17 Jan 2011


Katika siku za hivi karibuni,jina la Edward Lowassa limekuwa likisikika sana.Blogu hii inahisi kuwa kelele hizi za Lowassa ni sehemu ya jiihada za kuweka jina lake machoni na masikioni mwa Waanzania ili hatimae amrithi swahiba wake,Jakaya Kikwete, hapo 2015.Hebu msikie tena hapa chini,kisha tumjadili kiduchu


Lowassa: Mjadala wa Katiba usivuruge amani

na Betty Kangonga

MBUNGE wa Monduli, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ametahadharisha mjadala kuhusu Katiba nchini kuwa chanzo cha kuharibu wa amani iliyoko nchini.

Lowassa alitoa tahadhari hiyo jana wakati akifungua studio ya muziki ya FLEM, jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa hivi sasa inaoneka kuwapo kwa mashindano ya kuharibu amani kutokana na mjadala huo kupamba moto.

Alisema kuwa kadri siku zinavyozidi kusonga mbele ndivyo moyo wa kuharibika kwa amani unavyozidi kuongezeka.

Alisisitiza kuwa hata katika mijadala mbalimbali inayoendelea nchini hasa ya Katiba, wananchi wanatakiwa kupingana kwa hoja na si kwa kuhatarisha amani.

“Tunatakiwa kutunza amani yetu kama mboni ya jicho maana hata nchi jirani za wenzetu ikiwamo Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi hawajawahi kuwa na amani kama tuliyonayo sisi, hivyo tunatakiwa kuhakikisha tunaitunza kwa uwezo wetu wote,” alisema Lowassa.

Katika kusisitizia hilo, aliwashauri waimbaji wa Injili kuamka la kutunga nyimbo zinazohamasisha na kuchochea utunzaji wa amani, ili iendelee kudumu.

“Waimbaji wa Injili wanafanya kazi nzuri sana ingawa katika maisha kuna mahali unayumba, unaanguka na kupanda, lakini yote hayo ni kwa uwezo wa Mungu.

“Hakikisheni mnatunga nyimbo za kutetea amani maana kwa sasa kila mtu ana lake analosema, vyombo vya habari vinachochea kwa njia yake, hivyo tuilinde hii amani,” alisema.

Alisema kuwa bila kuwa na amani hakuna taifa linaloweza kufikia maendeleo, hivyo jamii inapaswa kupingana bila kusababisha mvurugano.

Alisema amani ni tunu pekee aliyotuachia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, hivyo tunatakiwa kuitetea kwa nguvu zetu zote.


Alisema kuwa ni kipindi cha ajabu sasa, kwani kila mtu amekuwa akiamka na jambo lake linaloonekana kuhatarisha amani.

Kwa upande wake, mchungaji wa kanisa la FPCT la Mtoni Kijichi, Joseph Malundo, aliwataka wamiliki wa studio hiyo kuacha kubweteka na mafanikio hayo bali wazidi kumuomba Mungi ili azidi kuwapandisha juu zaidi.

Alisema hatua hiyo itawezesha vijana wengi kupata ajira hasa kwa kumtumikia Mungu.

CHANZO: Tanzania Daima

Tatizo la Lowassa,na watu wenye mawazo kama yake,ni kuwaona Watanzania ni wajinga,wasio na kumbukumbu,na ambao wako radhi kufisadiwa milele.Pengine mawazo hayo yanatokana na ukweli kuwa licha ya mtu kama yeye kulazimika kujiuzulu uwaziri mkuu kutokana na kuhusishwa na ujambazi wa Richmond (mtangulizi wa Dowans) bado yupo huru,anapeta na licha ya kufanikiwa kurejea Bungeni,ameendelea kupewa heshima ya "Waziri Mkuu Mstaafu".Na si yeye tu,bali hata washirika wake Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi.

Laiti sheria ingefuata mkondo wake,tusingesikia matusi haya ya Lowassa.Ni dhahiri kuwa anafahamu fika kuwa tishio kubwa la amani ya Tanzania na Watanzania ni UFISADI na MAFISADI.Hawezi kuzungumzia hilo kwa vile linamgusa.Na ni wazi kuwa japo anajifanya kuguswa na umuhimu wa Katiba mpya,ni wazi kuwa yeye,rafiki yake Rostam Aziz,na mlinzi wao hapo Ikulu,Kikwete,wasingependa kuona Katiba mpya itakayompa nguvu Mtanzania kupambana na wezi,majambazi,wadhalimu na wabaka uchumi kama hao walioleta Richmond,na sasa wanataka kujizawadia mabilioni kwa usanii wa "fidia kwa wanaharamu wa Dowans".

Na nyie viongozi wa dini mnaoendekeza njaa zenu mnapaswa kuelewa sio kila sadaka inampendeza Mungu.Kwani Bwana Yesu alifanya kazi zake kwa kutegemea michango,achilia mbali michango ya wanafiki,wezi,majambazi au wapinzani wa Amri za Mungu?Njaa zenu ndio zinawapa watu kama Lowassa nafasi ya kujiosha machoni mwa jamii ilhali tunafahamu fika wasingepaa madaraka kuwa laiti Baba wa Taifa angekuwa hai-kwani alishawaona kuwa ni viumbe hatari kabisa kwa Tanzania yetu.

2 comments:

  1. Chahali uko sahihi kabisa. nami niliposoma habari hii mbona karibu nizimie!!! Sina uhakika kama anasafishika, lakini kama ameshauriwa na swahiba wake kuwa aanze kujisafisha, basi hiyo peke yake inabidi iwe chachu ya kuimarisha kambi ya upinzani. Maana CCm hata wakiweka 'kondoo mweusi' kugombea urais nafasi ya kuchaguliwa ni kubwa. Muumba ibariki Bongo!!!!

    ReplyDelete
  2. Asante kwa kutufumbua macho. Endelea kutujuza.

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.