18 May 2007

Asalam aleykum,

Siku chache zilizopita nilikuwa na mawasiliano ya barua-pepe na “webmaster” wa gazeti la Mwananchi kuhusu namna tovuti yao inavyoendeshwa.Katika barua yangu pepe ya kwanza nilimfahamisha kuwa kuna habari zinazokinzana kwenye ukurasa mmoja kwenye tovuti yao.Habari moja ilikuwa ikisema kuwa pambano la bondia Matumla huko Afrika Kusini limeahirishwa kwa vile mpinzani wake amezidi uzito.Lakini chini ya habari hiyo kulikuwa na habari nyingine kuwa Matumla amepigwa kwenye pambano hilo (ambalo kwa mujibu wa habari ya kwanza ni kuwa halingekuwepo).Kadhalika kwenye ukurasa huohuo kulikuwa na makala ya uchambuzi ambayo msomaji akibonyeza anakutana na habari tofauti kabisa (hilo ni jambo la kawaida kwenye tovuti ya gazeti la Uhuru).Webmaster wa Mwananchi alinipatia majibu ambayo kimsingi sikuafikiana nayo japo sikumfahamisha.

Nilimwandikia kwa mara ya pili baada ya kukerwa na tabia ya gazeti hilo kuweka habari mpya kwenye tovuti yao majira ya jioni kwa saa za hapa Uingereza.Katika majibu yake,webmaster wa Mwananchi alinieleza kuwa moja ya sababu ya kuweka habari mpya jioni badala ya asubuhi ni ushindani wa kibiashara.Sikuafikiana naye kwa asilimia 100.Sikuafikiana naye kwa sababu kama suala ni ushindani wa kibiashara,je ina maana tovuti nyingine kama ippmedia.com,freemedia.com (Tanzania Daima),dailynews-tns.com (Dailynews/Habari Leo)-ambazo kwa kawaida huweka habari zao asubuhi- hazijali ushindani wa kibiashara?Pia kama hoja ni ushindani wa kibiashara,iweje basi magazeti yanayochapishwa huko Kenya na kampuni mama ya Mwananchi yawe yanaweka habari asubuhi?Au tuseme huko Kenya hakuna ushindani wa kibiashara?

Naomba ieleweke kuwa huu ni mtizamo wangu binafsi na hauwakilishi maoni ya gazeti hili.Kwa hakika baadhi ya vyombo vya habari vinapuuza haki za wasomaji wa tovuti zao.Ndugu zangu wa Business Times (Majira) ndio huwa wanatusahau kabisa akina sie ambao tegemeo letu pekee la habari za huko nyumbani ni kwenye mtandao.Kwenye tovuti yao,kuna viunganishi ambavyo ukivibonyeza havikupeleki popote na mara nyingi uwekaji wa habari mpya unachukua muda mrefu sana.Nadhani ni muhimu kukumbushana kwamba japo vyombo vya habari vinaendeshwa kibiashara lakini lengo kuu ni kupasha habari.Mtandao unaviwezesha vyombo vya habari kuwafikia walengwa katika kila kona ya dunia.Ni muhimu kuondokana na dhana kwamba kuweka asubuhi habari za gazeti la leo kunapunguza mauzo ya gazeti hilo.Kuna wakati ulizuka mjadala hapa UK kwamba huenda mtandao ungeweza kuua soko la magazeti (hasa ikizingatiwa kuwa takriban ya asilimia 62 ya wakazi wa hapa wana “access” ya mtandao ukilinganisha na takriban asilimia 0.9 tu ya huko nyumbani-kwa mujibu wa http://www.internetworldstats.com). Lakini imethibitika kuwa wasomaji wengi wa magazeti wanapendelea njia ya asili ya kununua nakala ya gazeti hata pale ambapo wanaweza kupata habari za gazeti hilo kwenye mtandao.Ukweli unabaki kuwa nakala ya kielektroniki ya gazeti bado sio sawa kabisa na nakala halisi ya gazeti.Kwahiyo,makala hii inapenda kutoa changamoto kwa vyombo vyetu vya habari kuboresha tovuti zao na kutambua kuwa kwa namna hiyo wanafikisha habari kwa hadhira kubwa zaidi ulimwenguni.Pengine ni muhimu kutumia fursa hii kutoa changamoto kwa vituo vya redio na televisheni kuangalia uwezekano wa kutuwekea mtandaoni angalau “vipingiri” (clips) vya vipindi vyao.Clouds FM walijaribu lakini sijui imekuwaje tena!

Jingine lililonishtua sana ni habari kwamba Mkuu wa Mkoa wa Mbeya “amewawakia” wazee flani wa mkoa huo ambao kwa uzalendo wao walijitolea kutoa taarifa za siri kwa IGP na DCI.Pengine tunalopaswa kujiuliza kabla ya kumlaumu RC huyo ni je alipataje habari kuwa wazee hao walipeleka habari huko kwa vigogo wa polisi?Dhana nyepesi ni kuwa siri hizo zilivujishwa,yaani zilitoka Mbeya zikaenda zilikopelekwa kisha zikarudi tena Mbeya.Hili ni jambo la hatari sana kwa vile licha ya kupoteza imani na ushirikiano kati ya wananchi na jeshi la polisi pia linahatarisha maisha ya wazalendo hao.Wengi wetu tunafahamu namna ambavyo baadhi ya taarifa zinazowasilishwa polisi kuhusu watu waovu kwenye jamii huwa zinarejeshwa kwa waovu hao,na kibaya zaidi kuna wakati waovu hao hujulishwa kuwa ni nani “aliyewachoma”.Nimesoma kauli ya DCI lakini niseme bayana kuwa sijaielewa.Kwa upande mmoja alionekana kumshangaa RC kwa kuwatisha wazee hao lakini kwa upande mwingine anasema kuwa hapingani na RC huyo kwa vile mkoa huo uko kwenye mamlaka yake.Ni kweli kuwa RC ni sawa na “rais” wa mkoa lakini jeshi la polisi ni taasisi ya kitaifa.Je DCI hadhani kuwa kwa kutopingana na RC katika suala hilo inaweza kusababisha ma-RC wengine kuwadhibiti “mainfoma” wa polisi kwenye mikoa yao kwa kigezo cha kuwa na mamlaka “isiyo na kikomo” kwenye mikoa yao?Je na ma-DC nao wakiiga staili hiyo itakuwaje?

Ni dhahiri kuwa laiti kungekuwa na udhibiti wa kutosha wa taarifa zilishowasilishwa huko polisi wala huyo RC asingejua kuwa kuna wazee mkoani mwake wamewasilisha taarifa hizo.DCI alipaswa kutueleza kuwa ni nani amevujisha habari hizo na ameshachukuliwa hatua gani.Sakata hili linanikumbusha maneno ya mtetezi wa vijana,Mheshimiwa Amina Chifupa,alipoamua kulivalia njuga suala la biashara ya madawa ya kulevya.Alieleza bayana kuwa baadhi ya wananchi wanawafahamu “wauza unga” lakini wanahofia kuwaripoti polisi kwa kuogopa madhara watakayopata pindi habari zitaporejeshwa kwa “wazungu hao wa unga” kuwa flani ndio kakuripoti.Mara kadhaa mbunge huyo alieleza namna alivyokuwa akibughudhiwa na “wahusika” wa biashara hiyo,na wapo wanaoamini kuwa matukio ya hivi karibuni kumhusu mbunge huyo yana mkono wa hao aliokuwa amewatangazia vita.Inasikitisha kuona vita aliyoianzisha ambayo ingeweza kuokoa maisha ya mamilioni ya vijana wetu inafifia kama moto wa karatasi kwa kukosekana sapoti ya kutosha.

Nimalizie makala hii kwa kuzungumzia zoezi la kukusanya maoni kuhusu Muungano wa nchi za Afrika Mashariki.Nimesoma maoni aliyotoa Mwanasheria Mkuu wa zamani wa Kenya Charles Njonjo kuwa yeye na wenzake walikunywa “shampeni” jumuiya ya zamani ilipovunjika,na mawazo yake kwamba Kenya inahitaji angalau miaka 50 kabla haijafikiria kuungana kisiasa na nchi nyingine.Pengine kwetu miaka 50 ni mingi sana lakini hadi dakika hii sielewi kuwa hivi hilo shirikisho linaharakishwa kwa manufaa ya nani.Profesa Wangwe amejikuta lawamani kwa tuhuma kuwa anachofanya ni zaidi ya kukusanya maoni kwani mara kadhaa amenukuliwa akiwatoa hofu wananchi kuhusu kuanzishwa jumuiya hiyo.Hivi tumeshafanya tathmini ya kutosha ya faida na hasira ya ushirkiano tulionao sasa hivi kabla ya kukimbilia huko tunakokwenda?Jamani,nchi yetu ina matatizo mengi ya msingi na ya haraka zaidi kushughulikiwa kuliko hili la jumuiya.Kwanini nguvu zinazopelekwa kwenye suala hili zisielekezwe kwenye utatuzi wa matatizo ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar?Pasipo kudharau uamuzi wa kuunda tume ya kukusanya maoni kuhusu shirikisho,nashawishika kusema kuwa lingeweza kuwa jambo la muhimu zaidi iwapo ingeundwa tume ya kuharakisha mapambano dhidi ya rushwa au hata kuendeshwa kura ya kitaifa ya kutaja majambazi na wauza unga.

Alamsiki

1 comment:

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.