21 Feb 2023

Kundi la viongozi wa kanisa la kianglikana kutoka sehemu mbalimbali duniani wamemkataa Askofu Mkuu wa Canterbury, Justin Welby, kuwa kiongozi wao baada ya Kanisa la Uingereza kuunga mkono maombi ya baraka kwa wapenzi wa jinsia moja.


Maaskofu wakuu wanaowakilisha majimbo 10 kati ya 42 katika Ushirika wa Kianglikana wametia saini taarifa wakisema hawamfikirii tena Bw Welby "kiongozi wa ushirika wa kimataifa".

Waliongeza kuwa Kanisa la Anglikana "lilikataliwa" kama "Kanisa Mama" lao la kihistoria.

Ni mara ya kwanza kwa uongozi wa Askofu Mkuu wa Canterbury kukataliwa na kundi kubwa la makanisa.

Tangu ilipoanzishwa mwaka wa 1867, Askofu Mkuu aliye madarakani wa Canterbury amechukua nafasi ya kiongozi wa kiroho wa Ushirika wa Kianglikana, ambao ni ushirika wa kimataifa wa makanisa 42 ya Kianglikana.

Hana mamlaka rasmi - badala yake, ana mamlaka ya kimaadili na anaonekana kama "wa kwanza kati ya walio sawa".

Lambeth Palace, makao rasmi ya Askofu Mkuu wa Canterbury, ilisema hakuna mabadiliko rasmi katika muundo wa Ushirika wa Anglikana yanayoweza kufanywa bila idhini kutoka kwa "vyombo" vyake vinne vya utawala.

Maaskofu wakuu 10, pamoja na wawili kutoka majimbo ya kihafidhina yaliyojitenga nchini Marekani na Brazili, wanapinga kubariki au kuolewa kwa wapenzi wa jinsia moja.

Wanaunda sehemu ya wanachama wa kikundi kiitwacho Global South Fellowship of Anglican Churches (GSFA), ambacho kinadai kuwakilisha 75% ya Waanglikana duniani kote, hasa kote Asia na Afrika.

Waliotia saini ni pamoja na mwenyekiti wa GSFA, Askofu Mkuu Justin Badi wa Sudan Kusini, pamoja na maaskofu wakuu wa Chile, Bahari ya Hindi, Kongo, Myanmar, Bangladesh, Uganda, Sudan, Alexandria na Melanesia.

Katika taarifa ya Jumatatu walisema "hawana uwezo tena wa kumtambua Askofu Mkuu wa sasa wa Canterbury kama kiongozi wa kwanza kati ya viongozi sawa wa ushirika wa kimataifa".

"Kanisa la Uingereza limechagua kuvunja ushirika na majimbo hayo ambayo yanasalia kuwa waaminifu kwa imani ya kihistoria ya kibiblia," taarifa hiyo ilisema.

Mapema mwezi huu Kanisa la Uingereza, ambalo linaongozwa na Bw Welby, liliidhinisha maombi ya baraka kwa wapenzi wa jinsia moja kwa mara ya kwanza. Hata hivyo, msimamo wake kuhusu ndoa za mashoga haujabadilika na wapenzi wa jinsia moja bado hawataweza kufunga ndoa kanisani.

Mipango hiyo, iliyowekwa na maaskofu mwezi uliopita , imekosolewa na wale wanaodhani wanaenda mbali zaidi - na wale wanaofikiri hawaendi mbali vya kutosha.

Msemaji wa Ikulu ya Lambeth alisema "inathamini kikamilifu" msimamo wa GSFA lakini akaongeza "kutoelewana kwa kina" kati ya Waanglikana juu ya kujamiiana na ndoa ni ya muda mrefu, na kwamba mageuzi katika jimbo moja hayaathiri sheria katika maeneo mengine.

"Katika ulimwengu wa migogoro, mateso na kutokuwa na uhakika, lazima tukumbuke kuwa zaidi hutuunganisha kuliko kutugawanya.

“Pamoja na tofauti zetu, lazima tutafute mbinu za kuendelea kutembea na kufanya kazi pamoja kama wafuasi wa Yesu Kristo ili kuwahudumia wenye uhitaji,” walisema.


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.