31 Jan 2007



Asalam aleykum,

Katika makala ya wiki iliyopita niliwaletea mchapo kuhusu kasheshe iliyokuwa imetawala vyombo vya habari vya hapa Uingereza kuhusiana na kipindi cha “Celebrity Big Brother”.Kasheshe hiyo iliyovuka mipaka na kuchukua sura ya kimataifa,iliwahusisha washiriki watatu ambao ni wazaliwa wa hapa dhidi ya Shelpa Shetty,staa wa filamu za Bollywood aliyealikwa kushiriki katika kipindi hicho kutoka India.Watatu hao walilalamikiwa na maelfu ya watazamaji wa Channel 4 kutokana na matamshi yao yaliyotafsiriwa kuwa na mtizamo wa ubaguzi wa rangi.Jumapili iliyopita,Shelpa alifanikiwa kuwa mshindi katika fainali ya kipindi hicho ambapo alipata takriban ya robo tatu ya kura zote zilizopigwa na kufuatiwa na Jermaine,kaka yake Michael Jackson (Jermaine amesilimu na sasa anaitwa Muhammad Abdul Aziz,na amenukuliwa akisema anataka kumshawishi Michael nae asilimu).Inaelezwa kuwa ushindi huo wa Shelpa unaweza kumuingizia takriban pauni milioni 10 kutokana na ofa lukuki zinazomiminika kwake kutoka sehemu mbalimbali,ikiwa ni pamoja na maombi zaidi ya 25 ya makampuni ya filamu ya Hollywood,hapa UK na huko India.Kipindi hicho na kasheshe hiyo ya ubaguzi imesaidia kwa namna flani kuibua mjadala wa kitaifa kuhusu suala zima la ubaguzi wa rangi hapa Uingereza.

Tukiachana na hilo,leo ninataka kuzungumzia suala la ulimbwende,yaani mambo ya u-Miss.Lakini kabla sijaingia kwa undani,ngoja nizungumzie kile kinachoitwa “harakati dhidi ya warembo wenye saizi ziro (size 0).” Hivi karibuni,kumekuwa na kelele nyingi barani Ulaya na hata huko Amerika dhihi ya akinadada waliokaukiana katika kile wanachokiona kuwa ndio sifa muhimu ya urembo.Walengwa wakuu sio ma-Miss bali wale wanaojihusisha na mambo ya fasheni,au “models” kama wanavyoitwa katika “lugha ya mama (Kiingereza).” Sio siri kuwa kuna mabinti wamekuwa wembamba kupita kiasi na unaweza kudhani kuwa pindi upepo ukivuma kwa nguvu basi watapeperushwa kama makaratasi.Wajuzi wa mambo ya urembo wameanza kukubaliana kwamba urembo hauna maana kuonekana huna afya.Au kwa lugha nyingine,haihitaji binti akonde kupita kiasi ndio aonekane mrembo.

Nakumbuka makala flani niliyosoma kwenye gazeti la Guardian la hapa iliyokuwa inazungumzia kitu walichokiita “The J-Lo factor” kwenye urembo wa mwanamke mzungu.Hoja ilikuwa ni kwamba katika miaka ya karibuni baadhi ya wanawake wa kizungu wamekuwa wakitamani kuwa na “shepu za Kiafrika”.Ashakum si matusi,lakini wengi tutaafikiana kwamba kabla ya haya mambo ya utandawazi,siha ilikuwa ni miongoni mwa vigezo vikubwa vya urembo wa mwanamke wa kiafrika.Pengine sieleweki nachokiongelea hapa lakini sio kosa langu bali ukweli kwamba kuna mada flani zinakuwa ngumu kuziongelea kwa uwazi kwenye lugha yetu ya Taifa.Ila kwa kifupi ni kwamba maumbile kama ya Jenipher Lopez (ambayo kimsingi ni ya kawaida kwenye jamii za Kiafrika) yana mvuto wa kipekee.Kwa wazungu,urembo ulikuwa ukiambatana sana na wembamba wa mwili mzima.Lakini kadri miaka inavyozidi kwenda mbele akinadada wa kizungu nao wameanza kutamani kuwa na shepu za Kiafrika.

Sasa nirejee kwenye mada yangu kuhusu ulimbwende.Nimesoma kwenye baadhi ya magazeti ya huko nyumbani habari zinazomhusu Miss Tanzania wa sasa ambapo inadaiwa alipigwa picha “za ajabuajabu” akiwa na “staa” flani wa bongofleva.Sijabahatika kuziona picha hizo lakini inaelekea zimesababisha kasheshe ya namna flani.Hapa kuna mambo makuu mawili.La kwanza ni nafasi ya Miss Tanzania katika jamii na pili ni uhuru wake kama binadamu wa kawaida.Nianze na hilo la pili.Huyo binti ana uhuru wa kikatiba kufanya yale anayotaka kama binadamu mwingine yoyote yule.Uhuru huo unaweza pia kujumuisha kuwa na rafiki wa kiume,japo katika mila zetu za Kiafrika “tunajidai” kuwa hilo halipo.Tuwe wakweli,hilo lipo sana ila ni kweli kwamba halipendezi machoni mwa wazazi wengi ambao wangependa kuona mabinti zao wakijihusisha na mahusiano ya kimapenzi pale tu watakapoolewa.Nadhani wengi wataafikiana nami kuwa huko mitaani suala la kukiuka maadili linaonekana kuwa kama fasheni flani vile.Yaani ni hivi,binti akiwa hana rafiki wa kiume anaonekana kama haendi na wakati.Hiyo sio sahihi,na pamoja na ukweli kuwa imani hiyo imetapakaa mitaani,bado nasisitiza kuwa ni imani potofu na inapaswa kukemewa kwa nguvu zote.Mila na desturi zote zinatamka bayana kuwa binti ataruhusiwa kujihusisha na masuala ya mapenzi pale tu atapoolewa,na hilo halina mjadala hata kama halizingatiwi.

La pili ni nafasi ya Miss Tanzania katika jamii.Huyu ni sawa na balozi wetu.Aliiwakilisha nchi yetu kwenye mashindano ya kimataifa.Kuna mabinti maelfu kwa maelfu ambao wanamwangalia yeye kama “role model” wao.Kinadharia,yeye ndiye kioo cha urembo wa mabinti wa Kitanzania,ndani na nje ya nchi.Kwa mantiki hiyo,anapaswa kufanya yale yanayotarajiwa na jamii.Miss Great Britain wa mwaka 2004 alivuliwa taji lake kwa kufanya mambo kinyume na cheo chake ikiwa ni pamoja na kupiga picha za utupu kwenye gazeti la Playboy la Marekani.Pia Miss USA wa sasa ameponea chupuchupu kubwagwa na “Lundenga wa huko” Donald Trump baada ya matendo yake kuonekana yanaaibisha nafasi aliyonayo katika jamii.

Binafsi nimekuwa nafanya utafiti usio rasmi kuhusu fani hii ya u-Miss.Matokeo yasiyo rasmi ya utafiti huo yanaonyesha kuwa kuna matatizo yaliyofichika kwenye fani hiyo.Warembo wengi wamekuwa wakijitahidi kutueleza kuwa fani ya urembo si umalaya,lakini hakuna hata mmoja ambaye amewahi kutuambia kwanini baadhi ya watu katika jamii bado wana mawazo “potofu” kuhusu fani hiyo.Kuna mengi yasiyopendeza yanayotokea “nyuma ya upeo” (behind the scene) ambayo kwa kiasi kikubwa ndio yanayochangia kuleta hisia zinazoweza kuiharibia jina fani hiyo inayozidi kukua kila mwaka.Kuna tatizo la mfumo mzima wa fani hiyo,tatizo la tamaa za warembo wenyewe na tatizo sugu la uzinzi hasa wale wazinzi wenye fedha ambao udhaifu wao mkubwa ni kutembea na warembo wenye majina,na warembo wanaotaka kutembea na watu wenye majina.Mfumo mzima wa mashindano ya urembo huko nyumbani unakaribisha mazingira ya rushwa za ngono,na kwa wenye tamaa ya kushinda hata kama hawana sifa wanaweza kabisa kutoa rushwa hiyo ambayo nadhani TAKURU wanapaswa kuitupia macho.Mashindano ya urembo yanapaswa kuendeshwa kwa uwazi zaidi,na kwa vile wahusika wanafahamu fika kuwa kwa kiasi flani kuna “hisia potofu” kuhusu fani hiyo basi hawana budi kutengeneza mazingira ambayo yataishawishi jamii kukubali kuwa fani hiyo ni poa.

Mwisho, wanaoweza kuleta mabadiliko ya maana zaidi katika fani hiyo ni warembo wenyewe. Nadhani wanaharakati wa masuala ya wanawake nao wanapaswa kuwasaidia mabinti wenye nia ya dhati ya kushiriki kwenye fani ya urembo na pia kuwafumbua macho wale ambao pengine pamoja na ulimbwende wa asili walionao bado wanashawishika kutafuta “ushindi nje ya ukumbi wa mashindano.” Pia napenda kutoa changamoto kwa watafiti (researchers) hasa wa kike kufanya utafiti kwenye eneo hilo (nilofanya mie sio rasmi) hasa kipindi hiki tunapoelekea kuanza mchakato wa kumpata Miss Tanzania wa mwaka 2007 na pengine si vibaya iwapo TAKURU nayo itakuwa “beneti” kuhakikisha kuwa waombaji na watoaji wa rushwa za ngono kwenye mashindano ya urembo wanakaliwa kooni.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.