6 May 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-61

Asalam aleykum,

Hapa Scotland kuna mrindimo wa furaha kwa chama cha Scottish Nationalist Party (SNP) ambacho kwa namna flani kina mrengo wa kujitenga kutoka katika himaya ijulikanayo kama the United Kingdom au UK.Chama hicho kimefanikiwa kukibwaga chama kilichokuwa tawala cha Labour na hivyo kuvunja historia ya takriban nusu karne ya utawala wa chama hicho cha Tony Blair.Moja ya kete ambazo zilikuwa zikitumiwa sana na Labour “kuipiga madongo” SNP na kiongozi wake Alec Salmond ilikuwa ni suala la uhuru wa Scotland. Labour walikuwa wanadai kwamba Salmond na SNP yake wana ajenda moja tu ya kuiondoa Scotland kwenye Muungano unaounda UK.Unaweza kudhani kuwa hilo ni jambo dogo.Umekosea,kwani suala hilo ni nyeti sana.Wachambuzi wa siasa wananyumbulisha kwamba hisia za Waskotishi kuhusu uhuru zimegawanyika sana.Dereva mmoja wa teksi aliniambia kwamba pengine kinacholeta hisia za mgawanyiko ni ile hali ya kutokuwa na uhakika kama kweli Scotland inaweza kusimama kama taifa pekee nje ya UK.Sio siri kwamba Scotland ina utajiri wake wa asili hususan mafuta,lakini baadhi ya wachumi wanadai kuwa mafuta pekee hayawezi kuifanya sehemu hii ya UK ikajitegemea kwa asilimia 100.Pia kuna suala la mwingiliano wa kijamii na kiutamaduni.Pamoja na historia tofauti kati ya sehemu nne zinazounda UK,yaani Ireland ya Kaskazini,Wales,England na Scotland,bado “nchi” hizi nne “zinashea” mambo kadhaa kihistoria,japokuwa historia hiyohiyo ndio inayowapa baadhi ya watu kuwa na mawazo ya kutaka uhuru.

Hadi wakati naandaa makala hii bado haijafahamika nani atakuwa Waziri Mkuu (First Minister) wa Scotland hasa kwa vile SNP imeishinda Labour kwa tofauti ya kiti kimoja tu.Ili SNP waunde serikali inawalazimu washirikiane na chama kingine ili kupata viti vya kutosha zaidi kuunda serikali.Lakini dalili zinaonyesha kuwa Salmond anaweza kumrithi Waziri Mkuu wa sasa Jack McConnell.Kinacholeta ugumu kwa SNP kupata mshirika wa kuunda nae serikali ni suala hilohilo la uhuru wa Scotland.Vyama vingine vilivyopata viti vya kutosha,ukiacha SNP na Labour,ni Scottish Liberal Party na Scottish Conservatives,lakini vyote hivyo haviafiki kabisa hoja ya uhuru wa Scotland,na ili kuunda umoja wa kuunda serikali ni muhimu kwa vyama kuwa na sera ambazo hazitofautiani sana.Natumaini nitawapa picha kamili kwenye makala ijayo.Kinachonivutia kuhusu SNP ni siasa zake za mrengo wa kushoto ikiwa ni pamoja na upinzani wake mkali dhidi ya vita ya Irak.Pengine hili litakusaidia msomaji kutambua kuwa mtizamo wangu kisiasa ni wa kiliberali (liberal) na unaelemea zaidi kushoto kuliko kulia au kati.

Jingine lililovuta hisia za watu hapa ni hukumu dhidi ya Waingereza flani wenye asili ya Pakistani ambao walihukumiwa kwenda jela kwa miaka kadhaa baada ya kukutwa na hatia ya kupanga mashambulizi ya kigaidi kwa kutumia mabomu yaliyotokana na mbolea.Shirika la Ujasusi la hapa (MI5) nalo lilijikuta linakalia kitimoto kwa vile pamoja na ukweli kwamba lilifanikiwa kufuatilia nyendo za magaidi hao lilishindwa kwa namna flani kuwazuia washirika wao wengine waliofanikiwa kufanya mashambulizi ya kigaidi jijini London tarehe 7 Julai 2005.MI5 iliweza kunasa (ku-bug) maongezi ya magaidi hao na katika kipindi flani magaidi waliofungwa waliwahi kukutana na wale waliojilipua Julai 7 lakini haifahamiki ilikuwaje wakaweza kuwadhibiti hao walioko jela sasa na kuwashindwa hao waliojilipua.Hata hivyo,wajuzi wa mambo ya intelejensia (ushushushu) wanasema kuwa gaidi anahitaji nafasi ya sekunde moja tu “kufanya kweli” wakati taasisi za kuzuia ugaidi zinahitaji kila nafasi kuhakikisha madhara hayatokei.Ni rahisi sana kuwalaumu wanausalama pindi inapotokea balaa lakini ukweli ni kwamba watu hao wanakaa macho masaa 24 kuhakikisha wananchi wanaendelea kuwa salama.

Tayari Marekani imeshatahadharisha kuwa inaweza kuwazuia Waingereza wenye asili ya Pakistan wasiingie nchi hiyo (Marekani) bila viza (Waingereza hawahitaji viza kuingia Marekani iwapo hati zao za kusafiria zinasomeka kwenye mitambo maalumu).Inasemekana kuwa Wizara ya Usalama wa Ndani wa Marekani (Homeland Security) inasubiri Tony Blair ang’atuke tu kisha watangaze hatua hiyo ambayo inatarajiwa kuwaudhi sana Waingereza wenye asili ya Pakistani.Marekani inadai kuwa lengo lake sio kuwabagua Waingereza kutokana ana asili zao lakini inaona kuwa kuna tishio kubwa la ugaidi kutoka kwa Waingereza wenye asili ya Pakistani.

Na hapo ndipo napolazimika kuonyesha wasiwasi wangu kuhusu taarifa za hivi karibuni huko nyumbani kwamba mamia ya askari wa Kisomali wamekamatwa katika maeneo mbalimbali nchini.Nadhani kuna tishio la msingi na la kweli kutoka,sio kwa Wasomali tu,bali hata hao raia wengine ambao kuwepo kwao nchini hakueleweki vizuri.Unajua uchungu wa nchi ni kitu flani nyeti sana.Na uchungu wa nchi sio kitu ambacho kinajitokeza tu.Hapana,ni kitu kinachohusiana na historia ya mtu pamoja na asili yake.Bila kutaka kuleta hisia za kibaguzi,yayumkinika kuamini kuwa Mrundi,Mnyarwanda,Mkongomani au Msomali hawezi kuwa na uchungu sawa wa Tanzania sawa na Mndamba mie wa Ifakara au rafiki yangu Matiku anayetokea kule Musoma.Uchungu wa mgeni ni tofauti na ule wa mwenye nyumba.Wasiwasi wangu kwa hawa wageni wetu ni ukweli kwamba wengi wao wametoka katika mazingira ya vita na mfarakano wa wenyewe kwa wenyewe.Sie ni wakarimu lakini hekima zinatuasa kuwa ukarimu haupaswi kuzidi uwezo au kwa lugha nyepesi tuseme ukiwa na mke mrembo yakupasa kuwa makini na wageni wa kiume unaowakaribisha nyumbani.Nchi yetu ni kisiwa cha amani na hatuna budi kukilinda kwa nguvu zetu zote ili kiendelee kuwa hivyo.

Hawa Wasomali ambao wamekuwa wakichinjana wao kwa wao kwa miongo kadhaa sasa wanapaswa kudhibitiwa sana.Atakayelalamika arudi kwao kwa vile sio hatujazowea kuona watu wakikimbizana mitaani na majambia mikononi.Lakini pia huu ni wakati mwafaka wa kuangalia suala la uzalendo hasa kwa ndugu zetu tuliowakabidhi majukumu ya kulinda mipaka yetu,hususana watu wa Idara ya Uhamiaji.Sio siri kwamba siku za nyuma tumesikia malamiko kibao kuhusu baadhi ya watendaji wasio waadilifu wa Uhamiaji ambao wamekuwa wakiwaruhusu wageni kuingia nchini na kuishi isivyo halali.Hilo halihitaji mjadala bali kukaza buti zaidi.Atakayepokea “kitu kidogo” na kuwaruhusu Banyamulenge au Wasomali waingie nchini isivyo halali ajue kuwa tamaa yake ya fedha itaichafua nchi yetu ambayo ndimo ilipo familia yake huyo mpokea rushwa.

Lakini jukumu la kudhibiti wageni sio la Uhamiaji pekee.Kila Mtanzania anatakiwa kuhakikisha kuwa kila raia wa kigeni aliyepo nchini mwetu yuko hapo kihalali.Ndio tunavyoishi huku kwenye nchi za watu.Na huku suala la ukazi (residency) au uraia ni nyeti sana hasa katika zama hizi za matishio ya ugaidi.Japo mie ni miongoni mwa wale wanaojiita “raia wa dunia nzima” (global citizen) bado naamini kuwa sheria za uhamiaji zinapaswa kuheshimiwa kwa asilimia zote.Wenye nyumba za kulala wageni wanaoendekeza fedha bila kujali wateja wao wametokea wapi wanapaswa watambue kuwa kwa kufanya hivyo wanaweza kulaza magaidi kwenye “gesti hauzi” hizo,na akinadada wanaohifadhi “mabuzi kutoka ng’ambo” wanapaswa kuelewa kuwa uhai wa Taifa ni muhimu kuliko starehe za muda mfupi.Kadhalika,walimiki wa bendi za dansi wanaoamua kupuuza vipaji vya nyumbani na kung’ang’ania “mapapaa wa kutosha muziki mpaka jana yake” wanapaswa kuhakikisha kuwa wanamuziki hao sio majasusi wa Kibanyamulenge.Vilevile,wale waajiri wanaodhani ili kampuni zao zionekane za kimataifa ni lazima ziwe watumishi wa kutoka nje ya nchi wanapaswa kuhakikisha kuwa “ma-TX” hao wamekuja kwa ajili ya ajira kweli na si vinginevyo.

Kwa vile wenye mamsapu warembo hawazembei na kukaribisha wageni hovyohovyo kwa hofu ya “kupinduliwa” nasi Watanzania hatuna budi kuwa makini na taifa letu lenye urembo wa asili wa amani na utulivu.

1 comment:

  1. h a hha mkuu nimekusomaa... ni
    kweli na wala si uongo..
    leo nimepita tena hapa kuchota mavumba kutoka kwakoo...
    h ahaa

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.