25 Jan 2009


Hatimaye katika kukabiliana na wimbi la mauaji ya albino,Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameagiza leseni za waganga wa jadi wote zifutwe.Majuzi,Pinda alikaririwa akiagiza wananchi kuchukua sheria mkononi kwa kuwaua "wauaji wa maalbino".Hatua zote mbili zinaweza kutofanikiwa kwa vile inaelekea kana kwamba zimechukuliwa pasipo kufanyiwa utafiti wa kina.


Kuruhusu wananchi wafanye "jino kwa jino" dhidi ya wanaoua maalbino kunaweza kulipeleka Taifa mahala pabaya.Taasisi pekee yenye mamlaka ya kuhukumu ni mahakama zetu,na hizo ndio zinazoweza kuhakiki makosa halasi tofauti na majungu,chuki,visasi,nk na haki inatarajiwa kuwa imetendeka pindi hukumu itapokuwa ya kifo au mshtakiwa kuachiwa huru kulingana na ushahidi uliowasilishwa mahakamani.Hilo haliwezekani katika "mahakama za jino kwa jino mitaani".Si ajabu watu waliokosana kwa sababu zao binafsi wakishia kupigana mapanga kwa kisingizio cha "kudhibiti mauaji ya maalbino".Ikumbukwe kuwa ni rahisi kuruhusu uvunjifu wa sheria lakini ni zaidi ya vigumu kurejesha heshima na utiifu kwa sheria.


Tuje kwa hili la kufuta leseni za waganga wa jadi.Je amri hii inamaanisha ni marufuku kwa mtu yeyote kujihusisha na uganga wa jadi au...?Sijaelewa vizuri hapo lakini nahisi inamaanisha hivyo kwani katika hali ya kawaida,kufanya shughuli inayohitaji leseni pasipo kuwa na leseni husika ni uvunjifu wa sheria.Swali la kwanza,hivi ni waganga wa jadi wangapi wenye leseni (tukiachana na hao Maprofesa wanaojitangaza kwenye magazeti kuwa wanatibu ukimwi,wanawezesha kufaulu pasipo kusoma,na miujiza mingine)?Nauliza hivyo kwani haitaleta mnaana yoyote kumfutia mtu leseni ambayo hajawahi kuwa nayo hata siku moja.Swali la pili,je utekelezaji wa amri hiyo utasimamiwa vipi?Polisi watazungukia mganga mmoja hadi mwingine nchi nzima kuhakikisha kuwa hafanyi uganga?
Swali la tatu,je tumefikia hatua ya kufanya maamuzi kwa kigezo cha "samaki mmoja akioza basi wote wameoza"?Nauliza hivyo kwani tafsiri ya moja kwa moja ya kuwafutia leseni masangoma ni kwamba wao ndio wahusika muhimu katika suala la mauaji ya maalbino.Hii "overgeneralization" inatoka wapi?Mbona wale wazembe wa Muhimbili walipompasua kichwa mgonjwa wa goti na wa goti akapasuliwa kichwa walioadhibiwa ni madaktari husika tu na sio kada nzima ya madaktari hapo Muhimbili au nchi nzima?Au mbona ilipobainika kwamba kuna uhuni umefanyika pale BoT kwenye ishu ya EPA,aliyefukuzwa kazi ni Ballali pekee na wengine wameendelea kuwa madarakani hadi leo?Au mbona aliyekuwa balozi wetu huko Italy alipokumbwa na tuhuma za ubadhirifu wa fedha za umma haikupelekea kutimua mabalozi wote?Sasa iweje "uhuni" wa baadhi ya waganga wa jadi upelekee hukumu kwa wote wanaohusika kwenye taaluma hiyo (na yayumkinika kusema kuwa wengi wao-hususan vijijini-ni waadilifu katika kazi yao)?


Naomba nisisitize kwamba hapa simaanishi two wrongs make a right.Hapana,najaribu kuangalia approaches za nyuma katika kukabiliana na matatizo mbalimbali na namna zinavyokinzanna na hii ya ku-revoke leseni za waganga wa jadi.


Kwa wanaofahamu umuhimu wa tiba asili katika jamii husasan katika kipindi hiki cha uchangiaji wa gharama kwenye public health facilities,ni dhahiri hatua ya kuwafutia leseni waganga wote wa jadi itaathiri Watanzania wengi wanaotegemea huduma hizo (aidha kutokana na imani,nature ya maradhi yao au uwezo duni katika kumudu gharama za huduma za afya hospitalini).


Japo ni muhimu sana kutafuta ufumbuzi wa haraka kukomesha mauaji dhidi ya maalbino,ni muhimu zaidi kutumia common sense and viable approaches kuliko hatua ambazo pamoja na nia zake nzuri zinaweza kutuletea matatizo zaidi.Tukirihusu sheria zivunjwe kwa kuruhusu kuua wanaoua maalbino (badala ya kuwafikisha kwenye vyombo vya dola) basi tusishangae pindi baadhi ya wananchi watakapoamua kuchukua sheria mkononi dhidi ya mafisadi,kwa mfano,badala ya kusubiri kesi zilizoko mahakamani,ripoti za tume,nk

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.