11 Mar 2020


Kusema hukumu nzito dhidi ya viongozi kadhaa wa Chadema iliyotolewa jana kuwa ni ishara mbaya kwa demokrasia nchini Tanzania ni kutoitendea haki hali ya demokrasia katika nchi yetu. Kilichotokea jana hakipaswi kuangaliwa kama tukio pekee bali mwendelezo wa matukio lukuki yaliyojiri tangu Rais Magufuli aingie madarakani takriban miaka mitano iliyopita.


Sidhani kama kuna haja ya kueleza kwanini hukumu hiyo ni ya uonevu uliopindukia kwani takriban kila mtu aliyekuwa anafuatilia mwenendo wa kesi hiyo anaelewa kuhusu hilo. Lakini pia, takriban kila anayefuatilia mwenendo wa Magufuli na demokrasia Tanzania anaelewa hali ikoje kwa sasa.



Kwahiyo, badala ya kutumia muda mwingi kulalamika ni vema kujaribu kutafuta suluhisho japo la muda mfupi kuhusu hali hiyo. Kwa bahati mbaya, uzoefu wangu binafsi kuhusu kuwashauri ndugu zangu wa Chadema haujawahi kuwa mzuri. Kila inapotokea aidha kuwashauri au kuwakosoa, huwa wakali kama pilipili huku wengine wakitumia lugha isiyofaa.



Yayumkinika kuhitimisha kuwa tofauti pekee kati ya Chadema na CCM when it comes to kuwakosoa, ni kwamba CCM ipo madarakani na Chadema wapo upinzani, lakini tabia zao wanapokosolewa ni sawa: hawataki kusikia ushauri wowote tofauti na mtazamo wao hata kama ni fyongo.



Ni muhimu kutambua kuwa unyanyaswaji unaofanywa na Magufuli kwa Chadema hakuanza jana. Tangu kiongozi huyo aingie madarakani hajawahi kuficha chuki yake dhidi ya Chadema. Na anayedhani kuwa kuna siku hali itabadilika, kwamba ghafla chuki hiyo itageuka upendo, basi kichwani hayupo vema.



Ndio maana baadhi yetu tulimshutumu vikali mwenyekiti wa taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, alipomwomba Magufuli kuwe na MARIDHIANO. Lakini kama ilivyo kawaida ya wafuasi wa chama hicho, sio tu walimtetea Mbowe bali pia waliturukia kama mwewe sie tulioona mkakati huo ni fyongo.



It is this simple, huwezi kutaka maridhiano na mtesi wako. It simply doesn't work. Unawezaje kutaka maridhiano na mtu ambaye utawala wake umetawaliwa na matukio mabaya kabisa kuhusiana na wanasiasa na wanachama kadhaa wa Chadema?



Unasakaje maridhiano na Magufuli ilhali siku chache tu baada ya kuingia madarakani Kamanda Mawazo aliuawa kinyama?

Unatakaje maridhiano na Magufuli ambaye muda mfupi tu baada ya kuingia madarakani aliharamisha shughuli halali kikatiba za vyama vya upinzani ikiwa ni pamoja na Chadema?


Unatakaje maridhiano na Magufuli ambaye alimfunga mbunge Joseph Mbilinyi aka Sugu kwa "kosa feki"?

Image result for sugu afungwa

Unatakaje maridhiano na Magufuli ambaye utawala wake unapaswa kuwaeleza Watanzania alipo kada maarufu na mkosoaji mkubwa wa Magufuli, Ben Saanane?

Image result for bring back ben saanane
Unatakaje maridhiano na Magufuli ambaye utawala wake una damu za Diwani Luena na Katibu Kata Daniel?




Orodha ni ndefu lakini so far response ya Chadema imekuwa ya kusuasua




Na kibaya zaidi, baadhi ya tuonaguswa na madhila yanayowasibu tukijitolea kuwashauri twaishia kutukanwa.



Ni hivi, ili Magufuli alazimike kubadilika, ni lazima kuwa na "incentive" ya kumfanya abadilike. Naamini mmeona jinsi "shinikizo la mabeberu" lilivyomlazimisha amwachie huru mwandishi Eric Kabendera, aitishe mkutano wa kizushi na Maalim Seif, Mbatia na Lipumba, na amemtuma "Profesa aliyeokotwa jalalani" Kabudi aende kuomba suluhu huko Marekani. 



Pia sote ni mashuhuda wa jitihada binafsi za kiongozi mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo kuishinikiza benki ya dunia isitoe mkopo kwa Tanzania zilivyozaa matunda. Chadema kama chama kikuu cha upinzani ilishindwa kuwa mstari wa mbele katika hili.



Na hadi wakati huu hakujawa na mwamko wa kitaifa kwa chama hicho kushinikiza mabadiliko katika mwenendo wa siasa za Tanzania. Na kichekesho ni kwamba ajenda kuu ya chama hicho kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ilikuwa MABADILIKO. Je ajenda hiyo ilikufa baada ya Lowassa kushindwa uchaguzi huo na hatimaye kukikimbia chama hicho?



Pengine hadi kufikia hapa, msomaji ambaye ni kada wa Chadema utakuwa umefura kwa hasira ukilaumu kuwa sionyeshi huruma kwa yanayokisibu chama hicho na viongozi wake. Nawaonea huruma sana lakini ni nadra kwa hisia pekee kuleta mabadiliko. Huruma kwa akina Mbowe na wanasiasa wengine wanaoteswa na Magufuli haiwezi kumfanya dikteta huyo abadilike.



Ieleweke kuwa chuki ya Magufuli kwa Chadema inatokana na ukweli kwamba chama hicho ndicho cha pili kwa ukubwa baada ya CCM na kina mtandao mpana wa nchi nzima, na licha ya kuwa chama kikuu cha upinzani, pia ni potential mbadala wa CCM. Kwahiyo, kwa Magufuli ambaye anajua fika kuwa akirogwa tu kutoka madarakani ataishia jela, ni lazima kwake kuibana Chadema kwa nguvu zake zote. Huyu si mtu wa kutaka maridhiano nae hata chembe.



Kwa vile lawama pekee hazijengi, nihitimishe makala hii kwa kuikumbusha tena Chadema kuwa dhamira kuu ya Magufuli ni kuhakikisha chama hicho kinakufa. Najua kuna wanaosema "hawezi kukiua chama hiki" lakini ukweli ni kwamba kifo cha chama cha siasa sio lazima kiwe kama kifo cha binadamu. Endapo dhamira ya Magufuli kuwa katika uchaguzi mkuu ujao Chadema isiambulie jimbo na kata hata moja itatimia, huo ni mwanzo wa kifo cha chama hicho. 



Simaanishi kuwa kitakufa kwa maana ya kutokuwa na mwanachama hata mmoja bali kitabaki "chama kama chama" kama ilivyo CUF ya Lipumba au TLP ya Mrema au NCCR ya Mbatia. Uwepo au kutokuwepo kwa vyama hivyo hakuna maana kwa Watanzania.



Lakini ukiwakumbusha Chadema kwa mifano hai kuwa Magufuli amedhamiria kwa dhati kukiangamiza chama chao, sana sana utaishia kuambulia matusi. 



Nini kifanyike? Kwa bahati mbaya imebaki mezi saba tu kabla ya uchaguzi mkuu ujao hapo Oktoba. Kwa maana hiyo, hakuna muda wa kutosha kwa chama hicho kuanzisha programu kabambe ya kupambana na udikteta wa Magufuli.



However, uchaguzi huo unaweza kutoa fursa ya "kuua ndege wawili kwa jiwe moja," - kutekeleza programu kabambe ya kukomesha udikteta wa Magufuli kama mkakati kabambe wa chama hicho kuingia Ikulu. Kwamba, kama ajenda fyongo ya MABADILIKO (ya Lowassa) ya mwaka 2015, safari hii ajenda iwe kukomesha udikteta wa Magufuli na hatimaye kumng'oa hapo Oktoba.



Lakini ili hilo liwezekane ni muhimu kwa chama hicho kuachana kabisa na mtazamo fyongo miongoni mwa viongozi wengi wa ngazi za juu wa chama hicho na makada mbalimbali kuwa "adui yao mwingine zaidi ya  Magufuli na CCM ni Zitto na ACT-Wazalendo." Kuna wahuni kwenye chama hicho kama "jasusi Yeriko" ambao wamekuwa wakijibidiisha kujenga chuki dhidi ya Zitto na ACT-Wazalendo kwa ujumla pasipo viongozi wa Chadema kukemea upuuzi huo. 



Japo muda ni mchache kabla ya uchaguzi mkuu ujao, lakini ushirikiano wa dhati kati ya Chadema na ACT-Wazalendo - na pengine makundi mengine ya kijamii (rejea wazo la Zitto kuhusu "united front") - pamoja na shinikizo kwa mabeberu ambao fedha zao ndio zinampa jeuri Magufuli, unaweza kabisa kumwondoa madarakani huyo dikteta kwa njia za amani. Uzuri ni kwamba mabeberu wanafuatilia kwa karibu kila kinachojiri Tanzania


Mwisho, japo ninawapa pole viongozi wa Chadema kwa madhila wanayopitia, wanachohitaji zaidi sio huruma yetu bali ujasiri wa kupambana na huyo dikteta kwa kila njia inayowezekana. Na japo sidhauri matumizi ya nguvu katika kudai haki, busara hii ya marehemu Profesa Kighoma Ali Malima bado ina relevance kubwa kwa wanasiasa wa upinzani ikiwa ni pamoja na Chadema.


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.