31 May 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-64

Asalam aleykum,

Juzijuzi zimepatikana taarifa kuwa serikali ya Uingereza ina mpango wa kuchunguza mimba kabla kinamama hawajajifungua ili kubashiri tabia ya “vichanga” vitapozaliwa.Hii sio habari nyepesi nyepesi,bali ni taarifa za kweli ambazo ziliandikwa kwenye magazeti na kuonyeshwa kwenye runinga.Kuna kitu kinaitwa “police state” ambacho kwa lugha nyepesi ni kwamba serikali inaingilia uhuru wa mwananchi kupita kiasi,inataka kujua anaamka saa ngapi,anakula nini,anaongea na nani,na kadhalika na kadhalika.Simaanishi kuwa nchi hii nayo ni “police state” lakini katika kile inachokieleza kama mikakati yake dhidi ya uhalifu au ugaidi,inajikuta ikitengeneza sheria ambazo zinawafanya baadhi ya wanaharakati wa haki za binadamu kuhisi kuwa uhuru wa wananchi unazidi kuwekwa chini ya ulinzi.Hivi inaingia akilini kweli kwa mamlaka kuanza kumfuatilia mtoto tangu akiwa tumboni kwa minajili ya kumdhibiti?Na tuseme X-Ray (au vipimo vyovyote watakavyotumia kutambua tabia ya kichanga kilicho tumboni) ndio imeonyesha kuwa kichanga hicho kinaashiria kitakuwa jambazi au gaidi,watafanya nini?Kumshauri mama mwenye mimba aitoe,au mtoto atapelekwa jela mara baada ya kuzaliwa au ataandamwa na “surveillance cameras” tangu anatoka tumboni?

Na kama hiyo haitoshi,imefahamika majuzi kwamba serikali ina mpango wa kuwapatia polisi mamlaka ya “stop and search” (kumsimamisha mtu na kumpekua) kwa mtu yeyote yule anayeshukiwa kutaka kufanya ugaidi.Ni kweli kuwa ugaidi ni tishio sio kwa Uingereza pekee bali ulimwengu mzima lakini hiyo haihalalishi kuminya haki za binadamu.Wasiwasi wa watetezi wa haki za binadamu na baadhi ya wanasiasa ni kuwa uamuzi huo wa “stop and search” utawaathiri zaidi Waislam (ambao wengi wao wamekuwa wakilalamika kunyanyaswa na vyombo vya dola kwa kisingizio cha kudhibiti ugaidi) na wananchi wengine wenye asili ya nje ya nchi hii (kwa mfano watu weusi ambao mara kadhaa wamekuwa wakilalamika kwamba vyombo vya dola huwalenga wao zaidi kwenye “stop and search” ).

Kingine kilichowaacha watu mbalimbali wakiwa midomo wazi ni taarifa kwamba kampuni ya Endemol ambayo ni waandaaji wa kipindi maarufu cha runinga cha “Big Brother” inaanzisha kipindi huko Uholanzi ambapo washiriki watakuwa wakigombea figo la mwanamama mmoja aitwaye Lisa ambaye ameamua kujitolea kiungo hicho muhimu cha mwili kwa vile ana “terminal cancer” na hatarajii kuishi muda mrefu ujao.Katika kipindi hicho kilichopewa jina la “The Big Donor Show” watazamaji watakuwa wakituma ujumbe mfupi wa maneno (sms) kumpata mshindi miongoni mwa washiriki hao ambao wote wanahitaji figo ili waendelee kuishi.Tangu habari hizo zisikike,watu wengi wamejitokeza kulaani hatua hiyo ya Endemol huku wakiishutumu kampuni hiyo kuwa imekuwa na tabia ya kutengeneza vipindi vyenye dhamira ya kusababisha mkanganyiko kwenye jamii.Miongoni mwa washiriki wa “Big Brother” ya mwaka huu ambayo inaanza mwishoni mwa wiki hii ni pamoja na binti mcheza uchi (lapdance).Msimu uliopita mmoja wa washiriki alikuwa mwanaume mwenye jinsia mbili (transsexual),na huko Australia mshiriki mmoja wa Big Brother alijikuta amechanganyikiwa baada ya kutoka “jumba” la shoo hiyo na kutambua kuwa baba yake mzazi alifariki wakati mshiriki huyo akiwa mashindanoni lakini waandaaji “wakauchuna” (hawakumwambia),pengine kwa kuhofia kuwa angejulishwa kuhusu msiba huo angeamua kuachana na shinndano hilo.

Kimsingi,kuna ushindani wa hali ya juu kwa vyombo vya habari vya huku ughaibuni,pengine tofauti na huko nyumbani ambako majuzi niliwajulisha kuhusu webmaster wa gazeti moja ambaye haonekani kukerwa na namna anavyochelewa kuweka habari mpya kwenye tovuti yake.Hapa kuna ushindani ule unaoitwa “cut-throat competition” kwa “lugha ya kwa mama.”Sasa katika kuvutia watu baadhi ya waandaaji wa vipindi hujikuta wakienda mbali zaidi bila kujali athari za wanayofanya.Pia kuna ka-ugonjwa flani kwenye runinga kanakotokana na watazamaji wengi kupenda mno vipindi vinavyoonyesha maisha halisi (reality tv).Miaka michache iliyopita kituo cha runinga cha Channel 4 cha hapa Uingereza,ambacho kinasifika kwa vipindi vya utata,kilionyesha “laivu” mtaalamu mmoja akipasua maiti licha ya upinzani mkali kutoka kwa wanamaadili wa taaluma ya afya.Pia kumekuwa na vipindi mbalimbali vya “reality” vinavyoonyesha akinamama wakijifungua huko “leba.”

Yote hayo yanafanyika kwa jina la uhuru wa habari.Mgongano wa mawazo unajitokeza katika hoja kuu moja:nani wa kulaumiwa kati ya waandaaji wa vipindi hivyo vya kiuendwazimu au watazamaji wa vipindi hivyo?Ni sawa na ile hadithi ya makahaba na wateja wao.Laiti kukiwa hakuna wateja hakuna kahaba atakayekubali kwenda kuumwa na mbu kule Ohio (nasikia siku hizi kuna vijiwe lukuki vya madada poa),na kama hakuna makahaba maeneo hayo hakuna mtu atakayekwenda mitaa hiyo kununua ngono.Nadhani ni ile wachumi wanayoita mahitaji na ugavi (demand and supply).

Na huko nyumbani nako kuna mambo ya kushangaza vilevile.Nilisoma kwenye gazeti moja kwamba Katibu Mkuu flani mwanamama aliyeteuliwa hivi majuzi amedai kuwa baada ya MWAKA MMOJA ndio atakuwa na maelezo ya malalamiko yanayoikabili Wizara aliyoteuliwa kuiongoza.Kwanza nilidhani nimekosea kusoma nikidhani anamaanisha mwezi mmoja,lakini niliporudia kusoma tena nikahakikisha kuwa mwanamama huyo alikuwa anamaanisha mwaka mmoja wenye miezi 12.Nakumbuka kauli ya Rais Kikwete wakati anatangaza Baraza lake la Mawaziri kwamba uwaziri au unaibu waziri hausomewi.Kauli ya Rais ilikuwa na msisitizo kwa aliowateuwa kushika dhamana za uongozi wajibidiishe kusoma mazingira watakayoongoza na kuwatumikia wananchi kwa namna inayotarajiwa.Tofauti na mawaziri na manaibu wao,Makatibu wakuu wa wizara sio wanasiasa.Hawa ni wataalamu,na kwa vile kutafuta ufumbuzi wa matatizo kwenye wizara sio suala gumu kama kutafuta tiba ya ukimwi,inatarajiwa kuwa badala ya kujiwekea malengo ya mwaka mzima kuiweka sawa wizara husika,ni vema malengo hayo yangekuwa ya muda mfupi zaidi.

Mwisho ni kuhusu migogoro unaendelea kuliandama Kanisa la Anglikana huko Dodoma kutokana na sakata la ushoga.Hivi msimamo wa Askofu Mkuu wa Kanisa hilo Tanzania ni upi?Nauliza hivyo kwa sababu pindi migogoro huo usipopatiwa ufumbuzi mapema unaweza kulisambaratisha kanisa hilo.Nakubali kuwa Askofu wa Dayosisi ya Dodoma ana haki kama mwanadamu mwengine kuamini anachoamini kuhusu ushoga.Lakini sote tunafahamu kuwa haki inaambatana na sheria na taratibu,ndio maana japo kila mtu ana haki ya kwenda popote apendapo lakini akitia mguu Ikulu kudai ni haki yake kukaa hapo (ilhali anafahamu kuwa eneo hilo ni makazi ya Rais) basi atakumbana na mkono mrefu wa sheria.Na Askofu huyo ana uhuru wa kuamini kuhusu ushoga lakini sio kwenye kanisa ambalo linapinga suala hilo.Dayosisi hiyo iko Tanzania,na ushoga ni haramu kwa mila na desturi zetu za Kitanzania (japo akina kaka poa wapo mitaani).Dayosisi sio mali ya mtu mmoja bali jumuiya inayoungwanishwa na imani.Sasa huyu mtumishi wa kondoo wa Bwana anataka kuwaeleza nini waumini wake anaposhiria kushabikia ushoga?Nauliza tena,Askofu Mkuu wa Kanisa hilo anasemaje kuhusu hilo?Au anataka kuwaachia waumini wachukue sheria mkononi?Ifahamike kuwa Yesu hakuongoza ibada kwa msaada wa ulinzi wa polisi hata pale alipokwenda kuhubiri kwa wasiomkubali.Yanayotokea Dodoma ni ubabe ambao mwisho wake sio mzuri.Kama kondoo wa jinsia moja wana akili ya kutofanya tendo kati yao (yaani hakuna kondoo shoga) iweje basi mchunga kondoo wa Bwana (kiongozi wa dini) atetee vitendo hivyo vilivyoteketeza Sodoma na Gomora?

Mwisho kabisa,kocha mzungu wa Yanga,Micho,aache “longolongo” kwamba wachezaji wake hawafundishiki.Tatizo ni yeye wala sio wachezaji,kwani ni haohao waliokuwa wakifanya vitu vyao walipokuwa na Jack Chamangwana.Nadhani anaweza kuwasaidia sana Yanga kama watampa cheo cha ukatibu mwenezi au msemaji wa klabu kwa namna anavyopenda “kuchonga” kwenye vyombo vya habari.Matendo hukidhi haja maridhawa kuliko maneno.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.