26 Jun 2012



TAARIFA KWA UMMA
UBAGUZI UNAOFANYWA NA SERIKALI KWA VIONGOZI WETU NGAZI YA CHINI

Ndugu wanahabari

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kupitia Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi inapenda kutoa taarifa kwa umma na kukemea ubaguzi unaofanywa na baadhi ya watendaji wa serikali dhidi ya viongozi wa vyama vya siasa, hususan wale wa chama kikuu cha upinzani na chama mbadala, CHADEMA.

Chama kupitia Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi kimepata taarifa kutoka ngazi ya chini ya uongozi, yaani misingi na matawi kwamba mabalozi wa nyumba kumi wa CHADEMA wamekuwa wakibaguliwa katika utendaji kazi wao wa kila siku na watendaji wa serikali, huku watumishi hao wakiendelea kutoa ushirikiano kwa mabalozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ndugu wanahabari kupitia kwenu, tunaomba umma wa Watanzania ufahamu mambo mawili muhimu hapa;

Kwanza; balozi wa nyumba kumi wa chama cha siasa si sehemu ya uongozi wa kiserikali. Suala hili limewahi kusisitizwa na serikali yenyewe kwa kutoa kauli bungeni. Ngazi rasmi ya uongozi wa kiserikali inaanzia serikali za mitaa/kitongoji.

Lakini pia suala hili la ngazi za uongozi wa kiserikali na kuwa mabalozi si sehemu ya uongozi huo linaoneshwa pia katika katiba yetu ya sasa (pamoja na ubovu wake uliotusukuma tudai iandikwe upya).

Pili; Sheria ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992, inavitambua vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu kuwa vyote viko sawa mbele ya sheria. Halikadhalika  kutokana na sheria hiyo, katiba za vyama vyote vya siasa ni sawa, hasa baada ya kuwasilishwa na kupitishwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa na kupitishwa.

Kwa mantiki ya masuala hayo mwili hapo juu, Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi, inatumia fursa hii kutoa tamko kwa umma kuwa mabalozi wa CHADEMA na CCM, wana haki sawa mbele ya sheria, kwa sababu wanatokana na vyama vilivyo sawa mbele ya sheria, halikadhalika katiba za vyama hivyo ziko sawa mbele ya sheria.

Mabalozi wa CHADEMA wanapatikana kwa mujibu wa Katiba Mpya ya Chama ya Mwaka 2006, Sura ya Saba, ambayo inazungumzia ngazi, uongozi na majukumu ya vikao.

Tofauti pekee ya mabalozi wa CHADEMA na CCM ni kwamba mabalozi wa CHADEMA wanavaa magwanda wale wa CCM wanavaa magamba. Lakini pia wanatofauti ya tabia;
Mabalozi wetu wanasimamia ukweli, wakati wale wa CCM wanasimamia uongo, mabalozi wa CHADEMA wanasimamia uadilifu, wale wa CCM wanasimamia ufisadi, wakati mabalozi wetu wanasimamia na kutumikia wananchi, wale wa CCM wanatumikia maslahi ya chama chao na yao binafsi.

Pamoja na kazi zingine, baadhi ya majukumu ya balozi wa CHADEMA ni pamoja na kuwa mwakilishi wa chama na wanachama. Ana wajibu wa kuwatambua wanachama wenzake, wananchi wote na pia anaufahamu wa kutosha wa masuala mbalimbali katika eneo lake la nyumba kumi.

Tunasema hivyo kwa sababu wakati mwingine kutokana na kukosa mtandao mpana mpaka chini katika kaya za watu na wakati mwingine ukubwa wa maeneo ya kitongoji/mtaa unakuwa kikwazo, mamlaka za serikali katika kutekeleza majukumu mbalimbali zinashindwa  kumtambua kila mwananchi, hivyo zinalazimika kuhitaji mtu/watu wa kusaidia kazi hiyo katika nafasi za uongozi walizoaminiwa katika maeneo madogo ambayo ni rahisi watu kutambuana. Hapo ndiyo dhana ya kuwa na kiongozi wa kaya kadhaa kwa jina la balozi unatokea.

Mabalozi wetu CHADEMA kwa sababu wanatokana na taasisi inayotambulika kisheria, makini na imara wanafanya kazi kwa barua na mhuri wa chama.

Kupitia tamko hili, Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi ya CHADEMA, inawataka watendaji wa ngazi zote wa serikali kuacha mara moja tabia ya kuwabagua mabalozi wa CHADEMA kwani wanatokana na watu, wanatambua na wanaweza kutimiza wajibu wanaopaswa kufanya.

Chama pia kinatumia fursa hii kutoa mwito kwa mabalozi wote wa CHADEMA nchi nzima ambao wanakutana na vikwazo vya watendaji wa serikali katika kutimiza majukumu yao mbalimbali ya kila siku, watoe taarifa rasmi kwa ngazi za juu zao, ili ngazi hizo husika nazo ziwasilishe kunakohusika, kwa ajili ya chama kuchukua hatua zaidi.

Imetolewa leo Juni 24, 2012 Dar es Salaam na
Msafiri Abdulrahaman Mtemelwa
Mkurugenzi wa Kampeni na Uchaguzi CHADEMA 

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.