4 Jul 2015

Kwa niaba ya familia ya Mzee Philemon Chahali, ninaomba kuwashukuru nyote mnaoungana nasi kumwombea dua/sala ili apone. Hatuna cha kuwalipa bali kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu awabariki kwa upendo wenu. Pia kwa vile hali ya baba bado si ya kuridhisha, tunawaomba tuendelee na dua/sala zaidi. Wanasema 'penye wengi Mungu yupo' basi ni matumaini yetu kuwa ushirikiano huu katika sala/dua utapelekea kupona kwa Mzee Chahali. Again, asanteni sana, na Mungu awabariki sana.

Tangu nipate taarifa za kuumwa kwa baba, nimepunguza kujishughulisha na 'kelele' zangu kuhusu masuala mbalimbali yanayoikabili Tanzania yetu. Sijafanya hivyo kwa maana ya kupuuzia masuala hayo bali kichwa changu kimetawaliwa na suala la afya ya baba yangu kwani ndo mzazi pekee niliyebakiwa naye baada ya kufiwa na mama mwaka 2008.

Hata hivyo, leo nimelazimika kuandika makala hii baada ya kufanya maongezi na jamaa yangu mmoja huko Tanzania ambaye katika nafasi yake kikazi, anafahamu mambo mengi yanayojiri 'nyuma ya pazia.'

Alichoniambia kimenishtua sana. Ni kuhusu kampeni zinazoendelea mtandaoni zinazomhusisha mtoto mdogo anayejiita DOGO JEMBE. Pia kampeni hizo zinatumia hashtag #IkuluSio.

Huyo jamaa yangu, pengine kutokana na majukumu yake kikazi au ufuatiliaji tu, amenionyesha ushahidi unaothibitisha kuwa kampeni hiyo inaendeshwa na mtangaza nia mmoja wa CCM. Kwahiyo tofauti na picha inayojengwa na DOGO JEMBE kuwa yupo upande wa maslahi ya Watanzania, kimsingi mtoto huyo anatumiwa tu na mwanasiasa huyo anayetaka urais. 

Kwa mujibu wa jamaa yangu huyo anayefanya kazi katika taasisi moja 'nyeti' huko nyumbani, kosa la msingi lililofanywa na waandaaji wa kampeni hiyo ni kwenye kitu kinachofahamika kama IP Address ambayo kwa lugha nyepesi ni anwani ya mlolongo wa namba zinazotenganishwa na nukta ambao unaitambua kompyuta katika mtandao. 'Mtaalam' huyo amefanikiwa kubaini kuwa posts za kampeni hiyo zinatoka kwa IP address ya mdogo wa mwania nia fulani. Amenitumia screenshots zenye uthibitisho kuhusu suala hilo.

Amenijulisha pia kuwa taasisi anayoitumikia inafahamu bayana kuhusu 'uhuni' huo, na hii unaisoma hapa kwa mara ya kwanza, usishangae ukikutana na breaking news hii katika vyombo vya habari katika siku chache zijazo. Inaelekea kuna 'wakubwa' hawajapendezwa na mbinu hiyo ya kuwahadaa Watanzania kwa kisingizio cha kumsaka Rais bora.

Kilichomkera, kinachonikera, na ambacho pengine nawe Mtanzania kitakukera ni kitendo cha mwania huyo kuwafanya Watanzania wapumbavu. Kwanini nasema hivyo? Kwanza ni 'kosa' la kumtumia mtoto mdogo kuvuta hisia za watu, kuwaaminisha kuwa lengo ni kupigania maslahi ya taifa kwa kuamsha tafakuri ya nani hasa anatufaa kuwa Rais wetu ajaye, ilhali ukweli ni kwamba kampeni hiyo ina lengo la kumpigia debe mwania nia huyo.

Kumtumia mtoto huyo mdogo kwa minajili ya kisiasa hakuna tofauti na kile kinachoitwa CHILD LABOUR, yaani kuwatumikisha watoto. Sasa hapo tu yatupasa kutambua kuwa child labour ni ukiukwaji wa haki za binadamu, na kwa minajili hiyo, mwania nia anayesaka urais kwa kukumbatia ukiukwaji wa haki za watoto/binadamu HAFAI.

Pili, hadaa, usanii, na uhuni mwingine wa kisiasa ndivyo miongoni mwa vitu vilivyotufikisha hapa. Sasa kama katika hatua hizi za awali tu za kuwania kupitishwa na chama kuwania urais mwanasiasa anaanza kukumbatia vitu kama hivyo, huhitaji kuwa mwenye uelewa mkubwa wa kisiasa kubaini kuwa mwania nia huyo hafai hata ujumbe wa nyumba kumi, achilia mbali urais.

Tatu, japo watoto wana haki ya kikatiba na kidemokrasia kuzungumzia kuhusu hatma ya taifa letu ikiwa ni pamoja na Uchaguzi Mkuu ujao, hiyo sio excuse kwa wamasiasa yeyote yule kutumia haki hiyo ya watoto kwa manufaa yake binafsi. Angekuwa jasiri, angejitokeza mwenyewe hadharani badala ya kujikampenia kwa kutumia child labour.

Kwa mujibu wa jamaa yangu huyo ambaye kwa ninavyomfahamu hana kambi yoyote hasa kwa vile majukumu yake kikazi yanamzuwia kujihusisha na siasa, kuna data nyingine ambazo zinaihusisha moja kwa moja kampeni hiyo na mwania nia huyo.

Japo nipo katika wakati mgumu kutokana na kuzorota kwa afya ya Mzee Chahali lakini afya ya Tanzania yetu ni muhimu pia kama afya ya mzazi wangu, na nimeshindwa kukaa kimya baada ya kuletewa ushahidi kuhusu 'uhuni' huu. 

Amenieleza kuwa kauli ya Dogo Jembe kuwa 'Ikulu sio ya baba yako' ilimlenga Makongoro Nyerere kwa vile yeye ni mtoto wa Nyerere, na kauli kuwa 'Ikulu sio hospitali' illimlenga Lowassa kwa vile mwania nia huyo amedaiwa kuwa afya yake sio nzuri japo haijathibitishwa. 


Lakini pengine hata bila kupata 'ufunuo' huu, ilipaswa tujiulize NANI ANAYEFADHILI KAMPENI HII YA KISASA KABISA?

Kwa mtizamo wa jamaa yangu huyo, kosa jingine la kampeni hiyo ni kwamba imejitengenezea 'ufupi wa maisha' kwa maana kwamba ipo siku Dogo Jembe atalazimika kuwashawishi tena Watanzania kuwa 'mtaka nia flani ana sifa za dogo jembe, na ndio anafaa kuwa Rais,' na hapo all hell will break loose kwa sababu kila mwenye akili timamu atabaini nani alikuwa behind kampeni hiyo.

Anyway, ningetamani kuandika kwa kirefu lakini wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni mdogo tu: AKILI ZA KUAMBIWA, CHANGANYA NA ZA KWAKO. Tumeshwahi kuhadaiwa huko nyuma, tumeshaona matokeo ya hadaa hizo, chonde chonde, tusirejee tena makosa hayo. Kama katika kuwania tu kupitishwa na CCM, mwanasiasa yupo radhi kutumia mtoto mdogo kuwahadaa Watanzania, je akifanikiwa kuingia Ikulu itakuwaje? Ni muhimu pia kutambua kuwa mwanasiasa ambaye yupo desperate mno kuingia Ikulu lazima atakuwa na ajenda zake binafsi,

Nimalizie kwa kuwashukuru tena nyote mnaojumuika nasi kumfanyia dua/sala Mzee Chahali, na ninawashukuru sana, na kuwaombea Mungu awabariki sana. 



0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.