8 Dec 2008


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, ameonya kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinaweza kusambaratika ikiwa uadui uliopo ndani yake unaoendelezwa na makundi hautadhibitiwa. 

Membe alisema uadui huo unasababishwa na vitendo kama vile hujuma za kuangushana katika kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika chama hicho. 

Waziri huyo alitoa kauli hiyo jana wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Dar es Salaam. 

Membe, ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu (CC) ya CCM, alisema ni dhana potofu kuamini kuwa uadui wa aina hiyo unasababishwa na vyama vya upinzani. 

``Maadui wapo ndani, ni wenzetu sisi wenyewe, tunakaa nao lakini wanashiriki kupanga kuangushana, majungu yamekithiri hiyo ni kielelezo cha ugonjwa wa chama kusambaratika,`` alionya Membe ambaye pia ni Katibu wa Idara ya Mambo ya Nje ya CCM. 

Membe, alisema uzoefu ywa miaka miwili aliopata tangu ateuliwe kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, umemuonyesha kuwa vyama vingi vilivyotawala kwa muda mrefu vinaweza kuondoka madarakani kutokana na udhaifu uliopo, na si nguvu ya upinzani. 

``Mara nyingi sana vyama tawala vinajiua vyenyewe, si kwa sababu ya upinzani,`` alisema Mbunge huyo wa Mtama,. 

`` Tunapotafunana, kutoaminiana, kama CCM na jumuiya zake hatushikamani, tukagawanyika, hatuwezi kuwa chama imara, tutameguka,`` alisema. 

Membe alisema machafuko yanayotokea baada ya chaguzi barani Afrika, yanachochewa na kasumba ya kutokukubali matokeo. 

Alisema hali hiyo inawafanya watu wengine kuingia msituni ama kufikia hatua ya kufanya mapinduzi ya kijeshi. 

Alitoa mfano kuwa katika kipindi cha takribani miaka 50, viongozi 32 barani Afrika, waliuawa kutokana na mapinduzi ya kijeshi yaliyofanywa katika nchi zao na kwamba vyama vilivyopo madarakani, vina fursa nyingi za kufanikisha kubaki katika uongozi. 

Kwa mujibu wa Membe, baadhi ya fursa hizo ni kueleweka kwa sera zake, uwepo wa viongozi bora na jumuiya imara. 

Wakati Membe akitoa tahadhari hiyo, baadhi ya wajumbe wa mkutano huo nusura wapigane hadharani, kutokana na tofauti za kuwaunga mkono wagombea katika nafasi mbalimbali za UVCCM Mkoa wa Dar es Salaam. 
Hali hiyo ilijitokeza jana asubuhi, kabla ya Membe kuwasili kufungua mkutano huo. 

Taarifa za ndani zilidai kuwa kundi linalomuunga mkono mmoja wa wagombea wa uenyekiti, lilipanga njama za kuhujumu uchaguzi huo ili kutoa fursa kwa `mtu wao` kushinda. 

Miongoni mwa hujuma hizo, ni kusimamishwa kwa wajumbe zaidi ya 10, ili wasishiriki kupiga kura. 
Hata hivyo, baada ya kugundulika, baadhi ya vijana kutoka wilaya za Kinondoni, Ilala na Temeke, waligoma kuingia ukumbini. 

``Hatuingii ukumbini kama wenzetu waliosimamishwa hawatapewa vitambulisho, hatukubali kuburuzwa,`` walisikika baadhi yao wakisema. 

Hakuna kiongozi yeyote wa UVCCM Mkoa wa Dar es Salaam, aliyekuwa tayari kuzungumzia suala hilo, isipokuwa wanachama wengine wa umoja huo walisikika wakilalamikia kundi walilodai kwamba liliongozwa na mmoja wao. 

Baadaye, taarifa zilieleza kuwa vijana waliozuiwa kupiga kura, waliruhusiwa na kupewa vitambulisho.

CHANZO: Nipashe

WAKITAHARIDHISHANA WENYEWE INAKUWA SALAMA,MAANA KAZI HIYO IKIFANYWA NA WACHAMBUZI WA SIASA WANAISHIA KUNYOOSHEWA VIDOLE WAKITUHUMIWA KWA UCHOCHEZI.

JAPO MEMBE ANASTAHILI PONGEZI KWA KUJITOA MHANGA KUSEMA HAYO ALOSEMA NDANI YA CHAMA KILICHOZOWEA KUSIFIWA TU HUKU CRITICISM YA AINA YOYOTE IKITAFSIRIWA KUWA NI MITHILI YA UHAINI,ALIPASWA PIA KUONGELEA NAMNA CCM INAVYOJIMALIZA KWA KUKUMBATIA MFUMO  USIO RASMI AMBAPO ASIYE NA FEDHA HAWEZI KUSHINDA CHAGUZI YOYOTE YA CHAMA HICHO.RUSHWA IMEKITHIRI MNO NDANI YA CHAMA HICHO KIKONGWE.

MADHARA YA MUDA MFUPI (IMMEDIATE) YA RUSHWA KATIKA CHAGUZI HIZO NI NI PAMOJA NA UWEZEKANO WA KUPATA VIONGOZI WASIO NA SIFA STAHILI NA AMBAO WANAWEZA KUTOWAJIBIKA IPASAVYO KWA VILE WANAJIONA KAMA WAMENUNUA UONGOZI NA WANA HAKI YA KUFANYA MAMBO WAPENDAVYO.MADHARA YA MUDA MREFU (LONG TERM) NI REPRODUCTION YA MAFISADI.CCM NDIO CHANZO KIKUBWA CHA VIONGOZI WA NGAZI MBALIMBALI NCHINI.KWA MAANA HIYO,CHAMA HICHO KIKIZEMBEA KAMA SASA NA KUACHIA VIONGOZI WAPATIKANE KWA NJIA YA RUSHWA BASI TAIFA NALO LITAENDELEA KUPATA SUPPLY KUBWA YA VIONGOZI WALIONUNUA CHAGUZI AMBAO HAWATASHINDWA KULIFISADI TAIFA.

HABARI MBAYA NI KWAMBA HAKUNA DALILI YA CCM KUPAMBANA NA RUSHWA KATIKA CHAGUZI ZA CHAMA HICHO.NA KIKWAZO KIKUBWA CHA JITIHADA HIZO NI HIZI SIASA MUFILISI ZA MITANDAO.KWAMBA,UKIJITAHIDI KUSIMAMIA HAKI UTALIPULIWA NA WALE WANAOJUA UMEFIKAJE HAPO ULIPO.NDIO MAANA WANASIASA MAKINI HUJITAHIDI SANA KUEPUKA MAKUNDI YA KUSAIDIA USHINDI KWA VILE KUJIHUSISHA NAYO HUMGEUZA MWANASIASA HUSIKA KUWA MTUMWA WA MAKUNDI YA AINA HIYO.

1 comment:

  1. kaka hapo kazi pio kwani siku zote wanakanusha huku mambo yanajidhihirisha yenyewe, sasa kuongea membe mpaka leo nilikuwa nangojea kama kutakuwa na ukanushaji maana wamezoea lakini wapi mambo yamekuwa kama yalivyo.
    ANC tayari badi CCM{chai, chapati, maharage] kwa mujibu wa Prof. Richard Mabala

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.