2 Sept 2011


Na Nova Kambota,
Namkumbuka mwanamuziki wa kizazi kipya Seleman Msindi maarufu kama Afande sele na kile kibao chake cha “Darubini kali” anapohoji “kama unapenda pepo kwanini uogope kifo?”
Tungo hii kwa namna ya pekee inamgusa waziri mkuu wa Tanzania Mh Mizengo Pinda maarufu kama “mtoto wa mkulima” ndiyo namuuliza Pinda ataonaje pepo pasipo kufa kwanza?
Tangu kuteuliwa kwake mara baada ya Edward Lowassa kujiuzulu, Kwa wale wanaomjua Pinda walishasema kuwa “Pinda atapwaya sana”, sasa ikiwa ni takribani miaka mitatu na nusu tayari mambo hadharani kuwa Pinda “kashindwa kazi”
Kwa wasiomjua Mizengo Pinda tafuteni ukweli mtamjua tu, ni Mizengo Pinda huyu amebaki kuwa mshauri wa Kikwete badala ya waziri mkuu kufikia hatua ya kutamka bungeni kuwa hana mamlaka, ni Pinda huyu asiye na makundi lakini anakubali kumezwa na mitandao na makundi ya CCM na bosi wake Kikwete na sasa nimeanza kusikia watu wakimwita ni “mtoto wa mkulima anayeishi kibilionea”
Hakuna ubishi kuwa hata watetezi wachache wa Pinda waliobaki sasa wamefadhaishwa na udhaifu wake kama sio uwoga wa kupindukia, “jeuri” ya Luhanjo na sakata la Jairo limemwaka njia panda Mizengo Pinda, amebaki kujiumauma na kutapatapa tu, kadhalilishwa lakini hataki kuchukua hatua, katukanwa lakini anachekelea! Huyu ndiye Mizengo Pinda.
Waziri mkuu Pinda akiongelea sakata la Jairo akajiapiza kuwa angekuwa na mamlaka angemfukuza kazi Jairo kwa maana nyingine Pinda amekiri kuwa Jairo anastahili adhabu na serikali haikutaka kumwangusha waziri mkuu “ikamtwanga likizo ya malipo” Bw Jairo lakini ghafla katibu mkuu kiongozi anaibuka na kumdhalilisha waziri mkuu eti Jairo hana kosa arudi kazini, wakati Pinda akisita kuchukua hatua wabunge kwa umoja wao wameamua kumtetea waziri mkuu kwa kudhalilishwa sasa Bunge limeunda kamati.
Hivi katika mduara huu wa “kudhalilishana na kushushiana heshima” ipi nafasi ya Pinda? Yapi maamuzi ya Pinda? Kichekesho ni kuwa Pinda “yupoyupo tu” hajachukua uamuzi na dalili zinaonyesha kuwa kwa mara nyingine tena Pinda amekubali kupiga magoti na kujishusha sehemu aliyotakiwa apigiwe  magoti yeye huyu ndiye Pinda ambaye bilashaka hata “ukimpiga ngumi” yeye wakati wa kukurudishia lazima atavaa gloves ili asikuumize.
Pinda anataka pepo? Anataka watanzania tumkumbuke kuwa ni kiongozi jasiri? Basi hana budi kufa ili aione hiyo pepo! Naam amedhalilishwa sana, ameshushiwa hadhi yake, na sasa ni wakati wayeye kufikiria kujiuzulu.
Haiwezekani Luhanjo na Pinda waendelee kuitumikia serikali moja, hiki kitakuwa ni kiinimacho , ni lazima mmoja wao atoke, na kwa vile wote tunakubaliana Pinda anaitamani pepo, anataka kukumbukwa mioyoni mwa watanzania, lazima aachane na serikali hii ya akina Luhanjo na Jairo, hana budi kumwachia Kikwete ateue waziri mkuu mwingine ambaye atakubali kuvunjiwa heshima, Naam! Pepo haiji hivihivi, ni lazima Pinda afe leo ili aione pepo kesho!

Nova Kambota Mwanaharakati,
+255717 709618
Tanzania, East Africa,
Alhamisi, September 1, 2011.


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.