17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-46

Asalam aleykum,

Wiki hii ilianza vizuri kwa Watanzania wanaoishi hapa Uingereza kutokana na ziara ya Rais Kikwete.Kama nilivyoonyesha wasiwasi wangu katika makala iliyopita kuhusu iwapo ningehudhuria mkutano wa JK na wabongo hapo London,ndivyo ilivyotokea.Kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu sikubahatika kuhudhuria mkutano huo uliofanyika Jumapili iliyopita.Labda ntabahatika atakapokuja tena mwezi ujao kama alivyoahidi.Kwa mujibu wa waliohudhuria na kama nilivyotabiri katika makala iliyopita,kulikuwa na umati mkubwa uliojitokeza kumsikiliza kiongozi mkuu wa nchi yetu.Nimeambiwa kuwa ukumbi “ulicheua.”Japo mkutano huo ulimalizika bila wahudhuriaji kuuliza maswali kutokana na majukumu mengine alivyokuwa nayo Rais,wengi wa waliohudhuria walivutiwa na hotuba ya JK.Pengine jambo ambalo lilionekana kuwagusa baadhi ya watu ni kitendo cha baadhi ya wana-CCM tawi jipya la London walioonekana kama walitaka “kuiteka” shughuli hiyo.Binafsi sidhani kama hilo ni tatizo hasa ikizingatiwa kuwa nchi hii inathamini uhuru wa watu kuonyesha hisia na ushabiki wao katika kile wanachokipenda.Kwa mantiki hiyo,wana-CCM hao waliochangamka chapchap kufungua tawi la chama hicho siku chache zilizopita waliokuwa na kila sababu ya kujimwayamwaya na ujio huo wa Mwenyekiti wa chama chao ambaye pia ni Rais wetu.Napenda kuamini kuwa vuguvugu la ukereketwa wa chama tawala litakuwa ni la kudumu na sio la kupita tu kwa malengo ya watu wachache kupata nafasi ya kutambulishwa kwa JK.Kama wasemavyo waswahili,kupata ujauzito si kazi bali kazi ni kumtunza mtoto hadi akue.Vilevile,ufunguzi wa matawi ya chama si kazi bali shughuli ipo katika kudumisha na kumarisha matawi yanayofunguliwa.

Mwaka huu Muungano kati ya England na Scotland (ambao unatengeneza sehemu ya kitu tunachokijua kama the United Kingdom) unatimiza miaka 300 tangu uzaliwe. “Bethdei” ya Muungano huo inafika wakati vuguvuru la Scotland kutaka uhuru wake linazidi kupamba moto.Kwa mara ya kwanza,hivi karibuni kura ya maoni ilionyesha zaidi ya asilimia 50 ya Waskotishi walikuwa wanataka uhuru wao nje ya United Kingdom.Muda mfupi kabla sijaandaa makala hii nilikuwa naangalia mjadala uliokuwa unaendeshwa na BBC Scotland kuhusu suala hilo la uhuru wa Scotland.Kuna matukio mawili makubwa yanayotarajiwa hivi karibuni ambayo kwa namna flani yanachochea mjadala huu.Kwanza ni uchaguzi mkuu wa Scotland ambapo kiongozi wa chama cha Scottish National Party (SNP) Alex Salmond anaelekea kufanya vizuri kwenye kura za maoni dhidi ya “Waziri Mkuu” (First Minister) wa Scotland,Jack McConnell,ambaye anatoka chama cha Labour.Moja ya sera kuu za SNP ni kudai uhuru wa Scotland,na ingawaje siku za nyuma sera hiyo imekuwa ikipata mwamko mdogo,hivi sasa inaelekea kupata wafuasi wengi zaidi.Wachambuzi wa mambo ya siasa za Uingereza wanatabiri kuwa iwapo Salmond na SNP yake watashinda basi “ndoto” ya Scotland kuwa taifa linalojitegemea nje ya United Kingdom inaweza kutimia.

Kwa upande mwingine,Tony Blair anatarajiwa kung’atuka mwezi Juni mwaka huu na kila dalili zinaonyesha kuwa mrithi wake atakuwa Kansela Gordon Brown.Brown ni Mskotishi na hivi karibuni ameanzisha “jihad” dhidi ya wale wenye fikra za uhuru wa Scotland.Amekuwa akisisitiza kuwa Scotland inanufaika zaidi ikiwa sehemu ya UK kuliko itapotokea kuwa nje ya Muungano huo.Hivi majuzi alikishambulia chama cha upinzani cha Conservative kuwa kimekuwa kikisapoti madai ya uhuru wa Scotland.Kimsingi,baadhi ya wanasiasa wa England hawafurahishwi kuona wabunge kutoka Scotland wakipiga kura katika baadhi ya mambo ambayo yanaihusu England,ilhali hakuna mbunge kutoka England anayeweza kufanya hivyo katika bunge la Scotland.Kadhalika,baadhi ya wanasiasa wa England wanaona “influence” ya wanasiasa wa Kiskotishi inakuwa kwa kasi katika serikali ya Muungano.Hapa wanapointi watu kama Gordon Brown,Waziri wa Mambo ya Ndani John Reed,Waziri wa Usafiri Alistar Darling na Waziri wa Ulinzi Des Browne.Wote wanaonekana kushika nafasi nyeti katika serikali ya Uingereza,na kwa namna flani wanaonekana kama Waskotishi wenye uwezo wa kutoa maamuzi kuhusu mambo ambayo pengine ni ya England pekee ambayo kwa namna nyingine yangepaswa kutolewa maamuzi na wanasiasa kutoka England tu.Na suala la Gordon Brown kumrithi Tony Blair ambalo kwa kiasi kikubwa si la mjadala tena bali linasubiri muda tu,linaangaliwa kwa mtizamo huohuo:Waziri Mkuu Mskotishi ambaye atakuwa na mamlaka katika mambo ambayo baadhi ya watu wanayaona ni ya England pekee.Enewei,ndio mambo ya “miungano” hayo jinsi yalivyo.Kila kwenye Muungano huwa hapakosekani wale wanaoona kama wanaburuzwa au kupunjwa.

Kingine kinachoonekana kuwashtua wachambuzi wa siasa za Ulaya ni kukua kwa kasi kwa nguvu ya wanasiasa na vyama vyenye mrengo mkali kabisa wa kulia.Katika uchaguzi wa bunge la Ulaya,wanasiasa kutoka vyama hivyo wamefanikiwa kufanya vizuri zaidi kuliko hata ilivyotarajiwa.Na kama hiyo hazitoshi,ujio wa nchi za Ulaya ya Mashariki kwenye Jumuiya hiyo ya Ulaya (ambayo kimsingi imejaa nchi za Ulaya Magharibi) unaelekea kuchochea zaidi nguvu za wanasiasa na vyama vyenye mrengo mkali wa kitaifa (far right nationalist parties).Inafahamika kwamba siasa zanye mwekeleo mkali wa kitaifa zimetawala sana miongoni mwa nchi za Ulaya Mashariki, na kuruhusiwa kwa baadhi yao (mfano Bulgaria na Romania zilizojiunga Januari Mosi mwaka huu) kujiunga na Jumuiya hiyo,kunaonekana kuwanufaisha zaidi mafashisti na wengineo wenye mrengo wa kibaguzi.Tayari wanasiasa 20 kutoka vyama hivyo ambao ni wabunge wa Bunge la Ulaya wameunda kikundi kinachojiita “Identity,Tradition and Sovereignity” ambacho kimsingi kinataka kuweka shinikizo dhidi ya sera wanazoona kuwa zinavutia wahamiaji kutoka nje ya nchi zao pamoja na kutilia mkazo sera zao za ubaguzi wa rangi.Miongoni mwa wanasiasa hatari zaidi wanaotishia kurejea kwa siasa za kinazi na kifashisti ni pamoja na Alessandra Mussolini (mjukuu wa fashisti wa Italia Benito Mussolini) na Jean-Marie Le Pen wa Ufaransa.Huyu Le Pen ni mbaguzi sugu mno kiasi kwamba mwaka jana wakati wa fainali za kombe la dunia aliwataka Wafaransa kuisusa timu ya taifa ya nchi hiyo kwa vile eti haiwakilishi utaifa halisi wa nchi hivyo.Kisa,asilimia kubwa ya wachezaji wa timu hiyo waliokuwa weusi na wengi wao wakiwa na asili ya nchi nyingine kabla ya kuhamia Ufaransa.

Mwisho,ni vuguvugu la uchaguzi wa Rais wa Marekani hapo mwakani ambapo kwa sasa wanasiasa mbalimbali wameanza kuitangaza dhamira zao za kugombea kwenye ngazi za vyama kabla hawajapitishwa kuingia ngazi ya kitaifa.Kuna mtu anaitwa Barack Obama,mweusi ambaye ana asili ya Kenya.Kwa kweli Obama ametokea kuwa na mvuto mkubwa sana miongoni mwa watu wanaotajwa kuwania urais mwakani.Tayari Condeleeza Rice,Mwamerika Mweusi wa kwanza kuwa Waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo na swahiba wa karibu kabisa wa Joji Bushi,ameshasema kuwa nchi hiyo iko tayari kuwa rais wa kwanza mweusi.Niliwahi kuandika makala za nyota kwenye magazeti ya Kasheshe na Komesha kwa jina la Ustaadhi Bonge,na hapa nakumbushia enzi zangu:hawa watu hawako tayari kumwona mtu mweusi akiongoza Marekani,ndio maana hivi majuzi baadhi ya wahafidhina walileta hoja eti Obama,profesa wa sheria na seneta pekee mweusi,alishawahi kubwia unga (cocaine) katika ujana wake na wanahoji kama nchi hiyo iko tayari kuongozwa na “teja mstaafu.”

Alamsiki.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.