18 Feb 2018


Nianze makala hii kwa kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daniel John, ambaye hadi alipouawa kinyama alikuwa Katibu wa Chadema kata ya Hananasifu, na pia kwa familia, ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Acqulina Akwilin (samahani kama nimekosea jina).

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, mwili wa marehemu Daniel uliokotwa kwenye ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam ukiwa na majeraha. Alieleza kuwa awali marehemu alichukuliwa na Land Rover nyeupe na watu waliohifanya askari polisi, lakini tangu wakati huo Polisi hawakuwa na taarifa zozote za kiuchunguzi, na hata jitihada za kupatikana mwili huo zilifanywa na Chadema wenyewe.




Kwa upande wa marehemu Acquilina, kifo chake kilisababishwa na kasumba hatari inayozidi kuzoeleka kwa watumishi wa vyombo vya dola kufanya mzaha katika matumizi ya silaha za moto, ambapo katika tukio husika, polisi waliokuwa wakizuwia maandamano ya wafuasi wa Chadema, walitumia risasi za moto,na moja kati ya risasi hizo ilipelekea kifo cha binto huyo, ambaye hadi mauti yanamfika alikuwa mwanafunzi katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) akisomea shahada ya ununuzi na ugavi.
Ni muhimu kutambua kuwa vifo vyote hivi viwili vingeweza kuepukika laiti utu na ubinadamu wetu ungewekwa mbele ya chuki za kisiasa. Huhitaji kuwa mjuzi wa uchunguzi wa mauaji kufahamu kuwa vifo hivyo ni matokeo ya chuki, hujuma, uonevu na kila aina ya baya dhidi ya chama kikuu cha upinzani, Chadema, kuhusiana na kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Kinondoni, ambalo kama ilivyo kwa jimbo la Siha, ni "piga ua" kwa CCM ishinde. Yaani chama hicho tawala kilitarajiwa kutumia kila mbinu kuhakikisha inashinda katika majimbo hayo mawili.

Lakini kabda sijaingia kwa undani katika mada hii - ambayo lazima nikiri kwamba inanipa wakati mgumu sana kuiandika kwa sababu nimebanwa na mchanganyiko wa majonzi na hasira, sambamba na hofu ya kuona taifa langu likisukumwa kuelekea kwenye upotevu wa amani na mshikamano wetu – naomba kuweka wazi masuala matatu ya msingi kunihusu mie mwandishi wa mwakala hii.

Kwanza, mimi licha ya kuwa na makazi nje ya Tanzania kwa takriban miaka 15 sasa bado no Mtanzania. Utanzania wangu ni haki nilioirithi kutoka kwa wazazi wangu, na itabaki hivyo milele. Naeleza hili kwa sababu kuwa wabaguzi wanaopenda kutuhukumu Watanzania tunaoishi huku ughaibuni, na kutaka tuonekane kama Utanzania wetu sio kamili. Kwa mantiki hiyo, kama Mtanzania, nina kila haki ya kutoa maoni yangu kuhusu mustakabali wa taifa letu, hususan katika nyakati hizi ambapo kuna dalili za wanaotaka kulipeleka kubaya taifa letu.

Pili, mwaka 2015 nilishiriki kikamilifu katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais John Magufuli. Kwa upande mmoja nililazimika kumkampenia Magufuli kwa vile nilikuwa nina "sababu binafsi" dhidi ya aliyekuwa mpinzani wake mkuu, mgombea urais wa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Wanasema "adui ya adui yako ni rafiki yako."Kwa upande mwingine, nililipwa kutoa huduma ya ushauri wa kitaalamu (usadi, yaani consultancy kwa kimombo) hususan kwenye mitandao ya kijamii. Natanabaisha hili ili asije akakurupuka mtu na kusema "ah ulishiriki kutupigia kampeni kwa vile tulikupa pesa."

Tatu, huko nyuma nilikuwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Na kabla ya kuanza utumishi katika taaluma hiyo muhimu na nyeti, nilikula kiapo kwa nchi yangu, kiapo ambacho nitaishi nacho hadi ninaingia kaburini. Kiapo hicho sio cha kukitumikia chama flani au viongozi wake bali Tanzania yetu. Nchi ni muhimu  kuliko vyama vya siasa au wanasiasa.

Mtu aliyepikwa na kuiva kwenye taaluma ya uafisa usalama wa taifa, katika nchi yoyote ile, anapaswa kubaki kuwa mtiifu kwa nchi yake bila kujali yupo ndani au nje ya ajira ya taasisi inayohusika na usalama wa taifa wa nchi husika.

Wanasema hata nje ya ajira rasmi, kila mtu aliyewahi kuwa afisa usalama wa taifa anaendeshwa na "sense of public duty born in their previous lives" yaani wajibu kwa umma uliozaliwa katika maisha yao huko nyuma. Jasusi mmoja mstaafu anaeleza “...I have obligations, professional obligations. If there’s a national security emergency or possible national security issue, I should report it."


Kwahiyo, hata kama "maafisa wenzangu wa zamani" wataamua kukaa kimya kwa sababu moja au nyingine – wengi wanahofia usalama wa maisha yao – sie wengine hatuwezi kukaa kimya, hasa kwa vile baadhi yetu tumeshalipa gharama kubwa kwa kelele zetu. Kukaa kimya ni sawa na kuafiki uhuni unaoendelea ambao ni tishio kwa usalama wa taifa.

Lakini licha ya wajibu huo unaotokana na utumishi wetu kwa nchi huko nyuma, Rais Magufuli amefanikiwa kuvifunga mdomo vyombo vya habari kiasi kwamba haviwezi kusema lolote kuhusu "mabaya" yake, na amefanikiwa kuvijengea nidhamu ya uoga vyombo hivyo vya habari kiasi kwamba habari pekee zenye umuhimu kwao ni za kumtukuza na kumpamba "mungu-mtu" huyo. Kwahiyo na sie tuliopikwa na kuiva kuhusu ujasiri, kujitoa mhanga na kutokuwa waoga tukiufyata na kukaa kimya - ilhali media zetu ndio zishapigwa kufuli - hali itazidi kuwa mbaya.


Baada ya kuweka wazi nafasi yangu, sasa tuangalie kwa kina kinachoendelea huko nyumbani hasa kuhusiana na uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni na Siha na kuuawa kwa Daudi na Acquiline.

Ni muhimu kutambua kwamba ukandamizaji dhidi ya vyama vya upinzani sio kitu kilichoanza chini ya utawala wa Magufuli bali hali hiyo imedumu mfululzo tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1992. Labda kilicho tofauti kwa zama hizi ni "ujasiri" wa Magufuli kutoficha chuki yake dhidi ya vyama vya upinzani. Yaani angalau akina Mwinyi,Mkapa na Kikwete walikuwa "wanauma na kupuliza." Kwamba angalau walikuwa na "mshipa wa aibu" na walijitahidi japo kutowaonea Wapinzani waziwazi.

Kwa wanaojua "yanayojiri nyuma ya pazia" watakwambia kuwa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa CCM na serikali zake, na hiyo imepelekea kujengeka "symbiotic relationship" kati ya chama hicho tawala na taasisi za dola, ambapo kila mmoja anategemea uhai wa mwenzie.

Lakini kama kuna kitu kinachokera zaidi kuhusu hujuma dhidi ya demokrasia ni pale CCM na taasisi zake hasa za dola wanapoweka mbele maslahi yao mbele ya utu na uhai wa Watanzania. Na hili halijaanza jana au katika kampeni za chaguzi ndogo katika majimbo ya Kinondoni na Siha.

Uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 ulihusisha matukio mengi tu ambayo kwa makusudi hayapo kwenye kumbukumbu za wazi (japo yamehifadhiwa mahala flani).

Lakini kama wanavyosema "amekula asali sasa anachonga mzinga," baada ya hujuma za kimyakimya za mwaka 1995 kuzaa matunda, CCM na taasisi zake ikanogewa, na matokeo yake ni kwamba uchaguzi mkuu uliofuata, mwaka 2000 uliweka doa kubwa kwa historia ya Tanzania yetu ambapo kwa mara ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kufuatia unyama uliofanyika huko Zanzibar na kupelekea vifo kadhaa (idadi halisi ya vifo haijawahi kuwekwa hadharani japo "wenyewe" walisema zaidi ya watu 19 ndio waliokufa kwenye machafuko hayo. Wasichosema pia ni idadi ya watu waliobakwa, kuteswa na kuwekwa kizuizini.

Kwamba hujuma hizo za CCM dhidi ya demokrasia zilipelekea vifo na majeruhi ni kitu kibaya kabisa. Lakini kitu kingine kibaya ni ukweli kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyechukuliwa hata kutokana na unyAma waliofanyiwa Wazanzibari hao.

Kwa namna ya kipekee, CCM ikawa kama imepewa ruhusa ya kutumia vyombo vyake vya dola kufanya lolote itakalo ili ifanikishe hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla, kisha iibuke na ushindi.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ulikuwa na "uchafu kupindukia." Kundi lililofahamika kama "mtandao" lilijipenyeza katika kila sekta, kuanzia kwenye vyombo vya habari, taasisi za dola hadi kwenye taasisi za dini. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kwamba yaliyojiri wakati "mtandao unafanya jitihada za kumwingiza mtu wao Ikulu" ni mabaya zaidi ya haya tunayoshuhudia sasa tangu Magufuli aingie madarakani.

Kwanini basi hayo yaliyojiri kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 hayajulikani? Jibu ni kwamba, wakati mbinu iliyotumika mwaka 1995 na 2000 ilitegemea zaidi vyombo vya dola, uchaguzi wa mwaka 2005 na 2010 ulitegemea zaidi nguvu ya fedha, nyingi zikiwa fedha haramu. Na sehemu ya fedha hiyo ilitumika "kununua ukimya" wa wanahabari wengi tu. 

Lakini si fedha tu bali pia kuna hujuma mbalimbali – nyingine chafu na za kuchefua – zilizotawala safari za ushindi wa chama tawala kwenye chaguzi hizo.


Image result for lowassa kikwete 2005

Labda tofauti nyingine kuhusu mwaka 2005 na 2010 ni ukweli kwamba wakati chaguzi hizo zilihusisha "kikundi binafsi" yaani hicho cha wanamtandao ambacho hakikuwa taasisi ya serikali au chama.

Lakini muda wote huo, CCM ilikuwa kama imepwa ruhusa na Watanzania kuendeleza hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla. Hakujawahi na utashi miongoni mwa Watanzania kutaka kukabiliana kwa dhati za uhuni/uhalifu wa kisiasa. Na kwa bahati mbaya, kwa vile vipaumbele vya Watanzania wengi ni kwenye "ubuyu" na "kubeti/mkeka" basi habari mbaya ni uwezekano wa CCM kuendelea kufanya itakavyo kwa muda mrefu sana.

Sio kama kwa kubashiri kuwa unyanyasaji wa CCM utaendelea muda mrefu sana ninamaanisha kuwa nimekata tamaa. Hapana. Ninakuwa mkweli tu. Tatizo ni zaidi ya CCM na uhuni wake. Watanzania wenyewe ni sehemu ya mfumo unaowezesha CCM kufanya uhuni/uhalifu huo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulihusisha pia matuki kadhaa yaliyojiri "nyuma ya pazia." Na ukitaka kufahamu kuwa Tanzania yetu haijawahi kuhangaishwa na mauaji ya kisiasa – kuanzia yale ya mwaka 2001 huko Zanzibar hadi haya ya Daudi wa Hananasifu na dada Acquilina – ni kifo cha Mchungaji Christopher Mtikila.


Kwahiyo, na ninaandika haya kwa uchungu mkubwa uliochanganyika na hasira, kuuawa kwa Daudi na Acquilina kutaishia kuwa moja tu ya matuko yaliyowahi kutokea katika Tanzania yetu. Tutawasikia wanasiasa wetu wa vyama vya upinzani wakiongea kwa hisia kubwa. Tutashuhudia pia wanafiki wengi tu miongoni mwa wasanii wetu nao wakijifanya kuguswa na vifo hivyo, lakini wakiwa makini kuepuka kumuudhi "Bashite na baba yake" au kuitibua CCM. Tutashuhudia pia kundi la wanafiki hatari ndani ya CCM wakijifanya kuumizwa na mauaji hayo, na kutaka uchunguzi ufanyike, ilhali nao ni kondoo waliojivika ngozi ya mbwa mwitu.



Kama ambavyo "mauaji mengine ya kisiasa" yalivyoruhusiwa kupita kimyakimya, ndivyo unyama huu uliofanywa dhidi ya Daudi na Acquilina utakavyoruhusiwa uishe kimyakimya.

Kwa upande mmoja tusitarajie Rais Magufuli awajibike – sio kwa yeye binafsi kujiuzulu kwa sababu hilo litakuwa kutarajia zaidi ya muujiza – kwa kumtimua Waziri husika na watendaji katika jeshi la polisi. Kwa upande mwingine, hakuna wa kumshinikiza Rais Magufuli achukue hatua stahili dhidi ya wahusika.

Na nisingependa kuuma maneno hapa. Yeye Magufuli mwenyewe ni chanzo muhimu cha siasa hizi za uhasama zinazoendelea kuitafuna Tanzania yetu. Huyu ni mtu ambaye wala hapati shida kuonyesha chuki zake za waziwazi dhidi ya Wapinzani, Upinzani na demokrasia kwa ujumla.


Kama ilivyo kwa madikteta wengine duniani, Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutumia ajenda yake ya ufisadi kama kisingizio cha kusigina haki za binadamu nchini Tanzania, na kubinya kila fursa ya haki za kidemokrasia na uhuru wa habari. Kama nilivyoeleza awali, amefanikiwa kuviziba midomo vyombo vya habari na ndio maana hata habari za kusikitisha kuhusu mauaji ya Daudi na Acquiline hazijaripotiwa vya kutosha.

Kwa kuviziba midomo vyombo vya habari Magufuli amefanikiwa kuzuwia "habari asizozipenda" na ndio maana hadi muda huu ni Watanzania wachache tu wanaofahamu kilichojiri huko MKIRU katika kilichoitwa "operesheni dhidi ya ugaidi." Kuna siku yaliyojiri huko – na ambayo yamechangia "kupotea" kwa mwandishi wa gazeti la Mwananchi Azory Gwanda – yatajulikana hadharani. Haijalishi itachukua miaka mingapi.


Lakini "yaliyojiri MKIRU" ni uthibitisho mwingine wa hicho nilichoeleza hapo juu kuwa Watanzania wenyewe ndio wanaopaswa kubeba lawama nyingi katika kasumba ya CCM kutojali uhai katika harakati zake za kukandamiza demokrasia. Kwamba kama yaliyojiri MKIRU yameachwa yaishe kienyeji, kwanini tutegemee hali tofauti kwa vifo vya Daudi na Acquiline?

Kama ndugu zetu wa Chadema (na kila mpenda haki) "wamekubali yaishe" kuhusu kifo cha Kamanda Mashaka, "kupotea" kwa kada Ben Saanane (hata zile kampeni za #BringBackBenAlive zimejifia kifo cha asili), na hawasumbuliwi na serikali ya Magufuli kupuuzia jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu, kwanini tutarajie jipya katika mauaji yaliyofanywa dhidi ya Daudi na Acquiline?

Yaani Mnadhimu Mkuu wa upinzani anamwagiwa risasi hadharani wakati mkutano wa bunge unaendelea huko Dodoma, na tunaambiwa kuwa tukio hilo lilitokea katika eneo lenye ulinzi mkubwa na lenye CCTV, kwanini basi wanaosumbuliwa na tukio hilo wasitafute njia stahili za japo kuifanya serikali ione aibu na kufanya japo "uchunguzi wa kizushi"?

Kuhusu hujuma "za kawaida" za uchaguzi, kama kila aina ya uhuni uliofanywa na CCM kwenye chaguzi ndogo za madiwani katika kata 43 uliofanyika Novemba mwaka jana uliruhusiwa upite "kimya kimya" – kwa maana kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya uhuni huo – kwanini basi chaguzi hizi ndogo katika jimbo la Siha na Kinondoni zilitarajiwa kuwa tofauti?

Na katika hili, inapaswa wana-Chadema wajiulize kuhusu busara za viongozi wao kuamua kushiriki katika chaguzi hizo ndogo Siha na Kinondoni ilhali mazingira yaliyokuwepo yalikuwa yaleyale yaliyopelekea chama hicho kususia chaguzi nyingine ndogo tatu katika majimbo ya Longido, Singida Kaskazini na Songea Mjini uliofanyika mwezi uliopita.

Hadi wakati ninaandika makala hii, tayari Tume ya Uachaguzi ilikuwa imeshamtangaza mgombea wa CCM jimbo la Siha, Godwin Mollel kuwa mshindi kwa tofauti kubwa tu ya kura dhidi ya mgombea wa Chadema. Hata kama CCM wameiba kura, ukubwa wa tofauti kati ya kura za mgombea wao na huyo wa Chadema zinaashiria kuwa chama hicho kikuu cha upinzani kilipitisha mgombea fyongo.


Na kama ilivyotarajiwa mgombea wa CCM jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia, naye ametangazwa mshindi.


Mie mtumishi wako nilishabashiri mapema tu kuwa chama hicho tawala kingeshinda majimbo hayo, "iwe isiwe."

Ushindi kwa wagombea hao wa CCM ulipaswa kupatikana kwa gharama yoyote kwa sababu laiti wangeshindwa, kinachoelezwa kama "mkakati wa Magufuli kuua upinzani kwa kununua wabunge na madiwani wa Upinzani"  kingemfanya achekwe hata huko kwenye chama chake.

Na kwa vile hadi sasa wabunge na madiwani waliohama upinzani na kujiunga na CCM wamefanikiwa kurudi madarakani baada ya chama hicho tawala kuwapa fursa ya kuwa wagombea wake kwenye chaguzi ndogo, na kuwasaidia kwa hali na mali washinde, tutarajie wabunge na madiwani wengin zaidi kuhama vyama vya upinzani na kujiunga na CCM. Kisa? "Dili hilo linalipa," kwa CCM na kwa wanasiasa hao wanaohama.

Na unadhani mbunge au diwani "mwenye moyo mwepesi" akiona jinsi chama chake "kilivyochukulia poa" yaliyowasibu akina marehemu Mashaka na Daudi, na yaliyowasibu Ben Saanane na Lissu, kwanini iwe ngumu kwake kushawishika kuhama?

Ningetamani sana kuhitimisha makala hii kwa kushauri nini kifanyike lakini itakuwa kupoteza muda wangu na muda wako msomaji. Ni vigumu mno kuwashauri watu waliokubali kwamba mgao wa umeme ni stahili yao kwa zaidi ya miaka kumi sasa, na ambao kila mara umeme unaporudi wanashangilia kana kwamba wamepewa upendeleo flani.

Kama Watanzania wameshindwa kuilazimisha Tanesko iache mgao wa umeme, wataweza kweli kuilazimisha CCM iache hujuma dhidi ya vyama vya upinzani na demokrasia kwa ujumla? Ndio maana bila utu wala aibu, chama hicho tawala kinapata ujasiri wa kukifanyia mzaha kifo cha Acquiline ambapo kwa kudai polisi (haohao waliomuua binti huyo) wachukue hatua dhidi ya Mbowe. Utterly disgusting!


Na kama mauaji mbalimbali ya kisiasa huko nyuma yameachwa yapite na kusahaulika, kwanini tutarajie miujiza kwenye mauaji haya ya sasa dhidi ya wapendwa wetu Daudi na Acquline?

Na ukweli mchungu ni kwamba Magufuli ataendelea kuwapelekesha Watanzania atakavyo ka sababu si watangulizi wake -Mwinyi, Mkapa na Kikwete – wenye jeuri ya kumwambia "Ee bwana ee, huku unakoipeleka nchi siko." Hawawezi kwa sababu nao ni kama "mateka." Madhambi waliyofanya kwenye tawala zao yanawafanya wahofie hatma yao pindi wakimkosoa "mungu-mtu" aliyepo madarakani.

Na wakati wastaafu au watumishi wa zamani wa Idara za Usalama wa Taifa kwenye nchi kama Marekani wamekuwa mstari wa mbele kukemea kila tendo linalotishia usalama wa nchi hiyo – kwa mfano 'ndoa' kati ya Rais Donald Trump na Russia – wastaafu wetu sie hawana jeuri ya kufungua mdomo sio tu kwa vile wanahofia kuathiri posho na marupurupu yao bali kwa vile nao ni mateka wa "madudu" waliyofanya walipokuwa madarakani. Ukiwa mchafu unajinyima uhuru wa kukemea uchafu.


Basi niishie hapa kwa kurejea tena salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daudi na Acquiline. Ni vigumu kuwaambia maneno yanayotosha kuwaliwaza lakini la muhimu ni kuendelea kuzikumbuka roho za marehemu hao, hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma ambapo sisi Wakristu tunaadhimisha mateso ya Bwana Yesu Kristo. Pumziko la Milele awape Bwana, na Mwanga wa Milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amen


10 Jan 2018

Image result for magufuli lowassa
Jana Januari 9, 2018, wiki moja na siku mbili baada ya kuanza kwa mwaka huu mpya, duru za siasa za Tanzania zilitikiswa na habari kuhusu kiongozi maarufu wa Chadema, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kukutana na Rais John Magufuli kwa “mazungumzo”, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Baada ya “mazungumzo” hayo Lowassa alimmwagia pongezi Magufuli kwa kile alichokiita “kazi nzuri anayoifanya” na kutaja mafanikio katika sera ya elimu bila malipo, ujenzi wa mradi wa uzalishaji wa umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler’s Gorge), na ujenzi wa viwanda na ujenzi wa reli ya “standard gauge”.

Nimepata faraja sana kuja hapa Ikulu kuonana na Mheshimiwa Rais, tumezungumza nae na nimempongeza kwa kazi nzuri anayoifanya, lazima tukiri anafanya kazi nzuri na anahitaji kutiwa moyo,” alinukuliwa Lowassa aliyejiunga na Chadema miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 baada ya ndoto zake kuwania urais kwa tiketi ya CCM “kuota mbawa.”


Image result for magufuli lowassa

Mwanasiasa huyo ambaye baada ya kujiunga na Chadema alipitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya muungano wa vyama vinne vya upinzani – Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD – uliofahamika kama UKAWA, aliendelea kusema kuwa “Moja kubwa ambalo ni la msingi sana ni la kujenga ajira, katika kuanza ujenzi wa reli ya kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro hapo anajenga ajira, na kwenye nchi yoyote inayoendelea suala muhimu ni kujenga ajira, Stiegler’s Gorge ni kujenga ajira na mingine ya aina hiyo, lazima kuwepo na kipaumbele cha kusema kwamba tunajenga ajira. Jingine ni la elimu, ni muhimu sana, hauwezi kuacha elimu katika mambo yako unayofanya, hili nalo lazima lisemwe vya kutosha, kwa kweli nakushukuru Mheshimiwa Rais, you made my day.

Rais Magufuli kwa upande wake alimpongeza Lowassa kwa kile alichokiita “kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali” na kumtaja Lowassa kama mmoja wa viongozi ambaye kwa wakati wake alitoa mchango wake katika nchi.

Magufuli alimmwagia sifa Lowassa akidai kuwa “ni mwanasiasa mzuri kwani hata wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita ambao naye aligombea kiti cha Urais, hakuwahi kumtukana.”

Mheshimiwa Lowassa ameniomba mara nyingi nikutane nae, na leo nimekutana nae, tumezungumza mambo mengi, ameniambia ya kwake na mimi nimemwambia ya kwangu. Kwa ujumla Mheshimiwa Lowassa ni mwanasiasa mzuri na tuendelee kuwaenzi wazee hawa ambao kwa nyakati fulani walifanya mambo mazuri, na mimi napenda kumpongeza Mhe. Lowassa ambaye kama alivyosema hapa kuwa tumefanya mambo mazuri mengi,” alisema Rais Magufuli

Ametaja miradi mbalimbali tunayotekeleza, ametaja mradi wa Stiegler’s Gorge utakaogharimu zaidi ya Shilingi Trilioni 7, amezungumzia juu ya elimu bure, amezungumzia juu ya maji ambayo kwa bahati nzuri yeye alikuwa Waziri wa Maji na anafahamu sasa tumefikia wapi, amezungumza juu ya umeme tulivyosambaza katika vijiji mbalimbali, elimu bure, huduma za hospitali na mengine” aliongeza Rais Magufuli.

Kwanza, ni muhimu kutambua kuwa kama Mtanzania yeyote yule, Lowassa alikuwa na kila haki ya kukutana na Rais wake. Kadhalika, kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani, isingepaswa kuwa jambo la kushangaza kwa viongozi hao wawili kukutana.

Hata hivyo, Lowassa sio tu amekutana na Magufuli, bali pia ammemwamgia sifa. Je ni dhambi kwa kiongozi wa chama cha upinzani kumwagia sifa Rais aliyepo madarakani? Jibu lingepaswa kuwa “si dhambi,” laiti uhusiano kati ya Rais Magufuli, serikali yake na taasisi zake (kama vile jeshi la polisi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa), watendaji wa serikali (hasa mawaziri na manaibu wao, na wakuu wa mikoa na wilaya), pamoja na chama cha Magufuli yaani CCM, na chama anachotoka Lowassa, yaani Chadema, na Upinzani kwa ujumla, ungekuwa mzuri.

Lakini ukweli ni kwamba japo tangu kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, uhusiano kati ya CCM, serikali zake na taasisi zake, na vyama vya upinzani umekuwa “wa kusuasua,” hali katika miaka miwili tu ya utawala wa Magufuli imekuwa mbaya zaidi hususan kutokana na ukweli kwamba hakuna jitihada za kuficha chuki iliyopo dhidi ya Upinzani.

Kama kiongozi wa ngazi za juu kabisa wa Chadema, na pengine mwanasiasa anayeheshimiwa zaidi ya kiongozi mwingine yoyote ndani ya chama hicho, ni wazi Lowassa anafahamu vema msimamo na mtazamo wa chama chake kuhusu Magufuli na utendaji kazi wake, na serikali yake, na chama chake.

Pengine kwa kuweka picha sawia, inaelezwa kwamba hadi wakati huu, zaidi ya wana-Chadema 400 ikiwa ni pamoja na viongozi na wanachama, aidha wapo jela au wana kesi zinazoendelea mahakamani ambazo takriban zote ni matokeo ya chuki za kisiasa zinazofanywa na Magufuli, serikali yake na chama chake.

Kadhalika, katika utawala wa Magufuli, vyama vya upinzani ikiwemo Chadema ambayo Lowassa ni kiongozi wake wa kitaifa vimepigwa marufuku kufanya shughuli zao za kisiasa ikiwa ni pamoja na mikutano na maandamano. Hayo yanatokea wakati CCM ikiwa huru kufanya mikutano na maandamano itakavyo, mara nyingi ikitumia raslimali za umma.

Sambamba na jitihada za Magufuli kubana fursa ya siasa (political space), utawala wa kiongozi huyo umekuwa mstari wa mbele kuvibana vyombo vya habari na kudhibiti uhuru na haki ya wananchi kutoa mawazo yao kama Katiba inavyowaruhusu.

Lakini jingine ambalo Chadema ni mhanga mkubwa, kada maarufu wa chama hicho Ben Saanane “alipotea” Novemba mwaka jana na hadi leo hajapatikana.

Na ni wakati ninaandika makala hii nimebaini kuwa Lowassa hajawahi kuongelea suala la kada huyo (naomba nikosolewe kama nimekosea).
Kubwa zaidi linaloweza kuhalalisha hasira za Chadema kwa utawala wa Magufuli ni tukio la hivi karibuni ambapo Mbunge wake maarufu, ambaye pia alikuwa mpinzani maarufu dhidi ya Magufuli, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, kunusurika kuuawa baada ya shambulio la risasi kadhaa huko Dodoma. Kwa sasa Lissu yupo nchini Ubelgiji kwa matibabu, lakini japo Lowassa alimtembelea alipokuwa hospitalini Nairobi, Magufuli hakuwahi kutia mguu kumjulia hali mwanasiasa huyo ambaye pia ni mnadhimu mkuu wa upinzani bungeni na Rais wa Tanganyika Law Society (TLS).

Kwahiyo japo pongezi za Lowassa kwa Magufuli zinaweza kuwa na uzito, mapungufu ya utawala wa rais huyo wa awamu ya tano, hususan kuhusiana na chuki na uonevu dhidi ya vyama vya upinzani, hususan Chadema, yalipaswa “kumzuwia” kada huyo wa zamani wa CCM kumwaga pongezi hizo.

Kibaya zaidi, imebainika kuwa Lowassa alishawahi kumwomba Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amsaidie kukutana na Magufuli. Hata hivyo, Gambo alipotamka hilo hadharani, Lowassa “aliruka kimanga.”


Hata hivyo, jana Magufuli alitamka bayana kuwa Lowassa aliomba mara kadhaa kukutana naye. Kwahiyo, alichosema Gambo kilikuwa kweli, na Lowassa hakuwa mkweli alipokana kuwa hajaomba kukutana na Magufuli.

Tukio hilo la Lowassa kukutana na Magufuli na kumwagia pongezi limepokelewa kwa hisia tofauti. Wakati kuna kundi dogo la wana-Chadema waliopongeza hatua hiyo, kwa mfano “kada” mmoja wa chama hicho Yericko Nyerere, wengi ikiwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wamepingana waziwazi na Lowassa.

Wakati Yericko aliandika haya


Mbunge maarufu wa Chadema, Godbless Lema alikuwa wa kwanza kueleza bayana kutoafikiana na pongezi za Lowassa kwa Magufuli.


Baadaye, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, naye alieleza kuwa kauli za Lowassa ni zake binafsi na sio msimamo wa chama hicho.

Kadhalika, Mbowe alionekana kumkumbusha Lowassa kuhusu matukio mbalimbali yasiyopendeza katika utawala wa Magufuli

Lakini pengine aliyeeleza kwa kirefu kuhusu suala hilo ni Lissu, ambaye akiwa hospitalini huko Ubelgiji, alitoa waraka huu hapa chini.



Waheshimiwa habari za Tanzania na poleni kwa yote.
Naomba na mimi niseme kwa uchache kuhusu suala hili. Samahani kama 'uchache' wangu utakuwa mrefu kidogo.
Baada ya Mwenyekiti kuzungumzia jambo hili, inaelekea kuwa wazi kwamba Mheshimiwa Lowassa hakumshirikisha Mwenyekiti kabla ya kukubali au kuamua kwenda Ikulu kukutana na Rais Magufuli.
Na juzi tu wakubwa wetu hawa wawili walikuwa pamoja hospitalini kumsalimia Mzee Ngombale Mwiru.
Je, inawezekana Mheshimiwa Lowassa hakuwa anajua tayari kwamba ana appointment Ikulu?
Kama alikuwa anajua, kutokumshirikisha Mwenyekiti wake kuna tafsiri gani hasa?
Katika mazingira ya sasa ya Tanzania ya Magufuli, uamuzi wowote wa kufanya nae mazungumzo, hata kwa nia njema yoyote ile, bila kushauriana au kuwashirikisha viongozi wa juu wa chama, ni uamuzi usio sahihi na mgumu kukubalika.
Vile vile, kauli za aina ambayo tumeisikia leo kutoka kwa Mheshimiwa Lowassa, zina athari kubwa kisiasa.
Sio tu zinachanganya wanachama na wafuasi wetu, lakini pia zinawapa mtaji wa kisiasa maadui zetu.
Kuanzia sasa tutegemee sana kuwasikia maCCM yakishangilia 'busara' za Mheshimiwa Lowassa.
Masuala ya ukiukwaji haki za binadamu, uvunjwaji wa Katiba na mengine mengi sasa yatajibiwa kwa namna moja: Lowassa amemkubali Magufuli nyie wengine mnapiga kelele za nini.
Huu ni mtaji wa bure kwa Magufuli. Ukweli, ambao umesemwa sana humu, ni kwamba amefeli karibu katika kila jambo.
Hata hiyo reli anayosifiwa nayo na Lowassa bado ni ndoto tu: nani ajuaye itajengwa kwa hela za nani???
Za Wachina kama tulivyoambiwa mwanzoni; au za Waturuki kama tulivyoambiwa baadae; au za Afrika Kusini kama alivyosema mwenyewe anaenda kumwomba Zuma???
Kama chama hatujawahi kukataa mazungumzo na Rais au kiongozi mwingine yeyote wa serikali.
Na hatukatai kuzungumza na Magufuli kuhusu matatizo mengi na makubwa yanayoikabili nchi yetu.
Lakini ni muhimu na lazima viongozi wakuu wa chama washirikishane na washauriane kabla ya mazungumzo hayo.
Na baada ya mazungumzo, ni lazima viongozi wakubaliane juu ya kauli za kutoa hadharani kwa umma ili wote tuwe kwenye ukurasa mmoja.
Katika mazingira ya sasa, ambako viongozi na wanachama wetu wanashambuliwa hadharani kwa mapanga na hata kwa risasi, kumsifia Rais ni kumuunga mkono yeye na matendo yake.
Katika mazingira ya kesi nyingi za kutunga dhidi yetu, 'kazi nzuri' inayofanywa na Magufuli ina maana gani hasa, kama sio kuhalalisha ukandamizaji tunaofanyiwa.
Katika mazingira ambapo hata jumuiya ya kimataifa imeanza kuhoji mwenendo wa Rais Magufuli, kutoa kauli kwamba 'anafanya kazi nzuri' ni 'kumtupia taulo' la propaganda litakalomfichia madhambi mengi aliyowafanyia Watanzania katika miaka hii miwili.
Kwa vyovyote vile, kitendo cha Mheshimiwa Lowassa sio cha kunyamaziwa au kuhalalishwa kwa hoja nyepesi nyepesi.
TUNDU LISSU(MB).
Top of Form

Kadhalika, kada maarufu wa kike wa chama hicho, Hilda Newton nae alieleza masikitiko yake kutokana na kauli za Lowassa.



Kama alivyotahadharisha Lissu, ni wazi kwamba CCM watakuwa wamepewa “silaha” mpya katika “kumpamba” Magufuli na “kuwapenda” wapinzani, kwamba “hata Lowassa wenu anamkubali Magufuli.” Na ni rahisi kwa CCM kuonekana wana mantiki katika hoja hiyo, kwa kudai “kama mtu muhimu kabisa kwenye chama chenu (yaani Lowassa) ambaye ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Magufuli kwenye uchaguzi mkuu uliopita, anamkubali mkuu huyo wa nchi, ninyi ni akina nani kumpinga?”

Wakati ni wazi kwamba uamuzi wa Lowassa kukutana na Magufuli, na kumwagia pongezi, umezua “sintofahamu” huko Chadema, kuna masuala kadhaa ya muhimu yanayopaswa kuangaliwa kwa makini kwa ajili ya mustakabali wa chama hicho.

Kwanza, ni muhimu kwa viongozi na wanachama wa Chadema kutambua nafasi ya Lowassa katika chama hicho. Wakati baadhi ya wachambuzi wa siasa – mie nikiwa mmoja wao – wanaamini kuwa ujio wa Lowassa katika chama hicho ulikuwa na hasara zaidi kuliko faida, jitihada zilizofanywa na chama hicho kumpigania mwanasiasa huyo zimemjengea hadhi ambayo haipo kwa mwanasiasa mwingine yoyote ndani na nje ya chama hicho.

Ikumbukwe kuwa hadi wakati jina lake lilipokatwa na vikao vya CCM katika mchakato wa kusaka mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho tawala, Lowassa alikuwa ndiye mwanasiasa maarufu kuliko wote Tanzania. Yayumkinika kusema alikuwa mtu wa pili kwa umaarufu baada ya marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Licha ya kulazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008 kutokana na kashfa ya Richmond, Lowassa aliendelea kuwa mwanasiasa maarufu na mwenye nguvu kuliko yeyote yule ndani ya CCM, hata zaidi ya Rais na mwenyekiti wa taifa wa chama hicho wakati huo, Jakaya Kikwete.

Na japo kukatwa kwa jina la Lowassa huko CCM kulimpunguzia kidogo umaarufu wake kwa siasa za Tanzania – ilikuwa kama miujiza kuona CCM ilikuwa na ujasiri wa kukata jina la mwanasiasa huyo- alihamia Chadema akiwa na sapoti ya kutosha kiasi japo si kubwa kama ilivyotarajiwa.

Japo kuna “tuliopishana nae mlangoni” – kwa maana yeye alipoingia, sie tukatoka – ujio wake ulipelekea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi ya wote wa Upinzani. Na ndio maana haikuwa vigumu kwake kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA.

Nimeeleza kuwa baadhi yetu “tulipishana nae mlangoni” kwa sababu mie binafsi nilikuwa naiunga mkono Chadema, si kama mwanachama bali ukweli kwamba kwa muda mrefu nimekuwa nikijihusisha na harakati za mapambano dhidi ya ufisadi, na chama hicho kilijitokeza kuwa championi wa mapambano hayo. Kwahiyo, “naturally” nilijikuita nikikiunga mkono.

Hata hivyo, ujio wa Lowassa katika chama hicho ulinikimbiza. Sababu kuu ni binafsi zaidi, na nisingependa kuongelea hapa, lakini sababu nyingine ni kile nilichotafsiri kama usaliti wa Chadema. Ikumbukwe kuwa tangu mwaka 2006, chama hicho “kilimkalia kooni” Lowassa kumtuhumu kuwa ni fisadi, na ndicho kilichofanya jitihada kubwa zilizopelekea mwanasiasa huyo kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.

Sasa bila hata kutumia jitihada kidogo tu za busara, chama kilichomwandama Lowassa kuwa ni fisadi, kwa miaka 9 mfululizo, yaani 2006 hadi 2015, kilionekana kituko kwa baadhi yetu tuliokuwa tukikiamini, kwa sababu, pamoja na mengine, isingewezekana kutumia miezi mitatu (Julai 2015 Lowassa alipojiunga na chama hicho hadi Oktoba wakati wa uchaguzi mkuu) kumsafisha vya kutosha.

Na gharama ya ujio wa Lowassa ilikuwa kubwa. Moja kubwa zaidi ilikuwa lazima kwa Chadema “kuitosa” turufu yake muhimu, ajenda ya vita dhidi ya ufisadi. Ililazimika kufanya hivyo kwa sababu kuzungumzia ufisadi ilhali chama hicho kimemkumbatia mwanasiasa kiliyemwita “baba wa ufisadi” kwa miaka 9 mfululizo ingeonekana kioja.

Kadhalika, kwa kumpokea Lowassa, Chadema ilikuwa haina jinsi ya kukwepa tuhuma kutoka CCM kuwa chama hicho upinzani ni cha kifisadi kwa sababu ya kumkumbatia mwanasiasa ambaye kilikuwa kikimuita fisadi. Jitihada za Chadema kujibu mashambulizi kuwa “kama Lowassa ni fisadi mbona hajachukuliwa hatua,” zilikuwa hazina mashiko.

Lakini jingine lililoipa jeuri CCM ni ukweli kwamba kwa chama hicho, Lowassa alikuwa ni “makapi” sambamba na wanasiasa wengine waliomfuata huko Chadema. Hiyo ilikipa chama hicho tawala “jeuri” ya namna flani. Na waliitumia vema kwenye kampeni, kwamba “hawa jamaa si lolote si chochote. Yani wameshindwa hata kutafuta mgombea wao wenyewe mpaka wakasubiri makapi kutoka kwetu ndo wakapata mgombea urais.” Na pamoja na maneno hayo kuwa machungu, ndo ukweli ulivyokuwa.

Chadema na UKAWA kwa ujumla walikuwa na takriban mwaka mzima wa kujipanga; kuafikiana kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo, na kumnadi, huku wakitumia “advantage” ya “vita vya wenyewe kwa wenyewe” kati ya zaidi ya makada 40 waliokuwa wakichuana kuteuliwa na CCM.

Badala yake, kumbe tayari kulikuwa na makubaliano ya siri kati ya uongozi wa baadhi ya viongozi wa juu wa Chadema kwamba wasubiri kutangaza mgombea wao hadi baada ya mchakato wa CCM kupata mgombea wake, ka maana ya “kumhifadhia nafasi Lowassa endapo jina lake litakatwa huko CCM.”

Kabla ya kwenda mbali na makala hii ningependa nishauri Chadema irejee suala hilo la Lowassa kuandaliwa nafasi ya kuwania urais japo wakati huo alikuwa CCM. Hatua stahili zinapaswa kuchuliwa dhidi ya wote waliohusika na mpango huo.

Na ujio wa Lowassa ulipelekea Chadema kumpelekea mmoja wa magwiji wa siasa za upinzani, Dokta Willbrord Slaa. Umahiri wa Dokta Slaa haukuwa tu katika kuchukia ufisadi kwa dhati bali umahiri wake mkubwa katika kujenga hoja kisomi. Kadhalika, alikuwa akiaminiwa na watu mbalimbali muhimu ndani ya serikali, kiasi kwamba baadhi yao walihatarisha ajira zao kwa kumpatia mwanasiasa huyo nyaraka muhimu zilizoiwezesha Chadema kuwa na ushahidi mbalimbali katika vita yake dhidi ya ufisadi.

Na kuonyesha kuwa alikuwa na msimamo imara, Dokta Slaa aliamua kujiweka kando katika uongozi kupinga Lowassa kupewa ugombea urais wa UKAWA. Lakini jambo la kusikitisha mno, kiongozi huyo aliyekifanyia mengi chama hicho alidhalilishwa na kutukanwa kupita kiasi.
Na “akina sie” tulishindwa kustahimili ujio wa Lowassa, na kwa vile kwa baadhi yetu ilikuwa muhimu kumzuwia asiingie Ikulu, na hivyo kulazimika kumpigia kampeni mpinzani wake yaani Magufuli, tulitukanwa kila aina ya matusi. Sijui watu hawa waliojitoa ufahamu wataweka wapi sura zao pindi Lowassa “akirejea nyumbani” CCM.

Wakati anajiweka kando na uongozi wa Chadema, Dokta Slaa alikitahadharisha chama hicho kuwa ili kuleta mabadiliko ya kweli (badala ya hayo “ya kisanii” aliyokuwa akiyanadi Lowassa) chama hicho kinahitaji mkakati makini utakaoongozwa na watu makini. Na kwa hakika, tangu wakati huo, Chadema imekuwa kama kundi la wanaharakati wa kudandia hoja kuliko chama cha siasa chenye ajenda ya kueleweka. Uamuzi wa kuitelekeza ajenda ya vita dhidi ya ufisadi ulipelekea chama hicho kutokuwa na ajenda moja ya maana, huku CCM “wakipora” kiurahisi ajenda ya vita dhidi ya ufisadi.

Je mustakabali wa Chadema ukoje? Japo sio rahisi sana kubashiri kwa uhakika kuhusu hatma ya chama hicho, binafsi – kwa kutumia uzoefu wangu na uelewa wa kutosha wa siasa za Tanzania, sambamba na kuwa na fursa ya kufahamu “yanayojiri nyuma ya pazia” la siasa za nchi yetu – ninadhani kuwa kuna uwezekano mkubwa tu kwa Lowassa kurudi CCM kama sio kuachana kabisa na siasa.

Kwanini Lowassa anaweza kurudi CCM? Kuna sababu kuu mbili. Moja ni dalili za wazi kuwa ndoto zake za urais kupitia chama hicho ni kama zimeyeyuka. Umaarufu wake umegubikwa na kuibuka na kuimarika kwa umaarufu wa Lissu. Ni dhahiri kwamba ikipigwa kura ya maoni kuwa nani kati ya Lowassa na Lissu awe mgombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020, Lissu ataibuka mshindi. Na Lowassa anafahamu kuwa hakuna njia ya mkato kwa yeye “kulazimisha” awe mgombea katika uchaguzi mkuu huo ujao, licha ya ukweli kwamba alishatangaza kuwa atagombea.

Sababu nyingine ni binafsi zaidi. Lowassa ni mmoja wa matajiri wakubwa nchini Tanzania. Kama utajiri huo ulipatikana kihalali au kifisadi, si lengo la makala hii kujiingiza katika mjadala huo. Lililo wazi ni ukweli kwamba licha ya kuwa mwanasiasa, yeye pia ni mfanyabiashara. Na kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, serikali ya Magufuli imefanikiwa kutumia nyenzo yake muhimu dhidi ya wapinzani ambao pia ni wafanyabiashara, KODI.

Inaelezwa pia kwamba mali mbalimbali za mwanasiasa huyo zipo hatarini kutokana na uwepo wake huko Upinzani. Inadaiwa kuwa hata jengo la Tanesco Ubungo ambalo serikali imetangaza kulivunja, linamilikiwa na Lowassa, na tishio la kulivunja lilikuwa kama kufikisha ujumbe kwake.

Katika hili, Lowassa hatoonekana mtu wa ajabu akiamua kurudi CCM ili asibughudhiwe kuhusu biashara na mali zake. Ni nani kati yetu anayeweza kujitoa mhanga kwa ajili tu ya imani yake ya siasa? Si kama hawapo ila ni adimu mnooo! Na kibaya zaidi, hata akiamua kung’ang’ania huko Chadema, hatma yake na ya chama hicho haieleweki kwa sababu hadi muda huu – na hii ni licha ya zuwio la Magufuli dhidi ya vyama vya upinzani kufanya shughuli zao za siasa – chama hicho kikuu cha upinzani “kipo kipo” tu. Hakina ajenda moja ya kueleweka zaidi ya kudandia kila tukio linalojiri.

Iwapo Lowassa ataamua kubaki Chadema, hiyo itakuwa fursa mwafaka kwa chama hicho kumpumzisha. Naamini kuwa wana-Chadema wakiweka kando ushabiki wa kisiasa, wanafahamu fika kuwa mwanasiasa huyo hana nguvu, uwezo wala mvuto wa kukabiliana na siasa hatari zinazoendelea muda huu huko nyumbani.

Kwa upande mwingine, tukio la Lowassa kukutana na Magufuli Ikulu linaweza pia kuhusishwa na tamko la hivi karibuni la Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad, ambaye kama Lowassa, alimmwagia sifa Magufuli.

Nimefanya uchambuzi kuhusu kauli za wanasiasa hao wawili hapa, lakini ninachoweza kugusia hapa ni haja ya kutambua kuwa wanasiasa hao bado wanatunzwa na serikali kutokana na nyadhifa walizowahi kushika huko nyuma. Haihitaji uelewa mkubwa kuhusu "siasa za kibabe" kuhisi kwamba huenda "malezi" wanayopewa na serikali yametumika kama "chambo" cha kuwavuta karibu na Magufuli.

Kuhusu matatizo yanayoikabili Chadema muda huu,ukweli ni kwamba ni zaidi ya uwepo wa Lowassa ndani ya chama hicho. Japo huu ni ukweli mchungu usioruhusiwa kabisa kusikika ndani ya chama hicho, licha ya kazi nzuri ya kuifikisha Chadema ilipo leo, mwenyekiti wa taifa Mbowe anapaswa kutoa fursa kwa wana-Chadema wengine kusukuma gurudumu la chama hicho. Na hatua hiyo wala haihusiani na mchango wake mkubwa wa kumleta Lowassa ndani ya chama hicho na “kumpa” ugombea urais wa UKAWA.

Kirefu cha Chadema ni Chama cha DEMOKRASIA na Maendeleo. Sasa ni demokrasia gani hiyo ambayo inaruhusu mwenyekiti mmoja kuwa madarakani milele? What if “uenyekiti wa milele” ni miongoni mwa vikwazo kwa maendeleo ya chama hicho?

Lakini hata kama “muda wa Mbowe kutoka madarakani haujafika,” busara tu inapaswa kumfahamisha kiongozi huyo kuwa ni vema kuzingatia busara za akina Nyerere waliojing’atua wakiwa bado wanahitajika. Sipendi kubashiri hili, lakini laiti Mbowe asipohamasisha mageuzi kwenye medani ya uongozi wa chama hicho, haitokuwa jambo la ajabu akiishia kung’olewa kwa nguvu.

Na kwa bahati mbaya kwake, hili “songombingo” alilolianzisha Lowassa jana linaweza kuwa kama mnyororo mrefu ambao mahala flani yupo Mbowe. Ndiye aliyemkaribisha Lowassa.

Moja ya mapungufu makubwa mno yanayoitafuna Chadema muda huu ni pamoja na kulipuuza kundi muhimu linalokisaidia mno chama hicho, lundo la vijana wanaoshinda na kukesha katika mitandao ya kijamii wakijaribu kukinadi chama hicho angalau kwa kuikemea serikali ya Magufuli au CCM kwa ujumla.

Laiti chama hicho kingekuwa na ajenda ya kueleweka, basi jeshi hili la vijana lingekuwa nyenzo muhimu mno. Ni rahisi kuwalaumu vijana hawa kuwa “kazi yao kubwa ni kudandia hoja tu,” lakini ukweli ni kwamba chama chao hakiwapatii ajenda ya/za kueleweka. Kibaya zaidi, hata pale wanapojaribu kutengeneza ajenda wao wenyewe – kwa mfano jitihada za kumsaka Ben Saanane – hawapati sapoti ya kutosha kutoka uongozi wa juu wa chama hicho.

Ni hivi, wengi wa hawa vijana wanahatarisha maisha yao kwa kuwa tu “upande usiotakiwa” na serikali ya Magufuli. Hawategemei malipo yoyote zaidi ya kuamini kuwa siku moja wanaweza kukiingiza chama chao madarakani. Hakuna jitihada za makusudi za uongozi wa juu wa chama hicho kuwa karibu na kundi hili muhimu.

Ukiwa UVCCM una uhakika wa angalau “kuhongwa na Bashite” au kualikwa kwenye “mnuso” sehemu flani. Lakini ukiwa kijana wa upinzani, “zawadi” kubwa yaweza kuwa kusumbuliwa na vyombo vya dola na kuishi maisha ya wasiwasi. Kwahiyo vijana wa upinzani wana kila sababu ya kuichukia siasa, kwa sababu inahatarisha maisha yao, lakini mapenzi yao katika imani ya chama inawalazimisha kung’ang’ania hivyo hivyo.

Niionye Chadema kuwa katika zama hizi za “ununuzi wa binadamu kama zama za utumwa,” chama hicho kisishangae pindi wengi wa vijana hawa watakapoamua kubwaga manyanga na kukubali “kununuliwa.” Kwanini waendelee kuhatarisha maisha yao ilhali uongozi wa juu wa chama hicho hauna muda nao?

Akina Hilda Newton, Ben Malisa, Bob Wangwe, Ndehani Mwenda, Noel Shao, Gift Nanyaro ni miongoni mwa vijana wanaofanya kazi kubwa kwa ajili ya Chadema, bila ya matarajio ya malipo au fadhila flani, zaidi ya kuhatarisha maisha yao. Kama ilivyo kawaida ya mwanadamu yeyote yule, inaweza kufika mahala mtu akarudi nyuma na kujiuliza, “is it worth it?” Na japo sitarajii kuona makada hao vijana wakiamua kuipa kisogo Chadema, lakini sintoshangaa baadhi yao wakiamua kuipa kisogo siasa, hasa kama tasnia hiyo itaendelea kuwa “yenye manufaa kwa genge flani tu.”

Nihitimishe makala hii kwa kukuhamasisha msomaji kujipatia nakala yako ya kitabu changu kipya cha kielektroniki kinachochambua kwa kina miaka miwili ya utawala wa Magufuli. 




Baadhi ya niliyaoyazungumzia kwenye makala hii yamezungumwa kwa kirefu katika kitabu hicho ambacho hakielemei upande wowote. Kitabu hicho kwa sasa kinasubiri uzinduzi rasmi utakaokiwezesha kununulika kwa “mobile money” kama m-pesa, tigopesa,nk. Nitawataarifu. Ila kwa wasiohitaji kusubiri, waweza kukinunua HAPA

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.