22 Apr 2013


KWA mara ya kwanza, Rais Jakaya Kikwete amewabeza watu wote, wanaodai kuwa ameshindwa kuongoza nchi. 
 
Akizungumza na Watanzania waishio nchini Uholanzi na taarifa yake kurushwa na kituo cha runinga cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), mwishoni mwa wiki, Rais Kikwete alisema kamwe hajashindwa kuongoza na kusisitiza kama angeshindwa angechukua uamuzi sahihi.
 

“Sijashindwa kuongoza nchi kama watu wengine wanavyosambaza taarifa za kizushi na fitina, nachojua mimi nchi iko katika mikono salama na ninaimudu.

“Msikae na kusikiliza maneno ya wapuuzi wachache ambao wamekuwa wakieneza maneno yao ya umbea katika mitandao na mikutano ya kisiasa. 
“Ukiacha matukio machache ya uvunjifu wa amani ambayo Serikali yangu imekuwa ikiyashughulikia, tumefanikiwa kudhibiti hali hiyo na Watanzania wanaendelea na shughuli zao kama kawaida,” alisema Rais Kikwete.

Alisema japo kuongoza watu ni kazi ngumu na nzito, lakini yeye binafsi ameweza kuongoza kutokana na kulelewa na kukulia katika maadili mema ya uongozi.

Alisema kutokana na misingi hiyo, haoni haja ya kupigizana kelele na watu ambao hawamtakii mema katika uongozi wake.

Aliwataka Watanzania waishio nchini Uholanzi, kuhakikisha wanakuwa mabalozi wazuri kwa kutangaza vivutio vya utalii na rasilimali zinazopatikana Tanzania ili kuwavutia.

Kuhusiana na migogoro ya kidini ambayo imekuwa ikitokea nchini, Rais Kikwete aliwataka Watanzania kuhakikisha wanaenzi na kulinda tunu ya umoja na amani, iliyoasisiwa na viongozi wake, Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na mwasisi wa Zanzibar, Hayati Sheikh Amani Karume.

“Watanzania tumeachiwa tunu ya amani na umoja kutoka kwa waasisi wa taifa letu, tunapaswa kuienzi, kuilinda na kuidumisha kwa maslahi ya nchi yetu na vizazi vijavyo,” alisema Kikwete.

Kwa muda mrefu, baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakimshutumu Rais Kikwete kuwa nchi imemshinda kutokana na kukumbwa na misukosuko mingi.

Miongoni mwa misukosuko hiyo, ni pamoja na mgomo wa madaktari, mgomo wa walimu, mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), mauaji ya watu, kutekwa na kujeruhiwa vibaya.

Tuhuma nyingine, ni tatizo la kuenea kwa udini ambalo limesababisha vifo kadhaa Tanzania Bara na Zanzibar. 
 
Lakini katika matukio hayo yote Rais Kikwete amekuwa akiyakemea na kuwataka Watanzania waishi kama ndugu.

CHANZO: Mtanzania

ANAKIMBIA KIVULI CHAKE?

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.