1 Oct 2007

Kwanza,samahani nyingi kwa wapendwa wa blogu hii,maana niliadimika kidogo na hakukuwa na updates zozote.Ni vijimambo tu vilivyosababisha hali hiyo,lakini nimesharejea kamili-kamili.Badala ya title ya post kuwa Kulikoni Ughaibuni sasa tutakuwa na Mtanzania Ughaibuni.Sababu ya msingi ya kubadili jina ni ukweli kwamba makala zinazopatikana katika blogu hii ni kumbukumbu ya zile zinazotoka kwenye moja ya magazeti ya huko nyumbani.Kwa sasa makala zinazounda blogu hii zitakuwa zinapatikana kwenye gazeti la Mtanzania Jumapili badala ya gazeti la Kulikoni.Jina la blogu litaendelea kuwa hilohilo la Kulikoni Ughaibuni.Enjoy!!!
MTANZANIA UGHAIBUNI-1

Asalam aleykum,

Kwanza nianze na salam kwa wale wote waliojaaliwa “kuuona mwezi” na kwa sasa wanaendelea na funga ya Ramadhan.Salam pia kwa wale ambao kwa sababu moja au nyingine hawajaouna mwezi mpaka leo.Salam nyingi zaidi ni kwa wasomaji wote wa gazeti hili la Mtanzania Jumapili.Baada ya salam,nadhani ni vema nikajitambilisha maana hii ndio makala yangu ya kwanza kabisa katika gazeti hili maridhawa.

Jina la makala hii linashabihiana kabisa na maelezo yangu binafsi na mahali nilipo kwa sasa.Mie ni Mtanzania (halisi,Mndamba kutoka Ifakara) ambaye kwa sasa nipo masomoni huku Ughaibuni.Naomba kutamka mapema kwamba mie sio mwandishi wa habari kitaaluma,ila naipenda na kuiheshimu sana taaluma hiyo,na ni katika kuonyesha “mahaba” yangu kwa taaluma hiyo ndio nikaelekeza nguvu zangu kwenye uandishi wa makala.Nadhani wasomaji wengi wa magazeti wanafahamu kwamba makala inaweza kuandikwa na mwandishi aliyesomea kwenye fani hiyo,na pia inaweza kaundikwa na akina sie ambao kwa sababu moja au nyingine hatukubahatika kusomea.Yayumkinika kusema kwamba kinachomvutia msomaji ni ubora wa makala na sio sifa za kitaaluma za mwandishi.Kimsingi,makala zangu zitalenga kuhabarisha,kufundisha,kukosoa,kuchochea mijadala (pale inapobidi) na mwisho ni kuburudisha.Makala zangu ni za picha mbili katika moja,yaani kwa upande mmoja nitazileta kwa mtizamo wa Mtanzania aliye Ughaibuni (Mtanzania ambaye anajua alikotoka,anaijali lugha yake ya taifa,ana uchungu na nchi yake na sio mingoni mwa wale waliosahau kuwa nyumbani ni nyumbani),na kwa upande mwingine ni mtizamo wa Mtanzania kama Mtanzania,yaani hapo namaanisha kuwa nitachoandika kingebaki hivyohivyo hata kama ningekuwa Namtumbo,Kiberege,Nkasi au Temeke.Labda nifafanue kidogo katika suala hili la mitizamo ya makala zangu.Kwanza,zitakuwa na mambo ya Ughaibuni na pili zitakuwa na mambo ya huko nyumbani.Lakini,kuna nyakati haitakuwa directly (moja kwa moja) namna hiyo,bali nitajaribu pia kufanya comparative analysis (tuite mchanganuo linganifu) ambapo masuala,habari na matukio ya huku Ughaibuni yataletwa kwa namna ya kuyalinganisha na yale yanayoshabihiana na huko nyumbani.Hapo kutakuwa na mazuri tunayoweza kujifunza kutoka kwa hawa wenzetu na mabaya ambayo huko nyumbani tumebahatika kuwa nayo lakini hawa wenzetu wameyakosa.Enewei,mengi mtayaona katika makala zijazo.

Hebu tuangalie nini kinachoendelea hapa kwa “Kwin Elizabeti” (Uingereza).Kwa kawaida,kipindi hiki cha kuelekea kumalizika kwa majira ya joto (summer season) vyama vikuu vya siasa hapa hufanya mikutano yao ya mwaka.Tayari chama cha demokrasia ya kiliberali (Liberal Democrats) na chama tawala cha Labour wameshamaliza mikutano yao.Kwa Liberal Democrats “ishu” kubwa ilikuwa ni mwenendo usioridhisha wa chama hicho ambao kwa kiasi kikubwa umekuwa ukihusishwa na uongozi wa Sir Menzies Campbell.Wapo waliokuwa wanaomwona kiongozi huyo kama mzee asiye na jipya wala mvuto wa kukifanya chama hicho kipate umaarufu unaohitajika.Habari njema kwa Sir Campbell ni ukweli kwamba wengi wa wanachama wa chama hicho bado wanaelekea kuwa na imani na kiongozi huyo pengine kwa kuamini kuwa “utu uzima ni dawa” (Campbell ana umri mkubwa zaidi kulinganisha na viongozi wengine wa vyama vikuu vya siasa vya hapa).Kwa upande wa Labour ya Gordon Brown,mkutano mkuu haukuwa na “mbinde” yoyote hasa ikizingatiwa kuwa kura za maoni zinaonyesha kwamba Waingereza wengi wanaelekea kuridhishwa na utendaji wa Waziri Mkuu Brown na chama cha Labour kwa ujumla.Pengine kinachomsaidia Brown ni rekodi yake akiwa mwangalizi mkuu (kansela) wa uchumi wa Uingereza na “uzembe” wa Tony Blair katika siasa za kimataifa hususan uswahiba wake na Joji Bushi na “ishu” nzima ya Iraki.Lakini “kimuhemuhe” kikubwa kiko kwa chama cha wahafidhina (Conservatives) ambacho kimeanza mkutano wake Jumapili iliyopita.Kiongozi wa chama hicho David Camron ana mtihani mkubwa sana,sio tu kwa vile kura za maoni zinamweka nyuma ya Gordon Brown,bali pia ukweli kwamba mawazo yake ya kukibadili chama hicho kiendane na wakati yamekuwa yakipata upinzani mkali miongoni mwa wale “waliokunywa maji ya bendera” ya chama hicho.Cameron amekuwa muwazi kwa wahafidhina wenzie kwa kusema kuwa chama hicho kinaonekana mingoni mwa wengi kama kinachowakilisha “tabaka la wenye nazo” na “masapota” wake wakubwa ni wazungu weupe ilhali makundi ambayo yanakuwa kwa kasi nchini hapa kama watu weusi na wahindi wakikiona chama hicho kama cha kibaguzi.Cameron amekuwa akijitahidi kwa udi na uvumba kuonyesha kwamba uhafidhina haimaanishi kuwa tofauti na watu wa kawaida,lakini wakongwe katika chama hicho wanaonekana kutovutiwa na mwenendo wa kiongozi huyo kijana.Pia Cameron amewaeleza bayana wananchama wenzie kwamba pasipo dhamira ya dhati ya kukibadili chama hicho kwenda na wakati basi ni dhahiri kuwa sio tu hakitaweza kupata ridhaa ya kuongoza nchi hii bali pia kinaweza kujiandalia kifo chake siku za usoni.

Nadhani mazingira yanayokizunguka chama cha Conservative yanashabihiana kwa namna flani na chama tawala huko nyumbani,chama dume,CCM,japo tofauti ya wazi ni kuwa wakati Conservative ni chama cha upinzani hapa Uingereza,CCM ni chama tawala huko nyumbani.Lakini kabla sijaenda mbali naomba niseme yafuatayo.Miongoni mwa matatizo yanayozikabili siasa za nchi zetu za Kiafrika ni kwa wahusika kutopenda kuambiwa yale wasiyotaka kusikia (ikiwa ni pamoja na kuambiwa hivyo wanavyofanya sivyo inavyopaswa kuwa,yaani ndivyo sivyo).Kwa mantiki hiyo,ushauri wa maana kabisa kwa CCM unaweza kutafsiriwa na baadhi ya wakereketwa kuwa mtoa maoni ni mpinzani.Mie si mfuasi wa chama chochote,na japo nasomea siasa (za kimataifa) lakini huwa sioni aibu kusema kwamba naichukia siasa hasa kwa vile nadharia (theories) zinakinzana sana na vitendo kwenye dunia halisi tunayoshi.Angalau kwenye siasa za kimataifa (International Relations) ninapata fursa ya kuelewa kwanini kuna ubabaishaji au uimara kwenye siasa za eneo flani.Baadhi ya rafiki zangu huwa wananiuliza iwapo niliamua kusoma siasa ili baadae nije kuwa kiongozi lakini (baada ya kicheko) huwa nawafahamisha kuwa katika siasa za Afrika kinachomata sio digrii ya siasa bali “nyenzo” zitakazowafanya wapiga kura wawe tayari hata kung’oana macho kuhakikisha unapata madaraka.

Changamoto linalokikabili chama cha Conservative linashabihiana kwa namna flani na lile linaloikabili CCM kwa namna hii:Kwa mtazamo wangu,wapo wana CCM wanaogombea madaraka kwa vile wanaamini kuwa ni kwa kufanya hivyo ndio watapata nafasi ya kuwataumikia Watanzania wenzao.Lakini wapo pia wale ambao wanafahamu u-chama dume wa CCM na wanagombea madaraka ili kufanikisha tu mahitaji yao binafsi ikiwa ni pamoja na kujitengenezea mazingira mazuri ya kuendelea na madaraka hapo 2010.Lakini kundi la hatari zaidi ni lile la wasio na idea yoyote kuhusu siasa bali ustawi wa matumbo yao (na pengine nyumba ndogo zao).Hili kundi la tatu ni la kuogopwa zaidi ya lile la pili kwani wakati lile kundi la pili linajumisha watu wanaoweza kuwa wanagombea ili waendelee kuwa madarakani kama wanasiasa,hawa wa kundi la tatu hawajali sana kama watarejea madarakani kwa vile la msingi kwao ni wamechuma kiasi gani katika kipindi walicho madarakani.Changamoto kubwa kwa CCM ni kutengeneza utaratibu ambao utakihakikishia chama hicho kinaendelea kuwa chama cha wakulima na wafanyakazi (na wafanyabiashara ).Tofauti na wale wanaonekana kuwa na hofu kutokana na wafanyabiashara kuingia kwenye siasa,mie sina tatizo na kundi hilo alimradi lengo lao ni kuwatumikia wananchi (na pengine kuna umuhimu kwa bendera ya CCM kuongeza alama ya fedha kuashiria kuwa chama hicho ni cha wakulima,wafanyakazi na wafanyabiashara).Ikumbukwe kuwa hata wamachinga ni wafanyabiashara pia na miongoni mwao wapo wale wenye mwamko wa kisiasa sambamba na wakulima na wafanyakazi.

Naomba nimalizie kwa kuwa muwazi zaidi kwa hoja kwamba kwa namna flani “vimbwanga” vilivyojitokeza kwenye kinyang’anyiro cha kuwapata viongozi waCCM katika ngazi mbalimbali vimechafua jina la chama hicho tawala.Huo ni ukweli ambao kila mwenye mapenzi na chama hicho na uchungu na nchi yake atakuwa anaufahamu.Yayumkinika kusema kuwa baadhi ya hoja za vyama vya upinzani zinajengwa na CCM yenyewe kwani iwapo kungekuwa na “kuwekana sawa” katika masuala yanayogusa hisia za wananchi wa kawaida basi ni dhahiri kwamba akina Slaa au Kabwe wasingekuwa na hoja za kujaza maelfu kwa maelfu ya watu kwenye mikutano yao.Hii inaitwa na Waingereza kuwa ni “wake up call” au kwa lugha nyepesi ni changamoto.Kwa vile maslahi ya Taifa ni muhimu kuliko vyama vya siasa (vyama vya siasa huzaliwa,kukuwa na pengine kufa wakati nchi ni lazima iishi milele) basi naamini kuwa wenye mapenzi ya dhati na Taifa letu watanielewa na kufanyia kazi nilichoeleza.

Alamsik



0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.