26 Jun 2009

Ifakara katika picha niliyopiga mwezi Mei mwaka jana.

Mji una neema ya ardhi yenye rutuba inayokubali kilimo cha mpunga,mahindi,na mazao mengine lukuki.Ungetegemea mapinduzi ya kijani yaanzie sehemu kama hizi lakini kama kawaida ya wanasiasa wetu,maneno meeengi huku vitendo vikiishia kwenye michakato,mikakati,vipaumbele,semina elekezi na ubabaishaji mwingine kama huo.Habari hii hapo chini licha ya kunigusa kutokana na ukweli kwamba wilaya ya Kilombero ndio nyumbani,pia inawakilisha matatizo yanayowakabili mamilioni ya Watanzania wanaotegemea kilimo kama njia pekee ya kuwawezesha kuishi.Isome kwanza:

Kilombero, Ulanga wahofia njaa

na Joseph Malembeka, Kilombero

BAADHI ya
wananchi wanaoishi katika wilaya za Kilombero na Ulanga mkoani Morogoro wameiomba serikali kuingilia kati ununuzi holela wa mazao ya chakula unaofanywa na walanguzi sasa.

Ombi hilo limekuja kutokana na ongezeko kubwa la wafanyabiashara kuingia wilayani humo na kununua kwa kasi mpunga ukiwemo uliovunwa na uliopo mashambani.

Wakizungumza na Tanzania Daima juzi, John Lyapi na Selemani Kinana walisema kama serikaliikifumbia macho suala hilo kuna hatari ya wakazi wengi wa wilaya hizo kupata baa la njaa mwaka huu.

Lyapi alisema kwa sasa walanguzi hao wamevamia zaidi katika tarafa za Malinyi na Mtimbira na kuwarubuni wananchi kuwauziampunga wao kwa sh 5,000 kwa debe na huku wakiwafuatilia hadi mashambani.

Alisema kutokana na wengi wa wakulima kwa kipindi hiki wanatokea mashambani inawawia vigumu kukataa kupokea fedha hizo, kwani wengi wao huwa kama wanaanzamaisha mapya majumbani baada ya kuhamia mashambani kwa muda mrefu.

Naye Kinana mkazi wa Kilombero alisema kila kukicha bei ya mazao ya chakulaimekuwa inapanda na kushuka kutegemeana na kuongezeka kwa walanguzi hususanwakubwa.

Alisema endapo serikali itakabiliana kikamilifu na walanguzi haoitasaidia kuondoshwa chakula kingi wilayani humo na kunusuru janga la njaa.

Kwa mujibu wa wakuu wa wilaya hizo Evarist Ndikilo (Kilombero) na DkRajabu Rutengwe (Ulanga) kwa nyakati tofauti walisema tayari halmashauri zimeagizwa kuwatangazia wananchi kuacha mtindo huo.

Walisema mbali na kupiga marufuku kwa wananchi kuuza vyakula pia wanakusudia kuweka sheria itakayowasaidia, iliwaweze kujikwamua na janga la njaa kwa kutouza vyakula hivyo.

CHANZO: Tanzania Daima

Mkuu wa wilaya ya Kilombero anaweza hata kuamuru jeshi la polisi likamate wanaouza chakula,lakini haitokuwa ufumbuzi wa tatizo hilo.Bottom line is,watu wanauza akiba ya chakula chao ili kukabiliana na ugumu wa maisha.Unadhani kuna mkulima anayependa kula mbegu?

Hivi kwanini hizo trilioni moja na ushee zilizotengwa kukabailiana na msukosuko wa uchumi zisiangalie walalahoi kama hawa?Katika mpango huo ambao bado nina wasiwasi unaweza kuishia kuwa-bailout mafisadi kama si kuzua EPA nyingine,wakulima wa kawaida wamepewa kisogo licha ya hadithi za KILIMO KWANZA.

Ukitembelea Ifakara katika kipindi hiki cha mavuno utapata picha moja ya kusikitisha.Wakulima wa mji huo wanatumia takriban robo tatu ya mwaka kulima mpunga (na kilimo cha mpunga kiko very demanding huku kikitegemea kudra za Mungu kwenye hali ya hewa).Baada ya mavuno,mji huo unafurika wanunuzi wa mpunga na mchele,huku wengine wakiufuata hukohuko mashambani.Kwa vile muda huu wengi wa wakulima huwa hoi kiuchumi,bei ya mpunga na mchele huwa ni karibu na bure.Pia baadhi ya wakulima wenye mahitaji mengine muhimu kama vile nguo,sukari,nk huamua kupokea bidhaa hizo badala ya fedha (barter trade) alimradi siku ziende mbele.Na muda si muda,wakulima hao hujikuta wameuza hadi mbegu na kurejea mahala palepale walipoanzia: hawana hela,hawana chakula.

Tuna wizara ya wajibu wa kushukulikia kilimo,na tuna wizara yenye wajibu wa kuwasaidia wakulima kupata masoko ya kuaminika ya mazao yao.Pia tuna wizara inayowajibika na masuala ya ushirika.Kwa makusudi,wizara hizi zimebaki majina tu japo utasikia zinatengewa mamilioni kama sio mabilioni,sio tu kwa ajili ya "kuleta ufanisi" bali pia huduma za ukarimu-chai,chakula,nk.

Tuna takriban Watanzania wenzetu 50 wenye wadhifa wa uwaziri au unaibu waziri.Sehemu kubwa tu ya fedha za walipa kodi inatumika kuwahudumia waheshimiwa hawa.Lakini ni ukweli usiopingika kuwa utendaji kazi wao ni chini ya kiwango.Walikabidhiwa dhamana ya kutekeleza kaulimbiu ya MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA lakini yayumkinika kuhitimisha kuwa sanasana wamefanikiwa kujitengenezea maisha bora wao wenyewe na "wafadhili wao wa kisiasa".


Kwa mmiliki wa makazi hayo pichani juu,habari za Maisha Bora kwa Kila Mtanzania ni kama utani mbaya kwake.Japo amezungukwa na ardhi kijani yenye rutuba,hajui jioni itakuwaje let alone hiyo kesho au msimu ujao wa kilimo na mavuno.Ukimwambia kuwa kuna kaulimbiu mpya ya
KILIMO KWANZA anaweza kukushushia ngumi!

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.