22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Pengine kwa Kiswahili tunaweza kuzitafsiri kama Wilaya za Taa Nyekundu.Hapa zinaitwa Red Light Districts au kwa kifupi RLDs.Chanzo halisi cha neno hilo hakifahamiki vizuri huku wengine wakidai kuwa zamani hizo wafanyakazi wa reli walipokuwa wakienda kutembelea maeneo hayo walikuwa wakiacha zana zao za kazi nje,hususan taa nyekundu walizokuwa wakitumia kuruhusu treni kuondoka stesheni.Nadhani hadi hapa baadhi ya wasomaji mtakuwa hamjanielewa namaanisha nini.Ashakum si matusi,nachozungumzia hapa ni maeneo ambako akinadada wanauza miili yao.Mara nyingi maeneo hayo huwa karibu na bandarini au vitongoji vilivyotulia,labda pengine kwa madhumuni ya kuhifadhi siri kati ya watoa na wapokea huduma.

Nimesema ashakum si matusi kwa sababu najua wakati mwingine kuna kijitabia cha unafiki ambapo jamii inajifanya kama haielewi maovu yanayotokea,lakini ukiyaweka hadharani utaambiwa unakiuka maadili.Na unafiki huo hauko huko nyumbani pekee kwani hata hapa Uingereza,kwa mfano,kuna tatizo kama hilo.Kuna kitu kinaitwa a four-letter word (neno la herufi nne).Mara nyingi linaandikwa F***.Siwezi kulitafsiri hapa kwa sababu ni tusi.Cha kuchekesha ni ukweli kwamba neno hilo ni kama wimbo wa taifa vile,kwa sababu liko mdomoni kwa takriban kila mtu kuanzia kwa watoto hadi watu wazima.Lakini kwenye magazeti,redio na TV neno hilo linafichwa.

Nimesoma kwenye mtandao habari kuhusu jitihada za serikali ya mkoa jijini Dar es Salaam kupambana na vitendo vya Sodoma na Gomora katika maeneo ya Uwanja wa Fisi,Manzese.Inaelezwa kwamba kila aina ya maovu hufanyika katika viwanja hivyo.Niliwahi kuambiwa kwamba vilabu vya pombe za kienyeji mitaa hiyo vilikuwa vikirekodi taarifa ya habari ya,kwa mfano,saa 2 usiku na kisha kuipiga mida mibaya,kwa mfano saa 6 usiku,ili kuwazuga walevi waamini kwamba bado ni mapema.Pia niliskia kwamba supu,mishkaki na nyama choma za hapo inaweza kuwa ya mnyama yoyote yule kuanzia paka,mbwa pengine hata mamba. Mtu moja aliwahi kunichekesha aliposema kwamba ukiona watu wa Uwanja wa Fisi wanahangaika kuua nyoka au kenge usidhani ni kwa sababu viumbe hao wangeweza kuhatarisha maisha ya binadamu bali ni kwa ajili ya mishkaki.Nadiriki kuhisi kwamba mbwa koko anayekatiza mitaa hiyo atakuwa amechoka kuishi kwa vile uwezekano ni kwamba siku inayofuata nyama yake itakuwa kwenye supu.Na si ajabu hata tandu au ng’e wanakaangwa na kuuzwa kama pweza.

Kinachosikitisha zaidi katika miongoni mwa dhambi za maeneo hayo ni biashara ya ukahaba ambayo inasemekana inahusisha wasichana wenye umri mdogo kabisa.Inaelezwa kwamba wengi wa wasichana hao wanaletwa kutoka mikoani kuja kuuzwa kwa wanaharamu ambao kwao bidhaa ni bidhaa tu hata kama ni kinyume na utu.Ni kama biashara ya utumwa vile kwa sababu mara nyingi wanaonufaika ni hao matajiri wanaowaleta huku wasichana hao wakibakia na ujira mdogo unaowafanya wawategemee matajiri wao.

Lakini kwenye biashara ya kuuza miili sio Uwanja wa Fisi pekee bali kuna maeneo mengine chungu mbovu jijini Dar ambayo ni maarufu kwa dhambi hiyo.Kwa mgeni katika jiji la Makamba….ah siku hizi ni Kandoro,akitembea nyakati za usiku anaweza kudhani ukahaba ni biashara iliyohalalishwa na pengine wahusika wana hati za VAT.Nenda Jolly Club,nenda Kwa Macheni,nenda Kili Time,orodha ni ndefu.Wamiliki wa sehemu hizo wasilalamike kuwa nawaletea longolongo bali waelewe kuwa kwa kuwaacha makahaba kufanya shughuli zao katika maeneo hayo ni sawa na kuweka vituo vya kuokota ukimwi kirahisi.Wamiliki wa sehemu ambazo ni maskani ya changudoa hawataki kuwatimua kwa vile wanaamini kuwepo kwao kunavuta wateja hasa wale wenye uchu wa ngono holela.Tatizo jingine ni kwamba mara nyingi sehemu inayokuwa na biashara ya ukahaba huambatana na shughuli nyingine haramu kama vile kuuza na kutumia mihadarati,uporaji na ujambazi na hata utapeli.

Kama ilivyo kwenye kukabili matatizo mengine ya huko nyumbani,biashara ya ukahaba imeachwa kwa kiwango kikubwa kushamiri kana kwamba ni shughuli halali.Baadhi ya nchi za Ulaya wamehalalisha ukahaba kama sehemu ya kudhibiti biashara hiyo.Sisi hatujafikia huko na wala sidhani kwamba kwa mazingira tuliyonayo na mila zetu kuhalalisha ukahaba kutaleta mabadiliko au maendeleo.Kwa mantiki hiyo,biashara ya ukahaba ni haramu kama ilivyo ya mihadarati au shughuli nyingine za kujipatia kipato kisicho halali.Mashambulizi ya kushtukiza kwenye vijiwe vya makahaba hayawezi kuzaa matunda,hasa ukuzingatia kuwa mara nyingi mashabulizi hayo huyo ni kama ya moto wa kifuu…kasi kuubwa baadae unafifia.

Natambua kuwa ukahaba ni miongoni mwa biashara za kale kabisa duniani,na hakuna taifa linaloweza kuifuta kabisa biashara hiyo.Panapo nia, kinachoweza kufanyika ni kuidhibiti.Pia nafahamu fika kuwa tofauti na katika nchi tajiri ambapo makahaba wengi hujiingiza katika biashara hiyo kama hobby au kupata fedha za ziada za kukidhi mahitaji yao ya mihadarati,wengi wa makahaba katika nchi kama yetu wanajiingiza katika biashara hiyo kutokana na hali ngumu ya maisha.Wakati ufumbuzi wa mbali kwa makahaba wa namna hii ni kuwawezesha kiuchumi,haimaanishi kwamba umasikini wao ni sawa na ruhusa ya wao kufanya dhambi zao.Lakini ufumbuzi wa haraka wa tatizo hilo ni kuwabana matajiri ambao wanawatumia dada na mabinti zetu kama vyanzo vyao vya mapato ikiwa ni pamoja na wamiliki wa sehemu zinazoruhusu makahaba kufanya shughuli zao.

Harakati za kuivunja wilaya ya taa nyekundu ya Uwanja wa Fisi inapaswa iwe mwanzo wa tu wa zoezi la kudumu la kupambana na tatizo hili sugu ambalo si la kufumbiwa macho katika zama hizi za ukimwi.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.