Showing posts with label Susanna Nordlund. Show all posts
Showing posts with label Susanna Nordlund. Show all posts

28 Aug 2015

Hii ni simulizi ya kusikitisha kuhusu mwanaharakati wa mazingira kutoka Sweden, Susanna Nordlund, ambaye amekuwa akifanya harakati dhidi ya uporwaji wa ardhi na manyanyaso kwa wakazi wa Loliondo.

Kilichonigusa katika harakati za Susann ni ukweli kwamba ni raia wa kigeni anayepigani haki za Watanzania lakini amekuwa akifanyiwa hujuma na unyanyaswaji mkubwa.

Chini ni stori yake kama nilivyoitafsiri kwa idhini yake:

Ripoti fupi jinsi nilivyokamatwa Loliondo:

Niliwekwa rumande siku mbili katika kituo cha polisi cha Loliondo na pia nilikaa rumande usiku mmoja katika kituo cha polisi cha Arusha.

Sikuruhusiwa kuwasiliana na mtu yeyote, kompyuta yangu iliharibiwa, na badala ya kuelekwa kortini, nilifukuzwa Tanzania.


Wiki iliyopita safari yangu ya hivi karibuni huko Loliondo -sehemu ya dunia ambayo siku zote ipo akilini mwangu- ilikatishwa ghafla baada ya mtu fulani kuniripoti kwa mamlaka za eneo hilo. Nilipania kukutana na watu ambao hawapo online lakini wana taarifa kuhusu vitisho dhidi ya ardhi yao vinavyofanywa na 'wawekezaji.'


Niliwasili Wasso kwa basi tarehe 20 Juni mwaka huu, na sikuwa na mengi ya kufanya wakati ninatafuta gari la kuelekea vijijini. Nilipata ofa moja nzuri lakini dereva akadai kuwa haendi kwenye vijiji hivyo mchana. Hatimaye tarehe 23 nilipata gari kwenda Kirtalo kwa nusu siku. Nikiwa njiani, nilipata ujumbe kwamba mmoja wa madereva wa kampuni ya utalii ya Thomson Safaris alimpigia simu kijana mmoja kumweleza kuwa ameniona na rafaki yangu flani katika nyumba ya wageni ya Domel. Nilikutana na watu hapo Kirtalo, rafiki yangu alibaki hapo, na nilirudi Wasso na dereva. Njiani, tulikutana na gari lililokuwa na Diwani wa Oloipiri  'rafiki wa wawekezaji' William Alais. Mpango wangu ulikuwa kwenda Mondorosi na Sukenya siku inayofuata.

Nilirudi nyumba ya kulala wageni na kuingiza kwenye kompyuta niliyoelezwa na watu huko vijijini lakini baadaye nikaptiwa na usingizi. Nilipoamka, tayari ilikuwa usiku na nikaenda kupata chakula katika nyumba ya kulala wageni ya Honest, hasa baada ya kuona mengi hapo Domel. Gari moja liliwasili, na waliokuwa ndani ya gari hilo walishuka na kuniijia. Afisa Uhamiaji Angela aliniuliza ninafanya nini Tanzania na akataka kuona hati yangu ya kusafiria. Nilimweleza ratiba yangu ya safari na mipango yangu, bila kumtajia dhima yangu kufahamu kuhusu waporaji ardhi ya wafugaji.

Nilikuwa na nakala tu ya hati yangu ya kusafiria, na niliombwa kufuatana na maafisa Uhamiaji na askari polisi kwenda Oloip nilipokuwa nakaa. Nilijaribu kutuma meseji wka marafiki lakini nilinyang'anywa simu yangu. Niliambiwa kuwa Idara ya Uhamiaji ilikuwa ilikuwa ikinifahamu vema kutokana na taarifa za mtandaoni, jambo lililonipa ahueni nikidhani ningeweza kusimulia maoni yangu kuhusu kinachoendelea. Nilifahamishwa kuwa niko chini ya ulinzi na kutakiwa kupakia vitu vyangu. Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Hashimu Shaibu Mgandilwa, ambaye nilimtambua baada ya kumwona katika vyombo vya habari, alikuwepo pia, japo hakujitambulisha, na alikuwa akiongea na maofisa wa Uhamiaji. Wakati tunaondoka hapo kwenda kwenye gari la Idara ya Uhamiaji, kitambu cha kuandikisha wageni kilichukuliwa, na nikapelekwa kituo cha polisi cha Loliondo.

Baada ya kufika kituo cha polisi, niliambiwa kuwa sababu ya kukamatwa kwangu ni kuwa niliingia Tanzania kama mgeni haramu.

Mwaka 2010, nilitembelea Loliondo kama mtalii kuwauliza watu kama Thomson Safaris- kampuni ya Kiamerika ya kutembeza watalii ambayo inadai kumiliki ekari 12617 za ardhi ya Wamasai, na kudaiwa kuwanyanyasa watu- inaendana na ilichoandika kwenye tovuti yake. Nilipatwa na shauku kuhusu suala hili baada ya maongezi mtandaoni. Mengi kwenye tovuti ya kampuni hiyo si ya kweli, lakini pia nilifanya kosa la kumuuliza Afisa Mtendaji wa Kata ya Soitsambu , ambaye alimpigia simu aliyekuwa Mkuu wa Wilaya wakati huo, Elias Wawa Lali, ambaye alinijibu siku iliyofuata. 
Siku iliyofuata, nilifuatwa na polisi na kupelekwa katika Kamati ya Usalama. Nilituhumiwa vitu mbalimbali, kama vile kufanya utafiti bila kibali. Hati yangu ya kusafiria ilichukuliwa na ilinibidi kwenda Uhamiaji Arusha kuichukua, ambapo huko nako niliambiwa kuwa mie ni 'mgeni haramu' na kutakiwa kuondoka nchini humo.
Baada ya hapo ndio nilianzisha blogu yangu - Mtizamo kutoka kwenye kichuguu cha mchwa (A view from a Termite Mound) - kuhusu 'wawekezaji' huko Loliondo ambao ni tihshio kwa haki za ardhi - Thomson Safaris na wengine wanaofahamika zaidi OBC kutoka Falme za Kiarabu- ambao wamekuwa wakijitahidi kuishawishi serikali ya Tanzania kutangaza kilometa za mraba 1500 jirani na Mbuga ya Taifa ya Serengeti kuwa ni eneo lililohifadhiwa, na kuiondoa jamii ya Kimasai katika eneo hilo lenye umuhimu mkubwa kwa maisha yao. Mwaka 2009, suala hili lilipelekea wanavijiji kuondolewa kwa nguvu baada ya kurudi tena katika eneo hilo.
Nilirudi tena mwaka 2011 na 2013 bila matatizo yoyote lakini nimekuwa nikipata zaidi taarifa kuhusu adha zinazowakabili wakazi wa maeneo hayo kupitia watu wanaotumia mitandao ya kijamii (social media). Blogu yangu ni nyenzo muhimu kwa sababu sio tu serikali na 'wawekezaji' wanasambaza taarifa potofu bali pia taasisi na watu wanaopinga unyanyasaji huo wamekuwa wakichanganywa na taarifa potofu. Wenyeji wa Loliondo wanaopinga vitisho kuhusu ardhi yao wamekuwa wahanga wa unyanyasaji mkubwa, hususan kutuhumiwa kuwa ni Wakenya, lakini tishio kubwa zaidi ni kutoka kwa baadhi ya wakazi wanaonufaika na unyanyasaji huo kwa urafiki wao na 'wawekezaji.'
-------------------------------------------------------------------------
Kituo cha Polisi Loliondo

Baada ya kufikishwa kituo cha polisi Loliondo, nilitakiwa kuorodhesha vitu vyangu vyote. Lieleza bayana kuwa ninaamini kukamatwa kwangu kulitokana na 'siasa chafu' kuhusiana na suala la ardhi, na kwamba wanaopaswa kukamatwa ni hao wanaohatarisha maisha ya wanavijiji. Hata hivyo, niliambiwa nipo chini ya ulinzi, na sina haki yoyote. Afisa Uhamiaji Angela alinieleza kuwa nitapatiwa simu yangu siku inayofuata. Kisha nikaingizwa rumande nikiwa na kikoi changu ambacho nilikitumia pia kama blanketi. Nililala kwenye sakafu ya zege kwenye selo yenye kiza. Baadaye nilipewa chupa ya maji ya kunywa ambayo nilitumia kunawa uso, lakini sikunywa maji mengi kwa vile selo haikuwa na choo. Baadaye niliona ndoo inayotumika kama choo.

Loliondo ni sehemu yenye baridi nyakati za usiku, na madirisha ya selo hayakuwa na glasi bali nondo tu. Kulikuwa na mbu wengi na sikuwa na kinga ya kuzuwia mbu (mosquito repellent). Nilikuwa mfungwa wa kisiasa. Nilitetemeka kwa baridi, lakini maneno kutoka Kirtalo kuhusu blogu yangu yalinipa nguvu. Unyanyasaji dhidi  yangu ulikuwa kama kichekesho, na baadhi ya watu walionyesha dalili za kuniunga mkono.

Asubuhi, nilipewa kifungua kinywa na kuruhusiwa kwenye bafuni, na kupatiwa maji ya kunawa uso kabla ya kurudi selo. Kwenye kuta za selo, kulikuwa namnaandishi kadhaa yaliyoashiria baadhi ya mahabasu walikuwemo humo bila mlo kwa siku kadhaa. Baadaye, nilichukuliwa na Angela kwenda ofisi ya Uhamiaji kuchukuliwa maelezo yangu. Alikuwa mkarimu kwangu na kunipatia peremende. Nilitoa maelezo yangu, na kueleza nilichokuwa ninafanya Loliondo, lakini bila kutaja majina kwa kuhofia watanyanyaswa. Angela alinieleza kuwa nitapelekwa kwenye nyumba ya kulala wageni kuoga kabla ya kupelekwa Arusha. Hata hivyo, alionekana kutofahamu kabisa kuhusu suala la haki za ardhi.

Nilirudishwa kituo cha polisi na kusubiri kwa muda mrefu wakati maofisa Uhamiaji wanafanya kikao na Mkuu wa Wilaya. Nilipata mlo na kuendelea kusubiri. Baadaye nilirudishwa tena rumande.

Mkuu wa Wilaya wa zamani, Elias Wawa Wali, alifanya kazi yake kibadhirifu akiitumikia serikali na 'wawekezaji' dhidi ya wanavijiji lakini hakuonekana kuwa na dhamira ya kufanya mabo mbaya zaidi. Mtangulizi wake, DC Hashimu Shaibu Mgandilwa, alikuwa na mawazo ya ajabu kabisa, kwa mfano kuwaamuru viongozi wa chini yake kutembea umbali wa kilometa nane kutoka Wasso hadi Liliondo, na kuishia kutupwa rumande baada ya askari mmoja mla rushwa kupigwa na wanakijiji Mei 6 mwaka huu.

Ilikuwa usiku nilipoamshwa, ANgela alikuja akiwa na bosi wake na mtu mwingine, na tuliondoka sote kuelekea Arusha. Tulipofika Olduvai nilipatiwa vitu vya kufanya usafi mwilini na baadaye tulisimama katika hoteli ya kifahari ya Serena Lodge kupata kifungua kinywa. Sina hakika kama gharama zililipwa kwa fedha za walipakodi wa Tanzania au na hoteli hiyo. Niltamani kuona ana angalau mtalii anayeonekana kama Mswidi lakini haikuwezekana. Nilitaraji kuwa albda taarifa zangu zimeshafika Ubalozi wa Uswidi. 

Tulipofika Arusha, sikurejeshewa simu yangu. Angela, yule afisa Uhamiaji, alikagua vitu vyangu na kukuta orodha ya majina, na hilo halikumfurahisha. Ilikuwa ni orodha tu ya majina ya watu ambao nilipanga kufanya maongezi nao.

Baada ya hapo ilifuatia kusubiri kwa muda mrefu. Koo ilikuwa imenikauka na nilikuwa na uvimbe kufuatia kung'atwa na mbu. Nywele zangu, ambazo kwa kawaida huzisha kila usiku, zilikuwa ovyo ovyo. Nilijilaza kwenye benchi, na baadaye nikasikia mlango ukifunguliwa. Wanasheria waliotumwa na Onesmo Olengurumwa wa Kituo cha Haki za Binadamu waliwasili. Niliwaeleza kilichotokea na wakaniambiwa watashughulikia nipate dhamana ikiwezekana.  Nilishakuwa nimewekwa rumande kitambo sasa na haikuwa haki kuninyima mawasiliano na watu wengine. Nilitaraji kuwa baada ya kutoka rumande itafuatia kesi mahakamani.

Baada ya muda mrefu nilielezwa kuwa nitarudishwa kituo cha polisi. Muda wote huo nilipokuwa nasubiri, sikupewa taarifa yoyote kuhusu inachoendelea. Ufahamu wangu mdogo wa Kiswahili ulichangia pia kutoelwa kinachoendelea. Niliwekwa tena rumande. Humo rumande nilkutana na mahabusu wengine, Sidamu aliyedai ni mtaalam wa wizi kwenye ATM na Mary aliyeiba maji kwa ajili ya kumwagia kwenye shamba lake.

Masaa kadhaa baadaye nilichukuliwa kwenda ofisi ya Uhamiaji na kuchukuliwa alama za vidole. Mchana, nilifahamishwa kuwa mie ni 'mgeni haramu' na sintoruhusiwa tena kuingia Tanzania. Niliambiwa kwamba kitu pekee ninachoweza kufanya ni kuandika barua Wizara ya Mambo ya Ndani. Niliomba majina ya watu ninaoweza kuwasiliana nao kwa barua-pepe lakini sikupewa, na sikurudishiwa simu yangu. 

Nilisindikizwa hadi Namanga, nikiwa kati ya watu wawili katika gari. Mpakani Namanga kulifuatia kusubiri kwingi na kupigwa picha. Niliomba nakala ya hati ya kutangazwa 'mgeni haramu' lakini sikupewa. Nilisema kwamba ningerejea tena siku moja, na afisa mmoja wa Uhamiaji alimweleza mwenzie, "haogopi kitu."

Baada ya kuingizwa Kenya nilipatiwa simu yangu, na dereva mkarimu alinipeleka hotelini. Nilapata fursa kuangalia mitandao ya kijamii na kulikuwa na taarifa za kukamatwa kwangu. Pia nilipata wasaa kuwafahmisha ndugu na jamaa kuwa nimeachiwa huru. Familia yangu haikufahamishwa lolote nilipokamatwa, na maofa wa Ubalozi wa Uswidi hawakuruhusiwa kuwasiliana nami bila idhini yangu (ningewezaje kutoa idhini ilhali walizuwia mawasiliano yangu na mtu yeyote yule?)

Kompyuta yangu ambayo huwa nayo muda wote iligoma kuwaka. Kesho yake nilimpata mtaalam wa kompyuta hapo Namanga ambaye alibaini ilikuwa na matatizo.
Tarehe 30 nilifahamishwa kuwa mwandishi mmoja, Manyerere Jackton ameandika kwa kirefu kuhusu mimi katika gazeti la kila wiki la Jamhuri. Kesho yake niliweza kuiona habari husika........ na ilikuwa na uongo mwingi. Kama nilivyotarajia, mwandishi huyo alijaribu kunifarakanisha na Tina Timan ambaye sijawahi kukutana nae. Huyu ni anayelezwa kuwa ni mwanaharakati kutoka Kenya, japo amekuwa akiishi Tanzania kwa muda mrefu na ana watoto hapo. Mwandishi huyo amekuwa akichochoea vitu vingi dhidi ya wanavijiji wa Loliondo.

Manyerere- au mtoa habari wake- alidai kuwa nilisema kwamba ningehakikisha serikali ya Uswidi inakata misaada kwa Tanzania kama seriali haitoendelea kunisumbua. Licha ya kwamba sina uwezo huo, lakini kila anayenifahamu anajua nisingeweza kusema maneno kama hayo. Kitu pekee nilichosema kuhusu nchi yangu ni katika nchi yoyote yenye demokrasia, mtalii nanaweza kuongelea siasa na mtu mwingine, baada ya kuambiwa pale kituo cha polisi kuwa "hakuna sehemu yoyote duniani mtalii anaruhusiwa kuongelea siasa." Huu ni unafiki wa hali ya juu katika nchi ambayo ni mhanga wa ukoloni mamboleo. 

Katika habari hiyo, Kamishna wa Uhamiaji Abdullah Khamis Abdullah alimpongeza DC Mgandilwa kwa 'kudumisha amani wilayani kwake.' Sio tu uwepo wa Mkuu wa wilaya ni zao la ukoloni bali pia afisa huyo amekuwa akiwatenda wanavijiji kama ilivyokuwa zama za ukoloni.

Mwandishi huyo alinituhumu kuwa mie na 'washirika wangu' tumekusanya mabilioni ya shilingi kwa ajili ya wafugaji wanaonyanyaswa na kuzifadhili NGO za kuchochea vurugu katika vijiji husika. Sijawahi kuksanya fedha zozote wala kutoa chochote kwa NGO. Mie ni bloga tu.

Tishio baya zaidi ni kuwapeleleza wanavijiji wote wanaonisaidia, na kwa kukosa mwelekeo,miongoni mwa wahanga ni mmiliki wa nyumba ya kulala wageni niliyofikia kama mteja mwingine yeyote yule.Itanilazimu nimlipe fedha zake za huduma ya malazi, kupitia huduma ya kuta fedha ya Western Union, mara baada ya kurudi nyumbani, kwani nilichukuliwa kutoka sehemu hiyo ghafla.

Sijui kwanini sikufunguliwa kesi mahakamani. Ingekuwa fursa nzuri kuweka wazi kinachoendelea Loliondo, na kuuliza iwapo watalii hawaruhusiwa kuuliza mwaswali wawapo Tanzania, na iwapo watalii wanaooblogu wanahitaji viza maalumu kuingia katika nchi hiyo.

Sasa dhamira yangu ni kuendelea kuandika kuhusu Loliondo katika uhai wangu wote, na kwa hakika nitarudi tena.

NYONGEZA: Uchunguzi uliofanywa na mafundi wa kampuni ya Samsung umethibitisha kuwa Hard Drive ya kompyuta yangu ilichomolewa nilipokuwa Tanzania.

Pia,Manyerere alinitumia barua pepe kwamba amesoma blogu yangu na anaitetea nchi yake dhidi ya 'ukoloni mamboleo' wangu, akisema 'Tanzania ni kwa ajili ya Watanzania.' Jibu la wazi lilikuwa mshangao kwanini amekuwa akiandika makala mbalimbali za kichochezi dhidi ya wanavijiji wa Loliondo kwa maslahi ya wawekezaji kutoka nje. Badala ya kunijibu swali hilo, mwandishi huyo alijibu haraka kwa kunitumia picha za mtu aliyekuwa akitoa habari Loliondo, na kujigamba kuwa kila nyendo zangu 'haramu' nikiwa huko ilikuwa ikifuatiliwa japo hakubainisha uharamu wa nyendo zangu katika nchi ya kidemokrasia.

Habari hii imetafsiriwa kutoka blogu ya Susanna, kama ilivyoandikwa HAPA. Kadhalika, waweza kuwasiliana na mwanaharakati huyo wa haki za ardhi, kwa barua-pepe [email protected]

MTIZAMO WANGU: Nimemfahamu Susanna kutokana na kuguswa kwake na kujishughulisha kwake na haki za ardhi huko Loliondo. Nina imani wasomaji wengi mnafahamu kuhusu maslahi ya taifa letu yanavyowekwa rehani katika maeneo kadhaa yenye raslimali za taifa letu. Haiingii akilini, mwanaharakati kama Susanna aache shughuli zake huko Uswidi, aende Tanzania kuwachochea wanavijiji. 'Kosa' la dada huyo ni kuwa mtetezi wa wanyonge. Imekuwa kawaida sasa kwa kila anayejaribu kukemea maovu kuitwa adui wa taifa letu. Kwa hakika inaumiza sana kuona watu wanaojali maslahi ya taifa letu wananyanyaswa kiasi hiki na kutangazwa 'maadui wa taifa.' 








Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.