6 Jul 2007

Asalam aleykum,

Hivi karibuni niliona habari flani kwenye kituo cha runinga cha Aljazeera English ambayo kwa hakika iliniacha na uchungu mkubwa.Habari hiyo iliyokuwa kwenye kipindi kiitwacho “Witness” cha mtangazaji mahiri Rageh Omar,ilihusu unyama uliofanywa na majeshi ya Marekani huko Vietnam wakati wa vita kati ya nchi hizo mbili.Katika kipindi hicho zilionyeshwa picha za watoto wanaozaliwa wakiwa na maumbile ya kutisha na watu wazima wenye magonjwa yasiyoelezeka kirahisi.Yote hayo ni matokeo ya kemikali iliyonyunyizwa kutoka angani na ndege za jeshi la Marekani kwa lengo la kuwadhibiti wapiganaji wa Kivietnman (vietkong).Kemikali hiyo iitwayo “Agent Orange” iliponyunyizwa iliachia kemikali nyingine ya sumu iitwayo “dioxin” ambayo madhara yake yanaendelea nchini Vietnam hadi leo hii.Kuna watoto wanaozaliwa wakiwa na vichwa vikubwa kuliko miili yao huku wengine wakiwa wamezaliwa bila viungo muhimu kama mikono au miguu.

Marekani iliamua kutumia “Agent Orange” kama njia ya kuwafichua wapiganaji wa msituni wa Vietnam ambao kwa hakika walikuwa mahiri sana katika kushambulia kwa kushtukiza huku wakijificha kwa kuyatumia vizuri mazingira yanayowazunguka.Lengo la kitendo hicho kisicho cha kibinadamu lilikuwa kuteketeza uoto wa asili ili wapiganaji wa Vietnam wasiwe na mahali pa kujificha.Licha ya madhara ya kiafya kwa binadamu,matumizi ya “Agent Orange” yameacha athari kubwa za kimazingira kwani baadhi ya maeneo ambayo awali yalikuwa misitu sasa yamebaki yakiwa “tasa” mithili ya jangwa.Kikemikali, “Agent Orange” ni mchanganyiko wa tindikali mbili za kuua mimea (2,4-D na 2,4,5-T) ambazo zina tabia ya kuiga mfumo wa ukuaji wa kiumbe,lakini zinaiga mfumo huo sio kwa lengo la kuusaidia ukue bali kuuharibu.Enewei,hayo ni mambo ya kimaabara na pengine hapa sio mahala pake.

Katika makala yangu moja ya hivi karibuni niliandika kuhusu jinsi baadhi ya waandaa sera wa Marekani wanavyopenda kutoa maamuzi yatakayoleta matokeo ya haraka pasipo kuangalia madhara ya muda mrefu.Nilitolea mfano taarifa kwamba jeshi la Marekani huko Iraki lilikuwa na mpango wa kuwapatia msaada wapiganaji wa madhehebu ya Sunni ili wakabiliane na wapiganaji wa kikindi cha Al-Qaeda nchini humo.Katika makala hiyo nilitoa mifano kadhaa ya namna maamuzi ya kukurupuka ya Marekani yalivyochangia kuzaliwa na kuimarika kwa kikundi cha Al-Qaeda.Ni vichaa flani waliodhani kwamba kumwaga sumu huko Vietnam kungeleta ushindi wa chapchap,vichaa walioamini katika matokeo pasipo kujali athari za muda mrefu za matokeo hayo.Pia Marekani inaonekana kuwa mahiri sana katika kutafuta ushindi wa vita lakini iko dhaifu katika kuleta amani.Kwa lugha ya kwa mama wanasema “to win the war but lose the peace.”Ni hivi,watapiga mabomu na kuteketeza vijiji huko Iraki hadi wachoke wenyewe.Wakiamini kuwa wameshinda mapambano,vinachipuka vizazi vyenye chuki ambavyo vimepoteza wazazi na jamaa zao.Vizazi hivyo vya chuki vinabaki kuwa hifadhi ya jeshi la wapiganaji wa vita vijavyo (reserve army of future fighters).Ni dhahiri kuwa mzazi yeyote wa Kivietnam ambaye atajifungua mtoto mwenye mtindio wa maumbile uliosababishwa na athari za muda mrefu za “Agent Orange” atakuwa na chuki ya milele dhidi ya Wamarekani.


Nigeukie huko nyumbani.Hivi ni lini kutakuwa na uungwana kwa baadhi ya Watanzania wenzetu ambao kwa namna moja au nyingine wanatajwa kuhusiaka na skandali flani?Hapa namzungumzia Gavana wetu wa BOT.Sijamsikia hata siku moja akikanusha tuhuma dhidi yake japo naamini anafahamu kuwa zinamchafulia jina lake,uaminifu wake na wa taasisi anayoongoza.Dawa ya kukabiliana na tuhuma sio kuzipuuza,au kwa mtindo uliozoeleka huko nyumbani,kuzua tuhuma dhidi ya aliyekutuhumu.Dawa ni kujibu tuhuma hizo aidha kwa kuzungumzia na vyombo vya habari au kwenda mahakamani kudai mtoa tuhuma athibitishe anachozungumza.Mfano mzuri hapa ni namna aliyekuwa Waziri Mkuu katika awamu iliyopita alivyoamua kushughulikia tuhuma dhidi yake.Akirejea kutoka masomoni Havard,Fred Sumaye alieleza kuwa anawashangaa wanasheria wake kwa kuchelewa kufuatilia hatua za kisheria anazotaka kuzichukua dhidi ya wanaomtuhumu.Japo sijui kama kesi hiyo ishafunguliwa au la,na kama imeshafunguliwa walalamikiwa ni akina nani,lakini la muhimu hapa ni kwamba Sumaye ameamua kujibu tuhuma zake kwa njia za kisheria.Na hivyo ndivyo inavyopaswa kufanyika kwani kukaa kimya kunaweza kumaanisha kuwa mtuhumiwa anakubaliana na tuhuma hizo.

Nikuchekeshe(au nikuudhi) kidogo na moja ya mifano yangu ya ajabuajabu.Ni hivi,kwenye mbinu za medani za mtaani kuna imani miongoni mwa vijana wa kiume kuwa wakitongoza binti halafu akawa kimya bila kusema amekubali au hataki basi wajuzi wa fani hiyo wanasema kuwa hiyo ni dalili ya kukubaliwa.Yaani,kimya ni sawa na “yes” lakini mlengwa anaona aibu kutamka hivyo.Ok,ni mfano wa kizembe lakini unaweza kuwa na mantiki katika nachozungumzia hapa.Iweje kwamba mtu aliyepewa dhamana ya kushikilia uchumi wetu atuhumiwe kuwa anahusiaka na ulaji wa mabilioni ya dola katika mpango wa msamaha wa madeni na ujenzi wa Twin Towers,lakini akae kimya kana kwamba yanayosemwa hayamhusu yeye.Inawezekana ni dharau dhidi ya hao wanamtuhumu lakini kama filosofia yetu ya kutongoza (kwamba kukaa kimya maana yake ni kukubaliwa) ina mantiki ya kutosha,basi kimya cha Gavana kinaweza kutupa majibu ya maswali mengi tuliyonayo kuhusu skandali hizo.

Baada ya kutaja Twin Towers ndio nikakumbuka swali moja.Tunaambiwa kuwa Benki Kuu ni taasisi inayopaswa kuwa na heshima na hadhi kubwa.Na nadhani katika kuonyesha hadhi hiyo,likaja wazo la kuwa na Twin Towers.Hivi kungekuwa na dhambi gani kama BOT ingeendelea kuwa kama ilivyokuwa kabla ya ujenzi wa Twin Towers halafu hayo mamilioni ya dola yangepelekwa kujenga daraja la kisasa pale Kigamboni?Licha ya kuepusha balaa linaloweza kutokea siku yoyote ile kutokana na kutegemea feri zilizochoka,daraja hilo lingeweza kuwa alama ya jiji na kivutio cha utalii kama zilivyo alama za majiji mengine duniani kama “Jicho la London” (London Eye),jengo la opera la Sydney (Sydney Opera House,Australia),Taj Mahal huko India,mnara wa Eiffel hapo Paris,au Mnara wa Uhuru (Statue of Liberty) huko New York.Wakati hawa wenzetu wana uwezo wa kujenga vivutio kwa ajili ya “kujifurahisha” tu,sie masikini hatuna uwezo huo na hatupaswi kuwa na mawazo ya kitajiri wakati tungali masikini.Kwa mantiki hiyo,sio busara sana kuwa na jengo “bomba” kama Twin Towers za BOT kwa ajili ya kufurahisha macho ya wachache wenye muda wa kuyaangalia maghorofa hayo (ukiwa na njaa,huna nauli,utamudu kutoka Kimbiji kuja “kushangaa” Twin Towers?) ilhali tungeweza kutumia kidogo tulicho nacho kutengeneza utambulisho wa jiji letu (zaidi ya kile kisanamu cha Bismin) na kuwarejeshea imani wakazi wa Kigamboni kuwa ahadi za wanasiasa huwa zinatekelezeka (daraja hilo limeshaahidiwa mara nyingi zaidi ya ahadi za wagombea uongozi wa klabu ya Yanga walivyoahidi kugeuza Uwanja wa Kaunda kuwa wa kisasa au wale wa Simba wanaoahidi kujenga “wanja” kubwa zaidi ya ule wa watani wao wa jadi).

Mwisho,napenda kuuliza tena:hivi msimamo wa Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana ni upi kuhusu sakata linaloendelea huko Dodoma ambako baadhi ya waumini hawaafikiani na Askofu wa Dayosisi ya Kati katika msimamo wake wa kuunga mkono ushoga.Hivi anadhani mambo yatatulia kwa yeye kukaa kimya?Hivi ni nani aliyetuambia kuwa ukimya ni njia mwafaka ya kupata majibu ya maswali magumu yanayoikabili jamii yetu?Nilishtuka nilipoona picha ya askari wakitoa ulinzi ili Askofu Mhogolo aweze kuendeshwa ibada ya kipaimara.Japo mie si mjuzi hata kidogo kwenye kusoma Biblia lakini sijawahi kusikia kuwa Yesu alihitaji askari kuendeshwa shughuli zake za kuleta ukombozi kwa kondoo wake.Nguvu za dola zikitumika kudhibiti kondoo wa Bwana basi ni dhahiri kuwa “siku za kurejea Bwana zimekaribia.”Na bora arejee mapema kwani inaelekea baadhi ya alowakabidhi majukumu ya kumtumikia wameweka mbele maslahi yao kuliko ya kondoo wanaopaswa kuwachunga.Ole wenu,msije siku ya kiama mkageuzwa kuwa kuni za kuchochea moto wa milele dhidi ya wala rushwa,wazinzi,matapeli,watoa ahadi za uongo na maharamia wengine.


Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.