Showing posts with label KUMBUKUMBU. Show all posts
Showing posts with label KUMBUKUMBU. Show all posts

8 Jul 2016

Ilikuwa masaa, siku, wiki, miezi na sasa mwaka. Ni vigumu sana kuamini kuwa baba umeondoka moja kwa moja. Kila siku nakumbuka, lakini kuna kitu kingine kinachonikumbusha kila wiki: makala zangu katika gazeti la Raia Mwema. Ulikuwa 'shabiki nambari wani' wa safu yangu katika gazeti hilo, na ulihakikisha unasoma kila toleo la gazeti hilo.

Pamoja na mengi uliyotuachia wanao, moja ninalofanya kila siku ni kusoma na kuandika, vitu viwili ulivyonisisitiza mno tangu nikiwa mtoto mdogo. Na kwa hakika kama ulivyopenda sana kusoma na kuandika, ndivyo ambavyo kwangu vitu hivyo vimekuwa sehemu muhimu ya maisha yangu ya kila siku.

Pia wewe na marehemu mama mlinisisitza mno kuhusu umuhimu wa elimu.Nawashukuru sana mlivyojinyima ili kuhakikisha ninatimiza ndoto zangu za kielimu. Ninasikitika kwamba wakati wewe na mama mlikuwa na kiu sana ya kuniona nahitimu shahada ya uzamifu (PhD), kwa bahati mbaya nyote mmeondoka kabla sijahitimu. Hata hivyo, nime-dedicate thesis yangu kwenye.

Nakushukuru pia wewe na marehemu mama kwa kutuhimiza mno watoto wenu kuhusu upendo, kuthamini utu na kubwa zaidi, kumtanguliza Mungu katika kila tufanyalo. Upendo wako baba ulikufilisi mapema mara baada ya kustaafu mwaka 1981, ambapo mipango yako ya kuwekeza katika kilimo ilizidiwa nguvu na moyo wako wa kuwasaidia ndugu na jamaa pale Ifakara. 

Miaka kadhaa baadae, marupurupu yako ya utumishi wako katika Jumuiya ya Afrika Mashariki nayo yaliishia kwenye kuwasaidia ndugu, jamaa na marafiki. Siku zote ulikuwa unasisitiza kuwa utu ni muhimu ziadi kuliko vitu (including pesa). 

Iliniuma mno kushindwa kuja kukuaga katika safari yako ya mwisho. Lakni nakumbuka sana maeneo yako kuwa "lolote likinitokea, hakikisha kwanza usalama wako..." Wewe baba na marehemu mama siku zote mlikuwa mnahofia kuhusu kazi niliyokuwa naifanya lakini kwa vile mlinipenda mno, mlikuwa mkiniombea kila siku ya Mungu.

Kama kuna kitu kinaniumiza mno ni mapacha Kulwa (Peter) na Doto (Paul). Kwa vile wao walizaliwa wakati umri umeshawapita mkono nyie wazazi wetu, mapacha hawa walikuwa kama wajukuu zenu. Lakini kubwa zaidi, walikuwa ndio marafiki zenu wakubwa. Kila ninapoongea nao najiskia uchungu sana kwa sababu sio tu wamepoteza wazazi lakini pia wapoteza their best friends. Ninaendelea kuwasapoti ili wasielemewe na huu uyatima tulionao.

Kama kuna kitu kimoja nilikuangusha mno ni kutofuata matakwa yako nijiunge na seminari ya Kasita baada ya kuwa mmoja wa wavulana wanne tu waliochaguliwa kujiunga na seminari hiyo. Ulitamani sana niwe padri. Hata hivyo, japo nilikuangusha, angalau mdogo wangu, Sista Maria Solana aliweza kujiunga na utawa, na yeye sasa ndio guide wetu mkuu katika sala.

Pamoja na uchungu nilionao kutokana na kifo chako baba, faraja pekee ni kuwa ninaamini muda huu upo na mkeo mpendwa, mama yetu mpendwa, marehemu Adelina Mapango a.k.a Mama Chahali. Tangu mama afariki, baba ulikuwa ukisononeka mno, kwa vile mama hakuwa mkeo tu bali pia rafiki yako mkuu. Siku zote baada ya kifo cha mama ulijisikia kuwa wewe ndo ulistahili kutangulia kabla yake kwa vile ulikuwa umemzidi umri.

Kipimo cha upendo wako baba ni kipindi kile mama alipopoteza fahamu kuanzia mwishoni mwa Januari 2008 hadi alipofariki Mei 29, 2008. Baba ulikuwa unafunga mfululizo kumwombea mama apate nafuu.Nakumbuka nilipokuja kumuuguza mama tulikushauri upunguze kufunga mfululizo hasa pale sauti yako ilipoanza kukauka na nguvu kupotea kutokana na mwili kukosa lisha na maji. Ulimpenda mno mkeo, na kwa hakika mmetachia fundisho kubwa sana.

Mwaka 2005 niliwarekodi wewe na mama, katika maadhimisho ya miaka 50 ya ndoa yenu. Bado ninayo video ile lakini nashindwa kuiangalia kwa sababu inanitia uchungu sana. Hata hivyo, kila siku ninazingatia yote mliyoniusia katika video hiyo, na ndio mwongozo wa maisha yangu.

Basi baba, nakuombea uendelee kupumzuka kwa amani na marehemu mama na mwanga wa milele uangaziwe na Bwana. Mie ninawakumbuka kwa sala kila siku kabla ya kulala. Sie tulikupenda wewe baba na mama, lakini Baba yenu wa Mbunguni aliwapenda zaidi, akawachukua. Jina lake lihimidiwe milele. AMINA



29 May 2013


Tarehe kama hii, miaka mitano uliyopita,mama mpendwa Adelina Mapango, uliagana nasi. Nikisema 'uliagana nasi' inaweza kutafsiriwa kana kwamba ulipata nafasi ya kutuaga.Nilikuja huko nyumbani kukuuguza Februari 2008, lakini tangu nilipokuona pale Muhimbili hadi tarehe 29 Mei 2008 hukuwahi japo kuniambia neno moja la mwisho.Nakumbuka ulivyokuwa ukiniangalia kwa upendo wako mkubwa,nakumbuka pia tabasamu lako licha ya maumivu makubwa uliyokuwa nayo.Lakini kila nilipojaribu angalau kusikia neno lako moja tu,haikuwezekana hadi siku unafariki.

Mama mpendwa, kabla ya kifo chako sikuwahi kuelewa maana ya kufiwa na mzazi au mtu wa karibu.Sasa sio tu naelewa bali kila siku ya Mungu tangu siku ulipotutoka imekuwa kama ndoto mbaya ambayo natamani iishe ili hali irejee kuwa kama zamani.Kwa bahati mbaya, ndoto hiyo mbaya ni ukweli (hali halisi), na hadi sasa matarajio kuwa kuna siku nitaamka na kukuona au kukusikia ukiwa hai yanazidi kufifia.Kwa kifupi,mama mpendwa,hadi leo bado napata shida kuamini na kukubali kuwa haupo nasi.

Nyakati mbili ngumu zaidi kwangu ni wakati ninapofanya sala kabla ya kulala ambapo wakati wa uhai wako nilikuwa nikisali "Ee Bwana uijalie familia yangu yani Baba na Mama..." lakini sasa inabidi nimtaje Baba pekee.Pia wakati wa uhai wako,nilijenga utaratibu kwamba nikipiga simu naanza kuongea na Baba kisha anapitisha simu kwako tunaanza kutia stori mbalimbali.Sasa,mama,nikimaliza kuongea na Baba huwa najikuta nasahau kuwa haupo hapo nyumbani,na kumwambia Baba akupe simu...then nakumbuka haupo.Naishia kutoa machozi.

Nikiwa mbinafsi,nitaangalia tu jinsi ninavyopata shida kukabiliana na ukweli kuwa hauko nasi.Lakini kuna rafiki yako kipenzi Baba Mzee Chahali ambaye yeye amekuwa mtu tofauti kabisa tangu ulipoondoka.Kama unavyokumbuka,baba ni mtu mkimya,mwenye marafiki wachache, na rafiki yake mkuu ulikuwa wewe.Sasa tangu uondoke,baba amekuwa mnyonge kupita kiasi.Kibaya zaid, ameendelea kudai labda yeye ndio angestahili kutangulia mbele ya haki kwa vile alikuwa amekuzidi kiumri.Kwa hakika, baba ameendelea kuwa katika wakati mgumu sana licha ya sapoti kubwa tunayompatia.

Lakini pia kuna rafiki zako wapenda Kulwa na Doto (Peter na Paul). Pengine kwa vile wao ni last borns, walikuwa wakikuchukulia zaidi ya mzazi, ulikuwa kama bibi yao, shangazi yao, na kikubwa zaidi, rafiki yao.Kila ninapoongea na wadogo zangu hawa najiskia kutokwa na machozi.Kimsingi, sidhani kama waliwahi kuwaza kuwa na maisha bila ya uwepo wako mama.

Familia yote kwa ujumla inakukumbuka sana mama.Nina mkanda wa video niliowarekodi wewe na baba mlipokuwa mnaadhimisha miaka 50 ya ndoa yenu mwaka 2005,lakini kila nikijaribu kuuangalia najikuta nabubujikwa na machozi.Katika mkanda huo uliongea mambo mengi ya msingi kuhusu maisha.Kuna nyakati nataka kuuangalia ili nirejee wosia wako lakini nashindwa kwa sababu ya uchungu.

Mama nilikupenda sana,ninakupenda sana,na nitaendelea kukupenda milele.Kwangu, japo hupo nasi kimwili,lakini unaendelea kuishi nasi kiroho.Nitazidi kukukumbuka kwa sala kila siku,na ninaamini huko uliko unapata faraja kila ninapotenda mambo kwa kuzingatia mafundisho yako.

WE MISS YOU SO MUCH MAMA MPENDWA

PUMZIKO LA MILELE AKUPE EE BWANA NA MWANGA WA MILELE AKUANGAZIE UPUMZIKE KWA AMANI AMINA

29 May 2012


Mama mpendwa,ilikuwa siku kama yale leo,miaka minne iliyopita,uliondoka hapa duniani wakati tunakuhitaji sana.Japo miaka minne inaweza kuonekana ni muda mrefu kusahau machungu,kwangu mwanao imeshindikana.Kila siku ya Mungu ninaposali kukuombea pumziko na raha ya milele huko ulipo,hujikuta napatwa na uchungu usioelezeka.Kwa kifupi,mama mpendwa,kila siku baada ya kifo chako-siku kama ya leo miaka minne iliyopita,imeendelea kuwa ni hudhuni na majonzi yasiyoelezeka.

Mama mpendwa,ulikuwa ni zaidi ya mama kwangu,kwa mumeo-Baba Mzee Chahali,na kwa wanao wote na ndugu na jamaa.Nakumbuka mwaka 2005 nilipokuja likizo nyumbani,ulirukaruka kwa furaha,ukanikumbatia na kunipakata mwanao,ukaniandalia maji ya kuoga,ukanifanya nijsikie kama mtoto mchanga.Sikujua kuwa furaha ile ya mzazi kumwona mwanae waliopoteana kitambo kidogo sintoipata tena maishani.Inaniuma sana.

Nakumbuka wakati huo ambapo wewe na Baba mlikuwa mnasherehekea miaka 50 ya ndoa yenu,ulinipa mafundisho mengi kuhusu maisha,ndoa,upendo na zaidi ni kumweka mbele Mungu katika kila ninalofanya.Kabla ya kifo chako,nilikuwa nauangalia mkanda niliowarekodi wewe na Baba,na kila nilipofanya hivyo niligundua kuwa nina bahati ya pekee kuwa na wazazi wanaonipenda kiasi hicho.Sikujua kuwa mahojiano yale ndio ulikuwa wosia wako kwangu mwanao.Kwa sasa sina nguvu ya kuangalia video hiyo,kwani kila nikijaribu naishia kububujikwa na machozi.

Nakumbua nilipokwenda chumba cha maiti na kukuona umelazwa kwenye zile friji wanzohifadhia maiti.Nilikugusa mama,nilitaraji muujiza kwamba ungeamka na ndoto ile mbaya ingeisha.Hukuamka hadi leo hii.

Mama,inaniuma sana kwani nilipokuja kukuuza Februari 2008 ulikuwa umeshapoteza fahamu.Ulipokuwa Muhimbili na baadaye St Francis,Ifakara,nilikuwa najaribu kukusemesha.Kama vile ulifahamu mwanao nimekuja kukuuguza,kuna nyakati ulikuwa unatoa tabasamu lako lenye mwanya ulionirithisha.Nikategemea utaamka na kunieleza japo neno moja.Kwa bahati mbaya hadi unafariki hukuweza kuniambia chochote.Inaniuma sana mama.

Inauma zaidi ninapopiga simu nyumbani.Nilizowea kuwa nikimaliza kuongea na Baba anakupa simu wewe tupige stori.Sasa,kila ninapompigia mzee huwa najikuta nataka kumwambia Mzee akupe simu niongee nawe,kisha nakumbuka kuwa hauko nasi.Kila simu ninayopiga nyumbani inanirejeshea kumbukumbu hizo na kuniacha mpweke,mkiwa na mwenye uchungu mkubwa.

Nyakati nyingine baadhi ya watu wangu wa karibu (ninao wengi kutokana na malezi bora uliyonipatia) huwa wananiona kama dhaifu ninapowaeleza uchungu nnilio nao takriban kila siku tangu ufariki.Siwalaum,kwani wanachojitahidi kufanya ni kunishawishi nikubali ukweli kuwa haupo nasi na haiwezekani kukurejesha.Kuna wakati wananichukiza kwani najihisi kama hawaelewi jinsi kifo chako kinavyoniathiri.Lakini baadaye akili hunirejea na kutambua wanachofanya ni kujaribu kunisaidia tu.

Mama mpendwa,sijui nisemeje.Rafiki zako wakubwa,wanao vitinda-mimba,Kulwa na Doto,ndio wananitia uchungu zaidi,kama ilivyo kwa Baba.Watatu hao pamoja na wewe mlikuwa kama marafiki.Nakumbuka siku zile nawapigia simu na kuwasikia mnacheka,mnataniana na kunipa kila aina ya faraja.Kwa sasa imebaki kumbukumbu tu.

Mama mpendwa,siku ya mazishi yako Padre alituambia maneno haya: "Mama Adelina alikuwa mtu wa watu,na kila anayemjua anafahamu hilo.Japo mnaomboleza kifo chake,lakini mnapaswa kupata faraja kuwa kutokana na matendo yake mema,Baba Yake wa Mbinguni Ameamua kumchukua.Sote tulimpenda lakini Mungu alimpenda zaidi,na ndio maana amemchukua." Maneno hayo ndio nguvu pekee inayonisaidia kumudu kufanya mambo mengine maishani.

Basi naomba nikuage tena mama kwa kumwomba BWANA AKUPATIE PUMZIKO LA MILELE NA MWANGA WA MILELE AKUANGAZIE,UPUMZIKE KWA AMANI AMEEN.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.