13 May 2016

Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza umeingia lawamani kufuatia uamuzi wake wa 'kuwabagua' baadhi ya Watanzania wanaoishi nchi hapa na kuwanyima fursa ya kuhudhuria mkutano unaotarajiwa kufanyika kesho kati ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa kawaida, viongozi wa kitaifa wanapokuja hapa kutoka huko nyumbani huongea na Watanzania wanaoishi hapa, na utaratibu uliozoeleka ni kutangaza tarehe, mahala na muda wa mkutano, kinyume na hali iliyojitokeza sasa ambapo inaelezwa kuwa kuna kikundi kidogo tu cha watu walioteuliwa kukutana na Waziri Mkuu Majaliwa.

Blogu hii ilifanya jitihada za kuwasiliana na Watanzania kadhaa wa hapa, na ukiweka kando wachache waliosema kuwa wasingeenda katika mkutano huo hata kama wangealikwa, wengi wao walilaumu kitendo hicho cha ubalozi kuteua kundi la watu wachache, ambapo wala haifahamiki wachache hao waliteuliwa kwa vigezo gani.

Baadhi ya waliohojiwa na blogu hii walieleza kuwa huenda "ubalozi huo ni jipu, na umeamua kuteua kundi la watu wachache ili kuepusha uwezekano wa mtu 'asiyejulikana' kukurupuka na kumfahamisha Waziri Mkuu kuhusu malalamiko yanayouhusu ubalozi huo (kama kweli yapo)."

Kadhalika, ilielezwa kuwa kitendo cha ubalozi huo kufanya 'ubaguzi' huo kinaweza kuijiengea serikali ya Awamu ya Tano ya Rais John Magufuli taswira mbaya, kwamba "Waziri Mkuu amekwepa kuongea na Watanzania kwa wingi au uwazi na badala yake anakutana na kikundi kidogo cha wateule wachache."

Vilevile, kitendo hicho kinaweza kumtengenezea mazingira magumu Balozi mpya wa Tanzania nchi hapa, Dkt Asha-Rose Migiro, iwapo 'walionyimwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo' watabaki na mtizamo kuwa "mnatutenga wakati wa ziara za viongozi wa kitaifa basi nasi twawatenga katika maisha yetu ya kila siku."

" Au ndio yale ya Bunge Dodoma kwamba halirushwi live, basi sasa hata viongozi wetu wakuu wakija hapa, badala ya kukutana nasi kwa uwazi na wingi, fursa hiyo inatolewa kwa wateule wachache tu...kwa maslahi binafsi."

Wakati ubalozi hauwezi kukwepa lawama kwa vile kimsingi wenyewe ndio wenye mamlaka ya kufanya maandalizi ya mkutano huo, haieleweki kwanini 'jumuiya kuu mbili za Watanzania hapa Uingereza,' Kikosi Kazi na Kamati ya Mpito hazijafanya jitihada zozote kupigia kelele kuhusu kasoro hiyo. Badala yake, kila upande umekuwa ukiutuhumu upande mwingine 'kutumiwa na Ubalozi kwa maslahi binafsi.'

Awali, jana kulipatikana kipande cha sauti kilichorekodi sehemu ya kipindi cha Jahazi cha Clouds FM ya huko nyumbani, ambapo waendesha kipindi walijadili kwa ufupi kuhusu kasoro hiyo ya Waziri Mkuu kuandaliwa mkutano wa kuongea na idadi ndogo tu ya Watanzania, katika utaratibu usio wazi. Bonyeza hapa chini kusikiliza
Hadi wakati blogu hii inakwenda mitamboni, hakuna taarifa yoyote rasmi kutoka kwa ubalozi au makundi makuu mawili yanayowakilisha Watanzania hapa, kuhusu kwa mfano mkutano huo utafanyika lini, wapi na muda gani.

Hata hivyo, baadhi ya waliohojiwa walionyesha matumaini kuwa inawezekana Waziri Mkuu haelewi kuhusu 'usanii unaofanywa na ubalozi,' na akipata taarifa atauagiza ubalozi huo kufanya maandalizi ya kuwezesha Watanzania wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.