Showing posts with label MAMBO YA ANGA. Show all posts
Showing posts with label MAMBO YA ANGA. Show all posts

24 Sept 2011


Setalaiti 'chakavu' yenye ukubwa unaolingana na basi la abiria inatarajiwa kuanguka duniani kutoka angani muda wowote hivi sasa.Awali setalaiti hiyo ya Shirika la Mambo na Anga la Marekani (NASA) ilitarajiwa kuanguka duniani usiku huu (kwa saa za hapa Uingereza ambazo ni masaa mawili mbele huko nyumbani Tanzania) lakini inaelekea itachelewa kutokana na kasi mwendo wake kupungua.

Inaonekana kuwa vumbi linalotoka kwenye setalaiti hiyo linatarajia kuangukia Amerika ya Kaskazini japokuwa bado uwezekano huo ni mdogo.Setalaiti hiyo 'chakavu' ina uzito wa zaidi ya nusu tani (tani moja ni kilo 1000).Awali NASA walieleza kuwa setalaiti hiyo isingeweza kuangukia Amerika ya Kaskazini lakini taarifa zilizopatikana baadaye zimeonyesha kuwa hadi sasa haifahamiki chombo hicho kitaangukia sehemu gani duniani.

"Kuingia (kwa chombo hicho) duniani kunatarajiwa kutokea Ijumaa ya tarehe 23 Septemba (jana kwa saa za hapa), au mapema Jumamosi tarehe 24,mchana kwa saa za Mashariki ya Marekani (masaa matano mbele kwa saa za hapa au masaa saba mbele kwa saa za huko nyumbani)" ilieleza taarifa ya NASA.

NASA inatarajia vipande 26 vya chombo hicho,vyenye jumla ya kilo 532 vitabaki vimefungamana na kuanguka duniani.Vipande vidogo vidogo vya chombo hicho vinatarajiwa kusambaa kwa umbali wa maili 500 katika uso wa dunia.Kutegemea ukubwa wake,vipande hivyo vinatajiwa kuanguka duniani  kwa kasi ya kati ya maili 55 (kilometa 90) kwa saa  na maili 240 (kilometa 385) kwa saa.

Vituo vya rada sehemu mbalimbali duniani vinafuatilia safari ya chombo hicho lakini kuna uwezekano mdogo wa kutabiri vipande vipande vyake vitaangukia wapi.Matarajio ya wanaanga ni kuona vipande vipande vya chombo hicho vikiangukia baharini (na hivyo kuepusha madhara yoyote kwa wanadamu na mali zao).

Habari njema ni kwamba uwezekano wa vipande vipande vya chombo hicho kukuangukia ni takriban 1 kwa trilioni 20 (1:20,000,000,000,000)

NASA wanashauri mtu yeyote atakayeona vipande kutoka katika chombo hicho kutovigusa bali awasiliane na mamlaka husika (polisi kwa Marekani).Kwa mujibu wa mikataba ya kimataifa inayosimamiwa na Umoja wa Mataifa,kila kipande kitakachoanguka popote pale kinapaswa kurekjeshwa kwa mmiliki wake,yaani NASA.

Sasa kwa wale wanaofanya biashara za chuma chakavu wakiona vipande hivyo na kuvifanya dili watakuwa wanajitafutia kesi za bure na NASA na Wamarekani kwa ujumla.Well,hiyo ni changamsha-baraza,lakini ni matumaini yetu sote kuwa kuanguka kwa setalaiti hiyo hakutakuwa na madhara yeyote kwa wanadamu popote pale walipo.

Habari hii imetafsiriwa kwa ufupi kutoka gazeti la Guardian la hapa Uingereza

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.