21 May 2018



Kuna msemo usiopendeza kwamba, ukitaka kumficha kitu Mswahili, basi weka kwenye kitabu. Waswahili wengi wanaogopa maandishi kuliko virusi vya UKIMWI, except maandishi hayo yatakapohusu UBUYU, our nation's favourite.

Sasa, kwa vile lawama hazijengi, nimeamua kuendeleza utaratibu niliouanzisha huko Facebook ambapo mara kwa mara nilikuwa nawapatia watu machapisho mbalimbali BURE. Kwahiyo, angalau mara moja kwa wiki, nitakuwa naweka post yenye link ya kupakua kitabu chenye umuhimu kwako. Series hiyo ya vitabu takriban kila wiki ninaipa jina "Let's Read / Na Tusome."

Leo tunaanza na chapisho hili muhimu kuhusu "ushushushu." Ni mwongozo wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) kuhusu "kuzuga watu" (trickery) na hadaa (deception). Baadhi yenu mtakuwa mlishakipakua nilipokiweka mara mbili huko Facebook.

Pakua HAPA


Sambamba na vitabu, from time to time nitajitahidi kubandika makala mpya mara nyingi zaidi ya ilivyo sasa ambapo inaweza kupita mwezi mzima bila kubandika post yoyote ile.Tarajia mada za mbinu za kimaisha (life hacks), usalama wa mtandaoni (cybersecurity), nyeNzo za mtandaoni (internet tools), afya, na kadhalika. Hakikisha unatembelea blogu hii mara kwa mara.


21 Apr 2018


Jana ilitolewa taarifa kwa vyombo vya habari  kuwa Rais John Magufuli amemteua "Msalika Robert Makungu kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora." Hata hivyo, kwa makusudi, taarifa haikueleza kabla ya uteuzi huo, Makungu alikuwa na wadhifa gani, japo ilieleza kuwa anakwenda mkoani Tabora kuchukua nafasi ya Dokta Thea Ntara ambaye amestaafu.



"Kilichofichwa" kwenye taarifa hiyo ni ukweli kwamba Makungu alikuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (DDGIS) ambaye aliteuliwa wakati mmoja na Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo, Dokta Modestus Kipilimba, Agosti mwaka jana.

Japo taarifa husika haikutumia neno "kutumbuliwa," lakini haihitaji ufahamu wa mfumo wa utawala wa Idara ya Usalama wa Taifa kumaizi kwamba kutoka u-Naibu Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo nyeti hadi u-Katibu Tawala wa Mkoa ni kushushwa cheo (demotion). 

Kwa mujibu wa vyanzo vyangu vya kuaminika ndani ya taasisi hiyo, kilichopelekea hatua hiyo inayoelezwa kuwa ngumu kwa  Magufuli ni tofauti kati ya watendaji hao wakuu wa taasisi hiyo, yaani Makungu na aliyekuwa bosi wake, yaani Kipilimba.

Inaelezwa kuwa tofauti kati yao ilikuwa kubwa kiasi cha Kipilimba kutishia kujiuzulu iwapo Magufuli asingechukua hatua dhidi ya Makungu.

Hata hivyo, Makungu alikuwa "mtu wa Magufuli" kwa sababu ni wote wanatoka Kanda ya Ziwa, na ni miongoni mwa "circle ya karibu ya Magufuli" ambayo pamoja na watu wengine, inayojumuisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Katibu Mkuu wa Hazina Dotto James, na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.

Kwahiyo wakati  ingetarajiwa Magufuli "angemkumbatia poti wake Makungu" lakini kwa mujibu wa vyanzo vyangu, umuhimu wa Kipilimba kwa Magufuli ni mkubwa zaidi. 

Tukio hilo ambalo halikuvuta hisia za wengi hasa kwa vile lilitokea muda mfupi baada ya kupatikana taarifa za kifo cha mlimbwende maarufu Agnes Masogange aliyefariki jijini Dar jana.

Japo wadhifa wa "Naibu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa" (DDGIS) sio wa muda mrefu tangu uanzishwe (Makungu alikuwa mtu wa pili kushika wadhifa huo baada ya Jack Zoka kuwa wa kwanza), kitendo tu cha Mkurugenzi katika taasisi hiyo kutolewa na kupelekwa mkoani ni cha kushangaza na kinaingia moja kwa moja kwenye kumbukumbu za kihistoria.

Hata hivyo, kabla ya Makungu "kutumbuliwa" tayari kuna Mkurugenzi mwingine ambaye aliondolewa kwenye wadhifa wake kama  nilivyoripoti kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana wakati huo, kuondoka kwa mwanamama huyo kulichangiwa na mtazamo wake wa kutaka mabadiliko ndani ya taasisi hiyo ambao ulikinzana na wahafidhina wasiotaka mabadiliko yoyote kwa taasisi hiyo.

Wakati hayo yanatokea, Zoka, aliyekuwa Balozi wa Tanzania huko Canada nae alitolewa katika wadhifa huo hivi karibuni. Nilieleza kwa kirefu kuhusu tukio hilo katika makala HII

Kama ambavyo Zoka aliandamwa na lawama kwamba alikuwa akiongoza mkakati wa kuhujumu vyama vya upinzani, Makungu pia ametoka katika nafasi hiyo akikabiliwa na lawama kama hizo.


Kwa upande wangu binafsi kama afisa wa zamani katika taasisi hiyo, wakati fulani nililazimika kumwandikia barua Makungu kutokana na taarifa flani zilzonikera. Na katika barua hiyo nilimkumbusha kuwa cheo ni dhamana, na hakina mwamana.


Tatizo kwa wenzetu wengi wanaposhika madaraka ni ile hali ya kujisahau wakidhani watafia wakiwa kwenye madaraka. Hupuuzia ukweli kuwa ipo siku watatoka katika nafasi zinazowapa jeuri na kujikuta "mtaani." Maisha hayatabiriki, leo unalala ukiwa DDGIS kesho unaamka ukiwa RAS.



Kuhusu iwapo hatua hiyo ya Magufuli kuwa na atahri zozote, kwa sasa ni mapema mno kubashiri. Baadhi ya maafisa waliopo kazini na wastaafu  wa Idara ya Usalama wa Taifa walidokeza kwamba taarifa hiyo ya kuondolewa kwa Makungu imewashtua wengi

 Kwa upande mwingine, wakati yote haya yanatokea, haijafahamika hali ikoje kwa "Idara ya Usalama wa Taifa nje ya Idara ya Usalama wa Taifa," yaani kile kikosi kilicho chini ya Daudi Alabert Bashite.



Kwamba Kipilimba ameweza kumn'goa "poti wa Magufuli" Makungu, basi huenda pia akawezesha kung'oka kwa Bashite, mtu anayeutia doa utawala wa Magufuli kwa kila hali.



Ni muhimu pia kujumuisha tweet ya mtu mmoja ambaye hujitambulisha kama Gavana wa zamani wa Benki Kuu, Daudi Balali.


Nimalizie makala hii kwa kukushauri uwe ukiitembelea blogu hii mara kwa mara upate fursa adimu ya kusoma uchambuzi exclusive kama huu wa leo.

16 Apr 2018






Africa Confidential Toleo la 28 Machi 2018


27 Machi 2018

Hatua za kidikteta za Magufuli zinakumbana na upinzani unaoongezeka lakini ndio Ameshika uelekeo huo na anatishia wanaomkosoa

Katikati ya muhula wake wa kwanza, Rais John Magufuli anakabiliwa na shinikizo. Huku akikabiliwa na tishio kubwa kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), vikundi vya kiraia, viongozi wa kanisa, na sasa vijana kwenye mitandao ya kijamii, anaonekana kufurahia mapambano hayo. Dola pia inatishiwa na makundi yenye silaha yaliyokuwa viongozi wa serikali na chama mkoani Pwani (MKIRU). Majibu ya serikali kukabiliana na changamoto hizo yametawaliwa na ukatili ambao haujawahi kuonekana kamwe, na kupelekea kulaaniwa kutoka kila upande.

Kuongezeka kwa vurugu za kisiasa, hasa wakati wa uchaguzi mdogo wa jimbo la Kinondoni, kulipelekea lawama dhidi ya utawala wa mabavu wa Magufuli. Ubalozi wa Marekani ulitaka kufanyike uchunguzi kuhusu utekaji na mauaji ya kiongozi wa upinzani jijini Dar es Salaam wakati wa kampeni. Umoja wa Ulaya baadaye ulionyesha wasiwasi wake kuhusu "mwenendo wa hivi karibuni unaotishia kanuni za demokrasia" baada ya polisi kutumia risasi katika maandamano ya Chadema katika mkesha wa siku ya kupiga kura Februari 17, hali iliyopelekea majeruhi watatu na kuuawa kwa mpita njia.

Wiki mbili baada ya matamko hayo, Wizara ya Mambo ya Nje ilijibu kwa taarifa yenye kurasa tatu na nusu ikiyahusisha matukio ya huko MKIRU na "vikundi vya ndani na nje ya nchi vinavyochukizwa na jitihada za Magufuli kuondoa ufisadi, biashara ya mihadarati, ujangili, ukwepaji kodi na kujenga uwajibikaji."

Vikundi hivyo vyenye silaha, ambapo baadhi vinadaiwa kuwa na mahusiano na Al-Shabaab ya Somalia, vimewauwa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na baadhi ya watendaji wa serikali. Tatizo hilo lilianza tangu mwaka 2014 lakini likafikia kilele mwaka 2017 baada ya operesheni ya kikatili ya vyombo vya dola kushambulia. Serikali inajaribu kuushawishi umma kwamba maandamano ya amani dhidi ya haki za kiraia na mauaji hayo ya MKIRU ni pande mbili za kitu kimoja. Ni watu wachache tu wanaoshawishika kuamini.
Katika ujumbe wao kwa msimu wa Kwaresma, maaskofu wa Katoliki walionya kwamba kuendelea kwa ukandamizaji wa kisiasa kutapelekea migawanyiko itakayohatarisha misingi ya kitaifa ya umoja na mshikamano. Walieleza kwamba kuzuwia shughuli za kisiasa sio halali na kunakiuka katiba. Kituo ch Demokrasia (TCD), ambacho huvileta pamoja vyama vya siasa kilitoa tamko la pamoja na viongozi wa Kikristo na Kiislamu kudai mapitio ya Katiba. Hii ilifuatiwa na kauli ya kuunga mkono ya vikundi zaidi ya 100 vya kiraia.

Jumapili ya Majivu Machi 25 ilishuhudia maaskofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (ELCT) wakitoa tamko kali wakiilaani utekaji watu, utesaji watu, upoteaji watu, mashambulizi ya silaha dhidi ya wanasiasa, mauaji yanayotokana na itikadi za kisiasa, vitisho, kesi za kubambikizwa, na unyanyaswaji wa raia unaofanywa na vyombo vya dola. Pia walitaka katiba mpya iwepo kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. "Taifa huongozwa na katiba ambayo ndio msingi wa sheria zote", walisema. "Haiongozwi na ilani za vyama."

Pia kuna changamoto za kisheria. Mahakama Kuu inatarajiwa kusikia kesi mbili za kikatiba zilizoletwa na watetezi wa haki za binadamu ikiwa ni pamoja na Chama cha Wanasheria TLS, Umoja wa Watetezi wa Haki za Binadamu (the Tanzania Human Rights Defenders Coalition), na Taasisi ya sheria na haki za binadamu (the Legal and Human Rights Centre). Kesi zote zinaongozwa na Fatma Karume wa kampuni ya uwakili ya IMMA, ambayo ofisi zake zilichomwa moto Agosti mwaka jana. Akiwa anatoka kwenye familia yenye nguvu ya Karume, amekuwa mwiba kwa utawala uliopo madarakani. TLS inaongizwa na mmoja wa wateja wake, kiongozi wa Chadema Tundu Lissu, ambaye bado yupo Ubelgiji anakopata matibabu ya majeraha ya risasi kufuatia jaribio la kumuuwa.

Kumekuwa na ukosoaji ndani ya CCM pia. Nape Nnauye, mbunge aliyetimuliwa uwaziri mwaka jana, ametoa wito wa kuifanyia marekebisho Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) akieleza "kwa macho makavu" kuwa kama ambavyo taasisi hiyo imekuwa ikifanya kazi kwa manufaa ya dola, pia imekuwa ikiitumikia CCM, inaendeshwa kisiasa.

Mbunge mwingine wa CCM, Hussein Bashe, ambaye awali hakufahamika kuwa na mtazamo huru, na aliongoza kampeni ya Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kuwania urais, naye ametokea kuwa mtetezi wa uhuru wa kujieleza na mawazo mbadala.

Haya na matamko mengine yanaashiria demokrasia ya Tanzania ipo katika kipindi kigumu. Akiongea kwenye shughuli ya TCD ambayo ilipelekea wito wa katiba mpya, Askofu Benson Bagonza wa Kanisa la Kilutheri alitanabaisha kuwa kamwe hajawahi kuona polisi wakitumia risasi dhidi ya waandamanaji. "Nini kimebadilika?" aliulizwa.

Moja ya majibu kwa swali lake hilo ni "hakuna kikubwa (kilichobadilika)." Kunapokuwa na upinzani mkali kwenye chaguzi zilizopita, dola na chama tawala vimekuwa vikikimbilia kwenye ukatili. Kufanya vema kwa Chadema katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kulipelekea angalau miaka miwili ya ukatili. Ilianza Januari 2011 ambapo polisi walitumia risasi dhidi ya maandamano ya wafuasi wa Chadema Arusha.
Februari 2012, wanaharakati 16 wa haki za binadamu walikamatwa kwa kuunga mkono mgomo wa madaktari. Agosti mwaka huohuo, polisi walimuua kwa risasi muuza magazeti huko Morogoro wakati wa maandamano ya Chadema. Mwezi uliofuata, mwandishi wa habari Daudi Mwangosi aliuawa na polisi kufuatia kupigwa na bomu la kutoa machozi huku akiwa amekandamizwa chini na polisi. Katika mwezi huohuo, kiongozi wa maandamano ya madaktari, Steven Ulimboka alitekwa, akateswa na kuachwa ajifie mwenyewe kwenye msitu nje ya jiji la Dar es Salaam, tukio linalodhaniwa kufanywa na maafisa wa TISS. Baadaye mwaka huo huo, na pia Mei 2013, njia za kikatili zilitumika kukabiliana na maandamano yaliyoambana na wimbi kubwa la machafuko katika historia ya Tanzania.

CCM inakabiliwa na changamoto kubwa kudumisha utawala wake. Kwa kutoongelea suala la ufisadi mkubwa (katika kampeni zake za uchaguzi mkuu wa) mwaka 2015, ilitoa fursa kwa Chadema kupata mafanikio (ya kuridhisha) katika uchaguzi huo. Wimbo la ukandamizaji linaloendelea hivi sasa, linailenga Chadema, na pia linachangiwa na hofu kuhusu vikundi vyenye msimamo mkali vyenye silaha (kama ilivyokuwa huko MKIRU).

Sintofahaumu hiyo inaweza kueleza ukatili mkubwa uliotumika kukabiliana na kilichokuwa kikijiri katika mkoa wa Pwani. Miili kadhaa iliyofungwa kwenye 'viroba' iliyokutwa inaelea maeneo ya (Msasani) Peninsula jijini Dar es Salaam inaashiria jinsi hali ilivyokuwa.

Wizara ya Mambo ya Nje ilitoa tamko masaa tu baada ya tovuti ya African Arguments ya Royal African Society kuchapisha habari iliyoeleza kuhusu matumizi ya silaha za moto dhidi ya waandamanaji huko wilayani Rufiji katika ofisi za halmashauri ya mji.

Kwa kuunganisha vitendo vya vikundi hivyo vilivyokuwa vinavyotumia silaha (huko MKIRU) na upinzani dhidi ya mageuzi yanayofanywa na Magufuli, inatoa kisingizio kwa dola kutumia nguvu dhidi ya makundi yote mawili (vikundi vya MKIRU na upinzani dhidi ya Magufuli).

Mkuu wa Majeshi Jenerali Venance Mabeyo aliwataka Watanzania kuwa wazalendo dhidi ya tishio kwa amani, umoja, uhuru na mshikamano. Kichekesho ni kwamba aliyasema hayo katika maadhimisho ya viongozi waliopambana na utawala wa mkoloni mwaka 1907 katika Vita ya Maji Maji. Jinsi dola inavyopambana na vurugu na upinzani inarejesha kumbukumbu za jinsi serikali ya mkoloni ilivyopambana na upinzani dhidi yake.

Mafanikio yoyote ya kuelezea kuhusu tishio linaloukabili demokrasia nchini Tanzania yatategemea zaidi makundi mbalimbali ndani ya CCM na tabaka tawala. Wanaoonekana kama wapinzani ndani ya CCM kama Nape na Bashe watabaki ndani ya chama hicho kwa gharama yoyote, wakicheza mchezo mrefu wa subira hadi uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 ambapo inatarajiwa Magufuli atamaliza muda wake.

Viongozi wa dini – Magufuli anajitambulisha kama Mkatoliki mcha Mungu – wanaweza kufanikiwa kumshawishi kupunguza matumizi ya vyombo vya dola dhidi ya upinzani. Lakini wanaharakati na wanasiasa wa upinzani wanafahamu fika kuwa kudhibitiwa kwa asilimia 100.

MHALAKI (SOCIALITE) AONGOZA MAPAMBANO KUPITIA MTANDAO WA KIJAMII WA INSTAGRAM

Mashtaka yanayofunguliwa na taasisi za kiraia na matamko ya viongozi wa dini ni kitu kimoja, lakini wito wa kufanyika maandamano unaotolewa na bloga mwenye makazi yake Los Angeles (Marekani), Mange Kimambi, ni changamoto tofauti kabisa kwa Magufuli. Kimambi amekuwa sura ya hadharani ya wito wa maandamano ya nchi nzima tarehe 26 Aprili dhidi ya Magufuli.

Akifahamika zaidi kwa masuala ya fasheni na habari zinazohusu watu maarufu, akaunti ya Instagram ya Kimambi imekuwa ikihamasisha na kuyapa umaarufu maandamano hayo, yanayotarajiwa kufanyika siku ya Muungano, ambayo ni kumbukumbu ya Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar.

Kimambi anayedhaniwa kuwa anashirikiana na wanaharakati nchini Tanzania, anachukuliwa kwa uzito mkubwa na mamlaka za nchi hiyo. Akiongea kwenye tukio moja Machi 9 kijijini kwake Chato, Magufuli alisema "tusubiri na tuone wakiandamana, na watanitambua." Siku chache kabla, Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba aliwatuhumu waandaaji wa maandamano hayo kuwa wanapanga kuuwa watu na kisha kuvitupia lawama vyombo vya dola. Maonyo mengine yametolewa na angalau makamanda wa polisi wa mikoa saba. Inafahamika kuwa viongozi wa serikali na chama (tawala) wameelekezwa kuhamasisha upinzani dhidi ya maandamano hayo na tayari watu kadhaa wameshakamatwa.

Kimambi ni mwanaharakati ambaye haingekuwa rahisi zamani kumtarajia. Alipata umaarufu mwaka 2009 kupitia blogu yake ya 'U-Turn' ambayo ilikuwa ikisimulia kuhusu maisha yake kama mhalaki huko Dubai. Baadaye alihamia katika makazi yake ya sasa, Los Angeles, kabla ya kuanza kuiteka Instagram mwaka 2015, ambapo alimpigia Magufuli kampeni yenye ufanisi, licha ya yeye kushindwa kuteuliwa kugombea ubunge jimbo la Kinondoni.

Alimgeuka Magufuli takriban Mei 2016 ambapo alipinga vikali kusitishwa kwa matangazo ya moja kwa moja ya vikao vya bunge. Anachanganya upinzani wa kisiasa na nguvu yake kama mhalaki anayeweza kumjenga au kumbomoa mtu kwa kutumia mitandao ya kijamii. Awali ilikuwa kuhusu picha zake binafsi na "selfies" lakini baadaye mabadiliko yakajitokeza. Kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, akaunti yake ikawa sehemu kuu ya harakati za mtandaoni za upinzani dhidi ya serikali, na sehemu ya kuona nyaraka mbalimbali zilizovuja.

Akaunti yake imechukua nafasi ya Jamii Forums, jukwaa la maoni mtandaoni lililokuwa kitovu cha upinzani mtandaoni, na ambalo waanzilishi wake wanakabiliwa na kesi mahakamani na wamekuwa wakisumbuliwa na mamlaka kwa muda mrefu.

Huku akiwa na wafuasi zaidi ya milioni 1.4* kwenye Instagram, uwezo wa Kimambi kuwafikia watu unawazidi wanasiasa wote wa Tanzania, japo kuna shaka kuhusu maandamano ya April 26. Kujitokeza kwa watu wengi kwenye maandamano hayo kutategemea uwezo wa waandaaji wake wa maandamano hayo nchini Tanzania, ambao wanaokabiliana na utawala usio na huruma – polisi watamwaga risasi kwa ajili ya kuuwa, kama ambavyo wamefanya huko nyuma.

Haitojalisha hata kama hakuna mtu atayejitokeza kuandamana Aprili 26. Kutoka umbali wa kilomita 26,000, Kimambi tayari ameweza kufanya zaidi ya kutikisa mkia wa chui kwa kutumia simu ya mkononi tu. Na laiti ikitokea asalimisha yeye mwenyewe, mara moja kukamatwa kwake kutakuwa tukio kubwa kabisa litakaloiweka Tanzania kwenye macho na masikio ya dunia nzima.

MAELEZO YANGU: Makala hii ni tafsiri ya neno kwa neno ya makala ya gazeti maarufu la duniani la habari za kuchunguza kuhusu bara la Afrika la AFRICA CONFIDENTIAL Toleo laMachi 28, 2018 lililokuwa na kichwa cha habari "Enemies Without And Within."

Nimejitahidi kadri nilivyoweza kufanya tafsiri ya karibu kabisa kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili. Ni vigumu kufanya tafsiri timilifu kwa asilimia 100 hasa pale mwandishi na mtafsiri ni watu wanaoongea lugha mbili tofauti. Ni rahisi kwa mtu aliyeandika mwenyewe kufanya tafsiri ya alichoandika kuliko kazi hiyo kufanywa na mtu mwingine.
* Idadi ya "followers" kwenye akaunti ya Mange kwa sasa ni watu milioni 1.8.






27 Feb 2018




Nianze makala hii kwa kuwashukuru ndugu nyote mlionitumia salamu za upendo,kunipa pole/kunipa moyo baada ya jina langu kutajwa miongoni mwa watu 9 wanaodaiwa kuwa hatari kwa usalama wa Tanzania.

Orodha hiyo ilitajwa na mtu mmoja anayejiita Cyprian Musiba japo taarifa nilizonazo ni kwamba jina hilo lina walakini kama lilivyo jina la rafiki yake – na miongoni mwa watu waliofanikisha press conference yake – Daudi Albert Bashite. Waingereza wanasema "birds of a feather flock together."


Kichekesho ni kwamba mara ya kwanza kumfahamu mtu huyo ni wakati flani aliponitumia ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter akinifahamisha kuwa wana gazeti lao linaitwa 'Tanzanite' na kuniomba niwe nawatumia makala. Nilipuuza ombi hilo kwa sababu kutoka level ya kuandikia gazeti kubwa kama Raia Mwema kwenda kuandikia kijigazeti kipya kama hicho cha Tanzanite ingekuwa kujishushia heshima yangu.

Kwa upande mmoja,tuhuma za huyo mtu hazijanishangaza kwa sababu kadhaa. Kwanza, tunafahamu fika ugumu wa maisha huko nyumbani, na sio suala la ajabu kuona baadhi ya watu wakiuza utu wao ili mradi tu "njia ya kwenda msalani isiote nyasi."

Lakini pili, kuna jitihada kubwa za kuigeuza Tanzania kuwa kama wilaya ya Kanda ya Ziwa. Huyo mtoa tuhuma ana asili ya maeneo hayo, na kuna hali inayozidi kuota mizizi kwa baadhi ya wahuni wanaotoka eneo moja na Magufuli kujiona wana hatimiliki ya Tanzania yetu.

Jingine ambalo lilinifanya nipuuze hizo tuhuma za huyo bwege ni ukweli kwamba safari yangu kimaisha hadi hapa nilipo imepshapitia vilima na mabonde. Nimeshaeleza mara kadhaa kuhusu janga lililonisibu Februari 2, 2013 ambapo chombo kimoja cha usalama hapa kilinifahamisha kuwa kuna tishio dhidi ya uhai wangu, tishio from Tanzania. Na kwa zaidi ya mwaka mzima tangu wakati huo, nikawa ninaishi maisha ya kutambua kuwa muda wowote ule naweza kudhurika. Licha ya ugumu mkubwa, hali hiyo ilinipa uzoefu wa kuishi na vitisho.

Lakini pia, hiyo hatua tu ya huyo mzembe kunituhumu naona kama tusi flani kwangu. Mie sio wa kutuhumiwa na mtu asiyejulikana kama yeye. Ilipaswa labda awe kigogo flani wa Usalama wa Taifa, ndo ningeweza kuchukulia suala hilo seriously. Wanasema "usiongee na mbwa bali ongea na mwenye mbwa."

Hata hivyo, japo sikushangazwa na tukio hilo la kihuni, nilikerwa na vitu vikuu vitatu. Kwanza, wakati nina uhakika wa asilimia 100 kuwa huyo bwege ametumwa tu, nilikerwa mno na uongo wa mchana kweupe uliokuwemo kwenye tuhuma zake. Uongo huo ni pamoja na kudai kuwa FBI ni shirika la ujasusi la Marekani. Hivi hao wapuuzi waliomtuma hawakufanya research japo kidogo ya kuwaelewesha kuwa shirika la ujasusi la Marekani ni CIA na sio FBI?

Halafu huyo bwege akachapia tena kwa kudai kuwa chama cha Kansela Angela Markel ni CDP ilhali chama chake ni CDU. Halafu sijui ni mie tu na "macho yangu ya kishushushu" niliyeona huyo jamaa akiongea kwa kuhema kana kwamba anakimbizwa, huku amejawa na uoga mkubwa. Hizi njaa zitakuwa watu mwaka huu. Seriously!

Kingine kilichonikera ni jinsi huyo bwege alivyopewa umuhimu mkubwa asiostahili. Hivi kwa mfano hiyo video ya press conference yake ingepuuzwa, nani angejua kuwa kuwa mwendawazimu flani kuitisha press conference kutuhumu watu kadhaa wenye heshima zao katika jamii? Kuna nyakati ukimya una nguvu zaidi ya kupigiana kelele na mtu. So far, huyo mhuni amefanikiwa kufikisha ujumbe wake kwa watu wengi mno kutokana na sie wenyewe – including tuliotuhumiwa -kumsaidia kusambaza ujumbe wake muflis. Anyway, by muda huu hizo 15 minutes of fame zimeshaisha muda wake.

Lakini pia nilikerwa na ukweli kwamba uhuni wa aina hii ukiachwa tu bila kuchuliwa hatua unaweza kusababisha madhara makubwa huko mbele. Maana tumeshaona jinsi Bashite alivyoweza kuvamia studio za Clouds kisha Rais Magufuli bila aibu akamtetea hadharani na kumsifia kuwa ni mchapakazi. Kwa kifupi, huko ni kusherehesha uhuni.

Sasa huyu bwege si mara ya kwanza kuibuka na press conference za kiendawazimu.Last time aliitisha press conference na kutishia kumfungulia mashtaka shujaa Tundu Lissu. Katika tukio hilo nilikerwa zaidi na ukweli kwamba kuna viumbe wenye roho mbaya kama wachawi, ambao hawajatosheka na mateso aliyepitia Lissu baada ya karibio la kutaka kumuuwa. Mie nimesoma"War Studies" na miongoni mwa kanuni za vita ni kwamba pindi adui yako akiwa chini basi unatarajiwa kutomdhuru. Kwahiyo hata kama Lissu ni adui yao, basi angalau wangesubiri apone kwanza kabla ya kuanza kumwandama namna hiyo

Kwa taarifa nilizonazo, press conference ya huyo bwege inamhusisha Bashite ambaye bila shaka ana baraka za baba yake, lakini pia watu wa Kitengo nao wamehusika. Ni vigumu kujua "kitengo kipi" maana kwa sasa ni kama tuna "Idara mbili" – hiyo tunayoifahamu na hiyo "kampuni binafsi ya ulinzi wa JPM/Bashite."


Lakini kubwa zaidi, na hasa ndio lengo la makala hii ni kuwafahamisha Watanzania wenzangu kwamba tafsiri halisi ya tuhuma zilizotolewa kwenye hiyo press conference ni kuwafanya ninyi Watanzania hamna akili ya kuweza kubaini nani hasa ni tishio kwa usalama wa taifa lenu.

Twende hatua kwa hatua japo kwa umbali mfupi tu.Hivi katika ya hao watu tisa ni yupi alishiriki kupanga na kutekeleza shambulio la kinyama dhidi ya Lissu? Kibaya zaidi, Lissu nae yumo katika orodha hiyo.

Je ni yui kati ya hao tisa alitoa ruhusa kwa askari kumpiga risasi na kumuuwa binti asiye na hatia Akwilina? Je ni nani kati yetu aliyehusika na mauaji wa Katibu wa Chadema Kata ya Hananasifu marehemu Daniel na Diwani wa Kata ya Namwawala Marehemu Luena? Maana kwa matukio haya matatu tu, na pengine la nne ni la Lissu, inatosha kuonyesha kuwa kuna pattern ya mauaji dhidi ya raia wasio na hatia. Na kwa vile hakuna jitihada zozote za vyombo vya dola kuwasaka wahusika na kuwatia nguvuni, yayumkinika kuhisi ushiriki wa serikali ya Magufuli katika matukio yote hayo.

Sasa yule bwege kuwaona ninyi Watanzania hamnazo, kwamba "anamudu kuwalisha matango pori" kwa kudai kuwa huyo na huyu ndiyo tishio kwa usalama wa nchi yetu, ilhali kila mwenye akili timamu anafahamu bayana kuwa tishio kubwa zaidi kwa sasa linatoka kwa WATU WASIOJULIKANA.

Image result for watu wasiojulikana

Je sie tisa tuliotajwa ndo tumegeuka kuwa "watu wasiojulikana" ambao sote wenye akili timamu twatambua ndio tishio kwa usalama wa Tanzania?

Ni rahisi kulitazama suala hilo kama ni uhuni wa huyo mbwa dhidi yetu lakini kiukweli mbwa huyo kawanyea Watanzania wote wenye akili timamu. Kawafanya hamna uwezo wa kutofautisha pumba na mchele. Huyu mtu ni adui yenu zaidi ya adui wa sie aliotutuhumu.

Sasa je hasira yako dhidi ya mtu huyu na waliomtuma unaionyeshaje? Mie ushauri wangu ni mwepesi tu: kama una uwezo wa kuwasomea dua mbaya, itakuwa vema. Kama una utaalamu wa masuala ya asili, basi ni vema pia. Hata ukitukana kimoyomoyo ni vema pia. Lakini ukipata wasaa wa "kumpa a uso" popote pale – iwe mtandaoni au mtaani – tafadhali fanya hivyo.

Naamini kabisa kati ya sie tisa tuliotajwa na huyo bwege, tuna watu walio tayari kutafuta haki kwa ajili yetu.Na haki si lazima ipatikane mahakamani. Na mahakama zenyewe hizi zinazoendeshwa kwa rimoti na Magufuli hadi kumfunga Sugu wala hazina maana. Ombi langu kwenu ni kila aina ya laana dhidi ya mtu huyo, si kwa sababu labda ana umuhimu flani bali ukweli huo niliyotanabaisha hapo juu kuwa amewaona ninyi Watanzania kama hamnazo hadi kufikia hatua ya kutuzushia sie tusio na hatia tuhuma hizo za kuhatarisha usalama ilhali sote tunafahamu vema akina nani wanaohatarisha usalama wa Tanzania yetu.

Kama ukinitumia picha wakati unamfanyia kisomo huyo mbwa basi itakuwa vema sana haha


18 Feb 2018


Nianze makala hii kwa kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daniel John, ambaye hadi alipouawa kinyama alikuwa Katibu wa Chadema kata ya Hananasifu, na pia kwa familia, ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Acqulina Akwilin (samahani kama nimekosea jina).

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, mwili wa marehemu Daniel uliokotwa kwenye ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam ukiwa na majeraha. Alieleza kuwa awali marehemu alichukuliwa na Land Rover nyeupe na watu waliohifanya askari polisi, lakini tangu wakati huo Polisi hawakuwa na taarifa zozote za kiuchunguzi, na hata jitihada za kupatikana mwili huo zilifanywa na Chadema wenyewe.




Kwa upande wa marehemu Acquilina, kifo chake kilisababishwa na kasumba hatari inayozidi kuzoeleka kwa watumishi wa vyombo vya dola kufanya mzaha katika matumizi ya silaha za moto, ambapo katika tukio husika, polisi waliokuwa wakizuwia maandamano ya wafuasi wa Chadema, walitumia risasi za moto,na moja kati ya risasi hizo ilipelekea kifo cha binto huyo, ambaye hadi mauti yanamfika alikuwa mwanafunzi katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) akisomea shahada ya ununuzi na ugavi.
Ni muhimu kutambua kuwa vifo vyote hivi viwili vingeweza kuepukika laiti utu na ubinadamu wetu ungewekwa mbele ya chuki za kisiasa. Huhitaji kuwa mjuzi wa uchunguzi wa mauaji kufahamu kuwa vifo hivyo ni matokeo ya chuki, hujuma, uonevu na kila aina ya baya dhidi ya chama kikuu cha upinzani, Chadema, kuhusiana na kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Kinondoni, ambalo kama ilivyo kwa jimbo la Siha, ni "piga ua" kwa CCM ishinde. Yaani chama hicho tawala kilitarajiwa kutumia kila mbinu kuhakikisha inashinda katika majimbo hayo mawili.

Lakini kabda sijaingia kwa undani katika mada hii - ambayo lazima nikiri kwamba inanipa wakati mgumu sana kuiandika kwa sababu nimebanwa na mchanganyiko wa majonzi na hasira, sambamba na hofu ya kuona taifa langu likisukumwa kuelekea kwenye upotevu wa amani na mshikamano wetu – naomba kuweka wazi masuala matatu ya msingi kunihusu mie mwandishi wa mwakala hii.

Kwanza, mimi licha ya kuwa na makazi nje ya Tanzania kwa takriban miaka 15 sasa bado no Mtanzania. Utanzania wangu ni haki nilioirithi kutoka kwa wazazi wangu, na itabaki hivyo milele. Naeleza hili kwa sababu kuwa wabaguzi wanaopenda kutuhukumu Watanzania tunaoishi huku ughaibuni, na kutaka tuonekane kama Utanzania wetu sio kamili. Kwa mantiki hiyo, kama Mtanzania, nina kila haki ya kutoa maoni yangu kuhusu mustakabali wa taifa letu, hususan katika nyakati hizi ambapo kuna dalili za wanaotaka kulipeleka kubaya taifa letu.

Pili, mwaka 2015 nilishiriki kikamilifu katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais John Magufuli. Kwa upande mmoja nililazimika kumkampenia Magufuli kwa vile nilikuwa nina "sababu binafsi" dhidi ya aliyekuwa mpinzani wake mkuu, mgombea urais wa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Wanasema "adui ya adui yako ni rafiki yako."Kwa upande mwingine, nililipwa kutoa huduma ya ushauri wa kitaalamu (usadi, yaani consultancy kwa kimombo) hususan kwenye mitandao ya kijamii. Natanabaisha hili ili asije akakurupuka mtu na kusema "ah ulishiriki kutupigia kampeni kwa vile tulikupa pesa."

Tatu, huko nyuma nilikuwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Na kabla ya kuanza utumishi katika taaluma hiyo muhimu na nyeti, nilikula kiapo kwa nchi yangu, kiapo ambacho nitaishi nacho hadi ninaingia kaburini. Kiapo hicho sio cha kukitumikia chama flani au viongozi wake bali Tanzania yetu. Nchi ni muhimu  kuliko vyama vya siasa au wanasiasa.

Mtu aliyepikwa na kuiva kwenye taaluma ya uafisa usalama wa taifa, katika nchi yoyote ile, anapaswa kubaki kuwa mtiifu kwa nchi yake bila kujali yupo ndani au nje ya ajira ya taasisi inayohusika na usalama wa taifa wa nchi husika.

Wanasema hata nje ya ajira rasmi, kila mtu aliyewahi kuwa afisa usalama wa taifa anaendeshwa na "sense of public duty born in their previous lives" yaani wajibu kwa umma uliozaliwa katika maisha yao huko nyuma. Jasusi mmoja mstaafu anaeleza “...I have obligations, professional obligations. If there’s a national security emergency or possible national security issue, I should report it."


Kwahiyo, hata kama "maafisa wenzangu wa zamani" wataamua kukaa kimya kwa sababu moja au nyingine – wengi wanahofia usalama wa maisha yao – sie wengine hatuwezi kukaa kimya, hasa kwa vile baadhi yetu tumeshalipa gharama kubwa kwa kelele zetu. Kukaa kimya ni sawa na kuafiki uhuni unaoendelea ambao ni tishio kwa usalama wa taifa.

Lakini licha ya wajibu huo unaotokana na utumishi wetu kwa nchi huko nyuma, Rais Magufuli amefanikiwa kuvifunga mdomo vyombo vya habari kiasi kwamba haviwezi kusema lolote kuhusu "mabaya" yake, na amefanikiwa kuvijengea nidhamu ya uoga vyombo hivyo vya habari kiasi kwamba habari pekee zenye umuhimu kwao ni za kumtukuza na kumpamba "mungu-mtu" huyo. Kwahiyo na sie tuliopikwa na kuiva kuhusu ujasiri, kujitoa mhanga na kutokuwa waoga tukiufyata na kukaa kimya - ilhali media zetu ndio zishapigwa kufuli - hali itazidi kuwa mbaya.


Baada ya kuweka wazi nafasi yangu, sasa tuangalie kwa kina kinachoendelea huko nyumbani hasa kuhusiana na uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni na Siha na kuuawa kwa Daudi na Acquiline.

Ni muhimu kutambua kwamba ukandamizaji dhidi ya vyama vya upinzani sio kitu kilichoanza chini ya utawala wa Magufuli bali hali hiyo imedumu mfululzo tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1992. Labda kilicho tofauti kwa zama hizi ni "ujasiri" wa Magufuli kutoficha chuki yake dhidi ya vyama vya upinzani. Yaani angalau akina Mwinyi,Mkapa na Kikwete walikuwa "wanauma na kupuliza." Kwamba angalau walikuwa na "mshipa wa aibu" na walijitahidi japo kutowaonea Wapinzani waziwazi.

Kwa wanaojua "yanayojiri nyuma ya pazia" watakwambia kuwa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa CCM na serikali zake, na hiyo imepelekea kujengeka "symbiotic relationship" kati ya chama hicho tawala na taasisi za dola, ambapo kila mmoja anategemea uhai wa mwenzie.

Lakini kama kuna kitu kinachokera zaidi kuhusu hujuma dhidi ya demokrasia ni pale CCM na taasisi zake hasa za dola wanapoweka mbele maslahi yao mbele ya utu na uhai wa Watanzania. Na hili halijaanza jana au katika kampeni za chaguzi ndogo katika majimbo ya Kinondoni na Siha.

Uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 ulihusisha matukio mengi tu ambayo kwa makusudi hayapo kwenye kumbukumbu za wazi (japo yamehifadhiwa mahala flani).

Lakini kama wanavyosema "amekula asali sasa anachonga mzinga," baada ya hujuma za kimyakimya za mwaka 1995 kuzaa matunda, CCM na taasisi zake ikanogewa, na matokeo yake ni kwamba uchaguzi mkuu uliofuata, mwaka 2000 uliweka doa kubwa kwa historia ya Tanzania yetu ambapo kwa mara ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kufuatia unyama uliofanyika huko Zanzibar na kupelekea vifo kadhaa (idadi halisi ya vifo haijawahi kuwekwa hadharani japo "wenyewe" walisema zaidi ya watu 19 ndio waliokufa kwenye machafuko hayo. Wasichosema pia ni idadi ya watu waliobakwa, kuteswa na kuwekwa kizuizini.

Kwamba hujuma hizo za CCM dhidi ya demokrasia zilipelekea vifo na majeruhi ni kitu kibaya kabisa. Lakini kitu kingine kibaya ni ukweli kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyechukuliwa hata kutokana na unyAma waliofanyiwa Wazanzibari hao.

Kwa namna ya kipekee, CCM ikawa kama imepewa ruhusa ya kutumia vyombo vyake vya dola kufanya lolote itakalo ili ifanikishe hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla, kisha iibuke na ushindi.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ulikuwa na "uchafu kupindukia." Kundi lililofahamika kama "mtandao" lilijipenyeza katika kila sekta, kuanzia kwenye vyombo vya habari, taasisi za dola hadi kwenye taasisi za dini. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kwamba yaliyojiri wakati "mtandao unafanya jitihada za kumwingiza mtu wao Ikulu" ni mabaya zaidi ya haya tunayoshuhudia sasa tangu Magufuli aingie madarakani.

Kwanini basi hayo yaliyojiri kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 hayajulikani? Jibu ni kwamba, wakati mbinu iliyotumika mwaka 1995 na 2000 ilitegemea zaidi vyombo vya dola, uchaguzi wa mwaka 2005 na 2010 ulitegemea zaidi nguvu ya fedha, nyingi zikiwa fedha haramu. Na sehemu ya fedha hiyo ilitumika "kununua ukimya" wa wanahabari wengi tu. 

Lakini si fedha tu bali pia kuna hujuma mbalimbali – nyingine chafu na za kuchefua – zilizotawala safari za ushindi wa chama tawala kwenye chaguzi hizo.


Image result for lowassa kikwete 2005

Labda tofauti nyingine kuhusu mwaka 2005 na 2010 ni ukweli kwamba wakati chaguzi hizo zilihusisha "kikundi binafsi" yaani hicho cha wanamtandao ambacho hakikuwa taasisi ya serikali au chama.

Lakini muda wote huo, CCM ilikuwa kama imepwa ruhusa na Watanzania kuendeleza hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla. Hakujawahi na utashi miongoni mwa Watanzania kutaka kukabiliana kwa dhati za uhuni/uhalifu wa kisiasa. Na kwa bahati mbaya, kwa vile vipaumbele vya Watanzania wengi ni kwenye "ubuyu" na "kubeti/mkeka" basi habari mbaya ni uwezekano wa CCM kuendelea kufanya itakavyo kwa muda mrefu sana.

Sio kama kwa kubashiri kuwa unyanyasaji wa CCM utaendelea muda mrefu sana ninamaanisha kuwa nimekata tamaa. Hapana. Ninakuwa mkweli tu. Tatizo ni zaidi ya CCM na uhuni wake. Watanzania wenyewe ni sehemu ya mfumo unaowezesha CCM kufanya uhuni/uhalifu huo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulihusisha pia matuki kadhaa yaliyojiri "nyuma ya pazia." Na ukitaka kufahamu kuwa Tanzania yetu haijawahi kuhangaishwa na mauaji ya kisiasa – kuanzia yale ya mwaka 2001 huko Zanzibar hadi haya ya Daudi wa Hananasifu na dada Acquilina – ni kifo cha Mchungaji Christopher Mtikila.


Kwahiyo, na ninaandika haya kwa uchungu mkubwa uliochanganyika na hasira, kuuawa kwa Daudi na Acquilina kutaishia kuwa moja tu ya matuko yaliyowahi kutokea katika Tanzania yetu. Tutawasikia wanasiasa wetu wa vyama vya upinzani wakiongea kwa hisia kubwa. Tutashuhudia pia wanafiki wengi tu miongoni mwa wasanii wetu nao wakijifanya kuguswa na vifo hivyo, lakini wakiwa makini kuepuka kumuudhi "Bashite na baba yake" au kuitibua CCM. Tutashuhudia pia kundi la wanafiki hatari ndani ya CCM wakijifanya kuumizwa na mauaji hayo, na kutaka uchunguzi ufanyike, ilhali nao ni kondoo waliojivika ngozi ya mbwa mwitu.



Kama ambavyo "mauaji mengine ya kisiasa" yalivyoruhusiwa kupita kimyakimya, ndivyo unyama huu uliofanywa dhidi ya Daudi na Acquilina utakavyoruhusiwa uishe kimyakimya.

Kwa upande mmoja tusitarajie Rais Magufuli awajibike – sio kwa yeye binafsi kujiuzulu kwa sababu hilo litakuwa kutarajia zaidi ya muujiza – kwa kumtimua Waziri husika na watendaji katika jeshi la polisi. Kwa upande mwingine, hakuna wa kumshinikiza Rais Magufuli achukue hatua stahili dhidi ya wahusika.

Na nisingependa kuuma maneno hapa. Yeye Magufuli mwenyewe ni chanzo muhimu cha siasa hizi za uhasama zinazoendelea kuitafuna Tanzania yetu. Huyu ni mtu ambaye wala hapati shida kuonyesha chuki zake za waziwazi dhidi ya Wapinzani, Upinzani na demokrasia kwa ujumla.


Kama ilivyo kwa madikteta wengine duniani, Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutumia ajenda yake ya ufisadi kama kisingizio cha kusigina haki za binadamu nchini Tanzania, na kubinya kila fursa ya haki za kidemokrasia na uhuru wa habari. Kama nilivyoeleza awali, amefanikiwa kuviziba midomo vyombo vya habari na ndio maana hata habari za kusikitisha kuhusu mauaji ya Daudi na Acquiline hazijaripotiwa vya kutosha.

Kwa kuviziba midomo vyombo vya habari Magufuli amefanikiwa kuzuwia "habari asizozipenda" na ndio maana hadi muda huu ni Watanzania wachache tu wanaofahamu kilichojiri huko MKIRU katika kilichoitwa "operesheni dhidi ya ugaidi." Kuna siku yaliyojiri huko – na ambayo yamechangia "kupotea" kwa mwandishi wa gazeti la Mwananchi Azory Gwanda – yatajulikana hadharani. Haijalishi itachukua miaka mingapi.


Lakini "yaliyojiri MKIRU" ni uthibitisho mwingine wa hicho nilichoeleza hapo juu kuwa Watanzania wenyewe ndio wanaopaswa kubeba lawama nyingi katika kasumba ya CCM kutojali uhai katika harakati zake za kukandamiza demokrasia. Kwamba kama yaliyojiri MKIRU yameachwa yaishe kienyeji, kwanini tutegemee hali tofauti kwa vifo vya Daudi na Acquiline?

Kama ndugu zetu wa Chadema (na kila mpenda haki) "wamekubali yaishe" kuhusu kifo cha Kamanda Mashaka, "kupotea" kwa kada Ben Saanane (hata zile kampeni za #BringBackBenAlive zimejifia kifo cha asili), na hawasumbuliwi na serikali ya Magufuli kupuuzia jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu, kwanini tutarajie jipya katika mauaji yaliyofanywa dhidi ya Daudi na Acquiline?

Yaani Mnadhimu Mkuu wa upinzani anamwagiwa risasi hadharani wakati mkutano wa bunge unaendelea huko Dodoma, na tunaambiwa kuwa tukio hilo lilitokea katika eneo lenye ulinzi mkubwa na lenye CCTV, kwanini basi wanaosumbuliwa na tukio hilo wasitafute njia stahili za japo kuifanya serikali ione aibu na kufanya japo "uchunguzi wa kizushi"?

Kuhusu hujuma "za kawaida" za uchaguzi, kama kila aina ya uhuni uliofanywa na CCM kwenye chaguzi ndogo za madiwani katika kata 43 uliofanyika Novemba mwaka jana uliruhusiwa upite "kimya kimya" – kwa maana kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya uhuni huo – kwanini basi chaguzi hizi ndogo katika jimbo la Siha na Kinondoni zilitarajiwa kuwa tofauti?

Na katika hili, inapaswa wana-Chadema wajiulize kuhusu busara za viongozi wao kuamua kushiriki katika chaguzi hizo ndogo Siha na Kinondoni ilhali mazingira yaliyokuwepo yalikuwa yaleyale yaliyopelekea chama hicho kususia chaguzi nyingine ndogo tatu katika majimbo ya Longido, Singida Kaskazini na Songea Mjini uliofanyika mwezi uliopita.

Hadi wakati ninaandika makala hii, tayari Tume ya Uachaguzi ilikuwa imeshamtangaza mgombea wa CCM jimbo la Siha, Godwin Mollel kuwa mshindi kwa tofauti kubwa tu ya kura dhidi ya mgombea wa Chadema. Hata kama CCM wameiba kura, ukubwa wa tofauti kati ya kura za mgombea wao na huyo wa Chadema zinaashiria kuwa chama hicho kikuu cha upinzani kilipitisha mgombea fyongo.


Na kama ilivyotarajiwa mgombea wa CCM jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia, naye ametangazwa mshindi.


Mie mtumishi wako nilishabashiri mapema tu kuwa chama hicho tawala kingeshinda majimbo hayo, "iwe isiwe."

Ushindi kwa wagombea hao wa CCM ulipaswa kupatikana kwa gharama yoyote kwa sababu laiti wangeshindwa, kinachoelezwa kama "mkakati wa Magufuli kuua upinzani kwa kununua wabunge na madiwani wa Upinzani"  kingemfanya achekwe hata huko kwenye chama chake.

Na kwa vile hadi sasa wabunge na madiwani waliohama upinzani na kujiunga na CCM wamefanikiwa kurudi madarakani baada ya chama hicho tawala kuwapa fursa ya kuwa wagombea wake kwenye chaguzi ndogo, na kuwasaidia kwa hali na mali washinde, tutarajie wabunge na madiwani wengin zaidi kuhama vyama vya upinzani na kujiunga na CCM. Kisa? "Dili hilo linalipa," kwa CCM na kwa wanasiasa hao wanaohama.

Na unadhani mbunge au diwani "mwenye moyo mwepesi" akiona jinsi chama chake "kilivyochukulia poa" yaliyowasibu akina marehemu Mashaka na Daudi, na yaliyowasibu Ben Saanane na Lissu, kwanini iwe ngumu kwake kushawishika kuhama?

Ningetamani sana kuhitimisha makala hii kwa kushauri nini kifanyike lakini itakuwa kupoteza muda wangu na muda wako msomaji. Ni vigumu mno kuwashauri watu waliokubali kwamba mgao wa umeme ni stahili yao kwa zaidi ya miaka kumi sasa, na ambao kila mara umeme unaporudi wanashangilia kana kwamba wamepewa upendeleo flani.

Kama Watanzania wameshindwa kuilazimisha Tanesko iache mgao wa umeme, wataweza kweli kuilazimisha CCM iache hujuma dhidi ya vyama vya upinzani na demokrasia kwa ujumla? Ndio maana bila utu wala aibu, chama hicho tawala kinapata ujasiri wa kukifanyia mzaha kifo cha Acquiline ambapo kwa kudai polisi (haohao waliomuua binti huyo) wachukue hatua dhidi ya Mbowe. Utterly disgusting!


Na kama mauaji mbalimbali ya kisiasa huko nyuma yameachwa yapite na kusahaulika, kwanini tutarajie miujiza kwenye mauaji haya ya sasa dhidi ya wapendwa wetu Daudi na Acquline?

Na ukweli mchungu ni kwamba Magufuli ataendelea kuwapelekesha Watanzania atakavyo ka sababu si watangulizi wake -Mwinyi, Mkapa na Kikwete – wenye jeuri ya kumwambia "Ee bwana ee, huku unakoipeleka nchi siko." Hawawezi kwa sababu nao ni kama "mateka." Madhambi waliyofanya kwenye tawala zao yanawafanya wahofie hatma yao pindi wakimkosoa "mungu-mtu" aliyepo madarakani.

Na wakati wastaafu au watumishi wa zamani wa Idara za Usalama wa Taifa kwenye nchi kama Marekani wamekuwa mstari wa mbele kukemea kila tendo linalotishia usalama wa nchi hiyo – kwa mfano 'ndoa' kati ya Rais Donald Trump na Russia – wastaafu wetu sie hawana jeuri ya kufungua mdomo sio tu kwa vile wanahofia kuathiri posho na marupurupu yao bali kwa vile nao ni mateka wa "madudu" waliyofanya walipokuwa madarakani. Ukiwa mchafu unajinyima uhuru wa kukemea uchafu.


Basi niishie hapa kwa kurejea tena salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daudi na Acquiline. Ni vigumu kuwaambia maneno yanayotosha kuwaliwaza lakini la muhimu ni kuendelea kuzikumbuka roho za marehemu hao, hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma ambapo sisi Wakristu tunaadhimisha mateso ya Bwana Yesu Kristo. Pumziko la Milele awape Bwana, na Mwanga wa Milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amen


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.