Showing posts with label RAIA MWEMA. Show all posts
Showing posts with label RAIA MWEMA. Show all posts

11 May 2017


NIANZE makala hii kwa salamu za pole na rambirambi kwa ndugu, jamaa, na marafiki wa wanafunzi zaidi ya 30 waliopoteza maisha kufuatia ajali ya basi dogo la abiria, huko Karatu Arusha.
Nimeandika “zaidi ya mara 30” kwa sababu wakati ninaandika makala hii, zimepatikana taarifa kuwa inawezekana idadi ya abiria kwenye basi lililopata ajali ilikuwa kubwa kuliko iliyoripotiwa. Taarifa rasmi zinatajwa idadi ya waliofariki kuwa ni wanafunzi 33, walimu wawili na dereva mmoja.
Mungu awapatie marehemu wote pumziko la milele, na mwanga wa milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amina. Bwana ametoa, Bwana ametwaa. Wenzetu wametutangulia tu, lakini sote tupo safari moja, kwani kila nafsi huonja mauti.
Salamu nyingi za pole kwa wafiwa, maana uchungu wa mwana aujuaye mzazi. Wanafunzi hao wamekumbwa na mauti wakati wanaelekea kwenye mitihani yao. Kwa hiyo, tunaomboleza sio kifo tu bali pia kukatishwa kwa ndoto za kielimu za wanafunzi hao. Hili ni pigo kubwa sio kwa ndugu, jamaa na marafiki tu wa wanafunzi hao, bali taifa kwa ujumla.
Kwa mujibu wa mila na desturi zetu, si vema kuanza kulaumiana kuhusu msiba kabla hata mazishi hayajafanyika. Lakini kama kuna kasumba mbaya inayojitokeza katika kila majanga makubwa kitaifa, basi binafsi sioni haja ya kuwa na subira.
Kama kuna kitu kinanisumbua mno kila yanapojiri majanga ya kitaifa kama ajali hii ya Karatu ni ile hali kwamba “wenzetu huku nilipo wanathamini mno uhai uliopotea, pengine kuliko sisi. Hili nimekwishaliongelea mara kadhaa, na kuna mifano lukuki ya kuthibitisha hisia hizo zisizopendeza.
Nashindwa “kupata picha” hali ingekuwaje hapa Uingereza laiti kungetokea ajali kama hiyo ya Karatu. Naandika hivyo kwa sababu “ajali ndogo tu” kwa maana ya idadi ya vifo au majeruhi, hupewa uzito mkubwa mno kiasi kwamba takriban kila mkazi wa nchi hii anaguswa na janga husika.
Nabaki ninajiuliza, “je wenzetu wanathamini mno uhai kuliko sisi?” Sipati jawabu. Najiuliza tena, “labda wenzetu ni ‘wazima’ lakini sisi tumerogwa?” Siambulii jibu. Lakini kilicho wazi ni kwamba tuna upungufu mkubwa katika kuguswa kwetu na majanga makubwa kitaifa.
Mifano ya karibuni zaidi ni janga la tetemeko la ardhi lililoyakumba maeneo ya Kanda ya Ziwa, na kusababisha vifo na majeruhi kadhaa na uharibifu mkubwa wa mali; mauaji dhidi ya askari polisi wanane huko Kibiti, mkoani Pwani, na sasa janga hili ambalo limeripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari duniani.
Kitu kimoja kisichopendeza katika matukio yote hayo matatu ni kwamba serikali haikuona haja ya kutangaza maombolezo ya kitaifa. Katika udadisi wangu, nimesikia utetezi usio na mashiko kuwa “ili kuwe na maombolezo ya kitaifa, na bendera ipepe nusu mlingoti basi msiba husika shurti uwe wa kiongozi wa kitaifa.” Maana yake kwamba uhai wa viongozi wetu una thamani zaidi ya uhai wa wananchi wa kawaida. Ama?
Kitu kingine ambacho sio tu hakipendezi lakini pia kinashangaza ni Rais wetu, John Magufuli kutoungana na waombolezaji wakati wa kuaga miili ya marehemu. Hakuwepo katika tukio la kuaga miili ya waliofariki kwenye ‘Tetemeko la Kagera,’ hakuwepo kwenye tukio la kuaga miili ya askari polisi wanane waliouawa huko mkoani Pwani. Na hadi wakati naandika makala hii, mgeni rasmi kwenye kuaga miili ya wanafunzi hao wa Karatu ni Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Kuna wanaoweza kusema “kwani rais akiwepo atarejesha uhai wa waliofariki?” Hoja hiyo ni ya kukosa ubinadamu. Ni muhimu kutambua kuwa licha ya kuwa “commander-in-chief” wa majeshi yetu ya ulinzi na usalama, Rais pia ni “comforter-in-chief.” Rais ni kama baba, mlezi, na mtu ambaye taifa zima linamuangalia katika nyakati kama hizi.
Tukiweka kando ‘sintofahamu’ hiyo, Shirika la Utangazaji la taifa TBC, limeonyesha kasoro kwa kuendelea na ratiba za vipindi vyake badala ya kuongoza vyombo vingine vya habari katika maombolezo ya vifo vilivyotokana na ajali hiyo ya Karatu.
Nitumie fursa hii kuipongeza Clouds Media Group kwa uzalendo na ubinadamu wao mkubwa uliowasukuma kubadili ratiba za vipindi vyao ili kuungana na wafiwa na Watanzania kwa ujumla kuomboleza vifo hivyo.
Mwisho, japo ajali haina kinga, uzoefu unaonyesha kuwa ajali nyingi zinazotokea huko nyumbani huchangiwa na uzembe wa madereva ikiwa ni pamoja na kukiuka kwa makusudi kanuni za usalama barabarani, sambamba na ubovu wa vyombo vya usafiri wa abiria.
Japo sina maana kuwa sababu hizo ndio zilizochangia ajali hiyo ya Karatu, lakini ni muhimu sasa kama taifa kuliangalia balaa la ajali kama janga la kitaifa. Kwa kiasi kikubwa, madereva wazembe wapo barabarani huku wengine wakiendesha magari yasiyopaswa kuwa barabarani kwa sababu moja kuu, ugonjwa sugu wa rushwa kwenye kitengo cha polisi wa usalama barabarani. Pasipo kukabili rushwa kwenye kitengo hicho, uhai wetu utazidi kuwa mashakani kwa janga la ajali.
Poleni sana wafiwa, poleni Watanzania kwa ujumla. Njia mwafaka ya kuomboleza msiba huu mkubwa ni kwa kuwakumbuka marehemu katika dua/sala zetu

4 May 2017

MAKALA yangu wiki hii inahusu maoni yangu kuhusu hatua ya serikali ya Rais John Magufuli kufukuza watumishi wa umma takriban 10,000 kwa tuhuma za kugushi sifa zao kielimu/ujuzi.
Kwanza, nitanabaishe mapema kuwa sisi ambao tumetumia sehemu kubwa ya uhai wetu kusaka elimu – na tunaendelea kuisaka – hatua yoyote dhidi ya ‘wahalifu wa kielimu’ inastahili pongezi.
Kwa hiyo, hatua ya serikali dhidi ya watumishi wake walioghushi vyeti/ujuzi ni ya kupongezwa. Haipendezi kuona wadogo zetu wanahitimu kihalali katika ngazi mbalimbali lakini wanakosa ajira kwa vile baadhi ya nafasi za kazi zimekaliwa na watu walioghushi vyeti.
Hata hivyo, licha ya hatua hiyo inayostahili pongezi, kuna kasoro kadhaa. Kwanza, kama ilivyokuwa kwa wanafunzi kadhaa wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), ambao sio tu walikatishwa masomo yao lakini pia waliiitwa "vilaza" kwa kosa lisilo lao la kuingizwa katika kozi ya ualimu, japo alama za ufaulu za baadhi yao zilikuwa za chini.
Lengo la serikali ya awamu ya nne chini ya Rais Jakaya Kikwete kuwachukua wanafunzi hao lilikuwa zuri, kwa maana ya mkakati wa kukabiliana na uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi, lakini pia kutoa fursa ya pili kwa wanafunzi hao baada ya matokeo yao kutowaruhusu kuendelea na masomo ya kidato cha tano
Kama ambavyo wanafunzi hao hawakujichagua wenyewe, ndivyo ilivyokuwa kwa watumishi wa umma waliofukuzwa kwa ‘kufoji vyeti.’ Hawakujiajiri wenyewe. Waliajiriwa. Tumepasua jipu kwa kuwafukuza kazi lakini hatujashughulikia kiini cha jipu hilo. Na kwa kiasi kikubwa, kiini ni wanasiasa, ambao kama mzaha vile, hawakuguswa na zoezi la uhakiki wa vyeti vyao/elimu zao.
Uzoefu wangu katika utumishi wa serikali unaonyesha kuwa kwa kiasi kikubwa, ajira serikalini zimekuwa zikitolewa sio kwa kuzingatia elimu au uzoefu bali kujuana.
Nimeandika kuhusu hilo katika kitabu changu cha #Shushushu (kinachozungumzia kuhusu taaluma ya uafisa usalama wa taifa) kuwa moja ya changamoto kubwa kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa ni mfumo mbovu wa ajira unaotoa fursa ya ajira za kujuana/kubebana. Utumishi katika taasisi kama hiyo unahitaji utiifu kwa taifa, lakini ukiajiri mtu kwa vile ni mtoto wa fulani, sio tu anakuwa na utiifu zaidi kwa huyo "fulani" kuliko taifa, bali pia kunakuwa na dharau ya "ah watanifanya nini wakati fulani aliyeniingiza kazini yupo?"
Sasa tumeanza kuwafahamu kwa majina baadhi ya watumishi hao waliofukuzwa kazi. Hata hivyo, ni mapema mno kufahamu iwapo hatua hiyo iliwahusu watumishi wote wa umma au wale tu "wasio ndugu, jamaa au marafiki wa akina fulani"?
Je, wale watoto wa vigogo pale Benki Kuu nao waliguswa na zoezi hilo? Je, ndugu, jamaa na marafiki wa watawala wetu waliojazana kwenye balozi zetu za nje nao waliguswa? "Kitengo" je?
Ila jambo moja ninalohisi linaweza kuwa "matokeo yasiyotarajiwa" (unintended consequences) ni uwezekano wa baadhi ya waliofukuzwa kazi kufungua kesi dhidi ya serikali. Kuna kasoro kadhaa za kisheria katika utekelezaji wa amri hiyo ya rais lakini hapa sio mahala pake kuyajadili.
Japo siwezi kubashiri matokeo ya kesi hiyo iwapo itafunguliwa, vitu viwili vinavyoweza kuongeza uzito wa hoja za watumishi hao ni pamoja na kauli ya Rais Magufuli kwamba "wafungwe miaka saba." Ni kazi ya mahakama kutoa hukumu, sio Rais. Na kwa Rais katamka hivyo, ni kama anaiamuru mahakama itekeleze matakwa yake badala ya kufuata sheria.
Pili, ni wazi kuwa serikali imefanya ubaguzi kwa kuendesha zoezi hili kwa kuangalia “watumishi wasio vigogo” huku ikifumbia macho viongozi mbalimbali, ambao baadhi yao wanaendelea kuandamwa na tuhuma sio za kughushi vyeti vya elimu tu bali hata majina (ni nani asiyejua kuhusu suala la “Bashite”?)
Yayumkinika kuituhumu serikali kuwa imekwepa kwa makusudi kuhakiki sio elimu tu bali hata uraia wa viongozi wa kisiasa. Tuna wanasiasa wengi tu wenye elimu au uraia tata.
Kwa hiyo japo hatua ya kuhakiki elimu ya watumishi wa umma inastahili pongezi, ubaguzi wa makusudi uliofanyika katika zoezi hilo unapaswa kulaaniwa vikali. Lengo halikuwa kumnusuru ‘Bashite’ pekee bali pia baadhi ya wabunge, Wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, na viongozi wengine wa kisiasa ambao baadhi yao sio tu wana walakini kielimu bali pia uraia wao ni tete.

20 Apr 2017


NIANZE makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi kwa familia za askari wanane wa Jeshi la Polisi waliouawa kinyama wiki iliyopita, wilayani Kibiti, mkoani Pwani.
Huu ni msiba wa kitaifa, japo hakuna maombolezo ya kitaifa – sijui kwa vile hatuthamini uhai wa Watanzania wenzetu au tumekwishazoea sana vifo kama vile vya ajali.
Katika moja ya vitu nilivyojifunza katika miaka yangu kadhaa ya kuishi hapa Uingereza ni jinsi wenzetu wanavyothamini uhai. Laiti tukio hili la kuuawa polisi wanane huko Kibiti ndio lingekuwa limetokea hapa, basi huenda kila kitu kingesimama.
Na si hapa Uingereza pekee. Kwa hali ilivyo sasa katika baadhi ya mataifa ya Ulaya Magharibi sasa ni kama "tumekwishaanza kuzoea” matukio ya kigaidi, maana yanatuandama mno, hasa Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani, na majuzi hapa Uingereza.
Katika kila tukio, bila kujali idadi ya waathirika, takriban ndani ya saa moja tangu kutokea tukio husika, Rais au Waziri Mkuu wa nchi husika huongea na wananchi katika runinga mubashara, kutoa pole kwa waathirika, kuwahakikishia usalama wananchi, na kuwaonya wahusika kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Huu ndio uongozi.
Je, sisi hali ikoje? Sana sana ni taarifa ya salamu za rambirambi kutoka kwa Rais, matamko ya hapa na pale ya Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba, na kauli za vitisho za IGP Ernest Mangu – sio kwa “majambazi” bali “wananchi wanaochekelea vifo vya polisi hao waliouawa.”
Japo sio busara kwa mtu yeyote kufurahia kifo cha mtu mwingine – hata kama sio polisi – lakini hilo sio kosa la jinai. Kadhalika, ni vema nguvu ikaelekezwa kwenye tatizo halisi, ambalo Jeshi la Polisi chini ya uongozi wa IGP Mangu haliwezi kukwepa lawama, kwa sababu tishio la usalama mkoani Pwani limedumu kitambo sasa bila kupatiwa ufumbuzi, kuliko ‘tatizo la kufikirika’ (kuwa kuna watu wanafurahia vifo vya polisi hao)
Saa kadhaa baada ya kupatikana taarifa za mauaji hayo, Kamishna wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, alizungumza na waandishi wa habari, ambapo pamoja na mambo mengine alinukuliwa akisema kuwa jeshi hilo "halitokuwa na mzaha wala msamaha" katika operesheni maalumu kuhusiana na tukio hilo. Je, kulikuwa na mzaha na msamaha kabla ya tukio hilo, ambao sasa hautakuwepo wakati wa operesheni husika?
Tukiweka kando kasoro hizo, jambo moja lililonigusa mno ni kukosekana kwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwenye tukio la kuaga miili ya polisi hao. Badala ya kujumuika na wafiwa, Rais alihudhuria hafla mbili (ambazo zingeweza kabisa kusogezwa mbele) za uzinduzi wa hosteli za wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na makazi katika kitongoji cha Magomeni.
Sambamba na hilo, tukilinganisha na matukio makubwa mawili ya hivi karibuni – uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha Clouds na "kutekwa" kwa msanii wa bongofleva, Roma Mkatoliki – mauaji hayo ya polisi hao wanane yalipewa uzito mdogo na Watanzania wengi, angalau huko mtandaoni.
Hali hiyo inasikitisha lakini haishangazi. Sababu moja kuu ya "wananchi wengi kutoonekana kuguswa na mauaji hayo ya polisi wanane" ni ukweli kwamba uhusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi wengi sio mzuri. Polisi wetu kwa kiasi Fulani wamekuwa wakisifika kwa unyanyasaji dhidi ya raia wasio na hatia.
Na kama kuna kitengo cha polisi wetu "kinachochukiwa mno" ni hicho cha FFU (Kikosi cha Kuzuia Ghasia) ambacho askari hao wanane walikuwamo. Japo siungi mkono "chuki" hiyo, lakini naelewa jinsi gani Watanzania wengi wasivyopendezwa na utendaji kazi wa Jeshi la Polisi.
Kwa upande mwingine, jeshi hilo limekuwa likionekana kama "adui wa kudumu" dhidi ya vyama vya upinzani, huku likifanya upendeleo wa wazi kwa chama tawala CCM.
Kwa hiyo, wakati tunaomboleza vifo hivyo vya polisi hao wanane, ni muhimu mno kwa wahusika kuchukua hatua za makusudi kuondoa "uhusiano wa chuki na shaka" uliopo kati ya Jeshi la Polisi na asilimia kubwa ya Watanzania.
Kana kwamba uhusiano bora kati ya Jeshi la Polisi na wananchi sio muhimu ‘sana,’ moja ya nyenzo muhimu ya kujenga na kuimarisha ushirikiano huo, mpango wa Polisi Jamii, ulifutwa kwa sababu wanazozijua wahusika. Polisi jamii ilikuwa kiungo muhimu kati ya polisi wetu na jamii.
Kioperesheni, japo tukio hilo la mauaji ya polisi wanane linaelezwa kuwa ni la kijambazi, binafsi ninahisi kuwa kuna tatizo zaidi ya ujambazi. Na kwa tafsiri ninayoelewa kuhusu ugaidi, basi tukio hilo linastahili kabisa kuitwa la kigaidi. Ni majambazi gani wenye ujasiri wa kuwavizia polisi na kuwaua kwa namna hiyo ya uvamizi wa kushitukiza?
Halafu, hilo sio tukio la kwanza. Na hao polisi wanane sio polisi wa kwanza kuuawa katika eneo hilo, sambamba na wakazi wengine. Yayumkinika kuhitimisha kuwa Jeshi la Polisi na Wizara ya Mambo ya Ndani hawawezi kukwepa lawama, kwa kushindwa kukabili kushamiri kwa mauaji katika eneo hilo.
Sijui Rais Magufuli ameishiwa na zile sindano zake za kutumbulia majipu, au kaishiwa pumzi ya “TumbuaMajipu” lakini ni wazi kuna matatizo ya msingi katika uongozi wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi kwa ujumla. Ukimya wa polisi katika uvamizi huko Clouds, na "kutekwa" kwa Roma, na sasa hili la Kibiti, vilipaswa kumfanya Rais Magufuli achukue hatua.
Moja ya sababu maarufu ya polisi wetu wanapozuia mikutano au maandamano ya vyama vya upinzani huwa "intelijensia." Sasa kama intelijensia ipo kwenye kudhibiti shughuli halali za vyama vya siasa, kwa nini intelijensia hiyo isitumike kwenye kukabiliana na "magaidi" hao wanaotikisa Mkoa wa Pwani?
Nihitimishe makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa familia za askari hao waliouawa kinyama. Pamoja na upungufu wote nilioutanabaisha katika makala hii, hakuna kitu chochote kinachoweza kuhalalisha unyama waliofanyiwa askari hao.
Lakini pia wakati tunaomboleza vifo vyao, ni vema tukatafakari kama taifa kuhusu uhusiano kati ya Jeshi la Polisi (na vyombo vyote vya dola kwa ujumla) na raia, ambao ukiwa bora, unaweza kusaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na taifa kwa ujumla

13 Apr 2017


WANASEMA “wiki nzima katika siasa ni sawa na uhai mzima wa mwanadamu.” Maana ya msemo huo ni kwamba katika siasa, tunaweza kushuhudia matukio mengi katika muda mfupi tu. Kwa lugha nyingine, katika siasa, hata wiki tu ni ndefu kama uhai mzima.
Sasa kama “wiki tu ni uhai mzima” je hali ikoje kwa mwaka mzima? Pengine jawabu lipo kwenye kuiangalia Tanzania yetu, katika kipindi cha takriban mwaka na nusu sasa, kutoka zama za “tumbua majipu” na “hapa kazi tu” hadi muda huu ambapo kila kukicha ni “Bashite hili, Bashite lile,” “Bashite hiki, Bashite kile,” na mengineyo mengi.
Ni vigumu kuandika makala hii ili ifikishe ujumbe unaokusudiwa, kwa sababu takriban kila anayejihusisha na uandishi amekwishapewa angalizo kuhusu nini anatarajiwa kuandika kuihusu Tanzania yetu: habari nzuri tu.
Kwa hiyo inabidi ujuzi wa ziada utumike kuandika habari mbaya lakini ionekane kama nzuri, kwa mujibu wa matakwa ya watawala wetu.
Muda huu ninaandika kitabu kinachofanya tathmini ya “Tanzania: tulikotoka, tulipo, na tuendako” (ndio jina la kitabu husika). Na humo ninajaribu – kwa uhuru mkubwa – kujiuliza kwa mifano hai, nini hasa kimeikumba nchi yetu hadi kufikia hali hii tuliyonayo sasa?
Majuzi nilikuwa nazungumza na mtu mmoja, mzalendo anayefanya kazi kwenye taasisi moja nyeti. Ni maongezi na watu kama hawa yanayonifanya kufahamu yanayojiri nyuma ya pazia. Akanieleza kitu ambacho tangu nilipokisia kimekuwa kikinisumbua sana.
Kwa mujibu wa mzalendo huyo, kuna kikundi hatari ambacho kazi yake kuu ni aidha kunyamazisha watu kwa nguvu au kuepesha mijadala muhimu kitaifa. Kwamba kikundi hicho ambacho ni vigumu kukielezea kwa undani bila kuliingiza gazeti hili matatizoni kinahusika na “utata” wote unaoendelea huko nyumbani muda huu.
Niwatoe pembeni kidogo na kugusia kitu ambacho Rais Donald Trump amekuwa akikiongelea mara kwa mara katika siku za hivi karibuni. Kinaitwa ‘Deep state.’ Jina jingine ni ‘a state within a state’ (dola ndani ya dola).
Deep state anayoilalamikia Trump inaweza kuwa tofauti na inayowezekana kuwepo huko nyumbani. Trump anadai kuwa kuna ushirikiano kati ya taasisi za kiintelijensia za nchi hiyo na baadhi ya watendaji wa serikali, vyombo vya habari, wafanyabiashara na makundi mengine katika jamii, kwa pamoja wakiazimia kumkwamisha Rais huyo mpya wa Marekani.
Tatizo la Trump ni kwamba amekwishaongea upuuzi mwingi mno kiasi kwamba ni vigumu kuchukulia matamshi yake kwa umakini. Na pengine anachokiita ‘deep state’ hakina lengo la kumdhuru kwa kumwonea bali kushughulikia ukweli kwamba tajiri huyo alifanikiwa kushinda urais katika mazingira ya kutatanisha.
Katika Tanzania yetu tumekwishawahi kuwa na mazingira karibu na hiyo ‘deep state.’ Katika siku hizo (mazingira hayaruhusu kubainisha kwa undani kuhusu waliohusika), tulishuhudia watu wakitekwa na kuteswa katika mazingira ya kutatanisha. Nadhani sote tunakumbuka yaliyowasibu Dk. Emmanuel Ulimboka na waandishi wa habari Absalom Kibanda na Saed Kubenea.
Sasa ‘deep state’ imerejea tena, angalau kwa mujibu wa huyo mzalendo ambaye sina sababu ya kutomwamini. Na taarifa zinadai kuwa kuna angalau watu 10 wanaotakiwa “kushughulikiwa.” Baadhi ni wanasiasa wa upinzani na wa chama tawala, na wengine ni watu wenye ushawishi au nafasi muhimu au umaarufu kwenye jamii.
Kwa bahati mbaya, hadi wakati ninaandika makala hii, msanii “Roma Mkatoliki” ambaye pamoja na wenzake walikuwa “wametekwa” kabla ya kupatikana katika mazingira ya kushangaza, alikuwa hajaeleza kuhusu nini hasa kiliwasibu. Hata hivyo, maelezo ya awali yaliyokwishapatikana yanazua utata kuhusu suala hilo.
Msanii anapotekwa, kisha kundi la wasanii wenzake linakwenda kwa kiongozi fulani kuomba awasaidie kumpata mwenzao, na kiongozi huyo anasema kabla ya muda fulani msanii aliyepotea atapatikana, na kweli anapatikana kabla ya ‘deadline’ iliyotajwa na kiongozi huyo, ni wazi “kuna namna” hapo.
Nihitimishe makala hii kwa kutoa ushauri mrefu kwa ndugu zangu wa moja ya idara nyeti nchini Tanzania. Ninyi ndio tegemeo pekee kwenye mazingira kama haya. Kama mimi niliye mbali na huko nyumbani “ninasikia ninachosikia” ni wazi nanyi mtakuwa mnasikia pia. Kuna “uhuni unaofanyika huko mtaani,” na unachafua taswira ya taasisi yenu muhimu na nyeti.
Nafahamu kuwa jukumu lenu ni kushauri tu, lakini ninafahamu pia kuwa mnafahamu cha kufanya pindi ushauri wenu unapopuuzwa na pale zinapofanyika jitihada za waziwazi ku- “undermine” umuhimu wenu. Hivi kweli hizo “rogue elements” zinazohusishwa na “deep state” hazifahamiki? Msipochukua hatua mtahisiwa kuwa mmebariki hayo “yanayoendelea huko mtaani.”
Naomba isitafsiriwe kuwa ninawafundisha kazi. Laiti nisingekuwa na imani nanyi nisingepoteza muda wangu kutoa ushauri huu. Kama ilivyo kwa Watanzania wengi, nina imani kubwa nanyi. Hata hivyo, kuna haja ya haraka ya kuzuia kukua na kushamiri kwa hiyo “deep state.” Ikiachwa, itasababisha madhara makubwa.
Mungu Ibariki Tanzania

25 Mar 2017


Kuna wanaotusimanga tuliompigia kampeni Rais John Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 2015. Kwamba sie ndo tumemleta Magufuli. Kwamba bila sie kumnadi, Tanzania isingeshuhudia kipindi hiki cha 'maajabu' ambapo kwa mara ya kwanza tumeshuhudia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam'anayebebwa na Magufuli' akiwa na uhuru wa kuvunja sheria, na yeyote atakayemkemea atakuwa amenunua ugomvi na Magufuli.

Wanaotusimanga wanasahau kitu kimoja. Laiti Upinzani ungekuwa na mgombea imara katika uchaguzi mkuu uliopita, kazi ya kuiangusha CCM ilikuwa rahisi kuliko wakati mwingine wowote ule.

Nakumbuka kada mmoja mwandamizi wa CCM alinieleza wakati wa kampeni kuwa "laiti Wapinzani walivyoungana na kumsimamisha mtu asiye na rekodi yenye mawaa, kwa mfano Dokta Slaa hivi, basi uchaguzi huu ungekuwa mgumu sana kwetu." Alieleza kuwa UKAWA uliirahisishia CCM kampeni ya kumnadi mgombea wake kwa vile, pamoja na sababu nyingine, mgombea wa UKAWA -Lowassa- alikuwa akijulikana vizuri mno huko CCM, kitu kilichowarahisishia kumshinda 'kirahisi.'

Kwahiyo, kabla ya kuachana na suala la lawama hizo, niseme hivi: sie tuliomnadi Magufuli hatukujua kuwa angekuja kubadilika kiasi hiki, lakini laiti Upinzani ungesimamisha mgombea bora, sie wengine wala tusingekimbia, tungefanya kampeni kama mwaka 2010, na kwa vile kwa kiasi kikubwa Upinzani auliamia kuweka kando tofauti zao, basi uwezekano wa kuiangusha CCM ulikuwa mkubwa. Ila hayo yameshapita sasa, tugange yaliyopo na yajayo.

Na yaliyopo tunayaganga vipi? Ni kwamba wakati tunaendelea kukuna vichwa kufahamu kitu gani kilichomsibu Rais Magufuli, aliyeingia kwa kishindo kikubwa sio Tanzania tu bali kimataifa pia, na hadi kutawala dunia na alama ya reli #WhatWouldMagufuliDo hadi kufikia hatua aliyofikia sasa ya kutawala kwa vitisho, jazba, ubabe na kutetea waziwazi uvunjifu wa sheria uliofanywa na RC Makonda, ni vema basi tujipange imara kuzuwia jitihada zozote za kiongozi huyu kuwa wa kutumia mabavu tu.

Kuna mwanafalsafa mmoja aliusia huko nyuma kuwa "ili maovu yashamiri, yahitaji tu watu wema kutofanya lolote." Wenye uwezo wa kupiga sauti dhidi ya maovu tukikaa kimya, labda kwa vile tu tuliwahi kumpigia kampeni Magufuli, au kwa vile "yatapita tu," kuna kila dalili kuwa tunakoelekea sio kuzuri.

Moja ya mambo yanayotatiza sana kuhusu Rais Magufuli ni kile kinachoonekana kama kupenda ugomvi usio wa muhimu. Hilo nimelieleza kwa kirefu katika makala ninayoiambatanisha hapo chini ambayo ilipaswa kuchapishwa na gazeti la Raia Mwema toleo la wiki hii lakini ninahisi haikuchapishwa (njia pekee ya mie kufahamu imechapishwa au la ni kuona makala husika kwenye tovuti ya gazeti hilo, na wiki hii haipo).

Kati ya nilipoandika makala hiyo na leo, kuna matukio makubwa manne yaliyojitokeza. Kwanza ni Waziri wa Habari (na masuala mengine)  Bwana Nape Nnauye kusimamia vema wajibu wake kama waziri husika, kufuatilia uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha redio na televisheni cha Clouds. Nape alipokea ripoti ya Tume aliyounda, na licha ya msimamo wa Magufulikujulikana mapema kuwa "anambeba Makonda," Nape alionyesha ujasiri na kuiweka hadharani ripoti hiyo ambayo awali baadhi yetu tulidhani ingekuwa 'changa la macho.'

Tukio la pili ni uamuzi wa Rais Magufuli kumfukuza kazi Nape kwa kufanya mabadiliko kwenye kabineti yake, na nafasi ya Nape kukabidhiwa Dkt Harrison Mwakyembe, ambaye majuzi tu 'alilikoroga' kwa kupiga marufuku kufunga ndoa bila cheti cha kuzaliwa. Amri hiyo ya kizembe ilitenguliwa na Magufuli siku chache baadaye.

Tukio la tatu ni mkutano wa Nape na waandishi wa habari, ambao tukiweka kando aliyoyasema mwanasiasa huyo, kubwa zaidi lilikuwa kitendo cha afisa mmoja wa usalama (haijulikani kwa hakika kama alikuwa polisi au taasisi nyingine ya dola) kumtolea bastola Nape hadharani. Tukio hilo la kutisha, na lile na Makonda kuvamia Clouds, yatabaki kuwa historia isiyopendeza kwa taifa letu kwani hayajawahi kutokea...labda zama za ukoloni.

Tukio la nne ni 'mafuriko' ya maneno yasiyopendeza kutoka kwa Rais Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa jana wakati anawaapisha Mwakyemba na Profesa Kabudi, aliyerithi nafasi ya Mwakyembe. 

Sitaki kurudia vitisho alivyotoa Rais Magufuli lakini nachoweza kutahadharisha ni kuwa tunakoelekea sio kuzuri. Unapoona Rais anakerwa kwa vile habari zinazomhusu hazijapewa kipaumbele kwenye vyombo vya habari vingi, basi ujue tuna tatizo kubwa. Unapoona Rais anaamini kuwa habari za maandamano ya wafugaji na wakulima kuhusu migogoro ya ardhi ni "habari mbaya mbaya" basi ni wazi huyu si yule tuliyedhani ni tetezi wa wanyonge.

Tulipasw akuona dalili hizo mapema, kupitia baadhi ya kauli zake kama "I wish I could be Jaji Mkuu" na "I wish I could be IGP." Ukiona Rais anatamani madaraka zaidi ya aliyonayo, hiyo ni hali ya hatari.

Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli asikilize ushauri anaopewa na "wataalamu kuhusu hali ilivyo huko mtaani." Kadhalika, ninamsihi Rais wangu apunguze jazba. Hazitamfikisha popote. Aache kasumba ya kutafuta 'mabifu' yasiyo na msingi. Lakini jingine ni ukweli kwamba hatoweza 'kumbeba Makonda' milele, na kuendelea kumkumbatia kijana huyo kunaweza kumgharimu yeye Magufuli binafsi. 

SOMA MAKALA ILIYOPASWA KUTOKA KATIKA RAIA MWEMA TOLEO LA WIKI HII (JUMATANO 23/03/2017) LAKINI HAIKUTOKA (KWA SABABU WANAZOJUA WAMILIKI WA GAZETI HILO)


MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA MACHI 22, 2017

Disemba 31 mwaka juzi, siku ya mkesha wa ‘mwaka mpya 2016, nilichapisha kitabu cha kielektroniki kilichobeba jina “Dokta John Magufuli: Safari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake.”

Pamoja na watu wengi waliokisoma kitabu hicho kukipongeza, wapo pia walionikosoa, hoja yao kuu ikiwa “ni mapema mno kutathmini Urais wa Magufuli katika muda huu mfupi aliokaa madarakani.”
Kwa wakati huo, sikuafikiana na ukosoaji huo, hasa kwa vile tathmini ya uongozi ni kama maadhimisho ya siku ya kuzaliwa: yanaweza kufanywa siku 40 baada ya kuzaliwa, kila mwezi, na kila mwaka kama wote tunavyofanya.

Kwahiyo, sikuona tatizo katika kufanya tathmini ya urais wa Dokta Magufuli, hasa ikizingatiwa kuwa aliingia na “kasi ya kutisha.” Kati ya siku aliyopishwa, Novemba 5, 2015 hadi nilipochapisha kitabu hicho – takriban miezi miwili hivi – Rais Magufuli alimudu kukonga nyoyo, sio za Watanzania tu, bali dunia nzima kwa ujumla kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya uzembe, rushwa, ufisadi, sambamba na ari yake kubwa ya kubana matumizi.

Naamini sote tunakumbuka alama ya reli (hashtag) ‘iliyotikisa’ dunia nzima ya #WhatWouldMagufuliDo ambayo watumiaji mbalimbali wa mtandao wa kijamii wa Twitter katika kila kona ya dunia walijaribu kuonyesha jinsi gani Dokta Magufuli alivyo bora zaidi ya viongozi wengine duniani.

Lakini sababu nyingine ya kuandika kitabu hicho ilikuwa ushiriki wangu binafsi kwenye kampeni za kumnadi Dokta Magufuli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Pamoja na sababu nyingine, niliamua kumnadi kutokana na sababu zangu binafsi dhidi ya mpinzani wake mkuu.

Na haikuwa kazi rahisi kumnadi mwanasiasa huyu, kwa sababu baadhi ya watu walishindwa kabisa kunielewa, huku wengine wakihoji “kwanini unaweza kutusaliti wapinzani na kumpigia debe mgombea wa chama tawala, ambacho wewe binafsi ni mhanga wa unyanyasaji unaofanywa na serikali yake dhidi ya wanaoikosoa?” Na kilichoambatana na kauli hizo ni matusi mazito, udhalilishaji usiomithilika, na mengineyo yasiyostahili kukumbukwa.

Takriban miaka miwili baadaye, nimeshikwa na bumbuwazi baada ya kumsikia Rais Magufuli “akimkingia kifua” Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ambaye majuzi ameandika historia ya matukio ya kisiasa nchini Tanzania kwa kuvamia ofisi za kituo cha habari cha Clouds, akiambatana na askari wenye silaha nzito.

Niweke rekodi sahihi. Awali nilimtetea RC Makonda katika nilichoamini kuwa ni jitihada zake dhidi ya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Niliamini kuwa suala la ‘utata wa elimu yake’ ni sehemu tu ya mikakati za kumwondoa kwenye ajenda hiyo muhimu.

Hata hivyo, baada ya mawasiliano na “wenye uelewa wa yanayojiri nyuma ya pazia la siasa za Tanzania,” nilithibitishiwa kuwa tuhuma dhidi ya kiongozi huyo zina ukweli, na nikaelezwa kuwa “hata Dokta Magufuli anafahamu hilo.” Na kimsingi, awali nilipanga makala hii iwe ya ushauri kwa Rais kuchukua hatua stahili dhidi ya mteuliwa wake huyo “ili kuwatendea haki wanaomshauri.”

Lakini kabla sijawasilisha makala hiyo, ambayo ililenga zaidi kwenye kusisitiza haja kwa viongozi wetu kuzingatia ushauri wa kitaalamu badala ya kuendekeza ajenda binafsi, kukajitokeza tukio la RC Makonda kuvamia huko Clouds.

Nitumie fursa hii kuupongeza uongozi wa kampuni ya Clouds, hususan Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga, kuwa kufanya kile kilichotamaniwa na Watanzania wengi waliokuwa wakisubiri tamko la kampuni hiyo kuhusu tukio hilo la uvamizi wa Makonda, kwamba wasimamie ukweli.

Na kwa hakika, Ruge na Kusaga hawakuwaangusha watumishi wenzao wa Clouds na Watanzania kwa ujumla, wakaeleza “A hadi Z” ya kilichotokea wakati wa uvamizi huo ambao, kwa kumbukum bu zangu, ni wa kwanza kabisa kutokea nchini mwetu.

Ingeweza kuwa rahisi tu kwa viongozi hao wa Clouds “kuweka mbele maslahi yao binafsi” na kubadili maelezo, hasa ikizingatiwa kuwa lolote ambalo wangesema lingeweza kuaminika, lakini wakaamua kuhatarisha uhusiano wao na Makonda pamoja na shabiki mkubwa wa kituo hicho, yaani Rais Magufuli mwenyewe.

Akiongea kwenye uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara za juu, pamoja na mambo mengine Rais Magufuli aliwaomba Watanzania kujielekeza kwenye vitu vya maendeleo badala ya kujielekeza zaidi kwenye udaku. Ikumbukwe kuwa siku chache tu zilizopita, Rais alipiga simu kwenye kituo cha televisheni cha Clouds na kueleza kuwa yeye pia ni shabiki wa kipindi cha Shilawadu, ambacho ni cha “udaku” huo huo anaokemea Rais.

Suala hapa sio tu “kama ni sahihi kwa Rais kuwa shabiki wa kipindi cha udaku, basi isiwe dhambi kwa wananchi kupenda udaku” bali “kitendo cha Makonda kuvamia Clouds sio kujielekeza kwenye maendeleo.”

Dokta Magufuli alikumbusha pia kuwa “kampeni zimekwisha, ulie lakini Rais ni Magufuli, mimi kwangu hapa ni kazi tu, maendeleo.” Hivi kweli Rais anaamini kelele za kutaka Makonda achukuliwe hatua kutokana na uvamizi huko Clouds ni mwendelezo wa kampeni? Au ni “kelele za wasiojua kuwa Rais ni Magufuli”? Na sitaki kabisa kuamini kuwa Rais anaamini kitendo cha uvamizi wa Makonda huko Clouds ni sehemu ya “hapa ni kazi tu.”

Kilichonisikitisha zaidi ni kauli ya Dokta Magufuli kwamba “mnahangaika na viposti vyenu mara hili mara lile, mpaka wengine wanaingilia uhuru wangu kwamba nifanye hivi, ukiniingilia ndio unapoteza kabisa.”

Kwangu binafsi, nimeoiona kauli hiyo ya Rais kuwa kama dhihaka dhidi ya baadhi yetu tulioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni mwaka 2015 kwa kutumia “viposti” hivyo hivyo anavyovidharau. Na sio sahihi kwa Rais kudai tunamwingililia uhuru wake. Yeye ni mtumishi wetu, na tuna haki ya kumweleza matakwa yetu. Huko sio kumwingilia uhuru wake bali kudai stahili yetu kutoka kwake.

Rais alitukumbusha pia kuwa yeye hapangiwi mambo, anajiamini, na ndio maana siku ya kuchukua fomu alikwenda peke yake. Kumtaka amwajibishe mteule wake aliyevamia kituo cha habari sio kumpangia mambo bali kumkumbusha wajibu wake kama kiongozi. Na kupangiwa mambo kama “mwajiriwa wa Watanzania” sio kosa, isipokuwa tu pale “kumpangia mambo” huko kunalenga kuidhuru nchi yetu.

Sawa, Dokta Magufuli alikwenda peke yake kuchukua fomu za kuwania urais, lakini hakufanya kampeni peke yake. Na kwenda kwake pepe yake kuchukua fomu hakumpi ruhusa ya kutuongoza peke yake, bali kwa ushirikiano kati yetu waongozwa na yeye kiongozi. Hivi, sio Dokta Magufuli huyuhuyu ambaye kila mara anatusihi tumwombee, lakini leo anatuona tunamwingilia?

Kadhalika, Rais alimuunga mkono RC Makonda kwa kumwambia kuwa yeye (Rais) ndio anayepanga nani akae wapi na afanye nini…kwahiyo RC Paul Makonda achape kazi. Hivi Rais amesahau kuwa sio yeye kama Magufuli bali taasisi ya Urais ndiyo inayompa nguvu kufanya maamuzi kwa maslahi ya Watanzania wote?

Na je Dokta Magufuli anataka kutuaminisha kuwa ameridhia kitendo cha Makonda kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha, kiasi cha kumtaka Mkuu huyo wa mkoa “aendelee tu kuchapa kazi”? Je hiyo haitompa jeuri Makonda, na hata wengineo, kufanya “abuse of power” kwa vile “Rais kuruhusu”?

Nimalizie makala hii kwa ushauri huu kwa Dokta Magufuli: kwanza, hakuna tija katika kusaka ugomvi usio na umuhimu (picking up cheap fights). Uamuzi wa kuzuwia kurushwa matangazo ya bunge mubashara, kuzuwia mikutano ya vyama vya siasa vya upinzani, kuwaambia wahanga wa tetemeko Kagera kuwa “serikali haikuleta tetemeko hilo” na “kila mtu abebe msalaba wake mwenyewe”, kuwaambia wananchi wanaolalamikia njaa kuwa “wewe Rais huwezi kuwapikia,” nk sio tu ni “kusaka ugomvi usio wa lazima” lakini haziendani na matarajio ya Watanzania kwako Rais wetu.

Vilevile ninaomba sana kumshauri Rais kuzingatia ushauri wa kitaalamu anaopatiwa na wasaidizi wake. Ni vigumu kufafanua katika hili, lakini ninaamini “nimeeleweka.” Taifa litakuwa katika hali mbaya itapofika mahala “washauri watakapotumia njia mbadala kukufikishia ujumbe.” Na ndicho kinachotokea kuhusu “viposti.”

Mwisho, siku zote Rais wetu umekuwa ukimtanguliza Mungu katika hotuba zako mbalimbali na kuwasihi Watanzania wakuombee. Wewe ni Mkristo, na hii ni Kwaresma. Ni kipindi cha maungamo, kusamehe waliotukosea, kuangalia tulikotoka, tulipo na tuendako. Penye Mungu pana upendo, na penye upendo pana haki. Japo hupangiwi cha kufanya, naomba kukushauri uwapatie haki Watanzania kwa kumwajibisha RC Makonda kwa kuvunja haki za Clouds kutokana na uvamizi aliofanya.
Mungu Ibariki Tanzania


Baruapepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @cha



16 Mar 2017


MAJUZI, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilifanya Mkutano wake Mkuu Maalum huko Dodoma, ambao pamoja na mambo mengine ulikuwa na ajenda kuu ya "kujadili na kupitisha marekebisho ya Katiba ya CCM ya mwaka 1977 Toleo la 2012, pamoja na kanuni za chama hicho na jumuiya zake."
Nimeyawekea msisitizo maneno "kujadili na kupitisha" kwa sababu inaonekana kuwa wazi kuwa majadiliano yaliyofanyika hayakupaswa kutoyapitisha marekebisho hayo.
Ni rahisi kutafsiri hatua hiyo kama ya kuminya demokrasia (kwa maana kwamba kujadili pekee hakutoshi bali pia kuwepo uhuru wa kuyakubali au kuyakataa mapendekezo husika) lakini pengine ni rahisi pia kutambua kwanini CCM "ilijihami" mapema.
Mabadiliko hayo ya katiba ya chama hicho yamepelekea kupungua idadi ya wajumbe wa vikao vya ngazi za juu vya chama hicho na kupunguza 'kofia mbili' kwa viongozi wenye vyeo ndani ya chama, serikalini au bungeni.
Kutokana na mabadiliko hayo, mwanachama anatakiwa kushika nafasi moja tu ya uongozi, katika ngazi za Mwenyekiti wa Tawi, Kijiji, Mtaa, Kata, Wadi, Jimbo, Wilaya na Mkoa. Wengine ni Makatibu wa Halmashauri Kuu wa ngazi zote, Diwani na Mbunge/Mwakilishi.
Kwa hiyo ni wazi kuwa mabadiliko hayo yanawaathiri 'vigogo' kadhaa wa chama hicho, na pengine ndio maana ikaamuliwa kuwe na "mjadala na kupitisha mabadiliko hayo" badala ya "mjadala na kupitisha au kutopitisha mabadiliko husika."
Kadhalika, mabadiliko hayo yatapelekea kupungua kwa idadi ya wajumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, kutoka 34 hadi 24.
Vilevile, idadi ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho imepungua zaidi ya nusu, kutoka 388 hadi 168.
Miongoni mwa 'vigogo' waliotarajiwa kuathiriwa na mabadiliko hayo kutokana na kushika nyadhifa zaidi ya moja ni pamoja na William Lukuvi, Makame Mbarawa, Dk. Hussein Mwinyi, na Shamsi Vuai Nahodha.
'Kigogo' mwingine ni Mama Salma Kikwete, ambaye licha ya kuwa mjumbe wa NEC wa Mkoa wa Lindi, hivi karibuni aliteuliwa na Rais  Magufuli kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri.
Wengine ni wenyeviti wa CCM mikoa ambao pia ni wabunge, kama vile Joseph Musukuma, Martha Mlata na Deo Simba, ilhali Godfrey Zambi ni mbunge na mkuu wa mkoa, Adam Kimbisa ni Mjumbe wa Kamati Kuu na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma.
Kuna usemi mmoja, kwamba sio kila kitu sahihi ni kizuri, na sio kila kitu kizuri ni sahihi. Uamuzi wa CCM kuwapunguzia wanachama wake kofia zaidi ya moja kwenye uongozi ni sahihi lakini sio mzuri kwa watakaoathiriwa nao.
Jicho la uchambuzi litaelekezwa kwa 'wahanga' hao kadri chama hicho kinavyoingia kwenye mchakato wake wa uchaguzi mkuu baadaye mwaka huu, na kwenye kinyang'anyiro cha urais kupitia CCM katika uchaguzi mkuu ujao, mwaka 2020.
Siku moja kabla ya Mkutano huo Mkuu Maalum, chama hicho tawala kilitangaza adhabu kwa viongozi wake kadhaa, kubwa zaidi ikiwa kuwavua uanachama viongozi 12 akiwemo Sophia Simba, kada mkongwe wa chama hicho na ambaye hadi anapewa adhabu hiyo alikuwa Mwenyekiti wa Taifa wa jumuiya ya wanawake wa CCM (UWT), mjumbe wa Kamati Kuu na Mbunge.
Hatua hizo kali zilizochukuliwa na CCM chini ya uenyekiti wa Rais Magufuli, sambamba na mabadiliko niliyoyaongelea awali, yana tafsiri kuu mbili.
Kwanza, hatua kali za kinidhamu zinapeleka ujumbe kwa wana-CCM wa kada mbalimbali kuwa Rais Magufuli amepania kwa dhati kukisafisha chama hicho tawala.
Pili, mabadiliko kusudiwa, sambamba na hatua kali zilizochukuliwa dhidi ya viongozi kadhaa wa chama hicho, ni mtihani mkubwa, kwa Mwenyekiti Magufuli na CCM kwa ujumla.
Kwa Mwenyekiti Magufuli, hatua hizo zimemwongezea idadi ya maadui zaidi ya wale ambao tayari ni waathirika wa msimamo wake dhidi ya ufisadi na rushwa, ambapo watendaji kadhaa wa serikali wametumbuliwa huku wakwepa kodi wakidhibitiwa, na majangili na 'wauza unga' wakibanwa.
Japo ni mapema mno kufanya tathmini timilifu kwa hatua hizo, ile kuzichukua tu sio tu kwaonyesha dhamira lakini pia ni wazi zimetengeneza maadui wa kutosha dhidi ya Dk. Magufuli.
Katika hili, ni muhimu kutambua kuwa ni bora kuwa na kiongozi atakayechukiwa na kwa kutenda vitu sahihi kuliko atakayependwa kwa kufanya madudu.
Siku moja kabla ya Mkutano huo Mkuu Maalum zilipatikana taarifa za kukamatwa kwa makada watatu wa chama hicho, Msukuma, Hussein Bashe na Adam Malima.
Kilichonisikitisha ni maelezo kuwa "walikamatwa na kuhojiwa na polisi kwa tuhuma za kupanga njama za kuvuruga Mkutano Mkuu Maalum wa CCM."
Katika mazingira ya kawaida, sio rahisi kwa makada hao watatu kupanga kuvuruga mkutano mkubwa kama huo ila yayumkinika kuhisi kuwa kilichofanyika ni kuzuwia kile nilichogusia awali, yaani "sio kujadili na kupitisha tu mabadiliko husika" bali pia "kujadili na kupitisha au kutopitisha mabadiliko hayo."
Hili la kuminya fursa ya upinzani kwa mabadiliko hayo linaweza kuwa na athari kwa chama hicho huko mbeleni. Sauti za manung'uniko ni kitu cha kawaida lakini sauti hizo zikiakisi mtazamo wa watu wengi, zinaweza kuathiri mshikamano wa chama hicho.
Hata hivyo, kwa wanaotarajia kuwa "CCM itakufa kutokana na mabadiliko haya" wanapaswa wazielewe vema siasa za Tanzania yetu.
Si kwamba CCM itatawala milele, lakini kwa mazingira tuliyonayo hivi sasa, hakuna chama mbadala. Huo ndio ukweli mchungu.
CCM wanaweza kukandamiza upinzani dhidi ya mabadiliko ya Katiba yao lakini angalau wameitisha mkutano mkuu, wamejadiliana na kupitisha mabadiliko ya katiba yao, sambamba na wameadhibu waliokiuka taratibu za chama hicho.
Sio kamili, lakini hiyo yaakisi demokrasia kwa kiasi fulani. Kwa takriban vyama vyetu vyote vya upinzani, jaribio la kufanya kilichofanywa na CCM wiki iliyopita linaweza kutishia “kukiuwa” chama husika.
Ukiangalia wapinzani wakuu wa CCM, yaani Chadema, sio tu "wamegoma kabisa" kufanya tathmini ya kilichowaangusha katika uchaguzi mkuu uliopita bali pia wametelekeza turufu yao kubwa na iliyowajengea imani kubwa kwa Watanzania, yaani mapambano ya dhati dhidi ya ufisadi, yaliyoibua 'List of Shame,' skandali nzito kama Richmond, EPA, Kiwira, nk.
Cha kusikitisha ni kwamba vyama vyetu vya upinzani sasa vimekuwa kama vinachezeshwa ngoma na CCM. Wafuasi wa vyama hivyo "wapo bize" kujadili matukio yanayoihusu CCM badala ya kuwekeza nguvu kwenye mustakabali wa vyama hivyo.
Jiulize, hivi ajenda kuu ya Chadema, au CUF au ACT- Wazalendo ni ipi muda huu?
Ni katika mazingira hayo, baadhi ya viongozi wa CCM watavumilia mabadiliko yanayoendelea ndani ya chama chao kwa sababu hakuna mbadala wa chama hicho tawala kwa sasa. Tumebaki na miaka mitatu na miezi saba kabla ya uchaguzi mkuu ujao lakini wapinzani wetu wapo bize kuijadili CCM na serikali yake badala ya kujipanga vyema kwa uchaguzi ujao.
Moja kati ya vitu vilivyoiangusha UKAWA katika uchaguzi mkuu uliopita ni "kusubiri makapi ya CCM" badala ya kutangaza mgombea wao mapema na kisha kumnadi kwa nguvu zote, kipindi ambacho CCM ilikuwa na shika-nikushike ya makada wake 40+ waliojitokeza kuwania kuteuliwa kuwa wagombea wa nafasi ya urais kupitia chama hicho tawala.
Nihitimishe makala hii kwa kupigia mstari uwezekano wa aina mbili
Kwanza, CCM kuibuka imara zaidi baada ya Mkutano huo Mkuu Maalum pamoja na hatua za kinidhamu zilizochukuliwa dhidi ya makada kadhaa, kwa sababu nidhamu katika taasisi yoyote ile ni nguzo ya mafanikio, na pia, ili maendeleo yafikiwe shurti kuwepo na mabadiliko, na mabadiliko hukumbana na vikwazo ambavyo vyaweza kurukwa iwapo kuna nidhamu bora.
Japo yaweza kuwa mapema mno kuhitimisha hili, yayumkinika kusema kuwa “mahesabu ya Magufuli yamelipa” kwa maana ya uamuzi wake wa kumteua Mama Salma kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri hivi karibuni unaweza kuwa umesaidia “kumweka karibu” Rais Mstaafu Jakaya Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti mstaafu wa CCM Taifa, na mwenye ushawishi mkubwa katika chama hicho kuliko Dk. Magufuli mwenyewe.
Pili, mambo mawili – hatua dhidi ya makada walioadhibiwa na mabadiliko yaliyopelekea baadhi ya viongozi kupunguziwa nyadhifa – yanaweza kuzua manung’uniko ndani ya chama hicho. Ni wazi kuwa waliochukuliwa hatua za kinidhamu na walioathirika wa kuvuliwa kofia zaidi ya moja za uongozi hawatofurahishwa na hatua hizo. Hata hivyo, je wana pa kukimbilia? Na hapo ndipo utapobaini kuwa siasa za nchi yetu "zingechangamka sana" laiti tungekuwa na upinzani imara.
Na upinzani imara sio lazima upewe ruhusa na serikali kufanya mikutano/maandamano bali kama ule ulioibua 'List of Shame,' Richmond, EPA, nk…hawakuwa na ruhusa ya kufanya hivyo, na pia wanasiasa kama Dk. Willibrord Slaa na Zitto Kabwe walinusurika kwenda jela kwa ajili ya kuwapigania Watanzania.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.