17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-45:

Asalam aleykum wasomaji wapendwa.

Naomba nami niungane na Watanzania wengine kumpongeza Mama Asha-Rose Migiro kwa kuteuliwa kwake kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.Kwa hakika uteuzi huo unaiweka nchi yetu katika nafasi nzuri zaidi kwenye siasa za kimataifa na pia unasaidia kuitangaza nchi yetu.Pamoja na ukweli kwamba katika siku za hivi karibuni baadhi ya nchi duniani zimeanza kupoteza imani na Umoja wa Mataifa,chombo hicho bado ni muhimu sana kwa maendeleo na ustawi wa wanadamu popote pale walipo.Japokuwa UN ilianzishwa katika mazingira ambayo kwa kiasi flani ni tofauti na haya tuliyonayo sasa,sababu za kuianzisha na malengo ya taasisi hiyo bado yana umuhimu hadi leo.

Kuna changamoto mbalimbali zinazoikabili UN na ambazo kama haitazifanyia kazi mapema basi taasisi hiyo inaweza kupoteza nafasi yake muhimu katika nyanja mbalimbali za maendeleo ya binadamu.Yaliyopita si ndwele,tugange yajayo lakini sio rahisi kusahau uzembe uliofanywa na UN mwaka 1994 wakati Rwanda ilipotumbukia kwenye mauaji ya halaiki.Kwa namna flani hali hiyo inaonekana kujirudia kwenye mapigano yanayoendela huko Sudan hasa kwenye eneo la Darfur.Serikali ya Sudan,kwa sababu inazozijua yenyewe,imekuwa ikitoa kauli zisizoeleweka kuhusu kukomesha mapigano hayo.Kuna wakati imekuwa ikionyesha nia ya kukubali askari wa kulinda amani kutoka Umoja wa Mataifa na baadae kukataa katakata kuhusu ujio wa askari hao.Kwa vile UN ni kama mbwa asiye na meno inajikuta haina cha kufanya zaidi ya kutoa maazimio ambayo kimsingi ni mithili ya porojo ambazo haziwasaidii wahanga wa mapigano hayo.Kwa muda mrefu sasa,kumekuwa na mjadala unaokera kwa namna flani kuhusu nini hasa kinatokea huko Darfur.Marekani wanataka itamkwe bayana kuwa kinachoendeleo huko ni mauaji ya halaiki kama yale ya Rwanda,lakini UN imekuwa ikisita kutumia msamiati huo.Lakini hivi msamiati unamsaidia nini mtu anayeteseka huko Darfur.Iwe kinachotokea Darfur ni vita,mapigano,mauaji ya halaiki au machafuko,ukweli unabaki kwamba hali hiyo inabidi isitishwe haraka sana.

Jingine nalotaka kugusia leo ni ujio wa Rais Jakaya Kikwete hapa Uingereza.Kwa mujibu wa taarifa tulizosambaziwa na ubalozi wetu,siku ya Jumapili Rais atakutana na Watanzania waishio hapa na kuongea nao jijini London.Watu wamekuwa na kiu kubwa ya ujio huo wa Rais.Nadhani umati utaojitokeza unaweza kuwa wa kihistoria hasa kwa vile London ni sehemu inayofikika kirahisi na siku ya mkutano ni Jumapili ambayo watu wengi wako mapumzikoni.Pengine makala ya wiki ijayo inaweza kuelezea mawili matatu yatakayojiri kwenye mkutano huo,japo sina uhakika wa asilimia 100 kama nitahudhuria kwa sababu ambazo zinaweza kuwa nje ya uwezo wangu.

Ni habari za kufurahisha kusikia Shirika letu la Ndege (sijui ni ATC au ATCL…mie ntaliita ATC tu) limepata ndege mbili.Mwanzoni nilidhani hizo ni ndege mpya lakini baadaye imefahamika kuwa ndege hizo ni “mitumba” na zimekodiwa kwa gharama ya dola 50,000 kwa mwezi.Nadhani mwezi unakaribia kukatika sasa tangu ndege hizo zipatikane na sijui kama tayari zimeshaanza kutumiaka au la,ila nina uhakika kuwa iwe zimeshaanza kazi au bado,mwenye mali atapatiwa au ameshapatiwa hizo dola 50,000 zake za mwezi huu.Pamoja na uwazi uliopo katika suala hili bado ATC hawajaeleza iwapo itakuwa inalipa kiasi hicho kwa kila ndege au ni kwa ndege zote mbili.Naomba niseme kwamba sio siri kuwa hivi sasa Watanzania wengi wanaonekana kushtuka kila wanaposikia neno “mkataba” hasa ukizingatia kuwa ni majuzi tu “wameachwa kwenye mataa” na wajanja waliokuwa wanajiita Richmond Development Company.ATC wanatakiwa wafanye jitihada za dhati kuhakikisha kuwa wanatengeneza faida kila mwezi ili wakishatoa hizo dola 50,000 waweze kujiendesha kama shirika/kampuni ikiwa ni pamoja na kutekeleza wajibu wake wa maslahi kwa watumishi wake na kulipa kodi stahili kwa serikali.Biashara ya safari za anga ina ushindani mkubwa,na katika zama hizi ambazo watu wanataka kile kilicho bora kabisa basi ATC wakae wakijua kuwa wasipojifunga mkanda wataumia.

Nadhani ATC wataangalia uwezekano wa kutafuta pia “ruti” zinazolipa kimataifa kwa sababu safari za ndani pekee zinaweza kuwa hazitoshi kurejesha uhai wa shirika hilo.Kama wengine wameweza kufanikiwa katika biashara ya usafiri wa anga basi hata sisi Watanzania tunaweza pia tukidhamiria kwa nguvu zote.Wenzetu Wakenya wanasifika na Kenyan Airways yao na sio siri kuwa hilo ni miongoni mwa mashirika ya ndege maarufu duniani.Wazo la kukodi ndege hizo linapaswa kuwa ni la muda tu wakati ATC inajipanga vizuri kujiendesha kwa faida na hatimaye kumiliki ndege zake yenyewe.Kukodi ni jambo la kawaida kwenye biashara,na ATC wanaweza kuanza na kukodi ndege hizo mbili,halafu kama watafanya biashara ya faida wakafanikiwa kupata ndege moja au mbili nyingine,basi hapo warejeshe mitumba hiyo kwa wenyewe kisha wakaelekeza nguvu zao katika ndege zao halisi.Cha muhimu ni kwamba kuzalisha faida sio muujiza na kama mtu au taasisi anaingia kwenye biashara pasipo na malengo ya kuzalisha faida basi ni bora kutofanya kabisa biashara hiyo.Kama CRDB ya wazalendo imeweza kutengeneza faida basi hata ATC nayo inaweza,kinachohitajika ni nia ya dhati ya kutengeneza faida hiyo.

Jingine fupi ni hili la ku-“fast track” kuanzishwa Muungano wa Nchi za Afrika Mashariki.Hivi haraka hiyo ni ya nini?Naafikiana kwa asilimia zaidi ya 100 na Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere,Joseph Butiku, kuhusu wazo lake la kumwita Rais Museveni atueleze kwanini “ni lazima” awe rais wa Shirikisho hilo kabla hajaondoka madarakani.Hii inanikumbisha “umbea flani wa kisiasa” niliousikia miaka kadhaa iliyopita kwamba kuna kitu kama mkakati unafanywa kurudisha himaya ya Wahima,na championi wa mkakati huo hakuwa mwingine bali huyohuyo Museveni.Pengine huo ni umbeya tu lakini nadhani hakuna umuhimu wowote wa kuharakisha uundwaji wa Shirikisho hilo kwa sasa.Naipongeza serikali kwa uamuzi wake wa kukusanya maoni ya Watanzania,na nina imani kuwa maoni hayo yatazingatiwa kabla ya kufikia hatua ya kukubali au kukataa kuianzisha Shirkisho hilo.Maoni ya watu ni ya siri,lakini langu liko wazi:SIAFIKI wazo la shirikisho hilo kwa sasa labda hapo baadae.Hoja yangu ya msingi ni kwamba tuna mambo yetu kadhaa muhimu ya kuyashughulikia sie wenyewe kabla hatujawakaribisha wengine.Pia kila siku tumekuwa tukiambiwa na wanasiasa wetu kwamba Tanzania ni kisiwa cha amani,sasa je hilo shirikisho la Afrika mashariki nalo litakuwa kisiwa cha amani au je Tanzania itaendela kuwa kisiwa cha amani ndani ya shirikisho hilo?

Mwisho,kampuni ya Apple jana wameibuka na “mama wa simu zote.”Kuna kitu inaitwa “iPhone”.Hiyo itakuwa sio simu ya kawaida bali mkusanyiko wa mahitaji muhimu ya kimawasiliano na burudani.iPhone haitakuwa na vitufe (buttons) vya namba au herufi bali nyenzo muhimu itakuwa kidole cha mtumiaji simu pamoja na kioo cha simu (touch screen).Simu hizo zitaingia sokoni katikati ya mwaka huu kwa bei ya kuanzia dola 500.Mambo ya “teke linalokujia” (teknolojia) hayo!

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.