walikuwa wakiendelea na mgomo wao.

CHANZO: Nipashe

15 Oct 2008

WALIMU wa Mkoa wa Dar es Salaam jana walimshambulia kwa kumrushia mawe, chupa za maji, viti na meza, Rais wa Chama cha Walimu Tanzania nchini (CWT), Gratian Mukoba, kwa madai kuwa amewasaliti kwa kukubali kuahirisha mgomo wao, uliotarajiwa kuanza leo nchi nzima.

Tafrani hiyo ambayo inazidi kuliingiza taifa katika sura mpya ya migomo ya wafanyakazi nchini, ilitokea jana katika Ukumbi wa Diamond Jubilee wakati walimu hao walipokutana kwa ajili ya kufanya maandalizi ya mwisho ya mgomo wao waliodai kuwa usingekuwa na kikomo, wenye lengo la kuishinikiza serikali iwalipe malimbikizo yao, yanayofikia zaidi ya sh bilioni 16.

Kikao hicho kilianza majira ya saa nne asubuhi na kuhudhuriwa na maelfu ya walimu kutoka Mkoa wa Dar es Salaam na wawakilishi wa mikoa ya Shinyanga na Mwanza.

Mwanzoni mwa kikao hicho kilichovunjika kutokana na vurugu hizo, walimu walikuwa watulivu kwenye viti vyao, kusikiliza kauli za viongozi wao, hasa Mukoba aliyekuwa akizungumzia hatima ya mgomo huo.

Ilipofika majira ya saa 6:20 mchana, Mukoba alishika kipaza sauti na kuanza kutoa tamko la chama hicho kwa nchi nzima kwamba mgomo wao ambao ulipangwa kuanza leo, umeahirishwa.

Huku baadhi ya walimu wakianza kunyanyuka kwenye vitu vyao na kutoa kelele za miguno iliyosikika kila kona, Mukoba alisema CWT imelazimika kuahirisha mgomo huo baada ya kushauriana na Mwanasheria wao, Gabriel Mnyele, aliyewataka waahirishe ili wapate nafasi ya kukata rufaa kupinga amri ya Mahakama Kuu, Kitengo cha Kazi, iliyozuia mgomo huo usifanyike leo.

“Kwa tamko hili ninalolisoma hapa mbele yenu, mgomo unaahirishwa kwa nchi nzima, hadi mwanasheria wetu atakapotujibu baadaye kutokana na zuio la mahakama lililotolewa jana (juzi),” alisema Mukoba.

Mara baada ya kutoa kauli, huku akiendelea kusoma maazimio mengine, ghafla umati wa walimu ulisimama kutoka kwenye viti vyao na kuvamia meza kuu, huku baadhi wakiipindua na kusababisha viongozi wa CWT kumwagikiwa maji yaliyokuwa juu za meza yao.

Kama hiyo haitoshi, baadhi ya walimu walianza kurusha chupa za maji na viti kwenye meza kuu, kwa lengo la kuwapiga viongozi wao, hasa Mukoba, aliyeonekana kushambuliwa zaidi.

Tafrani hiyo ilidumu kwa takriban dakika 35 ndani ya ukumbi huo uliokuwa na kelele nyingi za kuzomea, huku maofisa usalama wakilazimika kufanya kazi ya ziada kumwokoa Mukoba na viongozi wenzake, waliotaharuki kutokana na kushambuliwa huko.

Vita ya kurusha makopo, chupa za maji na viti iliposhika kasi, Mukoba na wenzake waliamua kukimbilia kwenye moja ya kona za ukumbi huo kujisalimisha, lakini hali hiyo haikuwasaidia, kwani walizidi kushambuliwa kwa kurushiwa vitu kama vibaka.

Tukio hilo lililoonekana kama filamu, mbali ya kuwapo kwa mashambulizi ya kurusha vitu, pia baadhi ya walimu walitoa lugha chafu kuwatukana viongozi hao na kuwataka wajiuzulu mara moja kwa madai kuwa wamewasaliti.

“Leo hatuwaachii, ama zenu ama zetu, walimu tumeonewa, tumedhalilishwa na kuibiwa vya kutosha na wewe Mukoba funga mdomo wako hapo mbele, tena katisha kusoma hilo tamko lako la kilaghai…sasa leo tutakufunza adabu kwa kukucharaza bakora ili ukome tabia hii ya usaliti.

“Kama ulikuwa unajua unakuja kutusomea hilo tamko la kipuuzi, kwanini usingeenda kwenye vyombo vya habari ukautangazie umma, kuliko kutuita hapa ukumbini kuja kutueleza ujinga kama huu…sasa leo utatujua sisi ni nani,” walisikika baadhi ya walimu wakitoa kauli hiyo.

Wakati vurugu hizo zikiendelea, majira ya saa 7:20 mchana makachero wa Jeshi la Polisi wakiongozwa na Kamanda wa Mkoa wa Ilala, Faustine Shirogile, Kamanda wa Upelelezi Mkoa wa kipolisi Ilala, Mkumbo na makachero zaidi ya 20, wakiwa na gari tatu aina ya Land Rover ‘Defender’, walifika eneo hilo kwa ajili ya kuimarisha ulinzi.

Makachero hao, walifanikiwa kuwatorosha viongozi hao kupitia mlango wa nyuma, huku baadhi ya walimu, nao wakitoka nje, kuangalia mlango uliolengwa kutumika kumtoa Mukoba na wenzake.

Wakiwa wanajipanga kumtorosha Mukoba kupitia mlango wa nyuma na kutaka kumwingiza kwenye gari la Polisi badala ya ‘Shangingi’ alilokuja nalo, walimu walibaini hali hiyo na kuamua kusogea karibu na gari hilo bila kuogopa vitisho vya polisi waliokuwa wakifyatua risasi hewani, kuwatawanya.

Wakati huo walimu wengi walikuwa wameshatoka ndani ya ukumbi kwenda kujipanga kandokando mwa barabara ya kwenda Shule ya Msingi Olympio, kwa lengo la kutaka kuendeleza mashambulizi.

Bila kuogopa risasi, wengine wakiwa na mawe mkononi, walilisogelea gari hilo la Polisi lenye namba za usajili T 220 AMV, huku wakiwakebei polisi kuwa nao wana njaa kama walimu na mishahara yao ni midogo, hivyo hawapaswi kuwazuia.

Ilipofika majira ya saa 7:30, polisi walilazimika kumtoa Mukoba na baadhi ya viongozi wa CWT chini ya ulinzi kwa ajili ya kuwapandisha kwenye gari hilo, lakini walimu nao walivyoona hali hiyo, walirusha mawe na jiwe moja lilimpata Mukoba sehemu ya tumbo na kusababisha aanguke kabla ya kusimama tena na kukimbilia ndani ya ‘Defender’ ya polisi.

Baada ya kuingizwa ndani ya gari hilo, polisi walirusha risasi hewani kabla ya dereva kuliondoa kwa kasi ili kuwatawanya walimu hao ambao walikuwa wakiendelea kulirushia mawe gari hilo.

Baada ya gari hilo kuondoka, hasira za walimu hao ziliishia kwenye kuimba nyimbo za kumsifu Mwalimu Nyerere.

Moja ya nyimbo hizo ni pamoja na ule unaotumika kwenye migomo mingi ya wafanyakazi nchini, ambao wao waliongezea vionjo kwa kusema: “Kama siyo juhudi zako Nyerere; Kikwete, Maghembe, Ghasia wangetoka wapi!”

Pia waliimba wimbo unaodai kuwa CCM ni chama cha mafisadi, huku wakikisifia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa kuonyesha alama ya vidole viwili juu, inayotumiwa na chama hicho kusalimiana.

“CHADEMA, CHADEMA, CHADEMA oyeee! Sasa inatulazimu tufanye mapinduzi kama waliyofanya wenzetu wa Tarime kwa kuing’oa serikali ya CCM madarakani kwani inatukandamiza wanyonge na kukumbatia mafisadi,” walisikika wakisema baadhi ya walimu hao.

Hata baada ya Mukoba kuondolewa katika sehemu hiyo na kuliacha gari lake ambalo lilitolewa upepo na walimu hao, bado walimu hao walifunga barabara kuzuia magari yote yaliyokuwa yakipita eneo hilo huku, magari ya kifahari yakipigiwa kelele kuwa ni ya kifisadi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya walimu hao walisema licha ya kuwepo kwa amri ya mahakama kuzuia mgomo huo leo, wataendesha mgomo baridi, kwa kwenda kwenye shule zao, kujiandikisha kwenye vitabu vya mahudhurio, kisha kurejea majumbani mwao.

“Viongozi wa serikali wanajifanya wajanja, sasa sisi ndio walimu, na sisi ndio tunawafundisha watoto mashuleni, tutawafundisha uongo na mzazi mwenye uwezo ni vyema akampeleka mtoto wake shule binafsi,” alisema Mwalimu Lidyia Mhina.

Ilipofika majira ya saa 8:30 mchana, baada ya hali kuwa shwari, walimu walikusanyika nje ya ukumbi huo na Mwalimu Maulid Ng’umbe aliwatangazia walimu hao kuwa kuanzia sasa, CWT haina viongozi.

Juzi, Jaji William Mandia, wa Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, aliamuru CWT kusitisha mgomo mara moja, kwa kuwa unaweza kuharibu mfumo wa elimu, hasa wanafunzi wa kidato cha nne, ambao wapo katika mitihani.

Mgomo huo ulitarajiwa kuanza leo baada ya CWT kutoa notisi ya siku 60 ambayo imemalizika jana. Walimu wote nchini wanaidai serikali zaidi ya sh bilioni 16, zikiwa na fedha za malimbikizo ya mishahara, likizo na kupandishwa madaraja.


23 Sept 2008



Mgomo wa NMB nchi nzima-Mishahara kuchelewa

Na Waandishi Wetu 

ZAIDI ya wafanyakazi 5,000 nchini wanaochukua mishahara yao kupitia Benki ya National Microfinance Bank (NMB) watalazimika kutolipwa wiki hii kutokana na mgomo wa nchi nzima wa wafanyakazi wa benki hiyo ulioanza jana. 

Wafanyakazi hao waligoma wakiishinikiza Serikali kuwalipa mafao na kupewa asilimia tano ya hisa zilizotengwa kwa ajili yao wakati Serikali ilipoamua kuuza hisa zake. 

Mgomo huo umekuja baada ya Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (TUICO), kutoa notisi ya saa 48, Septemba 19 mwaka huu ikieleza kusudio la kugoma. 

Akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam jana kuhusu mgomo huo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo, Bw. Ben Christiaanse, alisema hatua iliyochukuliwa na wafanyakazi hao katika matawi 121 nchini, ni kubwa kuliko tatizo lililopo. 

Aliulaumu uongozi wa TUICO kwa kile alichodai mbali ya kusababisha matatizo mengine, umekiuka amri ya mahakama kwa kuwa suala la wafanyakazi hao bado lilikuwa linashughulikiwa na kusisitiza, kwamba mgomo huo umesababisha matatizo makubwa kwa mamilioni ya Watanzania. 

Akizungumza kwenye mkutano huo, Mwanasheria wa NMB, Bw. Rosan Mbwambo, alisema jana asubuhi benki hiyo iliwasilisha ombi rasmi mahakamani la kukiukwa amri hiyo iliyotolewa Januari 21 mwaka huu na kutaka wahusika kuchukuliwa hatua za kijinai. 

Alisema baada ya kuwasilisha ombi hilo, mahakama hiyo iliagiza pande mbili, Benki na Chama cha Wafanyakazi, kufika mahakamani leo asubuhi. 

Aliwataja viongozi wa TUICO wanaotakiwa mahakamani leo kuwa ni Katibu Mkuu wa TUICO, Bw. Boniface Nkakatisi, naibu wake Alquine Senga, Mwenyekiti wa NMB TUICO Tawi na Kamati ya Majadiliano, Bw. Joseph Misana na Katibu wa Tawi la NMB, Bw. Abdallah Kinenekejo. 

Kutoka Tanga, Benedict Kaguo anaripoti kuwa wateja wa Benki ya NMB waliulalamikia uongozi wa benki hiyo kwa kushindwa kusikiliza madai ya watumishi wao hadi kusababisha mgomo mkubwa ulioleta adha kubwa. 

Wakizungumza kwa jazba nje ya ofisi za benki hiyo tawi la Madaraka jana baada ya kukuta tangazo lililowaomba radhi wateja kuwa hakutakuwa na huduma, wateja hao walidai jambo hilo limetokana na kupuuzwa hoja za wafanyakazi hao. 

Walieleza kutofurahishwa na kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo, Bw. Christiaanse kung’ang’ania kuwa mgomo huo ni batili bila kueleza chochote ama ni hatua gani amechukua kutekeleza madai ya wafanyakazi wake. 

“Sisi tunamshangaa huyu Mkurugenzi wa NMB, anaacha kueleza ni nini atawafanyia wafanyakazi hawa ili wasigome, yeye anang’ang’ania kuwa mgomo ni batili haya ni mambo ya ajabu sana,” alisema Mwalimu Deo Temba. 

Alieleza kuwa NMB ni benki kongwe nchini, hivyo kitendo cha kutowajali watumishi wake kinaifedhesha benki hiyo ndani ya jamii. 

Kutoka Shinyanga, Suleiman Abeid anaripoti kuwa mgomo ulichukua sura mpya baada ya wafanyakazi benki hiyo kutishia kuwashawishi na kuwaomba wafanyakazi wa sekta nyingine nao wagome kuishinikiza Serikali ikubali kutekeleza madai yao. 

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini humo jana, wafanyakazi hao wakiongozwa na viongozi wao wa chama chao, ngazi ya tawi na mkoa, walisema watafanya chini juu kuwaomba wafanyakazi wenzao wawaunge mkono, ili Serikali ishughulikie haraka madai yao. 

“Iwapo madai yetu hayatapatiwa ufumbuzi mapema, sisi tutaendelea na mgomo wetu na ni wazi wafanyakazi wenzetu hawataweza kulipwa mishahara yao na hata baadhi ya wafanyabiashara watapata shida, tutawaomba nao wagome katika maeneo yao,” alieleza Bw. Emmanuel Samara Katibu TUCTA mkoani hapa. 

Naye Katibu wa TUICO Shinyanga, Bw. Gabriel Melchior, alisema wafanyakazi wa NMB hawajagoma bali wanaendeleza mgomo ulioanzishwa na Serikali na mwajiri wao. 

Naye Francis Godwin kutoka Iringa anaripoti kuwa mgomo wa wafanyakazi NMB ulikabiliwa na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) baada ya kutanda benki hiyo huku wateja wakiwa wamepanga foleni tangu asubuhi wakisubiri kuchukua fedha zao katika ATM. 

Kutokana mgomo huo baadhi ya wananchi walimtaka Waziri wa Fedha na Uchumi, Bw. Mustafa Mkulo, kuchukua hatua ya kujiuzulu haraka kwa kushindwa kumudu nafasi hiyo. 

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia wateja hao wengi wao wakiwa ni walimu na watumishi wa Serikali wakisubiri milango ya benki hiyo ifunguliwe, kutokana na kutokuwapo tangazo lolote lililoonesha kuwapo mgomo katika benki hizo. Matangazo hayo yalibandikwa saa 5 asubuhi. 

Kutoka Mwanza Jovin Mihambi anaripoti kuwa wafanyakazi katika matawi mawili ya NMB jijini humo walisema wataendelea na mgomo licha ya Menejimenti na Serikali kupuuza mwito wa kuwataka kukutana nao kutatua matatizo yao. 

Wakizungumza na Majira katika ukumbi wa DVN maeneo ya Posta jijini hapa, walisema awali walikubaliana na uongozi wa benki hiyo kupitia kwa Meneja wake, Bw. Methusela Israel, kuwa wangekutana kujua hatma ya nyongeza ya mishahara yao ambayo walisema kuwa ni asilimia tano. 

Katibu wa TUICO Mkoa wa Mwanza, Bw. Renatus Chimola, ambaye aliungana na wafanyakazi wa benki hiyo, alisema kama menejimenti na viongozi wa Serikali hawatatokea katika kikao hicho, mgomo huo utaendelea hadi leo mpaka uongozi huo utakapokutana nao na kujadili matakwa yao. 

Alisema wananchi ambao ni wateja katika matawi hayo watapata usumbufu, yeye na wafanyakazi hao, hawatajali usumbufu huo kwa madai kuwa wanachodai ni maslahi yao ambayo yatawawezesha kutenda kazi yao kwa ufanisi zaidi kama benki zingine nchini

SOURCE:Majira


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.