6 Jan 2016

Mwaka 1981, nikiwa darasa la tatu, marehemu baba aliamua kustaafu kazi, japo alikuwa amebakiwa na miaka kama 10 hivi ya utumishi katika Shirika la Posta. Wakati huo tulikuwa tunaishi Kigoma. Marehemu baba alikuwa na ndoto za kuwa mkulima mkubwa baada ya kustaafu maana tulikuwa na hekari kama 50 hivi za mashamba ya mpunga huko Ifakara. Kwahiyo, aliamini kuwa savings zake na mafao ya kustaafu vingekuwa mtaji wa kutosha kumwezesha atimize ndoto yake hiyo.

Hata hivyo, wanasema 'kuwa na ndoto ya kitu flani ni kitu kimoja, kuitimiza ndoto hiyo ni kitu kingine kabisa.' Mwaka mmoja baada ya kustaafu na familia yetu kurudi kijijini Ifakara, hali ya uchumi ilikuwa mbaya. Tatizo kubwa lililomkabili marehemu baba ni ukubwa wa ukoo huko kijijini ambao ulimtegemea yeye kwa msaada. Na wazazi wangu, yaani marehemu baba na marehemu mama, walikuwa watu wenye huruma mno. Kwahiyo waliona kuwa hawawezi kuacha kuwasaidia ndugu na ukoo kwa ujumla kwa vile tu wana mipango ya kilimo kikubwa. Pengine si wazo la busara lakini upendo ni kitu chenye nguvu mno na kikizidi chaweza kuvuruga kila mpango.

Maisha yangu kama mwanafunzi hapo Ifakara nilipohamia darasa la tatu hadi nilipomaliza darasa la saba, yalikuwa magumu mno. Kuna nyakati tulipitisha usiku kwa kunywa uji wa chukuchuku (usio na sukari wala chumvi), kuna nyakati tulilalia ndizi bukoba za kuchemsha na kikombe cha maji tu, mlo wa mchana ulikuwa wa kubahatisha, na mara kadhaa mchana ulipita kwa kunywa maji tu. Pia kuna usiku kadhaa tuliokwenda kulala bila kutia kitu tumboni.

Nilisoma kwa shida maana hatukuwa na umeme, japo umeme ulifika Ifakara mapema kabla ya sehemu nyingi za Tanzania kwa vile mradi wa umeme wa Kidatu ulikuwa jirani na mji huo. Familia iliyokuwa inahangaika na mlo wa siku moja isingeweza kumudu gharama za umeme ambazo wakati huo zilikuwa shilingi elfu kadhaa tu. Lakini licha ya kujisomea kwa kutumia koroboi na mara moja moja taa ya chemli pale tulipoweza kumudu kununua mafuta ya taa, Mungu alinijaalia nikafaulu kidato cha nne na kupata division one. Laiti ningefeli, ndio ungekuwa mwisho wa safari yangu kielimu maana familia isingemudu kunisomesha shule ya private.

Nikachaguliwa kujiunga na high school Tabora. Namshukuru Mungu kwani shule hiyo ilikuwa ya mchepuo wa kijeshi, maana niliondoka nyumbani nikiwa na nguo chache tu lakini pale shuleni tulitumia muda mwingi tukiwa kwenye yunifomu zetu za magwanda. Na hapo shuleni nilikwenda mikono mitupu, lakini bahati nzuri marafiki walinisaidia hela za matumizi. Na sikujali sana kwa sababu milishazowea shida.

Bahati ilinijia shuleni hapo nilipofanikiwa kuchaguliwa kuwa kiranja mkuu. Kwa vile ilikuwa shule ya kijeshi, 'cheo' changu kilifahamika kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi, kwa kimombo Students' Chief Commander, au kwa kifupi 'Chief.' Mpaka leo baadhi ya niliosoma nao huko Tabora wameendelea kuniita 'chifu.' Kupata ukiranja mkuu Tabora Boys' ilikuwa sio kazi rahisi hata kidogo. Mfumo wa uchaguzi ulihusisha uraia na ujeshi. Sikuomba kugombea bali nilipendekezwa tu. Na kimsingi haukuwa uchaguzi as such kwa sababu final say ilikuwa ni ya utawala wa shule na maafande. Nikabahatika kupata 'wadhifa' huo nikiweka historia ya kuwa 'chifu' mwenye umri mdogo zaidi katika historia ya shule hiyo (kwa muda huo).

Uchifu ulinisaidia sana kukabiliana na ugumu wa maisha shuleni hapo kwani licha ya privileges kadhaa zilizoambatana na 'wadhifa' huo, pia nilikuwa nikipewa zawadi mbalimbali na wanafunzi wenzangu. Ndo raha za uongozi hizo.

Nilihitimu masomo yangu vizuri na kupata Division Two ya pointi 10. Ninaamini laiti nisingekuwa nakabiliwa na ugumu wa maisha, ningeweza kupata Division One nyingine.

Kutoka hapo nikaenda JKT Maramba, Tanga, na hiyo ilimaanisha maisha mengine ya kijeshi kwa mwaka mzima (ukichanganya na miaka miwili ya ujeshi Tabora Boys'). Lakini bahati ikaendelea kuwa nami kwani baada ya miezi michache tu nikateuliwa kuwa miongoni mwa vijana waliotakiwa kujiunga na Jeshi la Wananchi JWTZ kuwa marubani na mainjinia wa jeshi. Kwahiyo takriban robo tatu ya maisha yangu ya JKT yalikuwa kwenye kambi ya mafunzo ya RTS Kunduchi. Huko ilukwa ni kula na kulala tu tukisubiri utaratibu wa mchujo wa urubani na uinjinia wa jeshi. Mwishowe, sikuchaguliwa na nikarudi JKT Ruvu (kambi ya watoto wa vigogo) kumalizia muda wangu. Hapo napo maisha yalikuwa mtihani kwa sababu licha ya kambi kujaa watoto wa vigogo lakini pia ilikuwa karibu na Dar. Nashukuru Mungu nilipata marafiki kutoka familia zenye kujiweza ambao walinistiri.

Nilipomaliza nikaenda Tanga, na baada ya muda mfupi nikaajiriwa kuwa mwalimu katika sekondari ya Eckenford. Sikupata nafasi ya kujiunga na chuo kikuu mwaka huo kwa vile kwa wakati huo, kujiunga na UDSM ulihitaji Division One ya Form Six, na mie nilikuwa na Division Two ya point 10 (yani kasoro point moja tu kuwa Division One).

Nikafundisha hapo kwa miaka miwili, kisha nikateuliwa kujiunga na Idara ya Usalama wa Taifa. Jinsi nilivyoteuliwa ni kama muujiza, lakini ninahisi walikuwa wakinifuatilia tangu nilipokuwa Tabora Boys' kwa sababu kuna wakati niliwahi kutembelewa na Afisa Usalama wa Taifa wa Mkoa huo.

Baada ya mwaka mmoja wa mafunzo ya kazi hiyo, nikaingia mtaani, lakini kwa vile nilikuwa na kiu ya elimu, baada ya miezi 9  'mtaani' nikachaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hata hivyo, wakati nikiwa chuoni niliendelea na kazi pia. Nilipomaliza nikarudi ofisini na takriban mwaka mmoja baadaye nikapata promosheni iliyodumu hadi nilipoteuliwa kuja kusoma huku Uingereza.

Japo baadaye yalijitokeza matatizo yaliyopelekea mie kuachana na kazi hiyo, utumishi wangu wa miaka 13 mfululizo haukuwa na doa, na ninajivunia rekodi yangu. Kilichoniponza ni kukataa umimi. Tulikuwa tukilipwa vizuri kabisa, kiasi kwamba nilionekana mjinga kuanza kukosoa maovu mbalimbali yaliyopaswa kukaliwa kimya. Siku zote nilikuwa nikiwaambia maafisa wenzangu, "tusiwe wabinafsi wa kufikiria hii mishahara mikubwa na posho tunazopewa ilhali huko mtaani ndugu, jamaa na marafiki zetu wanataabika. Basi angalau tutimize wajibu wetu na si kuendeshwa na maslahi binafsi." Pengine 'kimbelembele' ndo kiliniponza. Pengine ni ujinga tu, kama baadhi ya watu walivyohitimisha. Lakini deep in my heart, naamini nilifanya kitu sahihi, yaani kusimamia nilichoamini.

Fast forward miaka kadhaa mbele, leo japo sijafanikiwa kuhitimisha safari yangu ya elimu, kwa maana ya Shahada ya Uzamifu ambayo imenichukua kitambo sasa (nililazimika kusitisha masomo kutokana na matatizo niliyokumbana nayo kati yangu na mwajiri/mdhamini wa masomo yangu yaani taasisi niliyokuwa nafanya kazi.) Panapo majaliwa, mwaka huu, jina langu litaanza na "Dokta..."

Leo hii namshukuru Mungu, nimefanikiwa kuendelea kuwatumika Watanzania wenzangu kwa kutumia maandiko yangu, kitu nilichoanza rasmi mwaka 1998. Lakini pia namshukuru sana Mungu wangu na wazazi wangu kwa kuniwezesha kupata shahada tatu, na hii ya nne ndio naihangaikia. Nimepita katika vipindi vigumu mno, kulala na njaa, kusoma kwa koroboi, na kushindwa kuishi kama vijana wenzangu kwa vile nilitoka familia masikini.

Bahati nzuri, nikiwa hapa Uingereza, nilivutowa pia na wazo la kufanya kazi za kujitolea (volunteering). Na baadaye niliajiriwa kwenye taasisi zinazoshughulikia masuala ya wakimbizi. Fursa hizi zimeniwezesha kukutana na watu kutoka sehemu mbalimbali duniani, kutoka Somalia hadi Iraki, Venezuela hadi China, Zimbabwe hadi Kuwait, Eritrea hadi Sri Lanka. Nimejifunza mila na utamaduni wa mataifa mbalimbali. Lakini pengine kubwa zaidi, nimeweza kuwasaidia mamia na pengine maelfu ya watu waliokuja hapa kusaka ukimbizi. Laiti dua na sala zingekuwa zampatia mtu utajiri hapo kwa hapo, basi leo hii ningekuwa bilionea maana nimepata nyingi mno kwa kuwasaidia watu hao ambao wengi walikuja hapa kuokoa maisha yao.

Kwanini nimeandika yote haya? Kwa sababu licha ya kila shida niliyopata katika masiha ya umasikini niliokulia, nilijifunza kuhusu utu. Nimejifunza mengi kuhusu wale waliojinyima kwa ajili yangu, waliogawana nami kidogo walichokuwa nacho, walionishirikisha katika utajiri wa familia zao, walionijali licha ya kutoka familia masikini. Na pia nimejifunza kuwa wema hauozi. Mamia kwa maelfu ya wakimbizi niliowasaidia hapa Uingereza, ninapokutana nao mpaka natamani kujificha kwa jinsi wanavyonimwagia shukrani, sala na dua. Nimejifunza kuhusu utu.

Leo ninamiliki kampuni japo ndo imeanza tu mwezi uliopita. Jana nilikutana na mwalimu wangu (mentor) wa masuala ya biashara, akaniuliza  matarajio yangu kwa mwaka huu 2016. Nijamjibu kwa utani "ninataka hadi kufikia mwisho wa mwaka huu niwe nimetengeneza paundi milioni moja za kwanza kwa kampuni yangu..." kisha nikacheka. Hakupendezwa na kicheko hicho.Akaniambia "japo unaona kama mzaha, lakini una kila nyenzo ya kukuwezesha kutimiza hilo. Cha muhimu, amini katika uwezo wako wa kiakili, upeo wako mkubwa, na historia yako ulivyotoka kwenye umasikini hadi kufikia hapa." Hawa 'wazungu' hawana tabia ya kumpa mtu sifa asizostahili. Kama wewe ni 'bomu' watakwambia, kama wewe ni mzuri watakwambia. Hakuna 'kuzugana.'

Huko nilikotoka na nilikopitia ndo kwanifanya kuwa mtu niliye leo: namchukulia kila mtu kuwa ana thamani yake. Siangalii tofauti ya kielimu kama sababu ya kumdharau mtu ambaye hakubahatika kuelimika sana. Digrii zangu hazina thamani kama sina utu. Kidogo ninachomudu kukipata hapa (ambacho pengine ni kikubwa sana kwa shilingi yetu huko nyumbani) hakinifanyi kujiona tofauti na wanaopata pungufu ya changu.

Namshukuru Mungu kwa baraka zake, nawashaukuru marehemu wazazi wangu kwa kunifundisha kuwa humble (mtu asiyejikweza) na kuwa mtu wa msaada, nawashukuru wote walioniwezesha kupitia safari yangu ndefu iliyojaa milima na mabonde, hasa wale walionifundisha kujali utu badala ya kitu.

Kwa sie Wakristo, tunafundishwa katika Biblia Takatifu kuwa 'wajikwezao watashushwa, na wajishushao watakwezwa.' Naomwomba Mungu aniwezesha kuwa mtu niliye leo hata nikitokea kufanikiwa kimaisha kiasi gani. 

Ndoto yangu ya utotoni ni kuwa daktari wa utabibu ili niweze kuwasaidia watu wengi kadri iwezekanavyo. Bahati mbaya sikufanikiwa. Ndoto yangu ya pili ilikuwa kuwa shushushu (kwa hamasa za Willy Gamba), nilifanikiwa kuitimiza, nikalitumikia taifa langu kwa nguvu zangu zote. Bahati mbaya mambo yakaenda 'kushoto.' Ndoto yangu ya sasa ni kutumia elimu, kipaji, ujuzi na uzoefu wangu kuendelea kuwasaidia watu wengine hususan wale wanaoishi katika hali kama niliyokulia. 

Ninatumaini msomaji mpendwa waweza kujifunza kitu kimoja au viwili katika stori hii.

Happy new year!


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.