9 May 2011



Mkutano wa tatu wa Diaspora umemalizika majuzi jijini London huku,kama ilivyokuwa kwa Diapora I na Diaspora II,tumeishia kushuhudia zaidi picha za matukio kuliko maelezo ya mambo muhimu yaliyojiri katika mkutano huo (if there were any).Sina tatizo na watu wanaopenda kupiga picha na viongozi kwani huo ni uhuru wao wa kikatiba.Hata hivyo,nina tatizo kubwa na wale wanaodhani picha na viongozi ni muhimu kuliko kuwabana viongozi hao,hususan wanaposhindwa kutoa maelezo ya kueleweka.

Waziri wa Mambo ya Nje Bernard Membe amekuwa sura iliyozoeleka kwenye mikutano hiyo ya Diaspora.Kwa wadhifa wake,ni mtu mwafaka kuiwakilisha serikali,sambamba na kusikia maoni,ushauri,maswali,nk kutoka kwa Watanzania wanaoshi nje ya nchi.Lakini kwa mwenendo wa ushiriki wake kwenye mikutano hiyo,yayumkinika kusema kuwa Membe amekuwa kama mtalii tu wa kutoa porojo moja baada ya nyingine badala ya kuwaeleza washiriki wa Diaspora Forums mafanikio yaliyokwishapatikana kutokana na uwepo wake au umuhimu wa mikutano hiyo (kama upo).

Usanii wa kwanza wa Membe ni katika kauli yake kuwa moja ya changamoto zinazoikabili serikali anayoitumikia ni kujua idadi ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi.Huu ni usanii wa kitoto kwa vile Watanzania hao hajawaanza kuja nje wiki iliyopita,wala balozi za Tanzania nje-ambazo Membe ameziagiza kubuni mikakati ya kuwezesha kupata idadi ya Watanzania wanaoishi nje-hazijafunguliwa mwezi huu.

Badala ya kupachika jina la CHANGAMOTO,Membe alistahili kueleza bayana kuwa kutofahamika kwa idadi ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi ni moja tu ya UZEMBE ULIOZOELEKA kwenye balozi zetu.Ni uzembe kwa vile umuhimu wa kufahamu idadi hiyo ya wana-diaspora umekuwepo tangu zamani hizo na sio mwaka huu tu au kwenye Diaspora Forums pekee.

Laiti washiriki wa Disapora hiyo wangekuwa serious,wangemkalia kooni Membe kumhoji kwanini zoezi hilo la kufahamu Watanzania waliopo nje ya nchi halijafanyika huko nyuma,na kwanini tuamini kuwa sasa litafanyika?Ikumbukwe Membe amekuwa Waziri wa Nje kwa miaka sita sasa,hivyo kukurupuka wiki iliyopita kukumbuka umuhimu wa kuwa na idadi ya Watanzania nje ya nchi ni sehemu tu ya ubabaishaji wake.

Membe anadai kuwa sababu ya yeye kuja London kuhudhuria mkutano huo ni kukusanya hoja kutoka kwa wadau ili ziweze kusaidia tatizo la Diaspora kupelekwa Bungeni na hatimaye kuingizwa kwenye Katiba.Come on,Membe!That's too cheap politicking even in your own standards.Yaani kukusanya hoja za Watanzania wanaoishi ughaibuni ni lazima kufanywe na waziri ilhali tuna balozi zetu na vyama mbalimbali vya Watanzania?

Na hata tukimpa Membe benefit of a doubt,kwanini asituambie namna alivyokwisha shughulikia hoja alizokusanya kwenye Diaspora I na Diaspora II kabla ya kukurupuka na usanii mwingine kwenye Diaspora III?Kama hoja za nyuma hazijafanyiwa kazi,how come hizo mpya au mwendelezo wa zile za zamani zitashughulikiwa sasa?

Japo Membe anastahili lawama,lakini washiriki wa Diapora Forums nao wanapaswa kulaumiwa kwa kuruhusu cheap lies kutoka kwa same crooked politicians year in year out.Yayumkinika kuamini kuwa udhaifu wa wahudhuriaji wa Diaspora Forums kuuliza maswali magumu yanayostahili majibu ya msingi unachangia sana kumfanya Membe awe "MGENI RASMI WA KUDUMU" kwenye mikutano hiyo kwani anajua he would easily get away with usanii wake.Unadhani angejua kuwa atakaliwa kooni kuhusu ubabaishaji wake,kwa mfano kwenye suala la dual nationality,angetia mguu kwenye Diaspora Forum iliyopita majuzi?

Lakini kilichonikera zaidi katika usanii wa Membe ni kauli yake ya kitoto kuwa eti changamoto nyingine inayoikabili Diaspora ni "WATU WENGI HAWAFAHAMU VIZURI MAANA YA DIASPORA".Utterly rubbish!Hivi Membe anaweza kutueleza amejuaje kuwa watu wengi hawafahamu maana ya Diaspora?Au,je anaweza kutuambia kwanini hawafahamu maana ya neno hilo ambalo lipo kwenye kamusi?Ungetarajia waliohudhuria mkutanio huo wamzomee Membe kwa kauli hiyo isiyo na kichwa wala miguu.Na Membe ana lipi la kutuambia katika madai yake kuwa neno Diaspora halifahamiki kwa wengi,i.e. kutofahamu maana ya neno hilo kunakwamishaje maazimio ya Diaspora Forums zilizopita?

Haya ndio matatizo ya kualika wageni rasmi wanaokuja kutalii badala ya kuzungumza mambo ya msingi.Ni dhahiri kuwa laiti waandaaji wa Diaspora Forums wangetaka mkutano huo uwe na maana wangeandaa mazingira ya kuepuka wababaishaji kama Waziri Membe ambao ni mahiri sana katika kutoa hotuba za kuleta matumaini lakini hotuba hizo zinabaki kuwa hotuba tu,na kusahaulika mara baada ya kumalizika kwa shughuli husika.

Kama kupiga konzi kwenye kidonda kibichi,Membe pasi aibu aligusia suala la uraia pacha (dual nationality).Akaanza kwa kueleza umuhimu wa uraia pacha,na kusema kuwa nchi zilizoruhusu uraia pacha zimewafanya watu wao kupata kazi nzuri zenye mishahara mikubwa na hivyo kuwawezesha kutuma fedha nyingi katika nchi wanazotoka.Huu ndio uelewa wa Waziri wa Mambo ya Nje kuhusu umuhimu wa Diaspora!!!

Labda hakupitia speech notes zake vizuri,labda hakufanya brainstorming ya kutosha kabla ya kutoa hotuba yake kwa wana-Diaspora,lakini ni wazi Membe anafahamu fika kuwa umuhimu zaidi wa uraia pacha ni suala la haki za binadamu kuliko mishahara mikubwa au kazi nzuri.Nani aliyemwambia Membe kuwa wana-Diaspora wana kazi za ovyo ovyo zisizolipa mishahara mizuri kwa vile tu hawana uraia pacha?

Kwa hoja hizi mfu,ni wazi kuwa Membe si mwakilishi mzuri wa wana-Diaspora katika kilio chao cha muda mrefu cha uraia pacha.Membe amegeuza Diaspora Forums kuwa sehemu ya kuwapa matumaini kuhusu suala hili ilhali hafanyi jitihada zozote kuhakikisha suala hilo linahama kutoka kuwa ahadi hewa na kuwa sheria kamili inayotekelezeka.

Kuhusu changamoto ya kuwawezesha Watanzania walio nje ya nchi kuchangia maendeleo ya Tanzania,Membe anapswa kufahamu kuwa kila Mtanzania aliye nje ya nchi ana connection na Tanzania.Wengine tuna wazazi,kaka,dada,wadogo,nk huko nyumbani na licha ya nchi yetu kujifanya haitambua umuhimu wa Watanzania walio nje,wameendelea kupunguza makala ya ufisadi kwa ndugu na jamaa zao huko nyumbani kwa kuwatumia fedha za matumizi na misaada mingineyo.

Katika mkutano huo,mmoja wa wajumbe alipendekeza uanzishaji wa kumbukumbu mkeka ya ujuzi na fani wazizonazo Watanzania waishio nje.Wazo zuri lakini nadhani mtoa hoja amesahau umuhimu wa data protection,na namna taarifa hizo binafsi za Watanzania walio nje zinavyoweza kuishia mtaa wa Mkwepu kwa wanaotengeneza vitambulisho feki.I would never trust fisadi awe na taarifa zangu binafsi ilhali nafahamu fika kuwa zitaozea tu kwenye mafaili kama sio kufungiuwa vitumbua na maandazi.

Kama taafira zilizokusanywa kufahamu chanzo cha milipuko ya mabomu huko Mbagala na Gongo la Mboto zimepuuzwa,mtoa hoja anataraji mijuiza gani  kwa taarifa za Watanzania walio nje kutumiwa ipasavyo?Nadhani kuna baadhi ya Watanzania wenzetu walio nje hawajishughulishi kufahamu uharamia,ufisadi,ubabaishaji,uzembe na utapeli wa kisiasa unaendelea huko nyumbani kiasi kwamba wanaweza kupoteza muda wao kuwasikiliza akina Membe "wakiuza sura" kwenye Diaspora Forums.

Unajua kwanini nasema Membe anafanya usanii kwenye suala la uraia pacha?Ameshatoa kauli kadhaa za kibabaishaji kuhusu suala hilo,moja ikiwa aliyoitoa Januari mwaka huu kwenye mkutano wa IOM ambapo alidai kuwa utafiti uliofanyika umehitimisha umuhimu wa uraia pacha,Wizara yake imeanzisha kitengo cha kushughulikia suala la Diaspora,na sheria ipo mbioni kuanzishwa.

Lakini kwenye mkutano wa Diaspora uliomalizika wiki iliyopita,Membe wala hakugusia ni lini sheria hiyo itaanza kufanya kazi.Katika mkutano huohuo wa IOM,Membe aliwazuga wajumbe kwa kuahidi kuwa sheria ya uraia pacha ingekuwa tayari kufikia mwisho wa mwaka jana.Amekuja London miezi mitano baadaye na kuendelea ngonjera hizo hizo.

Hebu sikiliza porojo za Membe kwenye Diaspora Forum II iliyofanyika mwaka jana



Na hapa pamoja na kuongelea mambo mengine,mwishoni mwa clip ifuatayo anajibu swali na Freddy  Macha kwa kuahidi tena "MWISHO WA MWAKA HUU" kama alivyoahidi mwaka jana kuwa "MWISHO WA MWAKA HUO 2010".



Enewei,kulikuwa Diaspora Forum I,ikamalizika na picha tukaona.Ikaja Diaspora Forum II,ikamalizika na picha tukaonyeshwa.Na majuzi imemekuja Diaspora Forum III,imemalizika wiki iliyopita na picha tumeziona.Tusubiri Diaspora Forum IV...bila shaka tutaendelea kushuhudia picha nyingine na usanii mwingine unaohanikizwa na maneno kama "mchakato","changamoto","vipaumbele" na usanii mwingine kama huo.Blogu hii inatoa wito kwa wana-Diaspora kujaribu kuwaonyesha Watanzania wenzatu walio nyumbani kuwa licha ya kutopendezwa na ubabaishaji wa baadhi ya viongozi wetu huko nyumbani,hatuwezi kutoa fursa kwa ubabaishaji huo kuwa exported hadi huku ughaibuni.Ili Diaspora Forums ziwe na manufaa,they need to go beyond being just another photo-ops.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.