Showing posts with label SWAHILI FILMS. Show all posts
Showing posts with label SWAHILI FILMS. Show all posts

23 Nov 2008

Juzi nilipata kijiparaseli (hili neno nililiskia mara ya kwanza Tanga) changu kutoka Amerika,kikiwa kimesheheni dvd ya Bongoland 2.Nilivutiwa sana na Bongoland 1 na nilitarajia sehemu hii ya pili itakuwa moto vilevile.Awali ya yote,mimi sio mchambuzi wa filamu na nitachoandika hapa ni mtizamo wangu wa ki-novice katika fani hiyo.Lakini la muhimu zaidi ni pongezi kwa wote walioshiriki kutuletea burudani hiyo.I just wish tungepata Watanzania wengi zaidi wanaoweza kutonyesha taswira za popote walipo duniani kwa njia mbalimbali,kama filamu,katuni,maandishi,picha,nk.Ndugu yetu Kibira ameonyesha njia.

Sio siri,nilipoangalia Bongoland 1,nilijikuta nimekuwa Juma (mmoja wa wahusika wakuu wa filamu hiyo) tangu mwanzo hadi mwisho.Kwa kweli filamu ile ni nzuri na inakuacha mtazamaji ukijiuliza nini kinafuata.

Katika Bongoland 2,moja ya yaliyoniangusha ni kukutana na Juma "mwingine".Kwa akina sie tuliokwishamzowea yule Juma wa mwanzo hapo tumeangushwa kidogo.Nadhani katika kuleta mtiririko mzuri,jitihada zingefanyika za kuendelea na Juma yule wa mwanzo,japo hiyo haimaanishikwamba huyo "mpya" hakuimudu role yake vyema.Nadhani kaka Kibira alikuwa na wazo hilo lakini nahisi huenda "Juma orijino" hakuweza kujumuishwa kwa sababu zilizokuwa nje ya waandaaji wa filamu hiyo.

Pia nilitarajia kwamba baada ya Juma "kubwaga manyanga" ya maisha ya Amerika,angefika bongo na kukutana na hali halisi ya bongo.Ukiachia sekeseke za hapa na pale kati ya Juma "mpya" na mama mwenye nyumba,siri iliyofichuka ndani ya familia,mbinde za hapa na pale na bosi kazini pamoja na nyodo za Tatu,Juma hakuonekana kukutana na kile kinachoifanya bongo iitwe bongo.Kwa vile siwezi kujua lililokuwa kichwani mwa kaka Kibira,ni vigumu kufanya matarajio yangu yawe halisi.Lakini pengine ingependeza zaidi iwapo mara baada ya kuamua kuondoka Amerika na kurejea nyumbani,Juma angekutana na kile ambacho wengi wetu hutufanya tuhitimishe kwamba AHERA HAKUENDEKI DUNIANI HAKUKALIKI,yaani tunachukizwa na baadhi ya mambo yanayotusibu huku ugenini lakini tunajipa moyo kwamba "ahh haya yana mwisho pindi nikirejea nyumbani",only to get back home na kukutana na mambo kinyume kabisa na matarajio yetu.

Juma aliweza kupata nyumba ya kupanga kirahisi pasipo kukutana na ujanja ujanja wa madalali,au utapeli uliokubuhu katika biashara ya kupanga nyumba.Juma hakupelekeshwa vya kutosha pale ofisini kama ambavyo baadhi ya wenzetu wanavyoshuhudia "laana ya kutoka ng'ambo".Ukifanya hiki utaambiwa "aah usituletee mambo yako ya Ulaya/Amerika hapa..." Ukitaka kuleta mijadala ya msingi ya kuchochea maendeleo unaambiwa "hayo ni hukohuko kwa wazungu...." na pengine Juma angeweza kuonyeshwa akihaha huku na kule kutafuta ATM yenye hela (hususan Ijumaa jioni hadi Jumapili) maana hizo ni miongoni mwa mbinde za bongoland.Pia Juma ana bahati ya kutokutana na mbinde za daladala,"kupigwa mizinga" au hata kumendewa na akina dada walio "ready made" kwa "wachumba kutoka ng'ambo".

Inawezekana kabisa kwamba kuna Bongoland 3,na huenda baadhi ya haya niliyotamani kuyaona katika filamu hii yatakuwa katika filamu ijayo.Hata hivyo,hayo ni maamuzi ya kaka Kibira na timu yake.Who knows,pengine katika sehemu ijayo tutaonyeshwa namna Juma anavyoonja machungu ya ufisadi....maana ni vigumu kwa hali ya sasa kutokutana na jinamizi hilo.

Pamoja na hayo niliyoeleza (yanayoweza kutafsiriwa kama criticism japo sio dhamira yangu) Bongoland imeendelea kuwa kioo kizuri kwa Mtanzania alie ng'ambo kwani imejaribu kutoa picha ya namna mambo yalivyo huko nyumbani.Katika filamu hiyo kuna matukio kadhaa yanayoweza kukufanya utafakari mambo mbalimbali tunayokumbana nayo huku ng'ambo na jinsi yalivyo huko nyumbani.Again,kaka Kibira na timu yake wanastahili pongezi kubwa kwa ubunifu na jitihada zao za sio tu kutuburudisha bali pia kutuelimisha kwa njia ya filamu.

Mwisho,natarajia kitu kingine kikali cha mfanano wa NISAMEHE,filamu ambayo almanusura initoe machozi.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.