15 Dec 2016


KATIKA toleo la Oktoba 20, 2016 la gazeti hili niliandika makala iliyokemea madai ya uongo yaliyokuwa yakisambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu elimu ya Rais Dk. John Magufuli. Kwa mujibu wa madai hayo, shahada ya uzamifu ya kiongozi huyo ilikuwa feki, na kama sio feki basi athibitishe hadharani.
Binafsi nilikerwa sana na madai hayo. Nilijaribu kuyakemea huko kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook, kwa kuwashauri wenye kuhitaji uthibitisho wa elimu ya Dk. Magufuli waende Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, taasisi ambayo ndiyo ilimtunuku shahada hiyo kiongozi huyo.
Hata hivyo, ushauri huo haukupokelewa vema na kada wa Chadema, Ben Saanane, aliyekuwa mstari wa mbele kumtaka Dk. Magufuli ahakiki PhD yake. Badala ya kuzingatia ushauri kuwa kuna njia rahisi ya kusaka ukweli kuhusu suala hilo, kijana huyo alitumia lugha isiyopendeza dhidi yangu.
Baada ya kuona suala hilo linazidi kupamba moto hasa huko Facebook, nikaamua kuandika makala katika gazeti hili toleo la Oktoba 20 mwaka huu. Katika makala hiyo, niliepuka kutaja jina la mhusika mkuu katika madai hayo ya uongo dhidi ya elimu ya rais wetu.
Katika toleo la wiki iliyofuata (Oktoba 27, 2016), kada maarufu wa Chadema Ben Saanane alijitokeza kujibu makala hiyo, huku akidai kuwa ni haki kuhoji elimu ya Dk. Magufuli. Licha ya kutumia mifano mingi ya watu mbalimbali maarufu ‘waliofeki’ taaluma zao, Saanane hakuweza kuthibitisha madai yake kuwa PhD ya Magufuli ni feki pia.
Japo mara zote nimekuwa nikikwepa kujibishana na wasomaji wa makala zangu, ilinilazimu kujibu makala ya Saanane kwa vile ilinitaja moja kwa moja. Nilifanya hivyo katika toleo la gazeti hili la Novemba 3, 2016. Katika makala hiyo nilieleza bayana kuwa tatizo la madai ya kada huyo wa Chadema na wenzake sio kuhoji kuhusu elimu ya Rais bali kumtuhumu Rais kuwa PhD yake ni feki. Basi angalau yeye na wenzake wangejihangaisha kuonyesha ‘ukweli’ wa tuhuma zao badala ya kumtaka Rais athibitishe kuwa ‘tuhuma hizo dhidi yake ni za uongo.’
Wiki iliyopita, zilipatikana taarifa kuwa kada huyo ‘hajulikani alipo kwa zaidi ya wiki tatu sasa.’ Hadi wakati ninaandika makala hii, jitihada zilikuwa zinaendelea kumtafuta kada huyo. Hata hivyo, pengine kwa vile Saanane ‘alishikia bango’ tuhuma kuwa PhD ya Dk. Magufuli ni feki, tayari ‘kupotea’ kwake kunahusishwa na tuhuma zake hizo.
Wakati ninaungana na familia ya Saanane na makada wenzake wa Chadema kumwombea awe salama, kuna vitu viwili muhimu vya kuzingatia. Kwanza, wakati Saanane ‘alipojipa uhuru wa kudhalilisha elimu ya Rais,’ makada wenzake hawakuona haja ya japo kumsihi apunguze ukali wa lugha yake dhidi ya kiongozi mkuu wa nchi. Badala yake walimmwagia sifa, huku wakimshambulia kila aliyejaribu kumsihi kada huyo asitumie lugha isiyofaa.
Hili ni tatizo sugu katika mitandao ya kijamii. Kuna wenzetu wakiwa mtandaoni wanajiona kama majabali fulani, wenye uhuru wa kudhalilisha watu, kutukana watu, kunyanyasa watu na tabia mbaya kama hizo. Watu hawa hutumia kisingizio cha ‘uhuru wa kujieleza’ huku wakipuuza haki ya kila mtu kuheshimiwa. Uhuru wa kufanya jambo bila kujali kuwa linakiuka haki za wengine ni uhuni.
Pili, kuna mkanganyiko mkubwa kuhusu ‘kupotea’ kwa kada huyo. Inaelezwa kuwa ‘alipotea’ katikati ya mwezi uliopita, lakini taarifa kuhusu ‘kupotea’ kwake zimeibuka zaidi ya wiki tatu baadaye. Licha ya wadhifa wa Mkuu wa Sera na Utafiti wa Chadema, Saanane alikuwa pia ‘msaidizi binafsi’ (Personal Assistant) wa mwenyekiti wa taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe. Hadi wakati ninaandika makala hii, si Mbowe au kiongozi yeyote wa ngazi za juu wa chama hicho aliyetoa tamko kuongelea suala hilo.
Kuna wanaohoji, hivi inawezekana kweli msaidizi binafsi wa mwenyekiti wa taifa wa chama kikuu cha upinzani ‘apotee kwa zaidi ya wiki tatu’ lakini kiongozi husika asionekane kuguswa na tukio hilo? Kwa nini ‘wanaomtafuta’ Saanane wasiubane uongozi wa juu wa Chadema, ambao ‘ukimya’ wake katika suala hilo ni kama unaashiria kufahamu alipo kada huyo?
Nihitimishe makala hii, kwanza, kwa kuutaka uongozi wa Chadema kitaifa kujitokeza kuongelea suala hili (kama lina uzito stahili kwao), sambamba na Jeshi la Polisi kusaidiana na wahusika kumsaka kada huyo

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.