7 Mar 2014

MWISHONI mwa wiki iliyopita kulijitokeza malumbano makali, hususan katika mtandao wa kijamii wa Twitter, kuhusu suala la ushoga.
Sina hakika mjadala huo ulianza vipi lakini ninadhani kwa upande mmoja ulichochewa na sakata linaloendelea kati ya serikali ya Uganda na baadhi ya nchi za Magharibi baada ya Rais wa nchi hiyo, Yoweri Museveni, kusaini muswada unaopiga marufuku ushoga kuwa sheria inayoambatana na adhabu kali. Kwa upande mwingine, nahisi mjadala huo ulichangiwa na majadiliano yanayoendelea katika Bunge la Katiba huko Dodoma, ambapo suala la haki za mashoga limejichomoza.
Kwa upande wa Bunge la Katiba, kuna tuhuma kuwa ‘ajenda ya ushoga’ imeletwa makusudi kwa minajili ya kuepesha (divert) mtizamo wa Watanzania katika ‘masuala ya msingi zaidi’ yanayopaswa kujadiliwa katika Bunge hilo maalumu.
Lakini pengine kabla sijaingia kiundani katika mada hii ni vema nikaweka bayana msimamo wangu kuhusu suala hili la ushoga. Huko nyuma niliwahi kuandika makala iliyozungumzia mjadala wa ushoga, makala iliyobeba kichwa cha habari “Tatizo ni unafiki wetu, sio ushoga.”
Hoja kubwa ya ‘wapinzani wa haki za mashoga’ ni kwamba suala hilo haliendani na mila na desturi zetu. Lakini kabla ya kwenda mbali, hivi hizo mila na desturi zetu ni zipi hasa? Mara kadhaa tumekuwa tukiwalaumu ‘wazungu’ kwa kuiangalia au kuizungumzia Afrika kana kwamba ni kijiji kimoja kikubwa kinachoundwa na familia moja kubwa. Wengi wetu tumekuwa mahiri kuwakumbusha ‘wazungu’ kwamba Afrika ni mkusanyiko wa mataifa zaidi ya 50, na ndani ya mataifa hayo kuna makabila lukuki yenye mila na desturi tofauti.
Sasa tukirejea kwa Tanzania yetu, hivi ‘mila na desturi za Kitanzania’ ni zipi hasa? Naomba ieleweke kwamba sikatai kwamba tuna mila na desturi bali ninapata shida kuelewa hizo ‘mila na desturi za jumla’ zinazofuatwa na kila Mtanzania.
Kuna hoja nyingine inahusu imani za kidini, kwamba “katika dini zote, ushoga ni haramu.” Tunarejea palepale. Kwa sababu dini fulani zinasema kitu hiki ni haramu haina maana basi kila mtu (asiye muumini au hata muumini wa dini hiyo) lazima aafiki mtizamo huo. Tukumbuke kuwa dini ni imani, na imani hailazimishwi. Sasa kwa vile Tanzania yetu si nchi ya kidini, japo wengi wa Watanzania wana dini, kinachotakwa haramu katika dini fulani si sheria inayopaswa kufuatwa na kila Mtanzania.
Maana kama kila matakwa ya dini lazima yafuatwe kama sheria ya nchi, hali itakuwaje katika suala kama la ulaji wa nyama ya nguruwe ambayo ni ruhusa kwa Wakristo lakini ni haramu kwa Waislamu? Tupige marufuku ulaji wa nyama ya nguruwe kwa vile ni haramu kwa Waislamu au turuhusu kwa vile ni halali kwa Wakristo? Usuluhishi unapatikana katika busara za kutambua haki na wajibu: uhalali usikwaze haramu na haramu isikwaze halali.
Wakati mjadala huo wa ushoga unaendelea huko Twitter, muungwana moja alinihoji iwapo msimamo wangu kuhusu haki za mashoga unatokana na uwepo wangu huku Uingereza. Nikamjibu kuwa mie ni muumini wa haki za binadamu, na haki hizo ni pamoja na za mashoga.
Mwingine akaenda mbali na kuhoji iwapo nami ni shoga eti kwa sababu ninawatetea sana. Nilimuuliza, hivi tunavyopambana dhidi ya ujangili na kupigania haki za uhai wa tembo wetu, kwa mfano, basi nasi ni tembo?  Kuna vijana wanaopigania haki za wazee, wasio na ulemavu wanaopigania haki za walemavu, na wanaume wanaopigania haki za wanawake. Ni suala la imani.
Ninaendelea kuamini kuwa kwa mtu ambaye si shoga, sioni kwanini asumbuliwe na haki za mashoga. Ni haki za mashoga, sio za wewe usiye shoga. Kwanini basi zikusumbue? Oh dini yako inakataza. Sawa, lakini dini fulani inakataza kula nguruwe lakini yako inaruhusu. Oh mila na desturi zinakataza, vipi kwa asiyehusika na mila na desturi hizo?
Waingereza wana msemo ‘two wrongs don’t make a right’ ambao kwa tafsiri isiyo rasmi ni unamaanisha ‘kwa vile kosa la kwanza limeachwa kama si kosa, haimaanishi kosa la pili nalo liachwe pia.’  Msemo huu unatumika sana dhidi ya wanaohoji “kwanini hizo mila na desturi zikumbukwe kwenye suala la ushoga pekee na sio dhidi ya ufisadi, biashara ya dawa za kulevya, ukahaba na mengine kama hayo?”
Wapinzani wa haki za mashoga wanadai “kwa vile hatutilii mkazo kuhusu imani za dini zetu na mila na desturi zetu kupambana na maovu mbalimbali katika jamii, haimaanishi tusikemee ushoga.” Sawa, lakini haki za mashoga zinachangia vipi uwepo wa mgawo wa umeme usiokwisha? Au mashoga wanachangiaje kushamiri kwa biashara ya dawa za kulevya? Na ni kwa vipi mashoga wanahusika na kuzaliana kwa kasi kwa matapeli wa kisiasa katika mfumo wa siasa wa nchi yetu?
Ninatambua kuwa msimamo wangu katika suala hili sio popular (unaoafikiwa na wengi). Ninatambua pia kuwa kuna wasomaji watakaoniona mtu wa ajabu kabisa kwa kutetea haki za mashoga. Ninahisi pia kuna watakaodhani kuwa labda ‘nimechanganyikiwa.’ Sina tatizo na mtizamo huo kwa sababu ni matumizi ya haki na uhuru wao. Na ndio moja ya faida kubwa za haki na uhuru: kufanya hata kile ambacho mtu mwingine hakiafiki. Sasa, kama sio tu tunapenda haki na uhuru, kwanini tuchukie vitu hivyo hivyo kwa wenzetu?
Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuhusu ukweli huu ambao pengine ni mchungu kwa wapinzani wa haki za mashoga: Sio tu kwamba Tanzania yetu ina mashoga bali pia kasi ya kukua kwa ushoga ni kubwa. Na hata miongoni mwa wapinzani wa ushoga kuna mashoga pia lakini wanaotumia fursa hiyo ya kupinga ushoga kwa minajili ya kuficha ‘siri’ yao. Tunaweza kuendelea kudai ‘ushoga ni haramu...mila na desturi zetu zinapinga ushoga...” lakini hiyo haiondoi ukweli kuwa ushoga upo na mashoga wapo.
Wito wangu kwa ‘wapinzani’ wa ushoga sio wabadili mtizamo wao bali kama kweli wanaoongozwa na dini au mila na desturi kupinga ‘laana’ ya ushoga, basi ni vema pia wakielekeza hasira zao dhidi ya majanga ya kitaifa kama vile ufisadi na biashara ya madawa ya kulevya, sambamba na usaliti katika uhusiano au ndoa (suala maarufu la ‘nyumba ndogo’ na ‘mambo mengine yasiyofaa.’

- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/uhalali-usikwaze-haramu-na-haramu-isikwaze-halali#sthash.tuSqf3kJ.dpuf

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.