3 Jun 2013


THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail:  [email protected]
              [email protected]             

Fax: 255-22-2113425


PRESIDENT’S OFFICE,
      THE STATE HOUSE,
              P.O. BOX 9120,  
DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ban Ki Moon ampongeza Rais Kikwete kuhusu njia mpya ya kuleta amani DRC

KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Mheshimiwa Ban Ki Moon amempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kutoa mapendekezo muhimu na murua ya aina yake ya kuanza kutafuta amani ya kudumu katika eneo la Maziwa Makuu kwa njia ya mazungumzo badala ya kutegemea mapambano ya silaha peke yake.

Aidha, Katbu Mkuu huyo wa UN ameishukuru Tanzania kwa kuchangia askari wa kuunda Brigedi Maalum ya Kusimamia Amani katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na pia kutoa kamanda wa Brigedi hiyo.

Vile vile, Mheshimiwa Ban Ki Moon amemwomba Rais Kikwete kuendelea kuunga mkono jitihada za kuleta amani na utulivu katika DRC na eneo lote la maziwa makuu kupitia Mchakato wa Kanda wa Kusimamia Amani (Regional Oversight Mechanism) katika eneo hilo.

Mheshimiwa Ban Ki Moon ametoa shukrani na pongezi hizo kwa Rais Kikwete wakati viongozi hao walipokutana leo, Jumapili, Juni 2, 2013, kwa mazungumzo wakati wa Mkutano wa Tano wa Tokyo Kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD V) unaoendelea mjini Yokohama, Japan.

Wakati wa mazungumzo hayo kwenye Hoteli ya Intercontinental ambako viongozi hao wamefikia, Mheshimiwa  Ban Ki Moon amemwambia Rais Kikwete: “Nakushukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mchango wako mzuri kwenye mkutano wetu wa Jumapili asubuhi mjini Addis Ababa. Yako yalikuwa mapendekezo bora zaidi na mapya katika mkutano wetu mzuri. Asante sana kwa kuunga mkono Mchakato wa Kanda wa Kusimamia Amani katika eneo la Maziwa Makuu. Tunaomba uendeleaa kuunga mkono Mchakato huu.”

Ameongeza Katibu Mkuu wa UN: “Nilipokuwa Goma karibuni nilikutana na Jenerali kutoka Tanzania ambaye ni Kamanda wa Brigedi Maalum ya Kulinda Amani katika DRC iliyoko chini ya Umoja wa Mataifa. Tunakushukuru sana kwa kuchangia Brigedi hii na tunakushukuru sana kwa kukubali kutoa Kamanda wa Brigedi hii.”
Katibu Mkuu Ban Ki Moon pia amemwalika Rais Kikwete kushiriki katika kikao kijacho cha Mchakato kilichopangwa kufanyika kwenye Umoja wa Mataifa Septemba mwaka huu wakati wa Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa mwaka huu.

“Nakusudia kuitisha kikao kingine cha Mchakato wetu katika wiki kati ya Septemba 20 na 27, mwaka huu, 2013 wakatiwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na napenda kukualika ushiriki katika kikao hiki muhimu sana katika jitihada zetu za kuleta amani katika eneo la Maziwa Makuu na hasa katika Congo,” Mheshimiwa Ban Ki Moon amemwambia Rais Kikwete.

Rais Kikwete amemwambia Katibu Mkuu wa UN kuwa anaendelea kuamini kuwa matumizi ya nguvu za kijeshi na askari peke yake hayataweza kuleta amani katika eneo la Maziwa Makuu ikiwamo DRC.“Huu ndio msimamo ambao niliueleza katika mkutano ule wa Jumapili iliyopita mjini Addis Ababa hata kama baadhi ya watu hawakufurahishwa sana na msimamo huu.”

Tumekuwa tunajaribu kutumia nguvu kuleta amani katika DRC tokea mwaka 1997 na bado mpaka sasa hatujafanikiwa kuleta amani ya kudumu katika nchi hii jirani – tokea wakati huo tumejaribu kuunga mkono uasi mmoja baada ya mwingine lakini bado tuko pale pale na ndiyo maana naamini kuwa wakati umefika wa kuelekeza nguvu zetu katika mazungumzo ya hatua tatu kama nilivyoelekeza katika mkutano ule wa wiki iliyopita.”

Viongozi hao wawili pia wamejadili hali ilivyo katika Madagascar na maandalizi ya uchaguzi mkuu nchini humo. Aidha, viongozi hao wawili walijadili maendeleo ya kisiasa katika Zimbabwe ambako Katibu Mpya imepitishwa na sasa maandalizi yanafanywa kwa ajili ya uchaguzi mkuu nchini humo.

Rais Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuia ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ametoa ufafanuzi wa ndani kuhusu jitihada ambazo zimekuwa  zinafanywa na Asasi yake kuhusu suala la Madagascar baada ya kuwa ameombwa na Mheshimiwa Ban Ki Moon kuhusu jitihada hizo.

Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Ban Ki Moon kuwa viongozi wa SADC watakutana mjini Maputo, Mozambique wiki ijayo kujadili matukio ya karibuni katika Madagascar na maendeleo ya kisissa katika Zimbabwe.

Mapema leo, Rais Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Uchumi, Biashara na Viwanda (METI) wa Japan Mheshimiwa Toshimitsu Motegi.
Katika mkutano huo, Mheshimiwa Motegi ameomba Serikali ya Tanzania kuyasaidia makampuni ya Japan ambayo yanajaribu kuwekeza katika uchumi wa Tanzania. 

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

2 Juni, 2013


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.