26 Jun 2009


Kwa mujibu wa MZEE WA CHANGAMOTO,Hasheem Thabeet amenyakuliwa na klabu ya mpira wa kikapu ya Memphis Grizzlies katika draft ya NBA.

Hii ni miongoni mwa njia mwafaka-na nafuu-za kuitangaza Tanzania.Kila la kheri Hasheem.Mafanikio yako ni zaidi ya kufanikiwa kimichezo,umeingia kwenye orodha ya vitambulisho vya Tanzania kama vile Mlima Kilimanjaro,madini ya Tanzanite (japo mafisadi wamepania kuyamaliza kama walivyomaliza dhahabu ilivyo huko Tulawaka),Hifadhi ya Selous na vivutio vinginevyo.Kuna cha zaidi kuhusu mafanikio yako.Umevunja "utamaduni" wa Kitanzania wa ku-settle for less.Angalia timu yetu ya taifa,kwa mfano.Tumekuwa na Maximo kwa muda sasa,na wajuzi wa michezo wanatuambia tumepiga hatua.Kupiga hatua kwa kutoka sare na Senegal?Angalia Simba na Yanga,kila msimu wanahangaika na "wachezaji wa kimataifa",lakini huhitaji kuwa mtaalam wa soka kumaizi kuwa ma-pro" hao ni wababaishaji tu na hawajasaidia kuzifanya klabu hizo zitambe katika anga za soka la kimataifa (na tunaambiwa kocha wa Yanga ni profesa wa soka!Lakini msimu wa pili huu hakuna kombe la kimataifa na wana-Yanga wameridhika,sio na mafanikio ya klabu yao bali kuwa na kocha mgeni "profesa wa soka").Angalia baadhi ya mitazamo yetu.Shangwe na vigelegele tukisikia Zeutamu kakamatwa ilhali majambazi wa Kagoda bado wanapeta,na huku tukizugwa kuwa eti ufisadi wa Meremeta na Tangold ni siri za taifa! (Na kweli ni siri maana ni nadra kwa wizi kufanyika hadharani).

Mafanikio yako yanaweza kuwa chachu kwa Watanzania wengine kuondokana na unyonge wa kifikra kwamba kila baya linalotusibu ndio destiny yetu.Na ni kwa namna hiyo ndio mafisadi wanazidi kutufisadi kwa vile wanatambua unyonge na udhaifu wetu wa kukubali matokeo kirahisi.

Hongera sana,Hasheem.Sote tunajivunia jina lako.

1 comment:

  1. Tupo pamoja nawe Hasheem, Mungu akufanikishe kwa jina lako kisha la taifa lako (letu).

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.