21 Sept 2011

Kama kuna hoja inayotawala zaidi kuliko nyingine kwenye blogu na maandiko mengi ya wengi wa mabloga wa kike wa Kitanzania ni hii ya hisia kwamba WANAUME WA KITANZANIA SI WAAMINIFU KWENYE MAHUSIANO.Ninaposema inatawala simaanishi kuwa huo ndio mtizamo wa mabloga hao bali ni kitu kinachojitokeza mara nyingi pengne zaidi ya vitu vingine,hususan kwenye sehemu za kutolea maoni (comments).

Utakuta dada mmoja anaomba ushauri kwa wenzie kuhusu mwenza wake ambaye aidha anamhisi kuwa si mwaminifu au amemsaliti kwenye uhusiano wao.Ukiweka kando ushauri atakaopewa,wengi wa wachangiaji wa kike hukimbilia kuhitimisha kuwa tatizo la msingi ni "ukweli kwamba wanaume wa Kibongo si waaminifu",huku wengine wakienda mbali zaidi na kudai "wanaume wetu wa Kibongo wanatembea wakiwa na zipu zao wazi-kwa maana ya kuwa tayari kukamata chochote kile kitakachokatiza mbele yao".

Katika hatua hii siwezi kusema hisia hizo ni sahihi au la ila nisichokubaliana na hitimisho la jumla (blanket conclusion) kwamba WANAUME WOTE WA KITANZANIA SI WAAMINIFU.Sijui kama wanaohitimisha hivi huwa wanajaribu angalau kutafakari kidogo kuhusu baba zao,maana nao pia ni wanaume wa Kitanzania.Hatari kubwa ya kuhitimisha jambo jumla jumla ni kuwaingiza hata wale wasiohusika.Wengi wetu tunafahamu jinsi baba zetu walivyo waadilifu kwa mama zetu hadi kufanikiwa kutufikisha hapa tulipo.Japo si wote lakini kwa kiasi kikubwa baba zetu-hususan wale waliokula chumvi nyingi-wamejitahidi kadri wawezavyo kuwa waaminifu kwa mama zetu.

Kwa vile mada hii ni ndefu na ili kuijadili kwa ukamilifu inahitaji kitabu kizima basi niifupishe kwa,kwanza,kuangalia sababu za kitaaluma kwanini watu wana-cheat.Naomba ieleweke kuwa hata kwenye kusaka sababu kwenye masuala mengine ni nadra kupata sababu timilifu kabisa kwa sababu kuna vigezo vingine vinavyoathiri kila sababu,kwa mfano mazingira,umri,uchumi,malezi,nk

Hata hivyo,tafiti mbalimbali za mahusiano ya kimapenzi zinataja sababu zifuatazo kuwa 'maarufu' zaidi katika kuelezea kwanini watu wana-cheat

KULIPIZA KISASI:

Sie Wakristo tunafundishwa kwenye Agano Jipya kuwa ukipigwa kofi shavu la kushoto basi geuza na shavu la kulia.Hii inapigia mstari umuhimu wa kutolipiza kisasi.Lakini hata kwenye Maandiko hayo Matakatifu haikuwa hivyo siku zote.Katika Agano la Kale,mafundisho yalikuwa ni JICHO KWA JICHO na JINO KWA JINO.Kwenye stadi za dini inafahamika kama 'sheria ya kulipiza kisasi' (law of retaliation) na 'sheria ya mapatano' (law of reconciliation).Katika poetic justice 'jino kwa jino' inaweza kulinganishwa na kile kiitwacho adhabu ya kioo (mirror punishment),yaani-kwa kifupi-malipizi kwa kutenda kosa.Msingi hapa ni kwamba tendo jema huzawadiwa na tendo baya huadhibiwa.

Kwa hiyo,kwa vile mwenza wa kiume au wa kike ame-cheat basi yule aliyekuwa cheated anaamua kulipiza kisasi kwa ku-cheat pia.Jino kwa jino,au tit-for-tat.Lakini hitimisho la kisomi ni kwamba mara nyingi kulipiza kisasi hakusaidii sio tu kuleta ufumbuzi wa tatizo bali pia hata kuondoa maumivu ya kusalitiwa kwenye penzi.

Unajua kuna tofauti kati ya kufanya jambo pasipo msukumo wowote na kufanya jambo kwa vile kuna msukumo flani.Mwanaume au mwanamke anayeamua tu ku-cheat kwa vile anajiskia kufanya hivyo ana tofauti na yule aliyelazimika ku-cheat kwa sababu tu anataka kumkomoa flani.Tofauti hii ni sawa na ile ya binti anayefanya ukahaba kama hobby na yule anayefanya kwa vile anahitaji fedha au hana njia nyingine ya kipato zaidi ya kuuza mwili/utu wake.Kufanya jambo kwa uhuru ni,well,kuwa huru (hata kama ni makosa) wakati kufanya jambo kutokana na kusukumwa ni sawa na utumwa.

Anyway,hapa tunataja sababu za ku-cheat na sio kuhukumu kuwa anaye-cheat kwa sababu flani yuko sahihi au la.Twende sababu ya pili

KAMA KIPO KITUMIE

Kuna wenzetu wanaoamini kwamba kama nyama iliyopo kwingineko ni ya kupendeza,tamu,isiyo na sumu,na inapatikana,then kwanini isiliwe?Watu wa aina hii wanaamini kuwa wanachofanya ni kula kilicho bora,na ambacho kinapatikanika (available/accessible).Hawana uchungu kwa kufanya hivyo kwa vile wanaamini kuwa maridhio ya nafsi ni muhimu zaidi kuliko uhalali au ukosefu wa uhalali wa tendo husika.

Nadhani ushaskia misemo kama 'cha muhimu ni kupata fedha,jinsi ilivyopatikana sio muhimu'.Au wengine wanakwenda mbali zaidi na kudai kuwa watu wenye kuifaidi zaidi dunia ni wale waisoongozwa na 'hiki ni halali na hiki si halali'.Ishu kama uadilifu,uaminifu,nk sio muhimu kwao.

Katika kundi hili kuna wale tunaoweza kuwaita waathirika wa Columbus Syndrome (tafsiri ya Kiswahili ni ngumu lakini turahishishe kwa kuita 'ugonjwa wa kiu ya uvumbuzi kama Christopher Columbus.Yaani tamaa ya kujua mambo zaidi ya maelezo sahihi yanavyoelezea mambo hayo).Unakuta mwanaume 'anafukuzia sketi' kwa vile tu anataka kuonja sehemu za siri za mwanamke huyo.Haijalishi kama ana mwenza au hana,bali la muhimu kwake ni kwamba A sio B,na nyama ya mbuzi si ya ng'ombe,na japo maharage na kunde zote ni mboga lakini maharage si kunde.Hawa wapo katika kile kinachoitwa kwa kimombo kama taste-testing (kujaribu ladha).

Kwenye kundi hili pia kuna wale wanaotaka kupima kama ujuzi wao wa kufukuzia sketi bado upo,licha ya ukweli tayari wana wenza nyumbani.Kwa akina dada,inawezekana ni kupima kama "kama nilimudu kum-cheat yule bwege mwaka juzi na hakujua mpaka tunaachana kwanini nisijaribu tena safari hii?"Ni sababu zinazoweza kuonekana kama za kupuuzi lakini kumbuka kuwa mara nyingi wanaofanya upuuzi hawana muda wa kutafuta sababu.Na hata ukiwahoji wakupe sababu basi majibu watakayokupa yanaweza kukutibua kuliko upuuzi waliofanya.

Kufupisha maelezo,wanao-cheat kwa mujibu wa sababu hii wanafanya hivyo kwa vile,well,kama kipo kitumie.

WASIOTOSHEKA

Unakumbuka ule wimbo wa zamani wenye maneno "ee jamani mwanadamu hatosheki,hata ukimpa nini milele hataridhika...ukimpa kumi atataka mia..."Well,si kweli kwamba kila mwanadamu hatosheki bali ukweli ni kwamba kama ilivyo kuna wenzetu ni wepesi kutosheka,wenzetu wengine kamwe hawatosheki.Tuchukulie mifano halisi.Katika kusaka ufumbuzi watatizo la rushwa katika Mamlaka ya Mapato Tanzania ikashauriwa mishahara minono na marupurupu mazuri inaweza kusaidia kuondoa vishwawisho vya watumishi wa taasisi hiyo kudai na kupokea rushwa.Seriakli ikaridhia kufanya marekebisho katika muundo wa mishahara ya watumishi wa taasisi hiyo.Sihitaji kukwambia kuwa TRA ni miongoni mwa taasisi zilizobobea kwa rushwa,pengine mara dufu ya ilivyoluwa zama za mishahara kiduchu.

Kwanini watu hawa waendelee kudai na kupokea rushwa ilhali wanalipwa mishahara minono kabisa?Well,jibu rahisi ni tamaa.Lakini jibu jingine linaweza kuwa mazowea.Kuna msemo wa Kiingereza usemao "vyovyote utakavyomtunza,mbwa mwitu hawezi kuwa mbwa".Nenda porini,kamata mbwa mwitu,mpe kila aina ya matunzo kama mbwa wa kawaida,lakini kama hatoishi kukung'ata basi atatoroka na kurejea porini.Wanasema kunguru hafugiki,na samaki yake maji.Ukimtoa samaki majini,basi umemuua.Period.

Kwahiyo kama ambavyo kuna watu hawatosheki na fedha wanazopata (kwa mfano mafisadi serikalini ambao wanalipwa mishahara mikubwa kuliko mahitaji yao) basi pia kuna watu hawatosheki na tendo la ndoa.Hata mkewe/mwenza wake ampe uroda kiasi gani bado atahitaji nyongeza.Na kuna akinadada hata apewe-ashakum si matusi- 'mabao' mangapi bado atahitaji zaidi.

Katika sababu hii kuna marejeo ya sababu iliyopita ya 'kama kipo tumia' kwa maana ya kama una njaa na chakula kipo basi kula,na kama ukienda kwingine na bado unajiskia hamu ya kula endelea kula.Ma-Tiger Woods hawa wa kike na kiume wanahitaji zaidi na zaidi just like wale wala rushwa wa TRA.

Kwa wengine hili ni kama tatizo la kiafya linalohitaji tiba za kisayansi.Kabla ya tiba hiyo,dawa pekee ya kukabiliana na 'hamu isyoisha ya kula au kuliwa uroda' ni 'kula au kuliwa uroda' zaidi na zaidi.Ni mithili ya walevi ambao njia pekee ya kumudu maisha ni pombe.

Kwa bahati mbaya,watu wa kundi hili wanaweza kujikuta matatizoni zaidi ya kuharibu mahusiano na wenza wao.Yaleyale ya simba akikosa nyama anaweza kula majani,basi si ajabu kwa watu wa kundi hili kujikuta wakiamua liwalo na liwe na kudiriki hata kufanya tendo la ndoa na watoto wadogo,watu wa jinsia moja na wao,kubaka aua hata kufanya tendo la ndoa na midoli.Kwao,tendo la ndoa ni sawa na oksijeni,pasipo hiyo ni kama wanaelekea kukata roho.

Namkumbuka kijana mmoja enzi hizo za ujana,mitaa ya Kinondoni.Kila wikiendi alikuwa anakwenda Ambassador Plaza (Gogo Hotel) 'kukamatia',na kwa vile sehemu hiyo ilikuwa inapendelewa na mashoga basi alipokuwa akikosa binti wa kulala naye basi 'anakamatia' shoga.Na huyu kijana alikuwa na girlfriend mrembo kupita maelezo.

Na kuna mama mmoja niliyewahi kufanya nae kazi sehemu fulani ambayo mshahara,posho na fedha kwa ujumla ilikuwa sio tatizo.Lakini licha ya kuwa na mume mwenye uwezo wa kifedha na mwenye haiba ya kutamanisha mwanamke yeyote yule,mama huyo alikuwa yuko radhi kulala hata na wafagizi hapo ofisini,baada ya kuwamaliza mabosi wenzie na wafanyakazi wa kada ya kati.Wambeya walikuwa wanadai kuwa mama huyo 'alipokuwa kwenye siku zake' alilazimika kufanya tendo la ndoa kinyume cha maumbile alimradi akidhi addiction yake.

KITULIZA ROHO

Wakati mwingine mwenza hujikuta anashawishika ku-cheat kutokana na mapungufu yanayozidi kuathiri mahusiano yake na mwenzie.Naomba tuelewane hapa.Sio kama nahalalisha ku-cheat bali natoa moja ya sababu zinazoweza kumfanya mtu a-cheat.Ikumbukwe kuwa wizi ni wizi tu,hakuna wizi halali.Mtu anayekutwa na hai ya kuua,kwa mujibu wa sheria zetu,adhabu yake ni kunyongwa hadi afe.Hakuna tofauti kati ya aliyeua mtu mmoja na aliyeuwa watu 10,wote ni wauaji.

Kadhalika,anaye-cheat kwa vile mumewe/mkewe hamridhishi,hana tofauti na yule wa kundi la kwanza au la pili au la tatu hapo juu.Wote wame-cheat,na kama kuna adhabu dhidi ya ku-cheat,wote wataadhibiwa kama cheaters,period!

Inaelezwa kuwa baadhi ya wanawake wanapoolewa wanaweza kujikuta wanajisahau kuhusu vitu vilivyofanya waume zao watamani kuwaoa in the first place.Matokeo yake ndoa inakuwa dull,tendo landoa linakuwa kama kutimiza wajibu tu kama sio kutokuwepo kabisa.Nasisitiza kuwa ku-cheat sio ufumbuzi lakini kwa mhusika hiyo ni excuse tosha ya kwenda nje ya uhusiano.

Wanaume pia,iwe kwenye ndoa au mahusiano tu kati ya boyfriend na girlfriend,wanadaiwa kuwa wakati mwingine wakishapata wanachohitaji wanawachulia wenza wao for granted.Zawadi za 'enzi za kutongozana'-maua,perfume,kadi,sim/sms mfululizo,nkzinaanza kufifia kadri umri wa uhusiano unavyozidi kuongezeka.

Again,naomba kusisitiza kuwa hii sio kwenye kila uhusiano bali hutokea,wewe na mimi tumeshaskia simulizi za aina hii mara kadhaa.

Mwenza anajikuta yupo kwenye uhusiano ambao ni 'uhusiano jina',hakuna mahaba,hakuna msisimko,na pengine kibaya zaidi,hakuna tendo la ndoa,au hata kama likiwepo ni la 'kizushi' tu.Kuna wanaoanza kwa kutishia ku-cheat-si kwa maneno bali vitendo.Kwa mfano,binti ambaye baada ya kuwa na mwenza wake alianza kubadilisha uvaaji wake 'wa utatanishi' (kwa lengo la kuepusha wasumbufu mtaani) anaamua kurejea kwenye uvaaji huo ili kumpelekea ujumbe mwenza wake kuwa 'kama ulinitamani uliponiona katika mavazi haya siku hizo,basi hata sasa naweza kutamaniwa na wengine'.Kwa bahati mbaya,'tisha toto' hii inaweza kupelekea madhara yasiyokusudiwa.Kwamba akajitokeza mdau akaonyesha interest ya kutosha na hatimaye mwanadada akashawishika kutembea naye 'mara moja tu' (na hatimaye mara moja hiyo kuzaa mara ya pili na kadhalika na kadhalika).

Kuna wengine hawana hata muda huo wa kufikisha ujumbe na huamua kuingia kwenye hatua ya ku-cheat moja kwa moja.Hoja ya msingi kwao ni kwamba kama huwezi kunipa ninachohitaji basi kuna wengine w3anaweza kunipa.Na kwa vile mie na wewe sio dada na kaka basi sioni umuhimu wa kuishi na mwanaume au mwanamke ambaye hanitimizii mahitaji yangu ya kimahusiano.

Kama nilivyaondika awali,ningependa sana kuingia kwa undani na kujadili njia mwafaka za kusaka suluhisho kwa kila sababu ya ku-cheat niliyotaja hapa lakini kwa leo naomba niishie kwenye kutaja sababu tu,kabla ya kuhamia kwenye mada ya msingi ambayo ni hoja ya wanawake wengi kuwa Wanaume wa Kitanzania si waaminifu.

UCHAMBUZI

Kwa kifupi kabisa,naomba nikuachie msomaji uondoe MWANAUME WA KITANZANIA kwenye kila sababu niliotaja hapo juu na uweke MWANAUME WA KIKENYA,KIMAREKANI,KIINGEREZA au MWANAUME WA NCHI YOYOTE ILE.Kisha angalia kama kuna mwanaume wa uraia flani hawezi ku-fit kwenye sababu hizo hapo juu.

Kisha jaribu tena kuondoa MWANAUME (awe wa KITANZANIA au wa nchi nyingine) na uweke MWANAMKE WA KITANZANIA.Je hakuna mwanamke wa Kitanzania anayeweza ku-cheat kwa sababu tu ANALIPIZA KISASI (at least according to her)?Je hakuna mwanamke wa Kitanzania anayeweza ku-cheat kwa sababu tu anaamini KAMA KIPO KITUMIE?Au je hakuna mwanamke wa Kitanzania anayeweza ku-cheat kwa vile tu HATOSHEKI na anachopewa na mwenza wake?Na mwisho,je hakuna wanawake wa Kitanzania wanaoweza ku-cheat kwa minajili ya KUTULIZA ROHO kutokana na mapungufu yanayokabili mahusiano na wenza wao?

HITIMISHO:

Kwa kuangalia sababu hizo za kitaaluma as to kwanini wenza wanaweza ku-cheat,ni wazi kuwa,kwanza si mwanaume tu anayeweza kuwa na sababu (hata kama haikubaliki) ya ku-cheat.Na pili,si wanaume wa Kitanzania tu wanaoweza ku-apply sababu hizo wanapo-cheat,au kwa lugha nyingine,si wanaume wa Kitanzania tu wanao-fit explanations/sababu nilizobainisha hapo juu kuhusu kwanini watu wana-cheat.

Kwahiyo basi,natumaini makala hii inaweza kutoa jibu kwa niaba ya Wanaume wote wa Kitanzania wanaotuhumiwa kuwa si waaminifu katika mahusiano.Jibu ni kwamba si wanaume wa Kitanzania pekee,na si wanaume pekee,wanaoweza kuwa nasababu moja au nyingine ya ku-cheat.Makala hii haijaribu kwa namna yoyote kuhalalisha cheating kwa vile kama nilivyobainisha hapo mwanzo,ku-cheat si ufumbuzi wa tatizo lililopelekea mtu a-cheat.Faraja ya muda mfupi-iwe ni kulipa kisasi,kukidhi utafutaji ladha mbadala nje,kutibu kiu ya ngono au kujiliwaza-haiwezi kuwa ufumbuzi wa kukarabati uhusiano unaokwenda mrama.

Siku ya siku nitajadili njia mwafaka za kuboresha uhusiano na kuondoa fursa ya ku-cheat.

Inatosha kwa leo

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.