Showing posts with label ELLIOT MORLEY. Show all posts
Showing posts with label ELLIOT MORLEY. Show all posts

12 Mar 2010

 Habari zilizotawala vyombo vya habari vya hapa Uingereza ni kufikishwa mahakamani kwa wabunge watatu wa chama tawala (Labour) na mbunge wa bunge la mabwanyenye kutoka chama cha Conservatives.Kwa pamoja wabunge hao wanatuhumiwa kufuja fedha .Wabunge hao, Elliot Morley, David Chaytor na Jim Devine wa Labour na Lord Hanningfield wa Conservatives wanashtakiwa kwa ubadhirifu wa jumla ya takriban pauni 60,000 za mafao ya wabunge.Wakati hayo yakitokea hapa katika nchi ambayo ni wafadhili wetu wakubwa,hadi muda huu sie tumeendelea kuwekwa kizani kuhusu mdudu aitwaye Kagoda,huku mtuhumiwa wa ufisadi wa rada na wale wa ujambazi wa Richmond wakiendelea "kupeta". Ni dhahiri kwamba watawala wetu hawako serious na mapambano dhidi ya uhalifu wa vigogo.Hebu angalia mfano mwepesi wa ishu ya mtangazaji wa TBC,Jerry Muro.Japo blogu hii si mahakama ya kuamua kama mtangazaji huyo hana hatia au,kasi ya vyombo vya dola katika kushughulikia 'tuhuma' dhidi yake zilikuwa kubwa sana tofauti na namna vyombo vya dola vinavyojiumauma hadi leo kuhusu majambazi wa kampuni ya Kagoda waliokwiba shilingi bilioni 40 katika utapeli wa EPA.Watawala wetu wameendelea kuweka pamba masikioni na kupuuza kilio cha umma kuhusu haja ya angalau kutajiwa wamiliki wa kampuni hiyo ya kijambazi.

Ndio maana blogu hii imeendelea kuiona sheria mpya ya kudhibiti rushwa katika chaguzi kuwa ni mwendelezo wa ahadi lukuki za kunoresha ustawi wa taifa letu lakini ahadi hizo zimeendelea kuwa viinimacho visivyotekelezeka.Sheria hii inaweza kupelekea waheshimiwa wawili watatu kutiwa nguvuni (kama TAKUKURU watashikiwa silaha kuwezesha hilo), vichwa vya habari vitasomeka kwa herufi kubwa kwamba sheria imeanza kufanya kazi.Lakini kana kwamba wana ugonjwa wa kusahau historia,baadhi ya wanahabari wetu watazembea kurejea matukio ya nyuma ambapo kesi kama za akini Profesa Mahalu,na hizi za karibuni za Mramba na Yona zinaendelea kusuasua mahakamani pasipo dalili za haki kutendeka-kwa watuhumiwa na walipakodi wa Tanzania.

Watakaonaswa baada ya sheria hiyo 'kuanza kutumika' watakuwa mithili ya 'muzi wa kafara',na 'changa la macho' kuonyesha umma kuwa sheria inafanya kazi lakini mwisho wa siku itaishia kuwa 'flani kafikishwa mahakamani',and that's it.Suala sio kumfikisha mtuhumiwa mahakamani bali haki itendeke,na sio itendeke tu bali ionekane imetendeka.

Yayumkinika kusema kuwa kesi za EPA zinazoendelea kwa mwendo wa kinyonga hazikidhi haja ya umma hasa kwa vile japo wote ni watuhumiwa lakini wale wa Kagoda waliiba fedha nyingi zaidi.Cha kushangaza ni kwamba hadi leo wameendelea kuhifadhiwa.Sasa tukisema ufisadi ni sera ya CCM tutaambiwa tumekosa nidhamu?

Tukio la kufikishwa mahakamani kwa wabunge hawa wa Uingereza kunapaswa kutufumbua macho kwa vile kama nchi inayotufadhili iko hailei wabadhirifu iweje sie tunaotegemea misaada tunakuwa na 'sintofahamu' katika kuwachukulia hatua mafisadi?Hivi kuna sababu za msingi kwanini hadi leo Mzee wa Vijisenti Andrew Chenge hajafikishwa mahakamani kuhusu vijibilioni vyake huko visiwani Jersey?Basi hata kama wanamwonea aibu,yaani CCM wanashindwa hata kuona haya kwa mtuhumiwa huyo kuwa mwenyekiti wa kamati yake ya maadili?Au ufisadi ni sehemu ya maadili katika chama hicho?

Wakati tukiendelea kuaminishwa kuwa sheria hiyo ya kudhibiti rushwa kwenye chaguzi itakuwa 'kiboko' ya rushwa,toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema lina habari kuwa rushwa inamwagwa katika majimbo kadhaa kama wahusika hawana akili nzuri.Sijui huko ni kumkejeli Rais Kikwete aliyetamka bayana kuwa atasaini sheria hiyo kwa mbwembwe au ni kuujulisha umma kuwa CCM na rushwa ni damu damu!Kilicho wazi ni kuwa hakuna mgombea wa CCM atakayefanikiwa kupitishwa na chama hicho pasipo kutoa rushwa.Hilo halihitaji mjadala.Na kama Rais Kikwete anaamini kuwa sheria anayoipigia jaramba itakomesha rushwa kwenye chaguzi,basi ni vema naye akatafakari upya kama kuna umuhimu wa kuendelea kuwa kiongozi wa watu wasioafikiana na mtizamo wake.

Kinachosikitisha zaidi ni namna jamii isivyoonekana kukoseshwa usingizi na namna nchi yetu inavyozidi kutafunwa na mafisadi.Angalia mwitikio wa wananchi kuhusu 'makamanda wa vijana' wa CCM.Hivi watu hawajiulizi hawa makamanda walikuwa wapi siku zote kiasi cha kukurupuka ghafla kufishana makoti na joto lote hilo kwa kifuniko cha 'ukamanda wa vijana'?Na huo ukamanda unawasaidiaje vijana husika?Kwanini makamanda hao wasielekeze nguvu zao katika kupambana na ufisadi? Kwa asiyefahamu 'siri ya ukamanda wa vijana' basi aelewe kuwa kila anayevikwa wadhifa huo ni 'mgombea mtarajiwa'.Ni namna ya kujiweka karibu na wapiga kura.

Lakini sina tatizo sana na makamanda hao bali hao wanaoaminishwa kuwa ili waendelee wanahitaji makamanda wa vijana.Mie ni muumini mkubwa wa wazo kwamba UFISADI ni kikwazo nambari wani cha maendeleo yetu,au sababu kubwa ya kwanini tumeendelea kuwa masikini wa kutupwa licha ya utajiri lukuki wa maliasili tulionao.Logic yangu ni simple.Huwezi kujaza maji kwenye ndoo yenye matobo au kujaza upepo kwenye mpira uliotoboka.Paipo kudhibiti ufisadi na mafisadi,maendeleo yataendelea kuwa ndoto inayogeuka ukweli mchungu kila kukicha.

Na tukitegemea kwamba wanufaika wa ufisadi watajumuika nasi katika kukomesha kilekile kinachowawezesha 'kutanua' na ma-vogue,mahekalu ya bei mbaya na nyumba ndogo zisizohesabika basi tutaendelea kusubiri milele,au kwa lugha nyingine,TUANDIKE TUMEUMIA.

FUNGUKA MACHO,WAKATI NI SASA!.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.