29 Jul 2014

An armed pro-Russia militant stands guard at the MH17 crash site.
Katika jitihada za kubaini chanzo-nani na kitu gani-cha kudunguliwa ndege ya Shirika la Ndege la Malaysia MH17,kundi la waandishi wa habari wa kijamii (citizen journalism) wakitumia mtandao wa intanet na hisia zao tu wamekuwa wakikusanya habari pengine zaidi ya mashushushu wa Kimarekani.

Jumanne iliyopita, maafisa usalama wa Marekani walikiri kwamba japo ni kweli kwamba Russia imekuwa ikiwasaidia waasi wanaoiunga mkono, huko Ukraine, kwa miezi kadhaa, hakuna uthibitisho wowote kuonyesha kuwa kifaru cha kurusha makombora ya kutoka ardhini kwenda angani (surface -to-air missile) aina ya Buk SA-11, ambacho Marekani inadai ndio kilitungua ndege hiyo, kilikuwa cha Russia. Hata hivyo, waasi hao wa Ukraine walijigamba awali kuwa wana makombora ya aina hiyo.

Msemaji wa serikali ya Marekani alikiri kwamba kuna uhaba mkubwa wa maelezo kuhusu silaha iliyotumika kudungua ndege hiyo, na kuthibitisha kuwa ni vigumu kuja na ushahidi mpya wa kuthibitisha uhusika wa Russia katika tukio hilo.

Lakini kundi la waandishi wa habari wa kijamii likiongozwa na Ellliot Higgins, anayefahamika zaidi kwa jina lake la mtandaoni kama "Brown Moses," ameonyesha ushahidi mwingi kuhusiana na tukio hilo. Kwa msaada wa wafuasi wake (followers) katika mtandao wa kijamii wa Twitter, ameweza kuonyesha sehemu kilipokuwa kifaru cha kurusha makombora (launcher) ya Buk wakati kinasafirishwa katika eneo la Snizhne, lililopo chini ya milki ya waasi wanaoungwa mkono na Russia, kulingana na video inayosambaa kwenye mtandao wa video wa Yout Tube

Siku iliyofuata, Aric Toler, mfuasi wa muda mrefu wa Higgins, alionyesha eneo sahihi la kifaru cha kurushia makombora ya Buk katika mji uliopo Mashariki kwa Ukraine wa Torez, akitumia taarifa alizozikusanya kwa vyanzo vya wazi (open source information) na video nyingine za YouTube zilizorekodiwa eneo hilo.

Toler na Higgins waliweza kuthibitisha kuwa picha hiyo ilipigwa saa 5.40 asubuhi, kwa kutumia nyenzo ya mtandaoni iitwayo Suncalc, ambayo inawezesha kukokotoa nafasi (position) ya jua kwa kuzingatia muda na sehemu husika. Hiyo iliwawezesha kuthibitisha kuwa kifaru hicho kilikuwa eneo ilipodunguliwa ndege ya MH17.

Uchambuzi mwingine wa kutumia watu wengi (crowdsourced analysis) ambao Higgins aliukusanya Jumanne iliyopita unatoa ushahidi mkubwa kuhusu video iliyotolewa hadharani na serikali ya Ukraine ikionyesha kifaru husika kikihamishwa kutoka eneo linaloshikiliwa na waasi kuelekea Russia. Katika video husika, mtambo wa kurushia makombora (launcher) hauonekani 

Serikali ya Russia ilikanusha usahihi wa video hiyo, ikidai kwamba ilirekodiwa katika mji wa Krasnoarmeisk, ambao upo chini ya himaya ya majeshi ya Ukraine. Hata hivyo, shukrani kwa uchambuzi wa habari kwa kutumia vyanzo vya wazi, ilikuja kufahamika kuwa mji huo wala sio uliotajwa bali mwingine ulio chini ya himaya  ya waasi wanaoungwa mkono na Ruassia wa Luhansk, kilomita 30 kutoka mpaka wa Russia na Ukraine.

"Russia imeongopa," aliandika Higgins katika tovuti yake ya Bellingcat, anayoitumia kuhamasisha kazi za waandishi wengine wa wa kijamii wanaoandika habari za uchunguzi na kufundiha kuhusu nyenzo mbalimbali kwa ajili ya kazi hiyo. 

Matokeo ya uchunguzi huo hayathibitishi kwa hakika uhusika wa Russia katika kuidungua ndege hiyo ya Malaysia, kama anavyokiri Higgins mwenyewe, lakini yanathibitisha kuwa waasi wanaoungwa mkono na Russia wanamiliki kifaru cha kurushia makombora ya Buk,.na kilikuwa karibu na eneo ilipodunguliwa ndege hiyo.

Kwa Higgins, kazi yao ni sawa na ushushushu lakini kwa kutumia njia rahisi,na unaweza kuwasaidia wachunguzi wa ajali hiyo. Baada ya yeye na mwenzie Toler kuonyesha eneo na muda picha ya kifaru hicho lipopigwa, waandishi wa habari walikwenda huko na kukutana na mashuhuda waliothibitisha maelezo ya Higgins na mwenzake.

Uchunguzi wa aina hii ni mfano mzuri wa anachotaka kufanya Higgins kupitia tovuti yake ya Bellingcat: kujenga jamii ya waandishi wa kijamii mtandaoni wanaojuhusisha na uchunguzi ambao waweza kuibua ukweli mbalimbali. Higgins amekuwa akifanya hivyo kwa miaka kadhaa, akibandika mtandaoni video mbalimbali kutoka Syria ili kbainisha zipi ni za kweli au la.

Yeye alikuwa mmoja wa waangalizi huru wa mwanzo kuthibitisha kuwa utawala wa Rais Bashir al-Assad wa Syria ulitumia silaha za sumu katika kitongoji cha Ghouta Agosti mwaka jana,a aliibua biashara ya kuingiza silaha nchini humo, akiwa nyumbani kwake, Leicester, Uingereza.  Sasa anataka kuwaunga mkono watu wengine wanaofanya kazi kama yake na kuwafundisha jinsi ya kupata ujuzi husika.

"Ni muhimu kufahamu kuwa uchunguzi huu ulifanywa na na watu wa aina mbalimbali, na hiyo inaonyesha umuhimu wa kufanya nyenzo na mbinu za kukusanya habari kwa vyanzo vya wazi kuwa za wazi kwa yeyeote yule."

Chanzo: Imetafsiriwa kutoka mtandao wa WAtoday.com.au



0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.