Showing posts with label Magufuli. Show all posts
Showing posts with label Magufuli. Show all posts

5 Apr 2017


Habari iliyotawala mno jana ni taarifa kutoka Ikulu kuwa Rais John Magufuli amemteua kiongozi wa chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo, Profesa Kitila Mkumbo, kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na Umwagiliaji.
[​IMG]
Kwa tathmini ya haraka haraka, taarifa hiyo imepokelewa kwa mitazamo miwili: wanaounga mkono hatua hiyo na wanaoipinga. Wanaoiunga mkono wanaona hatua hiyo ya Magufuli kama mwafaka katika kujenga umoja wa kitaifa na ushirikiano bila kujali tofauti za kiitikadi.


Wanaopinga wanaona uteuzi huo umelenga kuidhoofisha ACT-Wazalendo, mtego ambao haijulikani una malengo gani, na unafiki wa baadhi ya wanasiasa wa upinzani - katika suala hili ni Profesa Kitila na bosi wake Zitto Kabwe ambaye tayari amepongeza uteuzi huo.



Kwa sie tunaoliangalia suala hili 'kwa jicho la tatu,' tunabakiwa na  maswali mengi yasiyo na majibu. Swali mojawapo ni hili: katika hotuba yake moja huko Zanzibar, Rais Magufuli aliapa kutowashirikisha wapinzani kwenye serikali yake (msikilize mwenyewe kwenye video hii hapa chini)



Je Prof Kitila alikuwa 'mpinzani feki kwenye chama feki cha upinzani?'

Na ukiangalia 'upendeleo' aliopewa Profesa Kitila katika wadhifa wake kama mhadhiri wa chuo kikuu cha Dar es Salaam, kisha ukalinganisha na sababu zilizoplekea Profesa Mwesiga Baregu asiongezewe mkataba chuoni hapo, utahisi ipo namna. Hadi wakati Profesa Kitila anapewa 'ulaji' na Magufuli, ushiriki wake kwenye siasa haukuwa tatizo kwa serikali, hiyohiyo 'iliyomkalia kooni' Profesa mzoefu Barefu. 

Lakini pengine unafiki mkubwa wa Profesa Kitila ni ukweli kwamba alishaweka msimamo wake huko nyuma, alipokemea teuzi zinazofanywa na Rais Magufuli kuwachukua wahadhiri pasipo kuandaa wa kurithi nafasi zao. 


Kwahiyo, sidhani kama kuna neno stahili kuhusu Profesa Kitila zaidi ya unafiki. Ndio, alikuwa mtumishi wa serikali, lakini pia alikuwa kiongozi wa chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo. Na hili la unafiki linahusu kotekote, kwenye kazi yake kama mhadhiri - aliyekwishakemea tabia ya serikali kupora wasomi kwenye taasisi za elimu - na kama mwanasiasa ambaye baadhi yetu tulikuwa tukimwona kama tegemeo japo kiduchu kwenye siasa za upinzani. Leo hii, Profesa Kitila ameibuliwa kutoka UDSM na ACT-Wazalendo katika namla ileile BASHITE alivyoibuliwa kwenye u-DC na kupewa u-RC.

Kuhusu Zitto, mie kitambo nimekuwa nikimwona kama mwanasiasa mnafiki. Nani asiyekumbuka ahadi yake ya kutaja majina ya mafisadi walioficha pesa za umma huko Uswisi? Na ni Zitto huyu huyu aliyewahi kurushiwa tuhuma za kuisaliti Chadema baada ya gazeti moja kudaka kile ilichodai kuwa mawasiliano kati ya mwanasiasa huyo na kiongozi mmoja wa Idara ya Usalama wa Taifa. Unaweza kuisoma stori husika HAPA.

Hivi majuzi tu, kulikuwa na tetesi kuwa "Zitto amepotea"

Baadaye "akapatikana" na "akamwashia moto" Rais Magufuli akidai kuwa atakuwa rais wa muhula mmoja tu. Mwanasiasa huyo machachari alilaani kile alichoita "tabia za kidikteta za Magufuli," na kwamba "Watanzania hawatamvumilia (Magufuli) kuwatawala kwa kuwaburuza kidikteta."

Muda si muda, kukajiri 'drama nyingine' kuhusu Zitto, ambaye inaelezwa kuwa alilazimika kujificha ndani ya jengo la Bunge ili asikamatwe na polisi.

Leo Magufuli kamteua Profesa Kitila kuwa katibu mkuu, katika moja ya miujiza ya kisiasa nchini Tanzania, na tayari Zitto 'amebadilika.' Hebu msikie hapa chini


Uzuri mmoja wa unafiki huu ni kwamba Magufuli kawarushia kitanzi Profesa Kitila na Zitto, wajifunge wenyewe au wakikwepe. Kwa sababu wanazozijua wenyewe wamejifunga wenyewe. Nasema hivyo kwa sababu kwa sasa haitowezekana kwa Profesa Kitila kuikosoa serikali kutokana na wadhifa wake huo mpya.

Kadhalika, Zitto na ACT- Wazalendo yake watakuwa na wakati mgumu kuikosoa serikali ambayo "nao wamo" kupitia uwepo wa Prof Kitila. 

Lakini pengine ni vema kukumbuka historia ya wawili hawa katika siasa za upinzani Tanzania. Mie ni mmoja wa watu wanaoamini kwa dhati kuwa laiti wawili hao - Zitto na Kitila - wasingefanya chokochoko ambazo baadaye zilipelekea kufukuzwa kao huko Chadema, basi huenda leo hii Chadema ingekuwa chama tawala. 

Nimaliie makala hii kwa kutahadharisha kuwa si ajabu katika siku chache zijazo mtamskia tena Zitto huyuhuyu anayemwagia sifa Magufuli akielezea kuhusu ishu moja nzito. Baadhi yetu twafahamu kuhusu mkakati fulani dhalimu unaomhusisha Bashite dhidi ya watu flani. Ninatarajia Zitto ataufahamu hivi karibuni. Tuliache hilo, muda utaongea.

Nawatakia siku njema

28 Nov 2015


Makala hii imechapishwa katika jarida la Raia Mwema toleo la wiki hii lililotoka tarehe 25/11/2015, lakini kwa sababu nisizoelewa tovuti ya jarida hilo haijawa-updated kwa wiki kadhaa sasa. Kwa vile makala ninazotuma gazetini hufanyiwa uhariri kabla ya kuchapishwa, yawezekana makala iliyopo gazetini ikawa na tofauti kidogo na hii.

MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA NOVEMBA 25, 2015

Hotuba hii ya Rais Magufuli ni moja ya hotuba bora kabisa katika historia ya siasa za Tanzania.” Hili lilikuwa hitimisho langu katika mtandao wa kijamii wa Twitter mara baada ya Rais John Magufuli kumaliza kulihutubia Bunge wiki iliyopita, huko Dodoma.

Na kwa hakika watu kadhaa waliafikiana na hitimisho hilo.  Kilichovutia wengi waliosikia hotuba hiyo, katika shughuli ya ufunguzi wa Bunge la 11, sio tu mpangilio wa hotuba yenyewe bali pia jinsi kila alilotamka lilivyoonyesha bayana kuwa lilitoka moyoni mwake kwa dhati kabisa.

Rais alianza hotuba yake hiyo kwa kuorodhesha matatizo mbalimbali aliyobaini wakati wa kampeni zake Urais ambapo alizunguka takriban Tanzania nzima. Alitoa uchambuzi wa kina wa matatizo hayo kabla ya kuelezea kwa undani ni kwa jinsi gani serikali yake itayashughulikia. Ilikuwa ni zaidi ya hotuba ya kisiasa, na pengine ingeweza kabisa kuwa mhadhara wa kitaaluma uliofanyika katika lugha nyepesi na ya kueleweka.

Moja ya vitu vilivyonivutia sana katika hotuba hiyo ni jinsi Rais Magufuli alivyoweza kutupatia jibu la swali ambalo kwa miaka kadhaa lilionekana kuwatatiza viongozi wetu mbalimbali: “Kwanini Tanzania ni masikini licha ya utajiri lukuki wa raslimali ilionao.” Alieleza bayana na kwa kirefu jinsi ufisadi, rushwa na uhalifu vinavyochangia kukwamisha maendeleo ya taifa letu. Kadhalika, alifafanua, kwa kutumia takwimu halisi, jinsi mabilioni ya fedha yalivyotumika visivyo kwa matumizi yasiyo muhimu na yaliyo nje ya uwezo wa taifa letu masikini.

Kwa hakika ilikuwa hotuba ya kihistoria iliyofunika kabisa utovu wa nidhamu wa hali ya juu ulioonyeshwa awali na wabunge wa upinzani ambao walitumia muda mwingi kabla ya hotuba hiyo kuzomea na baadaye kuamiriwa  kutoka nje ya ukumbi huo.

Lakini kwa vile sio rahisi kumridhisha kila mtu, baadhi ya wenzetu waliosikiliza  hotuba hiyo walidai kuwa eti “haina tofauti na hotuba nyingine kadhaa zilizokuwa nzuri kuzisikiliza lakini zikaishia kuwa maneno matamu tu.” Wengine walikwenda mbali zaidi na kudai kuwa hata mtangulizi wa Rais Magufuli, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete naye pia alianza urais wake kwa hotuba za kutia moyo kama hizo lakini mengi ya aliyoahidi, hususan lile la ‘Maisha Bora kwa Kila Mtanzania,’ yaliishia kuwa ahadi tu.

Sikubaliani kabisa na wakosoaji hao, japo hoja zao zinaweza kuwa na mantiki kidogo. Ni kweli kwamba ukosefu wa hotuba za kuvutia si moja ya matatizo yanayoikabili nchi yetu. Wengi wa wanasiasa na viongozi wetu ni mahiri sana wa maneno lakini tatizo huwa katika kutafsiri maneno yao kuwa vitendo.
Wakosoaji hao hawapo sahihi kwa sababu, kama nilivyoeleza awali, hotuba hiyo ilikuwa ya kutoka moyoni.Ilikuwa hotuba ya kiongozi anayeguswa na yanayoisibu nchi yake, kiongozi mwenye uelewa wa changamoto zinazoukabili uongozi wake, na mwenye dhamira thabiti ya kukabiliana na changamoto hizo.

Kuna mbinu moja muhimu ya kubaini iwapo mtu anaongea ukweli au anahadaa, nayo ni kumwangalia usoni. Tangu kuanza kwa kampeni zake za urais na hadi wakati wa hotuba hiyo ya wiki iliyopita, uso wa Rais Magufuli wakati anaongea unaonyesha bayana kuwa kila neno linalotoka mdomoni mwake ni la dhati, linatoka moyoni na si sehemu ya porojo tulilozowea kutoka kwa wengi wa wanasiasa na viongozi wetu. Mtaalam yeyote wa kubaini ukweli na uongo hatoshindwa kuafikiana nami kuwa uthabiti wa kauli za Magufuli upo wazi kwa yeyete anayemwangalia usoni wakati anaongea.

Lakini pia, hotuba hiyo ilikuwa mwendelezo wa ishara nzuri zilizoanza kujitokeza siku moja tu tangu Rais Magufuli aingie ofisini, ambapo alifanya ziara ya kushtukiza Wizara ya Fedha, kabla ya kufanya ziara nyingine kama hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Na siku ya uzinduzi wa Bunge, alitukumbusha enzi za (Waziri Mkuu wa zamani) hayati Edward Sokoine, aliyesifika kwa uchungu wa mali za umma, baada ya kuamuru zaidi ya shilingi milioni 200 zilizochangwa kwa ajili ya hafla ya mchapalo ya sherehe za uzinduzi wa Bunge jipya zielekezwe kwenye ununuzi wa vitanda katika hospitali ya Muhimbili, na kiasi kidogo tu kitumike kwa ajili ya hafla hiyo.

Kimahesabu, chini ya wiki tatu tangu aingie madarakani, Rais Magufuli ameshaokoa jumla ya shilingi milioni 900 kutokana na hatua alizochukua dhidi ya matumizi yasiyo ya lazima. Kwa kasi hii, tuna kila sababu ya kutarajiwa kuiona nchi yetu ikipaa kiuchumi, na hatimaye Watanzania kunufaika na neema lukuki ambayo nchi yetu imejaaliwa kuwa nayo.

Sina shaka kuhusu uwezekano wa mafanikio ya hatua za Rais Magufuli huko serikalini. Licha ya kuwa na Waziri Mkuu mchapakazi mzoefu, Majaliwa Kassim Majaliwa, kuna kila dalili kuwa baraza la mawaziri ambalo hadi wakati ninaandaa makala hii lilikuwa halijatangazwa, litasheheni wachapakazi kama yeye. Kwahiyo, kazi ya kurejesha nidhamu serikalini, kupunguza matumizi yasiyoendana na umasikini wetu na kupambana na ufisadi ina dalili kubwa za mafanikio.

Eneo ambalo Rais Magufuli hawezi kufanikiwa peke yake pasipo ushirikiano wa Watanzania wote ni nje ya serikalini na huko ‘mtaani.’ Mara kadhaa nimekuwa nikisisitiza umuhimu wa wananchi kujenga kasumba ya kudai haki na stahili zao badala ya kuona haki/stahili hizo ni kama fadhila au upendeleo flani. Wenzetu huku Ughaibuni wamejenga desturi ya kutokubali huduma au bidhaa inayotolewa chini ya kiwango wanachostahili. Haki na stahili za mpokea huduma ni miongoni mwa vitu vinavyopewa umuhimu mkubwa huku tulipo.

Haitokuwa rahisi kwa Rais Magufuli au wasaidizi wake kwenda kila sehemu kuwezesha au kuharakiasha upatikanaji wa huduma. Jukumu hilo linapaswa kusaidiwa na wananchi wenyewe ambao mara nyingi ndio wahanga wakubwa wa huduma mbovu. Kadhalika, watoa huduma nje ya serikali wanapaswa kutambua kuwa hizi ni zama mpya, na asiyeweza kuendana na kasi ya Rais Magufuli na ajiweke kando.

Lakini mchango mkubwa zaidi wa wananchi wote unahitajika zaidi katika kupambana na ufisadi, rushwa na uhalifu mwingine nje ya serikali. Wakati Rais ameahidi kukabiliana na ‘mapapa’ wa uhalifu kama kwenye biashara hatari ya madawa ya kulevya, pasipo wananchi kumsaidia kwa kuwatenga wahusika na kuwaripoti -  badala ya kuwasujudia na kuwapa majina ya heshima kama ‘wazungu wa unga’ au ‘mapedejee’ – basi tutamkwamisha, na nchi yetu itaendelea kuumizwa na vitendo hivyo viovu.

Kadhalika, ili kauli-mbiu ya ‘Hapa Ni Kazi Tu’ iweze kuleta matokeo kusudiwa na kuwa ya ufanisi ni muhimu kwa kila Mtanzania kuachana na dhana fyongo ya kusaka mafanikio kwa njia za mkato, turejee zama za Ujamaa na Kujitegemea ambapo waliokula bila kuvuja jasho tuliwaita ‘kupe.’ Sote tuchape kazi, tuache kufanya ‘ujanja ujanja,’ tuone fahari kuwa na shughuli halali badala ya kuamini kuwa ufisadi, rushwa, uhalifu,nk ndio njia rahisi na sahihi za kufikia mafanikio kwa haraka.

Baada ya kumpoteza Baba wa Taifa Marehemu Mwalimu Julius Nyerere aliyetujengea misingi imara ya taifa letu, japo sasa inamong’onyoka kwa kasi, na mzalendo wa daraja la kwanza, Marehemu Sokoine, sala/dua zetu katika wimbo wetu wa taifa katika maneno “Mungu Ibariki Tanzania…” zimesikika, na Mwenyezi Mungu ametuletea ‘Nyerere na Sokoine mpya’ kupitia kwa Rais wetu mpya Dkt Magufuli. Tusijiangushe wenyewe kwa kutotumia ipasavyo fursa hii adimu.

Nimalizie makala hii kwa wito ‘wa kitaalamu’ kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ambao pamoja na majukumu mengine, wana dhamana ya ulinzi wa Rais wetu na viongozi wengine wakuu kitaifa. Kama alivyosema mwenyewe, vita aliyoanzisha dhidi ya kila vitendo na kasumba zinazolikwaza taifa letu ni nzito na inawagusa watu wazito. Kwa vile yayumkinika kusema kuwa vitendo vya rushwa,ufisadi na uhalifu vimefikia hatua ya ‘kimafia,’ basi ni muhimu kuimarisha ulinzi wa Rais wetu (na viongozi wengine wanaopatiwa ulinzi) kwa sababu ‘tupo vitani.’

Simaanishi kuwa ulinzi uliopo una mapungufu lakini angalizo hili linazingatia ukweli kwamba ‘vita’ hiyo inagusa maslahi ya wengi, maslahi ya ‘kupe’ lukuki walioigeuza Tanzania yetu kuwa ni ‘shamba la bibi,’ la kuvuna wasichopanda, sambamba na wahalifu wanaoingiza, kuuza na kusafirisha madawa ya kulevya kana kwamba ni bidhaa iliyoidhinishwa na Shirika la Viwango la Taifa (TSB), majangili wanaoshindana kuua wanyamapori wetu na kusafirisha nyara za serikali, na wahalifu wengineo.

Rais Magufuli ameahidi kutotuangusha, basi nasi tusimwangushe.

Hapa Ni Kazi Tu!

Barua-pepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @chahali



21 Oct 2015




OKTOBA 25 mwaka huu, Tanzania itafanya Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani. Mchuano mkali zaidi unatarajiwa kuwa katika nafasi ya urais, ambapo licha ya vyama vinane kusimamisha wagombea wao katika nafasi hiyo, ushindani mkali ni kati ya mgombea wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, na yule wa umoja wa vyama vinne vya upinzani (Ukawa), Edward Lowassa.
Ushindani huo unatokana na unachangiwa zaidi na ukweli kwamba mgombea urais kwa tiketi ya Ukawa, Lowassa, awali alijaribu kuwania nafasi hiyo akiwa mwanachama wa CCM, lakini jina lake halikupitishwa, na hatimaye alijiunga na moja ya vyama vinavyounda Ukawa, Chadema, na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo unaojumuisha pia chama cha National League for Democracy (NLD), NCCR- Mageuzi na Chama cha Wananchi (CUF).
Yayumkinika kuhitimisha kuwa Rais wa Tano wa Tanzania, atakayemrithi Rais wa sasa, Jakaya Kikwete, atakuwa kati ya Dk. Magufuli au Lowassa, huku mgombea urais kwa tiketi ya chama kipya cha Alliance for Change and Transparency (ACT- Wazalendo), Anna Mghwira akitarajiwa kushika nafasi ya tatu.
Dalili kuwa uchaguzi huo ungekuwa na ushindani mkubwa zilianza kujitokeza katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake, ambapo licha ya baadhi ya wanasiasa wa chama hicho waliokuwa na nia ya kuwania urais kujitokeza kutangaza nia takriban mwaka mzima kabla ya kuanza rasmi kwa mchakato huo, jumla ya makada 43 walichukua fomu za kuwania kuteuliwa kuwa wagombea urais, huku 38 kati yao wakifanikiwa kurejesha fomu.
Kwa upande wa Lowassa, jina lake lilianza kusikika katika duru za siasa za Tanzania kuhusu mrithi wa Rais Kikwete, mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Ikumbukwe pia kuwa Lowassa alikuwa na mchango mkubwa katika kampeni za urais mwaka 2005, ambapo hatimaye Rais Kikwete alishinda. Kadri Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu ulivyozidi kujongea, ndivyo jina la Lowassa lilivyozidi kuvuma. Kimsingi, mchakato wa CCM kupata mgombea wake uligubikwa zaidi na shauku ya Watanzania iwapo Lowassa angepitishwa au la.
Hata hivyo, hatimaye jina la Lowassa halikupitishwa, na badala yake akapitishwa Magufuli, hatua ambayo pia ilihitimisha tetesi za muda mrefu kuwa urafiki kati ya Lowassa na Rais Kikwete ulikuwa umefikia kikomo, hasa ikizingatiwa kuwa hoja iliyokuwa na nguvu katika harakati za Lowassa kuwania urais kupitia CCM ni hisia kuwa huenda Kikwete angemsaidia Lowassa kuwa mrithi wake.

Kwa upande wa Ukawa, umoja wa vyama vinne vya upinzani ulioundwa katika Bunge Maalumu la Katiba mwaka jana kwa lengo la kushinikiza matakwa ya wananchi yaheshimiwe katika mchakato wa kupata Katiba mpya, mchakato wa kumpata mgombea wao wa urais ulitawaliwa na ukimya kwa muda mrefu, kabla ya Lowassa kujiunga na Chadema na hatimaye kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo. Ujio wa Lowassa uliamsha hamasa kubwa miongoni mwa wafuasi wa vyama vinavyounda umoja huo, sambamba na kuleta ushindani mkubwa dhidi ya CCM.
Hata hivyo, uamuzi wa Chadema kumpokea Lowassa, mwanasiasa ambaye chama hicho kilimwandama na tuhuma za ufisadi kwa muda mrefu, ulipokelewa kwa hisia tofauti na Watanzania wengi, huku baadhi wakiuona umaarufu wake kama mtaji muhimu kuwezesha kuishinda CCM, huku wengine wakidhani kitendo hicho ni cha usaliti, hususan kwa Chadema ambayo ajenda yake kuu ilikuwa kupambana na ufisadi.
Licha ya uamuzi wa Lowassa kujiunga na umoja huo wa wapinzani, ukweli kwamba kwa mara ya kwanza, vyama vya upinzani nchini humo vimeweza kushirikiana kwa kusimamisha wagombea mbalimbali katika nafasi ya urais, ubunge na udiwani, imeufanya uchaguzi huo kuwa wa kwanza katika historia ya Tanzania ambapo nafasi ya ushindi kati ya chama tawala na upinzani zinakaribiana.
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa idadi kubwa ya Watanzania sio wanachama wa chama chochote cha siasa. Na kundi hili licha ya kutarajiwa kuwa muhimu katika kuwezesha ushindi katika uchaguzi huo, pia linajumuisha wapiga kura wanaokabiliwa na uamuzi mgumu kujiunga mkono CCM na mgombea wake licha ya chama hicho kutuhumiwa kuwa kumechangia matatizo mengi yanayoikabili nchi hiyo, au kujiunga mkono Ukawa ambayo mgombea wake wa urais, Lowassa, licha ya kuhubiri kuhusu mabadiliko, anaonekana kama hana tofauti na chama hicho tawala, hasa ikizingatiwa alikuwa huko kwa muda mrefu.
Kwa tathmini hadi wiki hii ya mwisho kabla ya uchaguzi huo, chama tawala CCM 

kinatarajiwa kufanya vizuri zaidi ya vyama vya upinzani katika nafasi zote, yaani urais, ubunge na udiwani. Kwa upande wa urais, nguvu za CCM zimekuwa katika maeneo kadhaa ikiwa ni pamoja na kujenga picha kuwa mpinzani wao mkuu, Lowassa, hafai ndio maana jina lake lilikatwa katika mchakato wa chama hicho kupata mgombea wake.
Kujenga picha kuwa Lowassa, pamoja na viongozi wachache wa CCM walimfuata huko upinzani ni wenye uchu wa madaraka, wanaotumia malalamiko ya wananchi dhidi ya CCM kwa manufaa yao kisiasa.
Tuhuma za ufisadi dhidi ya Lowassa ambazo kimsingi zilitangazwa zaidi na vyama vya upinzani hususan Chadema. Katika hoja hiyo, CCM pia imejaribu kuionyesha Chadema na Ukawa kwa ujumla kama wanasiasa wasio na msimamo na walioikimbia ajenda yao ya kupinga ufisadi ili ‘kumsitiri’ Lowassa.
Kutofanikiwa kwa Lowassa na Ukawa kuelezea kwa undani kuhusu ajenda yao ya mabadiliko. CCM na mgombea wake Magufuli wamekuwa wakitumia muda mwingi kubainisha sera zao na jinsi watakavyotekeleza.
Takriban asilimia 85 ya Watanzania wanaishi maeneo ya vijijini ambayo kiasili ni ngome kubwa ya CCM kwenye chaguzi. Kwa upande mwingine, Ukawa hawajafanikiwa kujipenyeza vya kutosha katika maeneo hayo, ambapo pia kuna uelewa mdogo kuhusu muundo wa umoja huo.
Kwa mujibu wa takwimu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi, idadi ya wanawake –kundi ambalo kiasili ni ngome muhimu ya CCM – ni kubwa zaidi ya wanaume, na hii inatarajiwa kukinufaisha chama hicho tawala na mgombea wake Magufuli.
Magufuli, amekuwa waziri kwenye awamu mbili za urais Tanzania, Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa, na hii ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, na anasifika kwa uchapakazi. Kwa upande mwingine, ugombea wa Lowassa umeendelea kugubikwa na kashfa ya Richmond iliyosababisha ajiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.
Kadhalika, licha ya kuwa na mtandao mkubwa nchi nzima, kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa, CCM inanufaika na hoja inayojiri kwenye kila uchaguzi mkuu, kuwa kuwapa ushindi Wapinzani ni sawa na kuwapa fursa ya kufanya majaribio ya uongozi ilhali CCM ina uzoefu wa kutosha.
Mapema wiki hii ziliibuka tena taarifa kuwa mmoja wa viongozi wakuu wa Chadema alihamisha mabilioni ya shilingi kwenda nje ya nchi, fedha zinazodaiwa zilipatikana baada ya kiongozi huyo ‘kukiuza chama hicho’ kwa Lowassa.
Hata hivyo, changamoto kubwa kwa CCM ni kinachotafsiriwa kama hasira za Watanzania wengi kutokana na matatizo mbalimbali yanayoikabili nchi hiyo, ambayo CCM inabebeshwa lawama, kubwa zaidi likiwa ufisadi unaotajwa kama chanzo kikuu cha umasikini.
Wachambuzi mbalimbali wa siasa za Tanzania wanatafsiri kuwa ufuasi mkubwa kwa Lowassa na Ukawa unachangiwa zaidi na manung’uniko ya wananchi wengi dhidi ya CCM, kiasi cha kuwa radhi kumwamini mwanasiasa ambaye kwa muda mrefu ameandamwa na tuhuma za ufisadi. Kauli kama ‘bora kulipigia kura jiwe kuliko CCM’ sio tu imekuwa ikisikika mra kwa mara miongoni mwa wafuasi wa upinzani bali pia inaashiria manung’uniko hayo.
Kadhalika, kwa vyama vinne vya upinzani kuweza kushirikiana na kumsimamisha mgombea mmoja wa urais, na kuongezewa nguvu na ujio wa Lowassa pamoja na makada kadhaa waliohama CCM, kwa mara ya kwanza Wapinzani wanaona kuna uwezekano wa kukishinda chama hicho tawala. Mikutano yao ya kampeni imeshuhudia umati mkubwa japokuwa lawama kwa Lowassa imekuwa ni kuhutubia kwa muda mfupi mno.
Wakati Magufuli na CCM wanaonekana kujiamini na kuwa na uhakika wa ushindi, kwa upande wa Lowassa na Ukawa, licha ya kuwa na matumaini makubwa ya kushinda, wanaonekana kuwa na hofu ya kuhujumiwa na chama hicho tawala.
Kwenye nafasi za ubunge na udiwani, CCM inatarajiwa kusinda viti vingi zaidi kwa sababu licha ya kuwa na mtandao mzuri majimboni, Ukawa inaonekana kuwekeza nguvu zaidi katika kumnadi Lowassa kuliko katika kampeni zake majimboni. Kadhalika, takwimu zinaonyesha kuwa mgombea wa CCM, Magufuli, ametembelea maeneo mengi zaidi ya mgombea wa Ukawa, Lowassa.
Kwa upande wa vyama vingine vinavyoshiriki uchaguzi huo, inatarajiwa kuwa ACT-Wazalendo kitashika nafasi ya tatu nyuma ya CCM na Ukawa, na kinatarajiwa kuimarika zaidi baada ya uchaguzi huo hasa kwa vile inahisiwa kwamba iwapo Ukawa itashindwa, wafuasi wake wengi wanaweza kuiona ACT-Wazalendo kama mpinzani wa kweli dhidi ya CCM.
Kwa hitimisho, changamoto kubwa kwa chaguzi nyingi barani Afrika huwa kwa chama cha kikuu cha upinzani kukubali matokeo pindi kikishindwa. Kwa mara ya kwanza, Tanzania inafanya uchaguzi wake mkuu huku kambi ya upinzani ikiwa na imani kubwa kuwa itaibuka na ushindi.
Kadhalika, kadri uchaguzi unavyozidi kukaribia ndivyo Wapinzani (hasa Ukawa) wanavyozidi kuonyesha kutokuwa na imani na mfumo mzima wa uchaguzi. Bila kujali upande gani utakaoibuka na ushindi, mustakabali wa Tanzania unategemea busara za viongozi na wafuasi wa kila chama kuhamasisha amani badala ya vurugu. Ushindi mkubwa katika uchaguzi huo ni kwa Watanzania kuendelea kubaki na umoja na amani.
Pia, mshindi katika uchaguzi huo atakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazoikabili Tanzania, kubwa zaidi ikiwa kuleta uwiano kati ya utajiri wa raslimali lukuki katika nchi hiyo na hali ya maisha ya wananchi, kupunguza pengo kati ya matajiri na masikini, na kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi huu ambao kwa kiasi kikubwa umejenga mpasuko kijamii na kisiasa.
Mwisho, kwa vile hii ni makala yangu ya mwisho kabla ya uchaguzi huo hapo Jumapili, na kwa vile safu hii imekuwa ikifuatilia maendeleo ya uchaguzi huo tangu mwanzo, basi si vibaya kufanya ubashiri wa matokeo katika nafasi ya urais. Na ubashiri kuwa Magufuli atashinda urais, na CCM itashinda viti vya jumla katika nafasi za ubunge na udiwani, huku Ukawa, hususan Chadema, ikipata viti pungufu zaidi ya ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita.
Hata hivyo, mshindi halisi katika uchaguzi huo ni Tanzania na Watanzania wenyewe. Kuna maisha baada ya uchaguzi, kwa hiyo ni muhimu kwa upande utakaoshindwa kutanguliza mbele maslahi ya taifa, badala kufanya vurugu.
MUNGU UBARIKI UCHAGUZI MKUU. MUNGU IBARIKI TANZANIA.



Sababu Tisa kwanini CCM itashinda katika Uchaguzi Mkuu Jumapili hii, Oktoba 25

Na January Makamba

Tarehe 25 mwezi huu Oktoba, Watanzania watapiga kura kumchagua rais wao wa tano, wabunge na madiwani. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umekuwa na msisimko mkubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1995. Mengi yamendikwa kuhusu uchaguzi huu, hususan kutokana na hisia kwamba safari hii Upinzani una nafasi ya kukiondoa madarakani moja ya vyama vikubwa na vyenye muundo bora barani Afrika, chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). Matukio mbalimbali kuelekea uchaguzi huo yameleta shauku inayoweza kutengeneza hadithi ya kusisimua.

Nikiwa sehemu ya Timu ya Kampeni ya CCM,na kwa manufaa ya wote ambao wangependa kuwa na mtizamo tofauti, ninatoa sababu 9 kwanini tunaamini kuwa CCM itaibuka mshindi na kwanini Dkt John Pombe Magufuli atakuwa Rais ajaye wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

1.    Ugombea ‘fyongo’ (flawed) wa Edward Lowassa

Ilishabainika kuwa uchaguzi huu ungekuwa mgumu kwa CCM bila kujali nani angekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Upinzani. Lakini matokeo ya uchaguzi huu yalielemea upande wa CCM pale Upinzani ulipomchagua Lowassa kuwa mgombea wao. Ni rahisi kwa CCM kuchuana na Lowassa kuliko laiti mgombea wa Upinzani angekuwa Dkt Wilbrod Slaa, ambaye ndiye aliandaliwa kuwa mgombea kabla ya ‘ukusukumwa kando’ na nafasi hiyo kupewa Lowassa. Slaa alikuwa na uadilifu katika maeneo mengi, na aliaminika. Kwa Lowassa, ni vigumu na inanyima raha kuchuana na mfumo aliyoshiriki kujenga na ambao ulikuwa sehemu ya maisha yake hadi Agosti mwaka huu alipohamia Upinzani. CCM ilikuwa na nafasi ya kumpitisha Lowassa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais. Hatukufanya hivyo kwa sababu rahisi tu kwamba ingekuwa vigumu mno kumkabidhi kwa wananchi mgombea wa matarajio ya baadaye ambaye ni kiashirio cha yale yasiyowaridhisha wananchi kuhusu CCM. Kuna wanaoamini kuwa uchaguzi huu ni mgumu kwa vile Lowassa ndiye mgombea wa Upinzani. Sisi twaamini kwamba uchaguzi huu ungekuwa mgumu mara kumi zaidi laiti Lowassa angekuwa ndiye mgombea wetu.

2.    Upinzani umesalimisha ajenda yake ya kupinga ufisadi

Kipindi cha miaka 10 iliyopita kimetawaliwa na matukio mbalimbali ya kuwabainisha mafisadi na kuwachukulia hatua. Vyombo vya habari, taasisi za kiraia na Bunge vimefanya kazi nzuri kushughulikia suala hilo. Rais Jakaya Kikwete ameweka historia kwa kuamuru ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kupatikana kwa wananchi na kujadiliwa kwa uwazi Bungeni. Waziri Mkuu aliyekuwa madarakani, si mwingine bali Lowassa, alijiuzulu kwa sababu ya kashfa ya rushwa. Mawaziri kadhaa walitimuliwa kazi na manaibu waziri wawili wanatumikia vifungo jela. Huu ni uwajibikaji wa hali ya juu japokuwa kuna wanaoweza kudhani ni hatua ndogo. Umma umeamka.

Upinzani ulijenga hadhi yake kwa kuongelewa sana kuhusu ufisadi. Kilele cha Upinzani kilijiri mwaka 2007 katika mikutano mkubwa wa hadhara ambapo walitangaza majina 10 ya watu waliowaita mafisadi wakubwa zaidi, katika kilichokuja kufahamika kama Orodha ya Aibu (List of Shame). Lowassa alikuwa kinara kwenye orodha hiyo.

Ilitarajiwa kuwa Uchaguzi Mkuu huu uwe ‘hukumu’ kwa CCM kuhusu ufisadi. Upinzani ulitarajiwa kuitumia ajenda ya ufisadi ambayo inawagusa watu wengi. Lakini ghafla, kwa kumteua mwanasiasa, ambaye kwa jitihada zao wenyewe Wapinzani,  amefahamika zaidi kwa ufisadi, iliwalazimu kuzika ajenda hiyo. Kilichofuata baada ya hapo ni kituko na kichekesho. Wale mashujaa wa mapambano dhidin ya ufisadi walijikuta wakilazimika ‘kulamba matapishi yao.’ Wengi wao waliokuwa mahiri katika mitandao ya kijamii walilazimika kufuta historia ya baadhi ya waliyoyaandika mtandaoni walipokuwa wakikemea ufisadi, lakini si kabla ya maandiko yao kunaswa kwa ‘screenshots.’ Ulikuwa ni ukweli wa kushangaza. Ni Dkt Slaa na Professa Ibrahmi Lipumba, viongozi muhimu wa Upinzani tangu miaka ya Tisini, walioamua kujiuzulu nyadhifa zao kwa kukerwa na uamuzi wa Upinzani kumpokea Lowassa.Matokeo yake, Upinzani walijikuta wakichana kadi yao turufu- ajenda dhidi ya ufisadi. Ni nadra kwao kuongelewa suala hilo, na wanapojaribu kufanya hivyo, ni kwa kujitetea tu.

Jioni moja mwezi Agosti, nilimwona Mbunge wa Upinzani, Peter Msigwa, katika mdahalo kwenye runinga. Aliongelea kitu ambacho kilijumuisha mtizamo wa Upinzani kwa muda huo, na kiliniacha hoi. Alisema, kabla hawajampokea Lowassa, walifanya utafiti wao, na “ufisadi sio ajenda muhimu kwa taifa letu.” Alidai kwamba wenye ushahidi kuhusu ufisadi wa Lowassa wajitokeze hadharani.Alionekana kusahau kuwa walipomtaja Lowassa katika List of Shame, walitangaza hadharani kuwa wana ushahidi. Muda si mrefu uliopita, CCM ilikuwa ikiwaomba Wapinzani kuleta ushahidi kila yalipojitokeza madai ya ufisadi dhidi ya viongozi wa chama na serikali allegations were leveled against the party and its leaders. Haikupendeza kuingiza hoja za kisheria katika masuala ya kimaadili. Upinzani sasa umeamua kwa hiari yao kuchukua ‘chembemoyo’ wakati ambapo viongozi wa CCM wanaongelea ufisadi kwa ujasiri na msisitizo.

Uchaguzi huu Mkuu ni muhimu sana kwa Upinzani. Kimsingi, unaweza kuwa na madhara makubwa. Endapo watashindwa hapo Jumapili, ‘watapotea’ kwa muongo mzima ujao. Ndio maana inashangaza kuona wamechukua uamuzi wa kukimbia ajenda yao kuu ya kupambana na ufisadi  ambayo iliwatambulisha na kuwaimarisha. Na kuwapa nguvu kukubalika kwa wapigakura. Kuona wanatarajia kushinda ni miujiza mkubwa.

3.    Mabadiliko ambayo kamwe huwezi kuyaamini

Ukizinguka jijini Dar es Salaam utakutana na mabango ya Upinzani yanayodaia “Ni Muda wa Mabadiliko.” Lakini ukisikiliza mikutano yao ya kampeni, ni porojo na hasira tu. Wasemaji wakuu katika mikutano hiyo ni Waziri Mkuu wa zamani na kada wa muda mrefu wa CCM, Frederick Sumaye na Lowassa mwenyewe. Kwa pamoja, wamekuwa wana-CCM na katika nyadhifa  za juu serikalini kwa zaidi ya miaka 50. Kwa hiyo inasikitisha kusikiliza kauli zao – zinazokosa imani na kupalizwa na aibu – wakipambana na mfumo walioshiriki kujenga, uliojenga tabia zao za kisiasa, na ambao walikuwa wakiusifu miezi mwili tu iliyopita.
Kutokuwa wakweli na kuweka mbele maslahi binafsi kwawatuma kudai kuwa CCM haijafanya chochote katika miaka miaka 50 iliyopita. Inapotokea viongozi wawili waandamizi wa chama na serikali  kwa zaidi ya miaka 30, wote wakiwa walioshika Uwaziri Mkuu, kudai kuwa hakuna chochote kilichofanyika katika miaka 50 iliyopita, wajihukumu wenyewe. Si kwa muundo, mwonekano au ukweli, wanasiasa hao wanasimamia mabadiliko. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mabadiliko wanayoongelea ni kuhusu kubadili chombo kilichowaingiza madarakani, mabadiliko ya sare tu za chama. Hawana habari na mabadiliko ya maisha ya wananchi wa kawaida. Wapigakura wameanza kushtukia ukweli huo.

4.    Migogoro na mkanganyiko ndani ya UKAWA

Huko nyuma, kila ulipojiri uchaguzi, Upinzani ulijaribu kuunganisha nguvu ili kuing’oa CCM madarakani.Na kila mara jitihada za ushirikiano zilishindikana. Mwaka 2014, mjadala kuhusu Katiba Mpya kuataka serikali tatu uliwapatia ajenda ya kuwaunganisha pamoja. Kisha wakaamua kutafsiri ushirikiano huo kuwa wa kisiasa, wakaafikiana kusimamisha mgombea mmoja katika nafasi ya urais na kugawana majimbo.

Baada ya hapo kukajitokeza unafiki wa wazi. Kuonyesha kuwa matamanio yaliwekwa mbele ya kanuni zilizopatikana kwa jitihada ngumu, chama ambacho jina lake linajumuisha maneno ‘demokrasia’ na ‘maendeleo’ kilitemea mate mchakato wake chenyewe wa kidemokrasia na mshikamano kupata mgombea wake wa urais, na kukurupuka kumpitisha kada wa muda mrefu wa CCM ambaye jitihada zake kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho tawala ziligonhga mwamba.

Waliamini kwamba uamuzi wa Lowassa kuhama CCM ungekiathiri chama hicho tawala, wakitarajia vigogo kadhaa wangemfuata huo Upinzani. Badala yake, ujio wake huko ukapelekea kuondoka kwa wanasiasa wawili waliokuwa nguzo muhimu kwa Upinzani, Dkt Slaa na Prof Lipumba.Kadhalika, wanachama wengine muhimu waliohama na kujiunga na chama cha ACT- Wazalendo, ambacho hakikujiunga na UKAWA.
Kana kwamba hiyo haitoshi, makubaliano ya UKAWA kusimamisha mgombea mmoja  kila jimbo yalikumbwa na mushkeli katika majimbo kadhaa na kupelekea malalamiko yaliyosababisha ugumu katika kampeni za Lowassa.

Huko Masasi, mgombea mwenza wa Lowassa, Juma Duni, alilazimika kuokolewa jukwaani baada ya waliohudhuria mikutano wake wa kampeni kupiga kelele kuwa wataipigia kura CCM. Katika jimbo la Nzega, Lowassa alilazimika kuendesha ‘kura ya sauti’ kuwauliza waliohudhuria mikutano wake wa kampeni wanamhitaji mgombea gani kati ya wawili wa UKAWA waliokuwa wanachuana. Mpango mzima wa ushirikiano miongoni mwa vyama vinavyounda UKAWA umekwenda mrama.CCM sasa ipo katika nafasi nzuri ya kujinyakulia majimbo ambayo vinginevyo yangekwenda kwa wagombea wa Upinzani.

Lakini kilele cha unafiki wa UKAWA ni hiki. Umoja huo uliundwa ili kutetea Katiba Pendekezwa iliyoshauri muundo wa Muungano wa serikali tatu. Kanuni hiyo ya msingi iliwekwa kando pale UKAWA walipomchagua mgombea wao wa tiketi ya urais, Lowassa, ambaye alikuwa mtetezi mkubwa wa muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kwa wengi wasioendeshwa na propaganda, uamuzi wa kutelekeza suala la msingi lililopelekea umoja wa vyama hivyo, kwa ajili tu ya imani ya kufikirika ya kushinda urais, yaashiria uchu wa madaraka na sio mabadiliko yanayohubiriwa kwa wananchi.


5.    Lowassa kushindwa kufanya kampeni nchi nzima

Lowassa anaonekana kutokuwa na uwezo wa kusafiri kwa urefu na upana wa Tanzania kufanya kampeni. Mara nyingi amekuwa akitumia usafiri wa anga kwenda mikoani ambako hufanya mikutano mikubwa kwenye makao makuu ya mikoa, kutembelea majimbo mawili au matatu ya jirani kwa helikopta, na kurejea jijini Dar es Salaam. Huko Tanga, kwa mfano, alifanya kampeni katika majimbo matatu tu kati ya tisa mkoani humo. Mkoani Ruvuma, alifanya kampeni katika majimbo matatu kati ya tisa, Kigoma majimbo mawili kati ya manane, na Kagera majimbo matatu tu.

Kinyume chake, mgombea wa CCM, Magufuli amekuwa barabarani tangu Agosti 23, huku akipumzika kwa siku tatu. Anatumia usafiri wa gari, akitembelea kijiji baada ya kijiji, na kufanya mikutano kati ya minane hadi 12 kwa siku. Aina hii ya kufanya kampeni ‘kwa rejareja’ inabaki kuwa nguzo pekee ya kujihakikishia ushindi kwenye uchaguzi mkuu nchini Tanzania, hususan katika maeneo ya vijijini ambayo usikivu na kuonekana kwa vyombo vya habari ni mdogo. Wakati Lowassa anavutia wahudhuriaji wengi katika mikutano yake katika miji mikubwa, Magufuli anajipatia wahudhuriaji wengi katika kila kona ya Tanzania. Kama idadi ya wahudhuriaji katika mikutano hiyo ya kampeni inamaanisha wingi wa kura, basi kwa hakika CCM itashinda. Lakini tofauti na Upinzani, CCM haidanganyiki na wingi huo wa wahudhuriaji katika mikutano ya kampeni. Rekodi ya mahudhurio makubwa ilikuwa ikishikiliwa na Agustino Lyatonga Mrema, mgombea maarufu wa kiti cha urais kwa tiketi ya Upinzani mwaka 1995 (ambaye pia alijiunga na Upinzani akitokea CCM). Hata hivyo alishindwa kwenye uchaguzi huo. Sie twategemea kitu kingine.

6.    Mfumo imara wa CCM katika uhamasishaji kuanzia ngazi ya chini kabisa.

Katika Tanzania, vyama vichache mno vinavyoweza kuchuana na uwezo wa CCM kuhamasisha wananchi. Wakati Wapinzani huhadaiwa na ‘mahaba’ wakati wa kampeni za uchaguzi, mahudhurio makubwa kwenye mikutano yao ya kampeni na vichwa vya habari magazetini, CCM hutumika nguvu yake ya kimuundo na kuwasha ‘mashine zake za kisiasa,’ kuanzia ngazi ya mtaa (ujumbe wa nyumba kumi) kwa nchi nzima. Kimuundo, jumiya ya wanawake wa CCM (UWT) pekee ni kubwa kuliko Chadema, chama kikuu cha upinzani. CCM Haihitaji kusafiri ili kufanya kampeni. CCM ipo kila mahala, ikifanya kampeni katika makundi madogo, vijijini na mitaani, kila siku na mbali ya upeo wa vyombo vya habari. Kwa wanaofahamu muundo wa chama hicho, ushindi kwake si jambo la kushangaza.

Kwenye miaka ya 1950s, wakati wa harakati za kusaka uhuru kutoka kwa mkoloni, uwezo wa TANU kuhamasisha ulikuwa nguzo muhimu kwa Tanganyika kupata uhuru wake.CCM imerithi vinasaba vya TANU. Mwalimu Nyerere aliijenga CCM kuwa imara kwa nyakati kama hizi. Mwaka jana, huku umaarufu wake ukiwa umepungua, CCM ilimudu kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa kwa asilimia 80 dhidi ya umoja Huohuo wa Upinzani inaokabilina nao katika uchaguzi huu Mkuu.Tofauti haipo kwenye nini kinachoonekana kwenye vyombo vya habari au mitandao ya kijamii bali jinsi gani makada wa chama hicho tawala walivyofanya uhamasishaji katika kila mtaa na kijiji. Uchaguzi huo wa serikali za mitaa, ambao hufanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu, hutoa dalili nzuri kuhusu matokeo ya uchaguzi mkuu.

7.    Umahiri wa Dkt Magufuli

Mwaka jana, baadhi ya waandishi wa habari walikiri kwamba ni vigumu mno kumshambulia na kumshinda Dkt Magufuli. Ana rekodi imara ya usafi, uchapakazi na anayetaka kuona matokeo sahihi. Hajawahi kuvutiwa na harakati za kisiasa, na ilikuwa mshangao alipotangaza kuwania urais. Na alipotangaza, hakufanya mbwembwe wala kijitangaza kwenye vyombo vya habari. Alizingatia kanuni za chama kwa ukamilifu. Dkt Magufuli analeta kumbukumbu za mgombea mwingine aliyekuwa hajulikani mwaka 1995 -  Benjamin Mkapa. Wakati umaarufu wa CCM ukiwa chini, huku ikikabiliwa na upinzani kutoka kwa Naibu Waziri Mkuu aliyehama kutoka chama hicho tawala, CCM ilimchagua turufu yake ambayo ilikuwa ngumu kuikabili.Miaka 20 baadaye, ikikabiliwa na upinzani wa Waziri Mkuu maarufu wa zamani aliyehama chama hicho na kujiunga na Upinzani, CCM imefanya tena ‘vitu vyake.’ Siku zote, CCM hujua ‘kufanya pigo la haja.’

8.    Ufanisi wa CCM katika maeneo ya vijijini

Mimi ni Mbunge wa jimbo lisilo mjini, lenye idadi ya wastani ya wapigakura. Mwaka 2010, katika uchaguzi ulionekana kuwa mgumu, CCM ilishinda jimbo langu kwa asilimia 80., na kitaifa kwa asilimia 61. Hivi sasa, tunatarajia ushindi wa CCM kuwa wa asilimia 90 hivi. Tanzania ina  majimbo kadhaa yaliyo kama jimbo langu. Upinzani hupenda kuwapuuza wananchi katika majimbo yasiyo ya mijini, kama jimbo langu, kwa kudai kuwa wanaichagua CCM kutokana na ujinga wao. Wasingeweza kukosea zaidi ya hivyo.

Popote walipo, watu hupiga kura kulingana na mahitaji yao. Mwaka 2000, vijiji vinne tu katika jimbo langu ndivyo vilikuwa na umeme. Leo, vijiji 44 vina umeme. Japo hatujaweza kutoa huduma zote kwa kiwango cha kumfurahisha kila mtu, lakini hali halisi yaonyesha wingi wa wanafunzi mashuleni, walimu zaidi, madaktari na manesi zaidi, zahanati nyingi zaidi zimejengwa, huduma za mawasiliano ya simu zinapatikana kwa wingi, barabara nyingi za lami, nk. Porojo kuwa hakuna kilichofanyika Kwahiyo wapigakura wasiichague CCM haieleweki katika maoneo hayo ambay kimsingi ndiyo yenye wapigakura wengi. Na wagombea wa CCM wanaposema watafanya zaidi ya waliyokwishafanya, kwa kuzingatia mafanikio yaliyokwishapatikana, wananchi wanawaamini. Hotuba za kampeni ni mwonekano na mantiki.

Chaguzi sio kuhusu ahadi tu bali jinsi gani ahadi hizo zitaandaliwa na kutekelezwa. Jukwaa ambalo kila chama kitanadi ajenda zake za uchaguzi hujengwa wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama husika. Yahitaji mtu kuangalia tu uzinduzi wa kampeni za za Lowassa na Magufuli. Lowassa aliongea kwa dakika 9 tu  - akiahidi, pamoja na mambo mengine, kuwaachia huru wabakaji (sio kama ninazusha hili) wanaotumikia vifungo vyao na watuhumiwa ugaidi wanaosubiri kesi zao. Bila kujali alikuwa na malengo gani wakati anatoa ahadi hizo, makosa hayo hayastahili msamaha wa rais.  Kwa upande wake, Magufuli aliongea kwa dakika 58, akielezea kwa undani ajenda za maendeleo katika nyanja za elimu, ajira, afya, ufisadi, huduma za maji, na miundombinu. Kuanzia hapo, kwa muda wote wa kampeni, mwenendo umekuwa hivyo, kwa uzito wa ujumbe kwenye hotuba zake na muda wa kuhutubia

Wanaohudhuria mikutano ya Dkt Magufuli huondoka katika mikutano hiyo wakiwa na matumaini na wenye nguvu. Kwa upande mwingine, wahudhuriaji katika mikutano ya Lowassa huondoka wakiwa wamekanganywa. Siku ya kupiga kura, wapigakura wanamkumbuka jinsi mgombea alivyoonekana na alivyoongea, na jinsi walivyojisikia walipomwona jukwaani. Kwa kigezo hiki, ni bora ningekuwa upande wa Magufuli.  

9.    Uongo, uongo na takwimu

Tanzania haina utamaduni wa kura za maoni kupima nafasi za wagombea katika uchaguzi. Tuna utaratibu wa muda mrefu wa kupata maoni ya wananchi katika maamuzi makubwa ya kisera – kuingia mfumo wa vyama vingi vya siasa, marekebisho ya Katiba, na kadhalika. Mwaka 2005, kulifanyika kura ya maoni, iliyobashiri ushindi mkubwa kwa CCM. Na kwa hakika, CCM ilishinda kwa asilimia 80. Mwaka 2010, kura ya maoni iliyoendeshwa na kampuni ya Ipsos-Synovate iliashiria kuwa idadi ya kura za CCM ingepungua hadi kufikia asilimia 61. CCM ilipinga matokeo ya kura hiyo ya maoni ikidani kuwa yalikuwa kiasi kidogo sana. Matokeo ya uchaguzi huo yalikuwa kama yalivyotabiriwa katika kura hiyo ya maoni. CCM ilipata asilimia 61 ya kura zote.

Hivi karibuni, kura mbili za maoni zilichapishwa. Zote zilifanywa na taasisi huru zinazoheshimika. – Twaweza and Synovate-Ipsos tena- zote zikijihusisha na utafiti wa kusaka maoni. Taasisi mbili tofauti, zilizotumia mbinu tofauti za kufanya utafiti, katika nyakati tofauti, matokeo yaleyale. CCM itashinda kwa asilimia 62 ya kura zote.

Inaruhusiwa, na kwa yumkini ni jambo zuri, kupingana na sababu hizi tisa za kwanini CCM itashinda. Lakini namba zina tabia ya ukandamizaji. Ndio mwelekeo wa kura huwezi kubadilika. Lakini kwa kuzingatia yote yaliyokwishaongelewa kuhusu kinachodaiwa kuwa ufuasi mkubwa kwa Upinzani, basi muda huu ingetarajiwa tuwa tunajadiliana kuhusu ufuasi wa wengi kutoka Upinzani kuelekea CCM– na sio kutarajiwa ufuasi wa wengi kutoka CCM kuelekea Upinzani. Na ndiyo, kura za maoni zaweza kukosea, na tusiwekee mkazo sana.Lakini hoja hii sasa ndiyo hupendelewa zaidi na upande unaelekea kushindwa kwenye uchaguzi.


January Makamba ni Mbunge wa Bumbuli (CCM), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, na msomaji wa Kampeni za CCM 

23 Sept 2015

BAADA ya harakati na pilika lukuki za vyama vyetu na wanasiasa kusaka fursa ya kumrithi Rais wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, hatimaye tumefikia takriban mwezi mmoja tu kabla ya ‘siku ya hukumu’ kutimia.
Kufikia Septemba 23, tumebakiwa na mwezi mmoja na siku mbili kabla Watanzania hawajapiga kura kumchagua rais mpya, sambamba na kuwachagua wabunge na madiwani katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba 25, 2015.
Pengine ni mapema mno kufanya tathmini inayoweza kutoa mwelekeo wa chama kipi kitaibuka kidedea au mgombea gani wa urais atashinda, lakini angalau sote twatambua kuwa kwa upande wa urais, mshindi atakuwa aidha Dk. John Magufuli, mgombea kwa tiketi ya chama tawala CCM au Edward Lowassa, mgombea wa Ukawa kupitia Chadema.
Pamoja na changamoto nyingine zitakazomkabili mshindi katika uchaguzi huo, moja kubwa ni kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi. Sio siri kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umetugawa mno. Na sio kati ya wafuasi wa vyama pinzani tu bali hata walio ndani ya vyama husika na sie wengine tunaojitambulisha kama tusio na vyama.
Kwa upande wa CCM, mchakato wa kumpata mgombea wake umeacha makovu kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizotangulia maara baada ya chama hicho kuruhusu ushindani katika kumpata mgombea wake. Wakati CCM ilipompitisha Rais Benjamin Mkapa mwaka 1995 kulikuwa na manung’uniko kwamba kada huyo ‘alibebwa’ na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, na ‘kuwawekea ngumu’ makada wengine Kikwete na Edward Lowassa waliokuwa wakiwania fursa hiyo pia.
Mchakato wa CCM kumpata mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 uliacha majeraha makubwa zaidi, hasa kwa vile Mwalimu hakuwepo kusimamia mchakato huo, na kwa upande mwingine, Rais aliyekuwa madarakani, Mkapa, ni kama alizidiwa nguvu na kundi la mtandao wa Kikwete. Uchaguzi huo uliacha mpasuko mkubwa zaidi ambao umeigubika CCM hadi muda huu.
Lakini kilichojiri katika uchaguzi wa mwaka huu ni kikubwa zaidi kiasi kwamba kwa mara ya kwanza kabisa, chama hicho tawala kinakabiliwa na upinzani mkali ambao kimsingi ni matokeo ya mpasuko uliokigubika chama hicho tangu mwaka 2005. Kwa mara ya kwanza, CCM sio tu kinakabiliwa na upinzani uliotokana na ushirikiano wa vyama mbalimbali lakini pia mpinzani wake katika nafasi ya urais ni kada wake wa zamani, Lowassa, ambaye hadi anaondoka CCM alikuwa na nguvu kubwa kabisa katika chama hicho.
Kwa upande wa vyama vikuu vya upinzani, hali kwao pia ni tofauti kwa kiasi kikubwa. Kwa mara ya kwanza vyama vikuu vitatu, Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi, vikishirikiana na NLD, vimeweza kuruka kihunzi kilichowakwaza katika kila uchaguzi, yaani kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja. Awali, wazo zima la umoja wa vyama hivyo unaojulikana kama Ukawa, kumsimamisha mgombea mmoja lilionekana kama ndoto ya alinacha, hasa kwa kuzingatia historia. Kwamba kila jitihada iliyofanyika huko nyuma kujenga ushirikiano miongoni mwa vyama vya upinzani haukuweza kufanikia.
Lakini kadri siku zilivyokwenda, taratibu wazo la ushirikiano wa vyama hivyo likaanza kujenga picha kamili kuwa safari hii wamedhamiria kuwa kitu kimoja. Hata hivyo, kosa la msingi na ambalo pengine litawagharimu katikia uchaguzi wa mwaka huu ni kutotumia vema fursa kubwa waliokuwa nayo kukamilisha mchakato wa kumpata mgombea wao na kumnadi kabla CCM hawajafanya hivyo. Ninachomanisha hapa ni kwamba, kwa vile vyama vya upinzani vinauelewa vema mchakato wa CCM kupata mgombea wake- ni kama vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo waweza kudhani itakipasua chama hicho kikongwe- wangetumia fursa hiyo wao kujimmarisha na mgombea wao kiasi kwamba CCM baada ya kumpata mgombea wao wangekutana na mgombea wa Ukawa ambaye sio tu amejiandaa vya kutosha lakini pia anatambulika kwa wapigakura.
Hatimaye, kitendawili cha kwa nini Ukawa walikuwa wakisuasua kumtangaza mgombea wao kiliteguliwa baada ya Lowassa kukatwa CCM na hatimaye kujiunga na Chadema na baadaye kupitishwa kuwa mgombea urais. Kumbe muda wote tulipokuwa tunahoji kwanini Ukawa hawatangazi mgombea wao, wenzetu walikuwa wanamsubiri kitakachodondoka kutoka CCM.
Licha ya ujio wa Lowassa huko Ukawa kuonekana umeleta msisimko na matumaini makubwa kwamba angalau upinzani mwaka huu una mgombea ‘anayeweza kuisumbua CCM,’ kisichoongelewa sana ni mpasuko wa kawaida tu kati ya wanaodhani ni sahihi kumtumia Lowassa katika azma ya kuing’oa CCM madarakani na wale wanaoona kuwa suala hilo sio tu ni usaliti lakini pia linaonyesha mapungufu ya vyama hivyo vya upinzani, kwa maana ya kwamba ilivibidi visubiri mtu kutoka CCM ili kufanikisha azma yao ya kuingiza Ikulu.
Tukiweka kando mazingira ambayo CCM na Ukawa wamepitia hadi tulipo sasa, kuna mambo kadhaa yanaanza kujitokeza ambayo yanaweza kutoa taswira ya matokeo ya uchaguzi huo japo ni muhimu kutambua kuwa, kwanza, si rahisi kubashiri kwa usahihi kabisa matokeo ya uchaguzi wenye ushindani kama wa mwaka huu, na pili, kama wiki moja katika siasa ni sawa na takriban mwaka (kwa maana ya lolote laweza kutokea) muda uliosalia kabla ya uchaguzi ni kipindi kirefu kinachoweza kuathiri ubashiri wowote utakaofanyika muda huu.
Miongoni mwa mambo ya msingi yaliyojitokeza katika kampeni zinazoendelea ni pamoja na lile ambalo wana-Ukawa hawataki kabisa kulisikia, nalo ni mapungufu ya mgombea wao, yaani Lowassa. Sote twaifahamu CCM, na japo mgombea wake, Magufuli ni mgombea kama Lowassa, lakini kimsingi kwa huko Ukawa Lowassa si mgombea tu lakini yeye ndio kama Ukawa yenyewe. Kwa lugha nyingine, uchaguzi huu unakuwa kama vita kati ya CCM na Lowassa, hasa kwa sababu mgombea wa CCM anajinadi kichama zaidi ilhali Lowassa anajinadi na kunadiwa kama Lowassa zaidi.
Moja ya madhara ya wazi ya suala hilo ni uwezekano wa Ukawa kupoteza viti vingi vya ubunge kwa gharama ya kumnadi zaidi Lowassa. Niliwahi kuandika kwenye mtandao wa kijamii wa twitter kuwa nina wasiwasi kuwa mmoja au hata wawili wa viongozi wakuu wa vyama vinavyounda Ukawa kwa upande wa Bara, yaani Freeman Mbowe wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD, anaweza kushindwa katika uchaguzi huo. Pamoja nao ni viongozi wengine wakuu wa vyama hivyo ambao pia ni wabunge, hususan kwa upande wa Chadema.
Iwapo hilo litamtokea, na iwapo Ukawa watashindwa, basi hatma ya vyama hivyo itakuwa mbaya. Kwa Chadema, yayumkinika kuhisi kuwa salama yake pekee ni kufanikiwa kwa jaribio (experiment) la kumtumia Lowassa kuiong’a CCM. Ikishindwa, kuna uwezekano mkubwa chama hicho kikaingia katika mgogoro wa ‘kumsaka mchawi’ ambao waweza kutishia uhai wa chama hicho kilichokubali kutelekeza ajenda yake ya kupambana na ufisadi ili kumtengenezea mazingira mazuri Lowassa.
Kwa NCCR-Mageuzi, ili Mbatia aendelee kubaki kiongozi wa chama hicho itambidi lazima ashinde ubunge anaowania huku akitegemea Lowassa kushinda urais. Kinyume cha hapo yeye na chama chake watakuwa matatani, na hatma ya uhai wa chama hicho kuwa tete. Angalau kwa NLD, Makaidi anaweza kuendelea kuwa kiongozi wa chama hicho hasa ikizingatiwa kuwa kwa muda mrefu ‘chama hicho kimekuwa ni yeye na yeye ndio chama hicho,’ angalau kwa mwonekano.
Lakini kubwa zaidi ni upungufu wa Lowassa kisera na kujinadi. Ajenda ya mabadiliko imekuwa shaghala baghala kiasi kwamba watu wanaimba na kuhubiri mabadiliko pasipo hata kubainisha yatakuwaje. Ukiuliza unaambiwa la muhimu ni kuiondoa CCM kwanza, mengine baadaye. Baadaye lini? Hakuna mwenye jibu.
Kwa upande mwingine, Lowassa ameshindwa kabisa kujinadi. Haiingii akilini kuona umati mkubwa unaojitokeza kwenye mikutano yake ya kampeni ukiishia kuambulia hotuba ya dakika chache tu. Sawa, tumeshasikia hotuba nyingi za wanasiasa na nyingi zimebaki kuwa hotuba tu pasi kubadilisha chochote, lakini huu ni wakati wa uchaguzi, na hotuba ya mgombea ni fursa nzuri ya kubainisha nini atawafanyia wapiga kura na wananchi kwa ujumla pindi wakimchagua. Laiti Lowassa angetumia vema ‘mafuriko’ ya wanaojitokeza kumsikiliza, basi hata hiyo utata kuhusu ajenda ya mabadiliko isingekuwepo kwani angeweza kuwaeleza Watanzania kwa undani kuhusu suala hilo.
Kwa upande wa CCM, licha ya mgombea wake kusimama kama mgombea anayewakilisha chama na si ‘mtu binafsi,’ mtihani mkubwa umekuwa ni jinsi ya kumshambulia Lowassa pasipo kumjengea huruma kwa wapigakura. Lakini mtihani mwingine umekuwa ni kipi hasa cha kukizungumzia kuhusu Lowassa na Ukawa ambao kwa kiasi kikubwa wananadi ajenda ya mabadiliko pasi kuielezea kwa undani. Kwa kutambua hilo, Magufuli amekuwa akijinadi kwa kutumia rekodi yake mwenyewe na zile za chama chake badala ya kuelekeza mashambulizi kwa mpinzani wake. Ni wazi, ili umshambulie mpinzani wako basi angalau awe na cha maana cha kukishambulia, vinginevyo yaweza kutafsiriwa kama uonevu.
Nimalizie makala hii kwa ahadi ya kuendelea na uchambuzi zaidi kuhusu Uchaguzi Mkuu, kwa matarajio ya kuwa na nafasi nzuri ya kufanya ubashiri wa matokeo angalau siku chache kabla ya uchaguzi huo, sambamba na kukumbushana wajibu wetu kijamii kuutumia uchaguzi huo kama fursa ya kuboresha mustakabali wa Tanzania yetu.

13 Aug 2015

MAKALA hii ni mwendelezo wa ile iliyochapishwa katika gazeti hili katika toleo la wiki iliyopita. Katika makala hiyo nilijadili kwa kirefu kuhusu kile nilichokiyumkinisha kuwa usaliti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), si tu kumpokea Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa (aliyelazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu kufuatia skandali ya ufisadi wa Richmond), bali pia kumteua kuwa mgombea wake urais kupitia UKAWA.
Kadhalika, pamoja na mambo mengine, nilieleza kusikitishwa kwangu na kile nilichokitafsiri kama mwelekeo wa siasa za Tanzania yetu kutoka mfumo wa awali wa chama kimoja hatimaye vyama vingi na hiki tunachoshuhudia baada ya Lowassa kujiunga na Chadema, ninachokiita ‘chama cha mtu mmoja.’
Katika makala hii nitajadili nafasi za kufanya vizuri katika uchaguzi mkuu ujao kwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt John Magufuli, na huyo wa Chadema/UKAWA, yaani Lowassa, sambamba na vikwazo vinavyowakabili kila mmoja wao.
Nianze na Magufuli. Kwa kada huyo, binafsi ninaona kuwa ana nafasi nzuri ya kushinda hasa kwa sababu, kama alivyotamka Rais Jakaya Kikwete hivi majuzi, CCM ina uwezo na nyenzo kumwezesha mgombea wao kufanya vizuri. Vyote viwili – uwezo na nyenzo – vimeshathibitika kuwa na ufanisi mkubwa katika chaguzi zilizopita.
Na vyote viwili vipo katika pande mbili; halali na isivyo halali. Uwezo halali wa CCM unatokana zaidi na mitandao wake mpana hasa vijijini. Kwa bahati mbaya au makusudi, licha ya maeneo mengi ya vijijini katika nchi yetu kukabiliwa na umasikini mkubwa, pia yana uhaba wa ‘wasomi,’ huku wachache waliopo wakiwa aidha wamekumbatiwa na ‘mfumo unaoilinda CCM’ au wameukumbatia kwa minajili ya kulinda nafasi zao.
Ninaposema ‘wasomi’ simaanishi maprofesa au watu wenye elimu ya juu bali hata wale wenye elimu ya wastani tu ambao ni muhimu sana katika kuhamasisha na kuleta mabadiliko katika nyanja mbalimbali.
Katika mazingira ya kawaida, mtumishi wa umma kijijini anaweza kuwa na chaguo rahisi ‘kuitumikia CCM’ badala ya chama cha upinzani kwa vile hasa kwa vile katika maeneo mengi ya vijijini, ni vigumu kuitofautisha CCM na serikali.
Kuna tatizo la ziada kuhusu ‘wasomi’ wetu. Wakati katika stadi za matabaka, wasomi wanatarajiwa kuwa sio tu kiungo katika ya tabaka la walalahoi na tabaka tawala, wasomi wetu wengi sio tu hawamtaki kujihusisha na tabaka la walahoi bali pia wanajibidiisha – hata kwa kuiga tu – kuwa sehemu ya tabaka tawala. Na Wasomi wachache tulionao vijijini wanaotaka waonekane kama ‘vigogo’ au ‘vingunge’ badala ya wananchi wa kawaida au walalahoi. CCM inatambua udhaifu huu na kutumia ipasavyo.
Ikumbukwe pia kuwa wengi wa ‘wasomi’ hao ndio watumishi muhimu katika shughuli nzima ya uchaguzi, na yayumkinika kuamini kuwa wamekuwa na ‘msaada’ mkubwa kwa CCM katika chaguzi zilizopita, na wanaweza kuendelea kuwa nyenzo muhimu kwa chama hicho tawala.
Lakini pengine kubwa zaidi ni turufu ya CCM hasa katika maeneo ya vijijini kuwa ‘inaweza kuonyesha jinsi ilivyowatumikia wananchi’ tofauti na ‘vyama vya upinzani vinavyokuja kufanya majaribio ya kuongoza nchi.’ Ni hoja isiyo na msingi kwa wenye uelewa wa kuchanganua mambo, lakini kwa huko vijijini, kuipinga kwahitaji kazi kubwa na sio takriban miezi mawili iliyosalia kabla ya uchaguzi mkuu.

CCM inabaki kuwa ‘zimwi likujualo’ ilhali kwa vyama vya upinzani, tegemeo lao kubwa ni kuonyesha mapungufu ya chama hicho tawala, na kutegemea wananchi watawaelewa na kuwaamini, na ‘kucheza bahati nasibu’ ya kuwakabidhi madaraka.
Ukichanganya na ukweli usio rasmi kuwa CCM ni mnufaika mkubwa wa uhusiano wake na taasisi za serikali – Tume ya Uchaguzi, vyombo vya dola, nk – chama hicho tawala kitaingia katika uchaguzi kikiwa na nyenzo na uwezo wa kushindwa hata kama ni kwa tabu.
Kwa kifupi, mazingira yaliyoiwezesha CCM kushindwa chaguzi kuu zilizopita bado yapo na mfumo wa uchaguzi bado unakitengenezea chama hicho tawala nafasi ya kufanya vizuri.
Hata hivyo, ili Magufuli ashinde, inategemea zaidi mshikamano ndani ya CCM. Na nikiongelea mshikamano simaanishi matukio yanayoanza kujitokeza ya makundi ya wana-CCM kadhaa kuhama chama hicho na kujiunga na vyama vya upinzani. Ninamaanisha wanasiasa wenye nguvu na ushawishi katika chama hicho kumuunga mkono mgombea wa chama chao au kumsaliti.

Lakini tangu Lowassa ajiunga na Chadema/UKAWA, sijaona kile kilichotarajiwa kuwa ‘mafuriko’ ya viongozi muhimu wa CCM na maelfu ya wanachama kukiasi chama hicho tawala na kujiunga na wapinzani. Kwahiyo, yayumkinika kuhisi kuwa hadi muda huu Magufuli bado ana sapoti ya kutosha ndani ya chama chake.
Kanuni isiyo rasmi ya siasa za uchaguzi Barani Afrika ni kwamba ‘chama tawala hakishindwi uchaguzi, na kikishindwa basi si kwa sababu wapinzani wana nguvu kubwa bali migongano ndani ya chama tawala inayotoa fursa kwa wapinzani.’ Sawa, labda CCM kumkata jina la Lowassa wakati wa mchujo wa wagombea wake kumesababisha mpasuko wa aina flani, lakini kama nilivyobainisha hapo juu, mpasuko huo sio mkubwa kama ilivyotarajiwa, na sidhani kama unaweza kuwa na athari kubwa kwa CCM.
Kwahiyo, kwa upande wa Magufuli, takriban mazingira yote yaliyowawezewezesha wagombea wenzake wa nafasi ya urais huko nyuma kufanya vizuri bado yapo ilhali vikwazo dhidi ya yeye kufanya vizuri ni hafifu, na pengine vya kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Twende kwa Lowassa. Mtaji mkubwa wa mwanasiasa huyo ni umaarufu wake. Iwapo umaarufu huo unachangiwa na kinachoelezwa kuwa ni uwezo wake mkubwa wa kifedha au ‘uchapakazi’ wake, hilo ni suala linalohitaji mjadala katika makala tofauti. Lakini kilicho bayana ni ukweli kwamba umaarufu ni turufu muhimu kwa mgombea yeyote yule katika uchaguzi.

Turufu nyingine kwa Lowassa ni hali halisi ilivyo katika mahusiano kati ya CCM na Watanzania wengi. Kwa muda mrefu chama hicho tawala kimekuwa kikichukulia chaguzi mbalimbali, kuu na ndogo, kama utaratibu tu wa kukipatia nafasi za uongozi. Hakijawahi kupigania ‘kufa na kupona’ kubaki madarakani. Kwa sababu nilizozitoa hapo juu, ukichanganya na udhaifu wa wapinzani wake, bila kusahau hujuma mbalimbali dhidi yao, tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi, chama hicho tawala kimekuwa kikiingia kwenye chaguzi kikiwa na uhakika mkubwa wa kushindwa.
Hata hivyo, safari hii kinaweza kukumbana na ushindani mkubwa (japo hadi muda huu ni suala la kufikirika zaidi) baada ya kada wake maarufu kabisa, Lowassa, kujiunga na wapinzani. Sasa kwa vile CCM haijawahi na haijazowea kuwa katika mazingira yaliyopo sasa, yayumkinika kuhisi kuwa inaweza ‘kupaniki’ na hivyo kutoa mwanya kwa Lowassa na Chadema/UKAWA yake kufanya vizuri.
Lowassa na Chadema/UKAWA wanatambua bayana kuwa kuna mamilioni ya Watanzania waliokwishaichoka CCM na pengine wangependa kuoina iking’oka madarakani. Ni rahisi kwa wapinzani hao kubainisha ‘maovu’ ya chama hicho tawala kwa sababu mengi yanaonekana waziwazi. Hata hivyo, ni muhimu kukumbuka kuwa kuna ‘mazuri’ kadhaa ya utawala wa CCM, na uzoefuwaonyesha kuwa chama hicho tawala ni mahiri katika kuyanadi ‘mazuri’ hayo, ambayo pia si vigumu kuyaona.
Kikwazo kwa Chadema/UKAWA ni jinsi ya kubadili maelezo waliyoyasimamia kwa muda mrefu kuwa ‘Lowassa ni fisadi.’ Kwa mitizamo wangu, muda uliosalia haitoshi kwa vyama hivyo vinavyounda UKAWA kuwashawishi Watanzania kuwa ‘Lowassa sasa si fisadi kwa vile amejiunga nasi tuliokuwa tunapambana na ufisadi.’ Na kwa bahati mbaya, hasa kwa Chadema ambayo ilikuwa mahiri kukemea ufisadi, Watanzania wengi tu wanaonekana kutafsiri Lowassa kukubaliwa kujiunga na chama hicho ni usaliti kwa wengi waliokiamini.
Hoja kwamba ili ukiondoa CCM kuna haja ya kushirikiana na watu kama Lowassa inakabiliwa na hoja mbadala kuwa ‘kwanini tuwaamini watu msio na uwezo wa kuleta mabadiliko wenyewe hadi mtegemee makapi ya CCM?’ Hoja hiyo mbadala inapewa nguvu na ukweli kuwa UKAWA ‘walisuasua’ kwa muda mrefu kutangaza mgombea wao, na sasa twajua kuwa walikuwa wanamsubiri mwana-CCM kama Lowassa awasaidie.
Lakini mtihani mwingine kwa UKAWA na Lowassa ni huu: Magufuli anagombea urais kwa tiketi ya CCM, ambayo sio tu ni chama tawala na ambacho kipo madarakani hata kabla ya ujio wa mfumo wa vyama vingi, lakini pia kinafahamika kwa wengi. Kwa UKAWA, na hili ni kosa lao kwa kuchelewa kupata mgombea wao wa kiti cha urais, inaonekana kama ni chama ‘kipya’ cha siasa. Laiti muungano huo wa vyama vinne vya siasa (Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD) ungepata mgombea wake mapema, na kumnadi kwa nguvu wakati CCM inahangaika kupata mgombea wake, basi muda huu wangekuwa na kazi moja tu ya kupambana na Magufuli na CCM kwani wao tayari wangeshakuwa wanajulikana kwa wengi.
Vilevile, kuna suala nililozungumzia katika makala iliyopita ambapo, dalili zilizopo zinaashiria uchaguzi wa rais ni katika ya CCM na Magufuli wake dhidi ya Lowassa. Hapa ninamaanisha kwamba ni rahisi kumwona mgombea huyo wa CCM kama anayewakilisha chama chake ilhali kwa Lowassa ni kama ‘mgombea binafsi.’ Utafiti kidogo tu katika vyombo vya habari waweza kukuonyesha msomaji kuwa wakati ‘kampeni’ za CCM zimeelemea zaidi katika kumnadi Magufuli na CCM, kwa Chadema/UKAWA ni suala la kumnadi Lowassa pekee kana kwamba ni mgombea binafsi.
Na hilo linachangiwa na ukweli kuwa UKAWA si chama bali ushirikiano wa vyma ambavyo awali lengo lao lilikuwa suala la mabadiliko ya Katiba. Vyama hivyo vina sera tofauti, na japo vyawezxa kutengeneza ilani moja ya uchaguzi, muda hauko upande wao. Kwa CCM, ni mwendelezo tu wa walichokifanya mwaka 1995, 2000, 2005 na 2010.
Kadhalika, wakati nimetaja kuwa umaarufu wa Lowassa ni mtaji wake mkubwa huko Chadema/UKAWA, pengine ni mapema mno kuhitimisha kuwa umaarufu huo alioupata akiwa CCM, utaendelea kuwa juu wakati huu amejiunga na Chadema/UKAWA. Ikumbukwe kuwa wapinzani wakubwa wa Lowassa alipokuwa CCM hawakuwa ndani ya CCM bali katika vyama hivyohivyo ambavyo leo vimemfanya mgombea wao wa urais. Hilo laweza kuirahisishia CCM jukumu la kumbomoa kwani ‘wanamjua vilivyo.’
Kikwazo kikubwa lakini kisicho wazi ni nafasi ya Idara ya Usalama wa Taifa katika uchaguzi huo, kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizopita. Hata tukiweka kando kile kwenye Baiolojia wanakiita ‘symbiotic relationship’ (uhusiano wa kutegemeana kati ya kiumbe kimoja na kingine) ambapo ustawi wa taasisi hiyo na wa CCM na serikali zake ni wa kutegemeana, Idara hiyo yaweza kutumia ‘kisingizio’ kama ‘Lowassa ni tishio kwa usalama wa taifa letu,’ ambapo kwa taratibu zisizo rasmi za Usalama wa taifa sehemu nyingi duniani, anaweza ‘kudhibitiwa.’ Hili ni gumu kulieleza kwa undani kutokana na sababu za kimaadili.
Nihitimishe makala hii ndefu kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi zaidi kuhusu uchaguzi mkuu kwa ujumla, hususan katika nafasi ya urais, hasa ikitarajiwa kuwa tunaweza kushuhudia mengi zaidi ya tukio lililogusa hisia za wengi la aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba kujiuzulu ghafla, sambamba na ‘sintofahamu’ kuhusu hatma ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dkt Willibrord Slaa.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.