24 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-47


Asalam aleykum,

Kwa zaidi ya wiki sasa, habari iliyotawala zaidi hapa Uingereza ni kasheshe iliyojitokeza ndani ya jumba walimohifadhiwa washiriki wa kipindi kiitwacho “Celebrity Big Brother.”Hii ni Big Brother kama ile aliyoshiriki Mwisho kule “Sauzi” lakini hapa washiriki ni watu maarufu (au waliowahi kuwa maarufu). Kipo kipindi kingine kinachofanana kabisa na kile cha akina Mwisho ambacho kinawashirikisha watu wa kawaida (wasio maarufu) na tofauti na hiki kinachoendelea sasa, washiriki hupatikana kwa njia ya usaili. Hawa “celebrities” huombwa kushiriki na wakikubali hupatiwa maelfu au malaki ya pauni kwa ushiriki huo (hiyo ni nje ya zawadi kwa atakayeshinda). Mwaka jana mshiriki maarufu kwenye kipindi hiki alikuwa Mbunge machachari kabisa na mpinzani maarufu wa vita ya Irak, George Galloway wa chama cha Respect.Pamoja na washiriki wengine, mwaka huu kuna kaka yake Michael Jackson, aitwaye Jermaine, Miss England wa mwaka 2004,Daniella, mwanamuziki wa zamani Jo O’Mera, aliyekuwa mshindi wa Big Brother isiyo ya mastaa, Jade Goody na staa wa sinema za Bollywood (za Kihindi), Shilpa Shetty, pamoja na washiriki wengine ambao baadhi yao wameshatolewa kwa kupigiwa kura na watazamaji.Kasheshe nayoizungumzia ilijitokeza kati ya kundi la washiriki watatu ambao wote ni Waingereza(Jade,Daniella na Jo) dhidi ya nyota wa Bollywood,Shelpa,ambaye ni Mhindi na amealikwa kushiriki kutoka India.

Kwa kifupi,songombingo lilichipuka baada ya mabinti hao watatu kuanza “kumng’ong’a” (nadhani neno hili linamaanisha kusengenya) Mhindi Shelpa,ambapo kadri siku zilivyozidi kwenda maneno yenye kuleta hisia za ubaguzi wa rangi yakaanza kusikika.Kuna wakati mabinti hao wa Kiingereza walisikika wakimwambia Shelpa arudi kwao India akaishi kwenye vibanda vya masikini.Pia walisikika wakimwambia kuwa Kiingereza chake kina lafidhi inayochefua.Kama hiyo hazitoshi,mmoja wa mabinti hao alinukuliwa akisema kuwa eti wahindi wengi wamekonda kwa vile wana tabia ya kula chakula kisichoiva vizuri.Kama utani vile,baadhi ya watazamaji wakaanza kutoa malalamiko yao kwa mamlaka inayohusiaka na usimamizi wa vyombo vya mawasiliano,OFCOM,pamoja na kituo cha televisheni cha Channel 4 kinachorusha kipindi hicho.Kufikia mwishoni mwa wiki iliyopita,OFCOM ilikuwa imeshapokea malalamiko zaidi ya 40,000 ambayo katika historia ya vyombo vya habari vya hapa ni kiwango cha juu kabisa cha malalamiko kutolewa dhidi ya kipindi.Na kama bahati mbaya,wakati nyota huyo wa Kihindi anapewa maisha magumu na mabinti hao wa Kiingereza,Kansela Gordon Brown,mtu anayetarajiwa kumrithi Tony Blair baadaye mwaka huu,alikuwa ziarani India.Ilimbidi Brown kuomba samahani kwa wananchi wa India na kuwataka waelewe kuwa hao wanaompelekesha Shelpa hawamaanishi kuwa Waingereza wote wana tabia kama yao.Tony Blair nae ilimlazimu alizungumzie suala hilo bungeni akisema anakemea aina yoyote ile ya ubaguzi.Waziri mwenye mamlaka kuhusu masuala ya utamaduni nae alikishutumu kipindi hicho kwa kugeuza hisia za ubaguzi wa rangi kuwa burudani.Kasheshe hiyo ndio ikawa habari kuu kwenye runinga na magazeti yote ya hapa.

Ijumaa iliyopita kulikuwa na kura ya kumtoa mshiriki mmoja.Waliokuwa wanapigiwa kura ni Shelpa na Jade,ambaye kimsingi ndio alikuwa kinara wa maneno ya ubaguzi dhidi ya Shelpa.Kansela Gordon Brown akiwa India aliwataka Waingereza kupiga kura dhidi ya Jade ili kuonyesha kuwa hawaungi mkono kauli zake za kibaguzi.Magazeti nayo yakaanzisha kampeni kali dhidi ya Jade ili atolewe.Matokeo yakawa kama yalivyotarajiwa,na Jade akatolewa kwa zaidi ya asilimia 80 ya kura,ambayo ni rekodi kwenye vipindi vya Big Brother ya mastaa na ile ya watu wa kawaida.Hadi sasa,japo hali imetulia baada ya Jade kutolewa,bado watu mbalimbali wamekuwa wakiitaka Channel 4 ikifute kabisa kipindi hicho.OFCOM nayo imeanzisha uchunguzi dhidi ya tukio hilo.

Tukio hili limezua mjadala mkubwa kuhusu suala zima la ubaguzi wa rangi hapa Uingereza.Wapo wanaoipongeza Channel 4 kwa kuonyesha hali halisi ilivyo nchini humu.Hao wanasema kuna mamilioni ya akina Jade huko mitaani ambao wanaendeleza ubaguzi wa rangi.Wengine wanakilaumu kituo hicho cha televisheni kwa madai kwamba kinawatumia washiriki kuwanyanyasa watazamaji na baadhi ya washiriki wa Big Brother hasa wale wanaotaka nje ya Uingereza.Pia wapo wanaowapongeza wanasiasa kama Blair na Brown kwa kukemea yaliyojiri kwenye kipindi hicho.Lakini wapo pia wanaowalaumu wanasiasa hao kwa yaliyojitokeza kwenye kipindi hicho.Hoja ni kwamba,wanasiasa hao wanaelekea kushtushwa na yanayosemwa kwenye Big Brother kwa vile hawako karibu na wananchi wao.Wanaolaumu wanasiasa wanasema laiti kama viongozi hao wangekuwa karibu na wanaowaongoza basi ni dhahiri wangejua kuwa ubaguzi wa rangi ni suala la kila siku katika maisha ya hapa Uingereza.

Ni ukweli usiofichika kuwa mara kwa mara wageni wengi na hata wazaliwa wa hapa wenye asili ya nje wamekuwa wakikumbana na vitendo vya ubaguzi wa rangi.Nilishawahi kulielezea suala hilo kwenye makala zangu za huko nyuma.Na tatizo hilo halipo hapa tu bali takriban sehemu nyingi za nchi za Magharibi.Nakumbuka maongezi na rafiki yangu mmoja Mwamerika Mweusi ambaye aliniuliza kuhusu ubaguzi wa rangi hapa Uingereza.Nilipomwambia upo,alinipa moyo kwa kusema kuwa bora mie ambaye sijazaliwa hapa na nimekuja tu kujiendeleza kielimu,kuliko yeye ambaye amezaliwa Marekani na ni raia wa nchi hiyo kama ilivyokuwa kwa vizazi vyake vilivyomtangulia lakini bado anakutana na vitendo vya ubaguzi mara kwa mara kwa vile tu ni mtu mweusi.Hali ni mbaya zaidi huko Ulaya ya Mashariki ambako mashambulizi dhidi ya wageni ni mambo ya kawaida.

Tukirudi kwenye lawama zinazotolewa na watu dhidi ya wanasiasa waliojitokeza kuzungumzia kasheshe la Big Brother, nadhani kuna hoja ambayo kwa namna flani inaweza kuwa na maana hata huko nyumbani. Nimesoma kwenye gazeti flani kwamba hivi majuzi wananchi katika kijiji cha Hale-Mwakinyumbi huko Tanga waliamua kufunga barabara kwa muda kwa kulala hapo barabarani baada ya mwanafunzi mmoja kugongwa na gari na kufariki. Walichukua hatua hiyo kuonyesha kukerwa kwao na kutotekelezwa kwa ahadi ya kuwekwa matuta eneo hilo iliyotolewa na mbunge wao miezi kadhaa iliyopita. Mbunge ni mwakilishi wa wananchi na ni kiungo muhimu kati ya serikali na anaowawakilisha. Wapo ambao wamepata uwaziri kutokana na kura zilizowapeleka bungeni na hatimaye kuteuliwa kuwa mawaziri. Katika lugha nyepesi, waajiri wa mbunge wa kuchaguliwa ni wananchi katika jimbo analotoka. Kasheshe ya Hale ilizimwa na Mkuu wa Wilaya aliyelazimika kuweka ahadi ya maandishi kuthibitisha kuwa tatizo hilo la matuta litatatuliwa hivi karibuni. Laiti mbunge aliyeweka ahadi hiyo angeitekeleza basi wala kusingekuwa na haja ya kuwepo kwa zahma hiyo. Enewei, pengine alikuwa anasubiri wawekezaji kwenye mradi wa kuweka matuta hayo yenye lengo la kupunguza ajali. Na pengine kama wawekezaji hao wangepatikana mapema huenda ajali hiyo ingeepukika (japo waswahili hudai eti ajali haina kinga!!?)

Mara nyingi yanapojitokeza matatizo sehemu flani, lawama huelekezwa serikalini. Lakini serikali ni taasisi ambayo kwa kiasi kikubwa inaundwa na wataalamu na kiasi kidogo cha wanasiasa. Taasisi hii (serikali) inategemea zaidi habari kutoka kwa wale walio karibu na wananchi (japo haimaanishi kuwa serikali iko mbali na wananchi). Kama ilivyotokea kwa wanasiasa wa hapa walioonekana kushtushwa na yanayotokea kwenye Big Brother kwa vile wako mbali na wale wanaowaongoza, baadhi ya wanasiasa wetu hujikuta wanashangaa yanapotokea matatizo huko mitaani kwa vile hawako karibu na wanaowawakilisha. Kuna masuala mengi tu ambayo yanaweza kabisa kupatiwa ufumbuzi bila kusubiri ziara ya Rais au waziri iwapo wawakilishi wa wananchi hao watakuwa karibu nao zaidi na kujua yanayowasibu. Natambua kuwa wapo wawakilishi wanaojituma vya kutosha, na ofisi zao huko majimboni ziko wazi kusikia matatizo ya wanaowawakilisha lakini sote tunafahamu pia kuwa wapo wale ambao huonekana majimboni pale tu inapotokea ziara ya Rais au viongozi wengine wakuu, au kwa uhakika zaidi pale unapojiri wakati wa kuomba tena kura kwa wananchi.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.