16 Oct 2011




Tuhuma za kuuawa kwa Mwakyembe na wenzake kwa IGP na Mwandishi wetu FEBRUARI 8, mwaka huu, Dk. Mwakyembe alizungumza na baadhi ya viongozi waandamizi wa Jeshi la Polisi makao makuu ya jeshi hilo jijini Dar es Salaam. 

Baada ya maelezo hayo, polisi walimtaka aweke madai yake kwenye maandishi na siku moja baadaye Dk. Mwakyembe aliwasilisha taarifa yake ya maandishi. 

Dk. Mwakyembe amesema kwenye barua hiyo, “Pamoja na kwamba taarifa hii ni mpya yenye matukio ya takriban mwezi moja tu, naamini kwa dhati kuwa msingi wake (kwa maana ya wahusika na maudhui) hautofautiani na ule wa matukio mengine ya awali ambayo baadhi yake yalisharipotiwa polisi na vyombo vingine vya usalama kwa lengo la kuchunguzwa. 

Maelezo ya Barua ya Mwakyembe “Bado nina imani kubwa na Jeshi letu la Polisi kwamba litaifanyia kazi taarifa hii bila kujali nguvu ya ukwasi na ya kisiasa ya watuhumiwa na kwa kuzingatia misingi ya haki na ukweli. 

“Msingi wa mimi kushtuka na kuamua kulivalia njuga suala hili kwa kuwataarifu watu mbalimbali wenye uelewa na kuvitaarifu vyombo vya dola, ni taarifa nilizozipata kutoka Songea Januari 22, 2011 kuhusu kundi la watu saba lililoingia mjini humo usiku wa Januari 21, 2011 kwa gari iliyodaiwa kuwa ya wizara yangu (Ujenzi) aina ya Land Cruiser yenye usajili nambari STK 68… (ambayo kipindi fulani katika safari hiyo ilibadilishwa namba yake kuwa STK 68…). 

Gari hiyo iliwateremsha “abiria” hao saba sehemu iitwayo Madaba na baadaye kuchukuliwa na gari nyingine (Hardtop Land Cruiser yenye namba za usajili T7…BDU) hadi Top Inn ya mjini Songea. “Majina ya baadhi ya watu hao saba ni Wasomali wawili Hafidh na Faraj; kijana wa Kichagga kwa jina Mustafa a.k.a “Master”; Mkusa, jamaa ambaye wenzake wanaamini kuwa yuko Usalama wa Taifa; na mtu mwingine (jina tunalo) kutoka Tanga anayedaiwa kuwa na utaalamu mkubwa wa kukaba watu. 

“Mwenyeji aliyewapokea Songea watu hao saba ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya (kaitaja) akiongozana na mtu aitwaye Manya. Kilichowafanya baadhi ya watu waanze kulidadisi kundi hili ni dhamira ya safari yao. Tetesi zilisema walikuwa wanaelekea Mbunde kwa mganga maarufu wa kienyeji kwa jina (linahifadhiwa). Hivyo, udadisi ukaongezeka kujua nani anakwenda “kulogwa” safari hii. 

Tetesi zikarejea na jina langu na msululu wa majina mengine: Dk. Slaa (Willibrod), Anne Kilango - Malecela, Reginald Mengi, Profesa Mwandosya na Benard Membe. “Pamoja na kwamba sina imani na ushirikina au nguvu za giza, kutajwa kwa jina langu na fursa ya pekee niliyokuwa nayo ya kujua kilichokuwa kinafanyika, kukanipa ari, nguvu na shauku ya aina yake kutaka kulielewa zaidi suala hili ili ikibidi, niwataarifu wenzangu nao waelewe. 

“Usiku wa Jumamosi Januari 22, 2011 kundi hilo lilielekea Mbunde, wilayani Namtumbo, (kwa gari aina ya Defender STK 26…, likiendeshwa na (jina tunalo) kukutana na ‘mganga’ …ambaye anaishi ndani ya Selous Game Reserve With Impunity. Defender hiyo iligeuza kurejea Songea siku mbili baadaye na kuwaacha ‘wageni’ hao kwa mganga ambako walikaa siku saba ‘wakitengenezwa’. Walirejea Songea Januari 29, 2011 na kesho yake Januari 30, 2011 wakaanza safari ya kurejea Dar es Salaam. 

“Kutoka Songea hadi Mafinga walitumia ile Hard Top iliyowatoa Madaba hadi Top Inn ya Songea (T7… BDU). Walifika Mafinga milango ya saa mbili usiku na kukuta gari mbili zikiwasubiri: Hilux Mayai ya (kampuni moja) na Defender iliyowaongoza hadi Morogoro. Walipokewa Morogoro na askari (jina tunalo). 

Hapo kundi likagawanyika: watu wanne wakiwemo wale Wasomali wawili wakaingia kwenye Nissan Patrol (T8… ADH) mali ya (kampuni jina tunalo) na wengine wakabaki Morogoro. “Kufuatana na ‘mganga’ mwenyewe, ambaye wapelelezi wako wanaweza kuongea naye kama walivyofanya walionipa taarifa hizi, aliwapa masharti ya kutotumia silaha za moto ila njia nyingine kumuua kwanza Mwakyembe, baadaye Slaa, n.k., n.k, n.k. kwa zamu; alitengeneza dawa ya kuwapooza wale wengine (wanaosubiri) kwenye orodha ya kuuawa (Dk. Slaa, Anne Kilango, Mengi, Mwandosya na Membe) wasitaharuki na kupiga kelele za nguvu hata kuamsha hasira za wananchi mauaji yakitokea; aliwazindika vilivyo wasiweze kudhuriwa na tendo la kuua na alitengeneza dawa ya kuwapumbaza “waliohukumiwa kifo” (wawe mfano wa mbwa mbele ya chatu). 

“Jijini Dar es Salaam ‘wahitimu’ hao walifikia Kiwalani karibu na kiwanda cha Mohamed Enterprises. Jirani na kiwanda hicho kuna jengo la ghorofa: Februari 5, 2011, wageni wawili zaidi waliwasili kwa ndege kutoka Uganda; mwanaume mmoja (aliyechanganya rangi) na mwanamke mmoja (mweusi vilivyo). Walipokewa na gari mbili: moja ya polisi (PT 02…) na ya pili yenye namba za kibalozi (aina ya RAV 4). 

Ushiriki wa Al Shabaab “Jioni wakawa na mazungumzo ya kina na Wasomali wawili niliowaelezea awali ambao inadaiwa ni wapiganaji wa Harakat al-Shabaab al- Mujahideen (kwa kifupi Al- Shabaab). “Niliweza kupata picha pana zaidi kwa nini wapiganaji wa kikundi hicho (kinachopambana na wanaodhaniwa kuwa maadui wa Uislamu) wameingizwa nchini. 

Nimeweza kukusanya taarifa zinazodai kuwa awali walifikiriwa kuletwa wapiganaji kutoka Rwanda, lakini wazo hili lilikataliwa na wafadhili wa mpango huu ambao walitaka ‘wanaharakati’ wa aina hiyo watoke Somalia. Ndipo kikundi hicho kikashawishiwa kwamba Tanzania kuna tatizo la udini la Uislamu kutishiwa. 

Mimi na wenzangu hao watano tumejengewa hoja kuwa maadui wa Uislamu tunaotumiwa na makanisa, hivyo hatuna budi kukatishwa maisha yetu. “Niliweza vilevile kupata picha kuwa wafadhili wa kundi hili, wana mahusiano ya karibu na Sheikh …(jina tunalo) ambaye baadhi ya utabiri wake unatokana na agenda za wafadhili hao. 

Inadaiwa kuwa utabiri wa sheikh … mwaka jana ulimlenga Dk. Slaa ambaye alidaiwa kubebwa na makanisa. “Utabiri” huo haukutimia kwa kuogopa kuiingiza nchi kwenye machafuko makubwa ya kisiasa/kidini ambayo yangewaweka pabaya hata wafadhili wa mpango huo. “Inadaiwa kuwa Sheikh … ameombwa tena kutoa utabiri wa mwanasiasa na kiongozi mmoja kupoteza maisha mwezi huu (Fabruari). 

Inadaiwa kuwa mwanasiasa huyo anayetembea na kifo ni mimi na tayari maandalizi ya ‘hukumu yangu’ yamefanywa: “(a) Kijana mmoja kwa jina la Hassan alitumwa kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma siku ya Jumamosi Februari 5, 2011 kwa “maandalizi” hayo (mahali pa kufikia kikosi hicho cha mauaji, utambuzi wa nyumba ya kuishi niliyopangiwa na kumtafuta mhudumu mmoja wa Bunge ili ile ‘portion’ ya mganga ya kunipumbaza kabla ya hukumu, iweze kunyunyizwa kwenye kiti changu Bungeni); “(b) Kesho yake (Jumapili) Februari 6, mnamo saa nne usiku, kikosi hicho cha mauaji kikiwa na watu watano kiliondoka Dar es Salaam kwenda Dodoma kwa gari aina ya Land Cruiser nyeupe ya mkongo (T3… AKU) na kimejichimbia Dodoma mpaka leo (Februari 9). 

“Waliomo kwenye kikosi hicho ni Wasomali wale wawili, mgeni moja (wa kiume) kutoka Uganda, Mustafa a.k.a “Master” na kijana mmoja ambaye Januari 19, 2011 aliwabeba Wasomali hao kutoka Morogoro hadi Ununio kupitia Kibaha na Baobab kwa gari aina ya VX Land Cruiser (T6…APF). Kijana huyo ana shepu ya Kitutsi na anaongea Kifaransa. 

“Utabiri atakaoufanya Sheikh … (pengine aamue kuachana nao sasa baada ya kubaini kuwa tunaujua) utakuwa na lengo la kuwapumbaza wananchi waelekeze macho na masikio yao zaidi kwenye utabiri wake kuliko kwenye njama za kundi hilo za muda mrefu za mauaji. “Kila siku ya Mungu napata taarifa za ziada kutoka kwa raia wema kuhusu suala hili. 

Naziingiza kwenye taarifa hii ili ziwasaidie katika upelelezi: “Inadaiwa kuwa Wasomali hao waliingia nchini kutokea Kenya na wakaja kwa barabara hadi Dodoma. Walitumia gari aina ya RAV4 (new model – T8… AQS) Januari 8, 2011 na kusafirishwa hadi Morogoro ambako walipokewa na askari niliyemtaja awali… wa polisi Morogoro. “Mjini Morogoro, walikaa hoteli mbili tofauti: Hilux Hotel Morogoro na Top Life. 

Aliyewafanyia Wasomali hao booking hapo Top Life ni mmiliki wa hoteli ya….(jina la hoteli na mmiliki tunalo). “Magari waliyotumia wakiwa Morogoro ni RAV4 T8… AQS, VX Land Cruiser STK 1…, Mercedes Benz (Station Wagon) T8… BDT, Toyota Mark II GX100 nyeupe T2… BKR na wakiwa Dar es Salaam wametumia magari VX Land Cruiser T6… APF, Nissan Patrol T8… ADH.” 

“Naomba nihitimishe maelezo haya kuwa nimekuwa muwazi kwa asimilia 100 na hata vyanzo vyangu vya habari ni miongoni mwa watu hao niliowataja katika taarifa hii ambao naamini utachukua hatua ya kuwahoji kulipatia ufumbuzi suala hili. 

“Suala la msingi hapa, si uhai wangu, kwani iko siku lazima nitakufa kama ambavyo hao mafisadi wanaodhani wanaweza kufadhili vifo vya wenzao watakavyokufa hata wao hatimaye, watake wasitake, hakika ni suala la muda tu. Suala la msingi hapa ni mustakabali wa taifa letu, taifa aliloliasisi Mwalimu Nyerere na kulilea kwa misingi ya usawa, haki, umoja, amani na utulivu. 

“Nimejieleza awali kuwa nina imani kubwa na Jeshi letu la Polisi kwamba litaifanyia kazi taarifa hii bila kujali nguvu ya ukwasi na ya kisiasa ya watuhumiwa na kwa kuzingatia misingi ya haki na ukweli. 

“Hata hivyo nalazimika kusema nitasikitika sana ikiwa taswira ya ‘ukorofi’ niliyopewa kwenye kesi moja ya awali (2009) itapewa nafasi kwenye suala hili, hivyo kuninyima fursa ya kusikilizwa vizuri na ulinzi ninaostahili kama raia Kikatiba na kisheria. Niko tayari wakati wowote na mahali popote kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi litakaponihitaji.”

CHANZO: Jamii Forums

Kitu cha karibu na taaluma ya uchumi nilichomudu kukisoma ni Book Keeping(ambayo niliambulia C kwenye mtihani wa Kidato cha Nne) na Commerce (ambayo niliachana nayo Kidato cha Pili).Naomba nikiri,mie ni kilaza wa hesabu,na alama D niliyoipata katika Hisabati kwenye Mtihani wa Kidato cha Nne ilikuwa ni kama A kwangu kwani nilikuwa natarajia F.Sasa kwenye uchumi kuna mambo ya Statistics,which means namba (hesabu).Kuashiria udhaifu wangu kwenye namba,wakati ninasoma shahada ya pili ya uzamili (Shahada ya Uzamili ya Utafiti katika Utafiti wa Siasa-Master of Research in Political Research) nililazimika kuomba ku-drop somo la Quantitative Analysis.Aibu?No,ni ukweli huo!

Anyway,lengo la post hii sio kuzungumzia udhaifu wangu wa namba wala kuelezea kuhusu shule yangu bali ni swali linalonisumbua kuhusu kinachoendelea katika sehemu nyingi za nchi zilizoendelea ambapo kumekuwa na upinzani mkali dhidi ya uroho wa taasisi za fedha (mabenki,nk).

Lakini pengine kabla ya kuelekea huko,swali la msingi linaweza kuwa hili.Inakuwaje nchi kama Ugiriki ikumbwe na msukusuko wa kiuchumi ilhali akina sie (Tanzania) tunaonekana kama "tunapeta" tu?Pamoja na Ugiriki,nchi nyingine ambazo zinasumbuliwa na kuyumba kwa uchumi ni pamoja na Hispania,Ureno,na Italia (ambazo pamoja na Ugiriki zinaunda kinachoitwa PIGS-Portugal,Italy,Greece na Spain).

Hebu wachumi nifahamisheni.Hivi hao PIGS si wapo bora zaidi kiuchumi ukilinganisha na nchi kadhaa za Afrika?Sasa mbona sie tupo kama hakuna tatizo la uchumi?Au sie ni sugu?Au uchumi wetu ni kama haupo?

Halafu kuna hili la harakati dhidi ya uroho wa taasisi za fedha ambazo kwa kimsingi zimeanzia mtaa wa Wall (Wall Street) jijini New York na kupewa jina la Occupy Wall Street,na sasa zinaelekea kusambaa sehemu mbalimbali duniani kama picha zifuatazo zinavyoonyesha.Je,kwanza,kuna uwezekano wa harakati hizo kuhamia nchi masikini?Pili,kwani hazijatugusa hadi sasa?Au ni yale yale ya uchumi usiokuwepo na hivyo kutokuwa na umuhimu wa kuulalamikia?

Nitashukuru sana kama kuna mchumi yeyote atakayeniandikia kwa barua pepe [email protected], kisha nitachapisha hapa,na ninaahidi kuandika makala kwenye jarida la Raia Mwema na kumtaja mchumi mwenye jibu mwafaka

Enewei,hebu tuangalie picha za harakati za "Occupy Wall Street" zilivyosambaa sehemu mbalimbali duniani



 Wall Street,New York,Marekani

 Tokyo,Japan

 Seoul,Korea ya Kusini

 Sydney,Australia

  Sydney,Australia

 Hong Kong

 Zurich,Uswisi

 Seoul,Korea ya Kusini

 Roma, Italia

 Hong Kong

 Frankfurt,Ujerumani

 Roma, Italia

 Stockholm, Sweden

 London,Uingereza

 London,Uingereza

 Sydney, Australia

 Hong Kong

 Julian Assange na waandamani jijini London
 London
London

15 Oct 2011


Simba,Nyati,Faru,Chatu....haya ndiyo majina ya wanyama yanayoweza kukujia akili pindi ukiulizwa MNYAMA YUPI NI HATARI ZAIDI KWA MWANADAMU.Well,amini usiamini,kiumbe hatari zaidi ni mdogo mara elfu kadhaa akilinganishwa kiumbo na hao majabali tunaowafahamu.Na udogo wake si katika umbile pekee bali pia hata sauti yake ni ndogo kulinganisha na mbwa,paka au mbuzi,achilia mbali wababe kama Simba,Chui au Faru.Kiumbe huyo hatari wa kuogopwa kwa gharama yoyote ile ni MBU.

Kwa mujibu wa takwimu,Mbu ni kiumbe hatari zaidi kuliko wote duniani.Kiumbe huyo hatari ni maarufu kwa kuambukiza rundo la magonjwa,kubwa zaidi ikiwa ni homa ya malaria.Lakini pia mbu hueneza homa ya matende (elephantiasis), homa ya manjano (yellow fever),kindiga popo (dengue fever) na homa ya Mto Nile.

KESI DHIDI YAKE: Mbu anawajibika kusababisha kati ya vifo milioni2 hadi 3 kwa mwaka.

VIJIWE (Hangout) VYAO: Takriban dunia nzima lakini zaidi barani Afrika, Asia na Amerika ya Kaskazini

ANAVYOSABABISHA MAAFA:Mbu huambukiza maradhi ya kuuma kwenye ngozi ya binadamu na kumwaga mate yake yenye vijidudu vinavyosababisha homa husika.Ukiweka kando vipele vidogo vinavyotokea mahala alipouma mbu,anayeambukizwa na mbu hatambua maambukizo hadi pale kinga za mwili inaposhtuka (na kuleta dalili mbalimbali).

JINSI YA KUMKWEPA: Njia ya kupambana na mbu na maambukizo ni pamoja na  kutumia chandarua kilichomwagiwa kinga,kuangamiza sehemu za mazalio ya mbu na vidonge vya kinga.
------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Nyoka Wenye Sumu Kali

Japo kuna zaidi ya aina 2,000 za nyoka, 450 kati yao wenye sumu,ni aina 250 tu kati yao ndio wenye uwezo wa kuua binadamu.

KESI DHIDI YAO: Nyoka wenye sumu kali husababisha kati ya vifo 50,000 na 250,000 kwa mwaka.

VIJIWE VYAO: Zaidi ni Afrika,Asia na Amerika ya Kaskazini

WANAVYOSABABISHA MAAFA: Nyoka wana kasi sana na sehemu yoyote katika mwili wa binadamu inaweza kuwa kugongwa na kiumbe huyo hatari.Lakini ni hatari zaidi nyoka anapomgonga mtu kwenye mshipa wa damu kwani hiyo huharakisha kusambaa kwa sumu ya kiumbe huyo.Nyoka hutumia sumu yao kumlegeza mtu na pengine kumpotezea fahamu.Majoka makubwa kama Mfalme Kobra (King Cobra) yanaweza kusimama hadi usawa wa kichwa cha binadamu,huku wengine wakiweza kutema na kurusha sumu yao kutoka mbali kwenda kwenye macho ya mwanadamu.

JINSI YA KUWAKWEPA: Mara nyingi nyingi nyoka hushambulia pale tu pale anapobughudhiwa.Kwahiyo ushauri muhimu wa kuepuka shambulizi kutoka kwa viumbe hao ni kujiepusha nao (Stay away!).Pia ni muhimu kuvaa mabuti kwenye mazingira yanayoweza kuwa na nyoka.Epuka mapori yanayoweza kuwa makazi ya nyoka.Na ikitokea umeomwona nyoka,inashauriwa urudi kinyumenyume taratibu kwani anaweza kujirusha mara nusu ya urefu wake,na mtikisiko kidogo tu unaweza kumasha hasira za kiumbe huyo hatari. 
------------------------------------------------------------------------------------------------------------
Nge 

Ni kiumbe hatari mwenye sura mbaya maradufu.Inaaminika kuwa ng'e anaweza kuwa anasababisha vifo vingi zaidi ya vile vinavyorekodiwa rasmi,sababu ya kuhisi hivyo ikiwa ni mazingira wanayoishi viumbe hao na ugumu wa kupatikana tiba dhidi ya sumu yao.Hata hivyo,japo kuna aina tofauti 1500 za ng'e ni 25 tu kati yao ambao ni hatari kwa uhai wa uhai wa binadamu.

KESI DHIDI YAO: Ng'e husababisha kati ya vifo 800 hadi 2,00 kwa mwaka

VIJIWE VYAO: Duniani kote hususan Afrika,America ya Kusini na Kaskazini na Asia ya Kati.

WANAVYOSABABISHA MAAFA: Ng'e humlegeza binadamu baada ya kumdunga sumu kwa kutumia "vijisindano" vilivyopo kwenye mikia yao.Kama ilivyo kwa sumu nyingine za wadudu/wanyama,binadamu walio hatarini zaidi ni wale wenye aleji,japo ng'e wengi wenye sumu wanaopatikana Afrika wanaweza kumdhuru mtu yeyote yule.

JINSI YA KUWAKWEPA: Ng'e huwa active zaidi nyakati za usiku na hupendelea kujipumzika mchana.Kwahiyo ni muhimu kuhakikisha sehemu ya kujilaza ipo salama kabla ya kuubwaga mwili.Kadhalika ni muhimu kupunga mavazi na/au soksi kuhakikisha hakuna ng'e humo,vinginevyo itakuwa balaa.
---------------------------------------------------------------------------------------------------------
WENGINEO KWA KIFUPI

Paka Wakubwa (Simba,Chui,nk)


Paka Wakubwa (kwa mfano yaani Simba,Chui,nk) husababisha takriban vifo 800 kwa mwaka
---------------------------------------------------------------------------------------
Mamba
Mamba husababisha kati ya vifo 600 na 800 kwa mwaka
-------------------------------------------------------------------------------------
Tembo
Pamoja na upole wao,Tembo husababisha kati ya vifo 300 na 500 kwa mwaka
---------------------------------------------------------------------
Kiboko
Mwamba huyo wa majini mwenye sura mbaya husababisha vifo kati ya 100 na 150 kwa mwaka
--------------------------------------------------------------------------------------
Konyeza (jellyfish)
Kiumbe huyu wa baharini husababisha takriban vifo 100 kwa mwaka
-----------------------------------------------------------------
Papa
Kiumbe huyu hatari wa baharini husababisha takriba vifo 100 kwa mwaka
----------------------------------------------------------------------
Panda
Husababisha kati ya vifo 5-10 kwa mwaka
-------------------------------

CHANZO: Habari hii imetokana na vyanzo mbalimbali mtandaoni

14 Oct 2011





Mbunge wa Jimbo la Mvomero, Amos Makalla (wenye suti) akiangalia uzio uliowekwa na mwekezaji katika Kitongoji cha Kinyenze, Kijiji cha Kipera, Wilayani Mvomero, Mkoa wa Morogoro na kuziba njia inayokwenda katika mtaa wa Mwanga  na katika mashamba. Pia mwekezaji huyo raia wa kigeni amechukua sehemu ya mashamba ya wananchi hao bila ya taarifa yeyote kwa Halamashauri ya Kijiji na wananchi.

--
*Mroki Mroki
*
*Director MD Digital Company*
*General Secretary PPAT*
*Professional Photojournalist & BLOGGER
P.O.BOX 110097,*
*Mob: +255 755 373999 */*+255 717 002303,*
*DAR ES SALAAM, TANZANIA*
**

13 Oct 2011


Kuna tofauti kati ya kujipa ujiko na kuongea ukweli.Na japo kujipa ujiko si dhambi as long as ujiko huo ni stahili,lakini ukweli ni shurti usemwe hata kama utaleta tafsiri ya kujipa ujiko,which as pointed out earlier sio kosa la jinai.

Nimekuwa kwenye ulingo huu wa kublogu kwa kitambo sasa.Mara ya kwanza niliandika post ya kwanza bloguni mwezi April mwaka 2006-yaani miaka mitano iliyopita.Lakini mie si muumini sana wa maadhimisho na ndio maana hata blogu hii ilipotimiza miaka mitano nilisahau kuandika chochote kile.Kwa kawaida siku zangu za kuzaliwa husherehekewa kwa sala na simu kwa mzazi,na zaidi ni tafakuri ya wapi nimetoka,nilipo na niendako.Kuna maana gani ya "kusumbua dunia nzima" kwa vifijo na vigeregere kisa umetimiza miaka 50 ilhali akili yako ni haba zaidi ya mwenye miaka 10? (huo ni mfano tu,don't get me wrong).

Anyway,leo nimeamua kuweka flashback ya makala yangu ya kwanza kabisa katika blogu hii.Kimsingi,makala hiyo haikuwa kwa minajili ya kuwekwa bloguni kwa sababu niliiandika kwa ajili ya makala zangu kwenye lililokuwa gazeti maarufu la kila wiki huko nyumbani la KULIKONI.Na ni makala hizo ndizo zilizozua jina la KULIKONI UGHAIBUNI (ie safu hiyo ilibeba jina hilo la Kulikoni Ughaibuni)

Anyway,makala husika ni hii hapa chini

KULIKONI UGHAIBUNI


Asalam aleykum waungwana.

Nadhani kabla ya kubwabwaja mengi ingekuwa ni vema tukatambuana. Lakini kabla ya hapo, ngoja nikunong’oneze kitu kimoja kuhusu gazeti hili mwanana la KULIKONI.Hili sio gazeti la kawaida. Japokuwa hili ni toleo la pili tu, lakini nimeshuhudia kwa macho na masikio yangu maelfu kwa maelfu ya wapenda habari wakisema kwamba gazeti hili tayari limeshakidhi kiu ya wasomaji japo ndio kwanza linaanza. Na nawahakikishia wenye mtizamo huo kuwa hawajakosea. Ama kwa hakika huu ni mwanzo wa tofauti na mazoea. Japokuwa yapo baadhi ya magazeti yanayotoka mara moja kwa wiki ambayo ukilikosa linapotoka usitarajie kulipata siku inayofuata, kwa KULIKONI ukilikosa Ijumaa basi uwezekano wa kulipata kesho yake ni finyu sana. Kwa kifupi, ni gazeti linalokidhi matakwa ya kila aina ya msomaji: mtu mzima kwa kijana, kinababa kwa kinamama, waliojiajiri kwa walioajiriwa, na kadhalika na kadhalika.

Nirejee kwenye kujitambulisha. Mimi ni Mtanzania mwenzenu, na hadi naandika makala haya nipo hapahapa nchini, lakini nitakuwa nikiwaletea makala kutoka huko Ughaibuni ninakoishi. Naamini kuna mengi yanayotokea huko Ughaibuni ambayo ninyi wasomaji watukufu mngependa kuyapata sio kwa mtizamo wa CNN, Newsweek au Times, bali kwa mwenzenu ambae anayaona katika macho ya ki-Tanzania. Labda nifafanue. Mara ya kwanza nilipoombwa sigara na Mzungu nilidhani ni utani. Nilipompatia alinishukuru nusura anilambe miguu.Kumbe yule Mzungu alikuwa ombaomba kama rafiki yangu Matonya (japo ile staili ya Matonya inaweza kuwa kali kuliko zote ulimwenguni).Nilipokutana kwa mara ya pili na jamaa yule alieniomba sigara ,ambapo safari hii aliniomba pauni moja,ndipo nilipogundua huenda akawa ni ombaomba kweli.Uthibitisho niliupata nilipokutana nae kwa mara ya tatu lakini safari hiyo nikiwa na rafiki yangu mmoja Mghana ambae alikuwa hapo Ughaibuni kabla yangu.Huyo mjukuu wa Kwame Nkrumah ndiye alienithibitishia kuwa hapo Uingereza kuna ombaomba lukuki.Niliposimulia hadithi hiyo kwa jamaa zangu hapa baadhi walinibishia.Na walikuwa na hoja.”Mbona tunaangalia BBC kila siku na tunaowaona ni wazungu wanaoonekana kuwa hawana shida hata kidogo”,ilikuwa hoja ya mmoja wao.Ukweli ni kwamba hawa wenzetu wanapenda zaidi kuonyesha yale wanayoyaona kuwa yanaleta picha nzuri ya nchi zao.Angalau balaa la Katrina lilisaidia kuwafumbua macho watu kwamba hata huko kwa George Bush kuna masikini kama hapa kwetu,na wamesahaulika.

Kwa hiyo basi,makala hii itawasaidia Watanzania wenzangu kujua mambo mbalimbali-mazuri kwa mabaya-yanayojiri huko Ughaibuni ambayo ni nadra kwa mtu wa kawaida kuyapata.Naahidi wasomaji watukufu kwamba kama ambavyo hamtopenda kukosa nakala za KULIKONI basi ndivyo hamtotaka kukosa uhondo nitakaokuwa nawaandalia kutoka huko nje.Kama azma ya gazeti hili ilivyo-kuupatia umma chakula cha kila wakati-nami nitahakikisha nawapatia mlo wa kila wakati.Labda tofauti itakuwa ni kwamba mlo huo unaandaliwa kutoka nje.Lakini ugali si ugali tu.Ukitoka Uingreza au ukipikwa Manzese si bado ni ugali.Cha msingi upikwe kwa kuzingatia kanuni za upishi wa ugali.Pengine kingine ni kwamba mapishi haya ya kutoka nje yatakuwa tofauti ni yale uliyoyazowea.Haya yatamlenga mlaji wa kawaida.Kwa ufafanuzi,ni kwamba utofauti wa makala hii ni kwamba kama lilivyo gazeti lenyewe,itakuwa tofauti ni makala mlizozizowea katika baadhi ya magazeti ya kila wiki.Na tofauti yenyewe ni kwamba kipaumbele kitawekwa kwa watu wa kawaida na mambo ya politiki yatakuja tu pale yanapowagusa watu wa kawaida.

Basi hadi Ijumma ijayo,nawaomba make mkao wa Kula ambapo makala motomoto zitaanza kuwajia kutoka Ughaibuni.Ahadi yangu na ya timu nzima ya KULIKONI ni kubeba sauti za watu wa kawaida,na kwahakika hilo linawezekana.

Alamsiki





Kabwe ZuberiZitto, Mb



WaziriKivuli wa Fedha na Uchumi



TAARIFA KWAVYOMBO VYA HABARI



Waziri wa Fedha ndugu Mustafa Mkulo akae pembeni kupishauchunguzi dhidi yake kuhusu Shirika la CHC.

Katika Mkutano wa Nne wa Bunge la Kumi kulitokea malumbano makali kati ya Serikali na Wabunge wajumbe wa Kamati yaHesabu za Mashirika ya Umma kuhusu kuongezwa muda wa Shirika la CHC. WakatiWaziri wa Fedha alileta Azimio la kulivunja Shirika hili lenye taarifa nyingina nyeti kuhusu zoezi la Ubinafsishaji, Kamati ya Bunge ya POAC kutokana nauzoefu wake wa kukagua mahesabu ya Mashirika ya Umma na kufuatilia zoezi laUbinafsishaji wa Mashirika ya Umma, ilipinga hatua hii na kulitaka Bungekukataa Azimio la Serikali na kulifanyia marekebisho makubwa.

Hatimaye Bunge liliridhia kufanya mabadiliko makubwa katika Azimio la CHC, kwa kuamuru Shirikalipewe uhai wa miaka 3 na kuagiza uchunguzi wa namna bora ya kuendesha shughuliza Shirika la Consolidated Holdings. Mapendekezo ya Kamati ya POAC ni kulifanyaShirika hili kuwa la kudumu na kulipa jukumu la kumiliki na kusimamia uwekezajiwa Serikali kwenye kampuni binafsi (National Investment Agency) kama ilivyo Shirikala Tamasek ya Singapore na Shirika la Khazana ya Malaysia. Kwa sasa Uwekezajiwa Serikali katika Kampuni binafsi unasimamiwa na Hazina na usimamizi wake nimbovu na hauleti tija kwa Taifa.

Kitendo cha kushindwa kwahoja Bungeni kiliifedhesha Serikali na hivyo kwa kupitia Wizara ya Fedha kuamuakulihujumu Shirika kwa kumsimamisha Mkurugenzi wake Mkuu kwa makosa ya kimajungumajunguna kwa kuzusha kwamba CHC iliwahonga wabunge ili kuitetea. Waziri wa Fedha ndugu Mustafa Mkulo alilitaarifuBunge kuwa Bodi ya CHC imeomba ukaguzi maalumu kuhusu tuhuma za ubadhirifundani ya Shirika hilo. Niliitaka Serikali ichunguze pia tuhuma kwamba Kamati yaPOAC ilihongwa na kuahidi kuahidi kujiuzulu nyadhifa zangu zote ikithibitika.

Katika Uchunguzi wakeMdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Heabu za Serikali kwa kupitia Kampuni ya Ernest andYoung walitaka kufanya mahojiano na Waziri wa Fedha juu ya tuhuma mbalimbalizinazomkabili ndani ya CHC. Waziri Mkulo alikataa kuhojiwa na wakaguzi nabadala yake akaandika barua (kumb TYC/B/70/2/03 ya Oktoba 8, 2011) yenye kujibutuhuma moja, tena kwa juu juu, kuhusu yeye kuliamuru Shirika kuuza kiwanja cha Shirikabila kufuata taratibu za sheria.

Wakati Waziri anakanusha kuliagiza Shirikakuuza kiwanja kwa mtu aliyemtaka yeye, mimi nina ushahidi tosha wa Nyarakakutoka Hazina, kwa mfano barua TYC/A/290/13/4 ya Machi 9, 2011 ambayo inawagizaCHC kutekeleza agizo la Waziri la Fedha kuhusu kiwanja na. 10 barabara yaNyerere. Vilevile, nina ushahidi wa mkutano uliofanyika huko Morogoro Hotelkati ya Waziri wa Fedha na Mwenyekiti wa Bodi ya CHC kuhusu jambo hilo.

Siku mbili baada yakumjibu CAG, Waziri wa Fedha ndugu Mustafa Mkulo aliamua kutengua uamuzi wakewa kuongeza muda wa Bodi ya Shirika la CHC mpaka mwezi Disemba 2011 na hivyokuivunja. Uamuzi huu wa Waziri una lengo la kuficha ukweli kwani CHC bila Bodiya Wakurugenzi inaendeshwa na Hazina na hivyo taarifa ya ukaguzi itabidiipelekwe Hazina ambayo Waziri wake ni mtuhumiwa.

Uchunguzi wa kina
Ninapendekeza uchunguzi wakina ufanyike kwa kutumia vyombo vya dola na hasa TAKUKURU kuhusu tuhuma hizidhidi ya Waziri wa Fedha na alazimishwe kisheria kujibu maswali ya wakaguzi (Auditors) kuhusu tuhuma dhidi yake.

Wakati uchunguziunaendelea ndugu Mustafa Mkuloasimamishwe kazi ya Uwaziri wa Fedha hadi hapo uchunguzi utakapokamilika.Kitendo chake cha kuiamuru Bodi kumsimamisha kazi aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu kwatuhuma za kutunga na majungu na baadaye kuvunja Bodi ya CHC wakati inasubiritaarifa ya uchunguzi kutoka kwa CAG ni kuingilia uchunguzi na pia ni matumizimabaya ya Ofisi ya Umma ili kulinda maslahi binafsi. Ni dhahiri akiendelea kuwaWaziri wa Fedha ataharibu uchunguzi.Vilevile, Rais wa Jamhuriya Muungano wa Tanzania ndugu Jakaya Kikwete aangalie kama anaitendea haki nchina Uchumi wa nchi kwa kuwa na Waziri wa Fedha ambaye anasema uwongo Bungenibila kuogopa na mwenye kutumia Ofisi yake vibaya kwa kuchukua maamuziyanayoingilia uchunguzi unaomhusu ili kujilinda.

Taarifa ya Uchunguzi ikabidhiwe kwa Spika
Kutokana na ukweli kwambasuala la CHC lilianzia Bungeni na hata Waziri mwenyewe kukiri kuwa taarifa yauchunguzi inapaswa kuwekwa wazi. Kutokana na matokeo ya sasa ambapo Waziri waFedha mwenyewe ana tuhuma za kujibu na kwamba hivi sasa hakuna Bodi yaWakurugenzi ya Shirika na hata itakayoundwa itateuliwa na Waziri mtuhumiwaninashauri kuwa taarifa ya uchunguzi wa Shirika la CHC sasa ipelekwe kwa Spikawa Bunge kwa hatua zaidi.

KZZ
Dar es Salaam, 13 Oktoba,2011.


Nadhani unaweza kuhoji kwanini kichwa cha habari kimeanza na "KIKWETE UPO..." Well,kama tunavyoelewa,utamaduni wa kijiuzulu ni msamiati wa kigeni kwa viongozi wetu.Kutaraji kuwa Waziri Mkulo atatekeleza ushauri wa Zitto ni ndoto ya mchana.Kinachopaswa kufanyika ni kwa Rais Jakaya Kikwete kumpumzisha Mkulo hadi uchunguzi wa suala hili utakapomalizika.By the way,hatuwezi kuruhusu uwepo wa Waziri wa Fedha anayeandamwa na tuhuma za ufisadi.MTIHANI MWINGINE KWA KIKWETE.Let's wait and see!


Kama nilivyobashiri kwenye MAKALA HII,Kaimu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Benno Malisa ameundiwa zengwe zito kufuatia kauli zake jijini Arusha ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka viongozi wenzie wa CCM kuacha kuiandama Chadema.

Kwa mujibu wa habari iliyochapishwa kwenye jarida la Raia Mwema,Malisa anadaiwa kuwa amekuwa akiandaa mazingira mazuri kwa ajili ya Edward Lowassa endapo harakati za kuvuana magamba ndani ya chama hicho zitamkumba.

Japo tuhuma dhidi ya Malisa zinahusishwa zaidi na kitendo cha yeye kufungua mashina ya UVCCM (ambapo anadaiwa kufanya hivyo pasipo kushirikisha uongozi wa umoja huo ngazi ya mkoa) yayumkinika kuamini kuwa kilichomponza kiongozi huyo wa UVCCM Taifa ni kauli zake za kutaka demokrasia ya kiutu-uzima,sambamba na kuikumbusha CCM wajibu wake kuwatumikia Watanzania.

Na hili ndilo tatizo litakalopelekea mauti ya chama hicho kingongwe.Kiongozi au mwanachama yeyote yule atakayeamua kuongea ukweli ataanza kusakamwa na si ajabu akajikuta anavuliwa madaraka,CCM imekuwa ikiongoza nchi kwa namna ya uchawi wa kuwafumba macho Watanzania.Licha ya vyama vya upinzani (hususan Chadema) kuwaamsha Watanzania kuwa chama hicho tawala kinaendesha nchi kwa siasa za kimafia,CCM imekuwa ikijitetea kwa kuwaita wapinzani wachochezi na watu wa majungu,huku ikitumia taasisi za dola kupandikiza migogoro kwenye vyama hivyo.

Sasa anapotokea kiongozi au mwanachama wa kawaida wa chama hicho kuakisi yale yanayosemwa na wapinzani (aambayo kimsingi ni mtizamo wa Watanzania wengi) basi ataandamwa huyo hadi aonekane kama mhaini flani.

Wanachojisahau CCM ni ukweli kwamba kuficha ugonjwa hakuwezi kuwa sehemu ya tiba ya ugonjwa husika.Hata akina Malisa wakikaa kimya na kufuata porojo za "mshikamano wa chama" au "umoja wa kitaifa" ukweli unabaki kuwa ipo siku umma utaamka na kuking'oa chama hicho kwa nguvu kwani wanaweza kudanganya umma wote kwa muda fulani lakini hawawezi kuudanganya milele.

Anyway,soma habari husika hapa chini


Wakati huo huo, hali ya kisiasa ndani ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) ni tete ikibainika kuwa Makamu Mwenyekiti wa umoja huo, Benno Malisa, ameanza kucheza hadharani siasa uasi zinazoendeshwa na kambi inayotajwa kuwa ni ya kigogo mmoja wa CCM mkoani humo. 
Malisa sasa anahusishwa na tukio la hivi karibuni linalohusisha na ufunguzi wa mashina ya chama hicho Arusha mjini, unaotajwa kuratibiwa kinyemela bila viongozi wa chama hicho ngazi ya wilaya na mkoa kutoa kufahamishwa na kwamba, sehemu ya waratibu wa tukio hilo ni vijana waliosafirishwa kutoka wilayani Monduli. 
Taarifa za uhakika ambazo gazeti hili limezipata zinaeleza kuwa tukio hilo halikushirikisha viongozi wa UVCCM mjini Arusha na viongozi wengine wa chama hicho. 
“Mipango yote kwa kiasi kikubwa imeratibiwa na watu wa kutoka wilayani Monduli. Inasemekana kuwa hii ni sehemu ya mkakati wa maandalizi ya watu hao kumhami Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa endapo atabanwa kwenye mkakati wa kujivua gamba wa CCM, basi wajifanye kushusha bendera za CCM kwenye mashina hayo ili kuuonyesha umma kuwa anakubalika sana ndani ya chama,” anasema mmoja wa watoa taarifa wetu ambao ni vijana waliohusika kuratibu mpango huo. 
Hali kama hiyo ya kujiandaa kwa ajili ya mchakato wa kujivua gamba ilijitokeza wakati aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz pale alipotangaza kujiuzulu baadhi ya vijana waliandaa mabango yenye ujumbe unaomtaka ajisiuluzu na wengine wakihoji hatua hiyo huku taarifa zikisema mabango hayo yaliandaliwa muda gani wakati alikuwa bado kutangaza kujiuzulu. 
Kiongozi mmoja wa UVCCM Arusha anaeleza; “UVCCM Arusha mjini walikataa utekelezaji wa mkakati huo haramu kupitia kikao chake cha Kamati ya Utekelezaji kilichoketi Oktoba 7, mwaka huu, kwa kumwandikia barua Katibu wa Vijana CCM mkoani Arusha.” 
Inaelezwa kuwa barua hiyo ilimjulisha kiongozi huyo kuwa wao kama wilaya hawajapata taarifa rasmi za uzinduzi wa mashina hayo ya wakereketwa na hivyo kwa muda uliobaki wasingeweza kufanya maandalizi mazuri ikizingatiwa wao ndio wenye jukumu la kuandaa mashina hayo na si Wilaya ya Monduli. 
“CCM Mkoa baada ya kupata nakala ya barua hiyo waliamua kuitisha kikao cha sekretariati ya mkoa pamoja na kamati ya utekelezaji ya vijana Mkoa wa Arusha na Wilaya Arusha mjini, Oktoba 8, 2011. 
“Katika kikao hicho maazimio yalikuwa ni kusitisha zoezi hilo hadi hapo taratibu za chama zitakapofuatwa. Chama Mkoa walimwandikia barua hiyo Katibu wa UVCCM Mkoa wa Arusha ili aweze kuwataarifu na viongozi wengine pamoja na wanachama wa umoja wa vijana wa CCM. 
“Baada ya kupata barua hiyo Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Millya, alifanya kikao cha faragha na Mbunge wa Viti Maalumu, Catherine Magige na Benno Malisa. Baada ya kikao chao hicho, waliamua kufanya shughuli hiyo iendelee kama walivyokusudia pamoja na chama kukataza. 
“Jumatatu, Oktoba 10, 2011 walianza kushughulikia kibali cha maandamo na uzinduaji mashina hayo. Hadi saa nne asubuhi polisi waliwanyima kibali cha kazi hiyo,” alisema mtoa habari wetu mwingine ambaye naye amekataa kutajwa jina lake gazetini. 
Inaelezwa kuwa mkutano huo wa kufungua mashina uliofanyika 10/10/2011, ulihudhuriwa na vijana kutoka Monduli na vijana wengine wa vyama mbalimbali vya siasa. 
Katika shughuli hiyo, Benno Malisa ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alishambulia wazi wazi chama chake akitetea Chama cha Demokrasia na Maendeleo ( Chadema) chini ya mwavuli wa demokrasia na utawala bora. 
Katika hotuba yake hiyo, Benno Malisa amekejeli hata kauli ya viongozi wenzake wa CCM wanaoonyesha kwamba CCM ni chama tawala na kuonya dola kuingilia mambo ya siasa, hali inayozidi kuashiria mgawanyiko mkubwa ndani ya chama hicho tawala.

CHANZO: Raia Mwema


Rejea taarifa ya msiba wa Mzee Said Muhammad Sikamkono mazishi yatafanyika kesho tarehe 13/10/2011 katika makaburi ya Hainalt Garden of Peace saa nane mchana. Ila kabla ya makaburini tunaombwa wote tufike msikiti wa Sakina Walthamstaw (basi namba 179) saa sita na nusu mchana. Msiba uko nyumbani kwa marehemu Woolwich Dorkyard ambako wote tunakaribisha muda wowote kujumuika na familia ya marehemu wakati huu wa majonzi .Wakina mama pia wanaweza kufika msikitini au nyumbani kwa marehemu kwa ajili ya kutoa pole.

Address ya sehemu ya msiba ni;

Woolwich Ferry
405,Frances Street, London.
SE18 5JU.

Kwa maelezo zaidi  tafadhali wasiliana na;

07813539025 - Haruna mbeyu.Katibu Jumuiya ya Watanzania -london

07766454596 - Abdallah Mdidi

12 Oct 2011


Hello to all you lovely people,

Miss Jestina George Blog has been nominated for the Blog of the Year category at the 2011 (BEFFTA) Black Entertainment Film Fashion Television and Arts Awards. Please show your support by voting through this link, http://www.beffta.com/voting, under category select News 4. Blog Of the Year & Under Nominee select Miss Jestina George then submit your vote. Voting closes on 14th October and your vote would be very much appreciated. If you have any questions please feel free to contact this email.

Thank you for your time,


--
Jestina George
CEO & Founder - MISS JESTINA GEORGE BLOG
Telephone: +447404332910
Facebook: JestinaGeorge


Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.