Showing posts with label JESHI LA POLISI TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label JESHI LA POLISI TANZANIA. Show all posts

15 Apr 2017



Nianze makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi kwa familia za askari wanane wa Jeshi letu la Polisi waliouawa kinyama wilayani Kibiti, Mkoani Pwani. 

Huu ni msiba wa kitaifa, japo hakuna maombolezo ya kitaifa - sijui kwa vile hatuthamini uhai wa Watanzania wenzetu au tushazowea sana vifo kama vile vya ajali, nk.

Jambo moja lililonikera mno jana ni ukimya wa wahusika, na mpaka wakati ninaandika makala hii sijasikia kauli yoyote kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi. Labda kuna watakaosema "aanasubiri taarifa kamili." Hapana. Uongozi hauko hivyo. Sie huku Ulaya sasa ni kama "tumeshaanza kuzowea"  matukio ya kigaidi, maana yanatuandama mno, hasa Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani, na majuzi hapa Uingereza.

Katika kila tukio, bila kujali idadi ya waathirika, takriban ndani ya saa moja tangu kutokea tukio husika, Rais au Waziri Mkuu wa nchi husika huongea na wananchi katika runinga mubashara, kutoa pole kwa waathirika, kuwahakikishia usalama wananchi, na kuwaonya wahusika kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Huu ndio uongozi.

Je sie hali ikoje? Sana sana ni taarifa ya salamu za rambirambi kutoka kwa Rais, kama inavyoonekana hapa chini



Hadi wakati salamu hizo za rambirambi zinatolewa, hakukuwa na tamko lolote kutoka kwa uongozi wa jeshi la polisi. Awali, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba alithibitisha kutokea kwa tukio hilolakina akadai "hana taarifa" kuhusu tukio hilo hadi atakapowasiliana na IGP. 


Baadaye, Kamishna wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, aliongea na waandishi wa habari, ambapo pamoja na mambo mengine alinukuliwa akisema kuwa jeshi hilo "halitokuwa na mzaha wala msamaha" katika operesheni maalum kuhusiana na tukio hilo


Je, kulikuwa na mzaha na msamaha kabla ya tukio hilo, ambao sasa hautokuwepo wakati wa operesheni husika?

Tukiweka kando kasoro hizo, jambo moja lililonigusa mno ni ukweli kwamba matukio makubwa mawili ya hivi karibuni - uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha Clouds na "kutekwa" kwa msanii wa bongofleva, Roma Mkatoliki - yalipewa uzito mkubwa na Watanzania kuliko mauaji hayo ya polisi hao wanane.

Inasikitisha lakini haishangazi. Sababu moja kuu ya "wananchi wengi kutoonekana kuguswa na mauaji hayo ya polisi wanane" ni ukweli kwamba mahusiano katika ya Jeshi la Polisi na wananchi wengi sio mazuri. Polisi wetu wamekuwa wakisifika kwa unyanyasaji dhidi ya raia wasio na hatia. 

Na kama kuna kitengo cha Polisi wetu "kinachochukiwa mno" ni hicho cha FFU (Kikosi cha Kuzuwia Ghasia) ambacho askari hao wanane walikuwamo.

Japo siungo "chuki" hiyo, lakini naelewa jinsi gani Watanzania wengi wasivyopendezwa na utendaji kazi wa jeshi la polisi. 

Kwa upande mwingine, Jeshi hilo limekuwa likionekana kama "adui wa kudumu" dhidi ya vyama vya upinzani, huku likifanya upendeleo wa wazi kwa chama tawala CCM.

Kwahiyo, wakati tunaomboleza vifo hivyo vya polisi hao wanane, ni muhimu mno kwa wahusika kuchukua hatua za makusudi kuondoa "uhusiano wa chuki na mashaka" uliopo kati ya jeshi la polisi na asilimia kubwa ya Watanzania.

Kana kwamba uhusiano bora kati ya jeshi la polisi na wananchi sio muhimu "kihivyo," moja ya nyenzo muhimu ya kujenga na kuimarisha ushirikiano huo, mpango wa 'Polisi Jamii,' ulifutwa kwa sababu wanazozijua wahusika. Polisi jamii ilikuwa kiungo muhimu kati ya polisi wetu na jamii.

Kioperesheni, japo tukio hilo la mauaji ya polisi wanane linaelezwa kuwa ni la kijambazi, binafsi ninahisi kuwa kuna tatizo zaidi ya ujambazi. Na kwa tafsiri ninayoelewa kuhusu ugaidi, basi tukio hilo linastahili kabisa kuitwa la kigaidi. Ni majambazi gani wenye ujasiri wa kuwavizia polisi na kuwaua kufuatia 'ambush' kama hiyo iliyotokea eneo la tukio?

Halafu, hilo sio tukio la kwanza. Na hao polisi wanane sio polisi wa kwanza kuuawa katika eneo hilo, sambamba na wakazi wengine. Yayumkinika kuhitimisha kuwa jeshi la polisi na Wizara ya Mambo ya Ndani hawawezi kukwepa lawama, kwa kushindwa kukabili kushamiri kwa mauaji katika eneo hilo. Sijui Rais Magufuli ameishiwa na zile sindano zake za kutumbulia majipu, au kaishiwa pumzi ya #TumbuaMajipu lakini ni wazi kuna matatizo ya msingi katika uongozi wa Wizara ya Mambo ya Ndani na jeshi la polisi kwa ujumla. Ukimya wa polisi katika uvamizi huko Clouds, na "kutekwa" kwa Roma, na sasa hili la Kibiti, vilipaswa kumfanya Rais Magufuli achukue hatua.

Moja ya sababu maarufu ya polisi wetu wanapozuwia mikutano au maandamani ya vyama vya upinzani huwa "intelijensia." Sasa kama intelijensia ipo kwenye kudhibiti shughuli halali za vyama vya siasa, kwanini intelijensia hiyo isitumike kwenye kukabiliana na "magaidi" hao wanaotikisa Mkoa wa Pwani?

Nihitimishe makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa familia za askari hao waliouawa kinyama. Pamoja na mapungufu yote niliyotanabaisha katika makala hii, hakuna kitu chochote kinachoweza kuhalalisha unyama waliofanyiwa askari hao.

Lakini pia wakati tunaomboleza vifo vyao, ni vema tukatafakari kama Taifa kuhusu mahusiano kati ya jeshi la polisi (na vyombo vyote vya dola kwa ujumla) na raia, ambayo yakiwa bora, yanaweza kusaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na taifa kwa ujumla

13 Jan 2011

Baadhi ya Makamanda wa ngazi za juu wa Jeshi la Polisi Makao Makuu, wakiangalia sehemu ya video iliyokuwa ikionesha jinsi Polisi walivyokuwa wakituliza ghasia huko Arusha.


Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi nchini, Kamanda Paul Chagonja akizungumza na Waandishi wa habari katika Makao makuu ya Jeshi hilo leo



TAARIFA YA JESHI LA POLISI


10 Jul 2010

Kwa mara ya tatu ndani ya wiki moja askari wa jeshi la polisi amejiua kwa kujipiga risasi.Haya si matukio ya kuyachukulia kimzaha kwani licha ya ukweli kuwa vifo vya askari hao ni pigo na doa kwa jeshi hilo lakini pia inawezekana kesho na keshokutwa,Mungu aepushie mbali,tunaweza kusikia askari amemwagia risasi raia kadhaa wasio na hatia kabla ya kutoa uhai wake mwenyewe.Kuna tatizo ndani ya jeshi hilo lakini kama ilivyo ada kwenye maeneo mengine wahusika wanaendelea kujifanya mbuni kwa kuficha vichwa kwenye shimo huku mwili ukibaki nje.

Nilibahatika kufanya kazi na polisi kwa muda mrefu tu na kwa hakika utawahurumia ukisikia na kuona matatizo wanayokabiliana nayo kimaisha na kiutendaji kazi.Kubwa zaidi ni hali ya maisha yao hususan kwenye suala la makazi.Nenda Kilwa Road,Oysterbay au Temeke na shuhudia mazingira wanayoishi wanadola hao,na utakubaliana nami kuwa si vigumu kwao kukumbwa na shinikizo la kisaikolojia.Hebu tafakari kuhusu askari anayekesha lindoni Masaki,Mikocheni,Upanga,Oysterbay,nk kwa vigogo na kushuhudia watu wanavyokula keki ya taifa wakati mwanadola huyo anaishi maisha ya chini kabisa licha ya mchango wake mkubwa katika usalama wa nchi.Ni dhahiri anaweza kupatwa na mawazo kuwa maisha na kazi aliyonayo havina thamani.

Lakini pia kuna unyanyasaji unaotawala kwenye vyombo vyetu vya dola ambapo viongozi ni miungu watu huku wakipata maslahi manono kupindukia ukilinganisha na wale wanaowaongoza.Na hiyo sio huko polisi tu bali hata katika ofisi nyinginezo-za dola na zisizo za dola-ambapo viongozi hujijengea ukuta mrefu wa kuwatenganisha na wanaowaongoza.Vikao kati ya viongozi na watumishi wa ngazi za chini hutawaliwa na vitisho vinavyokwaza kero na malalamiko ya askari wa ngazi za chini kusikika.

Pasipo kutafuta ufumbuzi wa haraka katika wimbi hili la polisi kujiua kwa risasi basi tuwe tayari kushuhudia balaa.Silaha haziui watu,bali watu hutumia silaha kujiua au kuua wengine.Sasa kama askari wetu tunaowakabidhi silaha wanaweza kujiua kama njia ya ufumbuzi wa matatizo yao binafsi,yayumkinika kubashiri kuwa siku moja wanaweza kabisa kuua watu wengine kabla ya kujiua wao wenyewe.

Tusipoziba ufa tutajenga ukuta.Hebu soma habari kamili katika kiungo kifuatacho

Hebu soma habari kamili kwa kubonyeza KIUNGO HIKI.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.