13 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-28

Asalam aleykum.

Mwaka 2003 Mmarekani mmoja aitwaye Dan Brown alichapisha kitabu kiitwacho The Da Vinci Code ambacho baadaye kilipelekea kutengenezwa kwa filamu iliyobeba jina hilohilo.Hadi mwezi Mei mwaka huu zaidi ya nakala milioni 60 za kitabu hicho zimeshauzwa sehemu mbalimbali duniani.Idadi hiyo ni sawa na nakala moja kwa kila Mtanzania na bado nyingine kibao zitasalia.Nayo filamu ya Da Vinci Code iliyotolewa mwaka huu hadi kufikia tarehe 14 ya mwezi Agosti ilikuwa imeshaingiza dola za kimarekani 749,975,451 (sijui ni sawa na shilingi ngapi za huko nyumbani).Vyote viwili,kitabu na filamu,vinazungumzia mambo ambayo kwa namna flani ni kama kashfa dhidi ya Kanisa Katoliki.Brown anadai kuwa Kanisa hilo limekuwa likificha ukweli kuhusu maisha halisi ya Yesu Kristo na kwamba kwa makusudi makao makuu ya kanisa hilo huko Vatican yamekuwa yakifanya hivyo (kuficha ukweli) ili yaendelee kuwa na nguvu za kiutawala ulimwenguni.Huyu jamaa ametengeneza marafiki na maadui wa kutosha kwa utunzi wake huo.Nimekisoma kitabu chake,na mie ni Mkatoliki,kwa hiyo naomba mniruhusu nisieleze “upuuzi” uliomo kwenye kitabu hicho.Si unajua tena,mambo ya dini ni imani,sasa mtu akianza kuleta maswali ya ajabuajabu anakuwa anawakwaza wale wengine ambao utotoni kwenda kanisani hadi watishiwe kunyimwa chakula na wakisinzia kidogo tu wanalambwa na shetani (lugha za kidini hizo…samahani kwa ndugu zangu wapagani).

Ilipotoka filamu ya Da Vinci Code ulizuka mjadala miongoni mwa viongozi wa madhehebu mbalimbali ya Wakristo,hususan Wakatoliki.Kuna wale waliowataka waumini waisusie filamu hiyo kwa vile inamtukuna Yesu.Walisema kwamba kuiangalia filamu hiyo kunaweza kuathiri imani zao hasa kwa vile madai yaliyomo kwenye filamu hiyo ni mazito mno na hayazungumziki katika lugha za kiroho.Wengine wakadai kwamba ili kuweza kuapambana na hoja za mwandishi huyo ni muhimu kwa waumini kuiona filamu hiyo.Walidai kuwa mtu atakaepoteza imani yake kwa vile tu ameamini aliyoyaona katika filamu hiyo basi atakuwa na matatizo yake binafsi…kwa lugha za kanisani wanaita imani haba.Nadhani kundi hili la pili ndio lililopata wafuasi wengi zaidi,yaani watu wenye imani zao thabiti ambao walikwenda kuiona filamu hiyo kwa malengo ya kuelewa madai yaliyomo na kujiweka katika nafasi nzuri kuyakabili.Mimi sijapoteza muda wangu kuiangalia,sio kwa kuhofia kuiyumbisha imani yangu.Ni kwa vile tu nilishasoma kitabu ambacho kimsingi ndicho asili ya filamu hiyo.Kama nilisoma kitabu hicho na msimamo wangu haukuyumba basi ni dhahiri filamu hiyo isingebadili kitu kwangu.

Huko nyumbani tumepata kiji-Da Vinchi Kodi chetu kwa jina la Darwin’s Nightmare.Mengi yameshasemwa kuhusu filamu hiyo na mimi sitaki kuyarudia hapa.Nachotaka kukizungumzia hapa ni unafiki unaozunguka suala hilo.Hivi filamu hiyo si ilirekodiwa huko Mwanza?Hivi samaki si ndio maliasili zetu?Hivi Waziri wa Maliasili na Utalii Anthony Diallo hatoki Mwanza huyo?Alikuwa wapi hadi Rais Kikwete aikemee filamu hiyo?Huyu ni mguswa wa karibu kabisa wa sakata la mapanki.Na isieleweke kuwa namshikia bango.Hapana,ila nashindwa kuacha kushangaa kuwa Diallo ambaye alikuwa Naibu Waziri na Mbunge wakati filamu hiyo inatengenezwa na kutolewa mwaka juzi,angeweza kuwa na kisingizio cha kuakaa kimya katika awamu iliyopita kwa vile hakuwa wizara inayohusika na samaki au mapanki.Sasa ndio yuko wizara husika na yeye anatoka Mwanza.Kwanini alikuwa kimya muda wote huu?Kwanini kwa mfano,wataalam wa kompyuta wa wizara yake hawakuweka msimamo wa serikali alipoingia madarakani badala ya kusubiri kauli ya Rais?Naomba nisisitize tena kuwa namtaja Diallo kwa vile ni wa kutoka Mwanza na Wizara yake ndio inahusika na mambo ya samaki,na Darwin’s Nightmare imegusia maeneo hayohayo:Mwanza na samaki (mapanki).Na Zakia Meghji nae si ndiye alikuwa waziri wakati huo?Japo si mwenyeji wa Mwanza lakini yeye ni Mtanzania,na alipaswa pamoja na watendaji wake kuzuia utengenezaji wa filamu hiyo (iwapo ilikuwa muhimu kufanya hivyo) na iwapo Hubert Sauper alidanganya dhamira yake,basi Meghji na timu yake walipaswa kuwa wa kwanza kuizungumzia filamu hiyo.Waziri wa Maliasili na Utalii ni miongoni mwa wenye dhamana ya kulinda na kutetea vivutio vyetu (maliasili) na kuvutia wanaotaka kutembelea nchi yetu (watalii).Ina maana kabla ya kauli ya Rais Kikwete Mengji na baadaye Dialo walikuwa hawajui lolote kuhusu filamu hiyo?

Kuna mlolongo wa watu wengine kadhaa ambao kimsingi walikuwepo wakati filamu hiyo inatengenezwa na walikuwa wanajua kabisa maudhui yake,lakini hatujawahi kuwasikia wakisema lolote kuhusu filamu hiyo.Hivi viongozi wa serikali ya Awamu ya Tatu walikuwa hawajui kabisa kuwa kuna mtu anatengeneza filamu ambayo inaweza kuchafua jina la nchi?Sauper hakuja kwa kutumia ungo na kutengeneza filamu hiyo usiku wa manane,kisha kuondoka tena kwa ungo alfajiri.Aliomba viza kwenye ubalozi wa Tanzania huko alikotoka,alieleza anachokwenda kukifanya Tanzania,na akapewa viza na maofisa ubalozi ambao pia ni Watanzania.Aliingia Tanzania kupitia sehemu ambazo zinadhibiti wageni,yaani jamaa wa Idara ya Uhamiaji walimruhusu jamaa huyu.Wizara na mamlaka husika huko Mwanza zitakuwa zilimpatia kibali cha kutengeneza filamu hiyo baada ya kuelezwa maudhui ya filamu hiyo.Sasa hawa wote waliohusika wamekuwa wapi siku zote hizi?Kuwalaumu washiriki wazawa kwenye filamu hiyo ni kuwaonea.Wao walikuwa wanataka malipo ya ushiriki kwenye filamu hiyo.Na kwanini wasishiriki kama serikali yao ilimpa ruhusa mtengenezaji kuendelea na kazi hiyo?Eti tovuti ya Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa anakotoka Sauper ndio nayo imezinduka kueleza “ukweli” kuhusu filamu hiyo.Watueleze kwanini walimpa viza huyu jamaa,au ndio wanataka kutueleza kwamba hawana namna yoyote ya kuthibitisha dhamira halisi ya wageni wanaoomba kuja Tanzania?Mungu aepushie mbali,lakini hivi Sauper angekuwa ndio gaidi Osama sijui ingekuwaje!!!

Haiwezekani kila jambo lisubiri tamko la Rais wakati kuna lundo la watu wanaolipwa mishahara minono na kutembelea mashangingi lakini hawawajibiki ipasavyo.Nimesikia kuwa kuna tume imeundwa kufuatilia sakata la filamu hiyo.Bila kuathiri utendaji wa tume hiyo nadhani makala hii itakuwa na msaada kwao,na ni matarajio yetu kuwa matokeo ya tume hiyo hayatamwonea haya mhusika yoyote yule.Ukweli au unafiki wa Darwin Naitimea hautofautiani sana na ule wa kwenye Davinchi Kodi.Inategemea unataka kumwamini nani na nini na kwa sababu gani.Lakini tunaloweza kukubaliana ni kwamba hawa wanaolala mpaka wakurupushwe na kauli za Rais ni watu wanaoweza kukwamisha kasi mpya,nguvu mpya na ari mpya ya serikali ya Jakaya.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.