Showing posts with label MJASIRIAMALI. Show all posts
Showing posts with label MJASIRIAMALI. Show all posts

26 Dec 2007

MAKALA HII ILIPASWA KUTOKA KATIKA TOLEO LA WIKI HII LA GAZETI LA RAIA MWEMA LAKINI HAIKUTOKA KWA SABABU ZILIZO NJE YA UWEZO WANGU.

Majuzi niliongea kwa simu na rafiki zangu wawili wa siku nyingi.Mmoja ni “mjasiriamali” anayeishi Dar es Salaam (hakasiriki ninapomtania kwamba yeye ni “misheni tauni”).Mwingine yuko Ifakara,mji niliozaliwa.Niliongea na rafiki zangu hawa kuwatakia heri na Baraka za mwaka mpya 2008.

Nikiri kwamba mara nyingi huwa namkwepa rafiki yangu wa Ifakara kutokana na mlolongo wa malalamiko anayokuwa nayo kila ninapoongea naye.Na majuzi haikuwa tofauti.Alidai mwaka mpya hauna maana yoyote kwake kwani,kwanza,kinachobadilika ni tarakimu moja tu ya mwisho katika mwaka,yaani badala ya 7 inakuwa 8.Pili,alidai kwamba jitihada zake za zamani za kujiwekea malengo ya mwaka mpya yamekuwa kazi bure kutokana na kile anachokiita “nguvu za giza”,na katika miaka ya hivi karibuni amesitisha utaratibu huo wa kujiwekea malengo ya mwaka ujao.Alinifafanulia kwamba “nguvu za giza” anazozizungumzia sio zile zinazotajwa katika Biblia bali genge la mafisadi ambao wanafanya kila linalowezekana kuhakikisha mwaka mpya unaendelea kuwa mchungu kama uliotangulia.

Huyu bwana alikuwa miongoni mwa wanafunzi waliobahatika kuendelea na masomo baada ya kuhitimu shule ya msingi.Pia licha ya kuyapenda masomo ya sayansi,alikuwa anayamudu kweli.Na uthibitisho katika hilo ni namna alivyopata pasi za juu katika Fizikia na Hisabati wakati mie niliondoka na “F” na “D” katika masomo hayo,na hatimaye nikaamua kukimbilia kwenye mchepuo wa masomo ya “Arts”.Ndoto yake ya kuwa rubani ilifikia ukingoni baada ya kumaliza kidato cha nne na kukosa nafasi ya kuendelea na masomo.Kibaya zaidi,wazazi wake hawakuwa na uwezo wa kumpeleka shule ya kulipia.Hata hivyo,alichaguliwa kujiunga na chuo cha ualimu kabla ya kuajiriwa kufundisha shule moja ya msingi katika kijiji flani tarafani Ifakara.

Nakumbuka alivyolalamika siku ya kwanza alipotia mguu kwenye kituo chake “kipya” cha kazi.Alikumbana na lundo la wanafunzi wanaobanana kwenye madarasa ambayo majengo yake yanaombea kusiwe na upepo wa nguvu kwani utaezua paa.Madawati ni machache,uhaba wa vitabu vya kufundishia ni mkubwa na nyumba ya mwalimu mkuu ni kichekesho.Alinitania kwamba ni rahisi kwake kupata mwaliko wa kuitembelea Ikulu kuliko kukaribishwa na “hediticha” wake,sababu ni kwamba makazi ya mkuu huyo wa shule ni duni kupindukia.Mbinde nyingine ni mwisho wa mwezi ambapo rafiki yangu huyu anadai inamlazimu afanye dua mfululizo ili mshahara wake upatikane katika muda mwafaka.

Kama muumini wa siasa ya Ujamaa na Kujitegemea,licha ya majukumu yake ya ualimu,ndugu yangu huyu alikuwa akijishughulisha na kilimo.Huko nako ni matatizo kama shuleni kwake.Anadai kwamba sasa amesitisha masuala ya kilimo kwani anadhani anakineemesha zaidi chama cha ushirika kuliko yeye binafsi.Alinichekesha alipodai kuwa laiti angeendelea na kilimo na kuzidi kukikopesha chama cha ushirika,basi kuna uwezekano angeishia jela baada ya kumtwanga afisa yoyote wa chama cha ushirika ambaye kila kukicha anakuja na hadithi mpya kuhusu malipo ya mazao yaliyonunuliwa kwa mkopo.

Tumrejee yule “mjasiriamali” wa jijini Dar.Huyu anatoka kwenye familia inayojiweza na ni miongoni mwa watu wasioamini kabisa kwamba elimu ni ufunguo wa maisha.Aliacha shule alipokuwa kidato cha pili,lakini ana vyeti vinavyoonyesha taaluma mbalimbali.Baba yake alimfanyia mpango wa kazi kwenye taasisi flani ambayo licha ya kuwajali watumishi wake kwa mshahara mkubwa,inasifika sana kwa rushwa.Aliwahi kuninong’oneza kwamba alipata kazi hiyo bila kufanyiwa usahili kwani baba yake na Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa taasisi hiyo ni marafiki.

Kama rafiki yangu mwalimu alivyoamua kuacha kujishughulisha na kilimo kwa kuhofia kumng’oa mtu meno kutokana na fedha anazokidai chama cha ushirika,huyu “mjasiriamali” aliamua kuacha kazi kwa kuhofia kwenda jela pindi TAKUKURU wangejaliwa uwezo wa kunasa wala rushwa wakubwa.Baada ya kuacha kazi,sasa anaendesha kampuni binafsi “inayojihusisha na kila kitu”.Anajigamba kwamba anaweza kumpatia mteja huduma yoyote anayohitaji:iwe ni kushinda tenda bila kushiriki zabuni,kutoa mzigo bandarini kwa bei poa,kupata hati ya kiwanja isivyostahili,kuzungumza na hakimu ili kesi ifutwe,na hata kuwezesha kupatikana kwa cheti feki kinachoonyesha mteja wake hana ukimwi japo hajapima.

“Mjasiriamali” huyu anadai kwamba huduma pekee asiyoweza kutoa ni kurejesha uhai wa mtu aliyefariki,na haoni kufuru kudai kuwa hilo lingewezekana laiti Mungu angekuwa anaishi Tanzania.Wakati huwa nachoshwa na malalamiko ya rafiki yangu mwalimu,huyu mjasiriamali wangu huwa “ananiboa” na majigambo yake.Kikubwa nachonufaika kwa kuongea nae ni kupata “first-hand account” ya mtu anayeshirikiana na mafisadi kukwamisha uwezekano wowote wa ndoto ya maisha bora kwa kila Mtanzania kutimia.

“Mjasiriamali” huyu ana marafiki sehemu mbalimbali duniani,wengi wao wakiwa aidha walishawahi kuja kuchuma huko nyumbani au wanadhamiria kufanya hivyo.Wengi wa wawekezaji hao ni wale wa muda mfupi,wanaanzisha mradi na kupewa zawadi ya likizo ya kodi (tax holiday),na wakishapata faida ya kutosha wanaingia mitini.Rafiki yangu huyo ananieleza kwamba tofauti na zamani,siku hizi “wazungu” wanajua “kupenyeza rupia kwenye udhia hasa kwa vile hapo kwenye udhia kuna wanaobembeleza kupenyeshewa rupia”.Na hapo ndipo “mjasiriamali” huyu anapotengeneza ulaji wake kwa kuwaunganisha “wenye rupia” na “wanaohitaji rupia” kupindisha taratibu na sheria.

Rafiki yangu mwalimu na huyu mjasiriamali “feki” wanawakilisha picha mbili tofauti zinazoendelea kushamiri huko nyumbani.Kundi dogo la watu linaishi kwa jasho la wenzao linaendelea kuneemeka kwa kukumbatia rushwa,kuuza raslimali zetu na kupinga kwa nguvu manung’uniko yoyote kuhusu ugumu wa maisha.Kwa upande mwingine ni kundi kubwa la watu ambao liwazo lao pekee la kumaliza mwaka na kukaribisha mwaka mpya ni wao kuwa hai.Hawa ni watu ambao wanahitaji kweli baraka za mwaka mpya kwani wanaishi kwa hofu ya kupata ulemavu au kupoteza maisha kwenye hospitali ambazo badala ya kutibiwa miguu wanaweza kupasuliwa vichwa,wanapanda mabasi yenye kutumia chesis za malori na pengine injini za mashine za kusaga unga,wanaweza kubambikiziwa kesi na polisi kwa makosa wasiyofanya,wanaweza kufika kazini na kuambiwa ajira yao imefariki ghafla baada ya mwajiri wa kigeni kuamua kurejea kwao,pamoja na matatizo mengine kedekede.

Rafiki zangu hawa wawili wana mtizamo tofauti kuhusu kauli ya Waziri Ngasongwa kwamba uchumi unakua.Huyo mwalimu,ambaye mara kwa mara jina la Ngasongwa halimtoki mdomoni kwa vile ni Mpogoro mwenzake,anadai inawezekana kukua kwa uchumi kunakozungumziwa ni kwa kuongezeka idadi magari ya kisasa na ya “bei mbaya” pamoja mfumuko wa mahekalu jijini Dar es Salaam.Anatamani neema hiyo ingekuwa hivyohivyo kwenye elimu,afya,kilimo,miundombinu na huduma nyingine muhimu. “Mjasiriamali” anamuunga mkono Ngasongwa na kudai kwamba uthibitisho wa kukua kwa uchumi ni yeye “drop-out” wa kidato cha pili ambaye anamiliki gari lenye thamani ya mamilioni ya shilingi,ana hekalu huko Masaki na anamudu kuwa na nyumba ndogo takriban katika kata ya jiji.Kwa yeye kila siku ni mwaka mpya,na anadhani siku mambo yatapokwenda mrama atakimbilia nje ya nchi na kutangaza kustaafu ujasiriamali wake akiwa huko.





Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.